Search This Blog

Thursday 27 October 2022

MUUAJI ASAKWE - 3

 









    Simulizi : Muuaji Asakwe

    Sehemu Ya Tatu (3)





    SIKU hiyo ya Jumapili, majira ya saa nne za asubuhi, vijana wa John Bosho, Chogolo, Chikwala, Robi, Muba na Kessy, walikuwa wamejichimbia ndani ofisi yao iliyoko ndani ya bohari, eneo la Ubungo Machimbo ya Mawe. Walikuwa katika harakati za kupanga mikakati ya kazi yao iliyokuwa inawakabili, ambayo siyo nyingine zaidi ya kwenda kulifukua kaburi alilozikwa marehemu Anita.



    Wote walikutana pale baada ya kupewa maelekezo na John Bosho, kiongozi wao, kama yeye alivyokuwa ameelekezwa na mganga wa jadi, mzee Chiloto Bandua, anayeishi huko Chamazi.  Akiwa amekaa kwenye kiti kilichokuwa mbele yao, akiwaangalia wote, alivuta pumzi ndefu na kuzishusha, halafu akaanza kuwaambia:



    “Jamani, nimewaiteni hapa, kuna kazi nyingine tena…”



    “Sawa, bosi…” wote wakaitikia huku wakimwangalia kwa makini katika kusikiliza maelekezo yanayotolewa.



    “Ni kama mnavyojua, baada ya mimi kutekeleza mauaji ya mchumba wangu, Anita, niliamua kurudi kwa yule mganga, mzee Chiloto Bandua ili aweze kunigangua,” John Bosho akasema na kuendelea. “Baada ya kuongea naye jinsi ya kuweza kujinusuru nisijulikane kama ni mimi niliyefanya unyama huo, amenipa ushauri mmoja ambao kwa kiasi fulani hivi, umenichanganya sana!”



    “Ni ushauri gani unaokusumbua bosi?” Robi akamuuliza.



    “Ameniambia kuwa ili nifanikiwe katika azma yangu, ni lazima tufukue kaburi la marehemu Anita, kule Kiwalani!” John Bosho akawaambia huku akiwaangalia kwa zamu.



    “Ndiyo, bosi…” wakasema kwa pamoja.



    “Baada ya kulifukua hilo kaburi, tutoe baadhi ya viungo muhimu vilivyoko katika mwili wa marehemu. Na kazi hiyo inahitajika kufanyika usiku wa leo hii!”



    “Tunakupata, bosi,” wote wakaendelea kusema.



    “Vizuri kama mmenipata. Je, mko tayari kuifanya kazi hiyo?”



    “Tupo tayari bosi!”



    “Vizuri sana, kama mko tayari katika kazi hiyo, itabidi tutumie gari lile aina ya Toyota Land Cruiser, ambayo ni nzuri. Majira ya saa moja za usiku tukutane pale njia panda ya uwanja wa ndege, mkiwa mmeshachukua vifaa vyote, sururu, sepetu, nyundo na chochote kinachohitajika,” John Bosho aliendelea kuwapa maelekezo.



    “Sawa, tutafanya hivyo,” wakakubali wote!



    “Mara mtakapokuwa tayari, tutawasiliana kwa simu.”



    “Sawa,” Vijana hao waliendelea kuitikia tu, kwani hakukuwa na mtu wa kuweza kumpinga John Bosho kwa jinsi alivyokuwa ni mtu katili na mwenye fedha nyingi!



    Baada ya kumaliza kupeana maelekezo yale, wote waliondoka mle ndani ya bohari. Kila mmoja akelekea na njia yake, ambapo John Bosho alielekea nyumbani kwake, Ukonga kupumzika.Ukweli ni kwamba bado alikuwa amechanganyikiwa na kile kifo cha mchumba wake, Anita, ambapo sasa aliona kama kinataka kumtokea puani kwa jinsi mambo yalivyokuwa yanaonekana.



    John Bosho alipofika nyumbani kwake, Ukonga, alipiga honi mara mbili, halafu geti likafunguliwa na mlinzi. Gari likaingia ndani na kupaki kwenye uwanja mkubwa uliokuwa mbele ya nyumba yake, sehemu ya maegesho, na yeye akashuka na kuingia ndani. Alifikia kukaa kwenye sofa hapo sebuleni, na kabla hajaamua cha kufanya, alichukua simu yake na kumpigia simu Getruda. Mara baada ya kupiga, simu hiyo ikaanza kuita.



    “Haloo…” upande wa pili wa simu ukasema. Alikuwa ni Getruda.



    “Haloo Getruda, habari za saa hizi…”



    “Nzuri…” Getruda akaitikia kwa kusita.



    “Nisikilize Getruda kwa makini,” akamwambia kwa misistizo. “Nakuomba uje hapa nyumbani kwangu, Ukonga, nina maongezi muhimu na wewe…”



    “Maongezi gani tena?” Getruda akamuuliza baada ya kuona kuwa inakuwa kero.



    “Ni maongezi muhimu sana, juu ya mustakabali wetu, mimi na wewe…”



    “Mustakabali gani tena? Kuhusu marehemu Anita?”



    “Hapana, ni mengineyo!”



    “Sawa, nitakuja. Utakuwepo nyumbani?”



    “Ndiyo, niko hapa nyumbani nakusubiri.”



    “Haya, nitakuja…”



    Baada ya John Bosho kumaliza kuongea na Getruda, akakata simu yake na kujiegemeza kwenye sofa pale sebuleni. Mawazo yake yalikuwa mbali sana!



    Siku hiyo John Bosho aliamua kushinda hapo nyumbani kwake, mpaka ilipofika majira ya alasiri hivi. Muda huo alikuwa akimsubiri  Getruda ambaye alikuwa amempigia simu muda mrefu na kumwambia afike pale kwake jioni hiyo, kwa ajili ya mazungumzo maalum. Ni mazungumzo ambayo mpaka muda huo alikuwa akiyapanga kichwani mwake jinsi ya kumweleza ili wakubaliane!



          ********



    HAKUCHELEWA sana. Getruda alifika hapo nyumbani kwa John Bosho, Ukonga, kama alivyokuwa ameamriwa. Alifika kwa kutumia usafiri wa teksi, ikiwa ni kuitikia wito wake, akijua kuwa alikuwa ni mtu mkorofi aliyekuwa anamtafutia sababu za kumfanyia kitu kibaya kama alivyomfanyia Anita, rafiki yake



    Baada ya kumlipa dereva, Getruda akaijongelea nyuma ile kubwa ya kifahari iliyokuwa imezungukwa na uzio wa ukuta madhubuti na geti kubwa la chuma. Eneo la nje ya nyumba ile, palikuwa na mlinzi mmoja wa jamii ya kimasai, aliyekuwa amesimama akiwa amevalia mavazi yake ya jadi, lubega nyekundu. Ni mlinzi wa muda mrefu aliyekuwa ameajiriwa na John,  ambaye pia alimfahamu fika kama Getruda alikuwa ni mpenzi wa bosi wake.



    “Habari yako yero…” Getruda akamsalimia.



    “Nzuri, karibu…” mlinzi yule alimwitikia na kumkaribisha.



    “Ahsante, bosi yupo?”



    “Eee…mzee yuko ndani…”



    “Haya, nakwenda kumwona…” Getruda akamwambia mlinzi yule, kisha akapenya katika mlango mdogo uliokuwa pale getini, na kuingia ndani ya himaya ya kasri ya John Bosho.



    Baada ya kuingia tu, Gertuda alimkuta John Bosho amekaa pale nje katika bustani nzuri ya maua iliyozungukwa na miti yenye kivuli cha kutosha. Pia, ni sehemu iliyokuwa na viti na meza za plastiki maalum za kupumzika. Pale juu ya meza palikuwa na mzinga wa pombe aina ya ‘Jack Daniels,’ chupa kubwa ya maji ya kunywa na glasi ndefu, ambayo John alikuwa anatumia kunywea pombe.



    Vilevile pale chini ya meza palikuwa na ndoo ndogo iliyokuwa imejaa vipande barafu, na ndani yake palikuwa na vinywaji vya aina mbalimbali, kama, bia, soda na vinginevyo. Mbali ya hayo, palikuwepo na pakiti kubwa lililokuwa na korosho mbichi, ambazo pia alikuwa akizitafuna John ili kusindikizia kile kinywaji alichokuwa anakunwa.



    “Oh, karibu Getruda…” John Bosho akamwambia huku akitoa tabasamu pana.



    “Ahsante,” Getruda akasema, halafu akavuta kiti kimoja kati ya vinne vilivyokuwa pale, akakaa huku wakitazamana.



    “Habari yako Getu…” John Bosho akamwambia.



    “Habari ni nzuri tu…” Getruda akasema kwa sauti ya kinyonge akionekana mtu mwenye mawazo.



    “Mbona unaonekana mnyonge?”



    “Ah, basi tu…”



    “Basi nini mpenzi?”



    “Majonzi tu…” Getruda akasema na kuendelea. “Ni kuhusu kifo cha Anita. Ukweli ni kwamba hakupaswa kufa! Hakuwa na hatia yoyote!”



    “Usiseme hivyo…” John Bosho akasema huku akimwanglia Getruda na kuendelea. “Tambua kwamba Anita alikuwa ni mchumba wangu, na siri nyingi alikuwa ameshazijua kuhusu mimi. Sasa baada yakumtibua si ingekuwa rahisi kwake kunichoma kwa Jeshi la Polisi kiasi cha kuniharibia mipango yangu hi ambayo watu wengi hawaijui, au unasemaje?”



    “Hilo naelewa, John… ”



    “Basi, ndiyo maana nikammaliza!”



    “Maadam yametokea ni basi, hakuna cha kufanya zaidi ya kujihami usije ukajulikane kama wewe uliyehusika na mauaji ya mchumba wako, Anita!”



    “Hilo ndiyo la kusema!” John Bosho akadakia na kuendelea. Na pia polisi hawawezi kujua chochote, kwani mauaji yale nimeyafanya kisayansi, hakuna anayeweza kutegua kitendawili hicho! Labda awe mchawi!”



    “Hebu tuyaache hayo. Nieleze jambo uliloniitia hapa nyumbani kwako!” Getruda akamwambia John kwa kumsisitiza!



    “Usiwe na shaka, nitakwambia. Lakini ni vyema ukapata kinywaji cha kulainisha koo…” John Bosho akamwambia huku akiangalia kile kindoo kilichokuwa na vinywaji na mabonge ya barafu. Getruda akainama na kuchomoa soda moja aina ya Fanta na kuendelea kujihudumia kwa kuifungua na kuinywa taratibu.



    “Vizuri sana,” John Bosho akamwambia Getruda. “Nimekuita hapa kwa ajili ya maongezi muhimu na wewe, ukiwa kama mpenzi wangu. Natumaini unajua kuwa nakupenda sana, na pia ni tegemeo langu kwa sasa!”



    “Hilo naelewa kuwa unanipenda…”



    “Ndiyo, basi wewe ndiye tegemeo langu. Nimeshamuua Anita, ambaye alikuwa kikwazo kwetu…hivyo narudia kusema kuwa nakutegemea wewe!”



    “Kunitegemea kivipi?”



    “Kukuoa na kuwa mke wangu!”



    “Kunioa mimi?”



    “Ndiyo…kukuoa, kwani vipi?”



    “Mh, lakini…”



    “Lakini nini?”



    “Unafikiri watu watatufukikiriaje?”



    “Kutufikiria kivipi?” John Bosho akauliza huku akimkazia macho na kuendelea. “Ina maana wewe unaishi kwa kuangalia watu watakufikiriaje?”



    “Siyo hivyo John…basi tutapanga!”



    “Mambo si hayo?” John Bosho akasema huku akikenua meno yake!



    “Mungu wangu!” Getruda akasema kwa sauti ya chini ambayo John hakuweza kuisikia.



    Ukweli ni kwamba Getruda alimwitikia kwa shingo upande. Alishaanza kumwogogopa kiasi cha kumfananisha na mnyama aina ya Simba! Ikiwa aliweza kumuua fafiki yake Anita, pia ingekuwa rahisi kumuua hata yeye endapo wangekorofishana! Hata hivyo Getruda hakuwa na lakufanya, kwani thamana ya uhai wake ilikuwa mikononi mwa John Bosho.



    Ilimbidi Getruda afuate amri yake kwa kila atakalosema, na baada ya kumaliza mazungumzo yao, wakaendelea na mengine huku wakinywa vinywaji katika ile bustani nzuri na ya kupendeza, kama wapenzi wawili waliokuwa wakipanga mipango yao ya kimaisha. Hawakuonyesha huzuni juu ya kifo cha Anita, ambacho kwa namna moja ama nyingine kilikuwa kimesababishwa na wao wawili!



     Ni hatari!



    ********



    WAKIWA bado pale nje kwenye bustani, wakiendelea na mazungumzo yao, mara simu John Bosho iliyokuwa pale juu ya meza iliita. Haraka akaichukua na kuangalia namba za mpigaji, ambayo kwenye kioo ilionyesha ni mmoja wa vijana wake wa kazi aitwaye Chikwala. Hivyo akajua kuwa alikuwa amempigia akitaka apewe maelekezo.



    Kwa vile John Bosho hakupenda Getruda ayasikie mazungumzo yao, akanyanyuka na kwenda kusikilizia mbali kidogo na sehemu waliyokuwa wamekaa. Baada ya kufika kwenye kona ya nyumba, ndipo alipoanza kuwasiliana na Chikwala:



    “Haloo Chikwala…lete habari…”



    “Mambo safi bosi. Tumeshajiandaa kwa ile kazi uliyotupangia…”

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ok, kama mko tayari, nisubirini pale Asenga Pub, uwanja wa ndege. Nitawakuta hapo punde tu, kwani kwa sasa nina mgeni.”



    “Sawa bosi, utatukuta hapo.”



    “Lakini jihadharini sana ili mtu yeyote asiweze kugundua nyendo zenu!”



    “Hakuna shaka bosi..”



    Simu ikakatwa.



    John Bosho akarudi pale alipokuwa amemwacha Getruda, ambaye kwa wote alikuwa akimwangalia  jinsi alivyokuwa akiongea na simu ile, huku wakati wote akionyesha kwa vitendo. Baada ya kukaa tu, Getruda akamwuliza:



    “Ulikuwa unaongea na nani?”



    “Ah, nilikuwa naongea na jamaa yangu. Ni katika shughuli zetu za kikazi…” John akamwambia Getruda akijua kwamba ni uongo mtupu!”



    “Sawa, sasa kinachoendelea?”



    “Mimi sina la zaidi. Nilichokuitia ndiyo hicho nilichokueleza mpenzi!”



    “Haya, nashukuru, sasa mimi naondoka kurudi nyumbani, Ilala, kwani kumeshakuchwa!”



    “Ni sawa mpenzi, lakini itabidi uchukue teksi, kwani kwa muda huu sipendi kutumia gari langu kwa sababu ya kiusalama zaidi!”



    “Hakuna tatizo, nitachukua teksi,” Getruda akakubaliana na uamuzi ule.



    John Bosho akaingia ndani na kumwacha Getruda amekaa pale nje. Alipoingia ndani, alivalia kivingine, ukizingatia alikuwa harudi tena baada ya kumsindikiza Getruda. Kama kawaida alivalia mavazi ya kazi, halafu akachukua bastola yake iliyosheheni risasi na kuichomeka kibindoni kwa ajili ya kujihami endapo angevamiwa ghafla. Akiwa kama jambazi sugu, alijua kuwa muda wowote, saa yoyote, angeweza kukurupushwa na polisi! Ni lazima awe macho, piga nikupige!



    Baada ya kumaliza kujiandaa, John na Getruda walitoka wakiongozana hadi nje ya geti. Kule nje mlinzi wa kimasai alikuwepo, ambapo John alimuaga na kumwambia anamsindikiza mgeni na hatokawia kurudi. Basi, wakatoka huku wakitembea kwa miguu hadi eneo la Ukonga Mombasa, sehemu iliyokuwa na pilikapilika nyingi za watu, kukiwa na kituo kikuu cha mabasi ya daladala na teksi.



    John Bosho akachomoa pochi yake kubwa iliyotuna, halafu akachomoa fedha, noti tano nyekundu, shilingi elfu hamsini, akampatia Getruda, ikiwa ni nauli ya teksi. Getruda akazipokea na kushukuru, halafu wakaagana. Akapanda ndani ya teksi moja wapo kati ya zilizokuwa katika eneo lile, ambayo iliondolewa kuelekea mjini, ambapo John alibaki akiianglia ile teksi iliyombeba Getruda hadi ilipoishia machoni mwake kuelekea katikati ya jiji.



    Getruda alipoondoka, ndipo John Bosho alipokumbuka kuwa alikuwa na ahadi ya kukutana na vijana wake wa kazi, katika kuifanya kazi ile muhimu aliyoelekezwa na mzee Chiloto. Hivyo naye akachukua teksi na kumwambia dereva ampeleke njia panda ya uwanja wa ndege wa Julius  Nyerere, alipokuwa ameahidiana kukutana  na vijana wake, katika kazi iliyotakiwa kufanyika usiku ule wa aina yake! Ni kazi ngumu ambayo walikuwa hawajawahi kuifanya tokea wazaliwe!



    ********       



    Asenga Pub haikuwa mbali sana na barabara kuu inayoelekea maeneo ya Ukonga, Gongo la Mboto, Pugu, Kisarawe na kwingineko, njia panda ya kuelekea Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere, eneo la ‘Terminal 1.’ Ni sehemu iliyochangamka sana, kwa sababu pana pilikapilika nyingi za kibiashara zilizoshamiri.



    Teksi ile ilipomfikisha John Bosho, akashuka na kumlipa dereva, halafu akachanganya miguu kuelekea ndani ya Pub ile iliyokuwa umbali wa mita mia moja hivi kutoka katika barabara kuu. Giza lilikuwa limeshaingia na kumpa faraja ya kutoweza kuonekana na baadhi ya watu waliokuwa wanamfahamu, ambao wengi wao wangeweza hata  kumpotezea muda wake kwa kuongea maongezi mengi yasiyokuwa na mwisho, na hata wengine kumbomu fedha.



    Baada ya kuingia ndani, sehemu maalum iliyokuwa imejificha kiasi, na palipokuwa na taa yenye mwanga hafifu wa rangi ya bluu, akawakuta vijana wale wawili, Chikwala na Robi wamekaa katika sehemu ile iliyotulia sana, na haikuwa na watu. John akavuta kiti kimoja na kukaa huku akivuta pumzi ndefu, na pia akiwaangalia kwa zamu.



    “Karibu, bosi…” Chikwala akamwambia John Bosho.



    “Oh, ahsante sana,” John Bosho akasema huku akiangaza macho yake pande zote. “Naona mmenisubiri sana!” Akaendelea kuwaambia.



    “Ah, kiasi tu…” Chikwala akasema.



    “Siyo sana, bosi,” akaongeza Robi.



    “Basi ni vizuri, sasa ni vyema tunywe huku tukipanga mipango yetu, au siyo jamani?” John Bosho akawaambia huku akitaka kuagiza vinywaji.



    “Ni jambo la busara bosi,” Chikwala akasema.



    Vinywaji iliagizwa. Wakaendelea kunywa taratibu huku kila mmoja akiwa na mawazo yake kichwani, hasa Robi na Chikwala, ambao walishajua kile walichokuwa wameitiwa na bosi wao, kwa mujibu wa zile taarifa alizowapa asubuhi ya siku ile kule katika bohari lao, Ubungo Machimbo ya Mawe.



    Hata hivyo walijua kuwa ilikuwa ni mipango yao ya kazi na siyo zaidi, ambapo John akiwa ni mtu makini, na asiyependa mambo yake yajulikane kwa urahisi, akaendelea kuyazungusha macho yake pande zote za ukumbi. Akaridhika kuwa hali ni shwari, hivyo akakohoa kidogo kusafisha koo lake, na pia akiwaangalia vijana wake Robi na Chikwala kwa zamu kana kwamba alikuwa anawakagua.



    “Ni matumaini yangu kuwa nyote mko tayari kwa kazi niliyowaambia mchana, ikiwa ndiyo utaratibu wetu,” John Bosho akawaambia kwa sauti ndogo.



    “Tuko tayari kwa kazi bosi…” Wote wakasema.



    “Basi, nisikilizeni kwa makini,” John Bosho akaanza kuwaambia.



    “Tunakusikiliza bosi…” wote wakasema.



    “Ni kama nilivyowaeleza tokea mwanzo,” John Bosho akasema na kuendelea. “ Nimeamua kumuua mchumba wangu Anita, baada ya yeye kunikataa, huku akiwa ameshaijua siri yangu kuwa mimi ni mtu wa aina gani.



    Hivyo basi, ili nisiweze kukamatwa kuhusiana na tuhuma za mauaji, ndiyo niliamua kwenda kwa mganga wetu, mzee Chiloto, kule Chamazi…” John Bosho akanyamaza kidogo huku akiwaangalia Robi na Chikwala walivyokuwa wanamsikiliza kwa makini.



    “Ndipo mzee Chiloto aliponipa yale masharti,” John Bosho akaendelea kusema. “Ili nisiweze kukamatwa na polisi, ni lazima nimpelekee baadhi baadhi ya viungo vya mwili, katika maiti ya Anita, ambavyo ni kama, maziwa na sehemu za siri, ili azifanye dawa ya kunikinga polisi wasinigundu. Mmenipata?”



    “Mh!” Robi akaguna.



    “Aisee?” Akadakia Chikwala!                        



    “Mnaguna?” John Bosho akauliza. “ Itabidi mnielewe ninachosema!”



    “Tumekuelewa bosi!” Wote wakaitikia kwa pamoja baada ya bosi wao kuwashtukia!



    “Ok, sasa ndiyo kazi tunayotaka kwenda kufanya usiku wa leo. Ni kulifukua lile kaburi alilozikwa Anita, kule Kiwalani. Halafu tunalitoa sanduku lenye maiti na kuvinyofoa viungo vile muhimu ninavyohitaji kwa dawa. Natumaini mpaka hapo mnanielewa vizuri sana.”



    “Tumekuelewa bosi!” Chikwala akasema kwa niaba yao wawili. Lakini ukweli ni kwamba walikuwa na wasiwasi mkubwa!



     Ni kazi ngumu na ya hatari!



    “Nitawalipa vizuri sana!” John Bosho akaongeza kusema baada ya kuwaona Robi na Chikwala wakiwa na wasiwasi.



    “Hakuna shaka bosi,” Chikwala akasema kwa msisitizo.



    “Natumaini pia, zile zana za kufanyia hiyo kazi mmeziweka tayari…”



    “Ndiyo, zana zote, sepetu, nyundo, na sururu tumeshaviweka ndani ya gari,” Robi akasema na kuendelea. “Na gari lenyewe tumelihifadhi kule upande wa nyuma ili watu wasiweze kulishtukia na kulisoma namba, hasa ukizingatia tumeweka namba za bandia kwa usalama wetu zaidi.”



    “Vizuri, basi tuendelee na vinywaji mpaka muda ufike. Agizeni vinywaji mvipendavyo, msihofu!”



    “Hakuna taabu bosi…” wote wawiliwakasema.



    Robi na chikwala wakaagiza vinywaji na kuendelea kunywa, na pengine wakiendelea na maongezi mengine nje ya kazi ile iliyokuwa inawakabili kwa usiku ule. Wakati wote huo mawazo ya John Bosho yalikuwa mbali sana, akiwazia juu ya utekelezaji wa kazi ile, ambayo hakujua kama wataikamilisha bila kushtukiwa, hasa ukizingatia kwa kipindi kile kulikuwa na doria kali ya Jeshi la Polisi dhidi ya wahalifu.



    Ama kweli kitendo cha kulifukua kaburi na kuutoa mwili wa mtu aliyekuwa ameshazikwa zaidi ya siku mbili, ilikuwa ni hatari sana! Lakini hawakuwa na la kufanya!



    ********                           



    SAA tano za usiku, John Bosho na vijana wake, Robi na Chikwala, walinyanyuka kutoka katika viti vyao baada ya kuona muda muafaka ulikuwa umefika. Wakatoka katika eneo lile la  Asenga Pub, na kuliendea gari lao, aina ya Toyota Land Cruiser, lililokuwa limepaki mbali na hapo, upande wa nyuma wa Pub ile, likiwa ni gari maalum walilokuwa wanalitumia mara kwa mara kwa ajili ya kufanyia kazi kama zile, ambalo waliliwekea namba za bandia ili kuwavunga watu.



    Na mara nyingi hulitumia katika kazi za kijambazi, na nyingine za haramu ambazo huwaingizia kipato  njia ya mkato. Baada ya kulifika gari, wote wakapanda, na dereva akiwa ni Chikwala, ambaye alilitia moto na kuliondoa kwa mwendo wa taratibu na kuliingiza katika barabara kuu kuelekea mjini.Walikuwa wameshajiandaa na kuwa na vifaa vitakavyotumika katika kazi ile, na vyote walikuwa wameviweka nyuma ya buti ya gari.



    Waliifuata Barabara ya Nyerere moja kwa moja hadi walipofika eneo la Kipawa, kwenye taa za kuongozea magari. Pale Chikwala akapinda kulia na kuifuata barabara inayoelekea Jet Club, ambayo aliifuata moja kwa moja, halafu akapinda kulia kuifuata barabara nyingine inayoelekea Kiwalani. Ni hadi walipofika eneo la Kiwalani, sehemu yalipo makaburi yale yaliyokuwa yaliyozungukwa na miti mingi, pamoja na vichaka vilivyosababisha kuwe na kiza kizito.



    Wakaliacha gari lile mbali na yalipo makaburi, na siyo jirani sana na nyumba za wakazi, ili wasiweze kushtukiwa na wakazi wa eneo lile. Wakiwa kama watu waliokuwa katika shughuli zao, wakashuka na kuanza kuangaza macho pande zote ambapo palikuwa na giza zito lilitokana na ile miti iliyofungamana na kuwafanya wasiweze kuonekana.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    Bila kupoteza muda, Robi akazunguka nyuma ya gari na kufungua buti, halafu akatoa zile zana zote za kazi, mifuko mieusi,laini ya nailoni, sururu, sepetu na nyundo, halafu wakaongozana kuelekea ndani ya makaburi yale, wakiwa na tahadhari! Makaburi yalikuwa ni mengi sana, hivyo wakaanza kulitafuta lile kaburi alilozikwa marehemu Anita, ambalo lilikuwa katikati ya makaburi mengine.



    Hawakupata shida ya kuliona kaburi hilo, ambalo juu yake palikuwa na mashada mengi ya maua yaliyokuwa yamewekwa na waombolezaji. Pia, lilikuwa na msalaba uliosimikwa, ambao ulikuwa umeandikwa maandishi ya jina la Anita, tarehe ya kuzaliwa, tarehe ya kufa pamoja na mwaka aliokufa.  Kabla ya kuanza kulifukua, wakaliangalia kwanza na kuvuta pumzi ndefu! Ama kweli ilikuwa kazi nzito na ya kukata na shoka!



    Kama vile walikuwa wamekurupushwa, walilizunguka lile kaburi na kuanza kulifukua mara moja kwa kasi ya ajabu, hasa ukizingatia walikuwa wameshavuta misokoto kadhaa ya bhangi, ili waweze kuifanya kazi hiyo kwa ufanisi zaidi. Kwa  vile kaburi lenyewe lilikuwa siyo la muda mrefu, wakalifukua na kumaliza, kisha wakalitoa lile sanduku na kuliweka juu kando ya kaburi.



    Walilifungua sanduku hilo kwa kutumia ile nyundo nadi walipofanikiwa. Waliukuta mwili ule wa Anita, uliokuwa umevikwa nguo alizozikwa nazo, kwa haraka wakautoa na kuuvua nguo na kuziweka kando, kisha Robi akatoa kisu chake, aina ya ‘Okapi’ na kuanza kazi ya kuziondoa kwa kuzikata zile sehemu zilizokuwa zinahitajika na mganga.



    Akiwa na roho iliyojaa ukatili, Robi akafanikiwa kuyakata maziwa na sehemu za siri, vitu ambavyo alikuwa ameagiziwa na mganga. Baada ya kuzikata, akaziweka ndani ya mfuko ule maalum wa nailoni wa rangi nyeusi. Baada ya kumaliza kazi yao, wakajiandaa kuurudisha ule mwili ndani ya sanduku kama ulivyokuwa mwanzo kabla ya kufukuliwa.



    Muda wote huo, John Bosho alikuwa amesimama huku akiangaza macho yake pande zote ndani ya kiza kile, ili kuangalia kama kuna mtu yeyote anayeweza kuwatibulia mpango wao ule. Hata hivyo, ziliweza kusikika sauti ya watu waliokuwa wanapita sehemu ya nje usawa ule wa makaburi, na pia mwanga wa tochi uliokuwa unamulika chini na kuonyesha kuwa walikuwa wanapita.



    Lakini ghafla wakauona ule mwanga wa tochi iliyokuwa ikimulika, ukielekezwa usawa wa kule makaburini walipokuwa wao.Wote watatu wakachuchumaa chini na kuangalia kule mwanga wa tochi ulipotokea! Walikuwa ni walinzi wa sungusungu waliokuwa zamu usiku ule, na sauti zao katikati ya usiku ule ziliweza kusikika wazi kumaanisha kwamba walishangaa kuwaona watu wale wakiwa ndani ya makaburi!



    “Nani hao wanamulika na tochi?” John Bosho akauliza huku macho yake kayatoa pima!



    “Inawezekana ikawa ni walinzi wa sungusungu hao!” Chikwala aliyekuwa ameshika sepetu akadakia na kuongeza. “Watatuletea mkosi sasa!”



    “Na kweli ni sungusungu!” Robi akasema huku naye akiyakaza macho yake katika kiza kile kizito!



     Akaweza kuona kundi la watu!



    “Basi, acheni, chukueni mzigo wetu tuondoke zetu!” John Bosho akawaambia Robi na Chikwala kwa sauti ya msisitizo!



    Wote wakaondoka kwa mwendo wa kasi na wa kuinama, huku wakitimua mbio kuelekea kule walikoliacha gari lao. Lile sanduku la maiti wakaliacha pale pale juu bila kulifukia, na huku mwili wa Anita ukiwa kando ya sanduku, siyo mbali na lilipokuwa shimo!



    Ni ushenzi mtupu!



    “Simameni!” Sauti kali ikatokea katikati ya miti iliyofungamana  ndani ya eneo la makaburi!



     Sauti ile ilikuwa ni ya kiongozi wa kundi lile la sungusungu, ambaye alioendelea kuwamulika kwa tochi iliyokuwa na mwanga mkali! Hata hivyo, John Bosho, Robin na Chikwala walifanikiwa kutimua mbio hadi walipofika kwenye uchochoro mmoja, sehemu ile sehemu walipoliacha gari lao.  Kwa haraka wakafungua milango na kupanda, na kabla milango haijafungwa vizuri, Chikwala akalitia gari moto na kuliondoa kwa mwendo wa kasi!



    “Tumenusurika!” John Bosho akasema.



    “Duh, yule sungusungu mnoko sana! Unajua karibu atuharibie kazi!” Akadakia Robi!



    “Sijui wametokea wapi wale washenzi! Tena kidogo wangetuwahi kabla hatujakamilisha lengo letu!” Akaongeza Chikwala huku akipangua gea na kuongeza mwendo wa gari mara tu baada ya gari lile kufika katika barabara ya lami inayoyoelekea eneo la Vingunguti, hadi walipotokeza katika Barabara ya Nyerere. Usiku ule magari yalikuwa machache sana, hivyo Chikwala akaliingiza moja kwa moja barabarani!



    “Tunaelekea wapi bosi?” Chikwala akamuuliza John Bosho!



    “Tunakwenda Chamazi kwa mzee Chiloto Bandua!” John Bosho akawaambia Chikwa.



    “Sawa bosi!” Chikwala akasema huku akiifuata Barabara ya Nyerere kuelekea maeneo ya Tazara.



    Baada ya kufanikiwa kulitoka eneo lile la Kiwalani bila kukamatwa na wale walinzi wa Sungusungu waliokuwa kazini, John Bosho na wenzake hawakujua kilichoendelea tena kule nyuma. Kwa vyovyote walijua ni lazima kutakuwa na msako mkali unafanyika dhidi yao, punde tu baada ya kuukuta ule mwili wa Anita ukiwa umeondolewa ndani ya sanduku!



    Mbio za gari ziliendelea hadi walipofika Tazara, kwenye taa za trafiki, Chikwala alipinda kulia na kuifuata Barabara ya Mandela moja kwa moja hadi Kwa Sokota. Hapo wakaifuata  inayoelekea Chang’ombe, ambayo waliendelea nayo huku wakikatiza katika vichochoro, ili kukwepa kama walikuwa wanafuatiliwa nyuma!



    Hatimaye mbio hizo zikaishia kule Chamazi, nyumbani kwa mzee Chiloto Bandua, mganga wa jadi. Chikwala akalisimamisha gari mbali kidogo na kwenye makazi ya mganga huyo, halafu wakashuka na kuanza kutembea kwa miguu kuiendea nyumba. Sehemu yote ya Chamazi ilitisha kwa usiku huo, kukiwa kimya kabisa, lakini wanaume wale wa shoka hawakuwa na wasiwasi wowote. Tuseme ni kwamba walikuwa wanajiamini sana ukizingatia ni watu waliozoea kazi zile za hatari siku zote!



    ********



    NYUMBA ya mzee Chiloto Bandua ilikuwa ya kawaida tu, ambayo imejengwa kwa matofali na kuezekwa kwa mabati, ujenzi ambao haukukamilika vizuri. Kama walivyozoeleka kama wateja wake, baada ya kufika, John Bosho na wenzake walikaribishwa na kuingia ndani ya chumba kimoja ambacho ni maalum kwa kazi za kiganga.



    Kwa vile ilikuwa ni usiku, paliwashwa taa ya kandili iliyotoa mwanga hafifu, lakini uliowezesha kumwona mzee Chiloto Bandua aliyekuwa amekaa mbele yao katika jamvi lililotandikwa chini. Akiwa ni mzee mwenye umri wa miaka sitini hivi, alikuwa amekaa huku amezungukwa na vibuyu vidogovidogo, pamoja na madawa mengine ya aina mbalimbali. Aliwakodolea macho yake makali na kuwaangalia kwa zamu.



    “Ni matumaini yangu kuwa mmekuja na ule mzigo niliouagiza!” mzee Chiloto bandua akawaambia.



    “Ndiyo  mzee…tumekuja nao…” John Bosho akasema huku akiwa na matumaini.



    “Vizuri sana,” mzee Chiloto Bandua akasema na kuendelea. “Sasa nyie wawili tokeni nje. Mimi nitabaki na huyu mmoja tayari kwa kumganga!”



    “Sawa mzee…” Chikwala akasema.



    Robi na Chikwala wakanyanyuka na kutoka nje ya chumba kile na kwenda kukaa sehemu iliyokuwa na viti maalum kwa ajili ya wateja. Pale chumbani wakabaki mzee Chiloto na John Bosho aliyesubiri kufanyiwa uganga.



    “Hebu nipe huo mzigo,” mzee Chiloto Bandua akamwambia John ambaye alikuwa na mawazo mengi yaliyokuwa yamemjaa kichwani.



    “Mzigo huu hapa!” John Bosho akasema huku akimkabidhi mzee Chiloto ule mfuko mweusi uliokuwa na mzigo.



    “Oh, vizuri sana,” mzee Chiloto Bandua akasema huku akiupokea ule mfuko na kuanza kuufungua kwa makini akitegemea kukiona kilichoko ndani yake!



    Baada ya kuufungua ule mfuko, mzee Chiloto Bandua akavitoa viungo ile vilivyokuwa katika hali ya nyamanyama hivi. Kisha akaviweka ndani ya chungu kimoja kilichokuwa pale kando. Halafu akachanganya na maji na kuanza kukoroga kwa nguvu huku akitamka maneno fulani, ambayo hata upande wa John hakuyaelewa kamwe. Muda wote alikuwa akimwangalia alivyikuwa anafanya kazi ile ya uganga, kumganga yeye!



    Alipomaliza kuongea maneno yale, mzee Chiloto  Bandua akachukua wembe mpya na kuanza kumchanja chale mwili mzima katika sehemu muhimu. Halafu akampaka ile dawa iliyokuwa ndani ya chungu kile alichoweka viungo vya binadamu. Ni dawa iliyokuwa inauma sana ilipokuwa inaingia mwilini mwake katika zile chale.



     John Bosho akawa anajitingisha kadri alivyokuwa anapakwa hadi mzee Chiloto Bandua alipomaliza. Baada ya hapo, akampa dawa nyingine ambayo ingemfanya asiweze kujulikana na polisi, au mtu yeyote kwamba ndiye mhusika mkuu wa mauaji yale ya mwanadada Anita!



    “Naona mambo yote tayari… tumeshamaliza kazi yetu!” mzee Chiloto Bandua akamwambia John Bosho.



    “Oh, nashukuru sana,” John Bosho akasema huku akinyanyuka kutoka pale kwenye jamvi alipokuwa amekaa. Ukweli ni kwamba alikuwa ana matumaini!



    “Mambo shwari sasa!” mzee Chiloto Bandua akaendelea kumwambia John.



    “Ina maana hapa ndiyo kiboko! Hakuna mtu yeyote atakayekugundua!” Mzee Chiloto bandua akaendelea kumwambia John.



    “Unasema kuwa polisi hawataona ndani?”



    “Waone ndani? Wataona giza tupu!”



    “Basi poa,” John Bosho akasema huku akichomoa pochi yake na kuanza kuifungua. “Ni shilingi ngapi mzee?” Akamuuliza.



    “Ah, wewe ni mteja wangu wa kila siku… nifikirie kiasi cha mboga tu,” mzee Chiloto bandua akamwambia huku akikenua meno yake.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    “Haya, chukua pesa hii, natumaini inatosha…” John Bosho akamwambia na kumpatia shilingi laki moja.



    “Oh, nashukuru sana…” mzee Chiloto bandua akasema huku akitabasamu kwa kuona kiasi kile cha fedha!



    “Mimi natoka mzee,” John Bosho akaaga.



    “Haya kijana, karibu tena…” mzee Chiloto Bandua akamwambia huku akimwangalia John Bosho alivyokuwa anatoka nje ya kibanda chake.



    Ukweli ni kwamba mzee Chiloto Bandua alikuwa anasikitika sana, kwa vile alikuwa anamdanganya tu, hakuwa na uwezo wa kumtengenezea kinga ya kummfaya asikamatwe na Jeshi la Polisi. Ni njaa tu iliyokuwa inamfanya mzee huyo afanye kazi kama ile ya utapeli, kwa kuwadanganya watu kuwa alikuwa na uwezo mkubwa wa kuwakinga na dawa zake za asili. Na kwa vile watu wengi wanahusudu mambo ya ushirikina, basi aliweza kuwapata kwa wingi sana, maisha yakawa yanasonga mbele.



    Baada ya kumpatia zile fedha, mzee Chiloto Bandua, John akatoka ndani ya chumba kile na kuungana na wenzake, Chikwala na Robi, waliokuwa wanamsubiri kando ya chumba kile. Wote wakaondoka nyumbani kwa mganga huyo, na kuelekea sehemu ile walipoliacha gari lao, wakiwa na matumaini kuwa siri ile isingeweza kujulikana kabisa baada ya bosi wao kupata kinga! Walipofikia gari, wakapanda na dereva akiwa Chikwala, ambaya alilitia moto na kuliondoa kwa mwendo wa wastani kuelekea katikati ya jiji.



    *********



    MZEE Chiloto Bandua alipokabidhiwa zile fedha na John Bosho, alitoka ndani ya kibanda chake uganga, halafu akarudi ndani ya nyumba kubwa na kuungana na mke wake, Bi. Neema binti Shamte, aliyekuwa amekaa akiangalia runinga sebuleni.



    Hakika mzee huyo alikuwa na furaha baada ya kulipwa fedha zile, kiasi cha shilingi laki mbili kwa mara moja, tena fedha iliyomjia usiku akiwa hana uhakika wa kuingiza kiasi hicho. Baada ya kukaa kwenye kochi, kando ya mke wake, akapumua kwa nguvu na kumwambia:



    “Oh, mke wangu, nimeshamaliza kazi…”



    “Umeashamaliza sivyo?” Bi. Neema akamuuliza kana kwamba hakumsikia.



    “Ndiyo, nimemaliza. Unafikiri ilikuwa kazi kubwa sana mke wangu? Ni ya mara moja tu hata isiyotoa jasho!”



    “Mh,” Bi. Neema bint Shamte akaguna huku akimwangalia kwa uso uliojaa woga! Halafu akamwambia. “Mume wangiu wewe… mzee Chiloto…”



    “Labeki mke wangu…” mzee Chiloto Bandua akaitikia huku akimwangalia mkewe.



    “Mbona unajitafutia balaa?” Bi. Neema akaendelea kumwambia.



    “Balaa gani tena mke wangu?”



    “Si kuhusu hao wateja wako?”



    “Kwani vipi?”



    “Hivi ni kweli unawatibu?”



    “Ni kweli nawatibu, kwa nini unawauliza hivyo?”



    “Nauliza kwa sababu mwanzo kabisa ulikuwa unatibu wateja wa kawaida wenye matatizo kama ya kulogwa, kusafisha nyota, kupata bahati, na mengineyo,” Bi. Neema akasema na kuongeza. “Hivi naona umeanza kutibu hata majambazi! Hakika iko siku watakuja kukugeuka endapo hawatafanikiwa katika malengo yao!”



    “Usiwe na wasiwasi mke wangu. Mimi huwa natibu watu wa aina zote, haichagui majambazi, kwa vile hawana alama usoni. Dawa zangu ni kiboko!”



    “Haya, mimi kazi yangu ni kukwambia kwa jinsi ninavyoona, lakini nakupa tahadhari!” Bi. Neema akaendelea kumwambia.



    “Yaani tahadhari unanipa mimi mganga wa waganga?”



    “Ni lazima nikwambie, siku yakiharibika mimi nakimbia, siwezi kupigwa risasi nikijiona!” Bi. Neema akasisitiza!



    “Huo ni uchuro sasa, tuendelee na mengine!” Mzee Chiloto Bandua akamwambia mkewe baada ya kuona alikuwa anamletea mikosi sasa!



    Mjadala ukaisha!



    Mzee Chiloto Bandua na mke wake, Bi. Neema bint Shamte walimaliza yale majadiliana yao, huku mzee huyo akiona kuwa ule ulikuwa ni ukweli aliokuwa anaambiwa na mke wake, hasa ukizingatia baadhi ya wateja zake alikuwa akiwadanganya ili aweze kupata fedha za kujikimu. Siku zote alikuwa akisema wajinga ndiyo wali wao!



    Hata hivyo siku zake zinahesabika!



    ********    



    KACHERO Inspekta Malik  Mkoba aliamka kunako majira ya saa kumi na mbili za asubuhi. Baada ya kujiswafi alivalia nguo zake nadhifu, ambazo zilimpendeza baada ya kujitazama kwenye kioo kikubwa kilichokuwa ukutani. Yeye alikuwa bado kijana  mbichi tu, mwenye umri wa miaka 35 hivi,  na mmoja wa makachero shupavu na mchapakazi katika Jeshi la Polisi, hususan kitengo cha Idara ya Upelelezi.



    Kwa muda wote, kimakazi, alikuwa anaishi nyumbani kwake, eneo la Ilala, Shariff Shamba,  alipokuwa anaishi pamoja na wadogo zake wawili, Toni na James aliokuwa anawasomesha.Ni kwamba, alikuwa bado kijana mwenye malengo na bado hajaoa, lakini alikuwa na mchumba aitwaye Dora Damas, ambaye walikuwa katika harakati za mipango ya harusi, ambayo ingefanyika wakati wowote mambo yatakapotengamaa.



    Kachero Inspekta Malik alipohakikisha kila kitu tayari, alitoka nje ya nyumba yake na kuliendea gari lake aina ya Nissan Laurel, ambalo lilikuwa limepaki upande wa mbele ya nyumba yake katika uwanja mdogo wa maegesho. Baada ya kulifikia, akafungua mlango na kupanda, halafu kalitia moto na kuliondoka hadi nje ya geti la kutokea ambalo lilikuwa limeshafunguliwa. Baada ya kulitoa nje, akaifuata barabara ndogo ya udongo iliyotokeza katika barabara kuu ya Uhuru.



    Alipoifikia barabara hiyo, akapinda kulia kuifuata hiyo barabara ya Uhuru kwa mwendo wa wastani hadi alipofika kwenye kituo cha Polisi Buguruni. Ni kituo ambacho hakikuwa mbali sana, ni umbali kama wa kilometa mbili na nusu kutoka pale nyumbani kwake, Shariff Shamba, Ilala. Baada ya kufika kituoni, akalipaki gari sehemu ya maegesho iliyokuwa kando ya kituo.



    Kachero Inspekta Malik akashuka na kuiedea ofisi yake kwa mwendo wa kikakamavu hadi alipoingia na kuketi, tayari kuanza kazi zilizokuwa zinamkabili. Hata hivyo hakupoteza muda, alianza kuyapekuwa mafaili kadhaa aliyotakiwa kuyashughulikia likiwa lile la marehemu Anita. Lakini kabla hajafika mbali na upitiaji wa mafaili, akaingia Kachero Sajini Joel Kidampa, huku akitoa heshima kwa nidhamu.



    “Karibu Joel…” Kachero Inspekta Malik akamwambia.



    “Ahsante afande…” Kachero Sajini Joel Kidampa akasema huku akiwa bado amesimama.



    “Nipe taarifa…”



    “Kuna taarifa muhimu imetufikia muda huu afande…”



    “Taarifa gani?”



    “Afande, kuna wakazi watatu wa eneo la Kiwalani, akiwemo mjumbe wa nyumba kumi, na mzazi wa marehemu Anita, wamefika hapa kituoni asubuhi hii. Wamesema kuwa lile kaburi alilozikwa Anita juzi, limefukuliwa usiku wa kuamkia leo. Na haijulikani ni watu gani waliyelifukua; na walikuwa na maana gani!” Kachero Joel Kidampa akamaliza kusema, kisha akabaki akimwangalia Malik.



    “Mh,” Kachero Inspekta Malik akaguna na kusema. “Unasema kaburi limefukuliwa?”



    “Ndiyo afande…limefukuliwa…”



    “Hao watu wako hapo nje?”



    “Ndiyo, wako hapo nje…”



     “Hebu waambie waje hapa ofisini.”



    “Sawa afande…” Sajini Joel Kidampa akasema, kisha akatoka na kwenda kuwaita watu wale.



    Baada ya dakika mbili tu, Joel akaingia pale ofisini akiwa na wale watu watatu, Mjumbe wa Nyumba Kumi, mzee Shogholo Uledi, baba wa marehemu, mzee Anthony Mkonyi, pamoja na mkazi mwingine mwenye umri wa kati, Mwaipaja Mwanjelwa.



    “Karibuni wazee…” Kachero Inspekta Malik akawakaribisha.



    “Ahsante…” mzee Shogholo Uledi akasema.



    “Ahsanter kijana…” mzee Anthony naye akasema huku wakiingia pale ofisini.



    Wazee wote watatu wakakaa kwenye viti.



    “Ndiyo wazee wangu, karibuni na mnieleze kilichojiri…” Kachero Inspekta Malik akawaambia.



    “Tumefika hapa kituoni ili kueleza kilichotokea usiku wa jana huko katika eneo la Kiwalani tunapoishi,” mzee Shogholo Uledi, Mjumbe wa Nyumba Kumi akaanza kueleza. “Ni kwamba sisi huwa tuna mpango wetu wa kufanya doria za mara kwa mara nyakati za usiku ili kudhibiti wimbi la uhalifu kwa ujumla, ambapo huwa tunawashirikisha wakazi wa mtaa katika kujilinda…”



    “Hilo ni lengo zuri sana, katika Ulinzi Shirikishi na Polisi Jamii, katika kutusaidia sisi askari polisi kudumisha ulinzi na amani,” Kachero Inspekta Malik akadakia.



    “Ni kweli kabisa, dhana hiyo tunaifahamu sana. Basi, wakati tukiwa doria katika eneo la makaburi ya Kiwalani, ndipo tuliposikia sauti za watu waliokuwa wakiongea ndani ya makaburi hayo. Hivyo tukanyatia taratibu na kukuta kuwa ni kweli kulikuwa na watu ambao idadi yao haikufahamika, wakiwa wanafukua kaburi moja wapo. Baada ya kutuona, wakakimbia na kuondoka na gari lao walilokuwa wamefika nalo hapo…” mzee Shogholo Uledi akanyamaza kidogo huku akimwangalia Malik.



    “Watu wale walipokimbia, sisi tulikwenda mle ndani ya makaburi, na baada ya kufanya uchunguzi, ndipo tulipokua kaburi la marehemu, Anita, mtoto wa mzee mwenzangu hapa, likiwa limefukuliwa na mwili kutolewa ndani ya sanduku….” mzee Shigholo Uledi alieleza yote yaliyotokea kule kitu ambacho kilimshangaza sana Kachero Inspekta Malik.



    “Oh, poleni sana, je, baada ya watu hao kukimbia, mliweza hata kumtambua mmoja wao?” Kachero Inspekta Malik akamuuliza mzee Shogholo Uledi.



    “Hapana, kwa kweli hatukuweza kumtambua hata mtu mmoja, hasa ukizingatia kulikuwa na giza,” mzee Uledi akasema.



    “Pia umesema kuwa walifika pale kwa gari, je, ni gari ya aina gani?”



    “Kama sikosei ilikuwa ni Toyota Land Cruiser…”



    “Ulifanikiwa kuisoma namba?”



    “Hapana, sikufanikiwa kuisoma namba…”



    Mahojiano yakaendelea juu ya tukio lile la kukuta kaburi limefukuliwa usiku wa kuamkia siku hiyo, na baada ya mahojiano yale, Kachero Inspekta Malik akampa majukumu Kachero Sajini Joel Kidampa na askari wengine wawili wa magwanda, waondoke pale kituoni kuelekea eneo la tukio, Kiwalani. Hakika Malik alikuwa ametandwa na giza mbele yake na kujiuliza kuwa watu waliokuwa wamefukua kaburi lile walikuwa na maana gani?



    Hakujua!



            ********



    WOTE waliondoka hapo kwenye Kituo cha Polisi Buguruni kwa kutumia gari la matukio aina ya Toyota Land Cruiser , iliyokuwa na namba za kiraia. Walitumia kama saa moja na nusu tu kufika katika eneo la makaburi ya Kiwalani. Baada ya kufika, waliukuta umati mkubwa wa watu ukiwa umejazana, wengi wao wakishangaa juu ya kufukuliwa kwa kaburi lile lenye mwili wa Anita ambao ulishazikwa!



    Kwa vile watu walikuwa wengi, wakafanya kazi ya ziada kuwatawanya ili waweze kupita na kuingia kule makaburini bila bughudha. Makachero wale wakaingia katika eneo la makaburi, ambapo waliukuta mwili wa Anita ukiwa kando ya kaburi, ukiwa umeondolewa ndani ya sanduku, na baadhi ya viungo vimeondolewa kwa kukatwa!



    Baada ya uchunguzi mdogo, Kachero Inspekta Malik akalifananisha tukio lile na imani za kishirikina, kwa vile ulikuwa umeondolewa baadhi ya viungo. Hata hivyo akauruhusu uzikwe tena, na wakazi wa pale wakauzika  ule mwili, na makachero wale wakajiandaa kuondoka kurudi kituoni. Habari zile za mauaji ya kutisha na kufukuliwa kwa maiti ya Anita zikaendelea kutapakaa kote jijini  Dar es Salaam!



    Baada ya mwili wa Anita kuzikwa tena, Kachero Inspekta Malik akaona kulikuwa na usiri uliokuwa umejificha nyuma ya kifo cha Anita. Hata hivyo kabla ya kuondoka eneo hilo la Kiwalani, aliona lilikuwa ni jambo la busara kuwahoji wazazi wa Anita, ili aweze kupata mambo muhimu kutoka kwao, ambayo yangemsaidia katika upelelezi wake.



    Kachero Inspekta Malik alifika nyumbani kwa mzee Anthony, baba yake Anita, ikiwa ni mara ya pili tokea siku ile alipokwenda baada ya wao kumwita. Wakampokea vizuri, akaingia ndani na kufikia sebuleni. Mzee Anthony alikaa kwenye kochi dogo lilikuwa upande wa kushoto, na Bi. Matilda alikaa kwenye kochi kubwa. Yeye Malik alikaa kwenye kochi kubwa, ambapo aliweza kuwaangalia vizuri wazee wake.



    “Habari za hapa wazee wangu…” Kachero Inspekta akawaambia.



    “Nzuri, karibu sana…” mzee Anthony akasema,



    “Kwanza natanguliza tena, poleni kwa msiba…” Kachero Inspekta Malik amamwambia.



    “Ahsante sana,” wote wakajibu kwa pamoja.



    “Najua bado mna uchungu wa kufiwa na mtoto wenu mpendwa, lakini kwa sisi kama Jeshi la Polisi, inabidi tufanye kazi yetu ili kuupata ukweli!”



    “Hakuna shida baba, fanya kazi yako…” mzee Anthony akamwambia.



    “Narudia tena kuuliza swali lilelile nililowahi kuuliza mwanzoni nilipokuja hapa. Hivi Anita alikuwa na maadui?” Kachero Inspekta Malik akauliza.



    “Hapana, ni kama tulivyokueleza. Anita hakuwa na adui yeyote. Yeye alikuwa ni mtu mpole sana mwenye kufanya mambo yake kwa akili sana…” mzee Anthony akajibu.



    “Huyo mchumba wake alikuwa ni John Bosho sivyo?”



    “Ndiyo, alikuwa ni John Bosho…”http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    “Mchumba mwenyewe si mlikuwa mnamfahamu vizuri?”



    “Tulikuwa tunamfahamu, lakini si sana.”



    “Kwa nini unasema hivyo?”



    “Ni mtu wa kusafiri sana. Na hata kwenye msiba ndiyo vile hakuwepo. Alipopigiwa simu, akasema amesafiri…”



    “Na nyie mliridhika na mchumba huyo?”



    “Ilibidi turidhike, kwani watoto wa siku hizi wana uhuru wao wa kujitafutia wachimba, na siyo kama enzi zetu.”



    “Sasa nyie mnafikiri ni nani aliyehusika na mauaji ya Anita?”



    “Kwa sasa hatuwezi kumhisi mtu, kwa vile hatujui mwenendo mwingine wa marehemu…”



    “Labda alikuwa na wanaume wawili?”



    “Kwa hilo sidhani…”



    “Au ni imani za kishirikina?”



    “Kwa hilo ninaweza kufikiria hivyo. Inawezekana huyo mtu aliyemuua alikuwa na maana hiyo, lakini mengine tunawaachia nyie polisi kuifanya kazi hiyo.”



    “Sawa, nashukuru sana. Sisi polisi tutajitahidi kufanya upelelezi na apatikane!”



    “Ahsante baba…”



    Baada ya mahojiano yale, Kachero Inspekta Malik aliaga na kuondoka kurudi kituoni akiwa na makachero wenzake. Habari za mauaji ya kutisha na kufukuliwa kwa maiti ya Anita zikaendelea kutapakaa jijini Dar es Salaam. Vyombo vya Habari, redio, magazeti na televisheni vilitangaza tukio lile la kusikitisha, na kusisitiza kwa Jeshi la Polisi lijitahidi kufanya uchunguzi wa kina na kuweza kuwapata wale watu waliofanya tukio hilo la kishenzi! Ni kitendo ambacho kisingeweza kuvumilika kwa udhalilishaji wa ile maiti ya Anita iliyokuwa imeshazikwa!



    Kachero Inspekta Malik alipofika ofisini hakukaa sana, aliyapitia mafaili yaliyokuwa yanamkabili kwa harakaharaka na kuyamaliza. Halafu akajiandaa kwa safari ya kwenda eneo la Tabata Aroma, lilipo lile duka la kuuza dawa baridi za binadamu, ambalo lilijulikana kwa jina la Kishada Medics.



    ********



    DUKA la dawa la Kishada Medics, liko eneo la Tabata Aroma, na limepakana na Jengo la ghorofa la Aroma, lililoko umbali wa mita ishirini kutoka barabara kuu inayoelekea Segerea na kwingineko. Baada ya kufika eneo hilo, Kachero Inspekta Malik akalisimamisha gari sehemu ya maegesho yalipokuwa magari mengine yamepaki ya wateja wanaofika kupata huduma.



    Kabla ya kushuka ndani ya gari, Kachero Inspekta Malik akayatupa macho yake katika sehemu ile na kuweza kuliona duka hilo lililokuwa upande wa kushoto. Ndipo aliposhuka akiwa na ile bahasha iliyokuwa na bomba la sindano ndani yake, akaliendea kama mteja wa kawaida aliyekuwa anakwenda kujipatia mahitaji yake ya ununuzi wa dawa.



    Ni duka kubwa kiasi, ambalo limejengwa na kuwekwa mlango wa kioo, uliowezesha kuonyesha mpaka ndani. Yeye aliamua kwenda kufanya upelelezi kwa kuhojiana na muuza duka lile, ukizingatia tukio zima lilianzia pale kwa muuaji kununua bomba la sindano. Ukweli ni kwamba bahasha ile iliyokuwa imehifadhi lile bomba la sindano, ilikuwa na muhuri wa duka lile kudhihirisha kwamba aliyefanya mauaji ya Anita, alinunua mahitaji yake dukani pale, na kutimiza azma yake ya kuua.



    Kachero Inspekta Malik alipofika aliusukuma mlango na kuingia ndani ambapo alipokewa na hewa ya ubaridi iliyotoka kwenye kiyoyozi, na kwa kiasi fulani harufu ya madawa iliweza kusikika mle ndani. Pia, alikuwepo mwanadada mrembo, ambaye ndiye muuzaji wa duka lile. Akawa namwangalia Malik alivyokuwa anaingia ndani kwa hatua fupi, na kwa sauti nyororo ya kibiashara akamwambia:



    “Karibu kaka…”



    “Ahsante sana…” Kachero Inspekta Malik akasema huku akilikagua kwa macho duka lile. Halafu akamsalimia na kuanza mazungumzo yaliyompeleka pale.



    “Nikusaidie kaka…” mwanadada yule akamwambia.



    “Naomba msaada wako…mimi ni Kachero Inspekta Malik,” akajitambulisha. “Natokea kwenye Kituo cha Polisi Buguruni, na nimekuja hapa kwa kwa jambo muhimu…”



    “Karibu sana…” mwanadada yule akasema huku akimwangalia Malik kwa wasiwasi kidogo!



     Kachero!



    “Sijui unaitwa nani?” Kachero Inspekta Malik akamuuliza huku amemkazia macho.



    “Naitwa Paulina Mbagga.”



    “Oh, vizuri sana,” Kachero Inspekta Malik akasema huku akichukua kijitabu kidogo na kuanza  kuandika kile alichoona kinafaa.



    “Hili ni duka linalomilikiwa na nani?”



    “Ni duka la shemeji yangu….” mwanadada yule akajibu.



    “Basi, naomba unijibu maswali kadhaa nitakayokuuliza…wala usiwe na wasiwasi wowote!”



    “Unaweza kuniuliza tuu…”



    “Ni kuhusu yale mauaji ya mwanamke mmoja yaliyotokea kule Tabata Mawenzi siku tatu zilizopita…”



    “Mauaji?” Paulina akauliza kana kwamba hakumsikia.



    “Ndiyo, mauaji, natumaini umeyasikia…”



    “Ndiyo, nimeyasikia…” Paulina akasema na kuongeza.



    “Oh, Mungu wangu! Mauaji hayo yananihusu nini mimi?”



    “Hapana…usihofu wala hayakuhusu kabisa. Ila nakuuliza kwamba umewahi kuiona bahasha hii?” Kachero Inspekta Malik akamuuliza huku akimwonyesha ile bahasha iliyokuwa na muhuri wa duka lile.



    “Ndiyo…nimewahi kuiona. Bahasha hii iliyopigwa muhuri pamoja na nyingine zilizokuwa hapa, huwa nazitoa kwa wateja wanapokuja kununua dawa, kwani vipi?” Paulina akasema huku wasiwasi ukiendelea kumwandama!



    Mbona yamekuwa hayo tena?



    “Ina maana bahasha hii ni wewe uliyeitoa kwa mteja siku hiyo?” Malik akaendelea kuuliza.



    “Ndiyo ni mimi, kwa sababu hakuna mtu mwingine anayeuza hapa dukani zaidi yangu.”



    “Unaweza kukumbuka ulimuuzia nani, na lini huyo mteja wako? Pia, unaweza kukumbuka jina lake? Tafadhali naomba unisaidie…”



    “Nakumbuka siku tatu zilizopita, kunako majira ya saa nane za mchana hivi, alifika mteja mmoja hapa dukani…”



    “Baada ya kufika?”



    “Alipofika alinunua bomba moja la sindano. Yeye alikuja akiwa na gari lake, ambalo alilisimamisha kando ya barabara, karibu na sehemu ya maegesho. Baada ya kununua bomba hilo, akaondoka zake…” Paulina akasema lakini hakuweza kuelezea lile tukio la John Bosho kumuachia chenji baada ya kununua lile bomba la sindano na kutoa fedha kubwa!



    “Alikuja na gari gani?”



    “Kama sikosei ilikuwa ni Toyota Harrier ya rangi ya fedha…”



    “Aisee, vizuri sana, je, namba zake ulizisoma?”



    “Hapana, sikuzisoma, na wala sikuwa na sababu ya kuzisoma…”



    “Uliwahi kulijua jina lake?”



    “Silifahamu… na pia sikuona sababu za kumuuliza jina lake.”



    “Je, ukiiona sura yake utaikumbuka?”



    “Pia, siikumbuki sura yake kwa sababu wateja ni wengi sana huwa wanakuja hapa kununua dawa kila siku.”



    “Na kweli…” Kachero Inspekta Malik akasema huku akifikiria.Ukweli ni kwamba aliona kile alichosema Paulina, ni ya kweli, hivyo hakuona sababu ya kuendelea kumhoji.



    Kachero Inspekta Malik akamuaga Paulina, halafu akaondoka huku akiwa amegundua kuwa muuaji huyo alikuwa amenunua bomba la sindano katika duka hilo. Lakini hakuwa na la kufanya, kwani muuzaji hakuwa kumbukumbu zozote juu ya mnunuaji yule. Alipotoka hapo dukani, akaamua kuelekea Tabata Mawenzi, kwenye nyumba ile aliyokuwa anaishi marehemu Anita ili kuendelea na upelelezi.



            *********



    ALITUMIA kama dakika ishirini hivi kufika Tabata Mawenzi. Baada ya kufika, Kachero Inspekta Malik akalipaki gari lake upande wa pili wa uzio wa nyumba ile aliyokuwa anaishi Anita, halafu akashuka garini na kuiendea kwa mwendo wa taratibu. Alipokewa  na mama mwenye nyumba, Bi. Debora, ambaye alimkaribisha vizuri. Wote wakafuatana hadi walipoingia katika sebule nadhifu na kukaa kwenye sofa.



    “Karibu sana baba..” Bi. Debora akaendelea kumwambia Malik.



    “Ahsante sana…poleni kwa msiba…”



    “Ahsante, ndiyo hayo yametokea. Labda ni mipango ya Mungu aliyepanga Anita afe kwa kifo kile!”



    “Basi, ndiyo kama nilivyokueleza tokea mwanzo, mimi ni Kachero Inspekta Malik, ninayepeleleza juu ya mauaji ya mpangaji wako, Anita, ili tuweze kumkamata muuaji!”



    “Ni sawa baba, sasa nikusadie nini? Bi. Debora akamuuliza huku akimwangalia kwa huzuni!



    “Naulizia kwamba, je, vyombo vya marehemu bado viko chumbani?”



    “Ndiyo…vyombo vyake bado viko chumbani. Hakuna aliyevigusa, kwani tunasubiri ndugu zake waje kuvichukua punde msiba utakapomalizika!”



    “Funguo za chumba hicho unazo?”



    “Ndiyo, funguo ninazo mimi…”



    “Basi, naomba ufunguo wa chumba alichokuwa anaishi marehemu Anita. Nataka kuingia na kufanya uchunguzi huenda nikapata mambo mawili matatu.”



    “Hakuna tatizo baba…”

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kacheri Inspekta Malik alipewa ufunguo wa nyumba ya marehemu Anita. Akaufungua mlango na wote wawili wakaingia ndani ya hadi katika sebule nadhifu, kwa haraka Malik akatupa macho yake na kuanza kuchunguza, ambapo ndani ya sebule ile, palikuwa na seti moja ya sofa, kabati kubwa la vyombo, runinga, redio kubwa na vitu vingi tu. Hakika palikuwa pameenea ipasavyo na kuonyesha alikuwa ni mtu mwenye kujipenda sana na kuwa msichana wa kileo!



     “Tuingie chumbani sasa,” Malik akamwambia Bi. Debora, ambaye alionyesha kuwa na wasiwasi.



    “Sawa,  baba…” Bi. Debora akasema.



    “Usiogope mama…”



    “Hapana…siogopi…”



    Kachero Inspekta Malik akaufungua mlango wa chumbani, halafu wakaingia na kukiona kilikuwa ni chumba chenye ukubwa wa wastani. Upande wa kushoto palikuwa kitanda kikubwa cha futi sita kwa sita, pamoja na kabati la nguo lililokuwa kwenye kona ya chumba. Malik akaliendea na kulifungua huku Bi. Debora akiwa amesimama akimwangalia kila alichokuwa anafanya.



    Baada ya kulifungua, Malik akaanza kulipekua na kutoa nguo moja baada ya nyingine kwa umakini, na kuziweka kando. Alipomaliza kupekua, akakuta bahasha mbili za khaki na albamu moja kubwa ya picha, ambavyo vyote vilikuwa chini kabisa. Akavichukua na kumwendea Bi. Debora aliyekuwa bado amesimama. Akamwambia kwa sauti ndogo lakini iliyosikika:



    “Natumaini umeniona nilivyokua napekua ndani ya kabati la nguo…”



    “Ndiyo baba, nimekuona…” Bi. Debora akasema.



    “Hivyo basi, nachukua hii albamu ya picha pamoja na hizi bahasha mbili nilizozikuta ndani ya kabati. Nakwenda navyo kituoni kuzifanyia kazi, halafu nitarudi kesho.”



    “Unaweza kuchukua tu baba…” Bi. Debora akamwambia.



    Kachero Inspekta Malik akachukua ile albamu pamoja na zile bahasha mbili za khaki, halafu wote wakatoka hadi nje ya chumba kile cha marehemu Anita. Baada ya kutoka, Malik akaagana na Bi. Debora, kisha akapanda gari lake na kuondoka katika eneo lile la Tabata Mawenzi.



    *******



    Vijana wapatao sita walikuwa wameizunguka meza moja kubwa mfano wa meza ya kulia chakula, iliyokuwa na viti vitatu kila upande. Wote walikuwa wamemwangalia mtu mmoja, aliyekuwa amekaa katika kiti cha peke yake akiwa tayari kuwapa maelekezo.



    Ilikuwa ni ndani ya chumba maalum, kilichoko ndani ya bohari, katika maficho ya siri, eneo la Ubungo Machimbo ya Mawe. Ni kikundi hicho kilichokuwa kinaongozwa na John Bosho,  ambaye alikuwa amekaa kikao na vijana wake, Robi, Chikwala, kessy, Chogolo, Shabani na Muba. Alikuwa amewaita pale kwa dharura ili awahabarishe habari muhimu sana.



    “Jamani nimewaiteni tena hapa ili tupange mikakati yetu…”  John Bosho akawaambia vijana wake huku akiwaangalia kwa zamu.



    “Ni sawa, mkuu!” Chikwala akasema.



    “Tupo mkuu!” Robin naye akasema.



    “Tunakusikiliza!” Wakaongeza Kessy, Chogolo na Shabani kwa pamoja.



    “Mambo yanazidi kuwa mazito kwa upande wangu…” John Bosho akaendelea kuwaambia.  “Kwa nini mkuu?” Chikwala akamuuliza.



    “Natumaini nyote mnamfahamu Kachero Inspekta Malik Mkoba, wa Kituo cha Polisi Buguruni!”



    “Ndiyo, tunamfahamu…” akadakia Chikwala na kuendelea. “Hakuna asiyemfahamu yule kachero machachari anayejulikana katika jiji lote la Dar es Salaam. Kwani imekuwaje bosi?”



    “Basi, yeye ndiye mpelelezi wa kesi ya mauaji ya Anita, ambapo nimehakikisha mwenyewe baada ya kupata taarifa kwa mtu wangu aliyemwona alipokwenda kuchunguza katika eneo la tukio kule makaburini, wakati akilishughulikia lile tukio, baada ya sisi kulifukua usiku. Hivyo ndugu zangu, kama Malik akigundua kama ni sisi tunahusika, basi mjue tumekwisha, kwani polisi watagundua shughuli zetu zote tunazofanya!”



    “Aisee?” Chikwala akasema.



    “Mh!” Robi akaguna, lakini wale vijana wengine, Kessy, Chogolo, Shabani na Muba wakabaki wameyatumbua macho yao!



    “Basi, kuanzia sasa!” John Bosho akaanza kutoa maagizo kwa vijana wake. “Nakuteua wewe Chikwala, kumfuatilia Inspekta Malik popote pale alipo, na anapotembelea. Utakapopata mwanya mlipue mara moja! Sijui umenipata?”



    “Bosi, nimekupata vizuri sana, hakuna tatizo. Kazi hiyo nitaifanya na matokeo yake utayaona!”



    “Vizuri sana! Huo ndiyo moyo wa kijasiri! Unafaa kwa kazi hiyo!”  John Bosho akamwambia.“Tena nitaanza kumfuatilia leo hii, kwani sehemu zote anazostarehe nazifahamu sana!” Chikwala akaendelea kusisitiza na pia kujiamini.



    “Ok, nakuamini sana, basi fanya hivyo. Na nyie wengine mtabaki mkiwa macho na kujiandaa kwa jambo lolote ambalo linaweza kutokea. Pia, msizime simu zenu kwani wakati wowote mnaweza kupokea maagizo kutoka kwangu kadri mambo yanavyokwenda!”



    “Sawa bosi, tumekuelewa!” Wote wakasema kwa pamoja kudhihirisha wamemwelewa.



    “Ok, tunaweza kuendelea na shughuli nyingine!” John Bosho akawaambia vijana wake na wote wakamwelewa.



    Kikao kikafungwa.



    Wakati huo ilikuwa imetimu saa saba za mchana siku ya Jumamosi ya mtafutano!



    ******** 



    CHIKWALA Bwanga alikuwa ni kijana hatari anayeijua kazi yake, tokea alipojiunga na kundi lile linaloongozwa na mtu hatari sana, John Bosho. Alikula kiapo cha utii kwa kufanya kazi yoyote atakayopangiwa na bosi wake, hata kama ni kuifuata roho ya mtu kuzimu kama kulikuwa na uwezekano.



    Kamwe Chikwala hakuona hurunma yoyote kwa kuutoa uhai wa binadamu mwenzake, ili mradi afanikiwe katika maisha yake! Baada ya kutoka ndani ya chumba kile cha mkutano walipokuwa wanapewa maagizo na bosi wao, Chikwala  aliamua kuianza kazi ile mara moja. Walipofika nje ya bohari, walipanda gari lao, Toyota Corolla, na kuondoka eneo lile la Machimbo ya Mawe, na kurudi katikati ya jiji.



    Chikwala aliamua kushukia pale Buguruni Sheli, Barabara ya Nelson Mandela, na wenyewe wakaendelea na safari, kuendelea na mipango mingine. Akiwa amejiandaa vya kutosha, Chikwala alikuwa ameichimbia kibindoni, silaha yake aina ya bastola, iliyosheheni risasi. Ni silaha ambayo huwa anatembea nayo anapokuwa katika kazi muhimu sana inayopaswa kutumika kwa silaha inapobidi!



    Baada ya kushuka, akatembea kwa miguu kuifuata Barabara ya Uhuru hadi alipofika eneo la Soko la Buguruni, mkabala na kituo cha daladala kinachotumika kushusha abiria wanaotoka mjini na kwingineko. Lile ni eneo lenye pilikapilika nyingi za watu, wakiwemo wafanyabiashara na wasafiri wanaoshuka na kupanda daladala.



    Basi, yeye akaelekea katika baa moja ambayo kwa muda ule wa saa sita za mchana, ilikuwa na uhaba wa wateja, ukizingatia ulikuwa ni muda wa kazi. Baada ya kuingia ndani, Chikwala akatafuta sehemu nzuri iliyokuwa karibu na mlango wa kuingilia na kutokea, halafu akavuta kiti na kukaa huku akiangalia upande wa nje inapopita Barabara ya Uhuru. Ni sehemu ambayo pia aliweza kuwaona watu au askari waliokuwa wanaingia au kutoka ndani ya kituo kile cha polisi.



    Hivyo basi, Chikwala aliona pale ndiyo sehemu nzuri ya kuweza kuliwinda windo lake, Kachero Inspekta Malik, na akipata mwanya amlipue kwa risasi.  Ni kweli kwamba Chikwala aliweza kumwona Kachero Inspekta Malik alipokuwa anarudi kwa gari lake, akitokea Tabata, ambapo alikuwa amekwenda kumhoji Bi. Debora, mama mwenye nyumba aliyokuwa amepanga marehemu, Anita. Lakini hakuweza kufanya lolote kwa vile palikuwa na mkusanyiko wa watu wengi na atakachofanya ni lazima akamatwe.



    Baada ya kushuka garini, Kachero Inspekta Malik, ambaye hakujua chochote kilichokuwa kinaendelea,  aliingia ndani ya kituo cha polisi, na hakutoka tena, bali aliendelea na kazi nyingine zilizokuwa zinamkabili.  Hata hivyo Chikwala aliyekuwa anamwinda hakukata tamaa, kwani aliendelea kunywa kinywaji kama wateja wengine, na pengine akitaniana na wale wahudumu warembo wa baa ile, waliokuwa wamevalia nguo fupi zilizoyaacha maungo yao wazi.



    Ni hadi ilipotimu saa moja za usiku, ndipo Chikwala alipomwona Kachero Inspekta Malik akitoka na kuingia ndani ya gari lake, ambalo alilitia moto na kuliondoa kwa mwendo wa taratibu kwa kuifuata Barabara ya Uhuru hadi alipofika kwenye taa za trafiki, kwenye makutano ya barabara ile ya Uhuru na ya Nelson Mandela, gari la Malik likaifuata Barabara ya Mandela na kwenda kusimamishwa mbali kidogo na maegesho ya Kimicho Bar, iliyoko kando ya barabara hiyo ya Mandela, eneo la Buguruni.



    Chikwala ambaye alitoka ndani ya baa ile kumfuatilia, aliongeza mwendo kwa kutembea kwa miguu, ili amuwahi Malik asije akampotea na itakapobidi, ndipo angekodi teksi kumfuatilia. Chikwala alifanikiwa kuliona gari la Malik,  lakini alichelewa na kumwona akishuka na kuingia ndani ya baa ile ya Kimicho. Akamfuatilia ndani ya hiyo baa aliyoingia, halafu akaenda kukaa sehemu iliyokuwa na uficho, na kuendelea kumchunguza kwa makini kwa kila anachofanya.



    Hakika ilikuwa ni kazi ngumu sana kwa kumwinda mtu zaidi ya saa sita, lakini kwa mtu kama yeye alishazoea. Muda wote ule alikuwa ana silaha yake kibindoni, pamoja na simu, ambayo muda wote alikuwa akiwasiliana na John Bosho kwa kila hatua inavyokwenda. Hata hivyo baada ya kukaa kwa muda, Chikwala akaona afanye jambo moja. Akajifanya kama anakwenda msalani na kupita karibu na alipokuwa amekaa Kachero Inspekta Malik, ambapo palikuwa na giza kiasi lililosababishwa na mwanga hafifu wa taa ya rangi ya kijani iliyokuwa inamulika eneo hilo.



    Chikwala aliyatupa macho yake katika pande zote za ukumbi wa baa ile ya Kimicho. Wateja wengi walikuwa wakiburudika na vinywaji na wengine wakifuatilia kilichokuwa kinaendelea katika vipindi vya runinga, akiwemo Kachero Inspekta Malik. Utulivu ule ukampa mwanya Chikwala apange cha kufanya, ambapo ni kitendo bila kuchelewa!



    Akachomoa bastola yake!



    ********      



    AWALI Kachero Inspekta Malik alipolipaki gari lake mbali kidogo na Kimicho Bar, kando ya Barabara ya Nelson Mandela, ilikuwa imetimu majira ya saa moja na nusu za usiku. Alishuka na kulifunga gari lake vizuri, kisha akaondoka kwa mwendo wa taratibu na kuingia ndani ya baa hiyo iliyokuwa na ukumbi mkubwa wa kuchezea dansi.



    Mbali ya kuwa na ukumbi wa dansi, pia kulikuwa na kumbi nyingine na sehemu za kukaa wateja wanaofika kwa ajili ya kujipatia vinywaji. Baada ya kuingia, alitafuta sehemu nzuri ya kukaa, ndani ya ukumbi wa vinywaji, iliyokuwa kwenye kona, ambapo aliweza kuwaona watu waliokuwa wanaingia ama kutoka ndani ya baa ile.



    Huo ni utaratibu aliokuwa amejiwekea ili aweze kuona watu waliokuwa wanaingia na kutoka. Mhudumu, mwanadada mrembo wa haja alipomwendea, alimwagiza kinywaji, bia mbili aina ya Safari, ambayo alipendelea kunywa. Na baada ya kuhudumiwa, Kachero Inspekta Malik akaendelea kunywa taratibu huku akiangalia runinga iliyokuwa ikiendele na vipindi vyake, na pia akiangalia watu waliokuwa wakiingia na kutoka ikiwa ni moja ya sehemu yake ya kazi.



    Lakini wakati Kachero Inspekta Malik akiwa amezamisha mawazo yake katika kazi ile iliyokuwa inamkabili, ghafla akasogeza mkono wake wa kulia ambao uliigusa glasi iliyokuwa na pombe pale juu ya meza. Baada ya kuigusa glasi ile,  ikadondoka chini na kupasuka vipande vipande ambavyo vilitawanjika sakafuni! Malik akajiuliza imekuwaje? Akainama haraka kwa ajili ya kuangalia pale sakafuni jinsi glasi ile ilivyosambaratika. Ni kitendo kilichochukua kama sekunde moja hivi.



    Lakini ghafla tena, milio miwili kama ya nyuki ilimpitia karibu na kichwa chake, halafu ikafuatiwa na mlipuko wa risasi! Ni risasi ambazo ziligota ukutani nyuma yake na kuchimba katika ukuta na kumrushia vipande vya mchanga mwilini! Tuseme kama angechelewa tu, basi risasi zile zingefumua kichwa chake mara moja! Kutokana na milio ile ya risasi, watu waliokaa ndani ya baa, wakaanza kutawanyika kila mmoja kivyake.



    Kwa haraka Kachero Inspekta Malik akalala chini na kuanza kutambaa kama nyoka kuelekea mlangoni, huku akikwepa viti vilivyokuwa vimezagaa ovyo baada ya watu kukimbia. Alipofanikiwa kutoka nje ya baa ile, akamwona mtu mmoja akikimbia kwa kasi huku akirusha risasi ovyo angani, akikimbilia usawa wa kituo cha mafuta kilichoko karibu na taa za trafiki, kwenye makutano ya Barabara za Uhuru na Mandela.



    Watu wakaendelea kukimbia ovyo kila mmoja akitaka kunusuru maisha yake. Hakuna asiyejua madhara ya risasi. Mtu yule aliyekuwa anakimbia, ni Chikwala, ambaye alitaka kuvuka barabara kuelekea upande wa pili ili kuyawahi magari yaliyokuwa yanasubiri kuruhusiwa na taa ya kijani. Alipoanza kuvuka tu, ndiyo magari yalikuwa yameruhusiwa na taa, hivyo gari moja aina ya Mitsubishi Pajero lililokuwa upande wake, lilimgonga punde tu alipoutua mguu wake barabarani, akarushwa juu na kutua kando ya barabara!



    Gari lililomgonga Chikwala halikusimama zaidi ya kuongeza mwendo kuelekea eneo la Ubungo. Damu ikatapakaa pale barabarani alipoangukia Chikwala, huku umati wa watu ukikisanyika kumwangalia, wengine wakiwa ni vibaka waliokuwa na madhumuni ya kumsachi. Kachero Inspekta Malik hakuchelewa kufika sehemu ile alipoangukia huyo mtu na kuwasukuma watu waliokuwa pale na kumfikia  tayari kwa kuanza kumpekua na pia kumtambua ni nani?



    Baada ya upekuzi wa awali, Kachero Inspekta Malik alimkuta Chikwala akiwa na bastola moja aina ya ‘Star’ iliyokuwa imedondoka kando yake huku ikifuka moshi wa baruti. Lakini simu yake ya mkononi, ambayo nayo iliangukia mbali kidogo, iliokotwa na mmoja wa watu waliofika kwa ajili ya kutoa msaada, ambaye alitoweka nayo.



    Malik akaiokota ile bastola na kuihifadhi, halafu akaendelea kumchunguza na kumkuta bado akihema kwa mbali. Ili kupata machache kutoka kwake, akamwinua kichwa chake na kukiegemeza kwenye goti lake, na pia akimpatia huduma ya kwanza kwa kumpepea!



    “Haloo…vipi hali yako?” Kachero Inspekta Malik akamuuliza.



    “Oh…Oh…” Chikwala alikuwa anaguna kwa maumivu!



    “Hebu niambie…jina lako nani?” Kachero Inspekta Malik akaendelea kumuhoji.



    “Oh, naitwa Chikwalaaa…Oh!”



    “Chikwala?”



    “Ndi…yooo…oh!”



    “Nani kakutuma kufyetua risasi?”



    “Oh…nimetumwa…nikuue…oh!”



    “Umetumwa na nani?”



    “Hik… hik!…” Chikwalaa akatoa kwikwi na kuendelea.



    “Ni nani kakutuma?” Kachero Inspekta Malik akaendelea kumuuliza.



     “Nimetumwa na yule aliyemuua Anita…hik…hik…!” Chikwala akaendelea kusema kwa shida kuonyesha kutokuwa na matumaini ya kuishi tena, ukizingatia damu zilikuwa zinamtoka kwa wingi katika sehemu mbalimbali za mwili!



     “Chikwala…” Kachero Inspekta Malik akaendelea kumwambia na kuongeza. “Hebu niambie jina la mtu huyo aliyekutuma kuniua mimi tafadhali…”



    “Hik! Oh!” Chikwala aliendelea kutoa kwikwi mfululizo na hakuweza kusema kabisa. Akaendelea kutoa macho yake hadi alipokata roho na kukilaza kichwa chake!



    “Shenzi sana!” Kachero Inspekta Malik akasema kwa hasira! Ukweli ni kwamba alikuwa amechukia baada ya kushindwa kulipata jina la muuaji wa Anita!

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Hata hivyo muda siyo mrefu, gari moja la polisi aina ya Toyota Land Cruiser Hard Top, lilifika pale likiwa na askari polisi kumi. Kachero Inspekta Malik akajitambulisha, halafu akamwita kiongozi wa askari wale, aliyekuwa na cheo cha Sajini na kumpa maagizo.



    “Sajini!”  Kachero Inspekta Malik akamwita.



    “Afande,” akaitikia Sajini.



    “Pelekeni maiti hii katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, na muikabidhi, kwani huyu ni mtuhumiwa aliyefyetua risasi muda siyo mrefu, mimi nitakuja baadaye!”



    “Sawa afande…” akaitikia Sajini yule wa polisi.



     Askari wale hawakupoteza muda, wakauchukua mwili wa Chikwala na kuupakiza ndani ya gari lao, kuupeleka katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa ajili ya uchunguzi zaidi. Ule umati wa watu ukatawanyika baada ya askari wale kuondoka.



    Baada ya gari lile la polisi kuondoka, Kachero Inspekta Malik aliwasiliana na Mkuu wa Upelelezi, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi, Alfred Gonzo, ambaye naye hakukawia kufika katika eneo lile la tukio.



    Wakati huo askari wengine wa doria walikuwa wamejaa na na kulizunguka eneo lote la Kimicho Bar, kutokana na ile Mirindimo ya risasi iliyolipuliwa na Chikwala. Malik na Mkuu wa Upelelezi, Alfred Gonzo, wakishirikiana na askari wengine wakafanya uchunguzi wa awali, ambapo walifanikiwa kuyapata yale maganda mawili ya risasi. Wakayachukua na kuyaweka katika mfuko laini wa nailoni kisha wakarudi tena kituoni na kuyahifadhi katika ghala la silaha.



    Alfred Gonzo, ambaye alishtushwa na shambulio dhidi ya kijana wake, Kachero Inspekta Malik, hakuishia pale, bali alimwambia Malik waelekee katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili wakaikague ile maiti ya Chikwala, kama atakuwa ni mmoja wa majambazi wanaotafutwa na polisi kutokana na kufanya matukio mengi ya kihalifu.



    Walitumia gari la Malik na kuelekea Muhimbili, huku Malik akiwa na mawazo mengi sana juu ya mtu yule aliyemkosakosa kwa risasi! Malik alijiuliza kuwa, Je, ni nani aliyemtuma? Ama kweli kifo cha Anita kilikuwa na usiri mkubwa! Hata hivyo ilimbidi awe macho kwa kujilinda na watu wale, ambao ilionyesha walikuwa wamejizatiti!  Walipofika Muhimbili, Alfred Gonzo na Inspekta Kachero Inspekta Malik, walifikia sehemu ya mapokezi na kujitambulisha, ambapo waliruhusiwa kuuangalia mwili ule wa Chikwala.



    Mwili huo ulikuwa umehifadhiwa ndani ya chumba cha kuhifadhia maiti, ukiwa umelezwa katika machela. Wakauangalia kwa makini lakini hawakuweza kumtambua, hivyo wakaondoka na kusubiri mpaka kesho yake watakapojitokeza ndugu zake baada ya kutolewa taarifa juu ya mtu aliyegongwa na gari alipokuwa katika harakati za kukimbia baada ya kufyetua risasi katika tukio ambalo huwezi kuliita la kijambazi!



    Walipotoka katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, ilikuwa yapata majira ya saa tano za usiku. Foleni ya magari haikuwepo usiku ule kiasi cha kuwasaidia kupunguza urefu wa safari yao. Baada ya kumshusha Mkuu wa Upelelezi, Gonzo kituoni, Malik akaelekea  nyumbani kwake, Shariff Shamba, kupumzika kutokana na uchovu wa siku ile.



    Kachero Inspekta Malik alipofika nyumbani kwake, Ilala, Shariff Shamba, ilikuwa imetimu saa sita za usiku. Akalipaki gari ndani, sehemu ya uani, halafu akashuka na kuingia ndani, ambako aliwakuta wadogo zake, Toni na James wakimaliza kujisomea, na pengine kumsubiri yeye, akawasalimia na kupitiliza moja kwa moja hadi chumbani ili kufanya utaratibu wa kuoga na kuondoa uchovu wa mchana kutwa.  Baada ya kumaliza kuoga, hakuwa na hamu ya kula chakula kabisa, hivyo akajitupa kitandani huku akiwazia upelelezi wake!



    ********   



    SAA moja kabla Chikwala Bwanga hajafayetua risasi ndani ya Kimicho Bar, Buguruni, John Bosho alikuwa amebanisha mafichoni, sehemu maalum, akifuatilia nyendo za Chikwala. Kutwa nzima tokea alivyompa ile kazi ya kumfuatilia Kachero Inspekta Malik, alijaribu kuwa naye sambamba, na muda wote simu haikumtoka mkononi, akitaka kupata taarifa kwamba kachero huyo mahiri ameshauawa.



    Ni mpaka ilipotimu majira ya saa mbili za usiku, ndipo Chikwala alipomjulisha kuwa alikuwa anamfuatilia Kachero Inspekta Malik, ambaye alikuwa ameingia ndani ya Kimicho Bar, Buguruni muda siyo mrefu.



    “Bosi…nimemwona Malik…” Chikwala alimjulisha baada ya kumpigia simu.



    “Unasema umemwona?” John Bosho akamuuliza!



    “Ndiyo…ameingia Kimicho Bar…” Chikwala akamwambia.



    “Usifanye makosa, mfuatilie na kumlipua hukohuko”!



    “Nitafanya hivyo mkuu!”



    “Ok, baada ya kufanikisha unijulishe!”



    “Nitakujulisha bosi…”



    Baada ya mawasiliano yale, John Bosho akawa anaendelea kusubiri matokeo. Lakini baada ya nusu saa nzima kupita, tokea awasiliane na Chikwala, akajaribu tena kumpigia simu, ambayo iliita kwa muda halafu ikapokewa na mtu mwingine!



    “Chikwalaaa…”  John Bosho akasema kwa hamaki!



    “Hapana…mimi siyo Chikwala…” upande wa pili ukasema na kumshtukiza John Bosho!



    “Ni nani sasa?”



    “Ni msamaria mwema tu…”



    “Mh, mbona sikuelewi?”



    “Utanielewa tu…sikiliza!”



    “Unasema?”



    “Hii simu ni ya mtu aliyegongwa na gari muda siyo mrefu…”



    “Amekufa?”



    “Ndiyo, nafikiri amekufa…na maiti yake imechukuliwa na askari polisi kupelekwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili…”



    “Amechukuliwa na polisi?”



    “Ndiyo, kwani ni ndugu yako?”



    “Ni ndugu yangu…”



    “Basi, mfuatilie Muhimbili…”



    “Wewe ni nani…halooo…”



    “Nenda Muhimbili…kwaheri…”  mtu yule akasema.



    Halafu akaizima ile simu!



    John Bosho akawa kama mwendawazimu baada ya kuzisikia habari zile. Na ile ilikuwa ni kwa sababu walikuwa wameshaongea na Chikwala muda siyo mrefu na kusema kwamba alikuwa anamfuatilia Kachero Inspekta Malik amlipue! Sasa imekuwaje tena?



    Hakupata jibu!



    John Bosho alikurupuka na kuwasiliana na vijana wake wawili, Robi na Chogolo, ambao baada ya kuwapata akawaelekeza tukio lilivyotokea na walipolifuatilia katika vyanzo vingine vilivyokuwa Buguruni, ndipo walipozipata habari kamili! Chikwala alikuwa amekufa baada ya kugongwa na gari wakati alipokuwa anakimbia baada ya kufyetua risasi ndani ya Kimicho Bar.



    John Bosho akawapa majukumu vijana hao, Robi na Chogolo, kwa kutumia simu yake ya mkononi, kuwa wamfuatilie hatua kwa hatua, Kachero Inspekta usiku uleule, mpaka nyumbani kwake, Shariff Shamba, Ilala na kuhakikisha wanamwingilia kigaidi ndani kwake na kumlipua mara moja! Kamwe hakupenda wampe nafasi hata kidogo, kwani angewaharibia mambo yao!



    Vijana wale hatari walijiandaa, halafu wakaenda katika maficho yao na kuchukua silaha zao, bunduki moja fupi, aina ya Uzi Gun, pamoja na bastola moja. Wakapanda gari lao, Toyota Corolla na kuelekea nyumbani kwa Kachero Inspekta Malik, ambapo walikuwa wanapafahamu. Kwa vile walikuwa na ufunguo wa bandia, hawakuwa na wasiwasi wowote wa kuingia ndani ya nyumba hiyo iliyokuwa katika makazi ya watu na kumpata mhusika wao pasipo kushtukiwa na mtu yeyote!



    Usiku ule kulikuwa kimya kabisa, na baada ya kutoka huko kwenye maficho yao walipokwenda kuchukua silaha zao, Robi alikuwa anaendesha gari lile kwa mwendo wa kawaida akiifuata Barabara ya Uhuru, kama anaelekea katikati ya jiji. Muda huo wa saa saba za usiku, magari yalikuwa ni machache sana nay a kuhesabika tu barabarani, na walipofika eneo la Bungoni, Ilala, Robi alikata kushoto na kuifuata barabara nyingine ya udongo iliyokuwa inakatiza katika makazi hayo ya watu, kuelekea eneo la Shariff Shamba.



    Waliifuata barabara hiyo, ambayo ilikuwa na nyumba  za wakazi pande zote. Kwa mbali kama mita ishirini hivi, waliiona nyumba ya Kachero Inspekta Malik Mkoba, ambayo  ilikuwa imezungukwa na uzio wa ukuta na mbele yake kukiwa na geti kubwa la chuma. Wakaiendea nyumba hiyo kama vile walikuwa ni wapiti njia tu wanaopita kwa gari lao! Mtaa huo ulikuwa kimya kabisa, labda na mambwa koko na mapaka shume yaliyokuwa yakizunguka kwenye mapipa ya takataka kutafuta makombo ya vyakula.



    “Nafikiri unaiona nyumba ya Malik?” Chogola akamwambia Robi aliyekuwa anaendesha gari.



    “Nimeiona, si hiyo hapo mbele?” Robi akasema huku akiiangalia kwa makini



    “Sasa usisimaishe gari hapo karibu, twende mbele kidogo…” Chogolo akamwambia.



    “Ni kweli, ngoja nikasimame pale mbele, karibu na mti wa mkungu, ili tuweze kupoteza lengo…”



    “Ni jambo la maana…tusipende adui atutambue haraka!”



    Robi akaendelea kuendesha gari kuelekea mbele kidogo, halafu akalipaki gari karibu na mti mmoja mkubwa wa mkungu. Wakabaki ndani ya gari kwa muda huku wakijipanga cha kufanya, kabla ya kumwingilia kachero huyo waliokuwa wanamfuatilia!



    “Unajua kabla ya kumwingilia Malik, lazima tusome mazingira?” Robi akamwambia Chogolo.



    “Ni kweli, lazima tujue pa kuingilia na kutokea, si unajua mtu huyo ni askari mahiri? Lazima tujipange…” Chogolo akasema.



    “Nimeona hapo nje kwake, karibu na uzio kuna mti mmoja wa mwembe, ambao umezungukwa na miti mingine ya muarobaini…”



    “Ni kweli, hata mimi nimeuona…”

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Tena una matawi makubwa yanayoshukia ndani . Hivyo hapo ndipo tutakapopitia na kuingia ndani kama nyani vile!” Robi akamwambia mwenzake.



    “Poa, kama ni hivyo, basi tujiandae kwenda, akitokea mtu wa kututibulia mpango wetu tu, ni kumlipua mara moja!” Chogolo akasema huku akiikamata bunduki yake vizuri!



    Wakajiandaa kushuka!



    ********







    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog