Search This Blog

Thursday 27 October 2022

UHASAMA - 4

 









    Simulizi : Uhasama

    Sehemu Ya Nne (4)





    Sekunde zilipishana dakika zikayoyoma siku nazo zikapuputika ukafuata mwaka, Hemedy na Hilda wakaingia darasa la sita, darasa hilo nalo wakalivuka, hivi sasa walikuwa darasa la saba, Mkuu wake na Hilda aliishi na watoto hao kama wanae wa kuwazaa, aliwapenda na kuwapa kila wanachokitaka, Hemedy hakuwahi kubugudhiwa wala kunyanyaswa kwa kitu chochote na mwanamke huyo, nae pia alimchukulia ni mjukuu wake kama alivyomchukulia Hilda, alimpenda na kumfanya kama ni mwenye kuwa na udugu nae, pamoja na yote hakuacha kuwasisitizia kuhusu swala la masomo, aliwachunga sana kwa jambo hilo.



    Kipindi chote hicho, Mata na Moto hawakuuacha mpango wao wa kuiyondoa roho ya Hemedy, walijitahidi kujua mahali ambapo mtoto huyo yupo hadi wakafanikiwa kujua, haikujulikana walijua vipi, ila taarifa zote walikuwa nazo juu ya mtoto huyo, wakapanga kutuma watu watakaoenda huko huko alipo ili kuwatimizia adhma yao waliyoipanga, wakawatafuta wale vijana wawili waliofanya nao mauaji ya familia ya Mheshimiwa, haikuwa tabu kuwapata maana Mata alijua ni wapi pakuwapata watu hao.



    Aliwaita katika nyumba yake mpya iliyokuwa maeneo ya Makorora Center baada ya ile nyumba yake ya kwanza kuiuza na kununua nyumba maeneo hayo, ilikuwa ni nyumba ya thamani kiasi chake, kipindi hiki alikuwa ameoa na alifanikiwa kupata mtoto mmoja wa kiume mwenye umri wa mwaka mmoja na nusu, aliwakaribisha katika bustani ya nyumba hiyo na kukaa hapo pamoja.



    “Ni mudu mrefu thana hatuja onana" Mata alifungua maongezi.



    “Ni kweli, ila yote hayo yamesababishwa na mishe mishe kuwa nyingi" alijibu kijana mmoja huku mwenzake akiwa kimya.



    “Ok, kuna kadhi nataka niwape muifanye na ninajua nyinyi mutaifanya kwa uangalifu mkubwa thana"



    “Ndio, wewe tuambie hiyo kazi ni kazi gani halafu tujue tutaifanyaje"



    “Ni kadhi moja rahithi thana, kuna roho ya mtoto inatakiwa kutenganishwa na mwili wake, na nadhani hata nyie huyo mtoto mnamjua"



    “Ni mtoto gani huyo"



    “Kama mna kumbukumbu ndhuri, kuna kipindi niliwahi kuwachukua tukafanye mauwaji ya yule Mzee Mheshimiwa, tukawaua wote na kuondoka dhetu, ila haikuwa vile tulivyodhani, kumbe yule mtoto hakufa na ndio huyo ninaetaka muka mtoe roho yake"



    “Ni muda sana, sasa sidhani kama sura yake tunaweza kuikumbuka, labda utupe picha yake"



    “Hilo thio tatidho, thubirini nakuja thatha hivi" aliongea hivyo na kuingia ndani, baada ya dakika moja akarudi mahala hapo huku mkononi akiwa na picha.



    “Mtoto mwenyewe ni huyo hapo, hiyo picha ni yadhamani kidogo ila naamini thura yake haijabadilika thana, mnawedha kumjua mkimuona" aliongea hivyo huku akiwakabidhi hiyo picha, waliipokea na kuiangalia wote kwa pamoja.



    “Hakuna shaka, hii ni kazi rahisi sana, chamsingi ni wewe kutupa maelekezo ya wapi anapatikana na ungependa ichukue siku ngapi hadi kifo chake"



    “Tuelewane kwandha ni malipo kiasi gani kwa kadhi hii"



    Walielewana kiasi watakacho kwa kazi hiyo na kulipwa nusu huku nusu nyengine wakiahidiwa kupewa baada ya kukamilisha kazi hiyo, baada ya hapo walipewa maelekezo ya wapi anapatika mtoto huyo, zaidi Mata akawapa na gari watakayoitumia kipindi chote watakachokuwa wakiifanya kazi hiyo, waliahidi ndani ya wiki tu itakuwa kazi imekamilika.



    Daresalam.



    Siku moja wakati Hemedy anatoka shule akiwa amechelewa baada ya kufanya kazi walioachiwa yeye na wenzake wa darasa lao, walicheleweshwa kama lisaa limoja hivi, ikiwa kipindi hicho wenzao wamadarasa mengine tayari wamerudi majumbani kwao, Hilda yeye majira hayo, alikuwa yupo nyumbani kwao, yeye alikuwa akisoma na Hemedy darasa moja ila mikondo ilikuwa ni tofauti.



    Hemedy akiwa njiani anaelekea nyumbani, ghafla mbele yake ilisimama gari aina ya Mark 11 Grand, ikampigia honi Hemedy aliekuwa bado nyuma ya hiyo gari baada ya kumpita, honi hiyo iliaashiria kuwa atakapofika karibu na hiyo gari, asogee karibu yake maana mmiliki wa hicho chombo ni mwenye kumuhitaji, alilielewa hilo, alifika hadi dirishani upande wa abiria, alipofika pale, alibaki na mshangao baada ya kuziona sura ambazo aliwahi kuziona mahala fulani, swali likabaki, aliwaona wapi watu hao, akiwa bado anashangaa, akajikuta akivutwa ndani ya gari hilo, ni kitendo cha sekunde tatu tu, akawa yupo ndani ya gari hilo, walikuwa ni vijana waliotumwa na Mata wamuue Hemedy, bila kusubiri chochote, gari ilitiwa moto na kuondoka mahali hapo kwa kasi ya ajabu. Watu walioshuhudia tukio hilo, walibaki midomo wazi huku wengine wakiwa wameshika vichwa vyao kwa taharuki, walitaharuki kwa mambo mawili, kwanza ni kutekwa kwa mtoto huyo, pili ni jinsi gari lilivyoondolewa mahali hapo kwa kasi, wakasahau hata kuzisoma namba za hilo gari..









    Wakati wakiendelea na safari yao, majira hayo walikuwa wapo mbali na makazi ya watu. Mmoja wapo alimdhibiti Hemedy huku mwengine akiendesha gari. Walipanga wakamuulie mbali huko halafu na wao warudi Tanga siku hiyo hiyo. Wakiwa bado waposafarini kuelekea huko walipopanga wao. Ghalfa mbele yao palitokea gari aina ya Nissan Murano, gari hiyo ilisimama mita chache mbele yao baada ya kuwapita kwa kasi ya ajabu, kama sio kuchuna breki kwa nguvu na kuifanya gari yao iserereke, basi wangeenda kuigonga hiyo gari na kungetokea ajali kubwa sana ambayo ingeacha damu mahali hapo huku ikipambizwa na vipande vya miili ya watu hao.



    Bilashaka watu waliokuwepo kwenye gari iliyovamia safari yao, walijitolea kufa na kupona, inamaana wao hawakujua kufanya hivyo ni kusababisha ajali ambayo hata wao ingewadhuru kwa kiasi kikubwa? Wavamizi hao walishuka ndani ya gari lao kwa haraka mno na kuwaweka chini ya ulinzi wale watekaji, wakawaamrisha watoke nje ya gari na wao wakafanya hivyo huku wakiwa mikono yao wameiweka vichwani mwao, Hemedy walimuacha ndani ya gari, walitoka wenyewe wawili tu. Wavamizi hao walipeana ishara na mmoja wapo akatoa simu na kuiminyaminya na kuiweka sikioni mwake, akasubiri kwa sekunde kadhaa kisha akaanza kuongea.



    “Mkuu, tumefanikiwa kuwapata na hivi sasa tumewaweka chini ya ulinzi kwahiyo tunasubiri amri yako tu"



    “Nyie msiwadhuru kwa chochote, chakufanya ni kuwapa onyo tu kuwa waache kumfuatilia huyo mtoto na waondoke kwenye huu mji haraka iwezekanavyo, halafu muwaambie wakampe salamu huyo aliewatuma kuwa aachane na hayo mawazo yake ya kutaka kumuangamiza huyo mtoto na wakamuambie kuwa, mipango yake yote inajulikana, kwahiyo asije akafikiria tena kufanya hivyo, akijaribu kufanya tena hivyo, itamgharimu yeye na hao atakao watuma" sauti ya kwenye simu iliongea hivyo.



    “Sawa mkuu, na huyu mtoto nae?" Jamaa huyo aliuliza.



    “Huyo mtoto atarudi mwenyewe alipotoka kwahiyo nyie muacheni" mtu wa upande wa pili alijibu.



    “Sasa mkuu, huoni kama hiyo itakuwa ni hatari kwake, maana huku alipo na nyumbani kwao ni mbali sana, halafu isitoshe hizi njia sidhani kama atazijua"



    “Kwahiyo unanifundisha kazi?" sauti yenye mamlaka iliunguruma kwenye simu.



    “Hapana mkuu sikufundishi kazi" jamaa alijibu kwa uoga.



    “Ila?"



    “Nilikuwa najaribu kushauri tu mkuu, nisamehe sana"



    “Au unadhani mimi sijui kuwa huyo mtoto hapajui huko, au unadhani mimi sijui kama hazijui hizo njia za kurudi nyumbani kwao? Mimi ndio najua kuwa huyo mtoto anatakiwa awe vipi na sio nyie. Ok fanyeni kama nilivyo miagiza, hao wajinga wapeni hizo salamu wakamfikishie aliewatuma halafu huyo mtoto muacheni arudi mwenyewe nyumbani kwao hata pawe na umbali kiasi gani ila nyie hakikisheni anafika salama kwa kumuwekea ulinzi, ila sasa asijue kama kuna watu wapo nyuma yake wanamfuata. Kumbukeni huyo mtoto Kiongozi anamuhitaji kuliko kitu chochote, kwahiyo hakikisheni usalama wake unakuwa ni mkubwa"



    “Sawa mkuu tumekuelewa, tutafanya kama ulivyotuagiza"

    Baada ya hapo alikata simu na kuwaangalia jamaa hao waliomteka Hemedy.



    “Oya nyie washkaji, sote hapa ni vijana na ninadhani mnaakili timamu, akili mlizokuwa nazo zinauwezo wa kuzingatia yale ambayo mnayoambiwa, kwahiyo kwa haya ambayo nitakayowaambia sasa hivi, bila shaka mtayazingatia ikiwa mnapenda kuishi, ni hivi, uwezo wa kuwafanya chochote tunao hata kama tukiamua tuweke silaha chini tupigane mkono kwa mkono, tunamihakikishia sekunde tano nyingi, mtakuwa tayari kuvikwa sanda kwaajili ya kupelekwa kupumzishwa makaburini, tunaomba muwe waelewa, chakufanya sasa hivi ni kuondoka katika mji huu na kurudi mlipotoka, mkifika mpeni salamu huyo aliewatuma kuwa, aache na afute kisha asifikirie tena kupanga mipango ya kumdhuru huyu dogo kwanjia yoyote ile, akijaribu hata kuwaza kumdhuru huyu dogo, basi ajue atakufa kifo ambacho hata yeye mwenyewe pia kitamshangaza.....”akamgeukia yule mwenzake “Kanu, nenda kamtoe yule dogo kwenye gari"



    Huyo jamaa mwengine aliejulikana kwa jina la Kanu, akaenda kwenye gari na kumtoa Hemedy kwenye siti za nyuma za gari hiyo. Hemedy muda wote huo alikuwa akitetemeka asijue watu hao ni wakina nani na wanataka nini, kibaya zaidi kilichomchanganya ni kuhusu sura za wale watu wamwanzo, alihisi kama vile alishwahi kuziona sehemu flani ila hakuwa na kumbukumbu nzuri kuwa aliwahi kuziona wapi sura hizo.



    Nikama vile kuona kwake bastola ni jambo ambalo amelizoea, maana ni mara nyingi sasa aliziona sehemu tofauti tofauti, tena zote zikiwa na malengo na yeye, pamoja na kuziona sana lakini bado woga ulikuwa upo pamoja nae, alijua fika kifaa hicho hakina masihara pale kunapotumwa kuondoa uhai au hata kumjeruhi mlengwa, akabaki ni mwenye kulia tu muda wote huku akiomba msamaha kwa kosa asilolijua.



    Wavamizi hao wakawaruhusu watekaji wa Hemedy waondoke huku wakiwakumbusha kuwa wampelekee salamu bosi wao aliewatuma. Watekaji wakaondoka huku wakimshukuru mungu kwa kuokoka katika mikono ya hao wavamizi, walipanga waondoke jioni hiyo hiyo kurudi Tanga kama walivyohusiwa, wakaondoka mahala hapo na kuwaacha watu watatu tu, yani Wale jamaa wawili na Hemedy.



    Jamaa hao baada ya kuhakikisha watekaji wamefika mbali na wao wakaingia kwenye gari yao na kumuacha mtoto huyo akiwa amesimama asijue ni nini hatma yake juu ya kutekwa kwake, jamaa hao wakaondoka huku wakimuacha Hemedy akiwa haelewi mambo yanavyoenda akabaki akijiuliza. ‘inamaana watu hao walipanga kuja kumtelekeza mahala hapo au walikuwa na lao ambalo wamelipanga juu yake?’ hapo ndipo uoga ulipomzidi, akawaza kuwa watu hao walipanga kumuua kwa staili hiyo ya kumuacha hapo kisha kumshambulia kwa chochote kile watakachoona kwao kinafaa kumshambulia nacho.



    Alitulia kwa dakika kadhaa kishaapo akaanza kurudi na njia ile ile aliyoletwa nayo, aliogopa sana maana barabara nzima alikuwa yupo pekeake, hakukutokea gari ya aina yoyote wala mtu wa aina yoyote njiani hapo, hapo ndipo alipoiyomba msaada zaidi miguu yake imsaidie kukimbia, nayo haikuwa na kiburi eti kwamba igome kufanya kile ambacho mmiliki ametaka, akawa anakimbia huku akiangalia nyuma kila mara, alikimbia hadi akachoka, akawa anatembea nusu, nusu anakimbia.



    Majira hayo, jua tayari lilishazama na kufanya giza liitawale dunia, akaanza kukimbia tena safari hii alikimbia huku akilia, maana alishakimbia zaidi ya lisaa limoja na nusu lakini bado hakuweza kufika kule anapopataka. Baada ya kukimbia kwa nusu saa nyengine, ndipo alipopata matumaini ya kuishi pale alipoona magari kadhaa na nyumba kadhaa zilizokuwepo kando ya barabara hiyo huku magari hayo yakiendelea na safari zake.



    Majira hayo yalikuwa ni saa moja na nusu usiku, alitembea hadi akafika katika kituo cha daladala, akajisachi mfukoni na kukuta akiwa na elfu moja mfukoni mwake, akapanda daladala iliyompeleka hadi kwao Kinondoni, kisha akatembea kwa miguu tu hadi nje ya nyumba yao, muda huo ilikuwa ni saa mbili za usiku, akaingia ndani ya nyumba hiyo huku akiwa na wasiwasi wa kuulizwa kuwa alikuwa wapi muda wote.



    “We Hemedy, tulikuwa tunakusubiri muda wote huo, ulikuwa upo wapi?" alikutana na swali hilo mara baada ya kuingia sebuleni, Hilda ndie alikuwa muulizaji wa swali hilo.



    “Nilikuwa nipo shule, ilipofika saa kumi na mbili ndio nikaondoka kuelekea kituoni kupanda gari ila sasa kila gari lililokuja lilikuwa limejaa hadi kuja kupata gari ilikuwa muda ushaenda sana halafu pia foleni imechangia kuchelewa" Hemedy aliongea hivyo huku akiuwelekea mlango wa chumbani Kwake.



    “Muongo Hemedy wala haukuwa shule, wewe kuna sehemu zako umetoka huko ndio unanificha mimi" Hilda aliongea kwa hasira kiasi na kumfanya Hemedy aghairishe kuingia ndani ya chumba chake na kumgeukia yeye, hakuelewa imekuaje hadi mtoto huyo wa kike kuwa katika hali hiyo, kwanza alishangaa wakati akiingia hapo sebuleni alipomuona binti huyo alivyovimba kwa hasira, haikuwa mara ya kwanza kumnunia, mara nyingi alifanya hivyo pale alipomuona Hemedy akiwa amekaa au amesimama na mtoto wa kike kwa muda mrefu wakiwa shule, basi binti huyo anakuwa ni mwenye kununa tu kwa siku nzima na kisa kinachomfanya anune kisijulikane.



    “Sasa Hilda wewe unahisi mimi nilikuwa nipo wapi, mji wenyewe huu mimi siujui, mimi niwa nyumbani na shuleni tu mwenyewe unajua, asa ni vipi uniambie natoka sehemu zangu ninazozijua halafu nakuficha?"



    “Haya umeshinda, chakula kipo kwenye meza, kama unanjaa unaweza kwenda kula" Hilda aliongea hivyo huku akigeukia upande ilipokuwa luninga.



    “Sawa, vipi anti amerudi?" Hemedy alimuuliza.



    “Hajarudi bado" alijibu huku akiongeza sauti ya redio ambayo imeunganishwa na luninga kuashiria kuwa hataki tena maongezi na kijana huyo. Hemedy alisikitika tu na kuingia chumbani kwake maana alishajua kuwa tayari mtu huyo ameshakasirika. Hilda aligeuza macho yake kuangalia kule alipoingia Hemedy baada ya kusikia sauti ya kufungwa kwa mlango, aliuwangalia kwa sekunde kadhaa kisha akarudisha macho yake kwenye luninga, akapunguza sauti ya redio na kuendelea kuangalia kinachoonekana kwenye luninga hiyo.



    Saa 4:20 Usiku. Tanga.



    Wale waliotumwa na Mata kwenda kumuangamiza Hemedy, Waliingiza gari ndani ya uzio wa nyumba ya Mata, wakashuka kwenye gari na kumuona Mata akiwa amesimama kwenye kibaraza cha nyumba hiyo, inaelekea aliujua ujio wa watu hao ndio maana akawasubiri hapo. Akawapa ishara ya kuwa waelekee kwenye bustani na wao wakafanya hivyo huku akiwafuata nyuma, walipofika kila mmoja akachukua nafasi yake kwenye viti vilivyokuwa hapo na kukaa.



    “Enhee, nipeni taarifa, vipi mshamalidha kadhi niliyowatuma?" Mata aliwauliza vijana hao.



    “Bosi yule mtoto analindwa na ulinzi mkali sana" jamaa mmoja wapo alijibu.



    “Analindwa!! Analindwa na nani?" Mata aliuliza kwa tahamaki.



    “Wakati tukiwa tupo nae tukitafuta sehemu nzuri ya kumuulia, ghafla mbele yetu palisimama gari, yani gari hilo lilituziba njia, watu hao wakashuka na kuwahi kutuweka chini ya ulinzi, mmoja wa watu hao, akaongea na mtu kwenye simu kama dakika tano hivi, alipomaliza alitupa onyo na kuturuhusu tuondoke halafu wao wakabaki na yule dogo"



    “Onyo gani walilomipa, halafu watu hao mnawajua?"



    “Hapana hatuwajui, ila tu walituachia maagizo ya kukuletea wewe, walisema kuwa usijaribu tena kumfuatilia yule mtoto na kama ukifanya hivyo basi ndio unaweza ukawa mwisho wa maisha yako na hao utakao watuma tena"



    “Kwahiyo nyie mmeshindwa hata kupambana nao, mkakubali kirahithi rahithi wamitishe hivyo?"



    “Hapana, watu hao wanaoneka wanajiweza kimapigano hata hivyo pia walituwahi, kwahiyo hatukuwa na ujanja wowote wa kuwadhibiti"



    “Thawa, thubirini nakuja thatha hivi" Mata aliongea hivyo na kuingia ndani ya nyumba na baada ya dakika moja alirudi hapo huku akiwa mkonono ameshika bastola, bila kuuliza chochote, aliwafyatulia risasi mbili mbili kila mmoja na kuwafanya watu hao wasiache hata usia wa mwisho mahala hapo, hakukuskika milio ya risasi kutokana na bastola hiyo kuifunga kiwambo cha kuzuia sauti.



    “Washendhi nyie" hilo ndio neno alilomalizia nalo, kisha akarudi tena ndani na kutoka na funguo za gari, akaichukua miili hiyo na kuingiza kwenye buti la gari walilokuja nalo, alipomaliza, akaenda kufungua geti na kulitoa gari hilo nje ya nyumba hiyo, akarudi tena kulifunga geti na kuingia kwenye gari hilo, alipanga miili hiyo akaitupe kwenye daraja la Amboni, daraja ambalo linasifika kwa kuwa na mamba wengi na wakali, akapanga kuitupa miili hiyo hapo ili iliwe na wanyama hao wakali.



    Akaanza safari usiku huo huo kwenda kufanya kile alichopanga, wakati akiwa yupo maeneo ya Chumvini, mbele yake aliona gari la polisi limepaki pembeni huku askari wakiwa wamesimama nje ya gari hilo huku wakiwa wameshika bunduki, polisi hao walikuwa kwenye doria usiku huo. Polisi mmoja alilipiga mkono gari la Mata na yeye hakuwa nabudi zaidi ya kulipaki gari hilo pembeni, wasiwasi, uoga na vyengine vifananavyo na hivyo, vili mpata kwa pamoja, hakuelewa atawajibu vipi askari hao pindi wakiziona maiti zilizokuwa ndani ya buti la gari lake.



    “Za saa hizi?" askari mmoja alimuuliza baada ya kumfikia kwenye gari lake kilipo kioo cha upande wa dereva.



    “Thalama tu afande" Mata alionekana ni mwenye wasiwasi mbele ya askari huyo ambae alianza kumtilia mashaka.



    “Unatoka wapi na unaelekea wapi usiku huu?"



    “Natoka Tanga mjini naelekea Amboni"



    “Kuna nini huko?" swali hilo lilimfanya Mata atulie kwa sekunde kadhaa bila kujibu hapo ndipo askari huyo alipozidisha mashaka yake kwa mtu huyo.



    “Nimepigiwa thimu kuwa mwanangu amedhidiwa huko, kwahiyo naenda kumchukua nimpeleke Hothpitali ya Bombo"

    Alipata ujasiri wa kujibu hivyo na kumfanya askari huyo kumuangalia kwa muda kisha akaanza kutizama ndani ya gari hilo, alipoona hakuna chochote chakutilia mashaka ndani humo, akamuomba atoe loki ya kwenye buti ili aangalie na huko.



    “Thatha afande, mimi nachelewa mwanangu anaumwa thana na hivi thatha nimepigiwa thimu kuwa kadhidiwa, naomba tu uniruhuthu niondeke afande" Mata aliongea huku akiwa analia machozi huku mikono yake akiwa ameifumbata kifuani kwake kama mtu anaeomba mungu, haikujulikana kuwa alikuwa akilia kwa uoga au alikuwa anaigiza.



    “Aloo nimesema toa loki ya buti, usinililie mimi, Alaaa!!" Afande huyo aliongea kwa ghazabu kiasi kwamba akamtisha hadi Mata, hakuwa na jinsi nyengine, akatoa loki na kubaki akimuomba mungu wake kutokee muujiza maiti hizo zisionekane na afande huyo.

    Askari bila kuchelewa, alizunguka hadi nyuma ya gari hilo na kuliendea buti la gari kwaajili ya kulifungua..
    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/







    “AFANDE, muache aende bwana, anachelewa" hiyo ilikuwa ni sauti askari mwengine ikimuambia yule askari aliekuwa akitaka kulifungua buti la gari la Mata. Askari huyo akaghairisha kufungua buti na kumfuata Mata kule mbela na kumruhusu aende, hakika hakuamini hata kidogo kuwa ni kweli dua zake mungu amezikubali. Akamshukuru askari huyo na kuliondoa gari lake kwa mwendo wa kasi maana alihofia kuitwa tena.



    Alipofika kwenye daraja la Amboni, akasimamisha gari pembeni na kushuka, akaangalia huku na huko akaona pako sawa, akaliendea buti na kulifungua, akazitoa maiti hizo na kuziburuza hadi karibu na ukingo wa daraja hilo, kisha akazisukumia ndani ya daraja, akarudi tena ndani ya gari na kuchukua chupa ya maji na kwenda kufuta zile damu ambazo zimebaki wakati anaburuza zile maiti, alipoona kila kitu kimekaa sawa, akawasha gari na kwenda kutafuta gesti yoyote ambayo anaweza kulala usiku huo, alihofia kurudi kisha askari wale wamsimamishe tena halafu wasimuone huyo mtoto anaeumwa.



    Majira ya asubuhi, alianza tena safari ya Kurudi Tanga mjini, alipofika nyumbani kwake, akampigia simu Moto na kumtaka afike mara moja hapo na baada ya nusu saa Moto alifika nyumbani hapo akiwa yupo ndani ya gari aina ya Prado Tx, kwahakika alibadilika sana kimuonekano, alikuwa yupo kama mtoto wa tajiri flani au ni kijana kati ya vijana wachache wenye maendelea hapo jijini, alikuwa amevaa kileo zaidi kama wale wasanii wa muziki wa kizazi kipya, masikioni mwake alibandika hereni, shingoni mwake kulikuwa na cheni ya gharama iliyoning'inia huku vidoleni kukijazwa mapete na mkononi alikuwa ameshikilia simu ya maana, achilia mbali mavazi aliyoyavaa, yote hayo yalijidhihirisha baada ya yeye kushuka ndani ya hilo gari.



    Akanyoosha moja kwa moja mpaka ndani ya nyumba hiyo na kumkuta Mata akiwa amekaa kwenye sofa sebuleni hapo akimsubiri yeye, wakasalimiana salamu za vijana kwa kupeana tano, akaenda moja kwa moja hadi kwenye friji la hapo, akalifungua na kuanza kuangalia humo kwa sekunde kadhaa kisha akamgeukia Mata aliekuwa akimuangalia tu muda wote.



    “Vipi wewe mboma sioni vinywaji humu ndani ya friji?" Chaajabu hata uongeaji wake pia ulibadilika na kuwa kama wale mabitozi wa kimarekani weusi.



    “Wala hakuna pombe humo, thi unajua mimi huwa thitumii thana vinywaji hivyo, halafu hata mke wangu pia hapendi nikitumia, kwahiyo ndio maana thiweki hivyo vinywaji unavyotaka"



    “Kwahiyo unataka na mimi nitumie juisi kama mtoto mdogo, poa acha nitumie kwa dharula" akachukua jagi lenye juisi ya matunda na kumimina kwenye glasi, akaenda kukaa kwenye sofa na kuanza kunywa taratibu kinywaji hicho.



    “Ndugu yangu umebadilika thana yani" Mata aliongea.



    “Aaa! Kawaida tu mbona, si unajua watu tunaenda na wakati"



    “Hata kama lakini thio kwako, unakumbuka kipindi kile ulikuwa unathema, ohooo, nikidhipata hidhi hela, bathi chakwandha naoa, haya uko wapi ule mthemo wako, atha hivi umekuwa mtu wa kubadilisha wathichana tu, akitoka huyu anaingia huyu, angalia ndugu yangu, utakuja kufa kwa magonjwa"



    “Bab, kwanza hayo magonjwa tumeumbiwa sisi, kwahiyo mimi sijali kuhusu hilo, halafu hizo habari za kuoa nilikuwa nazisema kipindi kile sina hela, ila hivi sasa mimi ndio bosi, hahahah! Maisha ukiyaotea raha sana, yani mimi sijasoma ila nimeajiri watu waliosoma na ndio wananiita bosi tena kwa unyenyekevu, halafu hata kama nikioa huyo mwanamke atapata tabu tu, maana sijazoea kuwa na mwanamke mmoja, hata hivyo nioe kwani hivi sasa nakosa kitugani kwa hao ambao sijawaoa? Kwanza umenikumbusha kitu, shemu yupo wapi?" Moto aliongea.



    “Shemeji yako ameenda kwao kuthalimia"



    “Ndio ameondoka na jembe langu(akimaanisha mtoto wa Mata) au jamaa yupo?"



    “Wote wameondoka"



    “Sawa, niambie mzee nakusikiliza"



    “Ni hivi..." Akamuambia yote yaliotokea tangu anawatuma wale watu wakamuue Hemedy jijini Dar na kujakumletea vitisho kisha kuwaua, hakuacha kumuhadithia kilichomkuta wakati akienda kuzitupa zile maiti.



    “Haina haja ya kumfuatilia tena yule dogo, kwanza mimi naona hana madhara tena kwetu, kwahiyo tuachane nae tu"



    “Thawa kama ndio umeamua tufanye hivyo, pia ni thawa tu"



    “Basi mzee acha mimi nikalale maana hapa ninausingizi kibao wa jana usiku, si unajua mimi ni mzee wa kujirusha, jana nilikuwa klabu nainjoi na watoto wazuri tu, acha basi mimi nikalale" Akainuka pale alipokaa na kwenda kugongesha tano na kuanza kuondoka.

    Chaajabu zaidi, alikuwa akitembea kwa kudunda dunda kama kitenesi kilichokosa muelekeo baaada ya kupigwa shuti na mtoto mdogo aliekuwa akikichezea. Ama kweli wahenga hawakukosea pale waliposema msemo wao ‘Masikini akipata, matako hulia mbwata' masikini mwenyewe ndio huyo sasa, alikuwa akipeta na mali za dhuluma, huwezi kumdhania kuwa ndie huyu aliekuwa akikaa maskani bila kazi yoyote. Kwa hivi sasa. Alimiliki baa kubwa sana iliyokuwa maeneo ya sahare na supamaketi ndogo(Min SuperMakert)iliyokuwa katikati ya mji.



    Mata na yeye alimiliki mabasi mawili yaliyokuwa yakienda safari za Tanga, Dar na mafuso ya mizigo yaliyokuwa yakimletea pesa nyingi. Huku Mrutu nae akiongeza maduka ya spea za magari na alifungua showroom ya magari baada ya kuona biashara hiyo ilikuwa ikimlipa sana marehemu kaka yake. Kwahakika watu hawa kila mmoja alikuwa amejizatiti upande wake, hakuna ambae alitaka arudi nyuma kimaendelea, ndio maana kila mmoja alipambana kutaka kuzikuza mali hizo walizokuwa nazo.



    Mrutu majira hayo ya asubuhi, alienda kutembelea maduka yake na kukusanya pesa zote zilizopatikana kwa hiyo wiki na kuzipeleka benki, akaenda kwenye ofisi yake iliyokuwa ndani ya hiyo kampuni yake ya magari na kwenda kupiga mahesabu ya mauzo ya wiki hiyo, yeye alikuwa akipiga mahesabu kila baada ya wiki moja, alipoona pesa ziko sawa, nazo akazipeleka benki kwenda kuzihifadhi, akarudi nyumbani kwake, nyumba ambayo alikuwa akiishi marehemu kaka yake na familia yake, na kwenda kupumzika siku hiyo.



    Tabia yake na ya Moto hazikutofautiana sana ila yeye hakuwa mtu wa kwenda klabu, ila alipenda kubadilisha wanawake kila kukicha, hata hapo pia alimpigia simu mwanamke aliempata jana wakati alipoenda kununua gari kwenye kampuni yake, baada ya dakika kadhaa alifika mwanamke huyo na kumkaribisha kwa bashasha zote, walikaa sebuleni hapo na kuanza kupiga stori ambazo hazikuwa na maana yoyote, baada ya kuishiwa na chakuongea, Mrutu ndio aliona sasa huo ndio muda wa kufanya kile alichopanga juu ya mwanamke huyo.



    Akanza kumchombeza kwa maneno yake hadi pale mwanamke huyo alipoanza kukaa sawa, hakuwa na ujasiri wa kukataa hata kidogo, sio kwamba Mrutu alikuwa na maneno matamu kiasi kwamba yakamchanganya mwanamke huyo, la hasha! Ila angeanzaje kukataa wakati ikiwa hata bei ya gari alilonunua kwa mwanaume huyo alipunguziwa kwa kiasi kikubwa, hata hivyo hivyo pia alijiziwa mafuta fulutanki kwenye hiyo gari bure kabisa. Baada ya kuingia kwenye kumi na nane zake, wakavutana hadi chumbani ambako sijui ni nini kiliendelea maana walifunga mlango kwa ndani huku ikiwa mimi nimebaki nje ya mlango huo.



    Daresalam.



    Maandalizi ya mitihani ya kumaliza darasa la saba yalifanyika Tanzania nzima, kila mwanafunzi alikuwa katika mishemishe za kujiandaa kuukabili mtihani huo wa kuhitimu elimu ya msingi, wanafunzi wengi walionekana wakijaa katika vituo vya kufundisha masomo ya ziada(tution), Hilda na Hemedy pia walikuwa katika mkumbo huo wa kujianda kwa mitihani watakayo ifanya siku mbili mbele.



    Majira hayo ya saa kumi na mbili jioni, walikuwa wapo njiani kurudi nyumbani kwao wakitokea katika kituo cha kufundishia masomo ya ziada, walikuwa wakiongoe kwa furaha huku wakikumbushiana mambo mbalimbali ambayo yaliwafanya muda wote kufurahi, hata hivyo pia, ilikuwa ni moja ya kufupisha mwendo wa kufika nyumbani kwao, japokuwa hapo wanaposoma na nyumbani kwao sio mbali.



    Walifika nyumbani na kila mmoja kufanya kazi zinazomuhusu, kisha wakachukuana na kuelekea kwenye kibaraza kilichokuwa mbele ya nyumba hiyo na kukaa hapo, walitoa madaftari yao na kuyaweka juu ya meza iliyokuwa mahala hapo na kuanza kusoma kile walichoona kitawasaidia katika mitihani yao, walisoma hadi walipochoka na kuingia ndani kwenda kupata chakula cha usiku kisha kila mmoja akaingia katika chumba chake na kwenda kupumzika.



    Siku mbili mbele, wao na wanafunzi wengine wa darasa kama lao nchi nzima, walikuwa ndani ya madarasa yaliyo teuliwa kwa kufanyia mitihani hiyo. Mitihani hiyo waliifanya kwa siku mbili tu na baada ya hapo wakawa tayari ni wahitimu wa elimu hiyo ya kwanza, kila mwanafunzi alikuwa nyumbani akisubiri matokeo yake baada ya kumaliza kufanya mitihani hiyo, wengine walienda kujifunza masomo ya awali ya sekondari(Pre form one) ili hata kama wakibahatika kufaulu, basi wasibabaishwe na zile mada za mwanzo mwanzo pindi waingiapo kidato cha kwanza, na wao pia walienda kujifunza masomo hayo huku wengine wakisubiri matokeo wakiwa nyumbani kwasababu zao wazijuazo wenyewe.



    Miezi mitatu mbele, matokeo yao yalitoka na kuwafanya wanafunzi wengi kuwa na kiroho cha kutaka kuyaona matokeo hayo, wengi walikusanyika mashuleni mwao walipomalizia elimu zao, kwenda kuangalia kile walichokipanda kwa miaka saba iliyopita. Hemedy na Hilda, wao matokeo yao waliyaangalia kwenye intaneti na kujikuta wakiwa wamefaulu kwa kiwango kizuri tu, tena bahati ilikuwa kwao, walifaulu shule moja.



    Bila kuchelewa, Anti yao aliwafanyia maandalizi haraka haraka yakiwemo sare za shule hiyo na vitu vyengine kama hivyo vinavyohitajika shuleni kwa wale wanafunzi wapya. Mwezi mmoja mbele, wakaanza kwenda kwenye shule waliyochaguliwa, shule ya sekondari Benjamini Wiliam Mkapa. Wanafunzi wageni ndio walidhihirika shuleni hapo huku wenyeji wakimalizia likizo yao waliobakisha ya wiki moja.



    Wanafunzi hao wageni, wengi walionekana na nguo za shule ya msingi huku wachache ndio walikuwa wamevaa sare za shule hiyo, walikuwa wamezagaa tu ndani ya shule hiyo, baada ya muda wakaitwa wote na kuwekwa sehemu moja na mwalimu aliewapokea akanza kuwakaribisha shuleni hapo kwa kuwasisitizia wafuate sheria walizozisoma kwenye fomu walizopewa kabla.



    Baada ya kuwaeleza mengi, aliwataka waongozane hadi katika madarasa kwaajili ya kwenda kupangiwa, waliitwa kwa majina na kila aliesikia jina lake alitakiwa kuingia kwenye darasa aliloelekezwa. Zoezi hilo lilifanyika kwa lisaa limoja hadi kukamilika na kila mwanafunzi akawa yupo kwenye darasa alilopangiwa, baada ya zoezi hilo kuisha, waliambiwa waende kwenye madarasa mengine kwenda kuchukua viti na meza zilizofemea kwenye madarasa hayo. Hemedy na Hilda walipangwa darasa moja, hapo furaha yao ilizidi mara dufu.



    “Niaje jamaa" mwanafunzi mmoja alimsalimia Hemedy wakati wakiwa wapo darasani.



    “Freshi tu, niambie kaka" Hemedy nae alijibu huku akigongesha viganja vyake vya mkono huku akiwa amevikunja, vijana waliita ‘Tano'.



    “Safi tu, mwanangu mimi sijapata kiti wala meza humu ndani, kwahiyo jamaa naomba msaada wako kwenda kuchukua vitu hivyo madarasa mengine"



    “Usijali, maana hata mimi pia sijapata kitu hata kimoja humu ndani, kwahiyo tutasaidiana wote kuchukua vitu hivyo"



    “Poa kaka, twenzetu tukavichukue" mwanafunzi huyo alipoongea hivyo, wakaanza safari ya kuelekea madarasa mengine kwenda kuchukua viti na meza, walipishana na wanafunzi wenzao ambao nao walikuwa katika harakati za kuchukua vitu hivyo na kuvihamishia kwenye madarasa yao. Walifanikiwa kupata na kurudi navyo kwenye darasa lao walilopangiwa, kisha wakavipanga karibu karibu, Hemedy alikaa mbele na nyuma yake alikaa huo mwanafunzi mwengine, wakawa wamekaa kwa mfuatano.



    “Oya jamaa" mwanafunzi huyo alimuita Hemedy na kumfanya amgeukie.



    “Naitwa Ramadhani Kaoneka, ukipenda unaweza ukaniita Rama au kiswaga zaidi ukiniita Ramso, sijui wewe unaitwa nani?" mwanafunzi huyo aliejitambulisha kwa majina hayo alimuambia Hemedy huku akimpa mkono.



    “Hemedy Mheshimiwa Bhachu" na yeye alijitambulisha huku akiupokea mkono huo.



    “Dah! Jamaa jina lako linafanana na Tajiri mmoja hapa dar, sijui una undugu nae" Rama au Ramso aliongea.



    “Hapana sina undugu na mtu yoyote hapa dar" Hemedy alijibu.



    “Kwani wewe ni mtu wa wapi?" Rama aliuliza.



    “Mimi ni zao la Tanga ndugu"



    “Dah! Mwanangu hata mimi pia ni zao la huko huko, sema mimi niliondoka kule tangia nikiwa darasa la tatu ndio nikahamia huku"



    “Basi tupo pamoja kaka" Hemedy aliongea.



    “Hemedy, jina zuri sana, ila mimi ningependa kukuita Medy ile kiswaga zaidi au wewe unasemaje?"



    “Iko poa sana, na mimi ningependa kukuita Ramah ile kiswaga zaidi na wewe unasemaje?"



    “Hahaha! Jamaa yangu jina zuri sana ulilonipa, Ramah, dah! safi sana kaka nimelikubali" Muda huo huo akaja Hilda hadi hapo walipokaa, Hemedy akamuuliza kuhusu kupata kiti na meza akajibu ndio na tayari ameshavipanga katika mstari, akamuonyesha pale iliposehemu yake atakayo kaa kwenye darasa hilo.



    “Oya, Ramah ‘sister’ wangu huyu anaitwa Hilda" Hemedy alimgeukia Ramah na kumtambulisha Hilda.



    “Oooh! Sista karibu, naitwa Ramadhani au Ramah kama alivyoniita jamaa yangu" Ramah aliongea hivyo huku akipeana mikono na Hilda.



    “Naitwa Hilda Ganjo"



    “Nawewe umepangwa darasa hili?" Ramah alimuuliza utafikiri hakuona kipindi Hilda akimuonyesha Hemedy sehemu atakayo kaa darasani hapo.



    “Yeah, tupo wote humu"







    “Basi vizuri, naamini tutashirikiana wote vizuri tu"



    Majira hayo wanafunzi hao wageni waliyatumia kuzunguka zunguka shuleni hapo ili kuyasoma mazingira, walitembea sana hadi walipoona wameridhika kuyasoma mazingira hayo, wakatoka nje ya shule hiyo ili kwenda kupata chakula maana ndani ya shule hiyo hakukuwa na chakula chochote kilichopikwa hapo kutokana na shule kutofunguliwa rasmi, siku hiyo waliitumia kupiga stori tu kwasababu hawakuwa ni wenye kufundishwa chochote kwa siku hiyo ya kwanza.



    Muda wa kutoka ulipofika, wakaruhisiwa kuondoka huku wakikumbushwa kuwa siku inayofuata wa wahai kufika ili wafanye usafi wa shuleni hapo. Wiki hiyo iliisha, ikafuata nyengine, wiki hii ndio wiki waliokuwa wakifungua wanafunzi wote wa sekondari, wanafunzi wenyeji wakarudi shuleni na kuwakuta wageni, haikuwa tatizo kwao, kwasababu hata wao pia walikuwa hivyo hivyo.



    Ikapangwa ifanyike sherehe ya kuwakaribisha wanafunzi hao wageni, siku ya siku ikafika na sherehe hiyo ikafanyika kwenye ukumbi wa shule. Hemedy Tabia yake ya uongeaji na uchekeshaji hakuiacha, hivyo ilifanya ajulikane na wanafunzi wengi kwa haraka kuliko mwanafunzi yoyote, hata hivyo ni kama vile tabia yake na ya huyo rafiki yake wa kwanza shuleni hapo Ramah ziliendana, wote walikuwa ni waongeaji sana pindi wanapokaa na wenzao kikundi, walihakikisha kila baada ya sekunde moja, watu waliowazunguuka wayaache meno yao nje kwa kucheka. tabia yao hiyo ikawafanya waitwe mapacha.



    * * * *



    Zilianza sekunde, zikafuatia dakika, yakafuata masaa na kumalizikia mwaka, wakawa wapo kidato cha pili, kidato hichi, waliamua wakazane nacho kusoma maana walijua kuna kurudia kama hutofaulu mtihani wa mwisho wa kidato hicho, walikazana kusoma wote watatu nikimaanisha na Hilda pia, ili waweze kufaulu mtihano huo, na hawakuwa haba kufanya vizuri kwenye mitihani.



    Pamoja na kusoma sana na kufanya vizuri kwenye mitihani, pia hawakuacha tabia yao ya kuchekesha, na kitu chengine alichokijua Hemedy kwa Ramah ni kuwa kijana huyo ana kipaji cha kuimba, na mara nyingi sana alikuwa akimuimbia kila Hemedy atakapo taka hivyo, pamoja na hivyo, Ramah hakutaka ajulikane na wanafunzi wenzake kuwa ana uwezo mzuri wa kuimba, vijana hao walijulikana shule nzima kwa tabia yao ya kuongea sana hadi kupelekea kuwa komedi kwa wanafunzi wenzao, na sio kwa wanafunzi tu hadi kwa walimu pia waliwajua.



    Mwaka huo nao ukapita, ukaingia mwaka mwengine, mwaka huu walikuwa kidato cha tatu baada ya kufaulu vizuri mtihani wa kidato cha pili, kufaulu kwao hakukuwafanya waache kusoma, walisoma sana hadi kuamua kwenda kuanza kusoma na masomo ya ziada ili mradi watakapofika kidato cha nne wafaulu vizuri ili waendelee na masomo ya juu, wote watatu walichagua kusoma masomo ya sanaa, bahati ikawa kwao tena baada ya kupangwa darasa moja.



    “Oya jamaa, mbona huyo sisita wako anakununia ukiwa umekaa na gashi(akimaanisha mwanamke) ana nini kwani?" Siku moja wakati wakiwa wamekaa darasani kipindi hicho kilikuwa ni frii yani hakuna mwalimu anaeingia darasani kufundisha, kipindi hicho kiliachwa kwaajili ya kujisomea wenyewe wanafunzi. Ramah alimuuliza Hemedy hivyo.



    “Mwanangu hata mimi mwenyewe pia simuelewi, leo hataki kabisa kuzungumza na mimi kisa nimekaa na yule ‘montres’ wa darasa" Hemedy alijibu.



    “Sista wako anakupenda, hataki uharibikiwe kwa kujiingiza kwenye masuala ya wanawake" Ramah aliongea.



    “Hata kama, ila sio kiivyo, unajua hii tabia aliianza kitambo sana, sasa mimi simuelewi kabisa"



    “Enhee! Subiri nikuulize kitu, maana tokea kitambo nikitaka kukuuliza hii ishu nasahau. Hivi mbona majina ya wazazi wenu hayafanani kabisa, wewe mzee wako anaitwa Mheshimiwa na yeye mzee wake anaitwa Ganjo, sasa hapo ni vipi? embu niambie"



    “Mimi na yule hatuna undugu kabisa, yani sio ndugu yangu" Hemedy alijibu.



    “Kivipi yani, sijakuelewa mzee" Ramah aliongea hivyo huku akikaa vizuri kitini ili apate kumsikia vizuri, maana yeye alidhani Hilda na Hemedy ni ndugu tokea kitambo, asa ni vipi ajekuambiwa kuwa hawana undugu wowote?.



    “Ni hivi, mimi nina wazazi wangu na yeye anawazi wake, ila historia zetu zinafanana, yeye wazazi wake wamekufa na mimi pia hivyo hivyo, yeye akawa anaishi na babu yake huko Tanga, na huyo babu yake na baba yangu walikuwa ni marafiki wakubwa sana enzi za uhai wa baba yangu, sasa baba yangu alipofariki, ndipo baba yangu mdogo alipomuomba babu yake Hilda mimi nikaishi kwake maana yeye ana mambo mengi kwahiyo asingeweza kunihudumia vizuri, ndipo hapo mimi nilipoanza kwenda kuishi kwa kina Hilda nyumbani kwa huyo babu yake" Hemedy akamaliza kuelezea.



    “Kwahiyo hapo ndio ukakutana na huyu Hilda?" Ramah alimuuliza swali ambalo jibu lake lilikuwa wazi kabisa.



    “Ndio, ila mimi sikuanza kukutananae kwa siku hiyo nilipoanza kuishi hapo, kuna siku moja ilikuwa ni sherehe yake ya kuzaliwa ndio tukakutaniana hapo na ndio ukawa mwanzo wa kujuana"



    “Duh! Na yule bi mkubwa mnaeishi nae kule hom ni ndugu wa nani kati yenu nyie wawili?" Ramah aliuliza.



    “Ni anti yake na Hilda, yule bi mkubwa alimtaka Hilda aje kuishi nae huku ila Hilda alikataa kuja pekeake, akidai hawezi kuondoka na kuniacha mimi kule ndipo nikaambiwa na mimi nije huku, ila nahisi ule ulikuwa ni utoto tu ulimsumbua"



    “Jamaa huo sio utoto, kuna kitu chengine anacho" Ramah aliongea hivyo huku akiigamia kwenye hicho kiti alicho kalia.



    “Kivipi? Sijakuelewa"



    “Yani mimi nikiunganisha matukio, naona kabisa huo haukuwa utoto hata kidogo, unajua huyo unaemuita sista wako, alishawahi kumkunja shati demu flani hivi anasoma sayansi, anaitwa nani sijui, jina lake limenitoka kidogo. aliwahi kumkunja shati kule chooni kisa wewe ulienda kula nae msosi kwenye ‘break‘’, na sio huyo tu, nishawahi kumshuhudia akiwachimbia biti wanawake wenzake wengi tu kisa wewe muuni wangu" Ramah aliongea huku akitabasamu.



    “Duh! Mbona yote hayo mimi siyajui?" Hemedy aliuliza hivyo huku akiwa kayatoa macho yake utafikiri amepewa taarifa ya kifo chake na izraili.



    “Huwezi kuyajua kwasababu wewe ndio mlengwa, sasa je kama akiwachimbia biti anawapa onyo wasije kukupa taarifa, wewe unadhani hapo utayajuaje? Huwezi kujua mzee"



    “Duh! kwanini sasa anafanya hivyo?" Hemedy aliuliza.



    “Mi nakuambia yule sista wako anakitu chengine cha zaidi tofauti na huo usista"



    “Kitu gani?" Hemedy aliuliza.



    “Anakupenda yule" Ramah alisema kiufupi.



    “Kivipi mzee mwenzangu hapo sijakuelewa"



    “Aaaaa!! Medy wewe mkubwa bwana, miaka kumi na saba uliyonayo inakutosha kujua mengi, kwahiyo usijifanye mtoto mdogo"



    “Ila mwanangu hicho kitu hakuna bwana, unajua mimi na yeye tunaheshimiana kama kaka na dada japokuwa hatuitani hivyo, sasa ni vipi alete kitu chengine kama hicho, na kama ni hivyo, mbona hakuwahi kuniambia hata mara moja?"



    “Dah! Jamaa yangu uko nyuma sana yani, tangu lini mwanamke akamuambia mwanaume kuwa anampenda? Yani hadi ukiona mwanamke kamfuata mwanaume kisha akamuambia kuwa anampenda, basi jua mwanamke huyo amefikia hatua ya mwisho ya kuvumilia, nikisema hivyo namaanisha kuwa ameshamuonyesha ishara zote huyo mwanaume hadi zile za barabarani na huyo mwanaume akajifanya kuzivalia miwani ya mbao hizo ishara yani hazioni hata kidogo, kwani wewe hajawahi kukuonyesha ishara zozote?" Ramah alifafanua kisha akauliza.



    “Hapana, labda tu yeye anapenda kila wakati kuwa na mimi karibu na hivyo kuninunia ikiwa nimekaa na demu yoyote hapa shule kwa muda mrefu"



    “Basi mzee mwenzangu hata hizo pia ni ishara tosha kukuonyesha kuwa anakupenda, kwasababu gani ujue, yeye kama ingekuwa hakupendi kiivyo, basi asinge wachimbia biti wale magashi wengine unaopiga piga nao stori, anafanya hivyo akijua wao wanaweza wakakuchana laivu ikiwa yeye hawezi kufanya hivyo, sasa jamaa yangu jiongeze hapo, ohooo! asije akapata wanaojua kutia mavoko wakamteka halafu wewe akupendae akakuacha akijua wewe humpendi" Ramah wakati akiongea hivyo, mwenzake alikuwa yupo mbali kimawazo, akamshangaa kuwa kwenye mawazo wakati mwanzo walikuwa wakiongea vizuri, ikabidi amshutue na kumuuliza ni kipi anakichokiwaza kwa wakati huo.



    “Unajua wewe wakati unaongea hivyo, mimi kuna kitu nimekumbuka, kuna siku tulikuwa tumekaa hom baada ya kumaliza kusoma usiku..."



    KUMBUKUMBU.



    “Hivi Hemedy wewe, labda kimfano ukiwa kuna mtu umempenda, wewe kama wewe utafanya nini ili ajue kama umempenda" Hilda aliongea hivyo huku akiwa amemlalia Hemedy kwenye bega, huku madaftari yao yakiwa yapo juu ya meza waliyoitumia kujisomea wawapo nyumbani.



    “Mimi nitamuambia tu ukweli ili nae ajue, maana kama nisipofanya hivyo yeye hatoweza kujua kama mimi nampenda, si unajua hakuna anaejua yaliyojificha ndani ya moyo wa mtu mwengine, kwahiyo maneno yanahitajika"Hemedy aliongea.



    “Mmmh! Mimi siwezi kumuambia"Hilda aliongea hivyo huku akiupitisha mkono wake wa kulia kwenye singo ya Hemedy kwenda bega la kushoto.



    “Sasa wewe utafanyeje ili ajue kama unampenda?" Hemedy aliuliza.



    “Mimi nitamuonyesha ishara tu, ila kumuambia mmh mmh! siwezi"



    MWISHO WA KUMBUKUMBU.



    “Sasa hadi mtoto ukiongea nae anakukumbatia namna hiyo, hivi wewe ulikuwa unataka ishara za namna gani labda?" Ramah alimuuliza Hemedy baada ya kukisikiliza kitu kilichomfanya Hemedy awaze wakati akiwa yeye anaongea.



    “Sasa mwanangu huko kukumbatiwa pia niishara ya mapenzi? Je kama ni ile kiurafiki tu? halafu pia hilo swala la kunikumbatia wakati tukiwa wenyewe hakulianza siku hiyo"



    “Sawa, basi tufanye huku kukumbatiwa mkiwa wenyewe ni kiurafiki tu. Je hiyo ya kuwachimbia biti mademu wenzake kisa wewe, nayo ni vipi, au nayo pia ni kiurafiki tu?" Ramah alimuuliza.



    “Ila lakini wewe mwanzo si umesema kuwa huenda ikawa akinilinda nisiharibikiwe kujiingiza kwenye masuala ya kuwa na wanawake?" Hemedy aliuliza.



    “Jamaa yangu pale nilikuwa natafuta kiki tu yakukuuliza maswali yote haya, ndio maana nikasema vile, ila mimi niliona tokea kitambo kwamba yule demu anakupenda, ila wewe ukajifanya kumvalia miwani ya mbao usiyaone hayo"



    “Sasa wewe unanishauri vipi?" Hemedy aliuliza.



    “Mi sina cha kukushauri zaidi ya kukuambia umchane tu"



    “Duh! Mtihani huu, akini kataa je? si ataenda kumuambia anti halafu hapo ndio itakuwa mwisho wa kuishi pale nyumbani kwao?" Hemedy aliuliza, alionekana dhahiri alikuwa na hofu, haikujilikana kuwa ni hofu ya kutongoza mara ya kwanza au ya kufukuzwa nyumbani kwa anti yake Hilda pindi atakapoenda kumsemea. Akapeleka macho sehemu anapokaa Hilda na kumuona msichana huyo ni mwenye kumuangalia na yeye, wakajikuta wamegonganisha macho yao, Hilda akawahi kuyaondoa macho yake huku akijifanya amevimbisha mashavu yake kwa kukasirika kama maputo ya kwenye ile sherehe yake aliyowahi kufanyiwa kipindi akiwa na miaka kumi na moja. Hemedy akarudisha macho yake huku akiwa natabasamu usoni mwake.



    “Aaaa!! Jamaa hawezi kukukataa hata kidogo, kwanza mtoto mwenyewe anakupenda, sasa ataanzaje kukukatalia?"



    “Sasa mzee nitamuanzaje anzaje? maana sijawahi kutongoza mwanamke hata kwa bahati mbaya"



    “Hapo mzee mwenzangu itabidi tu upambane na hali yako yani ujitafute mwenyewe maana hata mimi sijui huyu mtoto leo nitaanzaje kumchana"



    “Haaa!! Kwani jamaa kuna gashi unataka ukamchane leo?" Hemedy alimuuliza.



    “Dah!! Kumbe mwanangu sijakuambia. Kuna demu mmoja anasoma ‘business‘ anaitwa Hawa, nataka leo nikamchane laivu maana nishachoka kuumia mwenyewe kila siku"



    “Duh!! Ila lazima akuelewa, yani vile ukimchana huku unamuimbia imbia, lazima akuelewe tu, embu kwanza kabla ya yote niimbie kidogo mzee maana kitambo sijaisikia sauti yako wakati ukiwa unaimba"



    “Usijali wewe ni mshikiji wangu lazima nikuimbie" alipoongea hivyo, akajikohoza kidogo na kuanza kuimba.



    .....................How many times do i have to tell you?

    Even when you're crying, you're beutifull too.

    The word is beating you down, I'm around Through every mood.

    You're my donwfall, you're my muse.

    My worst distraction, my rhythm and blues.

    Ican't stop singing, it's ringing in my head for you.

    Hayo ni baadhi ya maneno yaliokuwepo kwenye nyimbo hiyo aliyoiimba ya msanii mmoja mmarekani mweusi anaeitwa Jonh Legend, nyimbo hiyo iliitwa All of me. Kwahakika Ramah alikuwa na sauti nzuri ya kuimba.



    “Mwanangu safi sana, halafu hiyo nyimbo itabidi pia umuimbie ili akuelewa maana hiyo nyimbo inamashairi mazuri kinyama. Hivi jamaa nani aliekufundisha kuimba?"



    “Yani we jamaa kila siku lazima uniulize hilo swali, ila poa subiri nikujibu. Hakuna alienifundisha kuimba ni kipaji tu nimebarikiwa na mungu ndugu yangu, ila gitaa ndio nimefundishwa na mzee mmoja wa pale mtaani"



    “Ina maana hata gitaa pia unaweza kupiga?" Hemedy aliuliza.



    “Ndio ndugu yangu"



    “Fanya basi siku nijekukusikia ukiimba huku ukipiga gitaa, dah sipati picha jinsi utakavyoimba"



    “Usijali, sasa kaka subiri nimfuate yule demu nikamuambie kabisa kuwa muda wa kutoka shule ninamaongezi naye, yani sikufichi ndugu yangu, nataka nimuambie leo leo ili nijitue huu mzigo nilioubeba moyoni mwangu tangia muda" Ramah aliongea hivyo huku akinyanyuka kwenye kiti alicho kalia.



    “Poa poa kaka, nakuaminia" Hemedy alijibu huku akitabasamu.

    RamAh alipofika kwenye mlango wa hapo darasani, akageuza tena na kurudi mahali alipo Hemedy.



    “Dah!! Mwanangu nina hofu kinyama yani, sijui nighairishe leo?" Ramah aliongea hivyo huku akikaa kwenye kiti.



    “Jamaa hapo utaharibu, unajua unapoamua kufanya kitu basi kifanye kwa ule wakati ulioupanga, hofu isikufanye ukaghairisha ulichopanga kukifanya, huwezi jua huwenda ikawa leo ndio siku yako ya bahati" Hemedy alimpa moyo mwenzake.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    “Dah!! Nina hofu kinyama mzee mwenzangu iliyochanganyikana na uoga wa kutongoza kwa mara ya kwanza"



    “Kumbe hujawahi kufanya hivyo hata siku moja? Ila mi nakushauri leo isipite bila kumuambia na kama ikipita leo, basi usimuambie tena siku yoyote, subiri ifike siku kama ya leo, tarehe kama ya leo, mwezi kama wa leo na mwaka kama waleo ndio umuambie"



    “Hahaha! Jamaa nani aliekuambia siku hii itajirudia tena?" Ramah aliuliza huku akicheka.



    “Ndio hivyo sasa, unatakiwa siku ya leo isipite bila kumuambia kwasababu haitajirudia tena"



    “Sawa, ila nawewe siku ya leo isipite bila ya kumchana ukweli yule mama mvimbaji"



    “Hahaha!! Usijali ila anza wewe kwanza"



    “Basi poa kaka acha mimi nimfuate yule demu nikamuambie kuwa baada ya kengele ya kutoka hapa shule nina maongezi nae" Alipoongea hivyo akanyanyuka kwenye kiti na kutoka darasani humo.

    Hemedy akabaki akiwa amekaa mwenyewe, ila ghafla mbele yake akasimama Hilda aliekuwa akimuangalia kwa macho yake mazuri, alifanya hivyo kwa sekunde kadhaa kisha akakaa kwenye kiti kilichokuwa karibu na Hemedy, alionekana dhahiri kuna jambo anataka kumuambia.









    “Umekula wewe?" Hilda aliuliza.



    “Hapana" Hemedy alijibu.



    “Kwanini?"



    “Nitaanzaje kula ikiwa niliezoea kula nae ameninunia tena bila kujua kosa langu" Hemedy alijibu taratibu kama vile ni mwenye kuonewa kwa jambo hilo.



    “Kwahiyo tangia asubuhi hukula kisa mimi?" Hilda alimuuliza.



    “Hapana sio asubuhi, ila ni tangia jana usiku nilivyo kula ndio hadi sasa sikula kisa wewe" Hilda aliposikia maneno hayo, aliangalia saa yake ya mkononi na kusema.



    “Bado kama dakika ishirini kengele ya kutoka igongwe" akatulia kidogo na kusema. “twenzetu kantini tukale"

    Alimshika mkono na kunza kutoka nae humo darasani, wakaongozana hadi sehemu panapouzwa vyakula humo humo ndani ya shule, walipofika waliagiza wanachotaka na kuanza kula baada ya kuletewa chakula hicho, ilikuwa ni kesi ukikutwa una kula muda ambao sio rasmi kwa kufanya hivyo, viboko au adhabu yoyote itakuhusu pindi ukikutwa unakula kwa muda ambao haukupangwa kwaajili hiyo.



    “Hilda?" Hemedy aliita wakati wakiwa bado wanaendelea kula.



    “Abee" Hilda aliitikia huku akinyanyua kikombe cha chai na kukigusanisha na lipsi zake, akavuta ndani kinywaji aina ya chai kilichopo ndani ya hicho kikombe, kisha akakishusha kwa utaratibu juu ya meza.



    “Kwanini unaninunia kama sio kunichukia pale ninapokaa au kusimama na mwanamke yoyote hapa shule?" Hemedy aliuliza kwa utaratibu mno swali hilo na nikama swali hilo binti huyo hakulitegemea kuulizwa mahala hapo, akabaki kutafuna kipande cha chapati kilichokuwa ndani ya kinywa chake huku akiwa sura yake ameinamisha chini, haikujulikana ni uzito wa hilo swali au ni aibu zilizomkumba baada ya kuulizwa.



    “Kwani hujui?" aliuliza swali hilo baada ya kupata ujasiri wa kuongea.



    “Siku zote mwenye kuuliza hakijui aulizacho, ndio maana ameuliza ili ajue, na hata mimi nimeuliza ili nijue" Hemedy aliongea kwa utaratibu.



    “Huenda ikawa unakijua unachokiuliza, ila umeuliza ili upate uhakika zaidi" Hilda alijibu vile vile kwa utaratibu.



    “Sawa nimekuelewa. Unaweza ukanijibu, maana mimi sijajua ni kipi hasa kinacho kufanya uwe katika hali ile"



    “Muda sahihi ukifika nitakuambia, ila now, twenzetu maana tumeshamaliza kula"



    Hemedy hakuwa na jengine la kuongeza, wakalipa walichokula na kuanza kuondoka kuelekea darasani, walipofika, kengele nayo ikagongwa na kuwafanya wanafunzi kuanza kukusanya vilivyovyao na kuondoka mahala hapo.



    Katika darasa moja lilokuwepo hapo shule, wakati wanafunzi wengi wameshaondoka shuleni hapo, darasa hili lilihifadhi wanafunzi wawili wajinsia tofauti, wakiume alikuwa ni Ramah na wakike bado hatujapata kumjua, wanafunzi hao walikuwa wamekaa kwenye viti vilivyoangaliana na katikati yao kulitenganishwa na meza.



    “Hawa” Ramah aliita jina hilo, na hapo ndipo tulipopata kulijua jina la banati huyo.



    “Nakusikiliza" banati huyo au Hawa kama Ramah alivyomuita, aliitikia kwa sauti ya upole na yenye kutamanisha kila muda kuisikia. Ramah alimuangalia binti huyo kwa sekunde kadhaa kisha akajikohoza kidogo na kuongea.



    “Mungu alipoiumba hii dunia ambayo ndani yake kuna ardhi na mbingu, akaumba majini ili waje kuishi ndani ya sayari hii, ila baada ya kuona viumbe hivyo vinaleta vurugu katika ardhi yake, akaamua kuviondoa kwenye ardhi kwa kuleta gharika ambalo liliwakimbiza baharini na kwenye miti mikubwa viumbe hao. Alipoona ardhi imebaki tupu bila ya kuwa na kiumbe yoyote, akaona aumbe kiumbe chengine ambacho kitakuja kuishi kwenye hii ardhi, ndipo hapo alipomuumba Adamu, ila Adamu kabla ya kuja kuishi huku duniani, alikuwa akiishi pepono kwa muda mrefu, na wakati wote huo alipokuwa akiishi huko, alikuwa ni mpweke sana, na mungu kwavile alikuwa akikipenda kiumbe hicho alichokiumba mwenyewe, akaamua akiumbie kiumbe chengine ambacho kitakuwa ni faraja kwake, ndipo akamuumba na Hawa kwa kutokana na ubavu wa kushoto wa Adamu. Adamu alifurahi sana baada ya kupata mwenza wa kuishi nae sehemu hiyo, waliishi kwa furaha hadi pale walitolewa sehemu hiyo na kuletwa huku duniani baada ya kushawishiwa na shetani wale tunda ambalo wameambiwa na aliewaumba wasilile. Japokuwa walishushwa duniani, ila mungu aliwashusha kila mmoja sehemu yake tena iliyokuwa mbali, inasadikika kuwa Hawa alishushwa katika nchi ya India huku Adamu akishushwa katika moja za nchi za huko uarabuni" Ramah akanyamaza kidogo kisha akauliza. “Unaweza kujua ni kipi kilicho wafanya wakakutana na kuishi pamoja wakati kila mmoja alishushwa sehemu ya mbali na mwenzake?"



    “Hapana sijui" Hawa alijibu huku akijiweka vizuri kitini ili kuyaskiliza maneno ya huyo kijana.



    “Upendo. Upendo ndio ulisababisha wakakutana tena kwa mara nyengine. Hawa alitoka India kumtafuta Adamu wake mpaka katika nchi moja ya huko uarubuni, kwa nguvu ya upendo aliyonayo alifanikiwa kumpata. Hii haimaanishi kuwa Adamu hakuwa na upendo kwa Hawa, la hasha! Alikuwa akimtafuta sana Hawa, ila hapa tunaonyeshwa ni jinsi gani nyie wanawake mna roho ya huruma na upendo wa dhati juu yetu, kwasababu mmetubeba katika matumbo yenu kwa miezi tisa na mkatulelea hadi hivi sasa tumekuwa. Japokuwa sisi ndio sababu kubwa kupatikana kwa nyie ila nyie ndio sababu kubwa zaidi kupatikana kwa sisi." Akatulia kidogo ili maneno hayo yamuingie vizuri binti huyo, kisha akaendelea. “Unajua kwanini mungu alitaka viumbe hawa waishi pamoja?" Ramah alimuuliza.



    “Ili waijaze dunia, maana dunia kwa wakati ule ilikuwa haina watu, au nimekosea?" Hawa aliongea hivyo huku akitabasamu, bilashaka aliipenda stori hiyo, maana alisahau kuwa muda huo ni mwenye kuhitajika kuwa nyumbani kwao baada ya wanafunzi kutolewa shuleni.



    “Hujakosea hata kidogo, ila kuna jengine la zaidi lililomfanya mungu akataka watu hao waishi pamoja. Upweke ndio uliwafanya watu hao waishi pamoja. Kuna msemo unaosema kuwa hakuna mwanaume bila mwanamke na hakuna mwanamke bila mwanaume. Si hata wewe pia unakubaliana nao?" Ramah aliuliza.



    “Yeah, nakubaliana nao, kwasababu hata wazazi wetu pia si wako pamoja ili kuukamilisha huo msemo" Hawa alijibu.



    “(Huku akitabasamu) nimependa jibu lako" akatulia kidogo, kisha akaendelea. “Hata viatu huvaliwa kwa pea, huwezi kuvaa kiatu kimoja kwasababu itakuwa umeudhulumu mguu mwengine, hata hivyo huwezi kutembea bila viatu, hapo itakuwa umejidhulumu mwenyewe, na pia huwezi kuvaa viatu tofauti itakuwa umeidhulumu miguu yote miwili. Unajua nini nimemaanisha?"



    “Hapana sijajua, nasubiri uniambie" Hawa aliongea huku akijiweka vizuri zaidi kitini.



    “Nilipokuambia kuwa huwezi kuvaa kiatu kimoja kwasababu utaudhulumu mguu mwengine, nilikuwa namaanisha kuwa, mwanadamu hawezi kuwa pekeake siku zote, kwasababu anahitajika kupata mtu wa kumfariji kwenye huzuni na kufurahia nae kwenye furaha, na niliposema kuwa huwezi kutembea peku kwasababu itakuwa umejidhulumu mwenyewe, nilikuwa namaanisha. Huwezi kuwa na furaha pasi na kuwepo kitu cha kukupa hiyo furaha, ni lazima uitafute furaha yako popote pale ilipo ili nawe ufurahi kama wafurahiavyo wengine. Na niliposema kuwa huwezi kuvaa viatu tofauti, nilikuwa namaanisha, pamoja na kuitafuta hiyo furaha popote ilipo, nilazima kwanza uzingatie ni furaha ipi itakufanya uwe na furaha kila ukiiona au ukiwa nayo, kwasababu usipozingatia kutafuta furaha sahihi juu yako, basi utakuwa upo kama yule mtu alievaa viatu tofauti, kwasababu hatokuwa akijiamini pale anapopita mbele za watu akidhani labda watu watamcheka au watamsema kwa vile alivyovaa. Basi ataona afadhali avue kimoja ili aiepuke ile aibu ya kuvaa viatu tofauti, hata hivyo pia watu watamcheka kwa kuvaa kiatu kimoja huku mguu mwengine ukiwa hauna kitu. Mwisho wa safari ataamua avue tu hicho kimoja atembee peku akidhani hiyo itakuwa ni afdhali kwake, ndio hapo atakapokuwa amejidhulumu mwenyewe kwa kuitembeza miguu yake peku kwenye jua kali. Unadhani labda afanye nini mtu huyo ili aepukane na yote hayo?" Ramah alieleza kisha akauliza.



    “Itambidi kutafuta viatu vilivyofanana na avivae ili aepukane na kuchekwa na watu kisha kuvivua kabisa viatu badili alivyo vaa, kwakufanya hivyo ndio ataonekana yupo sahihi mbele za wtu" Hawa alijibu huku akitabasamu.



    “Safi sana, nimeyapenda majibu yako. Yote hayo nilikuwa namaanisha kuwa. Binadamu mwenye moyo wa nyama, inahitajika apate mtu wa kuwa nae pamoja, ambae atakuwa nae kwa kila hali, bila kuwa hivyo, basi mtu huyo atakuwa ni mpweke na hatokuwa na furaha kamwe hata awe na utajiri mkubwa, atakuwa ni kama yule mtu alievaa kiatu mguu mmoja. Na ikiwa amemtafuta mtu wa kuwa nae pamoja na mtu huyo asiwe sahihi kwake, basi atakuwa ni kama yule mtu alievaa viatu badili. Na kwavile amepata mtu asie sahihi kwake, basi atamchoka na kuamua amuache abaki mwenyewe, na ndio hapo tutakapo mfananisha na yule mtu alieamua kuvivua vile viatu badili na kuamua kubaki peku huku akidhani hiyo ndio njia sahihi ya kuamua. Ili apate furaha ya milele, basi inambidi apate mtu sahihi wa kuwa nae. Unajua nini namaanisha?"



    “Hapana sijajua bado" Hawa alijibu kwa utulivu huku akimuangalia kijana huyo.



    Akapeleka macho yake juu ya dari la hilo darasa walilomo na alipoyashusha, moja kwa moja akamtazama mnyange huyo mwenye kila aina ya sifa za kuitwa mrembo, maana alikuwa katika mavazi ya shule ila uzuri wake ulionekana dhahiri, sipati picha akionekana kwenye mavazi ya kawaida.



    “Kila mwanadamu ameumbwa kwa moyo wenye upendo ndani yake, na moyo huo hupenda pale unapoona mtu alieuvutia, najua utajiuliza moyo kwani nao unamacho, ila tambua kuwa unapokea taarifa hizo kwenye ubongo zikitokea kwenye mboni za macho pindi pale yanapokuwa yameona kitu kilicho yavutia. Hadi hapo, kinapatikana kitu kinachoitwa Hisia, kuna hisia za aina nyingi, ila ambazo nazizungumzia hapa ni zile hisia zinazompata mtu pale anapompenda mtu." alipofika hapo akacheka kicheko kidogo, kisha akamuuliza swali. “Unajua kwanini nimetabasamu kama sio kucheka kabisa?"



    “Hapana sijajua" Hawa alijibu.



    “Sijacheka eti kwavile ni upumbavu, ila hata hivyo ni upumbavu kweli, kwasababu gani nakuambia hivyo. Kuna ambao hawezi kuzikontroo hizia zao kwa wale wawapendao, ndio pale hujikuta wanaenda kuroga ili ampate mtu ambao hisia zake zimemuelewa, huku wakisahau kuwa hata ulimi pia unaweza kuroga pale utakapoutumia vizuri. Ndio maana nikasema huo ni upumbavu ila upande wao wanaona sio upumbavu, kwasababu gani nakuambia hivyo, pale unapomroga mtu ili akupende, ndio inaweza ikatokea hivyo, ila tambua kuwa zile dawa au kizizi kwa lugha rahisi, zinapungua nguvu kila baada ya kuisha kwa siku, na mwisho yule aliemroga mtu kwa kizizi, pale kizizi kile kitakapoisha, basi zawadi yake ni kupokea maumivu kutoka kwa yule mtu aliemroga ili ampende na mwisho wa siku maumivu yanapo mzidi hupelekea kuwa chizi au hata kujiua kabisa. Nikisema hivi simaanishi wale waliochizika Kwajili ya mapenzi au kujiua kwaajili ya mapenzi wote wale wameroga ili wapendwe, la hasha! ila wengine yanawakuta hayo kutokana na kupenda sehemu ambayo sio sahihi kwao, hapo tuna wafananisha na yule mtu alievaa viatu badili bila ya kujua hiyo sio njia sahihi ya kuitafuta suluhu ya miguu yake kwenye jua kali" Akamaliza hivyo na kumuangalia machoni binti huyo, ni kama vile alikuwa akivuta punzi ili aendelee mbele zaidi, maana alijua hadi hapo huyo banati hajajua nini lengo lake la kumuambia maneno yote hayo, akavuta punzi ndani na kuzitoa nje, kisha akaendelea.



    “Najua haujajua ni kipi hasa kilichonifanya mimi nikakuweka hadi muda huu ambao wenzetu tayari wameshafika majumbani kwao, ila napenda tu kukuambia kuwa, unaweza ukaishi na kitu moyoni kwa muda mrefu pasi na kujua ni vipi utakitoa nje ili mlengwa wa hicho kitu akijue, kwa muda mrefu nilikuwa nikimuomba mungu anijaalie ujasiri wa kukiwasilisha kile ambacho kipo moyoni mwangu kwa muda mrefu, sina uhakika kwa hichi ambacho nitakiongea hivi punde kitakuudhi ama la, na kama ikiwa ni hivyo basi huna budi kunisamehe kutokana wanadamu hatukuumbwa kwa ukamilifu, nilazima tukoseane kisha tuombane msamaha ili tuzidi kuimarisha urafiki wetu kama sio undugu kabisa". akatulia kwa sekunde kadhaa, kisha akaendelea kuongea, kipindi hicho binti huyo alikuwa kimya kabisa utafikiri si yeye mwenye kuambiwa maneno hayo.



    “Hawa Nakupenda, Nakupenda kumaanisha, sitaki kuwa na wewe eti kwavile na mimi nijivunie kuwa na mwanamke mzuri mwenye kila sifa ya kuitwa mrembo, hapana, ila nakupenda kwasababu moyo wangu ndio umekuchagua wewe, sikukurupuka kukupenda eti kwa vile umeuvutia moyo wangu, bali nilikaa nikafikiri na kuona wewe ndie ambae utakae kamilisha uwepo wa kiatu chapili kwenye maisha yangu ili nisichekwe na kusemwa kuwa nimevaa viatu ambavyo sio sahihi. Hawa narudia tena kukuambia kuwa Nakupenda" Ramah alipofika hapo akatulia na kusikilizia mnyange huyo atasema nini.



    “Mmmh!! Ramah" Hawa aliishia kuguna na kuita tu jina la kijana huyo halafu asijue kitu gani aseme, akabaki kimya.



    “Hawa" Ramah alimuita na kumfanya binti huyo kuinua uso wake na kumuangalia kijana huyo, macho yao yalipogongana, akawahi kurudisha uso wake chini, Ramah kuona hivyo, akaendelea na alichopanga kusema.



    “Najua huamini kuwa mimi ndio nimekuambia maneno hayo, najua kuwa nimekushtukiza kukuambia hivi, ila tambua kuwa sikuanza kukupenda leo wala jana, nilikupenda muda mrefu, unaweza kuniuliza, Kwanini sikukuambia muda wote huo, ila tambua kuwa kila kitu kinatokea kwa wakati, huenda ikawa siku zote hizo haukuwa wakati sahihi wa kukuambia haya na ndio maana nikaja kukuambia leo baada ya kuona wakati sahishi umefika. Hawa naomba niwe Adamu wako kama yule Adamu wa Hawa, naomba niwe ubavu wako wa kulia kama ambavyo Hawa alivyokuwa ubavu wa kushoto wa Adamu" alipofika hapo akaushika mkono laini wa binti huyo na kumuambia. “Naomba uwe huru na jibu lako, maneno yangu yasikulazimishe unipende, japokuwa moyo wangu unataka unipende, sikulazimishi uwe na mimi, japokuwa mimi nataka niwe na wewe, kwahiyo usiumize kichwa kwa kufikiria ni jibu gani unaweza ukanipa, nipo tayari kupokea jibu lolote japokuwa nitaumia nikisikia ombi langu limekataliwa, nikuambie tu kuwa huru na jibu lako" Ramah aliongea kwa sauti ambayo ilikuwa ni ngumu sana kuingia kwenye ngoma za masikio ya mnyange yoyote halafu isimletee msisimko. Labda awe hana haiba za kike.



    “Ramah, nikuambie tu kwamba, kama vile ambavyo hukukurupuka kunifuata na kuja kuniambia hivyo, basi na mimi nakuambia kuwa siwezi kukurupuka na kukujibu chochote kwa leo, kwasababu ninaweza nikawa sahihi au sipo sahihi kwa hilo jibu, kwahiyo nahitaji muda wa kufikiria na mimi" Hawa aliongea hivyo huku akiwa macho yake akiyapeleka huku na huko pasi na kujua ni wapi anataka kuangalia.



    “Sikatai kukupa muda wa kufikiria, ila jua utaniweka roho juu juu kama mtu anaesubiria majibu ya kupima ukimwi, ok, nadhani siku ya leo inaweza kukutosha kabisa kwaajili ya kulifikiria hili?" Ramah aliongea hivyo huku akimuangalia binti huyo.



    “Usijali, hadi kesho nadhani nitakuwa ninajibu sahihi la kuja kukupa" Hawa aliongea.



    “Sawa, lakini naomba basi unitoe wasiwasi kwa hilo jibu utakalonipa"



    “Usijali Ramah, kwasasa naomba niende nyumbani maana hata muda pia tayari ushakwisha sana" aliongea hivyo huku akiutoa mkono wake kwenye viganja vya Ramah ambavyo muda wote vilikuwa vimeushikila mkono wake.



    “Sawa, mimi nakuruhusu uende ila tambua kuwa tangu muda huu, yupo mwanaume anaekupenda dhati kuliko wote duniani, tukiachana na baba yako mzazi"



    Hawa aliishia kutabasamu tu, kisha akainuka na kuanza kupiga hatua ndogo ndogo. Hapo ndipo uzuri wake ulipojidhihirisha dhahiri, alikuwa na umbo matata sana lililo jichonga mithili ya namba nane, alibarikiwa miguu ambayo ni wanawake wachache sana hapa afrika walikuwa wamebarikiwa, hakuwa mrefu sana wala hakuwa mfupi, na chaajabu zaidi, ni pale alipoanza kutembea, alikuwa kama vile hataki au ni mwenye kuiyogopa sakafu ambayo alikuwa akitembea juu yake, ilikuwa si rahisi kwa mwanaume rijali kutogeuza shingo yake pindi akipishana nae barabarani.



    “Hawa" Ramah muda wote alikuwa akimuangalia binti huyo anavyotembea, ikabidi amuite muda huo alikuwa ameshafika karibu na mlango wa kutokea, banati huyo aligeuka kwa mgeuko wa kipekee sana, aligeuka kwa taratibu sana utafikiri alikuwa akipelekwa “slow”, kisha akasimama huku akimuangalia Ramah.



    Ramah baada ya kuona mnyange huyo amesimama, akainuka pale alipokaa na kumfuata hadi pale aliposimama, wakawa wanaangaliana kama majogoo yaliotoka kupigana muda mfupi uliopita wakigombania kuku jike. Ramah akaunyanyua mkono wake wa kulia na kuushika mkono wa kushoto wa Hawa, kisha mkono wa kushoto wa Ramah akaushika mkono wa kulia wa Hawa. Hawa muda wote alikuwa yupo kimya huku sura yake ameinamisha chini. Ramah akamuita tena na kumfanya binti huyo anyanyue sura yake na kumuangalia kijana huyo. Mdomo wa Ramah, taratibu ulisoge ulipo mdomo wa binti huyo na kujikuta midomo yao ikigandana huku ulimi wa Ramah ukiwa ndani ya kinywa chake, hakuwa na jinsi zaidi ya kufumba macho ili kuyakwepa macho ya Ramah aliekuwa akifanya kitendo hicho huku akimuangalia yeye.



    Kitendo hicho kilidumu kwa sekunde kumi, baada ya hapo midomo yao ikaachiana na kubaki wametulia tu huku Hawa uso wake akiurudisha chini tena. “Nakupenda" hilo ndio neno la mwisho kutamkwa na Ramah hapo kisha akamuachia binti huyo na kumfanya aondoke haraka humo na kumuacha Ramah mwenyewe huku akitabasamu, tabasamu hilo lilipelekea kuwa ni kicheko, na kicheko hicho kikapelekea kuanza kurukaruka kama mtoto mdogo aliemuona baba yake akiwa anatoka kazini huku mkononi ameshika ‘icecream’ aliyoomba aletewa asubuhi wakati akiwa baba yake anatoka.



    Baada ya kuruka ruka sana, akaona anaweza kuitoboa sakafu hiyo ya hapo darasani kwa kufanya hivyo, akaamia kwenye meza, akapanda juu yake na kuanza kurukaruka huku akirusha mikono juu hadi pale alipoanguka na kuuteua mguu wake wa kushoto, aliinuka huku akiwa ameukunja uso wake Kwa maumivu, alianza kutembea kwa kuchechemea kwa maumivu ya mguu huku akiwa amechukia sana, ila uso ukabadilika na kuwa ni wenye tabasamu baada ya kukumbuka kitendo kilichomfanya hadi kuanguka hivyo, akaondoka darasani humo huku akichechemea na kutokomea zake.



    Majira ya tatu usiku, Hilda na Hemedy walikuwa wapo sehemu yao waliyoifanya ni pakusomea wawapo nyumbani kwao. Walisoma kwa saa moja nzima baada ya hapo wakafunga madaftari na kuanza kupiga stori za kawaida hadi pale, walipoishiwa na maeneno ya kuongea.



    “Hilda" Hemedy aliita na kumfanya binti huyo kumuangalia ishara ya kumtaka aendelee na kile anachotaka kukisema.







    “Kwani bado hujachoka tu kukaa hapa?" Hemedy alimuuliza.



    “Kuchoka kivipi yani?" Hilda naye aliuliza.



    “Mi nishachoka nataka nikalale"Hemedy aliongea.



    “Mi sijachoka, ila kama wewe umechoka, basi tuingie ndani"

    Walikusanya madaftari yao na kuingia nayo ndani, kwa vile walikuwa tayari wameshakula chakula cha usiku, basi kila mmoja aliingia chumbani kwake kwenda kuisaka kesho yake.



    Siku iliyofuata, shuleni kwao, Hemedy alikuwa na hamu ya kutaka kuambiwa kuwa Ramah alifanikiwa kwa kile alichokipanga siku ya jana, ila muda wa kufanya hivyo ndio ambao ulikuwa hakuna kutokana na vipindi vya asubuhi darasani kwao, walimu wote waliingia, hakuwa na budi tu kusubiri, akapanga atamuuliza ifikapo muda wa mapumziko.



    Muda wa mapumziko ulipofika, walichukuana yeye na Ramah na kuanza safari ya kuelekea kantini, walikuwa na mazoea ya kwenda watatu, ila kwa siku hiyo, Hilda hakuweza kutoka kutokana na kazi za kufanya alizokuwa nazo kumbana, yeye akabaki darasani huku wenzake wakienda kantini.



    “Oya mzee, haya nipe habari, ulifanikiwa jana au mtoto kazingua?" Hemedy alimuuliza baada ya kukaa kwenye viti wakisubiri chakula walichoagiza.



    “Anaanzaje kuzingua labda kimfano?" Ramah aliongea kwa majigambo huku akitabasamu.



    “Kivipi sasa, mbona hutaki kuninyooshea maelezo?" Hemedy aliongea.



    “Mtoto jana nimempiga masaundi halafu nikadai jibu langu pale pale, ila akasema hawezi kukurupuka kunijibu, akaomba nimpe siku ya jana afikirie kisha leo aniletee jibu" Ramah aliongea hivyo wakati huo vyakula walivyoagiza vikiwa mezani tayari.



    “Ukimuangalia matumaini ya kukubali anayo?" Hemedy aliuliza huku akikata andazi na kulitia mdomoni.



    “Aaaa!! Sidhani kama atakataa, kwasababu vile anataka kuondoka, mtoto nikamuita, nilipofika karibu yake nikamla denda, halafu nikamalizia na neno nakupenda kisha nikamuacha aende" Ramah aliongea hivyo kisha akachukua kikombe cha chai na kunywa.



    “Ebwana eeee!! Kwahiyo umemla hadi denda, hajazingua lakini?"



    “Azingue wapi? Katulia tu, yani hapa nina asilimia tisini na tisa za kumpata naweka asilimia moja tu za kumkosa"



    Majira hayo wakawa tayari wamemaliza kula, wakalipa na kuanza kuondoka hapo kuelekea darasani. Ramah alimuambia Hemedy kuwa muda huo anaenda kumfuata Hawa darasani kwao ili akapewe jibu lake, akaondoka darasani kwao na kwenda kwenye darasa analosoma binti huyo, alipofika akamuulizia na kuambiwa kuwa siku hiyo hakufika shuleni, hakutaka kuamini maneno ya mtu huyo, ikabidi amuulize mwengine na kupewa jibu hilo hilo kuwa binti huyo Hakufika shuleni.



    Akaondoka darasani humo kwa unyonge kama kifaranga cha kuku kilicho mwagiwa maji, akarudi darasani kwao na kutulia sehemu yake kisha akamuambia Hemedy kuwa binti hakufika shule leo. Wakaendelea na vipindi hadi pale kilipofika kipindi cha frii, ndipo walipoanza kupiga tena stori.



    “Kwahiyo jana hukumuambia chochote?" Ramah aliuliza.



    “Ndio jamaa, sasa unadhani ningeanzaje labda" Hemedy alijibu.



    “Dah! Jamaa unazingua kinyama yani, asa umeshindwaje kumuambia?" Ramah alimwambia kwa kulalamika utafikiri hilo jambo ni la muhimu kulifanya.



    “Uoga kaka, nina hofu nyingi mshkaji, sijui nimuanzaje"



    “Kwahiyo unakiri kabisa kwamba umemkosa?"



    “Hapana, ila leo nitajitahidi"



    Walimaliza maongezi hayo na kupiga stori nyengine, muda huo nae Hilda alikuja hapo na kupiga stori wote watatu hadi pale kengele ilipogongwa ya kutoka, wakaondoka shuleni hapo kuelekea majumbani kwao huku Ramah akimsisitiza mwenzake siku ya leo asifanye makosa.



    * *



    Kama kawaida yao, majira hayo ya usiku walikuwa kwenye kibaraza cha nyumba yao huku mbele yao kukiwa na meza ambayo juu yake waliweka madaftari wao wenyewe wakiwa wamekaa kwenye viti kuielekea hiyo meza, walisoma kile walichofundishwa kwa siku hiyo, ila siku hii ya leo Hilda aliona mabadiliko kwa Hemedy, hakuwa ni mwenye kuchangamka kama siku zote, ikambidi amuulize ni kipi kilichomfanya hadi kuwa katika hali hiyo?



    “We acha tu" Hemedy alijibu hivyo huku akionekana dhahiri ana jambo lililomsibu.



    “Sasa niache nini wakati nakuuliza. unaumwa?" Hilda aliongea hivyo huku akiupeleka mkono wake kwenye paji la uso wa Hemedy kupima kama ana joto.



    “Hapana siumwi Hilda, ila kuna kazi nimepewa niifanye" Hemedy aliongea kwa utaratibu.



    “Kazi gani hiyo?" Hilda aliuliza kwa shauku.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Nimepewa kazi ya kuuokoa moyo wa mtu zidi ya waizi na mabedui wanao utaka moyo huo kwa hali yoyote ile, kisha wakishaupata waufanye vile watakavyo halafu wauwache na kutupilia mbali ukiwa na maumivu makubwa ya kutelekezwa" Hemedy aliongea hivyo, ila Hilda hakuambulia chochote kwenye maneno hayo, akabaki akiyatafakari, mwisho akakosa jibu na kuamua aulize nini maana ya maneno hayo?



    “Hilda, jua kwamba nikiuacha huo moyo upotee, basi nina cha kujibu mbele ya alienituma, na mimi sitaki yote hayo yanitokee kwasababu nitakuwa sijamfanyia haki alienituma, kwasababu alinipa kazi hiyo muda mrefu, ila mimi nilikuwa nakosa njia ya kuulinda moyo huo" Hemedy alizidi kumchanganya binti huyo kwa maneno yake ya mafumbo.



    “Unajua Hemedy mimi sikuelewi, embu acha kuongea kwa mafumbo basi ili nikuelewe"



    “Upo tayari kunisaidia hiyo kazi bila kujali ugumu uliyokuwepo?" Hemedy alimuuliza.



    “Ndio Hemedy, kumbuka mimi na wewe tumetoka mbali, langu lako, lako langu, sasa ni vipi nikuache uifanye mwenyewe hiyo kazi wakati huenda uwezo wa kukusaidi ninao?" Hilda aliongea kwa upole.



    Hemedy baada ya kusikia hivyo, akamuangalia banati huyo usoni, kisha macho yake akayapeleka kwenye madaftari yaliyokuwa juu ya meza, alipofika hapo aliyagandisha macho yake utafikiri ni mwenye kuyaomba msaada madaftari hayo yamsaidie kuwasilisha kile anachotaka kusema. Akayaondoa macho yake hapo na kumuangalia Hilda aliekuwa muda wote akisubiri kuambiwa kwa ufasaha hiyo kazi aliyopewa Hemedy.



    “Hilda kazi hiyo nimepewa na moyo wangu nije kuokoa moyo wako juu ya wale wanaoutaka moyo wako kwa hali yoyote halafu wakishaupata waufanye vile watakavyo kisha waje kuutelekeza ukiwa na maumivu yatakayopambwa kwa chozi lako, na mimi sitaki yote hayo yatokee" Hemedy aliongea.



    “Sijakuelewa nini unamaanisha" Hilda sio kwamba hakuelewa maneno hayo, ila alitaka uhakika zaidi ndio maana akauliza hivyo.



    “Namaanisha Hilda Nakupenda, sitaki kuona unawakabidhi watu wengine moyo wako, wasiojua ni furaha ipi unaitaka, wasiojua ni kitu gani unapenda, wakati nikiwa mimi ninaeyajua yote hayo nipo" Akatulia kidogo, na kuendelea. “Hilda, nikisema nakupenda basi jua sikuongopei, ninakupenda kweli, naomba uuruhusu moyo wako useme na moyo wangu, naamini ndio utaamini haya niyasemayo, ila kama hutofanya hivyo, ukiruhusu masikio yako tu yasikilize maneno yangu, basi utaona kama vile nikiongeacho sikimaanishi au utafikiria na mimi ni mmoja wa hao mabedui wanaoutaka moyo wako wauchezee kisha wauache pasi na huruma ukiwa na maumivu ya kutendwa.

    Hilda naomba niwe faraja yako pale utakapo kuwa na huzuni, naomba nikutoe wasiwasi pale utakapokuwa na hofu, naomba nilidake chozi lako pale litakapo dondoka, naomba niwe mlinzi wako wa moyo wako mnyonge. Hilda ruhusu moyo wako useme na wangu basi" Ramah aliongea Kwa upole na kwakulalamika.



    “Hemedy unasema unanipenda?" Hilda muda wote huo alikuwa amekumbwa na butwaa asiamini masikio yake kuwa maneno hayo yanatoka kwa mtu aliemhusudu tangia siku ya kwanza anamuona. Haikujulikana ameuliza swali hilo kwa kutoelewa kuwa ameuliza au aliuliza kwa kupata uhakika zaidi, ila ni uhakika gani anaoutaka wakati kila kitu kipo wazi?.



    “Yes I love you, I want you to be my mine, and i promise you, I can't broken you are heart na kukuachia maumivu ambayo kwangu itakuwa ni huzuni, tafadhali naomba unielewe" Hemedy alitumia lugha ya kingereza ili kusisitiza kile akisemacho.



    Muda wote huo Hilda alionekana akiwa haamini macho yake kwa anayoyaona na haamini zaidi masikio yake kwa anayoyasikia. Ghalfa aliinuka hapo alipokaa na kuondoka mahali hapo na kuingia ndani amabapo moja kwa moja akaenda chumbani kwake na kujifungia mlango. Huku nje Hemedy alikuwa haelewi kilichotokea, akabaki kujiuliza, amekuaje huyu mwanamke? Mbona ameondoka haraka na kuingia ndani pasipo kusema chochote?



    Akajua sasa yale aliyokuwa akiyahofia ndio yameshatokea, akanza kuwaza akifokewa huku akitolewa nje ya nyumba hiyo akifukuzwa arudi kwao Tanga na Anti yake Hilda baada ya kwenda kusemewa, akajiona ni mpumbavu kumuambia Hilda maneno hayo, akajua tayari amemuuzi na kilichobakia hapo ni kumuomba msamaha kabla hayajatokea makubwa, akakusanya madaftari yote na kuondoka nayo kwa unyonge hadi sebuleni, kisha akauendea mlango wa chumbani kwa Hilda na kujaribu kuufungua, ila akaona umefungwa kwa ndani, ikambidi agonge tu ila hakukuwa na matokeo yoyote, akajua Hilda amekasirika ndio maana hakutaka kufungua mlango, ikambidi aanze kumuita, kisha akasema.



    “Hilda najua nimekuudhi kwa yale maneno niliyokuambia, ila tambua mimi sina kosa, mwenye kosa ni moyo wangu baada ya kukupenda wewe ambae muda wote tuliishi kama kaka na dada, ila kwaniaba yake, nauombea msamaha na nitaongea nao kuuambia kuwa ulipopenda hapakuwa mahala sahihi kwake, naamini utanielewa na kuacha tena kukufikiria kila wakati na utatulia mpaka pale utakapo pata moyo sahihi wa kuwa nao, na ninakuahidi Hilda nitakuwa na wewe pamoja mpaka pale utakapopata mtu sahihi wa kuwa nae, mwisho naomba unisamehe na mimi kwa kukuambia yaliyokuwa ndani ya moyo wangu, nakutakia usiku mwema" Hemedy aliongea kwa hisia kiasi kwamba hadi chozi la jicho la kushoto lilitoka, akalifuta na kuyaweka madaftari ya Hilda hapo hapo chini ya mlango kisha yeye akaingia chumbani kwake.



    Huko ndani ya chumba, Hilda alikuwa yupo nyuma ya mlango alikuwa akisikiliza maneno aliyokuwa akiyasema Hemedy, alikuwa akitabasamu muda wote, aliposikia ametakiwa usiku mwema, na yeye alisema kwa sauti ya chini, ‘Usiku mwema na kwako kipenzi changu' kisha akaondoka mlangoni hapo na kwenda kujitupa kitandani huku uso wake ukipambwa kwa tabasu muda wote.



    “Hemedy kumbe na wewe ulikuwa ukinipenda muda wote? Sasa Kwanini hukuniambia, umeniacha nikidhani ni mimi mwenyewe ndio ninaekupenda, kumbe hata wewe unanipenda, asante mungu kwa kuzifikisha hisia zangu kwa mtu nimpendae tangia muda mrefu, Hemedy nimeuruhusu moyo wangu useme na wako, nimegundua kuwa unanipenda kweli, nikuambie tu kuwa hata mimi nakupenda zaidi yako, huna haja ya kuniomba msamaha kwa kuniambia kuwa unanipenda ukidhani labda nimechukia kwa kile ulichoniambia, bali unahaja ya kuniomba msamaha kwa kuchelewa kuniambia kuwa unanipenda, nakuahidi nitakupenda hadi pale mungu atakapo chukua roho ya mmoja wetu. Nakupenda Hemedy"



    Hilda alikuwa katika furaha ya aina yake, alikuwa akiongea maneno hayo huku akiwa mikono yake ameifumbata kifuani kwake, alikuwa akiongea kihisia sana kama vile aliekuwa akiongea nae yupo mbele yake, akajaribu kuutafuta usingizi ila ulimjia baadae sana baada ya kutawaliwa na mawazo juu ya kijana Hemedy.



    Asubuhi kulipokucha, walijianda kwenda shule huku Hilda akijifanya kununa kupita maelezo, hali hiyo ilimtesa sana Hemedy, akapanga kumuomba msamaha watakapo kuwa shule muda ambao ulikuwa ni wa ‘Free’, wakaongozana kama kawaida huku Hilda akijifanya kununa, walifika shule katika hali hiyo hiyo na kila mmoja kuchukua nafasi yake kusubiri vipindi vianze.



    Muda wa mapumziko ulipofika, Hemedy na Ramah walichukuana hadi kantini kwenda kula huku wakimuacha Hilda akienda na marafiki zake wa kike kwenda sehemu hiyo.



    “Haya broo niambie jana ulifanikisha kumuambia?" Ramah alimuuliza hivyo baada ya kukaa kwenye viti wakisubiri waletewe chakula.



    “Dah! Mwanangu nimeharibu kila kitu, najuta hata kumuambia" Hemedy aliongea kwa masikitiko.



    “Kivipi mbaba?"



    “Jana wakati tunasoma hom, nikaamua kumchana, ila akaondoka kwa hasira na kwenda chumbani kwake kujifungia. Mimi nilijua tu kuwa yule demu hanitaki kimapenzi we ukajifanya kulazimisha, sasa yaliyotea ndio kama hayo nasijui nitayaweka vipi sawa"



    “Duh! Ila usijali jamaa, mimi nitakuombea msamaha naamini ataelewa tu"



    “Ramah usifanye hivyo, utazidi kuharibu, mimi yule leo nitamfuata mwenyewe na kumuomba msamaha, kwahiyo wewe usijali"



    “Dah!! Haya bwana, ila pole sana" Ramah alimuambia hivyo huku wakiendelea kula chakula walicholetewa.



    “Oya jamaa, mtoto Hawa leo kaja shule, vipi tayari ushaonana nae?" Hemedy aliongea baada ya kumuona Hawa akiwa katika kundi alilokuwa Hilda hapo kantini wakipata chakula. Muda wote huo Hilda na Hemedy walikuwa wakiangaliana kwa jicho pembe, yani walikuwa wakiangaliana halafu kila mmoja anaendelea na shuhuli zake.



    “Kaka nimemuona tokea asembo, wewe wala usijali nitamtafuata baadae"



    Muda wakawa tayari wamemaliza kula wakalipa na kuondoka mahali hapo kuelekea darasani. Ilikuwa ni kawaida kwa madarasa ya sanaa, kuwa vipindi vya mwisho kabisa, vilikuwa ni vipindi vya kujisomea wanafunzi wenyewe, na muda huo ndio alipanga Hemedy amfuate Hilda akamuombe msamaha kwa kile alichokifanya jana. Akatoka sehemu anapokaa na kwenda anapokaa Hilda, alipofika akavuta kiti ambacho hakikuwa na mtu kisha akakaa kumuangalia Hilda. Wakati Hemedy anaondoka kumfuata Hilda, Hawa nae alikuwa akiingia darasani humo na kumfuata Ramah, akamsalimia, kisha akamuambia kuwa baada ya watu kutolewa shuleni hapo, basi wakutane kwenye darasa lilelile walilokutaniana mwanzo, alipomaliza akaondoka huku akimuacha Ramah akimsindikiza kwa macho hadi alipopotelea nje.



    “Hilda" Hemedy aliita baada ya kukaa kwenye kiti kilichoangaliana na cha banati huyo, ila binti huyo akabaki kimya ni kama vile hakusikia huo muito, ikambidi Hemedy aendelee tu.



    “Najua nimekuudhi kwa nilichokifanya jana, ila tambua haikuwa lengo langu mimi kukuudhi wewe, nilikuwa najaribu kukuelezea hisia zangu, ila wewe ukazipokea katika hali nyengine, ukaona kama vile mimi sikuheshimu, ukaona kama vile nimekukosea adabu, wewe ukaona sio sawa mimi kufanya vile, lakini sivyo, na kama ingekuwa ndivyo,basi mungu asingetuumba na moyo wenye kupenda, ila yote kwa yote, naomba unisamehe na nipo tayari unipe adhabu ya aina yoyote ile ambayo utaona inalingana na lile kosa nililolifanya jana" Hemedy aliongea kwa upole na kwa utaratibu mno, kiasi kwamba Hilda alimuonea huruma mtu huyo kwa kumfanya ajione ni mkosaji wakati hata yeye mwenyewe alikuwa akimpenda.



    “Sikiliza Hemedy, kwavile umesema nikupe adhabu yoyote kulingana na hilo kosa lako, basi wewe nenda, baadae nitakupa hiyo adhabu na ole wako uishindwe, naomba uniache mwenyewe kwa sasa" Hilda alipoongea hivyo, akaikunja mikono yake juu ya meza yake na kukiweka kichwa chake juu yake kumaanisha kuwa hakutaka tena mazungumzo na kijana huyo. Hemedy akabaki akimuangalia tu mnyange huyo, akataka kusema kitu, ila akaghairisha, akaamua aondoke na kwenda kwenye sehemu yake.



    Nusu saa mbele, kengele ya kutoka ikagongwa na wanafunzi wakaondoka shuleni hapo. Ramah yeye akaelekea kwenye lile darasa alikotakiwa aende, alipofika tu, macho yako yakakutana na ya Hawa, alimuona binti ni kama vile mwenye kumsubiri kwa hamu sana mahala hapo, akapiga hatua za taratibu kumsogolea.



    “Sikiliza Ramah nikuambie, sikutaki na sitaki kuwa na wewe, usione kisa juzi umenila ‘romance' ukadhani eti ndio ushanipata, tambua kuwa sikuile nilichukia ila sikutaka kukuonyesha pale, na ninaomba kuanzia sasa ukiniona unione kama mkweo" Hawa aliongea hivyo huku akiwa mkono wake wa kushoto ukiwa kiunoni mwake na mkono wake wa kulia ukipepea hewani kama bendera iliokumbwa na kimbunga, alikuwa akiufanya kama wale wanawake wa uswahili wanaposutana.



    “Lakin....." Ramah alitaka kuongea ila alikatishwa na sauti ya Hawa.



    “Lakini nini? Ndo nshakuambia hivyo, muone kwanza" alipoongea hivyo akamalizia na sonyo refu na lenye sauti mithili ya firimbi ya refa anapotaka kumaliza mpira uwanjani. Kisha akaondoka hapo, ila alipofika mlangoni, akageuka tena na kumfuata Ramah aliekuwa bado amepigwa na bumbuwazi asielewe kinachotokea mahala hapo, hapo akajua kinachofuata ni kupigwa makofi na mwanamke huyo.







    ILA alishanga baada ya kumuona akija na tabasamu mwanana usoni mwake, tena safari hii alikuwa akija kwa mwendo ambao Ramah ulikuwa ukimchanganya kila amuonapo akitembea, akabaki akimuangalia binti huyo anavyokuja karibu yake, kisha baada ya kufikiwa karibu, akaona mikono ya mnyange huyo akiitanua na kumkumbatia yeye, kwa tukio hilo, akabaki haelewi nini kinachoendelea, akabaki tu kutoa macho kuangalia mbele huku kichwa chake kikiwa juu ya bega la binti.



    “NAKUPENDA Ramah" Hakutaka kuamini masikio yake baada ya kulisikia hilo neno likitoka kwenye kinywa cha banati huyo alietoka kumtupia maneno mabaya muda mfupi uliopita. Akamtoa kwenye kumbato hilo huku akimuangalia usoni mikono yake ikiwa kwenye mikono ya binti. Ni kama vile hakuwa akiamini, akabaki kumuangalia tu usoni kwa macho ya mshangao, ila alikutana na tabasamu ambalo lilimfanya akiri kuwa banati huyo ni mzuri tangu kwa mara ya kwanza kumuona shuleni hapo. Hawa nae ni kama hakutaka kutolewa kwenye kumbato hilo, akajirudisha tena mwilini mwa kijana huyo kisha akarudia tena maneno aliyoyasema mwanzo.



    “Hawa ni kweli unanipenda?" Ramah alimuuliza hivyo huku akiwa bado haamini.



    “Ndio Ramah nakupenda, nimeamua kukukabidhi moyo wangu kwavile nimekuamini, imani yangu kwako isiwe sababu ya wewe kuyatoa machozi yangu halafu yakakosa wa kuyafuta. Ramah kumbuka mapenzi yanauma pale unaempenda akikusaliti, inaweza ikapelekea hata mtu kujiua au kupata ukichaa kabisa, naomba yote hayo yasinikute, sijataka wala sitaki na sitotaka kulia machozi kwaajili ya mwanaume yoyote, kwahiyo naomba usinilize, usinifanye nijekujuta na kujiona mwenye hatia kwa kukukabidhi moyo wangu" Alipofika hapo, akajitoa kwenye kumbato la kijana huyo kisha akamuangalia usoni na kusema.



    “Ramah naomba uniahidi kitu" Hawa aliongea hivyo huku akimuangalia usoni.



    “Hawa, kama nilivyokuomba mwanzo kuwa Adamu wako, ndivyo ambavyo nimeufunga moyo wangu kwako, kama ambavyo nilivyoomba unihifadhi kwenye moyo wako, ndivyo nilivyo uhifadhi moyo wako kwangu. Kumbuka Hawa nimeumbwa na moyo mmoja tu, na moyo huo umeumbwa kwajili ya mwanamke mmoja tu katika ulimwengu huu, na huyo si mwengine bali ni wewe. Sitokuacha ulie pekeako pale utakapo patwa na tatizo, bali nitalia na wewe huku tukitafuta ufumbuzi wa hilo tatizo, chengine usitegemee kudondosha chozi kwaajili yangu, labda iwe kwa bahati mbaya tena sitoruhusu chozi lako dhaifu lidondoke ardhini, bali nitalidaka na kulifikicha viganjani mwangu kisha nitapangusa katika uso wangu. Nitakapokosea naomba unisamehe na wewe utakapo nikosea basi tambua nishakusamehe tangu sasa, na la mwisho nakuahidi kuwa, nitakuwa na wewe hadi mwisho wa maisha ya mmoja wetu. Sikuahidi kufa na wewe kwasababu hata nikifa na wewe sitozikwa na wewe. Nakupenda Hawa" Ramah aliongea kwa hisia kali mithili ya sharukhan kwenye muvi yake ya kuch kuch hotahe.



    Hawa muda wote alikuwa akitabasamu kusikia maneno hayo yaliyotoka katika kinywa cha Ramah. Ghalfa alikutanisha kinywa chake na cha mwanaume huyo, na kubadilishana kinywaji ambacho hakiuzwi mahali popote zaidi kwa yule umpendae. Hadi muda huo, walikuwa wamejisahau kuwa wapo darasani tena shule ambako muda wowote anaweza akapita mtu na kuwaona kile wanachokifanya.



    Kusimama waliona haitoshi, badala yake wakavutana hivyo hivyo kwa kugandana hadi katika ukuta wa hilo darasa, hapo walianza kushikana kila mmoja kwenye mwili wa mwenkaze. Ramah baada ya kuona haitoshi kutalii kwenye mwili wa mnyange huyo akiwa na nguo zake, akapeleka mkono wake chini ya sketi ya binti na kuanza kuinyanyua hiyo sketi kwa kuipandisha juu. Ila kitendo hicho hakikupata bahati ya kutimia baada ya mkono wa binti kuwahi kuzuia.



    “Ramah, hapo sio sehemu salama kufanya hivyo" Hawa aliongea kwa sauati ambayo ilikuwa tofauti na ile Ramah aliyowahi kumsikia binti huyo akiongea, sio kama ilikuwa ni sauti mbaya au yenye kuogopesha, la hashah! bali ilikuwa ni sauti ambayo ingemuongezea hashki mwanaume yoyote ambae alikuwa ni mzima yani rijali. Ramah hakuwa na namna, ikabidi waache kile wanachokifanya na kila mmoja akatabasamu kama sio kucheka kabisa, kisha wakashikana mikono ya kuanza kutoka darasani humo na kuelekea wanapopajua wao.



    * *



    Masaa yalikatika hadi kufikia majira ya usiku. Hemedy na Hilda, walikuwa katika sehemu yao ya kujisomea nyumbani kwao, siku hiyo kila mmoja alikuwa ‘serious‘’ na mwenzake, japokuwa walikuwa wakiulizana maswali, ila hakukusikia kicheko wala tabasamu usoni mwao, walisoma kwa saa nzima kama ambavyo walipanga wajisomee kwa muda huo.



    “Hilda, naomba unipe hiyo adhabu nianze kuitumikia kuanzia sasa, maana sipendi tukiwa katika hali hii ya kununiana. Moyo wangu unaniuma ninapoona sisemeshani na wewe, naomba unipe hiyo adhabu niko tayari kuipokea" Hemedy aliongea hivyo baada ya kumaliza kujisomea.



    “Hemedy uko tayari kuitumikia hiyo adhabu, maana ni adhabu ya milele" Hilda aliongea.



    “Niko tayari kuitumikia ili mradi nione unaongea na mimi tena, sipendi tukawa na Uhasama baina yangu na wewe" Hilda akamuangalia kijana huyo na kusema.



    “Adhabu yenyewe ni kuokoa na kuulinda moyo wangu kwa wale wanaotaka kuuharibu na kuupondaponda kisha kuuacha na maumivu yatayosababisha nitoe machozi. Je ukotayari kuitumikia adhabu hiyo?" Hilda alimuuliza Hemedy ambae alikuwa ameyatumbua macho yake kumuangalia Hilda kwa mshangao uliomkumba baada ya kusikia maneno hayo. Hakutaka kuamini moja kwa moja eti Hilda amekubali kuwa mpenzi wake. Akabaki kutulia tu asiseme chochote, sio kwamba hakuwa na lakusema au hakujua aseme nini, hapana, ila alikuwa bado ameganda kwa mshangao uliomkumba.



    “Hemedy nakupenda pia. Tangu mara ya kwanza kukuona ulipokuja kwenye sherehe yangu, sikujua kule kukuhusudu namna ile kumbe kulikuwa ndio kukupenda, sikujua kule kutaka kuwa karibu na wewe kumbe ndio kulikuwa ni kuikuza mbegu ya upendo wangu kwako, sikujua kuwa kule kutamani kuisikia sauti yako kila mara kumbe ndio kulikuwa ni kuimwagilia maji mbegu ya upendo wangu kwako, naamini hata wewe ulijua kuwa nilikuwa nakupenda, ila ukajifanya kutotambua chochote kile kuhusu upendo wangu, ukajifanya kutoona chochote pale nilipokuonyesha upendo wangu." Akatulia kidogo, kisha akamuangalia usoni, akaendelea. “Hemedy mbona hukuuruhusu moyo wako useme na wangu tangu muda mrefu? Mbona hukuruhusu mboni za macho yako zione upendo wangu tangu muda mrefu? Hemedy jua wewe ndio mwanaume wakwanza na wa mwisho kupendwa na moyo wangu, sitoweza kuja kuvumilia hata kidogo maumivu pindi ukiniacha. Sikuahidi kukutendea mabaya pale utakapo niacha, bali nauahidi moyo wangu kuutendea mabaya kwa kukupenda wewe kwasababu huo ndio sababu kuu ya maumivu yatakayo nipata mwili mzima. Hemedy tambua nilikupenda kabla wewe hujaanza kunipenda, naomba usiutumie udhaifu wangu wa kukupenda kama silaha ya kuniumizia. Nipende kama ninavyo kupenda na mimi nitakupenda zaidi ya ninavyo kupenda, kama ikiwa hivyo, naamini hata mungu atalibariki pendo letu lifike mbali zaidi. Nakupenda Hemedy" Hilda alikuwa akiongea kihisia hadi jicho moja lilitoa chozi dogo lililoishia kwenye shavu lake.



    Kwa mara ya kwanza tangu kuzaliwa kwao, siku hiyo ndio siku ambayo waliijua ladha ya kinywaji ghali kupatikana madukani au hata sehemu yoyote ile panapouzwa vinywaji, ila kinywaji hicho hupatikana kwa yule umpendae tu, kwa lugha ngeni wanaita ‘romance' ila kwa kiswahili mnaita ‘denda',.



    “Nakupenda Hemedy" Hilda aliongea hivyo baada ya kutosheka na kinywaji hicho huku akiskilizia utamu huo kwenye kifua kilichoanza kupevuka cha Hemedy.



    “Hilda adhabu uliyonipa kwa kile nilichokifanya inastaili kwangu, adhabu ambayo nilipewa na moyo wangu kuokoa moyo wako usipate machungu ya wale ambao wanataka kuuchezea, moyo ambao unathamani kubwa kwangu kuliko kitu chochote kile hapa duniani, sasa ni vipi niupataie machungu yatakayo ishi ndani yake milele? ni vipi niuache usononeke na kulalamika kwa kunipenda mimi? Hilda tambua yote hayo hufanywa na yule asiejua thamani ya pendo kwa yule ampendae. Hufanywa na yule mpumbavu anaependwa kisha ule upendo akaufanya ndio udhaifu wa kumnyanyasa yule ampendae. Ni vipi mimi nimlize alienipenda tokea utotoni wakati sijui hata kuvaa vizuri? sijui kujizuia pale nilipochapwa darasani kulia machozi mbele yake. Kwanza naanzaje kukuacha, naazaje kukusaliti, naazaje kuliacha chozi lako lidondoke ardhini pasi na kulidaka, naazaje kuruhusu kinywa chako kitoe sauti ya kilio kwajili yangu, naazaje Hilda? Labda unililie kipindi ambacho nipo kaburini, labda unililie kipindi ambacho nipo kitandani siwezi hata kuunyanyua mkono wangu kulidaka chozi lako, hata kama nisipoweza kulidaka chozi lako na kulifanya liangukie sakafuni kama sio ardhini kabisa, basi naamini pale litakapo anguka litajichora jina langu kuonyesha ni kiasi gana unanipenda, naomba na mimi usilidake chozi langu, liache liangukie chini kisha lijichore jina lako ili uamini kwamba na mimi nakupenda kama unipendavyo, nakuhitaji kama unihitajivyo”. Alipofika hapo, akapeleka mikono yake kwenye mashavu ya Hilda ambae muda wote alikuwa yupo kimya akitabasamu tu, alifanya kama vile ni mwenye kufuta futa kitu kwenye mashavu hayo, kisha akaendelea. “Nitakuwa mwanaume wa kwanza mpumbavu kuyafanya mashavu yako yalowane kwa machozi kwa kukuacha". Kisha mikono yake akaipeleka chini kwenye pua ya banati, halafu akasema. “Nitakuwa mwanaume wa kwanza mjinga kuzifanya pua zako zitoe kamasi pindi ukinililia kwa kukusaliti“. Akapeleka mikono yake chini kwenye mdomo wa banati huyo, halafu akasema. “Nitakuwa mwanaume wa kwanza mpumbavu na mjinga kuruhusu kinywa chako kitoe sauti ya kilio kwa maumivu yatakayotoka moyoni mwako chanzo ikiwa ni mimi. Hilda nimekubali kuitumikia adhabu uliyonipa ya kuulinda moyo wako mpaka kifo changu au chako"



    Alipomaliza kuongea, wakakumbatiana kwa muda kisha wakakusanya madaftari yao na kuingia ndani ya nyumba. Sebuleni walimkuta Anti yao akiangalia luninga huku akiwa ameshika sahani iliyokuwa na matunda mbalimbali juu yake.



    “Nyie wana mbona mnafuraha namna hiyo? nishirikisheni basi na mimi nifurahi" Anti yao aliongea hivyo huku akila kipande cha parachichi.



    “Anti wewe ushazeeka tukiamua kukushirikisha itapelekea ucheke halafu ikiwa bandama zenyewe zishazeeka kwahiyo unaweza ukapata matatizo ya kutokucheka kwasababu itakuwa zimeshakufa tayari kwa kucheka sana" Hemedy aliongea hivyo na kuwafanya Hilda na Anti yake wacheke.



    “Hilda umemuona huyo anavyoniambia? Embu nipigie kofi hapo hapo alipo" Anti aliongea hivyo huku akicheka na kumfanya Hemedy asogee mbali kidogo na alipo Hilda.



    “Niafadhali hata ungekuja mwenyewe kunipiga, lakini huyo unaemtuma ndio hajiwezi kabisaa"



    “Haaa!! Hilda umemsikia anavyokuambia, embu mpige basi na wewe ili aamini kuwa upo ngangari" Anti alipoongea hivyo. Hilda alinza kumfukuza Hemedy hapo sebuleni.



    “Kione hata kukimbia pia hakiwezi" Hemedy aliongea hivyo huku akikimbia kuizunguka hiyo sebule, walifanya hivyo kwa dakika moja nzima.



    “Waone walivyopendezana kama mtu na mtu wake vile" Anti aliongea hivyo huku akicheka na kumfanya Hilda asimame kwa ghafla na kumuangalia yeye.



    “Antiii" aliongoea hivyo huku akitabasamu. Tabasamu la aibu.



    “Kwani uongo? halafu nimegundua unampenda sana Hemedy hadi umekataa kuja pekeako huku ukililia kuja nae" Anti alizidi kuongea maneno yaliyomfanya Hilda azidi kuona aibu.



    “Ndio nini sasa hivyo Anti?" Hilda aliongea kwa kulalamika utafikiri kinachosema ni uongo.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Nilishangaa sana kaka aliponiambia kuwa umekataa kuja pekeako huku eti ukidai huwezi kuondoka bila huyo. sasa mimi nikawa najiuliza, anti yangu huyo ambae hataki kumuacha ni nani, nikasema sio kesi acha nisubiri akija nitamuona. Dah anti yangu umejua sana kuchagua, unahaki uone wivu kumuacha mkwe wangu Tanga halafu wewe uje pekeako huku" Hilda aliposikia hivyo, akajifanya kulia huku mkono wake mmoja akiupitisha kwenye macho yake, kisha akaondoka hapo sebuleni na kuelekea chumbani kwake akiwaacha Anti yake na Hemedy wakicheka tu.



    “Haya nenda kambembeleze mke wako maana tayari amenuna" Anti aliongea hivyo huku akicheka na kumfanya Hemedy aondoke hapo kuelekea chumbani kwake huku na yeye akicheka.



    * * * *



    Siku iliyofuata, walienda shule kama kawaida, ila siku hii walikuwa na furaha kuliko siku yoyote ile ambayo walikuwa shuleni hapo. Siku hii walitambulishana wote wanne, yani Ramah alimtambulisha Hawa kwa Hemedy na Hilda kwamba ni mpenzi wake na Hemedy nae alifanya vivo hivyo, wakawa wakifurahi tu muda wote, ila vipindi vya darasani viliwanyima uhuru wa kufurahia pamoja, wakapanga wikiendi hiyo waende katika ufukwe maarufu katika mji huo, ufukwe ambao watu wengi hupenda kuenda kutokana hakukuwa na kiingilio ufukweni hapo, yani palikuwa ni free tu.



    Coco beach, ndipo walipopanga kwenda kufurahia wote kwa pamoja mwisho wa wiki hiyo. Baada ya muda wa kutoka shuleni hapo kufika, waliongozana kuelekea majumbani mwao. Ramah, Hemedy na Hilda waliachana na Hawa njiani huku wao wakielekea pamoja maana wao walikuwa wakikaa mtaa moja japokuwa nyumba zilikuwa ni tofauti, ila hakukuwa na umbali wowote kutoka wanapokaa wakina Hemedy hadi nyumbani kwakina Ramah.



    Hemedy na Hilda, walipofika nyumbani kwao, walikutana na ugeni uliowafanya wafurahi kukutana nao, hasahasa Hemedy ndie alikuwa ni mwenye furaha zaidi. Walimkuta Mrutu akiwa yupo hapo akiwasubiri wao, walisalimiana kwa furaha baada ya kutoonana kwa miaka mingi. Mrutu aliwaletea zawadi ya simu aina ya Samsung J7 kila mmoja yake na kuwafanya wafurahi zaidi, baada ya kufurahi sana, Mrutu akaaga kutaka kurudi Tanga siku hiyo hiyo akidai amekuja mara moja tu kibiashara, ila alikutana na pingamizi kubwa kutoka kwa Hemedy na Hilda waliomtaka alale tu kwa siku hiyo kisha kesho ndio aondoke, wazo hilo liliungwa mkono na Anti yao na kumfanya Mrutu kukosa tena cha kujitetea, akalala kwa siku hiyo.



    Sikuiliyofuata, Mrutu aliaga na kuondoka huku akiwaachia kiasi cha pesa Hemedy na Hilda, ambao walifurahia uwepo wake hapo, na wao wakajianda kuelekea shule wakaimalizie siku hiyo ya mwisho kabla ya kuingia wikiendi. Walipofika shule wakakutana tena na Ramah na Hawa, siku hiyo walikuwa wakisisitizana kuwa kesho yake ndio siku ya kwenda kuinjoi ufukweni. Hemedy na Hilda, walichukua namba za Ramah na Hawa baada ya kuwaambia kuwa na wao wanatumia simu, ikawa shangwe nyengine baada ya kupata mawasiliano yatakayoweza kuwaweka karibu zaidi.



    * * * *



    Siku iliyofuata. 10:45 Jioni. Coco Beach.



    Watu hao walikuwa katika furaha ya aina yake siku hiyo waliyoipanga kuja kufurahi hapo, Ramah na Hemedy hawakuishia kufanya mzaha kila muda ili mradi tu watu wao wafurahi, walifanya hiki na kufanya kile na kupelekea vicheko vitawale muda wote, baada ya kuzunguka zunguka sana kwa pamoja, wakatawanyika na kila mmoja akaenda kukaa sehemu yake na mtu wake, yani wakawa wawili wawili.



    Wakiwa hawana hili wala lile wao wakiendelea na kufurahi kwao, kwa mbali kuna watu walikuwa wakiwaangalia kwa umakini sana, watu hawa ndio wale tulianza kuwaona wakimfuatilia Hemedy tangu anashuka Ubongo kwa mara ya kwanza katika jiji hilo. Jamaa mmoja kati ya hao wawili, akatoa simu na kubonyeza bonyeza kisha akaiweka sikioni huku akiwaangalia vijana wale wote wanne japokuwa kwasasa walikuwa wamejitenga wapo wawili wawili.



    “Mkuu, naona huyu kijana amejiingiza kwenye mapenzi na yule mjukuu wa Inspekta" Kijana huyo akaongea hivyo baada ya simu kupokelewa.



    “Mnachotakiwa nyie ni kuwaangalia tu wasidhurike na chochote, hilo swala la kusema wapo katika mapenzi waachieni wao wenyewe, kwanza pia itazidi kumfanya awe kama vile KIONGOZI anavyotaka kwasababu atapitia mambo mengi yatakayo mfanya awe vile sisi tunavyotaka"



    “Lakini mkuu huoni kama hiyo itakuwa ni hatari kwake? Mi naona asijiingize kwenye mapenzi kwasasa" Kijana aliongea.



    “Asu, sikuhizi tunafundishana kazi sio?” Sauti ya upande wa pili ilinguruma.



    “Hapana mkuu, ila nilikuwa najaribu kushauri tu, nisamehe sana mkuu" Jamaa ambae kwa sasa tunamjua kwa jina la Asu baada ya mtu wa upande wa pili kumuita hivyo aliongea.



    “Basi fuata kile ninachosema mimi. nawaambia tena, hakikisheni ulinzi kwa huyo kijana unazidi kuongezeka siku hadi siku, kumbukeni kuwa Kiongozi anamhitaji huyo kijana kuliko vile mnavyofikiria nyie"



    “Sawa Mkuu. Halafu kuna jengine nataka kukuambia" Asu aliongea.



    “Lipi hilo?" Sauti ya upande wa pili uliuliza.



    “Ni kwamba, huyo kijana ana urafiki mkubwa na mwanao Ramadhani au Ramah kama ambavyo wanamuita"







    “Kwani wapo wapi?" Sauti ya upande wa ilisikika.



    “Wapo huku ufukweni Coco Beach" Asu alijibu.



    “Wapo wangapi?"



    “Wapo wanne mkuu, nikimaanisha kuwa kila mmoja yupo na mtu wake" Asu alijibu.



    “Kwahiyo Ramah pia anampenzi? Hahahah! watoto wa siku hizi bwana! haya endeleeni kuwaangalia, hakikisheni ulinzi kwa wote"



    “Sawa mkuu tumekuelewa" Asu alikata simu na kumgeukia mwenzake.



    “Oya Kanu, mkuu anasema tuimarishe ulinzi kwa wote wanne. Kama vipi twenzetu pale kwa yule mzee tukale madafu, au wewe unasemaje?" Asu aliongea.



    “Twenzetu kaka, ila hawa watoto wanafaidi kinyama, embu ona hao mademu waliokuwa nao, Dah! wakali kishenzi yani" Kanu aliongea hivyo akiwa anawatupia macho vijana hao huku wakielekea sehemu ambapo palikuwa kuna mzee amepaki baiskeli yake akiuza madafu na machungwa.



    Walipofika wakanunua madafu na kuanza kula hapo hapo huku wakiwatupia macho muda wote vijana hao. Ila muda kidogo waliwaona vijana wale wakiume wakiinuka sehemu walipokaa na kuwaacha wasichana zao huku wao wakija hapo hapo walipokuwa wapo wao.



    “Oya Asu, naona hao madogo wanakuja na hapa hapa, halafu si unajua kuwa huyo dogo mmoja tunaemlinda tulishawahi kumuokoa kwa wale waliomteka, sasa huenda ikawa bado sura zetu anazikumbuka, kwahiyo akituona hapa anaweza akajiuliza maswali mengi halafu ikapelekea mpango kuharibika, embu tuwape mgongo" Jamaa anejulikana kwa jina la Kanu alimuambia mwenzake hivyo baada ya kuwaona Ramah na Hemedy wakija sehemu hiyo hiyo waliyokuwa wao.



    “Unawasiwasi tu jamaa, miaka ni mingi sana tangu azione sura zetu sidhani kama atazikumbuka, ila kwa tahadhari zaidi tugeuke tu" Asu alisema hivyo huku akigeuka kwapa mgongo watu hao.



    Walipofika hapo walinunua kila mmoja anachotaka, Ramah yeye alinunua madafu mawili huku Hemedy akinunua machungwa mawili. Kisha kila mmoja akarudi sehemu ambayo amemuacha mtu wake na kwenda kukaa nae. Hemedy alipofika kwa Hilda, akamkabizi chungwa moja kisha akakaa karibu yake.



    “Sweetie" Hemedy alimuita huku akiwa macho yake ameyaelekezea baharini.



    “Abe Honey" Hilda aliitikia.



    “Unajua Kwanini nimeenda kununua machungwa?"



    “Hapana baby sijajua"



    “Embu kwanza kula kipande kimoja" Hemedy alipoongea hivyo, Hilda akang'oa kipande kimoja cha chungwa ambalo tayari lilikuwa limeshakatwa, kisha akalila nusu halafu akamuangalia Hemedy kusubiri aambiwe ni kwanini ameenda kununua machungwa. Ila aliambiwa akimalizie kipande chote na yeye akafanya hivyo.



    “Ni ladha gani umeipata wakati unakula kipande hicho?" Hemedy alimuuliza.



    “Tamu" alijibu.



    “Vizuri. Chungwa ni tunda ambalo lina ladha ya kipekee sana tofauti na matunda mengine yote. Mchungwa unatokana na mmea wa mlimao ambao umekatwa na kuunganishwa kiutaalamu na kuufanya utoke katika uhalisia wake wa mlimao hadi kuwa mchungwa" Hemedy alipofika hapo alikatishwa na swali la Hilda.



    “Kwahiyo unataka kuniambia michungwa yote inatokana na milimao?" Hilda aliuliza hivyo huku akionekana dhahiri kuwa na mshangao kwa hicho alichokisema Hemedy.



    “Hapana, kuna mengine kama ile ya zamani tena sanaa, ile ilikuwa yajitegemea, ila hii ya sasa mengi ni ya kupandikiza miche. Kipindi cha uhai wa baba yangu aliwahi kunipeleka kwenye mashamba yake huko kijijini, alionionyesha vitu vingi sana moja wapo ni hilo la kuubadilisha mlimao kuwa mchungwa, nilishangaa sana kuona hivyo, ila sikuwa na jinsi ya kubisha ikiwa mwenyewe nimeshuhudia kwa macho yangu"



    “Kwahiyo ukiuunganisha mlimao unabadilika hapo hapo na kuwa mchungwa?" Hilda aliuliza swali lililomfanya Hemedy acheke.



    “Hapana Hilda haubadiliki hapo hapo, ila unaweza ukachuku hata mwezi ila kama ukipata maji unaweza ukachukua hata wiki tatu"



    “Mmhu! Nakusikiliza mpenzi" Hilda aliongea hivyo huku mkono wake wa kushoto akiupitisha juu ya shingo ya Hemedy na kwenda kuishia kwenye bega lake la kushoto.



    “Wakati ukiunganishwa, unaanza kuchomoza taritibu ila hapo inakuwa ni baada ya wiki mbili na siku kadhaa, baada ya kuchomoza, unakuwa na kubadilika kabisa kuwa ni mchungwa halisi huku shina la chini likiwa ni la mlimao. Baada ya miaka, kunaanza kuchomoza kwenye matawi maua flani hivi na maua hayo ndio yanakuja kuwa ni tunda chungwa, ndio pale sasa unakuta watu wanakula au wengine kuuza kabisa ila hapo ni baada ya kuwa mbivu haliwezi kuliwa likiwa bichi, kwasababu badala ya kupata utamu utapata uchungu. Unajua nini namaanisha?" Hemedy alimuuliza hivyo Hilda. Ila alikataa kwa kichwa kuashiria kuwa hajajua nini amemaanisha.



    “Namaanisha kwamba, tunda hili halija kuwa tu hivi hivi na kuwa ni tamu, mmea wake ulianza kumwagiliwa maji baada ya kupandwa, kisha ukachomza na kutunzwa vizuri kwa kupaliliwa kwa kuondoa majani ambayo yameota pembeni yake, yani unaachwa ukiwa upo pekeake. Kisha ukaendelea na kukua na kukua na kukua hadi ukanawiri, ukafikia hatua ambayo hata pawe na kiangazi gani basi haiwezi kutetereshwa na chochote, hadi muda huu ambao wewe unalila na kuliona tamu, basi ujue mmea wake umepitia mambo mengi sana" Hemedy alimaliza kuelezea.



    “Nimekuelewa ulivyoelezea ila nataka unifafanulie zaidi maana" Hilda aliongea.



    “Maana yangu ni kwamba. Upendo huanzia chini sana, unaanza kwa kuchipua kwenye mioyo miwili iliyopendana, na ili ukue, basi inabidi umwagiliwe maji ya maneno mazuri yenye ladha kwa yule anaetamkiwa. basi mtaona upendo ukikuwa kadri siku zinavyozidi kwenda, lakini kuna watu ambao hawatapenda vile mnavyopendana, watamizongazonga kwa maneno mabaya au hata waongee maneno ya uongo ilimradi tu upendo ufe. Ndio pale kwenye mmea wa mchungwa unapopaliliwa kuondoa majani ambayo yanauzongazonga ule mmea, maana pasipo kufanya hivyo, itasababisha ule mmea kutokukuwa vizuri au hata kufa kabisa. Mapenzi nayo ndivyo yalivyo. ili tuishi vizuri, inatubidi tusisikilize ya watu, au tuwasikilize kwasababu maneno hayakwepeki, ila tusiyape nafasi sana ya kuyamini, inabidi tufanye uchunguzi kwanza, kisha tukibaini yana ukweli ndani yake, basi ndio tuchukue maamuzi" alipofika hapo, akamgeukia Hilda na kumuangalia usoni. “Ila tusichukue maamuzi wakati tunahasira" akageuza shingo yake mbele na kuendelea kuangalia bahari na watu baadhi waliokuwa wakiogelea. “Tukiupalilia upendo wetu basi utakua imara sana kiasi kwamba hakuna ambae ataweza kutetenganisha labda mungu pekee atakapo chukua roho ya mmoja wetu. Hapo tutakuwa kama ule mmea wa mchungwa ambao umepaliliwa na kukua, hata pawe na kiangaza kiasi gani hauwezi ukatetereshwa. Kwa vile itakuwa tumeuimarisha upendo wetu, basi tukakuja kufaidi baadae matunda ya upendo wetu na kuufurahia na kuuona mtamu kama vile ambavyo wewe umekisifia hicho kipande cha chungwa ulichokila. Nikisema hivi simaanishi kuwa kwa sasa hatufaidi upendo wetu, hapana tunafaidi sana, maana hata huo mmea wa mchungwa unatumika kama kivuli kipindi ambacho haujatoa matunda. hata sisi tutakuja kufaidi vizuri baadae tukija kuwa familia moja huku tukiwa na watoto wetu. Kwahiyo mpenzi wangu naomba tuwe kama mmea wa mchungwa, tuumwagilie maji upendo wetu maana tayari ushachipua, kisha tuupalilie kuondoa mabua na majani ambayo yataufanya upendo wetu kutokukuwa vizuri au hata kufa kabisa, tukifanya hivyo, utakua na kukua na kuwa imara hata watu wakiongea maneno yao kuhusu sisi tuwafananishe na kile kiangazi ambacho hakiwezi kuuteteresha mmea hata kidogo, mwisho tutakuja kufaidi upendo wetu baadae kama vile ambavyo tunayafaidi haya machungwa kwa sasa. Mpenzi wangu tuwe kama mmea wa mchungwa" Hemedy alihitimisha hivyo na kumpiga busu la kwenye paji la uso Hilda. Hilda busu hilo akaona kama vile halitoshi kwake, akataka na denda na bila hiyana akapatiwa, walifanya hivyo bila kujali watu waliokuwa wakipitapita mahala hapo.



    Turudi nyuma kidogo wakati Ramah anaenda mahali alipokaa Hawa huku mikononi akiwa ameshika madafu mawili, alipofika hapo akampatia Hawa dafu moja kisha akakaa karibu yake.



    “Malikia wangu" Ramah aliita.



    “Niambie Mfalme wangu" Hawa nae alimuita huku mkono wake wa kulia akiuingiza kwenye mkono wa kushoto wa Ramah kisha akamlalia begani.



    “Unajua kwanini nimenunua madafu?" Ramah alimuuliza.



    “Sijajua ila ninaweza nikabahatisha"



    “Embu bahatisha nione"



    “Ni kwavile yana maji matamu na nyama yake ya ndani pia ni laini na tamu" Hawa alijibu huku akitabasamu.



    “Safi sana umejibu vizuri hadi nimependa. Embu kunywa kidogo maji yake ili unisibitishie ni kweli ulichokisema?" Ramah alimuambia hivyo na kumfanya Hawa avute maji yaliyokuwa ndani ya dafu kwa kutumia mrija, akavuta kidogo na kuacha kisha akamuambia Ramah kuwa maji hayo ni matamu kama alivyosema. Ramah akasema.



    “Dafu ni mwanzo wa kuwa nazi, na nazi imeota kwenye mnazi ambao ulipandwa kwa begu ya nazi iliyokomaa. Katika mimea ambayo huchelewa kukua kuliko mimea yote ninayoijua mimi ni mnazi. Mnazi unaweza ukachukua miaka zaidi ya sita kukua na kutoa nazi, simaanishi hii minazi ya kisasa ambayo ikipandwa mwezi mmoja tu unatoa nazi hata kama haujakua vizuri, minazi ambayo haiwezi kuvumilia dharuba kubwa hata kidogo hadi kupelekea kufa. nazungumzia minazi ambayo babu zetu ndio waliokuwa wakiitumia, hawakuwa na papara kwa kukua kwake kwasababu walijua baadae itakuja kuwa imara zaidi. Walipofukia ardhini mbegu ambazo ni nazi zilizokomaa, wakasubiri baada ya muda mfupi, zikachomoza kutoka ardhini, hapo wakamwagilia maji na kuufanya mmea ule ukue zaidi, ukafikia wakati wa kuupalilia, wakapalilia na ilipofikia wakati wa kuvumilia jua kali na ukame, wakaiiacha ikue yenyewe, maana walijua mimea hiyo inauwezo wa kuvumilia chochote kile ambacho mimea mingine haiwezi kuvumilia na kupelekea kufa kabisa. Ulipofika wakati huo sasa ndio wakaachana nayo kwavile walijua mimea hiyo ni yenye kuvumilia kila hali, hawakuwa na papara kwa kusubiria miaka mingi kwasababu walijua baada ya miaka hiyo watakuja kupata zao lililokuwa bora, na sio zao tu, hata hiyo mimea haiwezi kufa yenyewe kwa hali yoyote ile, labda waamue kuiua kwa kuikata. na wataikataje wakati wameipanda wenyewe na kuimwagilia maji wenyewe na kusubiri kwa muda mrefu hadi kuja kupata faida? watakuwa wapumbavu kwa kufanya hivyo au labda wawe na maana yao kubwa kufanya hivyo. Sijui umenielewa vizuri na kujua kile ninachokimaanisha?" Ramah alielezea kisha akamuuliza.



    “Ndio nimekuelewa na nimejua vitu vingi sana ambavyo nilikuwa sivijui kuhusu mnazi, ila sijajua nini umemaanisha"

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ni kwamba. Mapenzi yanaanzia chini sana kama vile ambavyo mbegu ya mnazi ilivyopandwa chini. Kisha mapenzi huchipua taratibu na kuhitaji kumwagiliwa maji ya upendo ili yakue zaidi, halafu ya yaimarishwe kwa kutosikiliza maneno ya watu wasiyopenda yaimarike kama ambavyo mmea wa mnazi ulipopaliliwa kuondolewa majani yaliyouzunguka ule mmea ukapelekea ukue bila tabu. Naamini tukifanya hivyo haitakuwa na haja ya kuchungana kwenye mapenzi, zaidi kila mmoja atajichunga mwenyewe asiliharibu penzi lake kama ambavyo wale wazee walipoiyacha mimea hiyo ikue yenyewe baada ya kujua kwa hapo ilipofikia haiwezi kutetereshwa na chochote. Kisha tutasubiri japokuwa ni kwa muda mrefu sana hadi kuja kutimia malengo yetu hapo baadae, hadi hapo malikia wangu tutakuja kufaidi mazao ambayo yatakuwa ni imara zaidi na mapenzi yetu hatutaweza kuyaua wenyewe. Na kwanini tuyaue wakati tumepata tabu ya kuyatunza na kuwa imara hadi hapo yalipofikia? Labda mungu tu ndie anaeweza kuyaua tena atayaua kwa kuichukua roho ya mmoja wetu, lakini bado naamini upendo utaendelea kuishi mioyoni mwetu hadi pale tutakapo ingia katika ufalme wa mungu. Malkia wangu tuwe kama mmea wa mnazi" Ramah alimaliza kuongea na kuupitisha mkono wake wa kushoto kwenye kiuno bambataa cha Hawa, kisha ndimi zao wakaziunganisha mithili ya njiwa jike anapolilisha kinda lake.



    Majira hayo wakanyanyuka na kuwafuata wenzao waliokuwa mbali kidogo na walipokuwa wao, walipofika pale wakaungana wote kwa pamoja na kupiga stori hadi pale walipoona inatosha kuwa mahala hapo, wakainuka wote na kuanza kuondoka kuelekea yalipo makazi yao.



    * * * *



    Wikiendi iliisha na kufuatia jumatatu ambayo wanafunzi walitakiwa wawepo mashuleni baada ya kupumzika kwa siku hizo mbili. Shule ya sekondari Benjamini Wiliamu Mkapa, wanafunzi walikuwa wakiendelea na vipindi muda huo wa asubuhi, hadi pale ulipofika muda wa mapumziko, ulipofika, walienda wote kupata chakula, walipomaliza, Hawa alimuomba Ramah ampeleke chooni, wakaongozana kuelekea huko huku wakiwaacha wenzao wakirudi darasani.



    “Oya Babeli, si nilikuambia kuwa yule demu anachukuliwa na yule Ramah, haya sasa wale pale shuhudia mwenyewe kwa macho yako" alikuwa ni kijana mmoja aliekuwa amekaa na wenzake watatu kwenye gogo sehemu ambayo ilikuwa ni mbali kidogo na ilipo njia ya kuendea chooni akimwambia kijana mmoja aliekaa mwisho kabisa wa gogo hilo.



    “Dah! Yani yule demu mimi kanichomolea halafu kaenda kumkubalia yule boya?" Huyo kijana aliejulikana kwa jina la Babeli aliongea huku akisikitika asiamini macho yake kwa anachokiona, maana alishawahi kuambiwa kuwa Hawa mwanamke ambae alikuwa akimfukuzia kila siku anatoka na mtu mwengine, ni jambo ambalo lilimuuma sana kupita maelezo.



    “Jamaa, mimi nilikuwa nakuambia kila siku ila wewe ukawa unabisha, sasa unaona mwenyewe jamaa akimpeleka demu chooni" Kijana wa mwanzo kuongea alisema.



    “Hataa!! Mimi wanangu sikubaliani na hili jambo hata kidogo. Subiri nikamuamshie pale pale yulo boya" Babel baada ya kuongea hivyo, alinyanyuka hapo alipokaa na kuanza kupiga hatua kuwafuata Ramah na Hawa waliokuwa wakielekea chooni, alipanga akafanye fujo.





    ENDELEA..



    “We jamaa acha uboya wewe, sasa ukienda kufanya fujo pale mbele ya yule demu unadhani atakuelewa tena? Si atakuona mduanzi tu huna lolote, unatakiwa umfuate yule jamaa akiwa pekeake ndio umuanzishie ila ukimfanyia fujo mbele ya yule demu basi ujue ndio utamkosa kabisa" Babel alisimama baada ya kusikia maneno ya yule kijana wa mwanzao kuongea, akayapima na kuona yana ukweli ndani yake, akaghairisha alichotaka kwenda kukifanya na kurudi pale walipo wenzake.



    “Mwanangu ghadhabu sana yani, yule demu mimi kila nilivyokuwa nampanga anyee kwenye poti yeye alikuwa akijifanya ananyea nje, kapangwa kidogo tu na yule boya anajifanya amekubali, halafu sasa walivyo na dharau wanakuja kujipitisha mbele yangu kwa makusudi kabisa ili mradi tu waniumize moyo, ila mimi yule boya siwezi kumuacha hivi hivi hata kidogo, lazima nimfunze adabu" Babel aliongea kwa hasira hadi mishipa ya shingo ikamtoka, halikuwa swala la ajabu kwa wenzake maana waliijua ndio tabia yake ya kutaka wanawake kilazima hata kama ikiwa wenyewe walikuwa hawataki. Kilichomtia jeuri ni utajiri wa nyumbani kwao.



    “Nakukubali mkali unapoamua lako, ila kwa pale unatakiwa uende kistaarabu sana, ukienda hovyo hovyo basi ujue utamkosa" Kijana mwengine aliekuwa pembeni ya yule aliongea mwanzao akaongea.



    “Sijakuelewa shebe nini umemaanisha" Babel aliongea.



    “Ni hivi, yani unatakiwa umtafute Ramah halafu umkanye kwa maneno, akijifanya kichwa ngumu basi tunamzingua" Shebe aliongea.



    “Je kama tukimzingua halafu pia akijifanya haelewi?" Babel aliongea hivyo lakini alionekana dhahiri hakurizika na ushauri wa Shebe.



    “Hapo ndio tutajua cha kufanya mzee" Shebe aliongea.



    “Aaaa!! Mwanangu yule boya nishaanza kumtamani, yani nataka nikamfunze adabu hata sasa, asa we Shebe unaponiambia habari za kumkanya sijui na nini naona kama vile tunamlea tu"



    “Lakini Babel alichoongea Shebe ni cha kweli, tusimletee mtiti kabla hatuja muonya kwanza" Kijana wa mwanzao kuongea alisema kuunga mawazo ya Shebe.



    “Mnama mimi sio kama sijamuelewa Shebe, nimemuelewa sana ila naona kama vile habari za kumkanya ni kupoteza muda tu" Babel aliongea.



    “Lakini Babel yule gashi si alikukataa, muachie jamaa bahati yake, mimi naona haina haja ya kuwekeana Uhasama na mwaume mwenzetu kisa demu tu" Kijana wa mwisho anaetimiza unne wao aliongea.



    “Oya msikilizeni huyu boya anavyoongea? Mimi namiambieni huyu jamaa snichi tu, ona sisi tunapanga mipango ya kumteka demu yeye analeta maneno yake ya ki**nge hapa" Babel aliongea kwa sauti ya kupaniki hadi akamfanya huyo alieongea maneno hayo kuogopa, maana alimjua mtu huyo hakawii kuleta fujo sehemu yoyote hata iwe wapi. Anaikumbuka sana siku ambayo Babel alipo wagomea walimu kuchapwa kisa kuja shule na gari huku akiwa ameifungulia muziki mwanzo mwisho wakati huo ulikuwa ni wa asubuhi wanafunzi wakiwa wapo mstarini, kitendo kilichowafanya wanafunzi wote wageuke nyuma kuliangalia hilo gari linalo piga muziki kiasi hicho wakati wao wakiwa msatarini. ndipo hapo aliposhuka Babel kwa jeuri kubwa utafikiri kitendo alichokifanya ni sahihi, kitendo hicho kilipelekea kupelekwa osifi ya walimu na kutaka kumuadhibu, ila aliwagomea wote huku akiwatishia kuwafanyia kitendo kibaya endapo watamgusa na fimbo zao. kwa nguvu ya pesa za baba yake, kesi hiyo iliisha baada ya mzazi wake kuja shuleni alipopewa barua ya kumleta mzazi wake.



    “Oya Lacho unajua sisi hatukuelewi kabisa, yani wewe sio mara ya kwanza kupinga mipango yetu tunayoipanga, sasa wewe kama ushaona hili kundi limekushinda, basi likatae kimya kimya, hatuwezi tukashirikiana na maboya kama wewe" Mnama aliongea kumuambia Lacho kijana wa mwisho kuongea. Walimuita Mnama kutokana na kabila lake la Kichaga.



    Majira hayo kengele iligongwa na kuwafanya wainuke hapo walipokaa na kuanza kuondoka kuelekea madarasani mwao, wote hao wanne walikuwa wakisoma mchepuo mmoja wa masomo ya biashara kidato hicho hicho cha tatu. Walingia darasani huku wakipanga kumfuata Ramah baadae ili wamuonye kwa kile kitendo cha kuwa na Hawa kimahusiano.



    Muda ambao ulitumika kama mapumziko ya pili au muda wa kwenda kufanya ibada kwa wale wenye imani ya dini ya kislamu, ndio muda huo waliopanga wamtafute Ramah na kumuonya kama walivyopanga. Walifanikiwa kumpata na kumchukua kiurafiki tu hadi lilipo gogo ambalo wao wamelifanya kama ni maskani yao muda wa mapumziko.



    “Oya Ramah, unajua sisi sote hapa ni wanaume, na mwanaume siku zote anapoambiwa jambo huwa ni muelewa sana, sasa jamaa kama sote hapa ni wanaume kuna jambo tunataka tukuambie kistarabu kabisa" Mnama alianza kuongea baada ya kufika mahala hapo.



    “Nawasikiliza wana, ongeeni" Ramah aliongea.



    “Ni hivi, yule demu unaetembea nae ni demu wa mshkaji wetu hapa Babel. Jamaa roho ilimuuma sana baada ya kukuona na demu wake akataka kuja kukufanyia fujo ili tukamtuliza na kumuambia kuwa tukuite halafu tukuambie maana huenda ikawa ulikuwa hujui" Ramah aliposikia maneno hayo alitabasamu na kumuuliza.



    “Kwahiyo nyie mlikuwa mnataka nini?" Ramah aliongea huku akiwa anatabasamu, kitendo hicho na swali hilo, Babel alivitasfiri kama dharau, akataka kumuanzishia fujo ila wenzake wakamzuia.



    “Mimi niliwaambia kuwa huyu boya ni ms***ge tu, sasa si mnaona majibu yake ya kishoga shoga anayoyaleta hapa? Haikuwa na haja ya kumuonya wala nini, huyu alitakiwa afanyiwe tu kabla ya yote, tena anadharau anapita na demu wangu mbele ya macho yangu halafu nyie mnasema aonywe?" Babel aliongea kwa sauti kubwa kiasi kwamba hadi wanafunzi waliokuwa wakipita hapo walisikia alichokuwa akiongea.



    “Tuliza munkari Babel" Shebe akamtuliza, kisha akamgeukia Ramah na kumuambia. “Ramah sisi tulichokuwa tunataka ni kuachana na yule gashi wa mshkaji wetu, vinginevyo utatafuta vita na sisi" Shebe aliongea hivyo, lakini Ramah bado alikuwa na tabasamu usoni mwake, ilionekana hakutishwa na maneno ya Shebe wala kupaniki kwa Babel hata kidogo.



    “Sikilizeni majamaa, nadhani hiyo vita itakayokuja ni vita ya tatu ya dunia baada ya pili kuisha, na nimiambie tu kuwa sitishwi na maneo ya nyie washamba msiojua kubembeleza mademu mkitaka wamipende kifosi. Niko tayari kwa hiyo vita" Ramah aliongea kwa kujiamini kiasi kwamba akawafanya vijana hao midomo yao kuwa wazi kwa mshangao, maana hawakuwahi kumchimbia mtu biti halafu alete maneno ya kujiamini kiasi hicho.



    Ramah alipoongea hivyo, akanza kuondoka mahala hapo kwa kujiamini huku akimuacha Babel akishikiliwa na wenzake kwa kumzuia asimfuate Ramah aliekuwa akiondoka kwa majivuno sana. Babel baada ya kuona hawezi kuchomoka kwenye mikono ya hao wenzake, akabaki akimtukana Ramah huku akimuahidi kumfanyia kitendo kibaya ambacho hatoweza kukisahau maishani mwake.



    “Oya jamaa, wale wajinga leo wameniita hadi kwenye lile gogo lililokuwa njia ya kuendea chooni, mi basi nikadhani wataenda kuniambia maneno ya maana, kumbe wameenda kuniongelea maneno yao kike waliyozoe kuwatishia hao maboya wengine wakidhani na mimi nitakuwa boya" Ramah alimuambia Hemedy baada ya kufika darasani kwao.



    “Hao wajinga ni wakina nani na wamekuambia maneno gani?" Hemedy alimuuliza baada ya kuona hajamuelewa vizuri.



    “Si hao wanaojiita STAREHE BOYZ" Ramah aliongea na kumfanya Hemedy acheke sana kisha akanyamaza baada ya dakika.



    “Si wale mapimbi wanne? Wamekuambiaje?" Hemedy alimuuliza huku akiwa bado anatabasamu lililoelekea kucheka.



    “Hao hao Man, eti wameniita hadi pale, mi nikajua wanataka kuniambia ishu ya maana kumbe wananiambia eti niachane na Hawa kwasababu ni demu wa Babel" Ramah aliongea.



    “Kwahiyo na wewe ukaamini hicho kitu?" Hemedy alimuuliza.



    “Aaaa!! Jamaa naanzaje kuamini maneno yao ya kutolea sanduku kwa mke?"



    “Lakini ukanyeta kwa mkwara wao?"



    “Kumbe mwanangu na wewe pia unaniona mimi boya?"



    “Hapana man nimekuuliza tu, maana wale jamaa wamewachimbia biti watu wengi halafu wote wakanyeta kwa mikwara yao, ila sio kwamba nimekuona boya jamaa"



    “Asa mwanangu unadhani na mimi ni boya kama walivyo hao wengine? Mimi nilipofika pale, wakaanza kuniambia maneno yao, nikawa nawasikiliza tu, halafu nikawajibu kidharau na kutangaza vita na wao, kwahiyo mwanagu nina Uhasama na wale makolo, hivi ninavyokuambia muda wowote ninaweza kuwashiana moto na wale wajinga" Ramah aliongea.



    “Kumbuka mimi nimeanza kuwa na urafiki na wewe tangu siku ya kwanza kuja hapa shule, hadi hivi sasa tumekuwa marafiki wakubwa sana, tena sio marafiki tu, tumekuwa ni ndugu kabisa, kwahiyo mwanangu sitokubali hiyo vita uipigane mwenyewe, lazima mzee tutakuwa pamoja, hawatuambii chochote wale wajinga" Hemedy alichoongea alikuwa akimaanisha, maana alikuwa akiongea ‘serious’ huku uso wake ukiwa hauna tabasamu kama mwanzo. Kosa alilofanya Ramah ni kutokumuambia hilo jambao Hawa, wakapanga wapambane wenyewe wawili bila ya kujua kwa kutokumuambia Hawa hilo jambo linaweza kuja kuleta matatizo kwenye mapenzi yao baadae. Hawakujua. Na hawatojua kwasababu wametawaliwa hasira bila ya kuchukua hatua juu ya kitendo hicho. Hawakujua kamwe.



    * * * *



    “Sasa nyie madogo mtatupa kiasi gani kuifanya hiyo kazi"



    “Nyie semeni mnataka kiasi gani ili kazi ikamilike" Babel aliongea kuwaambia watu hawo walionekana dhahiri kuwa na vitendo vya kihalifu.



    “Kwavile katika hiyo kazi Kutahitajika gari la kukodi, inabidi mtupe laki tano, yani hapo hatupunguzi wala hatuongezi" Jamaa mmoja kati ya wenzake wawili aliongea.



    “Msijali ilimradi kazi ikamilike tu" Babel aliongea.



    “Msiwaze maninja, si mmesema asife yani tumuadhibu huku tukimkanya aachane na demu wako?"



    “Ndio ni hivyo tu" Babel aliongea.



    “Basi acheni hela nusu ili tupate kulipia hilo gari la kukodi" Jamaa huyo aliongea hivyo huku akiwasha bangi, wenyewe wanaita ‘sigara kubwa'. Babel aliingiza mkono mfukoni na kutoa kiasi cha pesa, kisha akazihesabu zilipotimia hela anazotaka akampatia Jamaa.



    “Nyie maninja wala msijali, hiyo kazi tutaifanya kesho, halafu usiku wa kesho tutawapigia simu kumijulisha kilichoendelea"Jamaa aliongea hivyo huku akizitia hela hizo kwenye mfuko wake wa suruali, kisha akatoa moshi wa bangi kwenye tundu moja ya pua yake, sijui aliweza vipi kuizibiti tundu ya pili isitoe moshi, kitendo hicho nilikifananisha na bomba la pikipiki aina ya YAMAHA inavyotoa moshi wakati ikiwekwa oili mpya.



    Babel na wenzake waliondoka kwenye jumba hilo chakavu(Boma) ambalo mmiliki wake alilitelekeza muda mrefu pasi na kulifanyia ukarabati wowote na kulifanya liwe ni jumba la kujihifadhi wahuni hao, waliondoka na kuelekea wanapopajua wao wakiwaacha wahuni hao wakifurahia kupata pesa za bwerere jioni hiyo.



    * * * *



    Siku iliyofuata majira ya jioni, Hemedy alienda kwa kina Ramah baada ya kijana huyo kuwa ni mwenye kumuhitaji nyumbani kwao kwa siku hiyo, hilo halikuwa tatizo kutokana na umbali uliokuwepo kutoka kwakina Hemedy hadi kwa rafiki yake. Alipofika hapo, wakasalimiana kidogo kisha wakaingia chumbani kwa Ramah, huko hakukuwa na chengine zaidi ya kucheza gemu mchezo ambao huupenda sana wawapo nyumbani hapo, gemu la mpira ndilo ambalo hupendelea sana kulicheza kuliko mchezo wowote kwenye hicho kifaa.



    Majira ya saa kumi na mbili kamili za jioni, walichoka kuicheza hiyo gemu na kuhamia sebuleni ambapo waliweka picha ya IP MAN kwenye luninga wakawa wanaangalia, ila hiyo picha haikufika hata robo yake, Hemedy akaaga kutaka kuondoka akidai nyumba yao hakuiacha na ulinzi mkubwa maana siku hiyo hakukuwa na watu zaidi ya yeye na mlinzi. Hilda na Anti yake waliondoka nyumbani hapo kuelekea wanapopajua wao huku mlinzi nae akitarajia kuondoka majira hayo ya jioni kuelekea alipoagizwa aende na Anti yao, kwahiyo nyumba itabaki tupu ikiwa nae mlinzi akiondoka.



    Ramah hakuwa na budi kuondoka nae, maana hata kama akisema abaki hapo nyumbani kwao, hatokuwa na kampani yoyote kwahiyo ni bora waende wote huko, halafu baadae kidogo atarudi nyumbani kwao, wakakubaliana hivyo na kuanza kuondoka nyumbani hapo. Wakati wakiwa wapo njiani kuelekea kwakina Hemedy, nyuma yao kulikuwa kuna gari inayowafuata bila wao kujua.



    “Hii ishu ishakuwa ngumu, si unaona wapo wawili na sisi tunamtaka yule mmoja" Jamaa ambae jana alitakwa na Babel wamteke Ramah aliongea kuwaambia wenzake wakiwa kwenye hiyo gari inayowafuatilia wakina Ramah bila wao kujua.



    “Hapa mazee haina budi kuondoka nao wote wawili" Jamaa mwengine aliongea.



    “Kwanini wakati sisi tunamtaka huyu mmoja tu" Jamaa mwengine aliekuwa amekaa siti za nyuma aliongea.



    “Kwasababu tukimchukua huyu mmoja, huyu atakaebakia anaweza kupiga kelele au hata kuzisoma namba za gari halafu baadae kwetu ikawa shida, kwahiyo ni bora tuwachukue wote wawili halafu tutajua chakufanya mbele ya safari"



    Wakakubaliana kufanya hivyo, wakawa wanawasubiri wafike sehemu ambayo haina watu wengi wafanye hilo tukio. Mbele kidogo wakaona sehemu hiyo itafaa kwa hiyo kazi, bila kuchelewa waliwaekea gari ubavuni mwao, kisha kwa haraka zaidi wakawashika kwa kuwavuta hadi ndani na kuwatia humo, walijitahidi kufurukuta ila ndio hivyo hawakuweza, walikuwa wamedhibitiwa na mikono yenye nguvu ya watu hao na kuwafunga kamba za mikono ambayo waliileta kwenye migongo yao, kisha usoni wakawafunga vitambara vyeusi ambavyo viliwadhibiti vizuri kutokuona chochote.



    Kitendo hicho kwa Hemedy kilikuwa ni kawaida japokuwa alikuwa na wasiwasi mwingi, maana yeye hayo matukio ya kutekwa kama hivyo hakuyaanza leo wala jana, aliyaanza tangia akiwa yupo Tanga, kwahiyo kwa kiasi fulani akawa ameyazoea. Ila kwa Ramah tangu azaliwe hakuwahi kufanyiwa kitendo cha kutekwa hata kwa bahati mbaya, yeye ndie aliekuwa na wasiwasi mwingi kuliko hata mwenzake, alikuwa akiwaomba sana watu hao wawasamehe bila kujua wamefanya kosa gani, ila alikuja kunyamaza baada ya kutulizwa na kofi moja matata lililotua kwenye mdomo wake, akaona mdomo wake ukimzidi uzito, bila kupenda akaacha mwenyewe kupiga kelele.



    Safari hiyo iliishia kwenye lile jumba chakavu ambalo wahuni hao au watekaji hao walilifanya kama ndio masakani kwao, jumba hilo lilikuwa lipo mbali na nyumba nyengine kutokana na sehemu hiyo kutokuwa na nyumba nyingi, kwahiyo hata kama wangesema wapige kelele kiasi gani wasingeweza kusikika. Waliingizwa ndani humo na kuanza kupewa mateso hasahasa Ramah huku akiambiwa kuwa kosa lake ni kuchukua mwanamke wa mtu, alipigwa sana huku akiambiwa akiri kumuacha huyo mwanamke mara atakapo achiwa hapo, ila kama akijifanya kiburi basi hatoweza kutoka salama humo ndani.



    Ramah alikataa katakata kukubali kumuacha huyo mwanamke anaeambiwa aachane nae, haikujulikana ni kiburi au ni nguvu ya penzi ndio inayomfanya akatae kusema kuwa amekubali kuachana na huyo mwanamke, lakini hiyo haikuwa ni kiburi kilichomfanya kutokukubali kusema kuwa amekubali kuachana na huyo mwanamke ambae hata kama angesema amekubali kuchana nae, basi asingeweza kusikia chochote kutokana na kuwa hapo hakuwepo. Sasa ni vipi akatae kukiri hata kwa uongo ili tu kuiokoa nafsi yake? Mapenzi bwana!.



    Walimpiga hadi sasa wakawa wanaona huko wanapoelekea wanaweza wakamzimisha kama sio kumuua kabisa, ikabidi wampigie simu aliewapa hiyo kazi, wakamuelezea vyote kwamba kijana amekataa kumuacha huyo mwanamke anaedai ni mwanamke wake, kilichowafanya kumpigia simu ni kutaka kujua wafanye nini maana mtu huyo anaoneka hakuwa na hata na dalili za kukubali kile wanachokita, ila jibu walilopewa kuwa wamvunje hata mguu lazima tu atakubali asitake atake, walipopokea agizo hilo, wakakubaliana nalo na kumfuata Ramah aliekuwa chini hajiwezi huku damu zikiupamba mwili wake wote, walipanga wamvunje mguu ama mkono ili tu akubali kile wanachomlazimisha kukikubali.







    JAMAA mmoja wakati akijiandaa kuuvunja mkono wa Ramah, alishtuka akipigwa teke la mbavu lililomfanya agugumie kama mbwa mdokozi aliepigwa jiwe wakati akiwa anajaribu kufunua mfuniko uliofunikiwa kwenye sufuri la nyama lililokuwa jikoni. Jamaa wa pili akiwa bado na kiwewe asielewe nini kilichomkuta mwenzake hadi kurushwa pemebeni mithili ya mcheza sarakasi. Alikuja kushtuka akipokea ngumi ya uso yenye uzito usio mithilika iliyomfanya aone kama dunia yote amebebeshwa kichwani huku nyota zikimzomea na kumdhihaki kwa kitendo alichotaka kukifanya, akakosa muelekeo kwa kuyumba yumba kama mlevi wa pombe chafu aina ya mataputapu, akabaki mikono yake kaiweka usoni mwake akishindana na maumivu anayoyasikia.



    Jamaa wa tatu na wamwisho alipoona wenzake kila mmoja akigugumia kwa maumivu, akajaribu kutaka kukimbia ili kuiokoa nafsi yake kwa hao watu waliowafanyia uvamizi wa ghafla. Ila alijishangaa kujikuta hewani akielea kama tiara iliyokuwa ikichezewa na mtoto, wakati akiwa huko hewani, alijiuliza ni kipi hasa kilichompeleka huko wakati muda mfupi tu uliopita alikuwa akitembea ardhini, ila kabla hajapata jibu sahihi, alijikuta akitua chini kwa nguvu mithili ya gunia la viazi lililotuliwa chini kwa ghadhabu na mbebaji aliekosa maelewano mazuri na tajiri aliemtaka ambebee alipeleke kwenye gari lake, alikuja kupata jibu ya kilichomfanya kuwa katika hali hiyo baada ya kuona guu la haja likitua chini baada ya kutoka kumuadhibu yeye.



    Wote watatu walibaki chini wakigaagaa kama watoto wadogo walionyimwa sufuria la uji walilotaka kulikombeleza baada ya uji kuisha. Waliofanya shambulizi hilo la ghafla walikuwa ni Asu na Kanu vijana ambao walitumwa kuhakikisha ulinzi wa Hemedy kwa masaa ishirini na nne, baada ya kumaliza kufanya tukio hilo, wakaondoka hapo bila ya kutoa msaada wowote kwa vijana hao na kwenda kwenye gari yao na kutimka mahala hapo.



    Huko ndani ya jumba, wale wahuni walikuwa bado wapo chini hawajiwezi hata kunyanyua vidole vyao kwa maumivu wanayoyasikia kwenye miili yao. Kipindi chote hicho Hemedy ambae alikuwa anaunafuu kwenye mwili wake kwasababu yeye hakupigwa sana na wahuni hao, alikuwa akisikilizia yote yanayoendelea hapo, hakuweza kuona chochote kutokana na kitambara alichofungwa nacho usoni.



    Baada ya purukushani kuisha humo ndani, akaona pako kimya sana, ikambidi aanze kujitahidi kuzifungua hizo kamba alizofungwa nazo mikononi mwake, haikuwa rahisi kuzifungua hizo kamba kutokana na kuwa zimekazwa sana, baada ya kujitahidi sana, akafanikiwa kuzifungua na kukifungua kitamabara alichofungwa nacho kwenye macho. Alipepesa pepesa macho kwa dakika moja baada ya kutoona vizuri kutokana na kufungwa kitambara hicho kwa muda mrefu, baada ya macho yake kupata nuru nzuri, aliwashuhudia watekaji hao wakiwa chini wamelala kila mmoja akishika sehemu yake anayoona inamfaa kwa kupoza maumivu aliyopatiwa na wavamizi waliowavamia kwa ghafla, hakujua ni kipi hasa kilichowakuta watu hao hadi kuwa katika hali hiyo, akapiga jicho pembeni na kumuona Ramah akiwa hajiwezi kwa kipigo alichopokea.



    Hemedy hakutaka kupoteza muda, akamuwahi Ramah na kumfungulia kitambara alichofungwa nacho machoni na kumfungulia na kamba alizofungwa nazo mikononi. Kisha akambeba mgongoni na kumtoa nje ya jumba hilo, hakujua aelekee uelekeo upi kwasababu walipoletwa hapo walikuwa wamefungwa vitambara kwenye macho yao, akashika njia iliyoekuwa kulia kwake baada ya kukosa jibu sahihi ya njia ipi aende.



    Wakati Hemedy akiwa amembeba Ramah mgongoni mwake huku akikimbia kuelekea njia ambayo hajui atatokea wapi. Mbali kidogo kulikuwa kumepaki gari ambayo tumezoea kuwaona nayo wale waliotumwa kumlinda Hemedy. Watu hao walikuwa wakiwaangalia vijana hao wanavyokimbia kutoka sehemu hiyo waliyotekwa. Asu kama ambavyo tunamjua, alitoa simu yake na kuiminyaminya kisha akaiweka sikioni kwake.



    “Ndio mkuu tumefanikiwa kuwasaidia na tumewaacha wenyewe wajisaidie na hapa tunapoongea Hemedy amembeba mwenzake mgongoni wakiondoka sehemu hii" Asu aliongea.



    “Vizuri sana, lakini Hemedy si hajaziona sura zenu?" Mtu wa upande wa pili alisifia na kuuliza.



    “Hapana mkuu hajaziona kwasababu walikuwa wamefungwa vitambara kwenye macho yao"



    “Anatakiwa asizione sura zenu maana hiyo itamfanya ajiulize maswali mengi kuhusu kufuatiliwa kila mara na nyie"



    “Sawa mkuu"



    “Hakikisheni ulinzi unakuwa mkubwa kwa hao vijana hadi watakapofika majumbani kwao. Kumbukeni Kiongozi anamuhitaji Hemedy kuliko kitu chochote" Mtu wa upande wa pili alisisitiza.



    “Sawa mkuu, ila nashauri na huyu kijana wako pia umuingize katika huo mpango maana nae anaonekana ni jasiri sana"



    “Huyo hawezi kuwa katika huo mpango, ila mimi nitamfunza mwenyewe kile ambacho tunataka kumfunza huyo mwenzake, kwahiyo huyo atakuwa ni wangu mimi kama mimi"



    “Sawa mkuu acha tuwafuatilie maana wameshafika mbali na tulipo sisi" Asu baada ya kuongea hivyo, alikata simu na kuwasha gari kuwafuatilia wakina Hemedy. Hawa watu ni wakina nani? Na wanampango gani na Hemedy? Na huyo Kiongozi ni nani? KIZUNGUMKUTI.



    Hemedy alitembea hadi akachoka, maana mgongoni mwake alikuwa amembeba Ramah ambae kidogo hali yake kwasasa inaanza kuwa nzuri kutokana na kipigo alichopokea. Alimbeba hadi alipofika barabarani na kukuta taksi zikiwa zipo nyingi mahala hapo, akaita moja na kuomba iwapeleke hospitali iliyokuwa karibu, kisha akamuingiza garini Ramah na yeye akaingia humo na safari ya kwenda hospital ikaanza.



    Walifika katika hospitali hiyo ya binafsi na kumshusha Ramah kwenye gari akisaidiwa na dereva taksi kumuingiza ndani ya hiyo hospital, walipokelewa na manesi waliokuwa eneo hilo na kumuingiza Ramah kwenye chumba maalumu kwajili ya matibabu. Hemedy alimlipa dereva taksi kiasi chake cha pesa alichokitaka na dereva akaondoka akimuacha Hemedy akielekea kwa daktari aliekuwa amemuita osifini kwake mara baada ya kutoka kwenye chumba alicholazwa Ramah.



    “Yule mgonjwa ni nani yako?" Daktari alimuuliza hivyo Hemedy baada ya kumkaribisha kukaa kwenye kiti kilichopo humo osifini mwake.



    “Ni ndugu yangu yule. Kwani hali yake inaendeleaje Daktari?" Alijubu kisha akauliza.



    “Hali yake sio mbaya sana ila inabidi leo alale hapa ili tujue hali yake itaendeleaje baadae. Kwani hakuna mkubwa yoyote uliekuja nae?" Daktari alimuuliza.



    “Hapana hatukuja na mtu yoyote Dokta"



    “Basi fanya mawasiliano na watu wa nyumbani kwenu ili waje hapa" Daktari alipoongea hivyo, Hemedy akainuka na kutaka kutoka humo ndani, ila sauti ya dokta ndio iliyomfanya akaacha kufungua mlango wa kutokea na kumuangalia usoni.



    “Vipi, mbona unaondoka tena?" Daktari alimuuliza baada kuona mtu huyo akitaka kuondoka.



    “Naenda kuichukua simu yake, maana hiyo ndio ina namba za watu wa nyumbani" Hemedy aliongea na kumfanya Daktari kumruhusu kwa kichwa. Kisha akaondoka na baada ya dakika moja akarudi na simu ya Ramah, akaingia sehemu ya majina na kutafuta jina litakalo faa kulipigia, akapiga baada ya kupata jina lililoandikwa ‘FATHER' kisha akamkabidhi simu Dokta baada ya kusikia ikiita.



    “Haloo" Sauti ya upande wa pili ilisikika ikongea.



    “Ndio. We ndio mzazi wa.." Alipofika hapo akamgeukia Hemedy aliekuwa ametulia kimya akisikiliza, ishara hiyo aliielewa na kulitaja jina la Ramah kisha Daktari akamtajia mtu huyo wa upande wa pili.



    “Ndio ni mimi" Sauti ya upande wa pili ilijibu. Sauti hii ndio ile sauti ambayo tunaisikia kila mara Asu anapoongea na simu kuhusu Hemedy. Daktari baada ya kusikia kuwa huyo anaeongea nae ndio mzazi wa mgonjwa, akamuambia aje hapo hospitali kuna tatizo limemkuta mwanae, mtu huyo wa upande wa pili akajifanya kushtuka na kutaka kuambiwa kuwa mwanae nini kimemkuta, ila Daktari akamuambia aje atakuja kujua huku huku.



    Baada ya dakika ishirini, ofisini humo kuliingia mtu mzima ambae kwa makadirio alikuwa na miaka arobaini hadi arobaini na tano, alikuwa mfupi na mwenye rangi ya maji ya kunde, hakuwa mnene sana ila alikuwa na mwili kidogo. Alipofika hapo akawasalimia aliowakuta na kuambiwa akae kwenye kiti chengine.



    “Niambie Dokta nini tatizo lililomkumba mwanangu" Mzee huyo aliongea kwa hofu utafikiri alikuwa hajui kilichomkumba Ramah.



    “Muulize huyu ndugu yake aliemleta ndio atakuelezea kila kitu kisha mimi nitakupa matokeo ya hali ya mwanao" Daktari aliongea.



    “Eti Hemedy, ni kipi kilichomkuta mwenzako" Mzee huyo alimgeukia Hemedy na kumuuliza hivyo. Utajiuliza imekuaje hadi mzee huyo kumuita Hemedy jina lake, ila ni kwamba Hemedy sio mara ya kwanza kuenda nyumbani kwakina Ramah, hata yeye alikuwa akifahamiana na huyo mzee kama baba wa rafiki yake.



    “Tulivamiwa na watu tusiowajua wakati tunatoka nyumbani kuelekea nyumbani kwetu, wakatuingiza kwenye gari lao na kutupeleka sehemu tusioijua,huko ndio wakatupiga sana ila Ramah ndio wamempiga sana hadi akawa hajiwezi" Hemedy hakutaka kuficha ila alificha kilichowapelekea kutekwa na watu hao.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    “Sasa kwanini wamiteke na wakamipigie huko msipopajua?" Baba yake Ramah alimuuliza. Ila swali hilo lilikuwa gumu sana kwa Hemedy kulijibu, akabaki kimya kwa sekunde kadha akifikiria ajibu nini.



    “Hatujajua kwasababu wao walikuwa wakitupiga tu bila kutuambia chochote" Hemedy aliamua kuongopa, jibu hilo lilimfanya Mzee huyo atabasamu baada ya kuoma dhahiri amedanganywa.



    “Ok, Daktari hali yake sasa hivi inaendeleaje?" Mzee huyo alimgeukia Daktari na kumuuliza swali hilo.



    “Hali yake sio mbaya sana, ila leo inabidi alazwe ili tujue ataendeleaje baadae"



    “Sawa naweza kwenda kumuona?"



    “Yeah, twendeni" Daktari aliongea hivyo na kuinuka na kuwafanya hao wengine nao kuinuka na kuelekea katika chumba alicholazwa Ramah. Walipofika huko wakamjulia hali na kusema kuwa kidogo afadhali ila anahisi maumivu kwenye kifua chake. Baada ya kumjulia hali, Daktari aliwaambia kuwa waje kesho ili kujua hali yake imeendeleaje kwa siku hiyo. Hawakuwa na budi, wakaaga na kuanza kuondoka ndani ya jengo hilo la hospitali na kwenda kupakia kwenye gari alilokuja nalo Baba yake na Ramah.



    Baba yake na Ramah alimpeleka Hemedy nyumbani kwao na yeye akaondoka hapo kuelekea anapopajua yeye. Hemedy aliingia ndani ikiwa ni mishale ya saa tatu usiku, alipofika sebuleni, akawakuta Hilda na Anti yao wakiwa wamekaa kwenye masofa huku wakiwa na wasiwasi mwingi, akajua yote hayo ni kwasababu yake.



    “Haya wewe ulikuwa wapi muda wote huo na kwanini simu yako umeizima?" Alikutana swali hilo kutoka kwa Anti na kumfanya ajipekuwe mfuko na kuitoa simu yake na kuiangalia, akakuta kweli ilikuwa imezima.



    “Tulipatwa na matatizo Anti mimi na Ramah" Hemedy alijibu.



    “Matatizo gani hayo yaliyokufanya hadi uzime simu kabisa?" Anti bado aliendelea kumkomalia na maswali. Hemedy alimuelezea yote yaliyo wakuta ila huku pia alificha sababu ya wao kutekwa.



    “Na huyo mwenzako vipi hali yake, anaendeleaje?" Anti aliuliza kwa masikitiko baada ya kuisikiliza hiyo taarifa, ila Hilda alioneka kutoamini maneno hayo.



    “Hali yake kwasasa iko vizuri ila bado yupo hospitali akichekiwa zaidi na kesho nitaenda kumuangalia"



    “Kwahiyo kesho hutoenda shule?"



    “Ndio Anti nilazima nikamuangalie"



    “Haya mimi nipo ndani huko napumzika" Anti aliongea hivyo huku akinyanyuka na kuingia ndani akiwaacha Hemedy na Hilda wakiangaliana utafikiri ndio mara yao ya kwanza kuonana. Hilda aliinuka hapo alipokaa na kwenda hadi alipo Hemedy, akamshika mkono na kumvutia nje na kusimama nae kwenye mti ambao ulikuwa ndani ya uzio wa hio nyumba.



    “Najua pale umemdanganya Anti. Haya nambie ukweli umetoka wapi we mwanaume?" Hilda alimuuliza Hemedy hivyo huku akiwa mikono ameikunja kwenye kifua chake na mguu mmoja akiuweka mbele huku mwengine ukiwa upo sawa. Swali hilo lilimfanya Hemedy akabaki mdomo wazi huku akimuangalia binti huyo. Akabaki akijiuliza, ina maana hakunielewa kile nilichokisema pale ndani au hakuniamini?



    “Hilda mbona sikuelewi? Sinime wahadithia yote yaliyotuka mimi na Ramah? Sasa ni kipi kilichokufanya ukanitoa ndani hai hai hadi huku nje halafu unakuja kuniuliza swali hilo? Hemedy alimuuliza.



    “Sikiliza Hemedy, nyie kuna sehemu zenu mmetoka mnajifanya kusingizia kutekwa, haya nyie mtekwe na nani? Mnakipi kinachowafanya hadi mtekwe?" Hilda alimuuliza kwa kutahariza. Hemedy alipoona hapo mlolongo unaweza ukawa mrefu, akaamua kutoa simu yake na kumpigia Ramah, baada ya muda mfupi simu ikapokelewa.



    “Oya Ramah, embu ongea na Hilda" aliposema hivyo akampa simu Hilda na kuanza kuongea nae.



    “Ramah niambie ukweli, mlikuwa mpo wapi? Mwenzako kaja huku nyumbani anajifanya kusingizia eti mlitekwa, kamdanganya Anti anadhani na mimi pia nitaamini huo uongo wake, ‘please’ Ramah usinifiche naomba uniambie ukweli" Hilda aliongea.



    “Hilda sikiliza nikuambie, wewe kama humuamini Hemedy anavyosema basi kesho asubuhi njoo nae hospitali, naamini ukija huku hutokuwa tena na swali la kuuliza. Mpe simu Hemedy" Ramah aliongea kwa sauti ya uchovu au kama ametoka usingizini muda mfupi.



    “Hemedy, mjulishe na Hawa pia maana mimi simu yangu salio limeisha" Ramah aliongea hivyo. Hilda aliposikia maneno hayo kidogo akaanza kuamini, maana simu hiyo iliwekwa sauti kubwa.



    “Usijali kaka, subiri nifanye hicho kitu sasa hivi" Hemedy alikata simu na kumpigia Hawa kisha akamuambia taarifa hiyo, binti huyo alikuwa na wasiwasi na maswali mengi baada ya kuisikia taarifa hiyo, ila Hemedy akamtoa hofu na kumuambia kama kuna uwezekano, kesho asubuhi waongozane wote wakamuangalie hospitali, kisha akakata simu na kumuangalia Hawa aliekuwa ametahayari muda wote.



    “Wewe!! Kumbe ni kweli!" Hawa aliuliza kwa taharuki mithili ya mwanafunzi aliepokea taarifa ya matokeo yake ya kidato cha nne na kuambiwa kuwa amefeli.



    * * * *



    Siku iliyofuata, waliongoza wote wanne yani Hemedy, Hilda, Hawa na Anti yao kwenda hospitali kumuangalia Ramah, walipofika walimkuta Baba yake na Ramah akiwa eneo hilo kilipo kitanda alicholazwa mwanae, Hawa alipofika hapo akangua kilio kilichomshangaza Anti yake na Hilda, kilio hicho hakiku mshangaza Baba yake Ramah kwasababu alijua huyo huenda ikawa ndio huyo mkwe wake alieambiwa na watu wake kuwa mtoto wake na yeye anampenzi siku ile walipokuwa ufukweni.



    Hawa aliacha kulia na sasa alikuwa amekilaza kichwa ha Ramah kwenye mapaja yake baada ya kukaa kwenye kitanda alicholazwa kijana huyo, hakujali watu wazima hao waliokuwa wapo mahala hapo, ila alichojali yeye ni mapenzi yake kwa kijana huyo. alikuwa akimuuliza hali yake huku akiwa anakichezeachezea kichwa cha Ramah, ila kijana huyo alimtoa hofu kabisa kwa kumuambia kuwa hali yake kwa sasa iko vizuri sana tofauti na jana, hapo kidogo banati huyo moyo wake ukatulia.



    Alikuja daktari na kumjulia hali kijana huyo kisha akamuomba mzazi wake amfuate ofisini, huko walipofika, hakukuwa na chengine zaidi ya kuambiwa maendeleo ya mwanae kuwa ni mazuri na kwa muda huo anaweza kuondoka nae. Akashukuru sana na kuomba kupewa muongozo mzima wa kulipia gharama zilizotumika. Daktari akampatia karatasi flani na kumtaka aende nayo kwenye dirisha la dawa kisha akampa na karatasi nyengine akimtaka aende nayo mapokezi baada ya kutoka kwenye dirisha la dawa.



    Mzee huyo alishukuru na kuaga, kisha akatoka na kuingia kwenye chumba alicholazwa Ramah na kuwataka waondoke hapo maana ruhusa ya daktari imeshatoka. Wakachukua kilichochao na kutoka chumbani humo. Baba yake Ramah alikamilisha kila kitu na kutoka nje ya hospotali hiyo, akawakuta wakiwa wanamsubiri nje, wakaondoka wote kuingia kwenye gari huku Anti yake Hilda akiaga na kuondoka kuelekea kwenye shuhuli zake.



    Safari yao iliishia nyumbani kwakina Ramah, wakaingia wote subuleni na kukaa hapo, muda wote huo Hawa alikuwa yupo karibu na Ramah kuliko mtu yoyote ndani hapo, Baba yake Ramah aliwaaga na kuondoka hapo huku akimuachia Ramah kiasi cha pesa ambazo zitamsaidia kununua chochote atakacho. Ramah aliingia chumbani kwake kwenda kuoga kisha akarudi tena hapo sebuleni. Hawa na Hilda walichukua jukumu la kuingia jikoni kwajili ya kupika chakula maana siku hiyo walipanga washinde hapo hapo.



    Siku iliyofuata, walienda shule baada ya hali ya Ramah kutengemaa, siku hiyo walikuwa na chuki zilizochanganyikana na hasira kwa lile kundi lililo sababisha kitendo cha kutekwa kwao, walipanga wakawafanyie fujo pindi utakapofika muda wa mapumziko.



    Muda wa mapumziko ulipofika, wakatoka darasani huku vichwa vyao vitawaliwa na hasira juu ya vijana hao, waliondoka wao wenyewe wawili na kuwafuata sehemu ambayo watu hao wanaifanya kama ndio maskani yao wawapo hapo shule. Hasira ziliwazidi baada ya kuwaona wakiwa wamekaa tena wakiwa na furaha kupitiliza, hapo wakaongeza mwendo kuwafuata.









    ENDELEA



    WALIWAFUATA palepale walipokaa, hawakujali uwingi wao, walichojali wao ni kutimiza adhma yao waliyoipanga. Ramah alipofika, hakutaka salamu wala salama, alichofanya yeye ni kumzawadia Bebel ngumi moja iliyoenda kutua kwenye mwamba wa pua na kumfanya kijana huyo kuishikilia pua yake na kuinamisha uso wake chini kwa maumivu aliyoyapata. Akarusha ngumi nyengine iliyokuwa na lengo la kupiga kwenye sikio la Babel, ila kabla ngumi hiyo haijatua sehemu lengwa, alijikuta akipokea ngumi iliyotua sawia kabisa kwenye mbavu zake za kulia na kumfanya ahisi maumivu ya aina yake, ila maumivu hayo hayakuifanya ngumi yake isifikie lengo, ngumi yake ilituwa kwenye sikio la Babel na kumfanya kijana huyo aone kuendelea kukaa hapo ni kujitafutia maumivu kama sio kujeruhiwa kabisa.



    Hemedy naye, alirusha teke kumuendea Shebe ambae ndie alimpiga Ramah ngumi ya mbavu, teke hilo lilienda kumpata mtu huyo la kifua na kumfanya arudishwe nyuma huku akiachiwa alama ya kiatu kwenye shati lake jeupe maeneo ya kifua. Hemedy wakati akirudisha guu lake chini baada ya kutoka kumuadhibu Shebe ambae kwa sasa alikuwa chini mbali na yeye kutokana na msukumo wa teke lake, ila kabla guu lake halijatua chini, alijikuta akichotwa mtama maridadi uliyomfanya na yeye kuenda chini bila kupenda. Mtama huo alipigwa na kijana wanaemuita Mnama.



    Wakati Ramah akizubaa kumuangalia Hemedy aliekuwa akijizoazoa pale chini baada ya kuchotwa mtama, naye alikuja kushtuka akipokea ngumi ya shingo iliyomfanya kukunja sura kwa maumivu ya sehemu hiyo huku mikono yake yote miwili akiipelekea sehemu hiyo kuishika, kabla hajajiuliza vizuri, alijikuta akipokea ngumi ngengine ya sikio iliyomfanya aone kama yuko njiani halafu mbele yake kuna njia mbili, moja ya kwenda peponi nyengine ya kwenda motoni huku akilazimishwa na viumbe asiovijua aende ile njia ya kwenda motoni, ngumi hizo alizipokea kutoka kwa Babel aliekuwa na hasira nae baada ya kutoka kusikilizia maumivu.



    Hemedy muda huo alishainuka na kumfuata Mnama ambae aliekuwa akimsubiri ainuke ili waendeleze mpambano. Alipoinuka akakaa sawa kimapigano kumuangalia hasimu wake kwa hasira, Mnama alipoona adui yake kainuka kwaajili ya pambano, akarusha ngumi ya kizembe sana, ngumi ambayo hurushwa kwa kuuzungusha mkono mithili ya feni. Hemedy ngumi hiyo aliiyona na kubonyea chini kidogo, ikapita na yeye hakutaka kumuacha hivihivi adui yake, alimzawadia ngumi nzito ya tumbo iliyomfanya kijana huyo agugumie kwa maumivu huku mikono yake ikilishikilia tumbo lake huku akirudi nyuma akiwa ameukunja mwili wake kama mgonjwa wa tumbo la kuhara, kitendo hicho kiliufanya uso wake kuwa mbele huku mwili wote ukiwa nyuma, bila kuchelewa Hemedy alipeleka tena ngumi kwenye uso huo chini ya kidevu na kumfanya uso wake kuinuliwa kwa ghafla kwa msukumo wa hiyo ngumi. Ngumi hiyo inaitwa ‘kata funua' Mnama alirudi nyuma na kwenda kutafuta sehemu ya kukaa, alighairisha kabisa mpambano huo baada kuona anaweza akajeruhiwa au kuvunjwa kiungo, hapo alipokuwa amekaa hakuelewa ashike tumbo au akishike kidevu chake, akabaki kuipa kazi mikono yote miwili, huu akiupeleka tumboni na huu akiupeleka kidevuni kwake, alikaa hapo huku akitema damu huku akijutia kitendo cha yeye kujiingiza kwenye ugomvi ambao hata kama Babel angefanikiwa kumpata huyo mwanamke anaemgombania, basi yeye asingefaidika kwa chochote kile, labda kama angefaidika kumuita mwanamke huyo shemeji tu.



    Shebe alikuja kwa kasi kuja kumvaa Hemedy na kumshushia ngumi zisizokuwa na idadi huku Ramah yeye akichezea kipigo kutoka kwa Babel. Dakika hiyo hiyo wanafunzi wa kiume walikuja wengi sehemu hiyo baada ya Lacho kwenda kuwaita waje kuamua huo ugomvi, walifanikiwa kuwaachanisha lakini Babel kama kawaida yake, wakati akiwa kashikiliwa na wanafunzi watatu wakimdhibiti asiende kule aliposhikiliwa Ramah, alitukana huku akidai achiliwe akamfunze adabu kijana huyo. Waliendelea kuwa katika hali hiyo hadi pale Hemedy na Ramah walipoondolewa Sehemu hiyo.



    Kengele iligongwa kuashira kwamba mapumziko yamekwisha na muda huo wanafunzi wanatakiwa waende madarasani, ndipo kundi hilo la watu wanne lilipoondoka hapo kuelekea darasani huku wakimalumu Lacho kwanini ameenda kuwaita watu waje kuwaamulia.



    Walipofika darasani kwao, walienda kukaa sehemu zao za nyuma kabisa ya darasa na kuanza kupanga mpango mwengine wa jinsi gani ya kuwakomesha mahasimu zao.



    “Yani wale was**ge leo nilikuwa nataka niwauwe pale pale, sijui huyu Lacho katumwa na nani kwenda kuwaita wale maboya wengine waje kuamulia wakati mchezo ulikuwa tayari ushanoga" Babel alilalamika.



    “Lakini jamaa huoni kama hapa ni shule, je kama angepita kiongozi yoyote au mwalimu, huoni kama ingekuwa soo upande wetu na wao, hapo tungeadhibiwa sana huku tukiulizwa tatizo nini hadi tukapigana, halafu tatizo lije kugundulika ni mwanamke ndie amesababisha tukapigana shuleni, huoni kama hiyo itakuwa ni aibu sana kwa wanafunzi wenzetu na hata kwa wazazi wetu?" Lacho aliongea.



    “Majamaa, mimi kwenye hiyo mipango yenu naombeni mnitoe, siwezi kupigana kisa demu, tena demu mwenyewe hatokuwa na faida kwangu hata kama tukimpata. Aloo kama hakuna mpango mwengine zaidi ya kupigana basi mimi najitoa tu siwezi hicho kitu" huku akipeleka mkono wake kwenye meno yake ya chini. “Dah! yule boya kanipiga ngumi kali sana, utafikiri ni ngumi za kieletroniki vile jinsi zilivyoniacha na maumivu" Mnama aliongea hivyo na kupelekea wenzake wacheke kwa hiyo kauli yake ya mwisho.



    “Mnama mimi pia nakuunga mkono, siwezi kupigana kisa demu wa mtu. Hemedy alinipiga teke la kifua hadi sasa kifua naona kinawaka moto ndani kwa ndani, yani nikitoka hapa moja kwa moja hadi Muhimbili nikapigwe X-ray, maana sio kwa teke lile, lile pushi kama nimegongwa na fuso la mchanga?" Shebe nae aliongea na kuwafanya wenzake wacheke sana.



    “Kwahiyo wanangu nyote mmeamua kunisaliti?" Babel aliongea.



    “Kwenye mapambano tumekusaliti ndio, labda tupange mpango mwengine lakini sio kupigana, hujui tu ni maumivu kiasi gani ninayoyasikia kwenye tumbo langu kwa ile ngumi niliopigwa, yani jamaa kanifanya nihisi njaa ya ghalfa kama nimezaa pacha" Mnama aliongea hivyo na kuwafanya wenzake wacheke.



    “Ila majamaa hata mimi pia sitaki tena kupigana, japokuwa tumewapiga sana ila nawao kuna sehemu zao wametuotea. Kama Ramah pale aliponipiga ngumi ya pua hadi sasa nahisi natakiwa nitumie mipira ya hewa ya oksjeni kuhemea nayo, na pale aliponipiga ngumi ya sikio, nilidhani kanipiga na nondo kama sio nyundo kabisa hadi sasa nasikia nyuki tu kwenye sikio langu wakivuma" Babel aliongea hivyo na kuwafanya wenzake wacheke. Ama kweli mabaya ndio yanayo chekwa, yani wao badala ya kuwa na hasira kwa kile walichofanyiwa, lakini ndio wanacheka kila wakikumbushiana kilicho wakumba.



    “Sasa mimi subirini niwape mpango rahisi na mwepesi utakaofanya tumchukue yule demu" Lacho aliongea hivyo na kuwafanya wenzake wote wamuangalie yeye na kusubiri wasikie huo mpango atakao usema.



    “Ili waachane wale watu inabidi tuwagombanishe, na kuwagombanisha huko ni kumtafuta mwanamke yoyote tutakae mpa hela ili tumfanyie mchezo Ramah ambao Hawa akiuona huo mchezo lazima atakasiraka na kuamua kuachana na yule jamaa. hiyo ndio njia rahisi na nzuri ya kumpata yule demu, lakini sio kwa kupigana, hivyo hatuwezi kumpata"Lacho aliongea.



    “Huo mchezo ni upi?" Babel aliuliza.



    “Tukishampata huyo demu, tutamuambia mchongo mzima halafu tutamtaka siku moja hapa hapa shule amuite Ramah kule nyuma ya majengo ya choo, afanye kila awezalo ili mradi waonekane kama vile kunakitu wanataka kukifanya, halafu wewe Babel kwa vile unamtaka yule Hawa, wewe ndie ambae utakaeenda kumchukua halafu utamuambia kuwa Ramah yupo nyuma ya majengo ya choo akifanya mapenzi na mwanamke mwengine, lazima tu atataka kwenda kushuhudia, sasa akifika pale halafu kweli akiona mazingira yapo kama vile ulivyomuambia, basi hapo ujue ndio itakuwa mwisho wa mapenzi yao na wewe utajichukukia mtoto kiulani kabisa" Lacho alimaliza kuongea.



    “Dah!! Mwanangu bonge moja la plani hilo apo, sasa mchongo kumpata huyo mwanamke atakae fanya hivyo, mimi niko tayari kumpa pesa" Babel aliongea.



    “Kuhusu mwanamke wa kufanya hivyo nyie wala msijali, kuna mwanamke mmoja anaitwa Shamsa, anasoma huko sayansi, yule demu alikuwa kila siku akiniambia kuwa nimfanyie mpango kwa Ramah akidai kuwa anampenda sana, ila mimi siwezi kumfanyia mchongo demu kumpata mwanaume mwenzangu, alikuwa akiniambia hivyo kipindi hicho mimi na Ramah zinaenda sana kabla haijatokea hii vita, sasa mimi nikawa namkwepa kila siku sitaki kumfikishia ujumbe jamaa. asa huyo demu tukimpa huu mchongo lazima tu atakubali kwasababu yeye mwenyewe pia anampenda jamaa" Shebe aliongea.



    “Shamsa mwenyewe si ndio yule mwenye rangi flani hivi ‘blackbeuty’ halafu ana umbo moja matata sana?" Mnama aliuliza.



    “Mnama undhani hapa ‘form three' kuna Shamsa wangapi zaidi ya huyo huyo mmoja tu?" Shebe aliongea.



    “Sikilizeni majamaa, kama kuna uwezekano huyo demu akaitwe basi tuje kumpa huo mchongo ili hiyo kazi aifanye haraka maana mimi namtaka yule demu hata sasa" Babel aliongea.



    “Subirini wana mimi nikamuite" Shebe aliongea hivyo na kutoka hapo darasani, baada ya dakika tatu alirudi akiwa ameongozana na mwanamke mmoja ambae alikuwa ni mzuri kupita kawaida, alikuwa na umbo matata lililoenda hewani, sura yake nyembamba mithili ya wasomali ili mfanya azidi kuonekana ni mzuri kwenye macho ya wanaojua ku‘point' watoto wazuri, alikuwa na rangi nyeusi isiyotisha, rangi yake ilikuwa ni mithili ya ‘chocolate'. Alitembea kwa mwendo wa madaha kuja huko nyuma ya darasa utafikiri ni mwenye kulazimishwa kutembea, alipofika akawasalimia na kukaribishwa kwenye kiti, muda wote huo Babel alikuwa akimtazama sana mwanamke huyo.



    “Sasa wanangu mtoto mwenyewe huyu hapa" Shebe aliongea hivyo huku na yeye akikaa kwenye kiti chengine. Walimuambia mpango mzima utakavyoenda na kumuuliza yupo tayari kwa hiyo kazi, binti nae bila ajizi alikubali kuifanya hiyo kwasababu hata yeye ni mwenye kumpenda sasa huyo kijana.



    “Ok, unataka kiasi gani kuifanya hii kazi?" Babel alimuuliza.



    “Wala sitaki hela kwasababu hata mimi nampenda sana Ramah, na hivyo mlivyoniambia kwamba anatoka na Hawa, moyo wangu umeniuma sana. mi niko tayari kuifanya hiyo kazi ili mradi nimpate Ramah" Shamsa alisema.



    “Safi. Hii ishu wewe utaifanya lini maana mimi nataka kuwa na yule mwanamke hata leo" Babel aliongea.



    “Kama ambavyo wewe unataka kuwa na huyo mwanamke, ndivyo na mimi ambavyo nataka hata sasa kuwa na Ramah. Nipo tayari kuifanya hii ishu hata leo" Shamsa aliongea.



    “Kwa leo haitowezekana, tufanyeni kesho" Shebe alitoa wazo.



    “Pia hakuna tatizo" Shamsa aliongea na kutaka kuondoka hapo akidai kuna kazi anataka kwenda kuimalizia darasani, wakamruhusu akaondoka, ila macho ya Babel yote yalikuwa kwa huyo binti hadi anapotelea mlangoni.



    “Mzee vipi, mbona unamuangalia sana yule demu" Shebe aliongea hivyo huku akitabasamu.



    “Dah! Mwanangu huyu mtoto ni mgeni au? Maana ndio kwanza leo namuona" Babel aliongea.



    “Duh! Jamaa wewe ni mzee wa totozi sana, lakini nashangaa ukiniambia eti humjui huyu mtoto, huyu mbona tumeanza nae hapa hapa tangia ‘form one’?" Shebe aliongea.



    “Nikimalizana na Hawa, naruka na huyu" Babel aliongea hivyo huku akikuna kidevu chake kilichoanza kuota ndevu.



    * *



    Majira ya usiku Hilda alikuwa chumbani kwa Hemedy, walikuwa wakiongea huku wakikumbatiana kumbatiana, muda huo ulikuwa ni muda ambao Anti yao alikuwa amejipumzisha chumbani kwake akiisaka kesho yake. Kumbatiana hiyo ilipelekea wahisi hali ya utofauti kwenye miili yao, wakataka kufanya kile ambacho hawakuwahi kukifanya kabla. Sijui walitaka kufanya nini, ila walionekana wakigaragazana juu ya kitanda huku Hemedy akionekana ndio mchokozi zaidi kwa mwenzake.



    “Hapana Hemedy, mi naogopa sijawahi kufanya" Hilda aliongea hivyo huku akim‘push' Hemedy aliekuwa kamlalia kwa juu.



    “Hata mimi naogopa wala pia sijawahi kufanya, lakini leo tufanye tu" Hemedy aliongea kwa masikitiko utafikiri alichotaka kufanya kilikuwa ni sahihi kukifanya.



    “Hapana bwana mimi naogopa, tutafanya siku nyengine" Hilda aliongea hivyo huku akinyanyuka hapo kitandani na kutoka chumbani humo, akimuacha Hemedy akimuangalia kwa macho ya ‘mbona umeniacha, umeniacha na nini, embu rudi tufanye kwa mara moja tu'. Hemedy akabaki ametahayari, akajilaza kitandani huku mikono yake akiinyoosha huku na huko huku uso wake ukiangalia dari ya hiyo nyumba, akatabasamu na kufumba macho yake.



    * * * *



    Siku iliyofuata ndio siku iliyopangwa kuwagombanisha Ramah na Hawa kwa staili ya kufumania fumanizi la kupangwa. Siku hii asubuhi hakukuwa na mwalimu alieingia darasani kutokana na walimu wote kuwa katika kikao cha shule kwenye ofisi ya walimu. Wanafunzi wasiopenda kujisomea walikuwa wapo nje ya madarasa wakiranda huku na huko ili maradi tu wasiwepo madarasani, muda huu ndio waliuona ni muda mzuri wa kufanya kile walichopanga.



    Shamsa alitoka darasani kwake na kuenda darasa analosoma Ramah, alipofika alimuomba kijana huyo amfuate kuna jambo anataka kumuambia, Ramah bila kujua chochote, akafuatana na banati huyo hadi huko alipotakiwa kufika, ilimshangaza baada ya kumuona banati huyo akimpeleka uelekeo wa vilipo vyoo, ila hakutaka kujali sana akawa ni mwenye kufuata tu. Walipofika nyuma vyoo, hakumuelewa binti huyo ni kipi hasa anachokitaka, maana hakuwa na maneno yenye kueleweka, mara amuulize kuhusu masomo, mara amuulize alifaulu kwa kiwango kipi ‘form two’, mara amuulize anamalengo gani baadae, ili mradi tu kupoteza muda.



    Babel baada ya kuona Ramah amepelekwa eneo la tukio, hakutaka kupoteza muda, pale pale alimuafuata Hawa na kumuita pembeni.



    “Hawa nadhani leo ndio utaamini kwamba huyo unaemuona anakupende wala hakupendi, ila mimi unaeniona sikupendi ndio ninae kupenda" Babel aliongea.



    “Babel nini, mbona sikuelewi unachokizungumza?" Hawa alimuuliza hivyo baada kuona hajamuelewa mtu huyo.



    “Utanielewa pale utakapoenda kwenye majengo ya vyoo nyuma kule, nenda kashushudie mwenyewe kwa macho yako huyo unaemuona anakupenda anavyofanya" Babel aliongea na kumfanya Hawa roho yake kuenda mbio mbio asiamini kile alichokisikia. Masikini bila kujua kwamba huo ni mpango, akanza kutoka mbio mbio mahala hapo kuelekea huko alipoambiwa aende akashuhudie mwenyewe kwa macho yake.



    Ramah baada ya kuona mwanamke huyo hamuelewi anachokizunguamza, akataka kuondoka mahala hapo kuenda zake, ila alijikuta akivutwa shati kwa mbele na kumfanya Ramah akose stamina, bila kupenda akaenda kumkumbatia huyo mwanamke, na muda huo huo ndio Hawa anafika mahala hapo na kushuhudia kile kilichoonekana na macho yake. Akabaki kuachama mdomo wake huku mkono wake wa kushoto ukiwa umeuziba mdomo huo, na mkono wa kulia ukiwa upo kifuani mwake sehemu ulipo moyo, bila kutarajia macho yake yalitoa machozi huku asiamini anachokiona hapo, akabaki kutikisa kichwa kushoto kwenda kulia na kulia kwenda kushoto, kisha akageuka nyuma na kuanza kukimbia kuondoka mahala hapo.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/





    HAWA kukimbia kwake alienda kuishia nyuma ya madarasa, alipofika huko, akaegemea ukuta na kushuka nao taratibu mithili ya maji yamwagiwavyo ukutani. Alipofika chini kabisa, akaikunja miguu yake, mikono yake akaiweka juu ya magoti huku kichwa chake akikiweka juu ya mikono. Kitendo hicho kilichagizwa na kilio cha kwikwi huku macho yake yakimwaga machozi mithili ya mbomba la mvua, akawa analia huku akiijutia nasfi yake kumkabidhi moyo wake mtu asiekuwa muaminifu kwake kama alivyoaminishwa na macho yake.



    Ramah alimuona vizuri Hawa alipokuja hapo, ila kujinasua kwenye kumbato hilo la ghafla ndio ikawa hawezi, maana kitendo hicho kilikuwa ni cha kushtukiza sana. Ramah baada ya kuona amefumaniwa kwa kitendo ambacho si cha kweli kwenye macho ya mchunguzi, ila kwa macho ya Hawa ni lazima aone ni cha kweli tena cha makusudi kabisa. Akataka kuondoka tena amuwahi Hawa huko alikokimbilia, ila alijikuta akivutwa tena shati lake, safari hii alivutiwa kwa nyuma baada ya kuwa ameshapiga hatua mbili. Aligeuka na kofi lililoenda sambamba kwenge shavu la binti huyo na kumfanya aliachie haraka shati la Ramah na mkono wake mmoja kuupeleka kwenye shavu hilo huku mwengine akiupeleka kuyaziba macho yake, akawa analia chini chini, akitegemea kuombwa msamaha kama si kubembelezwa kabisa kwa hicho alichofanyiwa, alilia kwa dakika nzima ila hakuona mrejesho wa aina yoyote, ikambidi afumbue macho kumuangalia kijana huyo. Alaaa!! Ramah hakuwepo mahala hapo, akaangalia huku na huko kumtafuta kwa macho lakini hakuihisi hata harufu yake mahala hapo. Akabaki akijiuliza, inamaana Ramah hajui kwamba amenipiga kofi na inahitajika animbembeleze?....



    Ramah baada ya kuondoka kwa banati yule aliemfanyia mchezo wa kuigiza, alikimbilia kumtafuta Hawa, akaenda darasani kwao kumuangalia, ila hakumkuta, akaenda darasani kwake nako pia hakumkuta, ikabidi aingie madarasa ya ‘form three’ yote, nako pia hakumkuta, akachoka, hakujua binti huyo amekimbilia wapi. Kuna wazo likamjia kuwa mtu akiwa na mawazo sana au kama akiwa na jambo linalomsibu, basi hawezi kukaa sehemu yenye watu wengi, ni lazima atatafufa sehemu iliyotulivu na kukaa hapo kufikiria ni jinsi gani atalitatua hilo jambo linalomsibu. Alipofikiria hivyo, akapata wazo la kumtafuta sehemu zilizojificha, katika tafuta yake, akaenda nyuma ya madarasa, huko alimuona binti akiwa amechuchumaa kama sio kukaa kabisa nyuma ya ukuta akiwa ameuigamia, alimsogelea mpaka pale baada ya kujua kuwa yule anaemtafuta ndie huyo mwenyewe.



    “Siwezi kuyalaumu macho yako kwa kile yalichokiona, bali nitaulamu ubongo wako kupokea picha iliyotoka kwenye macho yako bila kuitafsiri kuihakiki kwa kile kilichoonekana. Hawa tambua ule ni mpango, mpango ambao unataka kutuachanisha mimi na wewe kwenye mapenzi yetu, kumbuka nilipokuambia tuwe kama mmea wa mnazi na wewe ukakubali tuwe namna hiyo. Sasa ni vipi umekuja kutetereshwa na jambo dogo namna hii? tena jambo lenyewe wala si kweli na halina uhakika kabisa kwenye fikra zako. Hawa kumbuka nilipokuambia kuwa katika ulimwengu huu hakuna mwanaume yoyote anaekupenda zaidi yangu tukimtoa baba yako, na ndivyo ilivyo kwenye moyo wangu hakuna mwanamke mwengine zaidi yako Hawa. Jua kwamba zile ni hila tu za wasiotaka mapenzi yetu yaendelee" Ramah aliongea hivyo baada ya kumfikia karibu.



    Akainua kichwa na kumuangalia“Unasema sina uhakika na nilichokiona? Unasema ubongo wangu hauja kifikiria nilichokiona? Baada ya kunifanyia ule ushenzi unaona sasa uje kunitukana kabisa si ndio?" akainuka na kumuangalia Ramah huku uso wake ukipambwa kwa machozi. “Ramah tambua mimi sio mtoto mdogo, tambua kwamba mimi ni mtu mzima na nina akili zangu timamu. Ramah kwanini umefanya nijione mwenye hatia kwa kukukabidhi moyo wangu? Kwanini umeifanya nafsi yangu iulaumu moyo wangu kwa kukupenda wewe? Kumbe Ramah yale maneno yote uliokuwa ukiniambia yalikuwa ni ya uongo? Siwezi kusema sitopenda tena kwasababu nitakuwa nimeudhulumu moyo wangu haki yake ya msingi, ila nitajutia kukupenda wewe ambae hukua na mapenzi ya kweli kwangu. Ramah kwanini umenifanya nikupende, kwaniniiiii" Hawa alikuwa akiongea maneno hayo huku akilia, aliondoka hapo aliposimama na kumpita Ramah karibu kabisa na yeye, alipofika nyuma kidogo na Ramah akageuka.



    “Ramah uliniahidi hutoruhusu macho yangu yatoe machozi, ile ahadi yako leo ndio inajidhihirisha kwamba ni uongo tu ule uliokuwa ukiongea. Ramah najuta kukukabidhi moyo wangu, najuta kukupenda, najutia kuwa na wewe, jua kwamba kuanzia sasa sikupendi, sikuhitaji wala sina haja na wewe. Nakuomba usinifuate, usinisogelee, wala usiniguse. Sikupendi na nina KUCHUKIA Ramah" Hawa alipoongea hivyo, akaondoka hapo huku akijaribu kushindana na mchozi yaliokuwa yakitoka kwenye macho yake kwa kuyafuta na mkono wake. Ramah akabaki kutumbua macho kama ameona wanyama aina ya paka wakifanya mapenzi hadharani.



    Hakujua afanye nini ili amrudishie mnyange huyo imani na yeye, akabaki kusimama hapo bila ya kuwa na cha maana kufanya, baada ya kusimama kwa muda kidogo hapo, akaondoka huku kichwa chake akikitwisha mikono yake, akaenda darasani kwao na kutulia kwenye kiti chake. Hemedy hali hiyo aliyoingia nayo rafiki yake hakuiyelewa, ikambidi aondoke hapo alipokuwa amekaa na Hilda kumfuata pale alipokuwa Ramah.



    “Kaka vipi mbona katika hali hiyo tena, unanini?" Hemedy alimuuliza huku na yeye akikaa kwenye kiti.



    “Hawa kaka, tumeachana" Ramah aliongea kwa huzuni na masikitiko, ni dhahiri kwamba alikuwa akishindana kiume na machozi yanayotaka kumtoka muda wowote kwenye macho yake.



    “Kaka embu nifafanulie, sijakuelewa kabisa, mmeachana kivipi?" Hemedy aliongea hivyo huku akivuta kiti karibu kabisa na alipo Ramah. Ikambidi Ramah amuhadithie kila kitu kilichotokea.



    “Dah! Ila naamini ni hasira tu zile, akiwa sawa ukimfuata tena atakuelewa tu" Hemedy alimpa moyo mwenzake.



    “Hawezi tena kunielewa yule, kaniambia nisijaribu hata kumsogelea, tena kilichoniuma zadi aliponiambia kwamba ananichukia. Hemedy sio siri ndugu yangu, roho inaniuma sana kuona Hawa amekubali maneno ya kuambiwa na kushuhudia kile kisichokuwa kweli na kukiamnini moja kwa moja. Hawa hanipendi tena mimi. Hawa ananichukia mimi, aagh!!" Ramah alishindwa kuyazuia machozi yake yasimtoke kwenye macho yake, ikambidi alaze kichwa chake kwenye meza yake na kulia chini chini, Hemedy alimfariji kwa kumuambia kuwa ataenda kuongea nae, anaamini maneno yale ameyaongea kwasababu ya hasira tu. Hilda nae alikuja baada ya kuwashuhudia watu hao wakiwa katika hali hiyo, alipokuja na yeye akaambiwa kila kitu, hata yeye pia alimuonea huruma sana Ramah kwa kile kilichomkuta. Ila yote kwa yote wa kulaumiwa ni Ramah, kama angemuambia Hawa tangu mwanzo vitendo na maneno aliyoambiwa na Babel, naamini ingekuwa ni kazi rahisi sana ya kumuelewasha Hawa hata kama angekuwa na hasira kwa kile alichokiona. Ila sijui tuseme usilolijua ama ni uzembe, ndio kitu kilichomkuta Ramah hadi sasa analia na moyo wake.



    * * * *



    Siku zilipita na sasa ikawa imepita wiki tangu Ramah asiwe na maelewano mazuri na Hawa. Kipindi hichi Hawa alionekana akiwa karibu zaidi na Babel, tena walionekana ni wapenzi kama wa muda mrefu kwa jinsi walivyo. Hawa alipelekwa kila sehemu aitakayo na huyo kijana, alipelekwa sehemu nyingi za kujidai, alikula kila anachokitaka, hata wakiwa shule pia walionekana pamoja. Haikujilikana Hawa alikuwa na Babel ili kuyapoza machungu aliyopewa na Ramah au alifanya hivyo ili kumuumiza moyo Ramah. Na kama ni hivyo basi alifanikiwa kwa asilimia zote maana kijana huyo alikuwa na machungu kila akiwaona, faraja yake ikawa ni Hemedy na Hilda pindi aliapo, kuna muda alitamani hata kuacha shule kwajinsi anavyoumia.



    “Hemedy acha tu niache shule, siwezi kuvumilia kuwaona wakipita karibu yangu, tena wakionekana wakifanya makusudi kabisa"



    Ramah siku moja aligoma kabisa kutoka kwenda kula ulipofika wakati wa mapumziko baada ya kuwaona Hawa na Babel wakipita nje ya darasa lao, ikambidi Hemedy amlazimishe sana waende kula, lakini alikataa katakata na kumfanya Hemedy akose namna nyengine na kuamua na yeye akae tu hapo hapo na rafiki yake.



    * *



    Siku moja darasani kwao darasa la sanaa, walichanganywa na darasa la biashara alilokuwa akisoma Hawa na kundi la Babel na mwalima wa soma la uraia ‘Civics' walifundishwa wote kutokana na vipindi hivyo kufanana madarasa hayo mawili, ikambidi mwalimu huyo awachanganye wote pamoja na kuwafundisha somo hilo, baada ya kuwafundisha hadi pale alipoona panatosha kwa siku hiyo, akaamua kubadilisha mada.



    “Wiki chache zijazo kidato cha nne watafanya mtihani wao wa kumaliza elimu ya sekondari, baada ya mitihani hiyo kuisha kutakuwa na sherehe ya kuwaaga wanafunzi hao shuleni hapa ambayo itafanyika hapa hapa kwenye ukumbi wa shule, nimezunguka madarasa ya kidato cha kwanza na cha pili kutafuta wanafunzi ambao siku hiyo watatoa burudani ya aina yoyote ile ili mradi isivunje maadili ya shule" alipofika hapo, akatulia kidogo na kuwaangalia wanafunzi hao waliokuwa kimya wakimsikiliza yeye. Wanafunzi na burudani tena!! “Huko nimepata wanafunzi waliojitolea kuigiza igizo ambalo wamelibuni wao wenyewe na wamenipa uhondo kidogo nimeona linaafaa kuigizwa mbele za watu. Sasa nipo hapa kujua na nyinyi mtataka kutoa burudani ya aina gani siku hiyo. Jamani, hiyo sherehe ni ya kwenu nyote japokuwa wahusika wakuu ni hao kidato cha nne, kwahiyo inabidi muwape ushirikiano ili nawao wajihisi walikuwa na thamani ya uwepo wao hapa shuleni kwetu. Kwahiyo nipo hapa kujua nani na nani atataka kutoa burudani siku hiyo, iwe ya kuigiza, kuimba, kuchekesha au hata kuonyesha kipaji chochote kile ambacho unacho" mwalimu huyo wa somo la uraia na akiwa wa michezo pia, aliongea na kusubiri majibu kutoka kwa hao wanafunzi.



    Hemedy aliekuwa karibu na Ramah, alimgusa kidogo kumuashiria kuwa asimame. Ramah alikuwa na hofu uliochanganyikana na uoga wa kuimba mbele za watu wengi. Ni kweli kipaji cha kuimba alikuwa nacho tena kwa sauti nzuri tu, ila kipaji cha kuimba mbele za watu hakuwa nacho, ikabidi Hemedy amlazimishe sana kusimama, kutokana na heshima aliyokuwa nayo kwa rafiki yake, hakuwa na budi zaidi ya kusimama. Watu wote darasani walikuwa kimya wakimuangalia yeye aliesimama.



    “Enhee! huyo ndio mwanaume bwana, sio nyie wengine mnaambiwa muonyeshe vipaji vyenu mnaogopa mtafikiri mmeambiwa msimame uchi mbele za wakwe zenu. Enhe! Ramah wewe unataka kutuonyesha kipaji gani siku hiyo?" Mwalimu aliongea na kuuliza.



    “Kuimba" Ramah aliongea hivyo na kuwafanya wanafunzi darasani humo kucheka kutokana na alichokisema, wengi walimjua mtu huyo ni mwenye masihara mengi hata sehemu isiyo hitaji kitu hicho, hata hapo pia wakadhani ni masihara yake tu.



    “Sasa mnacheka nini?" Mwalimu huyo aliongea kwa ghazabu huku akichapa fimbo yake juu ya meza iliyopo mbele ya wanafunzi wawili wa kike waliokaa kwenye kiti kimoja baada ya viti humo ndani kuisha kutokana na kuchanganywa madarasa mawili na kuwafanya wanafunzi hao kushtuka. “Nimemiambia muonyeshe vipaji vyenu, mnajifanya kudengua, mwenzenu kasimama nyie mnacheka. Waone kwanza vimeno vyao vibaya kama punje za mahindi" mwalimu huyo alipomalizia na hilo bezo, aliwafanya wanafunzi hao washindwe kujizuia kwa kucheka, ila safari hii walichekea chinichini wakihofia kudhibiwa na mwalimu huyo.



    “Haya Ramah, embu imba kidogo tukusikie" mwalimu huyo aliongea hivyo na kumfanya Ramah kuanza kwa kujikohoza kidogo, kisha macho yake akayatupa sehemu alipokuwa amekaa Hawa na kuyarudusha mbele, kisha akaanza.



    Sauti na tabasamu lako, ndio linafanya nikukumbuke.

    Kinachoniumiza mwenzako, unapolia chozi nsifute.

    Mapenze sidhaani mimi, kilichobaki ni uadui. Kuniona hutamani kwanini, kwenye maziwa nimegeuka tui.

    Nami nina mooyo, yapita siku nyingi sijakuona. Nami nina moyo mama, upate siku moja ujeniona.

    Nami nina moyoo, yapita siku nyingi sijakuona. Nami nina moyo mama, ungalisema neno moja ningepona.

    Mwenzako sura yangu, nitaiweka wapi, oooh sura yangu, nitaiweka wapi.

    Ama moyo wangu, nitauweka wapi, oooh moyo wangu, nitauweka wapi. ×2



    Alipofika hapo, Hemedy ndio wakwanza kupiga makofi mengi huku wanafunzi wengine wakifuatia. Mwalimu alifurahi sana na kujikuta na yeye akipiga makofi baada ya wanafunzi kumaliza kupiga makofi, kitendo hicho kiliwafanya warudie tena kupiga makofi. Walikuwa na haki ya kufanya hivyo maana hawakuwa ni wenye kujua kuwa mwanafunzi huyo mwenzao kama alikuwa na kipaji hicho. Hawa macho yalimtoka asiamini alichokiona na kusikia hapo, hakuwahi kujua hata siku moja kuwa kijana huyo anakipaji hicho, tena kilicho pambwa na sauti yake nzuri mithili ya waimbaji wale wa ‘bend' inayoongozwa na Justin Timbelake huko ulaya. Akajua moja kwa moja hata kama Ramah alionyeasha kipaji chake, lakini pia hiyo nyimbo ilikuwa ni dongo kwake. ni kweli Ramah aliimba nyimbo hiyo kwajili yake, ndio maana akabadilisha baadhi ya maneno kwenye ‘verse' ya hiyo nyimbo aliyoiimba. Nyimbo hiyo ilikuwa ni ya msanii mmoja maarufu hapa nchini anaejulikana kwa jina la Richard Mavoko alieimba na kijana mmoja kutokea Nigeria alieitwa Patoranking, wimbo huo uliitwa ‘Rudi'.



    “Safi sana Ramah, naamini sio mimi tu hata hawa wanafunzi wenzako hawakujua kwamba unakipaji hicho ndio maana mwanzo wakacheka uliposema unaimba, ila baada ya kuwaimbia wenyewe wamekubali na kukupigia makofi. Ok kuna mwengine ambae atatuimbia?"



    Mwalimu baada ya kumsifia Ramah, aliwauliza tena wanafunzi swali hilo na kumfanya binti mmoja kutoka darasa la biashara kusimama, na yeye akapewa ruhusa, akaimba kwa sauti nzuri mno na kuwafanya wanafunzi wenzake wampigie makofi baada ya kumaliza kuimba. Mwalimu aliuliza kama kuna mwengine, ila kimya ndicho kilichomjibu kuwa hakukuwa na mwengine mwenye kipaji cha kuimba. Akaomba wasimame wengine wenye vipaji tofauti na hicho na kusimama wanafunzi wawili ambao hawa walikuwa ni mapacha wanaofanana kwa kila kitu, walikuwa ni wakiume na waliotoka kwenye darasa la biashara. Wanafunzi hao waliposimama, vicheko na shangwe ndivyo vitu vilivyosikika kwa wanafunzi wengine. Mapacha hao walijulikana kuwa wachekeshaji. Wanafunzi wa darasa la sanaa, walipiga kelele kwa kumtaka Hemedy ainuke aungane na hao wenzake, na yeye hakuwa na jinsi, akaiunka huku wanafuzi wakiendelea kupiga mbinja na makofi.



    Mapacha hao na Hemedy wao walichukua nafasi ya kuchekesha hiyo siku ya sherehe huku Ramah na huyo binti wakichukua nafasi ya kuimba. Mwalimu huyo aliwaomba waongozane wote kuelekea kwenye ofisi yake kwajili ya kuwapa utaratibu kabla siku ya sherehe haijafika.



    “Kumbe Ramah anajua kuimba kiasi kile?" hiyo ilikuwa ni sauti ya mwanafunzi mmoja wa kike akiongea pekeake baada ya vijana hao kuongozana na mwalimu.



    * *







    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog