Search This Blog

Thursday 27 October 2022

ANGA LA WASHENZI (2) - 5

 











    Simulizi : Anga La Washenzi (2)

    Sehemu Ya Tano (5)





    Kwenye korido za hospitali …







    Waziri mkuu anaingia, bwana Sospeter Mhenga. Ametoka kutumbukiza simu yake mfukoni muda si mrefu. Mwendo wake ni wa kasi na uso wake umepaliwa na mashaka. Kando yake anaongozana na ‘bodyguard’ wake lakini pia maafisa usalama wawili.





    Baada ya muda mfupi akaonana na maafisa kadhaa waliokuwepo kwenye tukio, kisha daktari anayehusika, bwana Mahenge, ambaye aliyeongozana naye mpaka chumba alimolazwa Raisi.





    Humo Waziri mkuu akapata shaka. Macho yake madogo yalitumbua ndani ya lenzi ya miwani.





    “Atapoa kweli?”





    Mheshimiwa Raisi alikuwa amezingirwa na mashine za kumsaidia kupumua na mashine za kumsaidia kusukuma mapigo yake ya moyo. Ndani ya chumba kulikuwa kuna milio ya ‘bip-bip’ ya mashine kadha wa kadha kumnusuru raia namba moja wa nchi.



    Ngozi yake ilikuwa imebadilika rangi kueleka zambarau wakati lips na kope zake za macho zikiwa na rangi ya njano.





    Waziri mkuu akaongozana na Daktari kutoka ndani ya chumba cha mgonjwa, koridoni wakakutana na familia ya Raisi, mke na mtoto wake mkubwa wa kiume. Wasitete sana, wakiwa katika hali ya haraka, Waziri mkuu akaongozana na Daktari mpaka ofisini kwake na kuketi.





    “Hali yake ….” Dkt Mahenge akabinua mdomo, “… si nzuri kabisa. Amevuta sumu kali sana. Mapigo yake ya moyo yanapungua kadiri na muda, napata shaka kama mashine ile itasaidia kwa kitambo.”





    “Kwahiyo tunafanyaje dokta kunusuru maisha yake?” akauliza Waziri akiwa na kimuhe.





    “Tutajaribu kadiri na uwezo wetu,” akasema Dkt Mahenge. “Ila kwa sasa, haraka iwezekanavyo, anatakiwa kufanyiwa upasuaji wa kupunguza pande la virusi linalotafuna mapafu na kuziba njia zake za fahamu. Baada ya hapo tutajua kama abakie hapa nchini ama aende nje kwa matibabu zaidi.”





    “Dokta,” Waziri akaita kwa upole. “Kuna nafasi ya yeye kupona lakini?” akauliza.







    Dokta Mahenge akameza kwanza mate kisha akatikisa kichwa chake kuafiki, “Natumai atakuwa sawa. Tutafanya kadiri tunaloliweza arejee kwenye hali yake.”





    Basi baada ya kusema vivyo, Daktari akaenda zake. Walikuwa ‘bize’ sana, kama unavyojua mgonjwa huyu hakuwa wa kawaida. Ni Raisi. Ni raia namba moja ndani ya nchi.





    Madktari wote walikuwa kazi waliyo nayo mbele ni kubwa, si ya mchezo kabisa. Na huenda kazi hii inaweza kuwavumisha ama kuwayoyomesha kwenye medani hii. Madaktari hawa, wakiongozwa na Dkt Mahenge, walikuwa wamedhamiria kwenye hili. Walikuwa wanataka kuuonyeshea umma kuwa hata wataalamu ndani ya nchi wana uwezo mkubwa pia.





    Hii ilikuwa ni nafasi yao adhimu. Lakini ilikuwa wazi kuwa mambo hayakuwa mepesi hata kidogo. Shughuli iliikuwa pevu haswa.





    Basi usiku mzima, madaktari wakawa wanahangaika wakitumia maarifa yao yote kumwokoa mheshimiwa Raisi. Oparesheni ilidumu kwa masaa tisa, watu wakiwa nje wanangoja kwa hamu kubwa taarifa za chumba hicho. Watu hao wakiwamo familia ya Raisi, Waziri mkuu na pia makamu wa Raisi ambaye alifika papo, pia maafisa kadhaa na wafanyakazi wengine wakubwa wa serikali.





    Walikuwa wanapeana habari na simulizi za hapa na pale juu ya mambo yalivyokuwa yametukia. Ilikuwa ni simulizi ya kuogofya haswa ambayo hakuna hata mtu aliyewahi kuwaza kuwa siku moja mbele ya macho yake atashuhudia Raisi kufanyiwa jaribio la kuuawa tena wavamizi ambao walidiriki kuivamia ngome yake kuu.





    Ni wakina nani hao, wametumwa na nani? Na nini walikuwa wanakitaka kwa Raisi? Kumshambulia Raisi ni kuishambulia nchi nzima!





    “Mmewatambua watu hao?” akauliza makamu wa Raisi, bwana Mrutu. Uso wake mnene mweusi wenye vioo vyembamba vya macho ulikuwa umefumwa kwa hofu na mkanganyiko.





    “Bado,” akajibu Mkuu wa idara ya Usalama wa taifa, bwana Jovetic Holombe. “Ila tutajua tu ndani ya muda, vijana wanaifanyia kazi.”





    “Ila unahisi ni wakina nani?” akauliza makamu wa Raisi. Mara Waziri mkuu naye akasonga karibu.





    “Makisio ni mengi, mheshimiwa. Naomba mtupatie muda tutatoa majibu ya uhakika, ila tu kitu nachoweza kusema kwa sasa ni kuwa watu hawa watakuwa ni makomando kabisa maana ni watu wenye ujuzi mkubwa sana. Lazima watakuwa wametumwa na watu wenye maslahi mapana.”





    Haikupita muda wakapata taarifa kuwa wanajeshi wale waliowafukuzia wale wavamizi wameuawa na wengine wapo majeruhi hawajiwezi. Na kama haitoshi, boti ya maafisa wa jeshi la majini imekombwa na kuwatorosha wavamizi. Habari hizi zilitolewa na mkuu wa kamandi hiyo.



    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    ***





    Saa kumi na mbili asubuhi, Bagamoyo …







    Maafisa wanne wa polisi walikuwa ufukweni wakipulizwa na pepo ya bahari. Wawili walikuwa wamebebelea bunduki mikononi na wamevalia sare. Wawili wengine walikuwa wamevalia nguo za raia ila mmoja ndiye aliyebebelea silaha miongoni mwao.





    Huyu ambaye hajabebelea silaha, alikuwa ameshikilia ‘radio call’ mkono wake wa kuume. Alikuwa anaongea na radio call hiyo akiwa amekunja ndita, sura ya kazi. Sauti yake ilikuwa kavu na yenye ‘punch’ ya juu.





    Mbali na maafisa hawa wa jeshi la polisi, kwa upande wao wa magharibi, kulikuwa na boti nyeupe ikiwa inaeleaelea. Boti hiyo, kwa ubavu wake wa kushoto, ilikuwa na chapa ya jeshi, kamandi ya maji. Pasi na shaka ndiyo ile iliyowatorosha wavamizi.





    “... ndiyo, afande …” aliteta yule afisa polisi mwenye radio call. “…sawa, afande, nimekupata vema, over!” akashusha chini mkono wake wenye kifaa cha mawasiliano kisha akawatazama wenzake na kuwapasha agizo walilopewa.





    “Watu hawa inabidi wapatikane. Naamini bado watakuwa ndani ya Bagamoyo hii. Vituo vyote vipewe taarifa hii na askari wote wafanye kazi hii leo hii.”





    Habari hii haikuwa nyepesi kabisa. Bagamoyo ni mojawapo ya eneo la kitalii. Wazungu wamejaa hapa wakizunguka kwenye fukwe, wakijilaza kwenye vitanda vya mabwawa ya kuogelea, ama wakifurahia huko kwenye vivutio mbalimbali.





    Kumtafuta mzungu mtuhumiwa ndani ya eneo hili haikuwa rahisi, achilia mbali ukubwa wa eneo.





    Basi kwakuwa jambo hili lilikuwa zito, maafisa wa jeshi la polisi, wanajeshi na maafisa wa usalama wa taifa walishirikiana kulitekeleza. Walisambaa huku na huko, wengine wakiwa wamevalia nguo za kiraia kuchangamana na watu.





    Vyombo vya usafiri vikawa vinasimamishwa na kukaguliwa kabla ya kutoka ndani ya Bagamoyo. Huko baharini, boti za wanausalama zinazungukazunguka kufanya doria. Na hata baadhi ya hoteli zikawa zinavamiwa na wana usalama, wageni wote wanakaguliwa.





    Msako huu ulikuwa mkali haswa. Uliwapa hofu raia waishio eneo hilo, lakini zaidi wageni ambao huenda wengine walikuja nchini kutokana na sifa walizosikia kuwa mahali hapa ni kisiwa cha amani. Sasa mambo yalikuwa yanageukia mbele ya macho yao.





    Kwenye majira ya saa nne asubuhi, taarifa ndipo zikaanza kuvuma sasa kuwa Ikulu ilivamiwa na Raisi yupo hoi hospitalini. Sauti ya makamu wa Raisi ilisikika redioni na sura yake ikaonekana kwenye televisheni kutangaza habari hiyo iliyowashtua watu haswa!





    “ ... Mpaka sasa wana usalama wanafanya kazi yao kuwatafuta wadhalimu waliohusika na tukio hilo. Natoa rai kwa wananchi wote, tuungane kwenye hili, kutoa taarifa zozote zitakazosaidia upatikanaji wa wahalifu hao. Pia tumweke Raisi wetu kwenye maombi ya salama. Mungu ibariki Afrika, Mungu ibariki Tanzania.”





    Taarifa hizo zikazua soga kila mahali ambapo watu walikutana. Si kwenye daladala, ofisini wala vijiweni, hiyo ndiyo ikawa habari kuu! Watu wakijiuliza na wengine wakibashiri nani atakayekuwa anahusika na tukio hilo kubwa kabisa kuwahi tokea tangu nchi ipate uhuru.





    Basi mambo yakaendelea kuwa katika hali hii ya homa ya matumbo. Ilipofika kwenye majira ya saa saba, kwenye hoteli moja kubwa, jina kapuni, inayopakana na bahari huko katika mji wa Bagamoyo, ikasikika sauti ya risasi! Ikachukua tena dakika moja, ikasikika sauti nyingine ya risasi, tena na kisha tena!





    Mara sauti za kilio zikasikika, na ndani ya dakika moja tu baada ya sauti hizo za risasi, gari moja ya Tour, Toyota Landcruiser Safari, ikatoka kwa fujo na kuvamia geti! Likiwa kwenye mwendo kasi, likadaka lami! Kwa pupa likakimbia likitawala barabara yote.





    Lilipokaa sawa, likatimka haswa na kuzua tafrani kubwa. Wanausalama wakapeana taarifa ndani ya eneo zima la Bagamoyo, na magari matano yakaungia kulifukuzia kwa nyuma.





    Wanausalama waliamini ndani ya gari hilo kulikuwa na watu wanaowahitaji hivyo kwa hali na mali ilibidi wawatie nguvuni. Hata vyombo va habari navyo vikaanza kurusha taarifa kuwa jeshi la polisi, kwa muda huo, lilikuwa njiani kufukuzana na watuhumiwa.





    Basi gari lile, Toyota Landcruiser Safari, likaendelea kukimbia sana. Ni kama robo saa tangu likae barabarani tangu kukwapuliwa kwake likiwa linatafuta njia ya kutokomea toka Bagamoyo. Likiwa linakaribia kutimiza adhma yake, mara matairi yakapasuka baada ya kutwangwa risasi!





    Matairi ya nyuma yakawa bazoka. Gari likaanza kuyumba, kwenda mrama! Halijakaa vema, matairi ya mbele nayo yakapasuka, sasa gari likayumba kupita kiasi, hatimaye likapinduka likibiringita mara nne na kisha kutulia. Wanausalama wakalizingira wakiwa wamelijalia silaha.





    Walipotazama ndani, wakamwona mzee mmoja wa kizungu akiwa anavuja damu lukuki. Hata hakukaa vema, mzee huyo akakata pumzi. Kusaka ndani ya gari, hakukuwa na mtu mwingine yeyote. Ila kulikuwa na simu iliyopo ‘on’.





    Wakaichukua simu hiyo na kuongea kujua nani aliyekuwa anaongea na mzee huyo kabla hajafa. Walichoambulia,





    “You are too stupid to catch us. Mind your president!” kisha simu ikakata. Baadae walipokuja kufanya mchakato wa kujua simu hiyo ilikuwa inapigwa tokea wapi, wakaja ipata kandokando mwa bahari.





    Na kumbe yule mzee alipewa agizo la kukimbiza gari kwa ajili ya kunusuru familia yake, mke na watoto wake watatu, waliokuwa wametekwa na wavamizi wa Ikulu, yaani bwana Denmark na mweziwe. Na asingeweza kudanganya kwani wavamizi hao waliifungia gari ‘tracking’, na huku wakimpa fursa ya kuwasiliana na watoto wake waliokuwa wakilalamika kubonyezewa tundu za bunduki vichwani.







    ***





    Saa kumi na mbili jioni …





    Dkt Mahenge anaweka simu yake ya mezani chini na kumtazama Makamu wa Raisi aliyekuwa amejawa na hamu ya kusikia neno toka kwake. Akashusha pumzi kwanza kisha akakuna kichwa chake chenye upara.



    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Mheshimiwa,” alafu akabinua mdomo wake. “Imeshindikana. Hamna namna, inabidi apelekwe nje kwa matibabu zaidi.”





    Makamu akatikisa kichwa chake kwa masikitiko.







    ***





    Baada ya masaa mawili, Uwanja wa ndege wa Julius K. Nyerere, Dar es salaam.







    Ilikuwa ni jioni ya saa moja. Ndege kubwa ya AIR TANZANIA nambari B. 20BC348 ilikuwa inangurumisha injini zake. Feni zilizo mbawani zilikuwa zinachanganyia taratibu kuelekea kwenye kasi kubwa.





    Punde kidogo ndege hiyo ikaanza kukaa tenge kwa ajili ya kupaa. Rubani alitoa maelekezo, tahadhari na pia taarifa kuwa ndege hiyo kituo chake cha kwanza itakuwa ni India moja kwa moja.





    Ila rubani huyu aliyejitambulisha kwa jina la Kassim Tolabora, alizingumza kutoa taarifa kwa lugha ya kiingereza pasipo kutia kiswahili kama ilivyozoeleka. Hili laweza likawa si tabu. Lakini lafudhi yake ilitia shaka. Ni wazi aliyekuwa anaongea hakuwa mswahili, alikuwa mzungu.





    Hakukuwapo na hilo kwenye ratiba.









    Ndani ya ndege kulikuwa na Daktari na manesi kadhaa wa ziada kwa ajili ya kumhudumia Mheshimiwa akiwa anaenda kupata huduma zaidi. Lakini pia kulikuwa na maafisa usalama waliokuwa wanamsindikiza, wanaume nane kwa idadi. Walikuwa wamevalia kaunda suti rangi ya majivu.





    Basi ndege ikaenda na kudumu kwa lisaa limoja hewani. Kasi yake ilikuwa kubwa ikikata pepo haswa. Watu waliokuwa ndani wakawa wanamtazama Raisi na taarifa yake ikitolewa kila muda, dakika na sekunde kuwa anaendeleaje. Huko aelekeapo pia wakapashwa taarifa kuwa anakuja mtu mkubwa kiasi hata maandalizi yalianza kufanyika.





    Lakini pia wakati hayo yanaendelea, vyombo vya habari vya nje navyo vilianza kurusha habari juu ya kile kilichotokea Tanzania. Habari hii ilikuwa ya moto na ilivuta wasikilizaji na hata watazamaji wengi. Mpaka muda huo ambao Raisi alikuwa anasafirishwa kupelekwa nje ya nchi kwa matibabu, hakuna aliyekuwa amekamatwa kwa kuhusika na tukio hilo kubwa. Ilikuwa ni ajabu kwa namna yake.





    Lakini pia swala hili likafukua makaburi, watu wa kawaida, wataalamu wa historia na hata wataalamu wa mambo ya siasa za Afrika wakaanza kulitafutia vyanzo kwa kutazama na kuchambua misimamo ya Raisi ambayo walikuwa wanadhani kwa namna moja ama nyingine ndiyo ambayo imemwadhibu.





    BBC - Idhaa ya kiswahili majira ya saa nne usiku …





    Mtangazaji, bwana Paul Chisanja, alikuwa beneti na Profesa Robert Waulaya wa chuo kikuu cha Mzumbe kuzungumzia jambo hilo. Kwa kujitanua na kutumia uhuru wao wa kujieleza, Profesa huyo akadadavua na kuhusisha jaribio hilo la kuuawa kwa Raisi na msimamo wake aliokuwa ameuweka kwenye mkutano wa Umoja wa Afrika uliofanyika hivi karibuni kuwa ni muda sasa wa nchi za Afrika kuanza kukataa misaada toka nje kwani yawafanya watumwa.





    Lakini akaenda mbele kwa kusema kuwa fukuto lililopo baina ya serikali ya saa na nchi za Magharibi huenda sasa ikawa sababu ya kutaka kumwondoa mwanaume huyo Ikulu.





    Swala hili likapokelewa pia na vyombo kama vile CNN na Deutchvelle wakijaribu kuhoji na kuwahusisha watu kadhaa kwenye mahojiano hayo, ilimradi tu swala hili limetawala habari.





    Basi ndivyo ilivyokuwa, wakati huo ndege ipo hewani kumsafirisha mkubwa wa nchi.





    Ila huko Uingereza, Birmingham, kwenye ofisi kumi na mbili zilizopo nchi ya ardhi kulikuwa ni mahali ambapo pametingwa na shughuli nyomi. Ofisi hizi za siri ambazo zilikuwa zimewamudu watu takribani hamsini zilikuwa zimefumwa katika namna ya sayansi ya juu kabisa. Tarakilishi zilizokuwa zinatumika hapa zilikuwa ni nyepesi kwenye michakato lakini pia ziki-access hata mitandao ya kiza (dark web) ambazo hazikuwa zimezoeleka na watumiaji wa kawaida bali wahalifu.





    Ndani ya ofisi hizi, mawasiliano yalikuwa kabambe na nadhifu. Huduma ndogondogo kama vile kuletewa chakula, maji, kahawa na hata ‘gluecose’ zilikuwa zinafanyika na roboti ndogo za matairi. Watu walikuwa ‘busy’ kuendesha na kusimamia mitambo.





    Taarifa zilikuwa zinatolewa hapa kwenda pale katika vitengo tofauti tofauti ambavyo vyote vilikuwa vinasimamiwa na wanawake waliokuwa wamevalia suti na miguuni viatu vyeusi vya visigino virefu. Wanawake hawa vifuani mwao walikuwa na vibandiko vya vioo vilivyokuwa vimeandikwa majina yao.





    Haya majina hayakuwa ya kawaida kama ujuavyo, lah! Yalikuwa yameandikwa kufuatia silaha. Mmoja, aliitwa Dagger, mwingine bullet, mwingine bomb, mwingine swords, mwingine arrow na kadhalika na kadhalika. Kwa idadi vitengo vilikuwa kumi, hivyo na wanawake kumi juu yao.





    Juu ya wanawake hao kulikuwa kuna mwanaume mmoja, mkuu wa kila jambo, ama tumwite mkurugenzi mtendaji. Yeye ofisi yake ilikuwa pweke kwa juu kidogo ya hizi zingine. Ndani ya ofisi yake, kulikuwa na kiti kirefu na meza ya kioo basi. Kwa macho ya kawaida ungesema ofisi hii ina uhaba wa vitu ukilinganisha na ukubwa wake.





    Ila ungekuwa umekosea haswa. Ndani ya ofisi hii kulikuwa na vitu lukuki ila vikiwa vimehifadhiwa kwa teknolojia ya juu. Kuta za ofisi hii zilikuwa zinabiduka na kuleta kinachoagizwa baada ya kubofya button ambazo zimejaa mezani.





    Bwana huyu mkubwa aliyekuwepo hapa, hakuwa na jina kamili. Na kama vile wale wanawake ambao wapo kule chini wakisimamia vitengo mbalimbali, jina lake lilikuwa la ajabu kwenye kibandiko kinachoning’inia upande wake wa kuume wa kifua.





    Kibandiko chake kilikuwa kirefu na maandishi yake rangi ya dhahabu kikisomeka ‘all of them’, kwa kifupi mabanoni A.OT. Kumaanisha kwamba yeye alikuwa ni mjumuiko wa vile vyote ambavyo wasimamizi wake walikuwa, yaani dagger, swords, bullet, arrow na kadhalika.





    Mwanaume huyu wa kizungu ambaye amejawa na ndevu lukuki kwenye taya zake, alikuwa amevalia suti nyeusi, amejilaza kwenye kiti chake na miguu yake mifupi ameilaza mezani, nyayo zikifunikwa na viatu vya Italia (Italian shoes).





    Alikuwa ‘amerelax’. uso wake haukuonyesha shaka. Masikioni alikuwa ana ‘earphone’ na kinywani ana ‘bubblegum’ anayoitafuna kwa kubadilisha pande za meno. Alikuwa mtulivu haswa.





    Ila punde akanyanyua mkono wa kushoto na kutazama saa yake ya mkononi. Kuna kitu alikuwa anatarajia. Punde mlango wake ulifunguliwa akaingia mwanamke mwenye kibandiko kisomekacho ‘Sword’, alitembea kwa madaha na kukomea mbele ya mkuu wake. Akamwambia,





    “They are on air with the President.”





    Mwanaume yule akatulia kana kwamba hajasikia. Alitafuna bubblegum yake mara tatu alafu akauliza, “So?”





    “They will finish their task,” akajibu mwanamke yule mleta habari. Mkuu akatafuna kwanza kama mara nne kisha akasema, “They better do that.”





    Basi mwanamke yule aliyeleta habari akashika hatamu kwenda zake, ila kabla hajafika mlanggoni mkuu akasema, “Make sure you are on touch.”





    “We are!” mwanamke akajibu na kwenda zake.







    ***







    “Make sure he doesn’t survive. That’s your order,” sauti ya kike ilisikika kwenye earphone kubwa za rubani mkuu, mwanaume mzungu aliyevalia sare za rubani. Naye mwanaume huyo hakuwa mwingine bali Bwana Denmark, na kando yake, alikuwa rubani wa pili msaidizi, naye si mwingine bali bwana Wales.





    Ilikuwa ni ajabu kwa wao kuwapo hapa. Hakuna aliyekuwa anadhania kuwa watuhumiwa wa jaribio la mauaji ya Raisi ndiyo haohao waliopewa dhamana ya kumpeleka mtu huyo nje ya nchi kwa matibabu.





    Kiuhalisia hakuna aliyepanga wala kuyajua haya, hata wale waliokuwemo ndani ya ndege hiyo hawakujua liendealo. Wanaume hawa, Denmark na Wales, walikuwa wamewavamia marubani na kuwamaliza muda mfupi kabla ya Raisi kupakiwa na safari kuanza.





    Maiti za marubani halisia waliotakiwa kupaisha ndege hii zilikuwa zimeachwa kulekule kwenye uwanja wa ndege. Hakuna aliyekuwa amelijua hilo mpaka sasa.





    “Let’s do it,” akasema Denmark akimtazama Wales. Wanaume hawa walikuwa wamekwishaandaa parachuti kwa ajili ya kutokomea wakishamaliza kazi yao. Basi walipoweka mitambo sawa, wakatoka ndani ya chumba cha marubani na kuelekea kule upande wa raia kukutana na wana usalama lakini pia Raisi wammalize kabisa.





    Mikononi walikuwa wameshikilia bunduki ndogo kwa ajili ya kurahisha kazi. Hawakupanga kutoana jasho, ni tendo na kuhepa tu.





    Basi baada ya kutoka kwenye eneo lao la kazi, tendo ambalo lilichukua sekunde nne tu, uso kwa uso wakakutana na kitu ambacho hawakukitarajia kabisa. Hii ilikuwa ni ‘surprise’ ambayo iliwaacha midomo wazi na kuwafanya watazamane.





    Uso kwa uso walikutana na Jona, Lee na Miranda wakiwa wameketi. Watu hao walikuwa wamebebelea bunduki mikononi mwao. Na kwenye viti vingine, maafisa usalama wote, nane kwa idadi, walikuwa wamelala hawajielewi hata chembe.





    Ilibidi Denmark na mwezake wapite kwenye bonde hilo la umauti kwenda kumkuta Raisi kwenye chumba chake maalumu. Humo alipofungiwa yeye na wahudumu.





    Basi ghafla, risasi zikaanza kutupwa. Watu hawa wakarushiana risasi kwa fujo sana. Na kwa kuona kuwa ilikuwa ngumu kukabiliana na hali ya hapa, basi bwana Denmark na Wales wakarudi upesi kwenye chumba cha rubani na kujifungia humo.





    Wakapasua mitambo yote mezani kwa rubani kwa kutumia risasi na sasa ndege ikaanza kwenda kombo. Wakati huo mlango wa chumba hicho ulikuwa unabamizwa kwanguvu, Jona na wenzake wakitaka kuzama humo.





    Ilikuwa ni fujo kubwa! Jona na wenzake walishindwa kubomoa mlango kwa kukosa nafasi kwani ndege sasa ilikuwa inayumbayumba hovyo kana kwamba mtu aliyevamiwa na maruwani. Walitupiwa huku na kule, hata silaha zao hazikubakia mikononi!





    Basi kwa wakati huo huo, wakina Denmark wakatumia mlango mdogo wa dharura uliokuwapo upande wa rubani, wakachoropoka toka kwenye ndege baada ya kupambana na pepo kali mno. Sasa wakawaacha wakina Jona wakipambana kwenye ndege inayoenda kuanguka.





    Hakukuwa na cha kufanya kunusuru ndege hii, hilo lilikuwa bayana. Ndege ilishapoteza mwelekeo na si tu hivyo, ilikuwa inaelekea kuanguka vibaya sana hivyo kubeba roho za wote wale waliokuwa ndani yake.





    Si Jona, Miranda wala Lee waliokuwa na la kufanya hapa. Upepo ulikuwa unaingia mwingi sana kwenye ndege, na muda si mrefu bawa la kulia likapata moto na kukatika, likaacha tundu kubwa kwenye ndege ambalo nalo likazidi kuzamisha upepo uso na kifani.





    Hata jitihada za kuchoropoka toka kwenye ndege haikuwa inawezekana. Upepo uliokuwa unaingia ndani ya ndege ulikuwa mkali sana. Uliwabamizisha na kuwang’ang’anizia watu kwenye kuta za ndege. Hata kuhema ilikuwa ni kazi kubwa. Kama ndege hii ingeendelea kufanya hivi kwa muda, basi watu wangekufa kabla haijagota chini.







    Kama baada ya dakika kumi na moja tangu ndege ianze kwenda mrama, Miranda akaanza kupoteza fahamu. Macho yake yalipanda juu na kifua chake kikihaha kuhema. Alikuwa anapitia wakati mgumu sana, na zaidi alikuwa ni mwenye ugonjwa wa kuhofia vimo virefu.





    Jona alimtazama mwanamke huyo akiwa hana la kufanya. Alichokuwa amekifanya Jona ni kujificha nyuma ya kiti ngangari cha ndege ambacho kilimziba na upepo mkali. Hali haikuwa njema hata kidogo.





    Alitazama kushoto na kulia kwake akiwaza namna ya kumkomboa Miranda. Hakutaka kukubali kuwa hamna jinsi. Alifikiri kutambaa aking’ang’ania viti mpaka atakapomfikia Miranda. Ila alipoanza tu kufanya hivyo, akajikuta anatupwa na upepo punde tu baada ya kutoka kwenye mgongo wa ‘siti’.





    Alibamiziwa ukutani na upepo ukawa unamsulubu ipasavyo. Alishindwa kuhema kabisa, upepo ulikuwa mwingi mno kiasi kwamba hakuweza kutoa hewa nje bali kuingia tu.





    Akiwa anatazama kwa mbali kama mtu aishiaye na uhai wake, macho yanatoa machozi, mdomo ameukaza, masikio hayafanyi kazi, akaona ndege ikiwa inakaribia kufika chini. Na kheri ndege hiyo ikiwa inaelekea baharini!





    Sekunde mbili tu, ndege ikakita juu ya uso wa bahari kwanguvu kana kwamba nyangumi mkubwa wa bluu. Ikazama, na taratibu mno ikaanza kusonga kwenda chini kabisa.





    Ndege hii wakati yachapa maji ya bahari, ilisababisha mfarakano mkubwa, vioo vilipasuka, viti vilingoka na kadhalika. Lee na Jona walikuwa ni wahanga wa hili, walichanjwa na vioo na hata kukitwa na vitu mbalimbali.





    Lakini hapa ndipo palikuwa mahali pa kuokoa roho zao. Ni kheri hata ndege hii ilikomea baharini maana kama ingeliangukia mahali pengine basi ilikuwa ni uhakika kuwa asingenusurika yeyote yule.





    Jona aliogelea kumfuata Miranda ambaye alikuwa ameishiwa na nguvu na aelekea kufa. Si kwamba mwanamke huyo hakuwa anajua kuogelea, lah! Bali hakuwa na nguvu kabisa. Mwili wake ulikuwa umeteseka sana angani hivyo hakuwa na nguvu ya kupambana na mawimbi ya bahari.





    Jona akambeba na kutoka naye ndani ya ndege. Akapiga mbizi kwenda mpaka juu, alipofika akavuta hewa fundo kubwa. Akamsaidiza pia na Miranda kuhema. Mara kidogo Lee naye akachomoza juu, Jona akampatia kazi ya kumtazama Miranda ambaye alikuwa ameanza kupata ‘momentum’.





    “Nata kurudi kule chini kutazama wengine!” alisema Jona na basi akavuta pumzi kadhaa za kutosha, akazama chini akiogelea kana kwamba samaki.





    Ila kinyume na alivyokuwa ametaraji, ndege ilikuwa imeenda chini zaidi, ilibidi afanye jitihada za ziada kuifikia na kuzama ndani kufanya uokozi. Na kwa muda huo huo afanye jambo hilo kwa wepesi kabla hajakaukiwa na pumzi kifuani.





    Basi akazama ndani ya ndege na moja kwa moja akapiga mbizi kufuata chumba alimokuwemo Raisi na wahudumu wake. Akafungua mlango huo kwanguvu. Kutazama ndani, akaona wahudumu wale pamoja na Raisi wakiwa hawana dalili ya uhai. Akamfungua Raisi toka kwenye kitanda chake na kumnyanyua pamoja na mhudumu mmoja, daktari, akaanza kupiga mbizi kwenda nje ya ndege.





    Ndege ilikuwa imeshuka chini zaidi ya mara alipoingia hivyo safari ya kupanda juu ilikuwa ni ndefu sana. Na kama haitoshi hakuwa peke yake, alikuwa pamoja na watu wawili mabegani, watu wazima wenye kilo zao.



    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Akajitahidi sana kupiga mbizi, lakini taratibu pumzi yake ikaanza kufikia kikomo. Bado alikuwa mbali na uso wa bahari. Alijitahidi kuongeza nguvu lakini bado hakuwa anaweza kutoboa kabisa. Hata yeye aliliona hilo, basi akawa hana budi kumwachia mtu mmoja apande na mwingine.





    Akamwachia daktari, sasa akabaki na Raisi peke yake. Akaongeza kasi maradufu lakini bado hakuwa na uwezo wa kumaliza hili zoezi. Juu kulikuwa mbali. Mbali haswa. Hata kama angelimwachia Raisi aende mwenyewe bado uwezekano ulikuwa mdogo.





    Ila hakukata tamaa. Hakutaka kushindwa kwenye hili kabisa. Aliamua ajitahidi kadiri awezavyo, na pale atakapoishia basi ndiyo uwe mwisho wake.





    Akaogelea tena na tena, akasonga kama mita tano tu, nguvu zikaanza kumwishia mwilini. Sasa akajihisi mwisho wake umefika. Hakuwa anasonga mbele tena, alianza kuhisi anarudi nyuma kwenda kwenye sakafu ya bahari ambayo hata ndege yenyewe bado haikuwa imefikia.





    Mapigo yake ya moyo yalianza kunyamaza. Mikono yake ilianza kupoteza nguvu kumwachia Raisi. Macho yake yalianza kupoteza uwezo wake akielekea kufa.





    Sasa akiwa amekata tamaa na amekubali kuwa anakufa, akahisi mkono wake umeshikwa! Akavutwa kwanguvu kuelekea juu. Na punde, sekunde kadhaa, akajikuta yupo juu. Mkono wake wa kuume bado ulikuwa umemshikilia Raisi. Akahema kwanguvu sana. Kwa muda wa kama dakika tano akawa anahema tu … anahema tu.





    Alipokuja kutulia, alimwangazia Raisi ambaye alikuwa amepokelewa na Lee na Miranda. Mwanaume huyo alikuwa amekwishafariki. Haikujalisha walifanya jitihada gani, hakukuwa na muitikio wowote ule toka kwake. Hata mapigo yake ya moyo yalikuwa yameshazizima.





    Asingeweza kudumu kwenye maji kwa muda wote ule ukizingatia hali yake iliyomfanya asiwe kwenye fahamu zake. Lakini pia inawezekana mwanaume huyo akawa alifariki hata kabla ya ndege kuzama majini. Yote yawezekana kuwa majibu.





    Basi Jona akaona ni kheri wautunze mwili wa mheshimiwa huyo kwani inawezekana kuja kuwa na matumizi kwa hapo baadae. Ni vema hata watakapopata nafasi ya kurudi nchini warudi na mwili huo kama kielelezo kuwa walijaribu, angalau walipambana kumnusuru mkuu wa nchi.





    Jua lilikuwa lataka kuchipukia, lakini likazongwa sana na mawingu.







    ***







    Saa mbili asubuhi, Julius Nyerere Airport.







    Wanaume wawili, maafisa Usalama waliokuwa wamevalia kaunda, walikuwa wamesimama kandokando na uwanja patuapo na paondokeapo ndege.





    Mmoja aliyekuwa mfupi na mweusi kuliko mwenzake, alikuwa ametia mkono wake wa kushoto mfukoni na wa kulia ukiwa umeshikilia simu yake kwa maongezi. Alikuwa anaongea na mkubwa wa kazi aliyekuwepo huko makaoni.





    “ … ndege imepaishwa na watu wengine, huenda ni maadui. Marubani wote waliotakiwa kuwapo ndnai ya ndege wamekutwa wamekufa! … ndio, mkuu. Tumejaribu lakini mpaka sasa hamna mafanikio. Ndege haionekani kwenye rada yoyote ile, na kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa, mara ya mwisho kupatikana ilikuwa ni juu ya bahari ya Atlantiki, upande wa Kaskazini Mashariki … sawa … sawa, mkuu!”





    Alipokata simu hiyo, wanaume hao wakaelekea kwenye ofisi ya mawasiliano ya ndege ipatikanayo kwenye Uwanja huo kwa ajili ya taarifa zaidi.





    Baada ya masaa mawili, taarifa ikawa rasmi sasa kuwa Ndege iliyokuwa imembebelea Raisi imepotea. Hakuna inapoonekana. Hata kule India ambapo ndipo ilitakiwa kuwapo kwa muda huo, hawana habari nayo.





    Taarifa hizi zikazidi kuweka watu kwenye hali ya taharuki na mshangao. Kwasababu za ndani, ikabidi wakubwa wa vyombo vyote vya Usalama wakutane kwa ajili ya kikao cha dharura. Makamu wa Raisi naye akhudhuria kikao hicho kutazamia nini cha kufanya kutoka na hali hii ya kustaajabisha.







    ***







    Miranda alikohoa akiwa amejikunyata. kwa muda wote huo, bado walikuwa kwenye maji. Mvua ilikuwa inanyesha, hali ya hewa ilikuwa baridi sana. Ukungu ulikuwa umetawala kiasi cha kutoona vema pande zao nne za duni.





    “Inabidi tumwache,” akasema Lee akimtazama Jona aliyekuwa amesmshikilia Raisi. “Umechoka sana. Anakutia uzito zaidi.”





    Jona akatazama mwili wa Raisi. Ulikuwa ni wa zambarau ukiwa na uweupe kwa mbali wa barafu. Ulikuwa ni wa baridi mno kana kwamba jiwe lililotoka kwenye jokofu. Hata mwili wa Jona ulikuwa wa baridi ila si kwa kiasi hiki.





    “Labda tutapata msaada,” akasema Jona. Ila sauti yake ilionyesha kabisa kuwa na upungufu wa matumaini. Walikuwa wamepiga mbizi sana lakini mpaka muda huo hawakuwa wameona kitu chochote isipokuwa maji tu. Watakaa humo kwenye maji mpaka muda gani na huku ni ya baridi chini ama karibu na nyuzi sifuri sentigredi?





    “Jona,” Miranda naye akaita. “Hatuna namna. Mwache tupambanie maisha yetu kwa mara ya mwisho au tufe wote.”





    Jona akashusha pumzi ndefu. Akatazama mwili wa Raisi kwa macho ya huruma, ila kabla hajauachia mwili huo uzame kwenda sakafuni mwa bahari, wakasikia mlio wa risasi! Kutazama wakamwona Miranda akiwa ametoa macho na kuachama kinywa.







    Jambo hilo lilimshtua sana Jona, alidhani Miranda atakuwa ametwangwa risasi. Akamshika akiwa ametoa macho, akamuuliza, “Miranda, nini?”





    Ni kama vile walisahau kuwa risasi yaweza kupigwa kwa mara nyingine tena na kuwadhuru. Miranda akamtazama Jona na kumwambia, “Risasi!”





    “Imefanyaje? Imekupiga?” Jona akauliza kwa pupa. Miranda akatikisa kichwa akiwa ameachama kinywa. Akasema kuwa risasi imempitia sikioni muda si mrefu ulopita. Na alikuwa anashangaa kwa kudhani aidha amekufa.





    Basi Jona akamzamisha, wote wakazama kwa haraka na kusonga ndani ya maji. Walikuwa wamepata nguvu ghafla, lakini pia tumaini kwenye wakati huu mgumu. Japo walikuwa wanashambuliwa kwa risasi, walipata kujua kuwa hapo karibu na wao kutakuwa na sehemu kavu ya ardhi ambayo husimamiwa na hao watu wanaotaka kuwaua.





    Na ni kweli walichokuwa wanadhani. Kwa umbali wa hatua kadhaa toka walipo kulikuwa na kisi kikubwa sana, lakini hawakuwa wamekiona kwasababu ya ukungu. Kisiwa hicho pweke kilikuwa kimejawa na misitu iliyofungamana kwa umbijani.





    Kwenye fukwe, mchanga mweupe unaovutia na hata pia matumbawe yakushangaza. Lakini papo hapo kulikuwa na wauaji waliokuwa wamebebelea bunduki, nao ni Denmark na mwenzake Wales.





    Wanaume hawa wa kizungu walikuwa wametua mbali kabisa na hiki kisiwa baada ya kujirusha toka kwenye ndege. Walijikuta baharini na hivyo basi wakafanya jitihada za makusudi kufika hapa.





    Lakini kinyume kabisa na matarajio yao, wanawaona watu waliowaacha kwenye ndege wakiwa hai. Jambo hili si tu kwamba linawashangaza, bali linawakasirisha mno.





    Haraka baada ya kubaini hilo, wanafanya jitihada za kuwamaliza kwa kuwatupia risasi lakini nazo bado hazikufua dafu. Na hapa tuongeapo tayari walikuwa wameshawapoteza watu hao wakiwa hawajui wapo upande upi wa maji.





    “You should have killed her!” aling’aka Denmark akimweleza Wales juu ya kosa lake la kumbakiza Miranda. Lakini Wales akajitetea kuwa ni sababu ya upepo. Upepo ulikuwa mkali na hivyo mahesabu yake yakaenda kombo.





    Basi hawakuwa na la kufanya hapa zaidi ya kutupa macho yao huku na kule kuwatafuta walengwa wao kwa kutumia hadubini yao. Wakafanya swala hilo kwa muda wa takribani dakika tano, hawakufanikiwa kuona kitu. Ni kama vile walikuwa wameshawapoteza watu wao kabisa.





    “Now what we do?” akauliza Wales.





    “Search them!” akafoka Denmark, kisha akamzaba Wales kibao cha kichwa. “Fool!”





    Wales akakwazika na hiko kitu, lakini hakuwa na la kufanya. Akazamisha macho yake kwenye matundu ya hadubini na kuendelea kusaka wapi walipo watu wao, wakati huo Denmark akaenda kujipumzikia chini ya mti akimtazama.





    Alisaka lakini hakufanikiwa. Jona na wenzake walikuwa tayari wameshazunguka upande wa nyuma wa kisiwa na kukomboa nafsi zao. Jona akiwa bado amembebelea Raisi wakazama ndani ya misitu kwa usalama zaidi. Wakatulia kuvuta hewa na kupumzika.





    Lakini walijuaje kama upande huu kuna kisiwa mbali na ukungu uliokuwa unasumbua macho yao?





    Punde walipopata nafasi ya kuongea baada ya kuzama ndani ya maji kuepuka risasi, Lee alimuuliza Miranda ni upande upi wa sikio risasi ilmpuliza. Naye Miranda alipojibu, basi wakapata kutengeneza jografia ya wapi risasi ilipotokea, na basi huko ndiko kwenye ardhi kavu.





    Sasa wamefanikiwa japo hawajui wapi adui alipo na nini amepanga. Kama litakuwa ndani ya uwezo wao, basi wahakikishe wanawahi kummaliza adui kwani endapo maadui watawawahi wao, basi itakuwa tabu sana maana wao hawana silaha mikononi mwao.





    Basi baada ya muda mfupi kupumzika, Jona akauficha mahali mwili wa Raisi na kuwataka wenzake waanza kuwasaka maadui zao kwa tahadhari. Sasa wakaanza kunyatanyata na kuangaza macho yao huku na kule. Ila bado miili yao ilikuwa mizito, na zaidi walikuwa wamechoka. Kupambana kwenye maji kwa muda mrefu, kuliwapunguzia nguvu kwa kiasi kikubwa na hawakuwa na muda wa kutosha wa kupumzika.





    Basi wakaendelea kutembea. Kisiwa hiki ni kikubwa, hapa sasa wakaanza kujua. Walitembea kwa muda mrefu lakini bado hawakuwa wamefikia kikomo. Na basi kwasababu walikuwa wamechoka mno, Lee akapendekeza wapumzike maana hata watakapokutana na maadui hawataweza kufua nao dafu kutokana na kuwa dhaifu.





    Wazo hilo lilikuwa jema ila hatarishi, watapumzikia wapi? Vipi wakiwa mapumzikoni wakavamiwa? Iliwalazimu kuwa waangalizi maradufu hapa.





    “Pengine tupumzikie juu ya miti,” Miranda akashauri, walipoona ni wazo jema, Jona na Lee wakaanza kukata matawi kuunda viota. Walidumu kwenye hilo zoezi kwa dakika kadhaa, walipomaliza wakavifunga viota hivyo mitini na kupumzika.





    Haikuwa rahisi kuonekana. Viota hivyo vilifanana na matawi ya miti. Miti ilikuwa mingi sana hapa, kwa mtu kung’amua kuwa kuna makazi huko juu ya miti basi ni juhudi kubwa zimefanyika.





    Na kabla hawajajipumzisha, Jona alihakikisha kuwa eneo hilo lipo vema kiulinzi, mbali na macho ya watu.





    Basi isichukue muda, wakapitiwa na usingizi. Ila usingizi wa mashaka. Walikuwa wanafumbua macho yao kila muda kutazama, haswa pale walipohisi huenda kuna shaka.





    Zikapita dakika kumi na tano, hatimaye wote sasa wakapitiwa na usingizi. Hawakuweza kudumu kutazamatazama tena. Walikuwa wamechoka mno, miili iliwazidi uwezo wao kumudu.





    Basi dakika zikasonga zaidi na zaidi. Kama baada ya nusu saa, kule fukweni, bwana Denmark na Wales wakagundua kulikuwa na nyayo za viatu vya binadamu. Walikuwa wamefika ule upande ambao Jona na wenzake walikuwa wameingilia.





    “You see,” akasema Denmark. “Now they are here. They are in the island!”





    Wakatupa macho yao ndani ya kisiwa. Kilikuwa ni kikubwa sana. Watu wao watakuwa kwa upande gani? Hicho kilikuwa ni kitendawili kikubwa kuking’amua.





    Wakafuatilia nyayo zile ambazo zilizama ndani ya msitu, lakini hazikudumu sana zikamezwa na majani. Haikuwa tena rahisi kuona nyayo za watu. Hapa sasa wakalazimika kwenda tu kwa hisia. Kitu pekee kilichokuwa kinawapa imani ni kuwa, walengwa wao hawakuwa na silaha kama wao.





    Lakini wakiwa njiani, Denmark aliendelea kumsema Wales kwa uzembe aliokuwa ameufanya. Alikuwa anamtupia lawama na hata kumtusi. Na si tu yeye, hata wale wengine ambao tayari walikuwa wamekufa, akisema kuwa wao ndiyo chanzo cha kasi hiyo kuzorota. Laiti kama wangelikuwa wametilia maanani, basi kwa muda huo wangekuwa wapo Uingereza.





    Maneno hayo yakawa yanamkwaza sana Wales. Hakuona hoja ya wao kulaumiana wakati walikuwa wapo pamoja kwenye kazi, na zaidi hakuona haja ya Denmark kumwendesha kiasi hicho ingali wote ni watu wa daraja moja. Denmark ni mkubwa kwasababu tu ya kuteuliwa, lazima awapo kiongozi, ila si kusema ana uwezo kushinda wenziwe.





    “I am sick and tired of your bullshit, Den!” Akafoka Wales. “Can I have a moment of peace, please?”





    “What did you say?” Denmark akauliza akimsogelea Wales.





    “You heard it!” akajibu Wales akimtazama Denmark machoni. Basi Denmark akapandwa na hasira na kumzaba kofi kali Wales mpaka kudondoka chini. Mwanaume huyo uso wake ukawa mwekundu kwa hasira.





    Akanyanyuka pasipo kusema jambo. Akajikung’uta, na ghafla akamwelekezea bunduki bwana Denmark na kumwagia risasi tatu. Denmark akiwa ametoa macho kwa kutokuamini, akadondoka chini na kufa macho yakiwa wazi.





    “Die you bitch!” akafoka Wales kisha akamkandika teke Denmark aliyekuwa mfu tayari. Alipomaliza hapo akachojoa chombo cha mawasiliano toka kwa Denmark na kutoa taarifa makaoni juu ya eneo walilopo, lakini pia kuwa wamepungukiwa idadi ya watu hivyo wanahitajika watu kadhaa kumsaidia.





    Alipokata mawasiliano akamtemea mate Denmark na kwenda zake. Ila milio ile ya risasi iliyomuua Denmark iliwashtua na kuwafanya wakina Jona kuwa tenge.







    ***







    Saa tano asubuhi …







    Makomandoo sita walikuwa wameshajipaki kwenye ndege ya kivita tayari kwa ajili ya kusafiri kwenda kumtafuta Raisi huko baharini mwa Atlantiki. Makomandoo hawa walikuwa wametoka kuongea na mkuu wao muda mfupi uliopita wakipewa hamasa ya kutenda kazi yao. Ilikuwa ni lazima warejee na Raisi nyumbani. Hata kama amekufa basi warejee na mwili wake.





    Basi pasipo kupoteza muda, ndee ikanyanyuka na kwenda kwa kasi sana. Makomandoo wale wakiwa wametulia ukutani mwa ndege wakiwa wamefungia mikanda yenye nguvu. Walikuwa ni wanaume walioshiba haswa. Miili mirefu iliyojengekea. Vifuani wamevalia vijishati vyeusi vilivyobana vifua vyao, miguu imekabwa na kombati za jeshi na vichwa vikiwa vimemezwa na kofia nyekundu za jeshi.





    Walikuwa wamejiandaa kwa lolote lile.





    Lakini pia kwa wakati huohuo, kuitikia wito wa Wales, Underground office kule Uingereza ilikuwa imeshatuma watu wake kadhaa kwa ajili ya kwenda kumsaidiza Wales kumaliza kazi. Hivyo lilikuwa ni swala la muda tu kwa tu hawa kukutana na kuonyeshana ubabe.





    Kisiwa hiki kilikuwa kinaenda kumezwa na damu.







    Basi kufikia usiku kukawa bado kimya kisiwani. Hakukuwa na tabu wala shaka sana, Wales hakuwa amekutana wala kuonana na wakina Jona, na hii ilikuwa ni kwasababu hawakutafutana. Baada ya kupungukiwa na mtu, Wales aliona afanye stara kungoja, na kwa wakati huohuo wakina Jona wakiwa wamejihifadhi ndani ya giza.





    Usiku ukakomaa zaidi na zaidi. Kwenye majira ya saa saba hivi usiku, makomandoo wa kitanzania wakawa wa kwanza kuwasili karibu na eneo la tukio. Wanaume hao walitua ndani ya maji na kisha kupiga mbizi mpaka kwenye kisiwa.





    Kulikuwa ni baridi sana na upepo ulikuwa unapuliza sana. Ila kwa makomandoo hawa halikuwa shida hata kdogo. Walikuwa ni watu walofundwa kuishi mahali mbalimbali na kukabiliana na hali mbalimbali. Kuitwa jina la komando halikuwa jambo la lelemama. Ni kuzoeza mwili na patashika na kila shurba za dunia.





    Wanaume hao ‘walipotimba’ hapo kisiwani wakatulia na kujadili kwa muda kidogo. Hawakuwa wanafahamu kama hapa palikuwa pana watu, dhumuni kubwa haswa ni kuangazia upande upi wa dunia ambapo ndege hiyo ilikuwa imeangukia ama kupotelea.





    Basi baada ya muda wakawasiliana na makaoni na kuwataarifu wapo juu ya ardhi kavu ndani ya bahari iliyosolemba. Kule makaoni walipozama kwenye ramani ya dunia iliyopo kwenye vifaa vya elektroniki, wakabaini eneo walilopo. Na hata walipo ‘trace’ ile ndege, wakabaini kuwa ukanda ule ndiyo ambapo ndege ilikuwa imepotelea kwenye rada.





    Kwa taarifa hizo, makomando wakaona ni vema basi vifaa viwahishwe ili wapate kuwandawanda kwenye bahari kuangaza. Vifaa hivyo vikahaidiwa kufika haraka iwezekanavyo.





    Mawasiliano yalipokata, wanaume hao wakaona wasipoteze muda, kwa wakati huo ambapo hawawezi kutanga baharini, basi wahakikishe pia na pale kisiwani ni mahali salama. Kwakuwa ndiyo ardhi pekee ipatikanayo karibu na ukanda wa kupotea kwa ndege, huenda ikawa na watu ambao wanawatafuta ama wanahitaji msaada.





    Huenda.





    Basi wakaanza kuzama ndani, mikononi mwao wakiwa wamebebelea silaha na macho yao yakiangaza dhidi ya msitu. Giza lilikuwa kubwa. Waliwasha kurunzi nzao na kuendelea na kazi. Wakatembea kwa umbali mrefu, kisiwa kilikuwa kipana. Wakiwa wanatembea, mtu wa kwanza kuwatia machoni akawa ni Wales.





    Mwanaume huyo aliyekuwa amejibana nyuma ya mti, aliwatazama vema kuwang’amua kuwa wale hawakuwa watu wake, yaani wale ambao alikuwa amewaomba waje kumsaidia. Akapata mawazo, ina maana maadui zao, yaani wakina Jona, na wao watakuwa wamewatuma watu wa kuja kuwasaidia?





    Basi akaona ni vema kama akiwatia watu wale machoni muda wote ili ajue nini watakuwa wanapanga na vilevile iwe rahisi endapo watu wake wakifika awapashe habari eneo ambapo walengwa wake wanapatikana.





    Sasa akawa anawafuatilia, taratibu akihama toka kwenye mti mmoja kwenda mti mwingine. Kwa hali ya utulivu kabisa na kwa tahadhari. Basi wakaenda kwa kama dakika tano, ila ikafikia muda mmoja wa wale makomandoo akahisi kuna kitu.





    Alisikia kitu kikitembea na si mara moja, zaidi ya mara tatu. Basi akiwa hajawaambia wenzake, akaanza kutilia maanani yale alokuwa anayasikia. Muda si mrefu, akagundua kuna mtu.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    Hakutaka kuwashtua wenzake na pia hakutaka kuanza kumwaga risasi kwanza kabla hajajiridhisha. Akapaza sauti, “wewe nani? Jitokeze!”





    Ila mtu yule, ambaye alikuwa ni Wales, akanyuti nyuma ya mti akiwa ametulia. Na sasa kutokana na sauti ile ya maulizo, makomandoo wengine wote wakawa nao wameelekezea nyuso na hata silaha zao huko.





    “Kuna mtu,” akasema yule komando aliyemwona Wales. Macho yao yaliganda eneo la tukio na wakiwa tayari kwa ajili ya lolote lile litakalojiri, aidha mtu huyo awe rafiki ama adui.





    Kwa wakati huo Wales akawa anawaza namna ya kufanya. Kama akikimbia, basi risasi zitatupwa kwa wingi kumfuata. Lakini pia kama akiendelea kukaa hapo, ni wazi wale watu watajongea kumfuata.





    Kichwa chake kikawa kimetingwa. Macho yake yakawa yanaangaza huku na kule kukimbizana na muda apate fursa ya kuokoa maisha yake. Hali ilikuwa tete.





    Baada ya sekunde kadhaa za ukimya, Wales akiwa bado hajafanya maamuzi, makomandoo wakaanza kujongea kuufuata mti alipojifichia. Kurunzi zao zilimulika hapo kuhakikisha hawapitwi na kitu. Miguu yao iliyovekwa buti kubwa ikawa inajongea ikipiga hatua kubwa na kwa upole.





    Bado Wales akawa amekwama hajui la kufanya. Alihema kwa sauti ya chini ila upesi upesi. Akashikilia bunduki yake vema na kuamua kupigania maisha yake kwa kupambana na maadui uso kwa uso. Hakukuwa na namna sasa.





    Basi ikiwa imebakia hatua kama sita tu kufikiwa, mara sauti kubwa ikasikika tokea baharini. Ilikuwa ni sauti ya boti lililokuwa linaendeshwa kwa kasi. Makomandoo wale wakasita na kutazamana kwa namna ya maswali.





    Kama haitoshi wakasikia na sauti kadhaa za watu wakizungumza. Usiku ulikuwa mtulivu hivyo basi sauti ilikuwa inavuma katika namna ya kusikika pasipo tabu, ukijumuisha na upepo wa bahari.





    Sauti hizo zilizokuwa zinavuma zilikuwa si za kiswahili bali za kiingereza hivyo basi zikazalisha shaka kwa wale makomandoo kwamba huenda hao watu wakawa ni miongoni mwa maadui walioshiriki na mpango wa kummaliza Raisi.





    Basi kitendo hicho cha kuzubaa, kikampatia mwanya bwana Wales. Akachoropoka upesi baada ya kujitupia kwa samasoti mbugani, na kwa upesi akaanza kukimbia akikakatiza mitini.





    “Ni mzungu!” akasema Komandoo mmoja aliyekuwa amebebelea kurunzi, kisha akaongezea, “Amevalia nguo za rubani!”





    Basi hapa wakawa na uhakika kuwa bwana huyu ni mmoja wa maadui wanaowatafuta, wakaanza kumrushia risasi pasi na kifani na hata kumkimbiza kwa kasi.





    Bwana Wales akakimbia mno akikatiza hapa na pale. Nyuma yake vyuma vya risasi vilikuwa vinapiga na kutoboa ama kuchana miti. Aliinamishia chini kichwa chake na kunyoosha mapaja haswa.





    Akaruka kuvuka matawi, majani na hata visiki. Muda mwngine kurunzi ya wanaomkimbiza ilikuwa inamsaidia juu ya wapi apite na kukanyaga. Akakimbia kwa kama dakika moja kabla hajachomoa chombo chake cha mawasiliano na kuanza kuwaelekeza watu waliokuja kumsaidia wafuate milio ya bunduki.





    Akiwa anatoa maelekezo hayo, akastaajabu kadunguliwa bega lake la kushoto. Akalalama kwa maumivu makali, ila hakusimama. Akaendelea kukimbia kwa kasi, akivuka, akipambana, akikumbatiana na miti na matawi yake.





    Mara akadondoka chini! Kama kheri alipodondokea palikuwa na korongo la wanda wa majani, akabiringita kama tairi na kwenda kujikuta chini akiangukia bega lililoumia. Akasaga meno kwa maumivu makali mno. Kabla hakanyanyuka, akasikia, “Yule kule chini!”





    Mara risasi tena zikaanza kumwagwa. Mojawapo ikamtoboa mguu wake wa kulia, hivyo hata alipoamka, akajikuta hawezi kukimbia tena kama awali! Makomandoo wakaserereka kwenye kile kikorongo na kuendelea kumkimbiza.





    Lakini kama kuna kosa walilofanya mabwana hawa basi ni kumkimbiza bwana huyu kwa wingi, takribani makomando wanne walikuwa wanalifanya hilo zoezi wakimkimbiza pasipo kujua ama kujali kwamba wanajiweka bayana kwa ajili ya shambulizi la kushtukiza.





    Kama inegeliwezekana, kwakuwa watu hawa walikuwa na mawasiliano, wangejigawa, na watu wawili tu wangetimiza hiyo kazi, kiasi kwamba hata wakishambuliwa na kuuawa, ‘gape of number’ isiwe kubwa.





    Basi hatua ya kwanza, ya pili, tatu … saba na nane, mara makomandoo wakawa wamempoteza bwana Wales. Hawakumwona wapi ameelekea. Alikuwa amjificha lakini bado sauti yake ya kuugumia maumivu ilikuwa inasikika kwa mbali.





    Makomandoo wakatembeza kurunzi yao huku na kule. Hili pia ikiwa ni mojawapo ya kosa kwenye vita za msituni kwani hukuweka wazi upo eneo gani hata pale adui anapokuwa mbali. Walipoyumbisha kurunzi juu mitini,, wakawaona watu nane kwa ghafla. Watu hao walikuwa wamevalia barakoa na macho yao yamezibwa na miwani.





    Bwana we, kabla hata hawajasema suuh! Wakamiminiwa risasi kana kwamba mvua ya vuli. Zikawatoboa vichwa na kupasua miili. Zikavujisha damu na kuwageuza bucha ndani ya kasi ya kufumba na kufumbua! Hakuna aliyeibuka salama! Wote wakalala chini wakiwa wamefunikwa na damu nzito.





    Wauaji wakatua chini na wawili miongoni mwao wakaelekea upande wao wa kushoto ambapo huko walimkuta Wales akiwa amelala chini. Upesi wakamfanyia huduma ya kwanza kwa kuziba majeraha yake, begani na mguuni, kisha wakambeba na kumpeleka kwenye boti waliyokuja nayo, huko tena kulikuwa na watu wawili, wanaume wa kizungu.







    ***







    “Siwapati!” akasema Komandoo mmoja akitikisa kichwa punde baada ya kushusha radio call yake toka sikioni. Alikuwa ametoka kuwatafuta wenzao wanne walioenda kumfukuzia Wales.





    “Jaribu tena,” mmoja akashauri. Komandoo yule mwenye radio call akaruda tena hilo zoezi, majibu yakawa yaleyale. Hawakuwa wanawapata walengwa wao. Basi hapa wakapata shaka kuwa huenda milio ile ya risasi waliyokuwa wanaisikia iliwamaliza wenzao.





    Wakiwa bado hawajaamua la kufanya, mara wakasikia sauti toka kwenye radio call. “Your friends are dead. Would you want the same service?”





    “Yes, you bitch!” akafoka komandoo mwenye radio call. Uso wake mweusi ulijawa na ndita na kona za mdomo wake zilishuka chini. “If you are a man, show yourself up!” akatema mate kwa kufoka.





    “Then come down where you heard shots. I will be waiting!” sauti ikamjibu.







    Bwana yule komandoo akasonya na kukata mawasiliano kisha akawatazama wenzake na kuwaambia kile alichoambiwa ya kuwa watu hao, waliowamaliza wenzao, wanataka washuke kufuata sauti ya mlio wa risasi ilipotokea.





    Ila wakakabwa na tahadhari. Kama wakienda huko, wanajuaje namna ambavyo watu hao wamejipanga? Ilibidi waibuke na namna ya kukabiliana nao kwanza kabla ya kwenda. Kama inawezekana wajue pia na idadi na hata silaha walizo nazo.





    Ila yote hayo watayafanyaje? Basi wakakubaliana kumtuma mmoja kama chambo, yeye aende kwa siri huko ambapo wanahisi hao watu wapo kisha atoe taarifa na basi wenzao wataenda kutimiza kazi.





    Mtu huyo akateuliwa, na pasipo kuuliza akaenda kutekeleza kazi yake. Wakati akienenda akawa anawasiliana na wenzake barabara juu ya wapi alipofikia.





    Basi wakiwa wanafanya hilo na wakitaraji matunda ya kazi yao, hawakujua ya kwamba tayari walikuwa ndani ya mpango kabambe wa kumalizwa.





    Watu wale, wauaji, ambao walikuwa wameongea nao kwenye mawasiliano walikuwa na vifaa bora kabisa vya mawasiliano. Kwa kupitia vifaa hivyo wakatambua makomandoo wale wapo pande gani ya dunia, na hata mipango ya kuwamaliza ikasukwa na sasa inatekelezwa.





    Wanaume hao wauaji wakajigawa kwenda kila pande kuwazunguka makomandoo. Walikuwa wananyata kiasi cha kutokutoa sauti yoyote. Watu hawa walikuwa wataalamu haswa. Kila nyendo yao ilikuwa ni ‘professional’. mikononi mwao walikuwa wamebebelea bunduki na masikioni mwao walikuwa wamechomelea waya za mawasiliano.





    Waya hizo zilikuwa hazionekani kwa haraka kwasababu ya barakoa walizokuwa wamezivaa. Ila ungetazama vema upande wa masikioni mpaka kinywani, basi ungepata kuziona.





    Basi watu hawa wakiwa wananyata, wakawa wanazungumza kwa sauti ya kunong’ona. Na baada ya kama robo saa, wakawa tayari wamewazunguka walengwa wao. Lakini kwa namna walivyotenda kazi yao, hakuna komandoo hata mmoja aliyebaini hilo!





    Hali ilikuwa tulivu sana. Baridi bado lilikuwa linatawala. Usiku huu ulikuwa mrefu sana. Na kabla haujakoma, wazi kulikuwa kuna mambo mengi yanakuja.





    “... Hakuna mtu, over… hakuna mtu, over!” sauti ya komandoo aliyetumwa ilivuma.





    Mwanaume huyo alikuwa tayari kwenye eneo ambalo wenzao wameuawa. Aliiona miili yote ya wenzao ila hakuona watu wengine wa ziada. Miili hiyo ambayo tayari ilikuwa imeanza kuvutia wadudu, ilikuwa inatisha. Japo komando huyu alikuwa amefundwa kuzoeza mambo haya, hili jambo lilimsisimua.





    Namna ambavyo miili ile ilikuwa imetifuliwa pasi na huruma kulimfanya akajita na hofu.





    Mara akasikia sauti ya kitu kikitembea. Haraka akageuza uso wake kutazama. Hakuona jambo. Akawasha kurunzi kuangaza akiwa amekodoa macho haswa. Napo hakuona kitu. Ila pale alipotazama juu, mara akavamiwa na mtu mzito aliyemwangusha chini. Mtu huyo alikuwa amebebelea kisu chenye mpini mdogo na ncha ndefu.





    Kwenye makali ya kisu hicho kulikuwa na mawimbimawimbi yaliyochongoka. Upande wake wa pili kulikuwa kumenyooka kisha kukajipindia kama upinde wa mshale kuelekea kwenye ncha. Kilikuwa ni kisu kizito na cha kutisha.





    Yule mvamizi akajitahidi akitaka kumchoma komandoo kichwani. Komandoo akakidaka na kumzuiza. Wakapambania nguvu, mwishowe komandoo akamzidi na kumtupia kando kisha akanyanyuka upesi. Akatazama kando na kando kutafuta silaha yake, akaiona! Kabla hajainyanyua, kisu kikarushwa kwanguvu kumchoma mkono. Akalalama kwa maumivu makali!





    Hajakaa vema, akakitwa teke la kifua na kujikuta chini kama kifusi. Hakukaa hapo, akachomoa kisu mkononi akiugulia maumivu, akakitupa kikaenda kombo, akasimama na kujipanga kwa ajili ya kupambana. Mkono wake wa kulia ulikuwa unamwaga damu, alikuwa anahisi maumivu makali sana, lakini hakuwa na wa kumdekea hapa la sivyo atatolewa uhai!





    Basi yule bwana mwenye barakoa nyeusi akaguna kwa cheko. Akatazama mkono wa yule komando unaovuja damu kisha akatikisa kichwa chake akiigiza masikitiko. Alipokaa tenge, akamkaribisha komandoo aje kupambana.





    Komandoo akatupa mitupo yake mizito, bwana yule akakwepa. Naye bwana yule alipotuma mashambulizi yake, komandoo ‘akazitoa’ kwa ustadi. Ila sasa shida ilikuwa ni mkono wake. Alikuwa anahisi maumivu makali. Kisu kilitoboa kabisa mkono wake na kutokezea upande wa pili.





    Alijituma kukwepa, kukinga na hata kushambulia lakini kasi yake ilikuwa inazorota. Kuna muda pia alikuwa anashindwa kujikinga kwa mashambulizi ya upesi kwasababu alikuwa anahisi maumivu makali mkononi hivyo akawa anabaki ‘uchi’ mbele ya adui.





    Na bwana yule, mwenye barakoa, akiwa ametambua udhaifu huo, akautumia ipasavyo na mwishowe akamdhibiti komandoo na kumlaza chini. Akamtwanga risasi tatu za kummalizia kabla hajauacha mwili hapo na kuondoka zake.







    ***







    “Don’t fire!” sauti ya kunong’ona ilisikika kwenye vipokea sauti. “I think we need them.”





    Wanaume hawa, saba kwa idadi, walikuwa wamelala chini wakifunikwa na majani yaliyojawa na umande. Hawakuwa wanaonekana kabisa kwa kumezwa na majani pia ukiongeza na rangi zao za nguo.





    Macho yao yalikuwa yamezama kwenye tundu za hadubini za bunduki wakiwa tayari wameshawaweka walengwa wao kwenye rada kwa ajili ya shambulizi, na tayari walishawazingira makomandoo.





    Basi baada ya amri ile kutoka, wakasimama na punde, “Hands up!” amri ikapazwa. Makomandoo kutazama, walikuwa wamezingirwa na watu saba kwa idadi. Kila pande ya dunia ilikuwa ina matundu ya bunduki!





    Wakaamriwa watupie bunduki kando ya mbali na kisha walale chini upesi, wakatii! Wakafungwa kamba mikononi na safari ikaanza kwenda kule ufukweni kukuta boti yao wapate kwenda.





    Wakatembea kwa muda wa dakika kadhaa, kama dakika kumi na hivi, wakafika fukweni. Huko wakawatweka makomandoo wale kwenye boti na kutaka kuondoka.





    “There are still more!” akasema Wales punde baada ya kuwaona wale makomandoo wakiingizwa botini, na akaendelea kwa kusema kuwa watu hao bado watakuwa huko kisiwani, ndiyo waliokuwako kabla ya hawa wengine kufika.





    “Those are more dangerous,” akatahadharisha akimtazama yule kamanda wa kikosi kilichokuja kumwokoa.





    “Worry out,” akasema kamanda kisha akauliza, “How many are they?”





    “Three!” akajibu Wales. Basi kamanda wa kile kikosi akateua watu wake sita na kurudi nao kisiwani kwenda kuwatafuta hao waliobakia, hivyo basi hapa botini wakabakia wawili, mbali na Wales wa tatu.







    **





    “You go to this side! … you two go over that one!” alisema kamanda wa kikosi akiwagawa watu wake. Wawili wakaenda upande wa mashariki wa kisiwa, wawili wakaenda upande wa magharibi wa kisiwa na yeye pamoja na mmoja wakazama katikati ya kisiwa.





    Msako ukaanza.





    Wakati huo majira yalikuwa bado ni ya usiku. Mwezi ulikuwa unaangaza lakini kwa ufifu sana ndani ya kisiwa kwani miti iliyofungamana matawi yalikuwa yanazuia mwanga usipenye.





    Hivyo kwa humu ndani, kulikuwa kuna kagiza katotoro, isipokuwa tu kwenye sehemu moja moja hapa na pale palipokuwa hapajazongwa na matawi magumu ya miti.





    Wanaume wakasonga kwa tahadhari na huku wakijiweka kwenye mawasiliano. Kwa kama mwendo wa dakika kumi, wakawa bado hawajaambulia jambo. Kulikuwa patupu. Ni kiza na ndege, matawi na popo.







    **







    “How long will this take?” akuliza mwanaume mmoja aliyekuwa amevalia barakoa kule botini, akiwa ni miongoni mwa wale wawili walioachwa pamoja na Wales. Hata kwa sasa walikuwa wamevulia barakoa zao, ila tutawaita kwa majina hayo tupate kuwatambua vema.





    “No one knows!” akajibu mwingine mwenye barakoa. Alikuwa amejegemeza akiwa anavuta sigara yake aliyoichoropoa kwenye droo moja ndani ya boti.





    “You know we have to be at the bay before the dawn,” akasema tena yule mwanaume wa kwanza. Ni yeye ndiye alikuwa karibu na usukani wa boti, bila shaka ni dereva. “We must be on time, otherwise we may miss the plane.”





    “I know that story, pal,” akajibu mwenzake. “But do you think we can do anything about this?”





    “Perhaps there was no need to go back for the others. If we leave them here, they will just die! Was there a need?” akang’aka yule mwanaume karibu na usukani kisha akamtazama Wales aliyekuwa amelala chini kwa uchovu, akamuuliza, “was there?”





    “Yes, it was,” akajibu Wales. “It is better we finish what we’ve started. If we leave these punks alive, I surely tell you they will come back knocking at our door.”





    Alipomaliza kusema hayo, wakahisi boti inapepesuka. Wakatazamana pasipo kusema jambo. Pengine wakahisi ni pepo ama maji ya bahari. Ila hapana, boti ikapepesuka zaidi na zaidi! Mmoja akalazimika kwenda kutazama.





    Ila alipoenda hakurejea ndani ya muda. Mwenzake, yule aliyekuwa karibu na usukani, akapata shaka. Kabla hajaenda kutazama huko nje, Wales akamsimamisha na kumwambia, “Be careful.”







    Mwanaume yule hakujali sana, akaenda zake huko nje na kumfanya Wales akae tenge kuskiza nini kitakachotokea. Alitamani kwenda lakini majeraha aliyonayo yasingemruhusu kufanya hivyo. Alitega sikio pasi na kusikia jambo. Ikapita dakika moja, akaamua kuita.





    Kimya.





    Hapa akapata sababu ya kuwa na shaka. Akajikongoja kusimama aende huko nje. Mkononi alikuwa na bunduki ya kumlinda dhidi ya shambulizi. Kufika huko nje hakuona mtu! Akastaajabu. Kugeuka akajikuta amekitwa nyuma ya shingo, akadondoka chini kuzirai! Hakupata hata wasaa wa kumwona aliyemshambulia.





    Alikuwa ni Miranda.





    “Mpo sawa?” mwanamke huyo akawauliza wale makomandoo waliokuwako ndani wakiwa wamefungwa. Akawafungulia toka kwenye kamba kuwaweka huru.





    “Wewe ni nani?” komandoo mmoja akauliza.





    “Msijali, mtanijua. Siko mwenyewe.”





    Baada ya muda mfupi, Lee naye akiwa ametokea upande wa pili wa boti, akajiri akiwa amelowana chepechepe kama ilivyokuwa kwa Miranda. Watu hawa ndiyo walikuwa wakiwavutia wale watu kwenye maji na kuwamaliza. Naye akajitambulisha kwa jina tu.





    “Nanyi mlikuwapo kwenye ndege?” akauliza Komandoo.





    “Ndio, tulikuwamo pamoja kwenye ndege kabla ya kuanguka,” akajibu Miranda.





    “Vipi kuhusu mheshimiwa? Yupo wapi?” akauliza Komandoo.





    Miranda akanywesha sura yake akisema, “Bahati mbaya alifariki safarini.”





    “Vipi mwili wake? - upo wapi?”





    “Msijali, upo. Utakuja hapa muda si mrefu bila shaka.”





    Makomandoo wakatazamana na mmoja kuuliza, “Utakujaje na umesema amefariki?”





    “Kuna mtu atauleta,” akajibu Miranda na kuongezea, “Kuna mwenzetu yupo huko nje. Yeye atakuja nao.”





    “Anafanya nini huko?” Komandoo akaulizia.





    “Anamalizia kazi kabla hatujandoka,” akasema Lee.





    Lakini ilikuwa inaleta mantiki kwa Jona kuwapo huko nje? Pengine waweza kuona hii ilikuwa ni fursa adhimu kwake kujiondokea pamoja na wenzake baada ya kushikilia boti hii, ila kinyume na hapo yupo kule kisiwani! Msituni!





    Atapambana na wanaume wale sita wenye silaha na ujuzi wa hali ya juu yeye mwenyewe?





    Dakika nane nyuma …





    “Nendeni,” alisema Jona baada ya kuchomoza nyuso zao toka kwenye maji, yeye pamoja na wenzake. Macho yao yaliyokuwa mekundu kwasababu ya kula chumvi ya bahari yalikuwa yanawashuhudia wanaume wale watano wakiwa wanazama msituni kisiwani kwenda kuwatafuta.





    “Twende wapi?” akauliza Lee wakimtazama Jona.





    “Nendeni kwenye boti,” Jona akasema. “Mimi nitarudi kule kisiwani kukabiliana nao.”





    “Mwenyewe?” Miranda akadakia.





    “Ndio, mwenyewe. Kuna haja gani ya kwenda wote kama kazi inaweza kufanyika na mmoja wetu?” Jona akasema akiwatazama wenzake kwa macho ya uhakika.





    “Una uhakika?” akauliza Miranda. Uso wake ulikuwa na mashaka.





    “Ndio, nina uhakika. Ikipita dakika arobaini na tano sijafika, basi nyie nendeni.”





    “Hatuwezi kwenda tukakuacha, Jona,” aliteta Miranda kisha akamshika Jona mkono na kumwambia, “Please, be safe.”





    “I will be safe,” akasema Jona na kabla mtu mwingine hajaongeza neno lingine, mwanaume huyo akazamia kwenye maji asionekane ameelekea upande upi wa dunia. Basi Miranda na Lee wakafanya kama vile walivyoambiwa, wao waende botini. Jona yeye ataenda kukabiliana na wale wanaume walioenda kule msituni mpaka arudi na kitambulisho, gate-pass (kama itakuwapo) na chombo cha mawasiliano alichobebelea yule mkuu wa kikosi kilichokuja kumwokoa Wales.





    Walijua mwanaume huyo alikuwa navyo kwani walishawafuatilia watu hao kwa muda fulani huko msituni. Yaani siri ilikuwa sirini. Wakati wanaume hao wakiwa wanajificha na kufanyia siri kwenye mashambulizi yao, na wao sirini walikuwa wanatazamwa ama kufuatwa!





    Kifuani mwa mwanaume yule aliyekuwa kamanda mkuu wa wenzake, kulikuwa kunaning’inia karatasi fulani iliyokuwa ‘laminated’. kwenye karatasi hiyo kulikuwa na picha ndogo na pembeni ya picha hiyo taarifa kadhaa.





    Ilikuwa ni jambo linaloleta maana masikioni kuona wakina Jona wanawinda namna ya mawasiliano ya mkuu huyu. Walijua watu hawa wametoka kutumwa na hivyo basi mawasiliano yao na makaoni huwa yenye nguvu na tija kuliko yale ya Wales. Walijua watu hawa watakuwa na cha ziada. Cha ziada ambacho kitawasaidia kuangusha ngome mbeleni.





    Lakini wote twajua kuwa kupata vitu hivyo haitakuwa nyepesi. Tena ikifanywa na mtu mmoja ambaye silaha yake ni mikono pekee.







    **







    Alipochomoza toka kwenye maji alipanda haraka ardhini. Alikuwa kwenye ubavu wa magharibi wa kisiwa. Alitazama huku na kule kabla upesi hajakimbia na kuzamia kwenye miti.





    Na basi akiwa amebeba tahadhari zote, akatazamia ardhi na kuona alichokuwa anakitaka baada ya hatua kadhaa, nacho si kingine bali alama za watu anaowatafuta. Majani yalikuwa yametawanyika mahali walipopita, na pengine ambapo hapakuwa na majani akaona nyayo za viatu.





    Akafuatilia kwa muda wa dakika sita. Akajibana kwenye kwenye mti baada ya kusikia sauti ya wanaume wakiongea. Aliporusha macho yake, akaona watu wawili. Ni wale ambao walipewa kukagua upande wa magharibi.





    Akaendelea kunyata kuwajongea. Ilikuwa ni hatari kwake kuwaonyesha alipo mapema maana walikuwa na silaha za moto, wangeweza kuzitumia kummaliza kabla hajatimiza adhma yake.





    Basi alipoona sasa amekaribia vya kutosha, akanyanyua tawi moja la mti lililo kavu, lakini kabla hajamaliza kunyanyuka, tawi lile likameguka kuvunjika! Likatoa sauti iliyowashtua wanaume wale na kuangazia upande huo upesi!





    Jona akatulia tuli nyuma ya mti akihema taratibu. Wanaume wale wakatazama eneo hilo kwa sekunde kadhaa. Na wasipuuzie jambo, wakatazamana na kupeana ishara ya kwenda kutazama kupata uhakiki. Taratibu wakajongea, ila ghafla wakasikia sauti ya kitu upande wao wa kushoto. Haraka wakageukia huko!





    Kutazama wakaona ni kipande cha tawi la mti. Kilikuwa ni kipande ambacho Jona amekirusha. Kabla hawajarejewa na akili, Jona akawa ameshawafikia. Kurejesha nyuso zao kule walipokuwa wanaelekea, bunduki zikakamatwa na kuviringitwa duara kamili, mikono yao ikachina, sasa haraka silaha hizo zikavutwa pasipo kipingamizi.





    Hawajakaa vema, silaha zao zikatumika kuwabondea vichwa na kuwaangusha chini wakiwa hawana fahamu. Jona akachojoa vyombo vyao vya mawasiliano na kuzihifadhi silaha zao kwa ajili ya matumizi ya baadae.





    “ … thirteen … fourteen … Fifteen!” alisema Jona kisha akapiga ngumi kiganjani mwake. Mpaka muda huo alikuwa ametumia robo saa. Hivyo ana nusu saa tu kutimia dakika arobaini na tano za kumaliza kazi yake. Muda ambao amewaambia wenzake kuwa ukifika na bado hajarudi, basi wawashe boti kwenda zao.







    **





    “Sure? … ok, we’re coming!” alisema yule kamanda mkuu wa kikosi kisha akamtazama mwenzake aliyekuwa anashirikiana naye kwenye ukaguzi wa kisiwa eneo la katikati. “They’ve got them in the West!” akamwambia kisha akawasiliana na wale wengine wa upande wa Mashariki kuwa hawana haja ya kuendelea kusaka kwani watu wao wamepatikana.





    Basi wakaanza funga safari kuelekea kule upande wa magharibi. Walikuwa wanatembea kasi wakiwasiliana. Baada ya dakika kama kumi na moja, wakawa wamefika upande huo wa magharibi wakiwa wote wanne.





    “Hey, where exactly are you?” akauliza kamanda mkuu. Punde akajibiwa, akawatazama wenzake na kuwapa ishara ya kichwa kuwataka wasonge mbele zaidi. Wakasonga kwa dakika mbili. Ila ghafla kamanda akawataka wasimame kwani alihisi kitu! Wote wakasimama!





    Kwa utulivu mkubwa akaskiza. Macho yake yalienda kushoto na kulia. Juu na chini. Hamaki! Akatokea Jona mbele yao toka nyuma ya mti mkubwa uliopo hatua nane tangu walipo.





    Mwanaume huyo alikuwa amebebelea bunduki kwenye mikono yake yote miwili na tayari tunduze ameshawaelekezea maadui. Basi kamanda kuona vivyo, kabla Jona hajabinya vitufe vya bunduki, upesi mno akamkamata mmoja wa wenzake na kumweka mbele yake kujikinga.





    Basi risasi zikanyesha haswa!! Ilikuwa ni ti!-ti!-ti!-ti!-ti!-ti!-ti!-ti! Wanaume wale wakizungu wote wakala za kutosha isipokuwa yule kamanda mkuu ambaye akiwa amejikinga, akawa anasonga kumfuata Jona.





    Aliposonga karibu kidogo, akamrushia Jona mtu yule aliyekuwa anamkingia. Jona kumkwepa mtu huyo na kukaa vema, kamanda akawa ameshamfikia akatengulia bunduki zake kando. Akachomoa bunduki yake ndogo, ila Jona naye akawahi mkono wake na kuutengua, bunduki ikadondokea chini. Sasa wote wakawa hawana bunduki mikononi.





    Wakatupiana mikono, ila wote wakafanya ustadi kujilinda. Wakakaa tenge kutazamana kana kwamba majogoo. Kamanda akauliza, “So you are the dangerous one?”





    Jona hakujibu akamvamia. Alikuwa hana muda. Alikuwa anakimbizana na muda na mpaka muda huo alikuwa amebakiza dakika kumi na mbili tu.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/





    Wakatupiana makonde ya nguvu. Wote walikuwa wana nguvu za kupambana na ustadi wa aina yake. Ilikuwa ni mapambano ya mafahali wawili ambayo yaliumiza majani. Waliparangana kwa muda wa dakika kadhaa asionekane nani aliye mwamba. Wakasimama tena kutazamana.





    “Anything left?” akauliza yule kamanda. Jona akatazamia muda. Sasa amebaki na dakika tano tu! Akapiga kelele kwanguvu na kumvamia kamanda kwa mashambulizi makali.





    Kamanda akajizuiza, akatupa pia na yake, Jona akajikinga na upesi akambana kamanda miguu kumwangusha chini. Kabla kamanda hajafurukuta, Jona akawahi kunyanyua silaha na kumtwanga nayo risasi tatu kifuani! Kamanda akaenda na ubabe wake.





    Jona akamkagua na kuchukua kila alichokiona kinastahili alafu akaanza kukimbia kwenda kuikuta boti waliyomo wenzake.





    Kupiga hatua mbili, akadakwa mguu na kuanguka chini. Kumbe kulikuwa na adui mmoja aliyebakia na uhai. Aling’ang’ania mguu wa Jona na upesi akavuta silaha yake iliyokuwa pembeni apate kumuua, ila Jona kwa haraka akatumia mguu wake uliokuwa huru, akatengua mkono wa adui uliobebelea bunduki na kisha akammaliza mtu huyo kwa kummiminia risasi nne za uhakika.





    Akanyanyuka na kuendelea kukimbia kwa kasi. Sasa alikuwa amebakiza dakika mbili tu kwenye muda wake. Hakutazama nyuma wala pembeni bali mbele aelekeapo!







    **







    “Tuondoke,” alisema Lee akimtazama Miranda aliyekuwa anaangalia msitu wa kisiwa.





    “Hapana,” Miranda akatikisa kichwa. “Hatuwezi kuondoka tukamwacha.”





    “Alisema ikifika daki ya arobaini na tano twende kama atakuwa hajafika,” Lee akakumbushia. Japo uso wake nao ulikuwa na huzuni kuyasema haya.





    “Najua alisema hivyo, ila hatutaondoka pasipo yeye,” Miranda akasisitizia. Muda si mrefu macho yake yakaanza kujawa na machozi. Jicho lake la kushoto likadondosha maji.





    “Najua atarudi,” akasema kwa sauti ya chini. Alikuwa anatazama miti kama vile mtu asomaye ramani. “Najua hatafia huko … atarudi tu.” akamtazama Lee na kumwambia, “Atarudi, si ndio?”





    Lee akashusha pumzi ndefu. Akatazama saa ya mkono wake, ilikuwa ni dakika ya sitini sasa na Jona hajaonekana. Akakosa cha kusema.





    “Atarudi, si ndio?” Miranda akauliza tena akiwa ameng’ata meno. “Na kama hatorudi, basi hapahapa nitawangoja waliomuua na kuwaadhibu.”





    Wakakumbatiana Miranda akiegamisha kichwa chake kwenye bega la Lee. Machozi yaliendelea kumtoka. Hakuwa anataka kuamini kwamba msitu ule umemmeza Jona.





    Basi punde wakiwa vivyo wamekumbatiana, wakasikia sauti, “Heey!”





    Miranda akasema, “ni Jona!” akaangaza kule msituni na akamwona mwanaume akiwa anakuja akikimbia, mikononi mwake alikuwa amebebelea mwili wa Raisi. Akamtazama Lee kwa furaha kubwa na kumwambia tena. “Ni Jonaa!”





    Basi wakaruka na kwenda kumlaki, Lee akapokea mwili wa Raisi na kuutanguliza botini. Miranda akafurahi sana kumwona Jona, hata akambusu mwanaume huyo shavuni na kumwambia, “Nilijua utarudi tu,” akasema akiwa na tabasamu pana. Akamkumbatia tena Jona kabla hawajakwenda botini.





    “Umepata kitu?” Lee akamuuliza.





    “Nimepata kila kitu,” Jona akajibu. “Sasa ni muda wa kwenda kumaliza kazi.”





    Basi wakatia moto boti na kuondoka zao. Wakiwa njiani Jona akawasiliana na makao makuu na taarifa ikawa ni kwenda kwenye ‘bay’ kama ilivyokuwa awali. Huko watakutana na ‘helicopter’ ya kuwachukua na kuwarejesha makaoni.





    Basi safari yao ikadumu kwa mwendo wa saa moja na nusu mpaka kufika ‘bay’ ya barafu kuu. Hapo kulikuwa na wanaume wawili ndani ya helicopter ambao walikuwa wanawangoja.





    Basi kwakuwa haikutakiwa wanaume hao wagundue mapema kuwa si wenyewe waliokuja hapo, wakawataarifu kwa njia ya mawasiliano kuwa kuna majeruhi wa kuja kuwasaidia kuwabeba, hivyo waje kuwapatia mkono.





    Wanaume wale wakashuka pasi na hiyana na kusonga kwenye boti. Tena walikuwa hawana hata silaha mikononi mwao. Wakajikuta wakiwekwa chini ya ulinzi na kuamriwa waanike mikono yao juu upesi! Kwa woga wakatii amri. Lee na Miranda wakawaswaga kwenda kwenye helicopter wakimwacha Jona peke yake na wale makomandoo.





    “Nadhani sasa mtarudi nyumbani kupeleka mwili wa mheshimiwa. Sisi tunaenda England kumaliza mzizi wa yote haya,” Jona aliwaambia wale makomandoo, watatu kwa idadi, watano wakiwa waliuawa kule msituni.





    “Tumekubaliana ataenda huko mmoja, na sisi wawili tutaongozana na nyinyi kwenda huko kupambana,” akasema yule kamanda wa kile kikosi cha makomandoo.





    Basi kwakuwa tayari ndege yao iliyokuwa inawasiliana nayo ilikuwa njiani, wakawasiliana nayo kuwaelekeza walipo, kisha walipofanya hivyo makomandoo wawili wakaondoka na wakina Jona wakitumia ile helicopter waliyoiteka. Wakadaka anga kwenda kuwatafuta na kuwamaliza washenzi.







    **







    Saa tano asubuhi …







    Baada ya mlango kufunguka, walitangulia wanaume wawili ambao ni wale waliokuwa madereva wa ile helicopter iliyotekwa. Wanaume hawa wazee waliokuwa wamevalia makoti meusi ya ngozi na jeans zilikoza kwa rangi ya bluu, walikuwa wamenyoosha mikono juu na nyuso zao zikiwa zimejawa na hofu.





    Nyuma yao alikuwapo Jona na wenzake, Miranda, Lee na Makomandoo wawili. Basi wakaketi na Jona akawauliza wale mateka juu ya taarifa zao. Wakajitambulisha kuwa ni madereva waliokodiwa kwa ajili ya usafirishaji. Hakuna kingine wanachokijua.





    Jona na wenzake wakafanya msako ndani ya makazi ya wanaume hao na wakabahatika kupata nyaraka na picha kadhaa ambazo zilithibitisha kuwa mateka walitoa taarifa za uongo. Walikuwa ni miongoni mwa wafanyakazi wa taasisi ya siri ya Uingereza, ila kwenye kitengo cha usafirishaji.





    “So you were lying, unh?” Jona akamnyooshea mmoja wao tundu la bunduki kichwani. “So choose one, to speak or die?”





    Mwanaume huyo akatetemeka kwa hofu. Jasho likamchuruza. Akabanwa na kigugumizi asijue nini aseme.





    “I’m gonna count up to five seconds!” Jona akafoka kisha akafungua bunduki yake na kutoa risasi nne, akabakiza risasi moja tu ndani ya bunduki alafu akaifunga na kumwekea mateka wake kichwani.





    “One …” Jona akahesabu kisha akafyatua kitufe cha bunduki. Bunduki ikalia kak! Kumaanisha imekosa risasi.





    “Two …” akahesabu tena na kufyatua kitufe cha bunduki, bunduki ikalia kak! Kumaanisha imekosa tena tundu la risasi.





    “Three! …” akahesabu tena na kufyatua kitufe. Tena, kak! Bunduki ikalalamika kwa kukosa risasi! Hapo mwanaume yule mateka akawa amelowana jasho ndembendembe. Alikuwa kwenye vuli la umauti. Pengine kwenye wakati mgumu zaidi tangu aingie duniani.





    Jona aliposema “Four! …” kabla hajafyatua, mateka akapiga kelele, “I’ll speak! … damn! I’ll speak!”





    Jona akafungua bunduki na kutazama, tundu lenye risasi ndilo lilikuwa limekaa tenge. Kwahiyo endapo angebonyeza kitufe basi mateka yule alikuwa anapasuliwa ubongo na kulazwa mfu!





    “Okay, one after another,” akasema Jona akiketi. “Tell us about your boss.”





    Mateka akamtazama na kumuuliza, “What do you want to know about him?”





    “Important things,” akajibu Jona. “Let’s start with where he lives, where he likes to go and what he likes to do.”





    Basi mateka akasema kila alichoulizwa, kwa ufasaha na kwa uoga. Ofisi za bosi ziko wapi, makazi yake yapo wapi na viwanja anavyopenda kutembelea. Pia pasipo kusahau nini huwa anapendelea kufanya.





    Sasa Jona na wenzake wakawa wana kazi ya kuanza kusuka mipango ya kutekeleza na kumaliza. Ila Lee akapata wazo, akaita,





    “Jona,” na kisha akasema kwa uhakika, “nadhani kuna mtu tunamhitaji kuturahisishia kazi yetu.”





    “Nani huyo?” Jona akauliza.





    “Mwanamke mmoja aitwa Glady,” Lee akajibu akimtazama Jona machoni.





    “Glady? Ni nani huyo na atatufaa vipi?”









    Lee akachukua zamu kueleza ni kwa namna gani Glady anaweza kuitenda kazi kwa kutumia kaliba yake ya kujiuza na kujua kushawishi, Jona akavutiwa na maelezo hayo, ila kwa namna gani Glady atakuja kuwakuta na pesa hata ya kumsafirisha hawana?





    “Usijali,” akasema Lee. “Nitamwelekeza Marwa aliyekuwepo nyumbani nini afanye na pesa atazipata. Zipo nyingi sana chini ya akaunti yangu na hata ya Sheng mwenyewe.”





    Wakakubaliana na Lee akafanya mpango wa kuwasiliana na Glady kwenye mtandao wa whatsapp. Kheri alikuwa anakumbuka namba ya mwanamke huyo. Alimpata ndani ya muda mfupi na akamweleza haja ya moyo wake. Jambo hilo likamshangaza na kumtisha Glady, ila akapata uthubutu baada ya kuambiwa kauli hii na Lee:





    “Nitakupa pesa unayotaka.”





    Akajichekesha na kuridhia dili hilo ambalo mbele ya macho yake lilionekana ni nono haswa. Uzuri alikuwa ana passport na kuhusu visa Lee akamwambia afike ubalozini, kuna mtu wake pale atakayempanga kufanikisha hilo ndani ya muda mfupi.





    Wakaelewana kila kitu na ikawa ndani ya mipango kuwa Glady atafika Uingereza keshokutwa kama mambo yakienda vile yanavyotakiwa.





    Basi baada ya hapo, Jona na wenzake wakaona ni vema wakienda kutembelea jiji la London na hata basi watakapopata fursa waende na kuyaona na yale maeneo ambayo wale mateka wao wamewaeleza.





    Ndani ya muda mfupi wakawa wamejiandaa. Wakawafungia wale mateka wao ndani ya chumba na kisha wakaondoka kwenda kubarizi jiji. Wakafanya vivyo ndani ya masaa matatu, walipomaliza kutalii huko wakaanza kupitia eneo moja baada ya lingine ya yale waliyopewa taarifa nazo. Uzuri Lee alikuwa msanifu mzuri kwenye uchoraji, akachora kila linalotakiwa, haswa muonekano wa majengo, njia na hata vituo.





    Kwahiyo kwenye majira ya jioni ndipo walirejea kwenye makazi yao, ya wale wakazi waliowateka, wakiwa wamefanya kila linalotakiwa. Ila walipofika walikuta mazingira tofauti, na jambo hili kidogo likawazusha shaka.





    Mosi, walikuta mlango u wazi. Pia walipotazama eneo walipowahifadhi wale mateka wao, hawakuwakuta! Zilibakia kamba tupu pasipo cha kufungia. Swala hili likawafanya damu zao zianze kuchemka!





    Kulikuwa na nyayo kadhaa za viatu kwenye zulia. Kwa harakaharaka nyayo hizo zilikuwa za watu watatu. Ina maana ndiyo hao waliokuja kuwakomboa mateka!





    Hawajakaa vema risasi zikaanza kurushwa kupasua vioo vya dirisha! Haraka Jona na wenzake wakalala chini. Risasi zikaendelea kutupwa kuchafua na kuharibu kabisa jengo. Zilikuwa ni risasi za mfululizo na nyingi!





    Watu waliokuwa wanashambulia walikuwa watano. Wanaume watatu na wanawake wawili. Wanaume walikuwa wamevalia makoti marefu rangi ya kaki, pengine ni sababu ya mvua za hapa na pale na baridi. Wanawake walikuwa wamevalia makoti ya ngozi yaliyobana miili yao na kufanya waendane na fasheni na kwa wakati huohuo kujiweka salama dhidi ya baridi.





    Nyusoni walikuwa wamevalia miwani meusi, ilikuwa ajabu ukitazama na muda huu wa giza. Labda, tuseme labda, miwani hizi hazikuwa za jua kama tujuavyo tuonapo kila miwani meusi.





    Basi mashambulizi yakaendelea kwa fujo. Ilikuwa ni kitu cha kushangaza maana Jona na wenzake hawakuwa wamkitarajia hili kwa ghafla hivi. Hawakudhani pengine vita ingeanza mapema kiasi hiki.





    Sasa maadui watakuwa wanajua kuhusu ujio wao, si ndiyo hivyo? Na pengine pia washajua kuwa wale makamanda wao waliowatuma tayari wameshauawa.





    Ndio, hilo lilikuwa bayana. Kumbe muda mfupi baada ya wao kuondoka, watu hawa wa kazi walifika kwenye makazi ya hawa madereva kwa ajili ya kukusanya taarifa toka kwao baada ya ukimya wa ajabu tangu watumwe. Ukimya pia kwa wale makamanda ambao hawakuwa wanapatikana hewani kwa ajili ya mawasiliano.





    Walichokikuta ni madereva hao wakiwa kambani na wakiwa tayari wametoa taarifa nyeti. Haraka wakapasha habari kule makao makuu na agizo likatolewa kwamba watu hao wamalizwe haraka kabla haijaleta kizazaa ndani ya nchi.





    Kumbuka taasisi hii ni ya siri. Hata waingereza wenyewe hawakuwa wanafahamu juu ya uwepo wake isipokuwa kwa watu kadhaa nyeti, tena wachache. Na ilitakiwa kuwa hivyo milele na milele, aamin.





    “Fuata silaha!” akapaza Jona. Kulikuwa kuna kelele sana. Risasi zilizokuwa zinapasuapasua madirisha zilifanya usikizani uwe hafifu. Ilibidi umtazame mtu anayeongea mdomoni ujue anasema nini au basi mpeane ishara.





    Taratibu wakasonga kwenda vyumbani. Kila mmoja na alipoweka silaha yake akachukua na kuziweka vema kwa ajili ya kujikomboa. Sasa wakaanza kupekua huku na kule kuangazia maadui zao wapo pande gani.





    “Wawili wapo upande wa mashariki …” akasema Komandoo mmoja, Blanko kwa jina la vitani. Mwingine naye, Chombo, akasema kuna wawili upande wake wa magharibi. Jona akamalizia kwa kusema kuna mmoja upande wa kaskazini.





    Basi baada ya jitihada hizo za kufahamu walipo maadui zao kufanikiwa, japo ilikuwa ni tabu wakipunyuliwa na ncha za risasi madirishani, wakagawana majukumu ya kuwashuhulikia. Makomandoo wawili, Chombo na Tito, wakapewa shavu la upande wa magharibi. Blanko na Miranda wakapewa upande wa mashariki na Lee akapewa upande wa Kaskazini.





    Jona yeye akabaki kuwa ‘free roller’ kazi yake ikiwa ni kuangazia na hata itakapobidi kwenda nje kuangalia kama kuna wengine na kupambana nao!





    Basi mashambulizi ya kutupiana risasi yakadumu kwa muda wa dakika sita. Wakafanikiwa kuwaangusha maadui watatu na kuwabakiza wanaume wawili tu. Ila hao wawili wakiwa wamefahamu kuwa wamezidiwa na mipango ya kimashambulizi, wakajificha, na basi wakawa wanatupa risasi zao kwa kutegea.





    Wakitupa mbili tatu, wanajiziba ama kuinama kusikizia majibu yaliyokuwa yanakuja kwa mkupuo.





    “We need backup!” alisema mmoja. Walikuwa wameweka migongo yao nyuma ya kuta wakihema kana kwamba wametoka mbio.





    “We are outnumbered! We need damn backup!” akafoka. Mwenzake akamtazama na kumwambia, “we need to go, not backup! Police are going to be here soon!”





    Hawajakaa vema, wakasikia king’ora cha polisi. Sasa wakaanza kutazamia nafasi watoroke kabla hawajatiwa nguvuni. Haikutakiwa kujulikana kama ni wao ndiyo walihusika na hilo tukio. Na hata kama wakikamatwa basi watajieleza kuwa wao ni majambazi na si wahusika wa taasisi yao ya siri.





    Walipotazama na kuona mazingira ni sawia, mmoja akachoropoka upesi akimwacha mwenzake nyuma. Mwenzake naye akatazamia usalama, mara naye akachopoka, ila alipokata kona akifuata upande ule alipokimbilia mwenzake, akastaajabu kumkuta mwenziwe chini!





    Hajakaa, mara akajihisi hana nguvu! Akajihisi analegea. Akadondoka chini asielewe kitu. Alikuwa gizani. Sauti ya king’ora cha polisi ilififia masikioni mwake na hatimaye ikakoma kabisa.





    Punde Jona akamsachi na haraka akatokomea hapo.







    **







    Saa tatu usiku …







    “We failed!” alifikisha taarifa mwanamke mwenye kibandiko cha upanga, yaani Sword., kifuani Alikuwa amesimama kwa ukakamavu akimtazama mkuu wao aliyekuwa amekaa vema kwenye kiti chake akiwa ameziba mdomo wake kwa kiganja chake kipana.





    “You failed,” mkuu akarejea kusema kauli hiyo kisha akatabasamu. “They’ve killed all our commanders. Kidnapped our drivers and got almost all information … Moreover, they are on our playground, at our home! … and you come here to tell me about failure!”





    Mkuu akabamiza ngumi mezani. Akasimama na kumkwida mwanamama aliyemletea taarifa, akamsogeza karibu na uso wake uliokuwa umegeuka kuwa mwekundu.





    “Don’t tell me that shit, okay? I am not used to failure, my dear. And don’t make me be, my dear. Got me?”





    “Yes, sir!”





    Mkuu akamsukumiza mwanadada huyo kando na kumfokea akimyooshea kidole.





    “I want them within reasonable time! Nobody can hide in this country as far as I know it like the palm of my hand! … And when you get them, bring them here to face me.”





    “Yes, sir!”





    Mwanamama akageuza mgongo wake kuufuata mlango. Mkuu akatoa agizo la mwisho. “Don’t return here with empty hands as I shall kill you with my bare hands, my dear.”





    Mwanamama akalipokea agizo na kwenda zake. Akakusanya kikosi cha wapambanaji kumi na wawili, na kabla hajatoka makaoni wakaingilia mifumo yote ya kamera zilizo mitaani na za utambulisho wa watu mahotelini. Hivyo punde watakapoona nyuso za walengwa wao zifanyiwe kazi haraka iwezekanavyo.





    Jambo hilo halikuwawia ugumu kwani nyuso za Jona na wenzake zilikusanywa upesi baada ya kufanya utaalamu wao wakizitoa kwenye kamera zilizokuwa zimefungwa kwenye nyumba za wale madereva waliotekwa.







    **



    Na basi sasa kazi inakuwa rahisi na pengine kabla ya jua kuchomoza kila jambo linaweza likawa limekamilika.





    Kwakuwa kumi na wawili ni watu wengi sana, kiongozi wao akaona si busara wakiongozana pamoja hivyo wagawane ipate kuwa rahisi kufanya kazi. Endapo taarifa zitakapotoka kuwa walengwa wapo upande fulani, basi waliopo karibu watafanya hiyo kazi wakati msaada zaidi ukiwa njiani waja.





    Kila kitu kikawa chema. Ni taarifa tu ndiyo ilikuwa inangojewa hapa na si kinginewe. Muda ukasonga mpaka majira ya saa kumi na mbili hivi ndipo mtandao ukatoa taarifa kuwa walengwa wamepatikana!





    Tiiiii! Tiiiii! Tiiiiii! Tarakilishi ya yule jamaa aliyebakizwa makaoni kwa ajili ya kuendesha mitambo ililia. Alikuwa anasinziasinzia. Alikurupushwa na alarm hiyo akarusha macho yake kwenye kioo.





    Akaona jina ni Queenland Hotel. Nyuso ambazo zilikuwa zimetunzwa kwenye ghala ya tarakilishi yake zilifanana kwa asilimia tisini na nane na zile ambazo zimeonekana kwenye hoteli ya Queenland!





    Akanyanyua simu ya mezani na kumpasha habari mkuu wa kikosi kilichopo huko mtaani pasipo kujali ukubwa wa usiku. Akamweleza bayana kuwa waelekee Queenland na watapata wanachokitaka.





    Basi taarifa ikapokelewa na kutumwa tena kwa watu wanne waliokuwa karibu na ilipo hoteli hiyo. Waende huko upesi na wenzao wapo njiani kuwafuata.





    Watu hao wanne, wawili majibaba na wawili wakiwa ni wadada, wakaenda mara moja kutekeleza agizo. Walikuwa ndani ya gari aina ya BMW x6 nyeusi ambayo vioo vyake vilikuwa vimefungwa kuwa giza.





    Gari likaenda kwa kasi, na lilipofika kwenye uwanja wa hoteli hiyo, kabla ya kushuka watu hawa wakafungia bunduki zao vyuma vya kupunguzia sauti, alafu wakahakikisha mifumo yao ya mawasiliano ipo sawia.







    **







    “Nimekipenda!” alisema Komandoo Chombo akitazama kuangaza chumba walichotoka kuingia muda si mrefu. Kilikuwa ni chumba kipana kilichokuwa na rangi mbalimbali za kuvutia. Taa kubwa na ya urembo ikining’inia na madirisha mawili ambayo yana mwonekano mzuri wa maghorofa mengine yaanayopakana nayo. Mbali na hapo kuna bafu pana lenye kila aina ya huduma.



    Ama kwa hakika vilikuwa vinavutia machoni na viliendana haswa na gharama zake. Wanaume hawa watatu, Komandoo Chombo, Tito na Blanko, wote kwa pamoja walivutiwa nacho.





    Wakawa wanaendelea kupekua, isipokuwa Chombo yeye akawa amejitupia kitandani alipopokelewa na godoro laini kubwa lililomhakikishia mapumziko ya furaha.





    Muda si mrefu, hodi ikagongwa. Kwakuwa wengine, yaani Tito na Blanko, hawakuwapo mazingira ya karibu, Tito alikuwa bafuni na Blanko akiwa ameenda mpaka kwa nje kuangalia mazingira, Chombo ikampasa kuitikia hodi hiyo.





    Akanyanyuka kivivu kujongelea mlango. Alipofika akauliza kabla hajafungua,





    “Who’s it?”





    Akaitikiwa ni mhudumu. Basi akafungua na kuangaza. Akakutana na mwanadada mrembo aliyekuwa amevalia sare. Mkononi alikuwa amebeba trey ya mvinyo na glasi zake nne.





    Akatabasamu akitembea kuzama ndani. Alipofikia mezani akaweka mvinyo ule na kumtazama Komandoo Chombo.





    “Are you alone?” akamuuliza akiwa anatazama huku na kule. Chombo akatabasamu kidogo na kusema. “No. I am wrih my friends!”





    Mhudumu akatabasamu na kusema, “Oh! It’s sweeter when it’s shared.” kisha akaenda zake kuufuata mlango Chombo akimtazama. Alikuwa anatembea kwa madaha kiasi cha kuvutia kumtazama, achilia mbali urembo wake maridadi.





    “Anything else, Mr.?” akauliza mhudumu akiwa ameshikilia mlango.





    “No! … Nothing,” akajibu Chombo kwa sauti ya kutokumaanisha.





    “Ok, I will be here so soon to take leftovers,” akaaga mhudumu kwa namna hiyo, na Chombo akamsindikiza kwa macho malaini kabla hajaufunga mlangowe kisha akarudi na kuungana na wenzake ambao walikuwa tayari wameshatoka huko walipokuwa.





    “Jamani kuna mambo yenu hapo,” akasema akionyeshea ule mvinyo ulioletwa na mhudumu.





    “Oooh!” akadakia Tito. “Ila nimekuona ulivyokuwa unamtazama yule mhudumu!” akatania wakacheka. Na basi kwakuwa mhudumu alisema kuwa atakuja kuchukua mabaki muda si mrefu, wanaume hawa hawakukawia wakabwia kinywaji na kuacha chupa i nyeupe ndani ya sekunde kadhaa tu.





    Vinywa na makoo yao yalikuwa yamezoea vinywaji vikali. Hii ‘wine’ ilikuwa ni kama sharubati tu. Hata glasi hawakutumia bali waligida kwa mtindo wa tarumbeta.





    Ila walipomaliza walijikuta wakihisi vichwa ni vizito sana. Hawakuweza kudumu tena, wakajilaza kana kwamba ng’ombe waliokuwa hoi kwa kulimishwa siku nzima.





    Lakini mabwana hawa, mbona si kujiuliza kuletewa kinywaji hicho muda kama huo wa usiku mnene? Pengine imani yao ilikuwa kubwa. Ama tuseme kiu za makoo yao zilizidi uwezo wa wa kufikiria.







    **







    Akiwa bafuni, anasikia hodi. Miranda anazima bomba lake la maji na kuskiza vema kama kweli akisikiacho ndicho. Ni kweli. Alijiuliza kidogo kabla hajavuta taulo lake akajifuta uso na kulikaza vema kifuani.





    “Comiiiing!”





    Akatoka kwenda mlangoni. Kabla hajafungua, akachungulia kwanza na kumwona mwanamke aliyevalia sare za wahudumu. Mkononi mwake alikuwa amebebelea trey lenye mvinyo mwekundu pamoja na glasi mbili.





    “You’re welcome!”





    “Thanks. Sorry for my disturbance.”





    “Never mind.”





    “Mam, it’s my pleasure to serve you with the finest and royal wine in the country. Hope you are going to enjoy it the same to your stay in our hotel.”





    “Thanks,” akasema Miranda akitabasamu kinafki. Mhudumu akazama ndani na kwenda moja kwa moja kwenye meza alipoweka mvinyo aliouleta na kisha akaaga.





    “I will be back soon to take leftovers.”





    Miranda asijali sana, akarudishia mlango na kurudi bafuni kumalizia zoezi lake. Lakini mhudumu yule, ambaye ndiye yuleyule aliyewapa wale makomandoo mvinyo, hakuwa amekomea kwake.





    Sasa akiwa amebebelea mvinyo mmoja wa mwisho akaelekea chumba kilichokuwa kimewahifadhi Jona na Lee. Mvinyo huo mmoja ulikuwa unasindikizwa na glasi mbili pia pembezoni. Kama kawaida akagonga na muda si mrefu akafunguliwa.





    “Hey!” alikuwa ni Lee. Kiunoni alikuwa amefungia taulo. Na kabla hajafungua alihakikisha kwanza mhudumu huyo yupo peke yake kwa kuchungulia.





    Mhudumu akaomba samahani na kuteta haja yake, amekuja kuwaletea mvinyo bora kabisa. Basi pasi na hiyana, Lee akamkaribisha azame ndani. Mhudumu huo akiwa anatembea kwa maringo, akaingia na kunyookea meza.





    Kitandani Jona alikuwa amelala ila si usingizi. Alikuwa anahisi uchovu na pengine isingezidi dakika tano angekuwa ameshapitiwa na usingizi. Hata hivyo kitu pekee kilichomfanya akadumu kwa muda akiwa amcho, ni kumngoja Lee atoke bafuni naye ajimwagie maji.





    Basi macho yake yakiwa bado ni mazima, yakamtazama yule mhudumu. Kichwani akajiuliza maswali kadhaa haswa la kuletewa mvinyo wakati ule. Ila akili yake ilikuwa imechoka, zembe kwa muda huo. Hakujali sana. Labda wanataka wateja wao walale unono, akawaza kaupumbavu.





    Ila wakati mhudumu anaweka mvinyo mezani, Jona akaona jambo lililompatia shaka. Alidhani pengine ni macho yake ila la hasha, alikuwa sahihi! Kwenye nyonga ya kulia ya mhudumu kulikuwa na bunduki!





    Bunduki hiyo ilikuwa imezibwa na sketi ya sare. Ni kuinama kwa mhudumu ndipo kulifanya silaha hiyo ihakisiwe tena endapo kama ungetazama kwa umakini.





    Mhudumu akamtazama Jona na kutabasamu, kisha akaanza safari yake ya kimadaha kwenda mlangoni.





    Kwa namna alivyokuwa anatembea na namna anavyovutia, mwanaume ungepata wapi wasaa wa kumdhania mwanamke huyu ni hatari? Macho yako yote yangekulevya kufaidi uumbwaji wa Mungu uje kutambua unamalizwa ukiwa unakufa!





    Akiwa amebakiza hatua tatu kuufikia mlango, sauti ya kiume ikakoroma, “Please, stop!”





    Akasimama.





    Akasikia Jona akitoka kitandani na kusimama, basi akaanza kujongesha mkono wake kwenda kwenye silaha. Huenda mambo yamebuma.





    Jona akasonga na akasimama hatua mbili nyuma yake. Mwanaume huyo alikuwa amevalia suruali pekee. Macho yake yaliyokuwa na uchovu sasa yalikuwa yanatazama kwa mashaka.





    “Who are you?” Jona akauliza.





    “I am the waitress!” akajibu mhudumu. Hakuwa amegeuka. Alikuwa anatazama mbele kuangazia mlango. Pale mlangoni alikuwa amesimama Lee, bado hajajua kinachoendelea hapa uzuri.





    “Why do you bring wine at this time?” Jona akauliza kwa sauti ya amri.





    “It’s our schedule,” akajibu mhudumu, alafu akageuka kumtazama Jona. Bado mkono wake ulikuwa karibu na nyonga yenye silaha.





    “Can you please taste it for us?” Jona akaomba. Mhudumu akatabasamu na kuuliza, “Why? You think we want to kill our clients?”





    “Maybe!” Jona akajibu akipandisha bega la kulia. “You never know.”





    Hapa mhudumu akamtazama Jona machoni, wakatazamana kwa sekunde nne pasipo kufanya jambo.





    “Okay!” Mhudumu akabinua mdomo. “I will do what you wish.” kisha akasogelea mvinyo na kumiminia kwenye glasi.







    **



    Kabla hajautia kinywani, akasita. Akamtazama kwanza Jona na kisha Lee. Nyuso za wanaume hao tayari zilikuwa zimebeba shaka. Mambo hayakuwa sawa.





    Basi mhudumu huyu akapeleka glasi kinywani, ila kabla hajafyonza, akachomoa upesi bunduki yake toka kiunoni. Alifunua sketi yake upesi kiasi kwamba hata nguo ya ndani haikuonekana. Kabla hajawanyooshea wakina Jona na kufyatua, Jona akawa amemfikia! Ila bado akafyatua. Risasi ikaruka na kutoboa mlango.





    Kabla tena hajafanya jambo, Jona akawa amempokonya bunduki. Ila naye mhudumu akawa na upesi, hakumruhusu Jona amshambulie, akamng’ang’ania mkono wake, Jona akauvuta kwanguvu na kumtandika kiwiko, akadondoka chini!





    Alikuwa anavuja damu puani. Kichwa kilikuwa kinamgonga sana. Hakuweza kunyanyuka tena na kupambana. Jona akamfunga kinywa na mikono kwa kutumia mkanda wake kisha akaenda upesi kwenye chumba cha Miranda kwani alihisi huenda mhudumu yule akawa ameshapitia huko kwani chumba chake kilikuwa cha mwisho kwenye utaratibu wa namba.





    “Who’s it?” sauti ya Miranda iliuliza.





    “It’s me, Jona!”





    “Jona?” Miranda akajiuliza kwa sauti yake ya chini. Alikuwa ameketi kitandani akiwa bado hajatoa taulo mwilini mwake. Kwa ujumla alikuwa amejifunga mataulo mawili, moja kifuani na lingine kichwani, ila kuendea mlango, akajivesha taulo kiunoni kutimiza matatu.





    “Umekunywa wine?” lilikuwa swali la kwanza la Jona. Aliuliza akiwa ametoa macho na akizama ndani kwa kuusukuma mlango. Alipotupa macho akaona chupa ya wine mezani. Haikuwa imefunguliwa. Hatimaye akashusha pumzi.





    “Kuna nini Jona?” Miranda akauliza kwa uso wa mashaka.





    “Tupo under attack,” Jona akamjibu akimtazama kwa macho ya hakika. Ila hakusema sana, akaenda kuufuata mlango atoke, ila kabla akamtazama Miranda na kumwonya, “Usinywe hiyo wine!” kisha haraka akauendea mlango kuelekea kwenye chumba cha wale makomandoo.





    “Vipi, amekunywa?” Lee aliuliza. Alikuwa ni punde ametoka kwenye chumba. Ameshavalia suruali na shati jepesi.





    “Hajanywa!” Jona akajibu akiwa na haraka. Akauendea mlango wa wale makomandoo akiwa anaongozana na Lee kwa nyuma. Akaukuta mlango ukiwa umefungwa. Akagonga pasipo mafanikio. Akauvamia kuuvunja.





    Kutazama ndani akawaona mabwana wale wakiwa wamelala kitandani. Hawakuonekana kujielewa. Na kama wangelikuwa wazima basi wangelikuwa wamedamka punde waliposikia mlago ukigongwa, hata basi ukivunjwa.





    Chupa ya wine ilikuwa tupu, haina kitu!





    “Wamekunywa!” Lee akaropoka. Walitazamana na Jona, Jona upesi akawafuata wale makomandoo na kuwanusa. Walikuwa wananuka pombe!





    Lakini zaidi hawakuwa wanapumua! Mapigo ya moyo yalikuwa yamezima! Kiufupi, walikuwa wamekufa.





    “Tunafanyaje, Jona?” Lee akauliza.





    “Sijui!” Jona akasema akiketi kwenye kitanda. Alishika kichwa chake kwa mawazo.





    Ila upesi akiwa amekumbuka jambo, akamtazama Lee na kumwambia, “Tuondoke hapa upesi! Wauaji wameshajua wapi tulipo.”





    “Na vipi kuhusu hii miili?” Lee akauliza.





    “Inabidi tuondoke nayo. Hatuwezi kuiacha hapa!” Jona akasema akisimama.





    “Hapana, Jona!” akasema Lee akitikisa kichwa. “Ni hatari sana kufanya vivyo. Hatujui maadui wapo wapi, wapo wangapi. Tutawezaje kujiokoa na huku tuna miili mitatu?”





    “Sasa tutafanyaje?” akauliza Jona. Alikuwa ni kama mtu aliyechanganyikiwa. Kwa muda akili yake ilikuwa haifanyi jambo. Alikuwa anawaza mambo mengi kwa wakati mmoja.





    “Tutapiga picha na kuzituma mtandaoni,” akasema Lee. “Tutaandika caption, najua picha itasambaa mtandaoni na watapata namna.”





    “Seriously?” Jona akatia shaka.





    “Ndio. Jona hatuna muda hapa. Lazima tufanye maamuzi ya hekima ama wote tuwe wafu!”





    Kabla Jona hajasema jambo, wakasikia sauti za vishindo. Wakahisi si shwari. Haraka Lee akachomoa simu na kupiga picha miili ya wale makomandoo …





    Huko nje koridoni kulikuwa na wanaume wawili na mwanamke mmoja. Watu hawa waliokuwa wanatembea sambamba walikuwa wamebebelea bunduki mikononi mwao. Nyuso zao zilikuwa za kazi na macho yao yalikuwa yanaangazia milango mitatu inayofuatana.





    Milango mitatu ya vyumba vya Jona na wenziwe.





    Basi punde walisimama mbele ya chumba cha wale makomandoo. Chumba hicho kilikuwa wazi tu. Hawakuona mtu. Basi wakausogelea mlango, walipofika, wale wanaume wawili, ghafla mlango ukafungwa kwanguvu na kuwakumba!





    Wakaweweseka. Walimparamia mwanamke aliyekuwepo nyuma yao na huo ukawa mwanya mzuri kwa wakina Jona kushambulia. Haraka Jona na Lee wakawarukia, na kwa ustadi wao, wakawapokonya silaha na kuwalalisha chini kwa maumivu.





    Haraka wakamshtua Miranda na kumwambia waende upesi kwani mambo yameharibika. Upesi Miranda akatoka na wakaelekea kaskazini mwa hoteli. Muda si mrefu, kwenye eneo la tukio, pale walipokuwa wameachwa wale watu walio hoi kwa kipigo, akawa amewasili mwanamke kamanda, Sword, akiwa ameongozana na watu wanne wengine.





    “Where are they?” Mwanamke huyo akauliza. Mwanaume mmoja akanyooshea kidole chake upande wa kaskazini, basi haraka mwanamke huyo kamanda akiwa ameongozana na watu wake wakaelekea huko.





    Walisaka, hawakuona mtu! Kabla hawajarudi kwa wale wenzao, wakasikia sauti ya mtu anagugumia. Kwenda kutazama, wakamkuta mlinzi akiwa amefungwa mdomo.





    “They’ve escaped!” Mwanamke kamanda akaropoka. Geti la uani lilikuwa wazi. Wakina Jona walikuwa wametoroka, na ni wazi haikuwa muda mrefu. Bado geti lilikuwa linachezacheza!





    Basi haraka kamanda Sword na wenzake wakakimbilia huko. Kutazama kushoto na kulia, kwa mbali mkono wao wa kuume, wakaona mtu anaishilia. Wakaanza kukimbia kuelekea huko, kufika hawakuona mtu!





    “Shit!” akalaani kamanda Sword akipiga kofi paja lake. Mazingira yalikuwa tulivu mno. Ni usiku huu tena mzito. Magari machache yalikuwa yanaonekana barabarani, watu wanaotembea kwa mguu hawakuwapo.





    Basi punde, mawasiliano yakaungana toka kule makaoni. Mwanaume yule aliyekuwepo kwenye mitambo akawaambia wapi alipowaona walengwa wao. Ni mtaa wa pili toka walipo. Wapo barabarani bado hawajapata usafiri!





    Lakini pia akawaonya kuwa mmoja wao ameshikilia bunduki.





    “Let’s go!” akaamuru kamanda. Moja kwa moja wakaenda huko walipoambiwa.





    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    **







    Asubuhi na mapema kila kituo cha habari kikarusha taarifa juu ya watu waliokutwa wakiwa wafu kwenye moja ya mtaa wa London. Watu hao walikuwa ni wale waliokuwa wanawafukuzia wakina Jona, kwa idadi watu wanne! Wawili miongoni mwao wakiwa majeruhi wapo hospitali kupokea huduma.





    Mbali na hayo, pia hata ile miili ya wale makomandoo na kile kilichotokea kule hotelini kikarushwa na watu wakajua. Hata watu wa Tanzania nao wakapata habari juu ya wanajeshi wao kwenye nchi ya kigeni. Kuitikia hilo, shughuli za kufuatilia miili hiyo ikaanza mara moja.





    Basi, mambo yakazidi kupamba moto. Kwakuwa kikosi nambari ‘wani’ kilikuwa kimeshashindwa kufanya kazi yake ya kuwamaliza wakina Jona, ikabidi sasa kitumwe kikosi cha pili. Cha sasa pia kilikuwa kinaongozwa na watu kumi chini ya kamanda mwanamke mwenye jina la Arrow.





    Nao wakadumu kwa siku moja. Wote wakapukutika. Kikatumwa kikosi cha tatu na cha nne, nao hawakuwa wameambulia kitu. Wote wakamalizwa kana kwamba maji. Ilikuwa ni kama utani, lakini watu wakienda hakuna aneyerejea zaidi ya taarifa ya habari ya watu kukutwa kwenye mahoteli, ama barabarani!





    Kabla ya kikosi cha tano hakijatumwa, Kamanda mkuu, akaona ni kheri kabla hawajafanya hilo, watulie kwanza kuona wapi wanakosea. Ni wazi sasa wakina Jona watakuwa wanafahamu wanachokifanya.





    Wakapanga mipango madhubuti ya kuwa, punde wakina Jona watakapoonekana kwenye kamera basi watoe taarifa polisi kwanza. Wahakikishe watu hao wanahitajika na serikali. Na basi picha zao zitazagaa kutangazwa kwenye vyombo vya habari.





    Hapo watakuwa wameihamishia kesi mikononi mwa serikali. Ila,





    “Don’t you think it will be risk even for us?” akauliza mmoja. Walikuwa wanafahamu wakina Jona watakuwa ni watu wanaujua nyendo zao, vipi wakikamatwa na polisi, hawatatoa taarifa zao huko kituoni?





    “No!” akasema Kamanda mkuu akitikisa kichwa. “Before doing that I will have already killed them!” Basi kikao cha dharura kikawa kimeishia hapo. Na siku hii ikaenda salama mpaka kwenye majira ya saa tano usiku.





    Kamanda mkuu akatoka kwenda kwenye tafrija fupi iliyokuwa imeandaliwa na Malkia kwa ajili ya kumpongeza mmoja wa vijana wake, kwa jina Prince Henry, kwa kupata mtoto wao wa kwanza na mwanamke aitwaye Diana Lavik, mwanamke mwenye asili ya kilatini.





    Tafrija ilikuwa imehudhuriwa na watu wakubwa na wazito. Ulinzi ulikuwa mkubwa. Watu walikuwa wamependeza kwa suti na magauni ya kumetameta aghali.





    Basi bwana Kamanda alipoiingia, haikuchukua muda kupata kinywaji mkononi mwake. Na pia watu wawili watatu wa kupiga naye soga za hapa na pale. Ila akiwa anafanya hivyo, mara akasikia sauti ya mwanamke nyuma yake.





    “Hey, gentleman.”





    Sauti hii ilikuwa kavu ila tamu masikioni. Haikumchukua muda kamanda akageuka kutazama. Hamaki uso kwa uso akakutana na mwanamke mwenye rangi ya dhahabu. Nywele zilizofundwa vema na macho ya kuvutia. Kiuno kimekabwa na gauni na amepanda kwa viatu virefu nyeusi.





    Mwanamke huyu alikuwa ni Glady.





    “Do I know you, madam?” Kamanda akauliza.





    “Yes, you do!” akajibu Glady akirembua. “Would you mind a dance?”





    “Off course!”





    Glady akamkwapua Kamanda na kusonga naye kando kucheza wimbo wa taratibu uliokuwa unapiga. Sikioni mwake sauti ya mbali ikamwambia, “Hakikisha unamuua.”







    Kamanda alimtazama Glady machoni akamwona mwanamke mrembo haswa. Mwanaume huyu hakuwa mtu wa kupenda rangi nyeusi, ila hapa kwa Glady akachina haswa. Hakuwahi kumwona mwanamke mrembo kama huyu. Kwenye mikono yake alikuwa anampatia joto fulani analolihitaji.





    Na zaidi ya yote Glady alikuwa na kitu ambacho wanawake wote wa kizungu aliokuwa nao hawakubahatika kuwa nacho - shepu! Kiuno kinajulikana kipo wapi, na baada ya kiuno basi nini kinafuatia.





    Hakika hapa bwana Kamanda alikuwa ameshikwa. Ugumu na ukatili wake wote ukawa ni sponji chakavu mbele ya mwanamke kubuhu. Mtambo. Bibie Glady.





    Kwa kujiamini kabisa mwanamke huyo alikuwa anamtazama mwanaume huyo machoni. Lakini siyo kumtazama kama ujuavyo wewe, lah! Kumtazama kiuanamke. Kumtazama kwa macho yanayoomba huba. Macho yanayolilia mapenzi ya ndani!





    Ama kwa hakika chunusi ilipata kucha ndefu. Kiuno cha Glady kilichokuwa kimeshikiliwa na mkono mpana wa Kamanda kilikuwa kinaenda kutoka na midundo ya muziki. Nyonga yake iliaga kila melodi.





    “Who are you?” Kamanda akajikuta anauliza. Alishindwa kuvumilia zaidi. Hakutaka muziki ukome. Hakutaka mwanamke huyu atoke mikononi mwake. Na hii ndiyo ilikuwa sababu ya Glady kulipiwa kila kitu aje Uingereza. Hata wale waliokuwa wanatilia shaka, sasa walianza kusadiki. Kila kazi na mkono wake.





    “My name is Rebentha…” akasema Glady pasipo kutumia nguvu. Lips zake zilizokuwa zimechovya ‘lipstick’ hazikuwa zikihangaika bali ulimi.





    “Rebentha?” Kamanda akaguna. “Rebentha from?”





    Glady akatabasamu. Kamanda akahisi amepigwa shoti, kwa muda kidogo akasahau hata alichouliza, akasema, “You are so beautiful, Rebentha!”





    “Thanks,” Glady akaipokea kwa madaha na kusema, “I am from Caribbean.”





    “Caribbean! Wow! I have never been there. How did you know me?”





    “How long does it take to see a handsome lonely man in the party?”





    Kamanda akatabasamu pasipo kutia neno.





    “Honestly I don’t know you. But my eyes just fell on you. Is it wrong?”





    Kabla Kamanda hajatia tena neno, Glady akatazama kushoto kwake kwa mbali na kusema alikuwapo kule akinywa kinywaji kabla hajamtia machoni mwanaume huyo aliyependeza akiwa mpweke, aongea tu na wazee hapa na pale.





    “You are so confident!” akasema Kamanda.





    “Doesn’t that turn you on?” Glady akauliza. Basi Kamanda akaishia kutabasamu, akamkumbatia kwanguvu mwanamke huyo na kucheza naye kwa muda kabla hajamwomba wakapumzike kidogo na kufanya maongezi zaidi.





    Lakini kabla ya kwenda huko, Glady akamlaghai wacheze zaidi kwani bado ana hamu ya kufanya vivyo. Akiwa nyumbani huwa hapati huo muda na yeye kucheza ndicho kitu anapenda zaidi.





    Basi Kamanda hakuona tabu. Hakutaka kumghafirisha mwanamke huyo mrembo, akampatia dakika tatu za ziada. Wakacheza na akiwa anamuuliza maswali ya hapa na pale, wapi ametokea na amekuja na nani?





    Wakiwa hapo wanacheza kutafuna hizo dakika tatu za ziada, ndipo Glady akawa anapanga namna ya kufika kwenye kilele cha kazi yake. Wigi lake refu lilikuwa linamziba masikio yaliyokuwa yana ‘earphone’ za mawasiliano na pia hereni zake zenye ncha kali.





    Baada ya kutazama huku na kule, akiwa anapiga mahesabu kichwani, akatengeua mguu wake wa kuume, kisigino cha kiatu kikameguka, akaangushia kichwa chake kwenye bega la Kamanda. Mara Kamanda akaguna kutoa sauti ya maumivu akiwa amekunja sura.





    “I am sorry! … shit! Its my earring!” Glady akasema akitoa kichwa chake akijitahidi kusimama. Shingo ya Kamanda ilikuwa imechanjwa kidogo. Kwa mbali kulikuwa kuna kamstari kekundu. Na punde, damu ikaanza kuchuruza.





    “It’s okay, never mind!” Kamanda akasema akishika eneo lenye maumivu. Kutazama vidole vyake akaona alikuwa anavuja damu, basi akamwomba mrembo muda mchache akapate kujiosha, atarejea.





    “Its ok. I will be waiting,” akasema Glady akiwa na sura ya taharuki na huzuni. Mwanamke huyu aliigiza haswa. Basi Kamanda akaenda zake ‘washroom’ Glady akimtazama mwanaume huyo akiishia, kisha akaweka kidole chake sikioni na kusema,





    “Nimemaliza kazi!”





    Ama kweli vitamu ndivyo venye sumu.







    **





    Alijihakikisha kama yupo sawa. Anhaa akaridhika. Damu ilikuwa haitoki tena hata tone. Basi akajifuta kwa mara ya mwisho na kitambaa chake kilicholowana maji alafu akajitengenezea vema. Bado alikuwa amependeza na suti yake toka Italia.





    Kamanda akajirekebisha nywele zake kabla ya kwenda kukutana tena na mrembo. Alipojihakikishia kuwa yuko sawia kwa kila kitu, akatoka kuuendea mlango. Ila kabla hajaufikia, akahisi kichwa chake kinagonga. Alisimama na kuskizia, akajiona bado yu vema, basi akaendelea na safari yake.





    Alipofika kwenye uwanja akaangaza huku na kule, hakumwona Rebentha! Lakini punde , si Rebentha tu, hata watu wengine akawa hawaoni. Walianza kuwa maruweruwe, asione cha kueleweka! Kichwa kikamgonga sana, na damu zikaanza kummiminika toka puani kwa fujo.





    Hakudumu kwa muda mrefu akiwa amesimama, akajikuta chini!





    Watu wakamtazama na kumsogelea. Damu hazikukatika, zikaendelea kummiminika zaidi na zaidi kuchafua suti yake aghali. Kwa muda kidogo shughuli ikawa imesimama. Mwili wa Kamanda ukanyanyuliwa na upesi ukatiwa kwenye gari la wagonjwa lililokuwapo eneoni kuwahishwa hospitali, huku nyuma tukio hilo likiwa limeacha zogo.





    Gari hilo la wagonjwa likatimka haswa, ving’ora vikitawala barabarani. Lakini kumbe waliopo humo ndani si wahudumu bali ni Jona na wenzake. Walikuwa wamevalia sare na vichwa vyao vimemezwa na kofia zenye chapa ya huduma.





    Sasa watu hawa walikuwa wamempata Kamanda. Tena kwa ulaini kabisa. Gari hilo la wagonjwa baada ya kutembea kwa takribani dakika kumi na tano, likazima ving’ora na kutoka kwenye barabara kuu.





    Likapotelea huko kusikojulikana.







    **





    Baada ya juma moja … Dar es salaam, kituo kikuu cha polisi.







    Sauti ya kishindo cha miguu yenye buti ilikomea mbele ya lango la nondo za chuma, hapo akasimama Askari mnene mweusi mkononi akiwa amebebelea bunduki na kiunoni mwake amening’iza pingu.





    Akatazama ndani ya chumba cha mahabusu, macho yake makubwa yakaangukia kwa mtu mmoja aliyekaa nyuma kabisa. Jona. Akampa ishara ya kichwa kumtaka asonge karibu. Jona akafanya hivyo. Akashika nondo na kumuuliza askari,





    “Mmefanya nilichokiomba?”





    Askari hakumsemeza jambo, akachojoa ufunguo na kufungua lango, Jona akatoka. Akaongozana naye mpaka kaunta ambapo huko alikutana na Makamu wa Raisi, ambaye kwa sasa ndiye alikuwa amekaimu kiti cha Raisi.





    Akamsalimu na Makamu akamuuliza, “Ndiyo wewe Jona?”





    “Ndio, mheshimiwa.”





    “Hata kama usingeliomba kuonana na mimi, ningekuja kuteta nawe maana nahisi nina mengi ya kusikia toka kwako.”





    Basi Jona akapatiwa nafasi ya kuteta pamoja na Makamu wa Raisi kwa faragha. Akamweleza yote toka herufi A mpaka Ze. Na kama haitoshi, akamkutanisha mheshimiwa huyo na wenzake: Miranda, Lee na Marwa. Nao kila mmoja kwa nafasi yake akaeleza yote yale ya kweli, na hata kuthibitisha wayasemayo kwa nyaraka na shahidi mbalimbali zilizokuwa mikononi.





    Makamu wa Raisi akapigwa na butwaa na yale yote aliyoyasikia. Ilikuwa ni ngumu kuyakataa kwani hata matukio yaliyokuwa yanatukia ndani ya nchi pasipo na majibu ya uhakika, yaliungana mkono na maelezo na shahidi zilizotolewa.





    Akaamuru wale wachimba madini, wakina Nyokaa, watiwe nguvuni upesi. Pia akatoa agizo wakina Jona waachiwe huru, lakini akamtaka Jona aonane naye faragha baada ya majuma mawili. Zaidi akawapatia kiasi fulani cha fedha kama motisha kwa kupigania nchi yao kwa dhati.





    Siku hiyo Jona na wenzake wakafanya tafrija nyumbani kwa kujipongeza. Wakamwalika pia Glady na Miriam ambaye hakusita kuja upesi. Tafrija ikafana sana na kila mtu akafurahia isipokuwa kwa Sheng ambaye alikuwa mlemavu wa kudumu kwa kupooza.





    Yeye alikuwa kwenye ‘wheelchair’ akitokwa na machozi. Hakuwa anaweza kusogeza mwili wake hata kidole. Alikuwa ni wa kufanyiwa kila kitu, na kwakuwa hakukuwa na mtu mwenye muda huo, wote walishakubaliana kuwa mwanaume huyo atatumwa kwenda kwao China kukutana na familia yake.





    Kwa mujibu wa daktari hakuwa anaweza kudumu hai zaidi ya miezi miwili tangu sasa.





    “Samahani sana, Sheng,” alisema Lee. “Sitaweza kuwa nawe tena kwa sasa maana nimepata familia mpya. Nasikitika maana utakuwa mpweke sana, na mikono yako iliyozoea kuua haiwezi tena kufanya kazi hiyo.





    Ila nina furaha pia maana kwa sasa hatimaye utakuwa huru kuwa na familia yako. Hautakuwa na haja ya kujificha tena maana wote wameshamalizana wenyewe kwa wenyewe. Pengine kwa muda kidogo tutaiona dunia ikiwa tofauti.





    Kwaheri Sheng.”







    Lee aliposema hayo, akambusu Sheng kwenye paji la uso na kurudi tafrijani alipokutana na Glady na kukumbatiana kwa huba. Ila muda si mrefu, Jona akamwita na kumtaka faragha.





    “Kuna lolote?” akauliza.





    “Ndio, lipo,” Jona akajibu na kisha akatazama kushoto na kulia kuhakikisha kama wapo wenyewe. Akamnong’oneza jambo Lee, Lee akatabasamu. Ghafla, Lee akamshika mkono Jona na kumvutia tafrijani kisha akapaza sauti,





    “Naomba tuskizane tafadhali!” muziki ukazimwa. Watu wote wakawatazama. “Jona hapa ana kitu cha kuwaambia…”





    “Mimi?” Jona akatahamaki.





    “Oooh basi nitakusaidia kusema …” Lee akapayuka. “Jona wants to marry Miranda!”





    Watu wakalipuka kwa shangwe, ila Miranda akaziba mdomo wake akiwa ametoa macho kwa kutoamini. “Serious?” akauliza akitahamaki. Basi Jona akamtazama na kujikaza akimwambia, “Yes, serious!”

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    Mara Miriam akadondoka chini na kuzirai.







    ***





    MWISHO WA SEASON 2







0 comments:

Post a Comment

Blog