Search This Blog

Monday 27 March 2023

GARI LA KUKODI - 2

  



Simulizi : Gari La Kukodi

Sehemu Ya Pili (2)

mwanasheria wa kampuni na familia ya Mr. Oduya kwa miaka zaidi ya kumi.


“Abbas, nadhani umeona kinachoweza kukutokea endapo hutaonesha ushirikiano, tambua hatupo hapa kukuumiza. Ni rahisi tu… tuambie ni kipi chanzo chako cha taarifa kisha tutakuacha uende zako!” sauti nzito ya Mr. Oduya ilivuma ndani ya kile chumba kupitia spika.


Abbas aliendelea kukaa kimya pasipo kujibu chochote. Spoiler alimwachia na kuchukua koleo ndogo mbili kisha akakibana kidole kimoja cha Abbas kwa koleo na kuanza kung’oa kucha.


“Aarrgghh! Fu** you… motherfu***r!” Abbas alipiga kelele kubwa iiliyofuatana na matusi mazito kutokana na maumivu makali.


“Kama hutaki tuumizane sema ukweli ili nisiendelee kung’oa na hizi kucha zingine,” Spoiler alisema kwa ukali lakini Abbas aliendelea kuporomosha matusi mazito, akitukana ukoo wote wa Spoiler.


Spoiler alimchapa kofi kali usoni lililomsababisha kuona vimulimuli, hakuishia hapo, aliachia tabasamu la kinyama na kuanza kumshushia kipigo kikali. Ndani ya dakika tano tu chumba chote kilitapakaa damu na Abbas alikuwa hatazamiki.


“Sasa tueleze tunachotakiwa kujua…” Spoiler alisema huku akishusha pumzi ndefu.


Pamoja na yale mateso makali lakini Abbas aliendelea kuwa kimya, alikuwa ameazimia kutosema chochote, hata ikibidi kuuawa. Uso wake haukuwa na chembe ya mashaka wala uoga. Ni kama alikwisha kata shauri la kufa na siri yake moyoni.


Spoiler alimtazama kwa kitambo kisha alichukua kibubu kidogo cha gesi na kukiwasha, akarekebisha moto kwenye kile kibubu na kumfuata Abbas.


“Tunazo njia nyingi za kukulazimisha uongee ukweli usitake tufike huko, sasa sema ukweli vinginevyo nitakuharibu usiweze kutambulika,” Spoiler alimwambia Abbas huku akiupeleka ule moto wa gesi na kuupitisha kwenye kifua chake.


“Unanitishia kuniua? Wewe ni mpumbavu. Kwa taarifa yako siogopi kifo… hutapata chochote toka kwangu, bora mniue tu kuliko kuendelea kupoteza muda wenu,” hatimaye Abbas alifoka na kumtemea mate Spoiler.


“Naona umejitolea kufa peke yako huku wanaokutuma wakiendelea kustarehe huko waliko,” Spoiler alisema na bila kusita aliujaribu ule moto wa gesi hewani kisha aliupeleka kwenye maeneo nyeti ya Abbas, akaupulizia na kuanza kumuunguza. Abbas alitoa sauti kali ya maumivu.


“Sema ukweli ili nimwambie aache hili zoezi, sipendi tuumizane,” sauti ya Mr. Oduya ilisikika kutoka kwenye spika.


“Hamtopata chochote toka kwangu, wala msihangaike,” Abbas alisema kwa ukali huku akiendelea kugugumia kwa maumivu.


“Unaonekana shujaa, eh! Sijawahi kumuona mtu mpumbavu kama wewe, unadhani kwa hiki unachokifanya utaandikwa kwenye vitabu vya kumbukumbu za mashujaa wa nchi hii? Kwa taarifa yako, hata famlia yako hawawezi kukusifia kwa upuuzi huu!” sauti ya Mr. Oduya ilisikika ikiongea kwa hasira kutoka kwenye spika.


“Naona anatuchezea akili zetu, mpe kubwa kama hataki kutapika taarifa muhimu anazozifahamu,” Mr. Oduya alisema kwa hasira.


“Hawezi kuhimili na anaweza kupoteza maisha…” Spoiler alisema huku akiminya midomo yake.


“Nani anajali!” Mr. Oduya alijibu huku sauti yake ikionesha ghadhabu.


Sasa Mr. Oduya alimtaka Mafuru kwenda kusaidia, na bila kuchelewa Mafuru aliingia kwenye kile chumba. Kufumba na kufumbua Abbas alivuliwa nguo zake na kubaki mtupu kama alivyozaliwa kisha alibebwa na kutundikwa kwenye vile vyuma mfano wa vyuma vya kuning’inizia nyama buchani, kichwa chini miguu juu.


Dakika mbili baadaye Spoiler alikuwa ameshika visu viwili maalumu vilivyokuwa kwenye sinia juu ya meza, akavikamata na kuanza kuvinoa kwa kuvisugulisha vyenyewe kwa vyenyewe huku akitembea mbele ya Abbas.




“Hamtopata chochote toka kwangu, wala msihangaike,” Abbas alisema kwa ukali huku akiendelea kugugumia kwa maumivu.


“Unaonekana shujaa, eh! Sijawahi kumuona mtu mpumbavu kama wewe, unadhani kwa hiki unachokifanya utaandikwa kwenye vitabu vya kumbukumbu za mashujaa wa nchi hii? Kwa taarifa yako, hata famlia yako hawawezi kukusifia kwa upuuzi huu!” sauti ya Mr. Oduya ilisikika ikiongea kwa hasira kutoka kwenye spika.


“Naona anatuchezea akili zetu, mpe kubwa kama hataki kutapika taarifa muhimu anazozifahamu,” Mr. Oduya alisema kwa hasira.


“Hawezi kuhimili na anaweza kupoteza maisha…” Spoiler alisema huku akiminya midomo yake.


“Nani anajali!” Mr. Oduya alijibu huku sauti yake ikionesha ghadhabu.


Sasa Mr. Oduya alimtaka Mafuru kwenda kusaidia, na bila kuchelewa Mafuru aliingia kwenye kile chumba. Kufumba na kufumbua Abbas alivuliwa nguo zake na kubaki mtupu kama alivyozaliwa kisha alibebwa na kutundikwa kwenye vile vyuma mfano wa vyuma vya kuning’inizia nyama buchani, kichwa chini miguu juu.


Dakika mbili baadaye Spoiler alikuwa ameshika visu viwili maalumu vilivyokuwa kwenye sinia juu ya meza, akavikamata na kuanza kuvinoa kwa kuvisugulisha vyenyewe kwa vyenyewe huku akitembea mbele ya Abbas.


Sasa endelea...


Saa sita na robo mchana, bado kulikuwa na mvua, lakini ilikuwa imepungua na kuwa ya manyunyu mepesi, Sammy alikuwa bado kasimama pembezoni mwa korido za lile jengo lenye maduka ya mavazi na vipodozi katika eneo la Kinondoni Studio.


Baada ya mvua kunyesha kwa takriban saa moja na ushee hatimaye ilianuka na kuliachia jua lenye kupunga la mchana likijitokeza kwenye mawingu na kuifanya miale yake mikali kuleta uhai mpya.


Kukatika kwa mvua kulimfanya Sammy aanze kujivuta taratibu kusogea kwenye kituo cha daladala cha Kinondoni Studio ili apate usafiri wa kumpeleka Tabata Chang’ombe.


Kama yalivyokuwa maeneo mengi ya vituo vya daladala yenye pilika pilika, kituo cha Kinondoni Studio kilitawaliwa na pilika pilika za hapa na pale za kibinadamu. Kulikuwa na wachuuzi wa maji na ice cream, wauzaji wa korosho na bila kusahau wapiga debe waliokuwa wakishindana kuita abiria.


Kwa muda ule wa mchana wa saa sita na ushee hakukuwa na shida yoyote ya usafiri, magari mengi yalikuwa na abiria wachache. Sammy hakusubiri kwa muda mrefu mara akaliona basi moja aina ya Toyota Coaster lililofanya safari zake kati ya Tabata Chang’ombe na Makumbusho, likiwa na abiria waliokaribia kujaza siti huku zikibakia siti chache zilizokuwa wazi.


Sammy alijivuta taratibu na kuingia ndani ya lile basi akiwa na abiria wengine watatu, akaiendea siti ya nyuma kabisa ya dirishani upande wa dereva na kuketi. Kelele za wapiga debe na wachuuzi wa biashara ndogo ndogo ziliendelea kusikika katika eneo lile.


Dakika chache baadaye lile daladala likaanza safari ya kuelekea Tabata Chang’ombe. Muda wote Sammy alikuwa ameketi kwa utulivu akiangalia nje na sura yake ilionesha huzuni kubwa kwa kuwa hakujua hatima yake baada ya kile kilichotokea.


Alionekana kuzidiwa mno na mawazo yaliyomjia kichwani kwake, hasa tukio la kukutana na Mr. Oduya nje ya fensi ya hoteli ya Udzungwa Beach Resort, na lile tukio la kuzuka kwa mtafaruku kati yake na yule muhuni aliyetumwa na Mr. Oduya lilikuwa bado mawazoni mwake na lilimshtua mno kuliko hata tukio la kupewa barua ya kusimamishwa kazi.


Alihisi donge la uchungu likimkaba kooni, alimeza mate kwa nguvu mithili ya mtu aliyejaribu kumeza pande la nyama mbichi lililokuwa limemkwama kooni, kuna wakati alishindwa kuuzuia uchungu na kujikuta akitokwa na machozi.


Alipojishtukia aliyafuta machozi haraka na kugeuza shingo yake kuwatazama abiria wengine waliokuwamo humo garini kabla hajayaondosha macho yake haraka na kuangalia nje akihisi macho ya wale abiria yalimtazama muda wote.


Alichukua leso toka mfukoni na kujifuta vizuri uso wake kisha akairudisha ile leso mfukoni, aliendelea kutafakari kwa kina. Alijiuliza ikiwa angeendelea na mpango wake wa kukata rufaa kutokana na kusimamishwa kazi kwa kitendo alichodhani ni cha uonevu au aachane na suala hilo na kutafuta kazi sehemu nyingine!


Hata hivyo, alipomkumbuka Mr. Oduya na timu yake alihisi mwili wake ukisisimka kwa woga, kwani aliamini wasingeacha kumfuatilia baada ya kugundua kuwa alikuwa amesikia mengi ya siri yaliyohusu mipango yao.


Sasa mawazo mengi mchanganyiko yalizidi kutawala kichwa chake na kumfanya ahisi kuchanganyikiwa, kichwa chake kilianza kuwa kizito na alianza kunyemelewa na usingizi.


Mara alijikuta akiwa katika pori lililokuwa na miti mingi mikubwa na nyasi fupi fupi, hali ya hewa ilikuwa haioneshi kama ilikuwa mchana au usiku. Sammy alikuwa anakimbia huku akitweta, hakujua kwa nini alikuwa anakimbia.


Aliamua kugeuka kutazama nyuma na hapo akamuona askari wa kampuni ya ulinzi ya Spark K7, Fred akimkimbilia na mkononi alikuwa ameshika bunduki. Sammy aliogopa sana na kujaribu kuongeza mwendo lakini pumzi zilianza kumuishia.


“Bosi simama, mimi sina nia mbaya na wewe!” Fred alisema huku akihema kwa nguvu.


Sammy hakusimama, alijitahidi kuongeza mwendo lakini kila alivyokuwa akikimbia, miguu yake ilimjulisha kwamba ilikuwa imeishiwa damu na hivyo ilikaribia ganzi. Hakutaka kukata tamaa, alijikaza na kuiburuza wakati ikizidi kunyong’onyea.


Alipogeuka tena kutazama nyuma alihisi miguu yake ikikubali na kumpa hatua, akaamua kuongeza mwendo lakini alishtukia mguu wake wa kushoto ukitumbukia kwenye shimo dogo lililokuwa mbele yake na kumfanya apepesuke kabla hajaanguka kama mzigo.


Fred alimfikia huku akitweta, akamshika bega la kushoto na kuanza kumtikisa taratibu. “Bosi, vipi!”


Sammy alinyanyua uso wake kumtazama Fred kwa mshangao kwani sauti aliyoisikia haikuwa ya Fred bali ilikuwa kavu ya mwanamume mwingine, ilisikika vyema masikioni kwake kisha ikifuatiwa na milio ya sarafu.


Kama ilivyokuwa ada ya makondakta wengi wanavyochezesha fedha za sarafu mikononi kwa mtindo wa kipekee, mlio wa sarafu ulimgutusha Sammy kutoka katika usingizi ambao hakujua ulimpitia muda gani.


Sammy aliinua uso wake kumtazama yule kondakta aliyekuwa akichezesha sarafu huku akimtikisa bega lake taratibu, na hapo akagundua kuwa ilikuwa ndoto aliyoota baada ya kupitiwa na usingizi. Alitazama nje na kugundua kuwa walikuwa kwenye foleni ya kuvuka taa za kuongozea magari barabarani za Buguruni Shell.


Kondakta aliendelea kuchezesha zile sarafu mbele ya Sammy kumkumbusha alipe nauli, na haraka Sammy aliingiza mkono wake mfukoni na kutoa pochi yake, kisha alitoa noti ya shilingi 10,000 na kumpa yule kondakta.


Wakati yule kondakta akirudisha chenji ya Sammy lile daladala lilikuwa linavuka zile taa za kuongozea magari barabarani za Buguruni na kushika uelekeo wa barabara ya Mnyamani iliyokuwa ikipitia Vingunguti.


Barabara ile ilikuwa na watembea kwa miguu wengi waliopita kando ya barabara nyembamba ya Mnyamani, lakini ikiwa na magari machache muda ule wa mchana, yaliyotoka au kwenda katikati ya mji, na mengi yalikuwa ni daladala. Sammy alishusha pumzi za ndani kwa ndani huku mwili wake ukitetemeka kwa njaa.


Alifumba macho yake na kujiegemeza kwenye siti huku akipiga miayo ya uchovu na njaa. Hakika siku ile ilikuwa ndefu sana kwake, hakujua hatima yake baada ya kile kilichotokea kazini kwake. Aliitupia jicho saa yake ya mkononi na kushtuka baada ya kuona kuwa ilikuwa imeshatimu saa saba na robo.




Baada ya dakika kadhaa hatimaye walilivuka daraja la Mto Msimbazi uliokuwa ukiyatenganisha maeneo ya Vingunguti na Tabata, na mara mvua ya manyunyu mepesi ilianza tena kunyesha. Muda wote Sammy alikuwa mwingi wa mawazo na macho yake yaliangalia nje. Alikuja kushtuka baada ya kumsikia kondakta akitangaza kuwa wamefika katika kituo cha daladala cha Barakuda.


Daladala lilisimama na abiria wachache wakaanza kushuka. Sammy aliamua kushukia hapo kisha akajiweka sawa na kuruka mtaro uliokuwa kando ya ile barabara, ilikuwa imekwishatimu saa 8:00 za mchana.


Sammy aliamua kuelekea kwenye pub maarufu ya Barakuda ili kupata chakula na ikibidi apunguze uchovu na mawazo huku akitafakari jinsi ya kumweleza mkewe kilichompata kazini kwake.


* * * * *


Ilikuwa imetimu saa 5:30 usiku, Spoiler aliwaongoza vijana wawili, Uledi Mkama na Dulla Mcomoro, vijana shupavu waliokuwa wafanyakazi wa siri wa Mr. Oduya waliotumwa kutekeleza mipango yake haramu, kuingia katika chumba cha mateso, maarufu kama Hell.


Uledi Mkama mwenye umri wa miaka therathini, alikuwa mfupi na alivaa fulana nyeusi iliyombana na kulionesha vyema umbo lake lililojengeka kwa misuli na suruali ya jeans ya rangi ya bluu. Miguuni alivaa buti ngumu aina ya ‘safari boot’ za rangi ya hudhurungi.


Dulla Mcomoro alikuwa mrefu na mweupe mwenye asili ya nchini Comoro, alikuwa na umbo kakamavu kama wachezaji wa mpira wa kikapu wa Marekani. Alikuwa amevalia shati la bluu la mikono mirefu, suruali nyeusi ya jeans na raba nyeusi. Alikuwa na macho makubwa na mekundu yenye uchovu lakini yaliyokuwa na kila dalili ya kuonya.


Walipoingia katika chumba cha mateso waliukuta mwili wa Abbas ukiwa umelala sakafuni ukionekana umechakazwa vibaya na damu zilikuwa zimeenea chumba kizima. Kwanza waliduwaa, hawakuelewa! Ilikuwa kama wanaota ndoto ya ajabu ajabu inayotisha kuliko vitisho vyote.


Walitanabahi kuwa hawakuwa ndotoni, bali walikuwa wanatazama sinema ya kuogofya kupita kiasi. Pamoja na kuwa wamekwisha shiriki katika matukio mengi ya kihalifu lakini kwa mara ya kwanza walihisi kushikwa na kichefuchefu. Hawakuhitaji kutapika badala yake walijikuta wakitokwa na sauti ya mshangao wa ghafla.


Walikuwa wazoefu wa masuala ya utesaji na hata mauaji na walitegemea kuwa hawangeweza kushtuka sana kwa kukabiliana na maiti, lakini hiyo ilikuwa picha ya kutisha, picha isiyoelezeka wala kutazamika kwa jinsi mwili wa Abbas ulivyoonesha kuwa alikuwa amekufa kinyama.


Walimtupia jicho Spoiler huku wakihisi kuwa hakuwa binadamu wa kawaida isipokuwa mnyama. Vinginevyo, angewezaje kumuua yule mtu namna ile! Spoiler aliachia tabasamu, ni kama vile aliyasoma mawazo yao.


“Msijali… huyu bwana alistahili kabisa kufa,” Spoiler aliwaambia huku akibetua kichwa chake baada ya kuwaona bado wamezubaa kisha aliongeza, “Fanyeni kazi yenu haraka, hatuna muda wa kupoteza.”


Waliuchukua ule mwili wa Abbas, wakautoa pale na kuuingiza katika kiroba kikubwa, eneo lile lilisafishwa vizuri kwa maji yenye dawa maalumu, kisha walipulizia dawa maalumu iliyoondoa harufu ya damu na kuliacha eneo safi.


Walipomaliza waliondoka wakakichukua kile kiroba chenye mwili wa Abbas hadi katika buti la gari, wakaondoka zao na kwenda kukizamisha kile kiroba baharini kwenye kina kirefu cha maji.


Habari ya Abbas Dalali, mwandishi mahiri wa habari za uchunguzi wa gazeti la MamboLeo ikaishia hapo...


* * * * *


Zilikuwa zimebakia dakika chache tu kutimia saa 6:00 usiku, katika ukumbi wa wazi kwenye pub ya Barakuda wateja walikuwa wachache wakiwa wameketi kwenye meza za duara na pana za plastiki zilizokuwa zimezungukwa na viti vinne vinne na zikiwa chini ya miavuli mizuri na mikubwa ya kujikinga na mvua au miale ya jua.


Kulikuwa na wahudumu wa kike warembo waliokuwa wakiwahudumia wateja wale waliokuwa wameketi kwa utulivu kwenye zile meza huku wakijipatia vinywaji, na eneo lote lilipendezeshwa na taa nzuri za rangi mbalimbali zenye mwanga hafifu.


Kulikuwa na runinga mbili pana zilizokuwa zimetundikwa ukutani pale ukumbini na zilikuwa zimejikita katika kurusha matangazo ya mpira wa miguu wa Ligi Kuu ya Uingereza.


Hata hivyo, sauti ya muziki laini wa kubembeleza unaoweza kuacha kumbukumbu ya muda mrefu kwa mtu yeyote baada ya kuondoka eneo lile ilikuwa ikisikika kutoka katika spika zilizokuwa zimetundikwa maeneo fulani kwenye kona za ukumbi ule na hivyo kuzikonga vizuri nyoyo za wateja waliokuwa pale.


Sammy alikuwa bado yupo pale kwenye pub ya Barakuda na alikuwa ameketi kwenye meza moja ya pembeni kabisa, karibu na kibanda cha kutolea pesa kwa njia ya simu, akiwa peke yake. Alikuwa ameinamisha kichwa chake na kukilaza juu ya mikono yake aliyoikunja na kuiegemeza juu ya meza. Ni wazi alikuwa amelewa chakari.


Kuna muda alionekana kushtuka na kuinua kichwa chake, akafinya macho yake kwa ulevi na kuangaza huku na kule huku akiyumbayumba kiasi. Mkoba wake mdogo wa kiofisi ulikuwa chini katikati ya miguu yake.


Jasho lilikuwa linamtoka kwenye paji la uso na tai shingoni ilikuwa imelegezwa na kuachwa ikining’inia. Juu ya meza yake kulikuwa na chupa kubwa ya pombe ghali aina ya Grant’s Blended Scotch Whisky, bilauri moja na chupa ndogo ya soda aina ya Club Soda.


Hadi muda ule Sammy alikuwa ameshakunywa aina tofauti za pombe, kwanza kabisa aliagiza Savanna akaigida kama maji na kutaka aletewe nyingine, hiyo nayo aliigonga fasta ikaisha. Kisha aliagiza Heineken na kunywa yote lakini bado alikuwa na stress, hivyo akaagiza konyagi ndogo.


Alipomaliza tayari alikuwa ameanza kuchangamka, akaagiza chupa kubwa ya Grant’s na chupa ndogo ya soda aina ya Club Soda, sasa alianza kunywa taratibu.


Sammy aliitazama ile chupa kubwa ya Grant’s, akasonya na kuinyanyua bilauri iliyokuwa na pombe nusu na kuinywa pombe yote kwa mkupuo mmoja huku akisisimkwa mwili, kisha aliikita ile bilauri juu ya meza na kuinyanyua ile chupa ya Grant’s, alitaka kumimina pombe nyingine kwenye bilauri lakini hakuna kilichotoka. Chupa ilikuwa tupu!


Sammy alisonya tena na kumwita mhudumu, msichana mrefu na mweusi mwenye haiba nzuri ya kuvutia aliyekuwa akipita jirani na meza yake. Yule mhudumu alikuwa na nywele nyeusi ndefu na laini alizokuwa amezifunika kwa kofia ya kapelo.


Alikuwa amevaa sare ya baa, fulana nyeupe iliyokuwa imeyaficha vyema matiti yake makubwa na suruali nyeusi ya jeans. Yule mhudumu alikuwa amebeba kitenga kidogo cha kubebea vinywaji kwa ajili ya kupeleka kwa wateja na ndani yake kulikuwa na chupa mbili za bia zilizokuwa tupu.


“Enhe, unasemaje kaka yangu?” yule mhudumu alimuuliza Sammy huku akimwangalia kwa makini.


“Ongeza chupa nyingine kama hii,” Sammy alisema huku akiyumbayumba.


Yule mhudumu alimtazama Sammy kwa kitambo fulani na kutingisha kichwa chake kukataa. “Umeshalewa sana, isitoshe ni saa sita usiku, muda wa kufunga baa,” alisema.





Yule mhudumu alimtazama Sammy kwa kitambo fulani na kutingisha kichwa chake kukataa. “Umeshalewa sana, isitoshe ni saa sita usiku, muda wa kufunga baa,” alisema.


“Noo… nimesema leta chupa kubwa ya Grant’s Blended Scotch Whisky, mimi siyo mwanafunzi… sina shida na hapa nimejileta mwenyewe,” Sammy alisema huku akimkazia macho yule mhudumu.


Macho yake yalikuwa yamewiva na kuwa mekundu kwa sababu ya ulevi, alitema mate huku akiiangalia ile chupa kubwa ya Grant’s iliyokuwa juu ya meza.


“Kwanza hii chupa ni ndogo, mimi niliagiza chupa kubwa, au unadhani mimi kipofu, siyo?” Sammy alifoka huku akiinua ile chupa kubwa ya Grant’s na kumuonesha yule mhudumu.


Yule mhudumu alimtazama Sammy kwa mshangao mkubwa kana kwamba alikuwa ameona kitu cha kushangaza sana, akatingisha kichwa chake huku akiachia mguno.


“This is small bottle, iko wapi chupa yangu kubwa?” Sammy alifoka kwa hasira huku akiinua ile chupa na kuanza kutikisa tikisa huku akiipunga hewani.


“Hii ndiyo chupa kubwa. We kaka nilikuona mstaarabu kumbe ni mkorofi kiasi hiki!” yule mhudumu alisema kwa mshangao huku akionekana kukerwa sana.


Sammy aliinyanyua tena ile chupa ya pombe na kuipunga hewani, safari hii aliinua uso wake kuitazama kwa dharau sana. “No. This is small bwana! Call the manager.”


“Meneja hayupo…” yule mhudumu alisema huku akigeuka kutaka kupiga hatua za kuondoka na hapo hapo Sammy akamkata kauli.


“I don’t care! Call the manager now! Wezi wakubwa nyie… niitie Meneja!” Sammy alifoka kilevi huku akiinuka.


Yule mhudumu aligeuza shingo yake, akamtazama Sammy kwa hasira kisha alianza kupiga hatua za kuondoka lakini Sammy aliwahi kuinuka, akamshika mkono na kuung’ang’ania kwa nguvu.


“We mwanamke, unadhani mimi nimelewa, eh? Sijalewa… mimi siyo mjinga,” Sammy alisema huku akiyumba yumba.


Yule mhudumu aliutoa mkono wake kwa nguvu kutoka kwenye mikono yenye nguvu ya Sammy huku akionekana kupandwa na hasira. Sammy aliyumba na kuanguka chini kisha aliachia tusi zito. Yule mhudumu alimwangalia Sammy kwa makini huku akiwa amekunja sura yake akionekana kutafuta ufumbuzi kisha alishusha pumzi na kuondoka haraka eneo lile.


Sammy aliinua uso wake kumtazama yule mhudumu aliyekuwa anaondoka eneo lile na kusonya kilevi. Alijitahidi kuamka taratibu pale chini alipokuwa ameanguka huku akipepesuka na kufanikiwa, kisha akajiweka sawa.


Alisonya na kuanza kuvuta hatua zake taratibu huku akipepesuka akionekana kutaka kuondoka eneo lile, kama aliyekumbuka jambo, aligeuka akaichukua ile chupa ya pombe na kuondoka huku akisahau ule mkoba wake wa kiofisi.


Mara alisimama na kuanza kujipekua pekua kwenye mifuko yake ya suruali akionekana kutafuta kitu, kisha akafikiria kwa kitambo cha sekunde chache na kurusha mikono yake hewani, akajiweka sawa huku akiyumba yumba.


“Msifikiri nitakaa kimya… lazima niende polisi… kwenye vyombo vya habari… nitawaambia watu woote kwamba ninyi ni wezi! Shenzy taipu!” Sammy alifoka kwa sauti kali ya kilevi na kuwafanya watu wachache waliokuwepo eneo lile kugeuka na kumtazama kwa mshangao.


Aliondoka taratibu na kuruka kizingiti cha uzio uliotenganisha lile eneo la baa na maeneo mengine huku akipepesuka, kisha akashika njia ya kuelekea kwenye barabara ya kuelekea Segerea.


Yule mhudumu alirudi eneo lile akiwa ameongozana na meneja wa ile baa, mwanamume mfupi na mnene mwenye tumbo kubwa na uso wa mtoto mdogo, lakini Sammy hakuwepo eneo lile ila mkoba wake wa kiofisi ulikuwepo! Walimtizama huku na huko lakini hakuwepo!


“Yule kule anaondoka!” mteja mmoja miongoni mwa wateja wachache waliokuwepo eneo lile muda huo alisema akiwaonesha kwa kidole kule alikokuwa Sammy. Walimuona Sammy akitembea kwa kuyumba yumba, akipita kwenye eneo lenye mwanga hafifu.


Wakati huo alikuwa anavuka barabara ya kuelekea Segerea huku akiyumba na kukoswa koswa kugongwa na gari dogo aina ya Toyota RAV4 lililokuwa linapita kwa mwendo wa kasi.


“Afadhali kaondoka, asije akatuletea matatizo,” alisema yule meneja wa baa na kuongeza, “Fungua mkoba wake tuone kuna nini ndani kisha utauhifadhi vizuri kule stoo, najua kesho pombe zikimuisha kichwani ataufuata.”


Yule mhudumu aliufungua ule mkoba wakatazama ndani na kuiona kompyuta mpakato (laptop) aina ya MacBook Pro na nyaraka kadhaa za kiofisi, wakaufunga na kuuchukua kisha waliondoka nao kuelekea ndani ya ile baa.


Sammy aliendelea na safari yake, alipita chini ya miti kisha akakatiza katikati ya kiwanja cha mpira chenye mchanga huku akipepesuka, miguu yake ilionekana kuwa mizito kiasi wakati alipokuwa akipiga hatua na alionekana kana kwamba alikuwa anashindwa hata kuinyanyua sawasawa wakati akitembea. Mkononi alikuwa bado ameshika ile chupa tupu ya pombe.


Mvua iliyokuwa imenyesha mchana wa siku ile ilikuwa imesababisha maji kutuama na kusababisha madimbwi ya maji. Sammy aliteleza na kuanguka mara mbili kisha alijinyanyua akaendelea kutembea huku akipepesuka mithili ya mtoto mdogo aliyekuwa anajifundisha kutembea.


Aliingia kwenye dimbwi kubwa la maji yaliyotuama na kuanguka kwa mara ya tatu, akajaribu kukusanya nguvu zake ili ainuke lakini hakuweza. Alianza kutambaa kwa mikono kama mtoto, akijitoa ndani ya lile dimbwi la maji, lakini kila alipojaribu kujiinua alishindwa.


Alilazimisha kuinuka kwa nguvu na kufanikiwa kusimama wima lakini alishindwa kuhimili myumbo wa mwili wake na kuangukia kando kidogo ya lile dimbwi la maji, akalala chali huku nusu ya kiwiliwili chake kuanzia eneo la kiuno kuelekea miguuni likiwa ndani ya lile dimbwi la maji.


Nguo zake zilikuwa zimelowa chepechepe na muda huo alikuwa anahema kwa nguvu akionekana kukosa kabisa nguvu, alitulia kidogo na kusikilizia akiwa bado ameshikilia ile chupa tupu ya pombe.


Muda ule ule simu yake ya mkononi iliyokuwa imedondoka kando kidogo ya lile dimbwi la maji, kwenye eneo kavu kiasi lenye nyasi ilianza kuita.


Ilikuwa ni simu kutoka kwa mkewe Joyce, na Sammy alikuwa amemhifadhi kwenye kumbukumbu ya majina ndani ya simu yake kama “Wife”. Sammy alianza kutawanya mikono yake huku na huko kupapasa akiitafuta ile simu.


Simu iliita hadi ikakatika, Sammy akakusanya tena nguvu zake zote na kufanikiwa kuinuka, alisimama huku akionekana kuanza kupata nguvu kutokana na kuoga yale maji baridi ya mvua yaliyotuama kwenye dimbwi. Hata hivyo alikuwa hatamaniki kwa jinsi alivyolowa chapachapa.


Muda ule ule walionekana vijana wawili wakora walioelekea kule alikokuwa, mmoja alikuwa ameshika panga na mwingine alikuwa na nondo mkononi.


Sammy aliwaona wakati wakimsogelea na kupatwa na hofu, hata hivyo hakuondoka eneo lile bali alisimama huku akipepesuka tayari kwa kukabiliana nao, wale vijana wakora walimfikia na kumzingira, mmoja mbele yake na mwingine nyuma.


Mambo yanazidi kunoga, tukutane hapahapa kwa ajili ya muendelezo wa kisa hiki cha kusisimua





Nguo zake zilikuwa zimelowa chepechepe na muda huo alikuwa anahema kwa nguvu akionekana kukosa kabisa nguvu, alitulia kidogo na kusikilizia akiwa bado ameshikilia ile chupa tupu ya pombe.


Muda ule ule simu yake ya mkononi iliyokuwa imedondoka kando kidogo ya lile dimbwi la maji, kwenye eneo kavu kiasi lenye nyasi ilianza kuita.


Ilikuwa ni simu kutoka kwa mkewe Joyce, na Sammy alikuwa amemhifadhi kwenye kumbukumbu ya majina ndani ya simu yake kama “Wife”. Sammy alianza kutawanya mikono yake huku na huko kupapasa akiitafuta ile simu.


Simu iliita hadi ikakatika, Sammy akakusanya tena nguvu zake zote na kufanikiwa kuinuka, alisimama huku akionekana kuanza kupata nguvu kutokana na kuoga yale maji baridi ya mvua yaliyotuama kwenye dimbwi. Hata hivyo alikuwa hatamaniki kwa jinsi alivyolowa chapachapa.


Muda ule ule walionekana vijana wawili wakora walioelekea kule alikokuwa, mmoja alikuwa ameshika panga na mwingine alikuwa na nondo mkononi.


Sammy aliwaona wakati wakimsogelea na kupatwa na hofu, hata hivyo hakuondoka eneo lile bali alisimama huku akipepesuka tayari kwa kukabiliana nao, wale vijana wakora walimfikia na kumzingira, mmoja mbele yake na mwingine nyuma.


Sasa endelea...


Yule aliyeshika panga alimtazama Sammy kwa makini kisha alinyanyua lile panga lake kutaka kumpiga na ubapa mgongoni lakini kabla hajapata fursa hiyo Sammy aliwahi kulikwepa kirahisi na kusababisha lile panga likate upepo.


Pigo hilo lilikuwa kama la kumzindua tu kwani wakati huo huo alifyatuliwa miguu kwa namna ambayo hakuitegemea na kujikuta akiviringika chini kwenye maji machafu. Mara tu alipotaka kuinuka alifyatuliwa tena, na hapo kengere ya hatari ikalia kichwani kwake.


Sammy hakutaka kujilegeza, akiwa amekwisha jiandaa alianguka hali huku akiachia teke lililompata mmoja wao tumboni na kumfanya apepesuke. Kisha alianza kuwarushia ngumi na mateke huku akikwepa lile panga na nondo vilivyomkosakosa kichwani.


Lakini kutokana na pombe alizokuwa amekunywa alikuwa anayumba na hatimaye alianguka chini, alipotaka kuinuka mkora mmoja alimuwahi kwa teke kali la kwenye mbavu na kumfanya aachie yowe hafifu la maumivu huku akijikunja pale chini.


Wale wakora walizidi kumshambulia Sammy kwa vipigo ili kumlegeza, yeye alijitetea huku akipangua mateke, ngumi, ubapa wa lile panga na nondo. Wakati akiendelea kupangua alifanikiwa kusimama lakini ghafla alipigwa pigo moja bila kutegemea lililompata barabara usoni na kumpa kisulisuli, akadondoka huku akitoa yowe kali, nguvu zikaanza kumuishia.


Muda ule ule zikasikika sauti za watu waliokuwa wanakimbilia eneo lile ili kutoa msaada. Wale wakora walimsachi haraka haraka na kuchukua pochi yake, wakachukua fedha na kuitupa kando, mmoja alimvua viatu vyake kisha wakakimbia kutoka eneo lile wakimwacha anatokwa na damu sehemu mbalimbali za mwili wake.


* * * * *


Palishakucha muda mrefu na ilishatimu saa nne za asubuhi. Sammy alikuwa bado chakari akiwa amelala fofofo na asubuhi ile kwake ilikuwa bado liamba. Alikuwa amelala kifudifudi akiwa ana uchovu mkubwa uliotokana na pombe mchanganyiko za usiku uliotangulia, ‘hangover’.


Chumba chake kilikuwa kikubwa chenye maliwato ya ndani kwa ndani (master bedroom) na hakikuwa na vitu vingi sana isipokuwa kitanda kikubwa cha samadari cha futi sita kwa sita, cha mbao ngumu za mkongo, chenye droo mbili kila upande zilizokuwa na taa za rangi ya bluu.


Pia kulikuwa na kabati kubwa la nguo la ukutani na meza nzuri ya vipodozi maarufu kama ‘dressing table’ iliyokuwa na kioo kirefu cha kujitazama mwili mzima.


Sakafuni kulikuwa na zulia pana la bluu lililokuwa na maua ya rangi nyekundu na manjano. Chumba kilikuwa na madirisha mawili mapana yaliyokuwa yamefunikwa kwa mapazia marefu yenye nakshi za michoro ya maua yaliyodariziwa vizuri.


Sammy akiwa bado yupo chakari akiuchapa usingizi, kichwa chake kilikuwa kizito mithili ya mtu aliyekuwa ametwishwa kiroba cha mchanga.


Ghafla, watoto walioanza kupiga kelele nje ya nyumba walimtoa katika usingizi na kumkera, tena walimkera hasa! Sammy aliinua shingo yake, akakigeuzia kichwa chake upande mwingine huku akiziba masikio na kuendelea kulala, hata hivyo zile kelele zilizidi kumkera masikioni. Akasonya kwa hasira.


Alijaribu kuinua kichwa chake lakini aliuhisi ule uzito wa kichwa na alikuwa bado ana mawenge ya usingizi, ukichanganya na uvivu uliomjaa, vilimpa hali ya kutaka kuendelea kuuchapa usingizi, licha ya jua la asubuhi kuhanikiza nuru ya kutosha mle chumbani mwake.


Miale ya jua la saa nne asubuhi ilikuwa imepenya dirishani na kutuama ikienea hadi pale kitandani alipokuwa amelala tangu kulipopambazuka. Joto la miale ile ya jua lilikuwa limeamsha homa hafifu mwilini mwake, homa iliyotokana na pombe mchanganyiko alizokunywa usiku ulioitangulia siku ile.


Sammy alikuwa mnywaji wa kawaida wa bia mbili au tatu tu basi na hakuzoea kunywa pombe kali, hivyo aliutaka utulivu kwa gharama yoyote ile, japo aweze kumalizia n’gwe ile ya usingizi, hakujua uchovu ule ungekwisha saa ngapi. Alichojua yeye ni kulala tu hadi pale mwili wake ungemruhusu kufarakana na kitanda. Watoto walizidi kumkera kwa kelele zao.


Walikuwa watoto wa pale mtaani, eneo la Tabata Chang’ombe, waliokuwa wanacheza asubuhi ile baada ya kushiba chai ya asubuhi. Hawakuwa na kingine cha kufanya isipokuwa kucheza tu, kwani ilikuwa ni siku ya Jumamosi na hapakuwa na shule.


Hao watoto ndio waliomgutua Sammy toka usingizini, kwa kuwa walikuwa wanacheza karibu na dirisha la chumba chake. Japo nyumba yake ilikuwa imezungukwa na ukuta lakini umbali kutoka ule ukuta hadi pale dirishani kwake ulikuwa mdogo sana, isitoshe kulikuwa na uwanja mpana ulioruhusu watoto kucheza.


Kelele za watoto zilimfanya Sammy ajihisi kama mtu aliyekuwa anapigiwa zumari sikioni, alisonya huku akiminya sura yake kana kwamba alikuwa anahisi maumivu makali ya kichwa. Alikuwa amechefukwa kweli kweli!


Aliwavumilia kidogo wale watoto huku akiinua shingo yake na kuzisikiliza sauti zao kwa makini, akazitambua kwani mojawapo ilikuwa sauti ya mtoto wake wa miaka 8 aliyeitwa Pendo, na nyingine ilikuwa ya dada yake mdogo wa miaka 17 aliyeitwa Winifrida.


“Winnie! We Winnie!” Sammy aliita kwa sauti kali ya kukaripia.


“Abee!” Winifrida aliitikia kwa sauti ya juu huku akisogea zaidi pale dirishani.


“Naomba niondosheeni hizo kelele zenu hapo dirishani kwangu. Alaa!” Sammy alitoa amri yake kwa sauti ya kufoka kidogo huku akihisi kizunguzungu na mate kumjaa kinywani, alikunja ndita usoni.


Winifrida aliwaondosha wale watoto kutoka eneo lile, na muda ule ule Sammy alisikia mlango wa chumba chake ukifunguliwa, aligeuza haraka shingo yake kumtazama aliyekuwa akiingia mle chumbani, macho yake yalikutana na macho ya mkewe, Joyce Jengo.





Joyce, mwanadada wa Kidigo kutoka eneo la Pongwe nje kidogo ya jiji la Tanga, alikuwa mrefu mweupe na mwenye uzuri wa asili, akiwa na umri wa miaka 32 alikuwa amejaaliwa uzuri wa sura ya kitoto na umbo. Macho yake yalikuwa makubwa na legevu ya kike, pua yake ilikuwa ndefu kama ya kihabeshi na midomo yake ilikuwa laini yenye kingo pana kiasi.


Joyce alikuwa mbunifu wa mavazi aliyekuwa na ndoto za kuwa mbunifu wa kimataifa na mtayarishaji wa kipindi cha runinga kuhusu ubunifu wa mitindo ya mavazi ya Kiafrika. Alikuwa msomi wa Shahada ya Kwanza ya Ubunifu wa Mitindo (B.A. In Fashion Design) aliyoipata katika Chuo cha Mitindo cha Elizabeth Galloway cha Cape Town, nchini Afrika Kusini.


Asubuhi ile Joyce alikuwa amevalia gauni zuri la kitenge lililoshonwa na kudariziwa vizuri, likimfanya apendeze na kuvutia kwa muonekano wake wa Kiafrika zaidi. Joyce alisimama akamtazama Sammy kwa makini, macho yake yalionesha uchungu fulani.


Sammy hakusubiri tena, alijiinua kutoka pale kitandani na kuketi kitako huku akifinya uso wake, halafu taratibu alijitoa pale kitandani na kuchukua taulo kisha alielekea maliwato huku akipepesuka.


Akiwa na hakika kuwa macho ya Joyce yalikuwa nyuma yake yakimsindikiza, Sammy aliingia haraka maliwato na kuurudisha mlango. Alijimwagia maji na kupiga mswaki, dakika chache baadaye alirudi pale chumbani na kuanza kuchagua nguo kutoka kwenye lile kabati la nguo, akaanza kuvaa huku akionekana mwenye mawazo mengi.


Muda wote Joyce alikuwa akimtizama kwa makini huku akijitahidi kuwa mtulivu, uso wake ulionekana kumtilia maanani Sammy kwa kila alichokifanya. Sammy aliendelea kuvaa taratibu na baadaye alijitazama kwenye kioo kirefu cha meza ya vipodozi, akagundua kuwa alikuwa na jeraha kwenye jicho lake la kushoto.


“Hivi ni nini kilikupata jana ukaamua kulewa kiasi kile?” Joyce alimuuliza Sammy kwa sauti tulivu huku akimwangalia kwa makini.


Sammy alimtupia jicho Joyce na kuyahamisha haraka, akapeleka macho yake kuangalia juu darini, alijaribu kuvuta kumbukumbu ya kilichotokea usiku lakini hakuweza kukumbuka chochote.


“Haki-yanani, ya jana sijapata kabisa kuyaona tangu nikufahamu! Yaani unalewa hadi unaletwa kwenye mkokoteni ukiwa chapachapa! Hii ni kali ya mwaka!” Joyce alisema huku akiachia kicheko hafifu na kupiga kofi moja hafifu hewani.


“Halafu ulisahau kabisa kama jana ilikuwa ni siku yako ya kuzaliwa, tumesubiri jioni tukufanyie ‘surprise’ badala yake wewe ndiyo ukageuka kutusapraizi,” Joyce alisema huku akitingisha kichwa kwa huzuni.


Sammy alitamani kucheka lakini akajizuia, alimsogelea Joyce kisha akapeleka mkono wake wa kulia kwenye uso wa Joyce kumpapasa huku akiachia tabasamu, si kwa kulazimisha.


“Don’t touch me… ninapokuwa naongea vitu siriazi sipendi kufanywa katuni… au labda naongea upuuzi!” Joyce alisema huku akiusukuma mkono wa Sammy.


Sammy alishusha pumzi, akashika kiuno chake kwa mikono yake yote miwili huku akimtazama Joyce kwa makini. Alitaka kusema neno lakini akasita na kuinamisha kichwa chake, alifikiria kidogo akionekana kutaka kumwambia ukweli kuhusu matatizo ya kazini kwake, lakini hakujua aanzie wapi.


“Haya, endelea tu kuniona mpuuzi, siku moja utaujua umuhimu wangu,” Joyce alilalama na kumfanya Sammy atingishe kichwa chake kwa huzuni huku akibabaika kidogo.


“Siyo hivyo, unajua… nime… nime-e…” Sammy alitaka kusema lakini akasita baada ya kumuona Joyce akianza kupiga hatua taratibu kuondoka huku akirusha mkono wake hewani kama ishara ya kutotaka kumsikiliza.


Joyce alifungua mlango na kutoka akiurudishia mlango nyuma yake. Sammy alipigwa butwaa asijue la kufanya, alibetua mabega yake juu akionesha kutokuwa na namna nyingine ya kufanya…


Nyumba yao ilikuwa kubwa yenye vyumba vitatu vya kulala na ilizungukwa na ukuta uliojengwa kwa matofali. Ilikuwa na sebule pana yenye seti moja ya makochi ya sofa yaliyopangiliwa vizuri upande wa kulia wa sebule hiyo.


Makochi hayo yalikuwa yanatazamana na seti moja ya runinga pana ya ukutani aina ya Sony Bravia iliyounganishwa na decorder ya DStv yenye chaneli nyingi za kimataifa.


Kwenye kona kulikuwa na meza fupi ya mapambo na katikati ya sebule kulikuwa na meza nzuri ya kioo yenye umbo la yai na stuli ndogo nne zilizopangwa kuizunguka meza hiyo.


Ukutani kulikuwa na saa kubwa na picha tatu kubwa, picha moja iliwaonesha Sammy na mkewe Joyce katika pozi la harusi, picha ya pili ilikuwa ya familia nzima na picha ya tatu ilikuwa ya Joyce akitunukiwa shahada ya ubunifu wa mavazi katika Chuo cha Mitindo cha Elizabeth Galloway.


Upande wa kushoto wa sebule kulikuwa na ukumbi mdogo wa chakula wenye meza kubwa ya chakula iliyotengenezwa kwa mti wa mkongo na ilikuwa imezungukwa na viti sita vya mbao ya mkongo vyenye foronya laini, pia kulikuwa na jokofu kubwa aina ya BOSS.


Jirani na ule ukumbi wa chakula kulikuwa na korido pana iliyoelekea vyumbani na kulikuwa na milango mitano, milango miwili ikiwa upande wa kulia na milango mingine mitatu upande wa kushoto.


Mlango wa kwanza kulia ulikuwa wa kuingia jikoni na mlango wa pili ulikuwa wa chumba cha Sammy na mkewe Joyce. Milango iliyokuwa upande wa kushoto wa kwanza ulikuwa mlango wa kuingia kwenye maliwato ya wote, uliofuata uliingia kwenye chumba cha wageni na wa mwisho kabisa ulikuwa wa chumba cha kulala watoto.



Pale sebuleni Winifrida Kambona, binti wa miaka 17, aliyekuwa anasoma kidato cha nne katika Shule ya Sekondari ya Zanaki, alikuwa anakata keti vipande viwili vidogo na kuviweka kwenye sahani kisha akaviweka juu ya meza mbele ya Pendo.


Winifrida alikuwa na umbile dogo lakini lililovutia mno. Kwa mlingano wa macho tu, alitoa tafsiri ya kuwa na ule uzuri usiomithilika, hasa kutokana na rangi ya ngozi yake nyeupe mithili ya chotara wa kizungu iliyowafanya wanaume wakware, pasipo kujali umri wao, wasahau kama alikuwa yupo chini ya umri wa miaka kumi na nane, na zaidi alikuwa mwanafunzi.


Ki ukweli Winifrida alikuwa miongoni mwa wasichana walioitwa nusu malaika! Nywele zake zilikuwa zimekatwa kwa mtindo wa ‘Lowcut’ na alikuwa na kope ndefu zilizong’ara na kuyafanya macho yake yawe wazi nusu. Pua yake ilikuwa ndefu kiasi, nyoofu ya wastani ikiiacha midomo yake ijidai kwa kuhifadhi meno meupe yaliyojipanga vizuri huku yakiachia kimwanya kidogo.


Hata hivyo, Winifrida alikuwa mapepe na msumbufu sana kwa kaka yake. Alipoweka vile vipande viwili vya keki alimimina sharubati (juice) ya parachichi na kumpa Pendo kisha aliketi kwenye sofa na kutulia akiangalia kipindi cha wanyama kilichokuwa kikirushwa kwenye kituo cha runinga cha Safari Channel.


Pendo aliachia tabasamu na kujiweka vizuri kwenye kochi. Alikuwa mtoto mchangamfu sana na muongeaji ingawa alikuwa na tatizo la seli mundu (sickle cell) lililomfanya mara kwa mara kulazwa hospitali. Hata hivyo alipenda sana kudadisi mambo na mara kwa mara aliuliza maswali yaliyoonekana yenye utata.


“Anti Winnie, mbona wewe hunywi juisi na keki?” Pendo alimwuliza Winifrida huku akianza kula taratibu ile keki na sharubati. Winifrida aliachia tabasamu huku akijiangalia kwa madaha.


“Aku! Mimi sitaki kuwa bonge… najitunza ili niwe mwanamitindo maarufu duniani,” Winifrida alisema na kuinuka, kisha alianza kutembea kwa miondoko ya madaha aina ya ‘Cat walk’ kama watembeavyo wanamitindo na warembo wanapokuwa katika majukwaa ya urembo.


“Eti Wifi, hebu nicheki sifai kuwa mwanamitindo?” Winifrida alimwuliza Joyce wakati akitembea kwa madaha na kupita mbele yake.


Joyce alikuwa kwenye cherehani akishona nguo huku kipimo cha kupimia nguo kikiwa kimening’inia kwenye shingo yake na alikuwa akitazama jarida maarufu la mitindo ya mavazi. Kando yake kulikuwa na sanamu kubwa la mwanamke likiwa limesimamishwa na kuvishwa vazi la kitambaa cha bazee lililoshonwa na kudariziwa vizuri na kichwani lilikuwa limevishwa kilemba kikubwa.


Aliinua uso wake na kumtazama Winifrida kisha akaachia tabasamu pana. Pendo aliachia kicheko kikali lakini Winifrida hakuonekana kujali, aliendelea kutembea kwa maringo huku akimtazama Joyce kwa bashasha.


“Umeona, eh! Kila mtu lazima azimike na pozi zangu,” Winifrida alisema huku akipunga mkono wake mmoja hewani na kumfanya Joyce aangue kicheko hafifu.


“Wewe andaa tu mavazi yako halafu mimi nitakufanya kuwa mbunifu wa nguo maarufu sana, siyo Tanzania tu bali Afrika yote,” Winifrida alisema na kumfanya Joyce agune.


“Mbona mimi tayari ni maarufu,” Joyce alimwambia Winifrida. Pendo aliendelea kucheka na kumfanya Winifrida ageuke kumtazama Pendo.


“Wewe cheka tu, usishangae siku moja ukiniona kwenye runinga napishana jukwaani na kina Naomi Campbell,” Winifrida alisema huku akilivuta neno la mwisho kwa mikogo mingi, Joyce alikuwa bado amemtumbulia macho.


“Wewe ukionekana kwenye runinga mimi ndiyo n’takuwa meneja wako!” Pendo alisema kwa mbwembwe huku akipunga mkono wake hewani na kuwafanya wote waangue kicheko, hata hivyo kicheko chao kilisitishwa ghafla baada ya Sammy kuingia pale sebuleni akitokea chumbani.


Sammy alikuwa amevaa suruali ya kadeti ya rangi nyeusi, shati la rangi ya samawati na buti ngumu za ngozi miguuni. Usoni alivaa miwani mikubwa myeusi ya jua, japokuwa mle ndani hapakuwa na jua lakini miwani ile aliitumia kuficha jeraha lake kwenye jicho lake la kushoto


Sammy alisimama akawatazama wote kwa zamu akianza na Winifrida aliyekuwa amesimama akiwa kashika kiuno kisha macho yake yalihamia kwa Pendo, akashusha pumzi za ndani kwa ndani na kumtupia jicho la wizi Joyce.


Alisogea alipokuwa ameketi Pendo na kumtazama kwa tabasamu. Aliionja kidogo ile sharubati ya Pendo na kuirudisha ile bilauri juu ya meza na wakati huo Pendo alikuwa akimtazama kwa makini kwenye jicho lake, wakabaki wakitazamana. Pendo alitaka kuuliza swali lakini akaonekana kusita na kubinua midomo yake kitoto akionekana kuzuia kicheko.


Kitambo kifupi cha ukimya kikapita na kuifanya ile sebule ionekane kuwa eneo lenye ukimya sana. Watu wote walibaki kimya wakimtazama Sammy kwa makini.


“Shikamoo, baba!” Pendo alivunja ukimya kwa kumsalimia baba yake huku akikenua meno yake.


“Marhaba mwanangu, naona unajipendelea peke yako,” Sammy alisema huku akimpapasa kichwani.


“Hii ilikuwa keki yako ya bethdei lakini jana ulirudi usiku umelewa ukaanza kupiga mikelele,” Pendo alisema huku akimuonesha Sammy kipande cha keki.


Winifrida alionesha kutaka kucheka lakini akawa anajizuia kwa kufunika mdomo wake kwa kiganja cha mkono, hata hivyo, alishindwa kujizuia na kuachia kicheko hafifu cha chini chini. Joyce alimtazama Winifrida kwa makini.


“Shikamoo!” Winifrida alimsalimia Sammy huku akijikausha na kutazama kando.


“Marhaba, Winnie, mbona leo hujaenda shule?” Sammy aliuliza huku akigeuka kumtazama Winifrida na bila hata kusubiri jibu alianza kuondoka.


“Leo Jumamosi, hatuendi shule, ila baadaye n’taenda twisheni,” Winifrida alijibu.


“Okay!” Sammy alisema huku akianza kupiga hatua taratibu ili kuondoka.


“Sasa unaenda wapi hata chai hutaki kunywa?” Joyce alimuuliza Sammy alipomuona akipiga hatua zake kutoka nje.


“Mmh, saa hizi chai haipandi, ngoja nikapate mchemsho wa kuku kwa Elli,” Sammy alisema huku akifungua mlango na kutoka. Watu wote walimsindikiza kwa macho hadi alipotoka kabisa. Kisha Pendo alimgeukia mama yake.





“Kwani baba kafanya nini kwenye jicho, mbona ameficha macho na miwani?” Pendo aliuliza huku akimkazia macho mama yake.


“Si ungemuuliza mwenyewe alikuwepo hapa! Umemsubiri kaondoka ili uniulize mimi!” Joyce alisema huku akitabasamu.


“Nimeogopa!” Pendo alisema na kumfanya Joyce acheke.


“Makubwa! Leo wewe wa kumuogopa baba yako?” Joyce alisema kwa mshangao.


Kisha Winifrida na Pendo walianza kufanyiana mzaha. Kwa kweli ilionekana ni familia yenye furaha sana.


_____


Sammy alifika kwenye kituo cha daladala cha Tabata Chang’ombe na kusimama kwenye meza moja ya muuza magazeti, aliwakuta watu wakiwa wamezunguka wakipitia vichwa vya habari kwenye magazeti ya siku ile.


Kulikuwa na habari tofauti zilizopewa uzito katika magazeti yale, lakini habari iliyomshtua zaidi Sammy ilikuwa ni ile ya tukio la kutoweka kwa mwandishi mahiri wa habari za uchunguzi wa gazeti la MamboLeo, Abbas Dalali.


Habari ile iliandikwa na gazeti la MamboLeo ikimkariri mke wa Abbas, Bi Somoe Dalali akisema Abbas aliondoka nyumbani kwao Tabata Kinyerezi na watu ambao hawakutambulika katika gari jeupe aina ya Toyota Noah. Abbas alikuwa amemwambia mke wake kwamba anakwenda kuonana na mtu muhimu ili kupata taarifa fulani nyeti na tangu wakati huo hakurudi tena nyumbani na wala simu zake hazikupatikana.


Bi Somoe alikuwa na wasiwasi na usalama wa mumewe, hasa baada ya kuona harudi wala namba zake hazipatikani, hivyo alikwenda kutoa taarifa kituo cha polisi.


Pia gazeti lile liliandika kuhusu tamko la Kamati inayotetea waandishi wa habari, CPJ, ilipotoa wito kwa serikali ya Tanzania kufanya uchunguzi wa kuaminika ili ifahamike kilichokuwa kimemtokea mwandishi huyo mahiri wa habari za uchunguzi.


Sammy alinunua lile gazeti la MamboLeo kisha alipanda kwenye daladala la kuelekea Mnazi Mmoja lililofika pale likiwa na abiria wachache.


* * * * *


Mchana wa saa saba kasoro dakika tatu, Joyce alikuwa ameketi sebuleni kwenye sofa akionekana kuwaza mbali sana, alikuwa ameshika jarida la mitindo lakini macho yake muda wote yalikuwa yakiitazama kwa makini saa ya ukutani mpaka mishale ifike saa saba kamili.


Bila ya sababu, moyo wake ulikuwa unamdunda, hatimaye ilitimu saa saba kamili, kisha dakika moja ilipita, ikaja ya pili na baadaye ya tatu… Joyce hakujua alichokuwa anakisubiri muda ule. Je, alikuwa na miadi na mtu? Nani? Hakuwa na jibu.


Moyo wake ulimpasuka mara tu simu yake ilipoanza kuita kwa fujo, aliinyanyua na kuitazama kwa makini, ilikuwa namba ngeni asiyoifahamu, alishusha pumzi akaipokea na kuipeleka sikioni.


“Hallo!” Joyce alisema kwa sauti ya kutetemeka mara baada ya kupokea, kiasi kwamba alianza kujishangaa.


“Mrs. Joyce Kolimba…” Ilikuwa sauti tamu ya mwanamke kutoka upande wa pili wa ile simu, Joyce alipoisikia alishusha pumzi za ndani kwa ndani na kuminya midomo yake, alihisi kuifahamu sana ile sauti lakini hakujua ni ya nani.


“Ndiyo… n-nani mwenzangu?” aliuliza huku akiwa na wasiwasi kidogo.


“Madame Norah…” ilisema ile sauti kutoka upande wa pili wa ile simu na kumfanya Joyce ashtuke sana. Aliikodolea macho ile simu kwa mshangao kana kwamba lilikuwa bomu lililotaka kulipuka muda wowote.


Mmh… Madame Norah! Joyce hakuamini kabisa! Kwa nukta chache alihisi kama moyo wake ulisahahu mapigo yake, na mara yalipoanza tena alijikuta akivuta pumzi ndefu za ndani kwa ndani, kisha akazishusha taratibu.


Haiaminiki! Madame Norah kampigia simu! Kwani ni yeye Joyce aliyekuwa akihangaika usiku na mchana kutafuta mawasiliano ya Madam Norah bila mafanikio! Alikwishakwenda ofisini kwake zaidi ya mara tatu lakini ilikuwa vigumu kumpata kwani wapambe waliomzunguka hawakutaka kumpa nafasi Joyce… Hapana, haiaminiki! Joyce alidhani labda yupo ndotoni!


Madame Norah mwenye umri wa miaka 50, alikuwa mwanamke mjasiriamali mwenye mafanikio makubwa, alikuwa amejitosheleza kwa vitu vingi. Alimiliki kituo cha redio na cha televisheni, kampuni kubwa ya samani za majumbani na ofisini, mgahawa wa kisasa katikati ya jiji la Dar es Salaam na duka kubwa la vipodozi na nguo za kike.


Alikuwa mrefu na mweupe mwenye umbo kubwa kiasi lililosheheni vema na kunesanesa, likafanya kila jicho la mwanamume lililomuona kumtazama mara mbili mbili. Alikuwa mcheshi na mwenye ushawishi mkubwa asiyependa kuwa chini ya mwanamume, ndiyo maana hakutaka kuolewa.


Ingawa alikuwa na umri mkubwa, lakini ilikuwa vigumu mno kumtofautisha na wasichana wenye umri mdogo kutokana na urembo wake usiochujuka, hakuwa mwanamke wa kumtazama mara moja tu ukamwacha. Watu wengi walijiuliza kuwa endapo aliweza kuonekana mrembo kiasi kile katika umri huo, ilikuwaje enzi za usichana wake?


“Joyce, are you there?” sauti ya Madame Norah ilimgutusha Joyce aliyekuwa ameanza kutekwa na mawazo.


“Oh… Madame Norah! Samahani mama’angu, kwa kweli sikutegemea kabisa kupata simu yako…” Joyce alisema huku akibabaika kidogo.


Mambo yanazidi kunoga! Je, Sammy anaelekea wapi? Na huyu Madame Norah ni nani hasa na kwa nini amempigia simu Joyce? Endelea kuufuatilia mkasa huu wa kusisimu





Madame Norah mwenye umri wa miaka 50, alikuwa mwanamke mjasiriamali mwenye mafanikio makubwa, alikuwa amejitosheleza kwa vitu vingi. Alimiliki kituo cha redio na cha televisheni, kampuni kubwa ya samani za majumbani na ofisini, mgahawa wa kisasa katikati ya jiji la Dar es Salaam na duka kubwa la vipodozi na nguo za kike.


Alikuwa mrefu na mweupe mwenye umbo kubwa kiasi lililosheheni vema na kunesanesa, likafanya kila jicho la mwanamume lililomuona kumtazama mara mbili mbili. Alikuwa mcheshi na mwenye ushawishi mkubwa asiyependa kuwa chini ya mwanamume, ndiyo maana hakutaka kuolewa.


Ingawa alikuwa na umri mkubwa, lakini ilikuwa vigumu mno kumtofautisha na wasichana wenye umri mdogo kutokana na urembo wake usiochujuka, hakuwa mwanamke wa kumtazama mara moja tu ukamwacha. Watu wengi walijiuliza kuwa endapo aliweza kuonekana mrembo kiasi kile katika umri huo, ilikuwaje enzi za usichana wake?


“Joyce, are you there?” sauti ya Madame Norah ilimgutusha Joyce aliyekuwa ameanza kutekwa na mawazo.


“Oh… Madame Norah! Samahani mama’angu, kwa kweli sikutegemea kabisa kupata simu yako…” Joyce alisema huku akibabaika kidogo.


Sasa endelea...


“Ooh… usijali,” Madame Norah alijibu, na papo hapo akauliza, “Kesho Jumapili utakuwa na ratiba gani?”


“Kesho muda gani?” Joyce aliuliza kwa shauku kubwa.


“Jioni.”


“Nitakuwepo tu nyumbani, sina pa kwenda.”


“Naomba uje ofisini kwangu Mikocheni tuongee, japo maongezi yangu yanaweza yasiwe matamu kama ya mumeo! Au wasemaje?” Madame Norah alisema kwa madaha na kuachia kicheko hafifu.


“Sawa tu nitafika muda huo, sijui saa ngapi?” Joyce aliuliza huku akishusha pumzi za ndani kwa ndani.


“Saa kumi na mbili…” Madame Norah alisema na kuongeza, “See you at that time.”


“Okay, Madame!” Joyce alisema huku akipitisha ulimi wake kwenye mdomo wake ulioanza kukauka, na hapo simu ikakatwa. Joyce hakuamini, alibaki akiitazama simu yake huku uso wake ukiwa umepambwa na tabasamu bashasha. Alionekana kuwa na furaha isiyo kifani.


Kisha alijiegemeza kwenye sofa huku akiendelea kutabasamu, na kushusha pumzi za ndani kwa ndani. Muda huo kipindi cha “Madame Norah Show” kilichokuwa kinaendeshwa na Madam Norah mwenyewe kilikuwa kinarushwa kwenye runinga, Joyce alichukua rimoti ya runinga akaongeza sauti.


Muda wote tabasamu lake lilikataa kwenda likizo, alimwangalia Madame Norah kwenye runinga kwa makini sana na kuonekana kuvutiwa naye. Pendo alikuwa ameketi kwenye sofa jirani na mama yake akifuatilia kwa makini kila kilichokuwa kinaendelea pale sebuleni. Hakusema neno bali alikuwa anamwangalia mama yake kwa makini.


Winifrida aliingia pale sebuleni akitokea jikoni na kuketi juu ya mkono wa sofa huku akimwangalia Joyce kwa makini, kisha akaguna.


“Wifi, mbona umefurahi sana, inaonekana unampenda sana Madam Norah!” alisema Winifrida.


“Madame Norah ni mfano mzuri wa mwanamke mjasiriamali… natamani sana kufikia mafanikio kama yake,” alisema Joyce huku akishusha pumzi ndefu.


“Mama, kwani na wewe unataka kuwa kama Madam Norah?” Pendo alimwuliza mama yake huku akimkazia macho kwa makini.


“Ndiyo mwanangu, natamani sana na ninaamini Mungu atanisaidia.”


“Kwa hiyo na wewe utamwacha baba yangu?” Pendo alimwuliza tena Joyce na kumfanya amtazame kwa mshangao.


“Kwa nini nimwache baba yako? Kwani haya maneno huwa unayapata wapi we mtoto!” Joyce alimwuliza pendo huku akiendelea kumtazama kwa mshangao.


“Si wanasema Madam Norah hataki wanaume!” Pendo alisema kwa kujiamini na kuwafanya wote wamkodolee macho kwa mshangao. Winifrida aliziba mdomo wake kwa kiganja cha mkono.


“We mtoto wewe… ni nani kakwambia maneno haya?” Joyce aliuliza huku mshangao ukiwa bado haujamtoka usoni kwake. Winifrida aliachia kicheko hafifu na kumfanya Pendo naye acheke.


“Watu wanasema, hata anti Winnie alikuwa anasema…” Pendo alisema huku akinyoosha kidole chake kumuonesha Winifrida.


“Aka! Lini mimi nimekwambia? Utakuja kusutwa we mtoto!” Winifrida alimkata kauli Pendo na kumruka huku akiinuka na kubetua mabega yake juu. Joyce aliguna tu na wala hakujua la kufanya wala kusema.


* * * * *


Sammy alikuwa ameketi kwenye kiti kifupi chenye foronya laini ndani ya mgahawa mkubwa wa kisasa wenye kuta safi za vioo, uliokuwa ukimilikiwa na rafiki yake, Elli Kiango, na juu ya meza ya mbao ya mti wa mpodo kulikuwa na chupa kubwa ya maji baridi ya Kilimanjaro na bilauri ndefu.


Nje ya ule mgahawa kulikuwa na bango kubwa jeupe juu yake lililokuwa na maandishi makubwa ya rangi nyekundu yakisomeka ‘ELLI’S’. Pia kulikuwa na eneo la maegesho ya magari na kulikuwa na takriban sabini yaliyokuwa yameegeshwa kwenye eneo la maegesho ya magari na mengi yalikuwa ya watu wenye vipato vya juu.


Elli’s ulikuwa mgahawa wa kisasa kabisa wenye kila aina ya vionjo vya daraja la kimataifa, ukifananishwa na migahawa mikubwa duniani kama McDonald; Royal Dragon; West Lake ulioko Mji wa Changsha, China; Varsity Downtown wa Atlanta, Georgia; Lundy’s wa Brooklyn, Newyork; Cosmo wa Croydon, Uingereza n.k.


Kutokana na umaarufu wa mgahawa huo, Elli’s ulikuwa na uwezo wa kuhudumia watu zaidi ya 2,000 kwa siku na uliajiri wafanyakazi zaidi ya 200 waliotoa huduma mbalimbali katika mgahawa huo.


Mgahawa huo ulikuwa na mandhari yenye ubora iliyowafanya wageni wengi kuingia kwa wingi na kujionea mandhari yake na vivutio vilivyopo kwenye mgahawa huo.


Pia ukubwa wa majengo yake yaliyotengenezwa kwa ustadi wa hali juu yakiambatana na nakshi zilizochorwa na kutengenezwa kwa ustadi zikiashiria mila na tamaduni za makabila yaliyopo Tanzania ndiyo sababu zilizowafanya watu wengi pamoja na wageni mbalimbali kutembelea mgahawa wa Elli’s.


Ulikuwa na ukumbi maalumu mkubwa wa vyakula mbalimbali (dining hall) vya watu wa mataifa tofauti uliokuwa na utulivu wa kutosha, ukiwa na meza ndefu za kisasa zilizozungukwa na viti vizuri vya sofa vyenye foronya laini. Ukumbi huo ulikuwa na uwezo wa kubeba takriban watu 500, ambapo wateja walikaa kwa vipindi fulani (shifting zone).


Pia kulikuwa na ukumbi mwingine mkubwa wa kisasa uliotumika kwa ajili ya burudani au mikutano mbalimbali, ukumbi ule ulikuwa na jukwaa zuri la kisasa lililokuwa likitazamana na viti vingi vya kisasa na ulikuwa na uwezo wa kuingiza watu wasiopungua 1,000 kwa wakati mmoja bila bugudha yoyote.


Huduma ya mtandao wa intaneti ya WiFi (Wireless Fidelity) haikukosekana ndani ya ukumbi ule, hasa kwa mtu mwenye kifaa kilichoweza kunasa taarifa za kimtandao wa intaneti, kama simu za kisasa za mkononi, kompyuta na kadhalika.


Muda ule wa mchana kulikuwa na sauti ya muziki laini wa taratibu iliyosikika kutoka katika spika zilizokuwa sehemu fulani ndani ya ule mgahawa na kuzikonga vizuri nyoyo za watu waliofika kwa ajili ya chakula, vinywaji au huduma zingine muhimu.



Ndani ya ule mgahawa kulikuwa na wahudumu wa kike warembo kwelikweli waliokuwa wakihudumia wateja. Wahudumu wale walikuwa wamevaa sare za kazi, sketi fupi nyeusi zilizoishia juu ya magoti, makoti ya suti ya rangi nyeupe yenye kola nyeusi na kofia nyeusi kichwani, na walikuwa na nyuso zilizopambwa na tabasamu la kirafiki muda wote.


Ukumbi ule wa chakula na vinywaji ulikuwa na meza nyingi ndogo fupi na pana zilizozungukwa na viti vifupi vyenye sofa laini, na muda ule wa mchana kulikuwa na watu wasiopungua mia moja walioketi kwa utulivu kwenye viti vyao huku wakijipatia chakula na vinywaji, wengi wao wakiwa Wazungu na Waasia.


Sammy alikuwa ameketi kwenye kile kiti kifupi chenye foronya laini kwa utulivu mno akionekana kuwa mbali kimawazo, muda ule ule mwanamume mmoja mrefu na mwenye mwili uliojengeka kwa mazoezi, alifika pale na kuketi kwenye kiti kingine kifupi chenye foronya laini kilichokuwa mkabala na kile alichoketi Sammy.


Mwanamume yule mcheshi na mwenye macho ya upole alikuwa amevaa suti nadhifu ya rangi ya kijivu ya ‘single button’ na shati jeusi lililomkaa vyema na kumpendeza. Miguuni alikuwa amevaa viatu vyeusi vya ngozi kutoka Italia na mkononi alivaa saa aina ya Rolex Submariner.


Aliitwa Elli Kiango na alikuwa rika moja na Sammy, huyo ndiye aliyekuwa mmiliki wa ule mgahawa wa kisasa. Yeye na Sammy walifahamiana tangu utoto wao, walikuwa ni zaidi ya marafiki, walikuwa ni ndugu hasa.


Wakati Sammy alikuwa msomi wa ngazi ya Uzamili aliyesomea biashara ya kimataifa na lugha (M.A. in International Business With Languages), Elli pia alikuwa msomi wa ngazi ya Uzamili aliyesomea Uongozi wa Biashara (M.A. in Business Administration).


Tofauti kubwa kati yao ilikuwa katika misimamo, wakati Sammy alikubali kuajiriwa, Elli hakupenda kabisa kuajiriwa na aliona kuwa elimu yake ingemletea mafanikio makubwa akiamini katika falsafa kuwa: ‘huwezi kutimiza ndoto yako kama utakuwa chini ya mtu mwingine, ukimfanyia kazi na yeye akikupangia na kukulipa mshahara’.


Elli alipoketi kwenye kiti aliweka miguu yake juu ya kiti kingine kilichokuwa mbele yake, akashusha pumzi za ndani kwa ndani huku akimtazama Sammy kwa makini kwenye jicho lake la kushoto lililokuwa na jeraha. Sammy alijaribu kuyakwepa macho ya Elli kwa kutazama kando huku akiilamba midomo yake.


“Samahani kuna mambo yalinitinga kidogo nikalazimika kukuacha peke yako, I hope you are not bored,” Elli alisema huku akijiweka vizuri pale kwenye kiti.


“I’m not bored at all,” Sammy alisema huku akiachia tabasamu na kutazama kando. Kilipita kitambo fulani cha ukimya kila mmoja akionekana kutafakari.


“Kama ulivyoniambia, bado sioni mantiki ya wewe kusimamishwa kazi kwa utovu wa nidhamu, mbona kama hainiingii akilini! Au kuna kitu wewe na bosi wako mmepishana au kuchukuliana?” Elli alivunja ukimya huku macho yake yakiweka kituo kwenye uso wa Sammy na kumtazama kwa makini.


“Wala hatujapishana au kuchukuliana chochote, yeye tu na roho yake!” Sammy alisema na kushusha pumzi. Usoni wake haukuonesha tashwishwi yoyote na badala yake alikaa kimya akiupisha utulivu kama afikiriaye jambo fulani.


Jibu lile lilimfanya Elli amtazame Sammy kwa mshangao kisha akamuuliza kwa sauti tulivu, “Inaonesha kama kuna jambo fulani unalijua ila hutaki kuniambia, don’t you trust me?”


“Kwani lini nimewahi kukuficha jambo, ndugu yangu?” Sammy naye aliuliza huku akimkazia macho.


“Sikumbuki… lakini niseme tu ukweli nilishtushwa sana pale mkeo aliponipigia simu asubuhi kunieleza kuwa ulirudishwa nyumbani usiku wa saa 7 ukiwa umebebwa kwenye mkokoteni chakari hujitambui,” Elli alisema na kushusha pumzi za ndani kwa ndani.


Sammy hakusema neno, alibaki kimya akiwa ameinamisha uso wake akiangalia chini kwa fadhaa, ni wazi alionekana kuwa na huzuni.


“Anasema ulipoingia ndani ukaiangukia meza ndogo ya kioo na kuivunja, kisha ukatapika kwenye korido na ulipotaka kukimbilia kwenye mlango ukabamiza jicho… mkeo akakuburuza kukupeleka chumba cha kulala, na alipoanza kukuvua nguo ukapiga kelele ‘niache, mi nimeoa’,” Elli alisema na kuangua kicheko hafifu.


Sammy alitamani kucheka lakini alionekana kujizuia na kuangalia kando kwa aibu. Alishusha punzi za ndani kwa ndani na kukunja sura yake akijaribu kukumbuka, hata hivyo hakuonekana kukumbuka chochote.


“By the way… sidhani kama kulewa ni suluhisho la matatizo yako, unatakiwa kuyakubali matokeo na uwe tayari kwa chochote, kwa sababu kilichotokea siyo mwisho wa dunia,” Elli alisema na kumwita mhudumu mmoja mrembo sana aliyekuwa akipita eneo lile.


“Hamisa, naomba uniletee juice ya avocado,” Elli alimwambia yule mhudumu ambaye aliitikia kwa kubetua kichwa chake huku akitabasamu, kisha akageuka na kuondoka haraka kutoka eneo lile huku mtikisiko wa mzigo wa makalio yake ukiwafanya wateja kugeuza shingo zao kumtazama kwa matamanio.


Baada ya yule mhudumu kuondoka Sammy alishusha pumzi za ndani kwa ndani. “Kwa kweli nipo njia panda,” alisema kwa huzuni.


“Nadhani sasa utakuwa umepata funzo, usikubali tena kuwafanyia kazi watu wasioona umuhimu wa wengine, bali wanachojali wao ni kutengeneza fedha tu na kutunisha mifuko yao,” Elli alisema kwa msisitizo na kuongeza.


“Kwa nini usifikirie kuanzisha kampuni ya kukodisha magari, a car rental… naamini unao uzoefu wa kutosha kwa kuwa uliwahi kufanya kazi ya kutembeza watalii kabla hujafanya kazi katika hoteli.”


“Ninatamani sana kumiliki kampuni yangu tatizo fedha ninayoitegemea haitatosha.”


“Si lazima kuanza na magari mengi, hata moja au mawili yanatosha na utakuwa unaongeza kadiri biashara inavyochanganya… tafuta gari zuri na lenye utofauti ili kukabili ushindani,” alisema Elli na kumfanya Sammy ashushe pumzi huku akionekana kukosa uthubutu. Alitazama kando akionekana kufikiria jambo kwa kitambo fulani.



“Itakuwaje iwapo nitatumia akiba yangu yote na mambo yasiende vyema?” Sammy aliuliza.


“Tatizo lako kwa kuwa umesomea biashara ya kimataifa basi unafikiria kimataifa badala ya kufikiria huku chini, wewe amua mimi nipo nitakusaidia kusajili kampuni, unajua inapendeza zaidi kufanya kazi unayoipenda, ambayo wewe mwenyewe ndiye bosi,” Elli alisema huku akimtazama Sammy kwa makini na kutabasamu.


“I’m still in dilemma, nahisi nnaweza kupoteza thamani kwa familia yangu pindi ikibainika kuwa nimepoteza kazi, japo nina ndoa thabiti, lakini hali hii inaweza kubadili kila kitu kwenye uhusiano wetu,” Sammy alisema kwa wasiwasi.


“Mwambie Joyce ukweli na umdokeze kuhusu wazo la kuanzisha kampuni,” Elli alimwambia Sammy na kuongeza, “Ila tafuta njia nzuri ya kumweleza na umpe nafasi aongee ili usikie mawazo yake.”


“Mmh!” Sammy aliguna huku akishusha pumzi za ndani kwa ndani, akaminya midomo yake.


“Kuambiana ukweli ni muhimu sana katika kuijenga familia…”


“Nakubaliana kabisa na wewe, ukweli ni mzuri lakini si kwa mwanamume kumwambia mwanamke kuwa amesimamishwa kazi eti kwa madai ya utovu wa nidhamu!” alidakia Sammy.


“Unadhani utaendelea kumficha hadi lini? Huoni kama siku akigundua mambo yanaweza kuwa mabaya zaidi?” Elli alijaribu kumtahadharisha Sammy.


“Ndiyo hapo sasa! Nadhani natakiwa kukubaliana na wewe na nimweleze tu ukweli, tena nitamweleza leo hii hii.”


“Fanya hivyo, mara nyingi ili kushinda vita ni lazima ukubali ukweli, usahau yaliyopita na uyaishi yaliyopo,” Elli alishauri na kumfanya Sammy kubetua kichwa chake huku akiachia tabasamu.


“Nitazame mimi, nilikataa utumwa wa kuajiriwa na kuamua kufungua biashara yangu mwenyewe kwa sababu sipendi kutumika kumuingizia mtu mwingine fedha nyingi ili anilipe mshahara,” Elli alisema na kuongeza, “Pia ninapenda nifanye kitu ninachokipenda na niwe bosi wa kazi yangu mwenyewe.”


Japo Sammy alikuwa bado ana wasiwasi lakini alianza kupata matumaini kwa mbali, sasa shauku ya kuanzisha biashara yake ilijionesha waziwazi usoni kwake, alinyanyua uso wake kuangalia juu kwa kitambo akitafakari sana kuhusu hatma yake, kisha alishusha pumzi za ndani kwa ndani.


* * * * *


Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) kilikuwa na pilika pilika nyingi sana jioni hiyo, kulikuwa na hali ya mawingu kiasi. Watu mbalimbali walikuwa katika pilika pilika za kusafiri au kupokea wageni wao kutoka ndani na nje ya nchi.


Gari la kifahari aina ya Toyota Landcruiser GX V8 la rangi nyeusi, mali ya Mr. Oduya lililokuwa likiendeshwa na Madjid Chege liliwasili katika kiwanja hicho cha ndege saa 10:30 za jioni, likaelekea katika kituo namba tatu (terminal III) cha kiwanja cha ndege.


Mr. Oduya alikuwa ameketi kwa utulivu ndani ya lile gari na alikuwa amekuja kumpokea mgeni wake binafsi na muhimu sana, mwanadada Zainab Semaya, hiyo ilikuwa nusu saa kabla ya mgeni huyo kuwasili na ndege ya shirika la ndege la Ujerumani la Lufthansa.


Mipango yote ilikuwa imepangwa kwamba mgeni huyo akiwasili tu katika kiwanja cha ndege cha Julius Nyerere apelekwe moja kwa moja Paradise Club alikotakiwa kufikia, kabla wafukunyuku wenye kufuatilia mambo yasiyowahusu hawajamtia machoni.


Madjid Chege, dereva wa Mr. oduya aliyedumu naye kwa miaka kumi na mbili sasa, aliliegesha lile gari kwenye eneo maalumu la maegesho ya magari la kile kituo namba 3 cha JNIA, kituo kilichokuwa na uwezo wa kuruhusu ndege kubwa 24 kwa wakati mmoja na abiria milioni 6 kwa mwaka kikiwa na mandhari ya kupendeza, yaliyomvutia kila aliyefika pale kwa mpangilio wake mzuri.


Mr. Oduya aliangaza macho yake huku na kule akionekana kutafuta kitu kisha alitoa simu yake lakini kabla hajapiga alimuona Mafuru akielekea pale walipoegesha gari lao. Kumbe muda wote Mafuru alikuwa ameliona gari la Mr. Oduya tangu lilipokuwa likiingia pale kiwanjani.


Waliongea kwa dakika chache, kisha Mafuru aliondoka haraka akimwacha Mr. Oduya ndani ya gari, akavuta hatu zake kuelekea ndani ya lile jengo la kituo namba 3, hasa katika eneo la kusubiria wageni. Akajichanganya na watu waliokuwa katika eneo hilo wakisubiri ndugu na jamaa zao.


Muda wote Mr. Oduya alionekana kuwa na wasiwasi, alijiegemeza kwenye siti yake na kushusha pumzi za ndani kwa ndani, kisha alifumba macho na kuanza kutafakari.


Ingawa hakupenda kabisa Zainab aje Tanzania lakini hakuwa na namna nyingine ya kumzuia, alihofia kuwa endapo wapinzani wake kisiasa wangejua kuhusu uhusiano wake na Zainab na ujio wa Zainab nchini wangeweza kutumia kama silaha ya kumharibia katika harakati zake za kutaka kuwa Rais wa Tanzania, nafasi aliyoitamani kwa miaka mingi.


Zainab alikuwa ameng’ang’ania kuja jijini Dar es Salaam na kama Mr. Oduya angekataa basi angetakiwa yeye aende nchini Canada alikoishi Zainab na watoto wake wawili, Jasmine na Latifah. Ilikuwa imeshapita takriban mwaka mmoja na ushee bila Mr. Oduya kwenda nchini Canada kuwaona, japo walikuwa wanawasiliana kwa simu na njia ya skype takriban kila siku.


Mr. Oduya alishindwa kwenda Canada kwa kuwa alikuwa kwenye harakati za kuweka mambo yake sawa kabla ya pazia la kampeni za uchaguzi halijafunguliwa, hivyo hakuwa na namna nyingine isipokuwa kukubali kwa shingo upande Zainab aje ili asimuudhi, lakini kwa sharti kuwa safari hiyo iwe ya siri sana na asije na watoto, pia asikae muda mrefu arudi Canada.


Zainab na Mr. Oduya wamekuwa na uhusiano wa siri na mapenzi yao waliyafanya kuwa ya siri sana kwa zaidi ya miaka kumi na miwili, Mr. Oduya alikuwa amempora Zainab kutoka kwa mumewe, Hemed Kimaro, aliyekuwa mfanyabiashara wa madini.




Hemed alikuwa shemeji wa Mr. Oduya, kwani alikuwa ndugu wa tumbo moja na Dk. Salma K. Oduya, mke wa Mr. Oduya. Ilitokea wakati ndoa yao ikiwa katika mgogoro ndipo Mr. Oduya alipopata mwanya huo kumshawishi Zainab kwa kila njia ikiwemo kumpa fedha nyingi ambazo hakuwahi kuota kuzipata. Hatimaye waliingia kwenye uhusiano wa mapenzi.


Kabla, Zainab alikuwa mwanamke mtulivu na mwaminifu sana kwa mumewe licha ya urembo na upole wake, lakini Hemed alikuwa ‘bize’ na biashara zake na muda mwingi aliutumia kusafiri huku na huko au kuwa na washirika wake wa kibiashara, jambo lililosababisha mgogoro wa mara kwa mara kwenye ndoa yake.


Kabla ya uhusiano na Zainab, Mr. Oduya alishakuwa na uhusiano na wanawake kadhaa warembo akitumai kupata faraja aliyoikosa kutoka kwa mkewe Dk. Oduya, ambaye alikuwa ana gubu na alijaa kisirani. Ilifika kipindi Mr. Oduya alijilaumu kwa nini alimwoa.


Kwa Zainab alijikuta akiweka kituo, na wote wawili (Zainab na Oduya) walijikuta wakihitaji faraja nje ya ndoa zao, ndiyo maana mapenzi yao ya siri yalichipua na kumea kama mche kwenye udongo wenye rutuba, japo kulikuwa na tofauti kubwa ya umri kati yao.


Mr. Oduya alikuwa akimpatia Zainab chochote alichokitaka ikiwemo kumnunulia kwa siri jumba la kifahari eneo la Kijitonyama na penzi lao kukua kwa kasi mithili ya moto mkali ulao nyika.


Kwa kuwa Zainab hakuwahi kuwa na uhusiano mwingine wowote wa kimapenzi kabla na hata baada ya ndoa yake, hivyo alijikuta akilivamia penzi la ‘shuga dadi’ kwa miguu yote miwili, alikuwa ni kama aliyepatwa na wazimu wa mapenzi na pepo la uzinzi lilikuwa limeingia kazini.


Hatimaye Hemed alianza kuzishtukia nyendo za mkewe, alianza kuhisi kuwa mkewe alikuwa akiisaliti ndoa yake na mwanamume mwingine, ingawa hakujua ni mwanamume gani. Aliumia sana na kuanza kufuatilia, siku moja alirudi ghafla nyumbani usiku na kumfumania Zainab akiwa na Mr. Oduya kitandani, akaishiwa nguvu na kupoteza fahamu.


Mr. Oduya alihofia mambo hayo kumfikia mkewe, isitoshe Zainab alishakuwa na ujauzito. Kesho yake asubuhi mwili wa Hemed ulikutwa kwenye mtaro wa maji machafu nyuma ya nyumba yake ukiwa umetapakaa damu baada ya kuchakazwa risasi tatu kifuani...


“Naona ndege ndiyo inaingia,” sauti ya Chege ilimzindua Mr. Oduya kutoka kwenye mawazo. Alichungulia dirishani na kuiona ndege kubwa ya shirika la ndege la Lufthansa ikishuka taratibu katika Kiwanja cha ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere.


Mawazo yalikuwa yamemteka Mr. Oduya, alikwishaanza kuchoka kuishi mbali na Zainab na aliazimia kuwa baada ya kushinda uchaguzi na kuwa Rais wa nchi, asingeendelea kuficha bali angefanya kila njia, hata ikibidi kusababisha kifo cha mkewe ili Zainab awe mkewe rasmi ‘first lady’.


Aliamini kuwa mambo yalikwisha isha kwani miaka mingi ilikwishapita tangu mauaji ya mumewe Hemed Kimaro na baadaye jaji aliyekuwa kimbelembele katika ile kesi kabla hajapandishwa cheo kuwa jaji mkuu, Sylvester Lutego. Hata hivyo alikuwa na uhakika faili la kesi ya mauaji ya Hemed halikuwepo tena, kwani waliliteketeza kwa moto na hakukuwa na kumbukumbu zozote zilizoachwa...


_____


Saa kumi na moja kamili, ndege kubwa ya shirika la ndege la Lufthansa ilikuwa ikikimbia kwa kasi kwenye barabara ndefu ya lami maarufu kama ‘runway’ iliyokuwa imewekwa alama elekezi za kuwaongoza marubani wa ndege, katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere.


Baada ya muda ilipunguza mwendo na kugeuza, kisha ikaingia katika barabara nyingine ya lami ambayo pia ilikuwa imechorwa alama elekezi za kuwaongoza marubani wa ndege kisha aliingia kwenye maegesho tayari kwa kuteremsha abiria waliokuwa wameabiri katika shirika hilo.


Muda mfupi baada ya ile ndege kusimama na abiria kuruhusiwa kufungua mikanda ya siti zao milango ya ndege ikafunguliwa na ngazi zikiwekwa sawa, abiria walikuwa katika foleni ya kushuka. Mmoja wa abiria wale aliitwa Zainab Semaya.


Zainab alikuwa mwanamama mrembo kwelikweli, alikuwa na umri wa miaka therathini na nane, mrefu na mweupe kiasi mwenye umbo la kuvutia, nywele ndefu na laini alizokuwa amezifunika kwa kofia ya kapelo na alivaa miwani mikubwa myeusi iliyoyaficha vyema macho yake makubwa ya kike yenye ulegevu.


Sura yake ilikuwa ndefu kiasi, midomo laini yenye kingo pana kiasi zilizopakwa rangi nzuri ya mdomo ya chocolate, pua yake ilikuwa ndefu na vishimo vidogo mashavuni mwake viliwafanya wanaume wababaike kila walipomtazama.


Alivaa suruali nyeusi ya jeans, iliyoshikiliwa na kiuno chembamba kiasi mithili ya dondola lakini imara kilichoshikilia minofu laini ya mapaja yake yaliyonona, fulana nyepesi nyekundu iliyoyaficha vyema matiti yenye ukubwa wa wastani na juu yake alivaa jaketi jeusi la jeans. Miguuni alivaa raba ngumu za rangi nyekundu.


Baada ya taratibu zote za uhamiaji hatimaye alishika uelekeo wa upande wa kulia akifuatana na abiria wengine, wakaifuata korido ndefu iliyokuwa ikipakana na ofisi mbalimbali za utawala wa kile kituo namba 3, na kutokea eneo maalumu la kuchukulia mizigo yao iliyokuwa ikipita kwenye mikanda maalumu.


Alichukua begi lake kubwa la magurudumu na kuelekea kwenye korido nyingine upande wa kushoto iliyokuwa ikipakana na ofisi mbalimbali za mashirika tofauti ya ndege, migahawa ya kisasa, maduka ya kubadilishia fedha za kigeni, ofisi za mawakala wa kampuni za utalii na kadhalika.


Mwisho wa ile korido wakatokea kwenye eneo pana la mbele sehemu kulipokuwa na watu wengi waliokuja kupokea wageni wao na nyuma yao kulikuwa na maegesho ya magari. Mafuru alikuwa amesimama huku akiangaza macho yake huku na kule kumtazama mgeni aliyepewa maagizo na Mr. Oduya kumpokea.


Mkononi alikuwa ameshika bango dogo jeupe lililoandikwa maandishi makubwa ya: “Welcome Suzanne Ross”.


Zainab alikuwa akijongea eneo lile taratibu huku akitazama huku na kule akiwa anaburuta begi lake kwa mkono mmoja na begani akiwa ametundika mkoba mdogo mzuri wa kike wa rangi nyekundu. Mara alimuona mwanamume mmoja aliyekuwa ameshika bango dogo lililoandikwa jina la Suzanne Ross.





Alishtuka kidogo na kumtazama kwa makini yule mwanamume huku akijiuliza kama kulikuwa na mtu mwingine aliyeitwa Suzanne Ross aliyekuwa akiwasili katika kiwanja kile cha ndege. Hili lilikuwa jina lake alilobadilisha ili kukwepa utambulisho wake baada ya kuhamia Canada.


Alimtazama yule mwanamume kwa makini, akakumbuka kuwa alikuwa ameambiwa na Mr. Oduya kuwa mwanasheria wake aliyeitwa Adam Mafuru angempokea pale kiwanjani na kumpeleka sehemu salama, hivyo akaamua kumkabili.


“I’m Suzanne Ross,” Zainab alijitambulisha kwa Mafuru huku akinyoosha mkono wake kumsalimia. Mafuru alionekana kubabaika sana na uzuri wa Zainab.


“I’m Adam Mafuru,” Mafuru naye alijitambulisha huku akimpa mkono wake. Kisha kwa unyenyekevu Mafuru alimwambia Zainab kuwa Mr. Oduya alikuwepo pale kiwanjani ila kwa sababu maalumu asingeweza kujitokeza kumpokea, na kumtaka amfuate.


Walianza kutoka huku Mafuru akiliburuta lile begi la Zainab kuelekea kwenye gari aina ya Toyota Lexus RX la rangi nyeupe lililokuwa na vioo vya ‘tinted’ nyeusi isiyomruhusu mtu kuona waliokuwemo ndani, ambalo lilikuwa likitumiwa na Spoiler.


Spoiler aliwaona na kufungua sehemu ya nyuma ya gari, akaweka lile begi la Zainab na kwa heshima zote na tabasamu la kirafiki Mafuru alimfungulia Zainab mlango wa nyuma wa gari na kumkaribisha aingie.


Muda wote Mr. Oduya alikuwa ametulia kwenye gari akishuhudia kila kitu, hakutaka kabisa kushuka kwa kuwa hakupenda watu waliomfahamu wamuone au wajue nini kilikuwa kinaendelea kati yake na Zainab.


“I see! Nimeimisi sana nchi yangu, ni bahati iliyoje kurudi tena baada ya miaka mingi ya kuishi uhamishoni,” Zainab alijiambia nafsi mwake huku akishangaa kuona kulikuwa na maendeleo makubwa tofauti na wakati alipokuwa akiondoka.


Gari lilianza kuondoka kutoka eneo lile na safari ya kuelekea mjini ikaanza. Aligeuza shingo yake kuyatazama mandhari ya kupendeza ya Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere yaliyomvutia sana kwa mpangilio wake mzuri wa majengo.


* * * * *


Saa 12:30 jioni gari dogo la kifahari aina ya BMW X6 xDrive 50i la rangi nyeupe likiwa na vioo vilivyowekwa ‘tinted’ nyeusi isiyomruhusu mtu kuona waliokuwemo ndani, lilikuwa kwenye foleni likizivuka taa za kuongozea magari barabarani za Buguruni Shell.


Gari lile lilikuwa linatokea katika barabara ya Uhuru na lilipozivuka taa za kuongozea magari barabarani liliingia barabara ya Mandela likielekea eneo la Tazara.


Ndani ya lile gari kulikuwa na watu watatu, Elli, aliyekuwa akiendesha lile gari na mwanadada mrembo sana alikuwa ameketi pembeni yake kwenye siti ya abiria. Kwenye siti ya nyuma aliketi Sammy akionekana mtulivu sana. Lile gari lilipokivuka kituo cha daladala cha Buguruni Chama likasimama kando ya ile barabara ya Mandela.


Sammy alishuka huku akimshukuru Elli, wakaagana kisha alianza kutembea taratibu kando ya ile barabara na kukivuka kituo cha daladala cha Buguruni Chama akielekea ziliko taa za barabarani za kuongozea magari.


Pale kwenye kituo cha daladala abiria walikuwa wengi wakiwa wanakimbilia kupanda magari ya Gongolamboto na Mbagala yaliyokuwa yamejaza abiria. Sammy aliendelea kutembea taratibu na kuwapita vijana waliokuwa wanauza maji na wengine wakiwa wamebeba madeli ya barafu (ice cream) za Ukwaju.


Yeye alitembeaa taratibu pasipo kujishughulisha na mambo ya watu wengine, alionekana kuwa na mawazo. Muda huo jua lilikwishaanza kuzama na kiza kuanza kuchukua nafasi ya mchana, hivyo magari yalianza kuwasha taa.


Sammy aliangalia huku na huko na kuvuka barabara ya Mandela iliyokuwa na magari yanayoelekea Tazara kisha akapanda juu ya ukuta wa katikati uliotenganisha magari ya kuelekea Tazara na yale yaliyokuwa yakielekea Ubungo, akitaka kuelekea upande wa pili wa barabara.


Wakati akianza kuvuka barabara upande wa pili sauti ya breki kali za gari ilisikika na kumshtua sana, alijikunja na kuruka huku akiongeza mwendo. Dereva wa lile gari alijitahidi kumkwepa kisha gari lilisimama katikati ya barabara. Sammy aligeuka kutazama kule kwenye gari huku mwili wake ukitetemeka kwa hofu.


Aliliona gari la kifahari aina ya Toyota Landcruiser GX V8 la rangi nyeusi likiwa limesimama huku dereva akimtazama kwa hasira, kisha macho ya Sammy yakatua moja kwa moja kwenye uso wa Mr. Oduya aliyekuwa ameketi kwenye siti ya nyuma akiangalia nje kupitia kioo cha dirisha.


Japokuwa Mr. Oduya alionekana kutafakari jambo fulani kwa kina lakini alikuwa makini sana kumtazama Sammy. Waliangaliana kwa kitambo na Mr. Oduya akaachia tabasamu.


Sammy alionekana kushtuka sana na kukimbilia kwenye baa ya Kimboka lakini akaona haitoshi, akajichanganya na watu wengine akiwapita wauzaji wa biashara ndogo waliopanga biashara zao kando ya barabara ya waenda kwa miguu na kuifuata njia nyembamba iliyokuwa ikielekea kwenye hoteli ya New Popex.


Mr. Oduya alibaki akiwa mtulivu huku akitazama kule alikokuwa amekimbilia Sammy huku akiendelea kutabasamu, muda huo huo magari mengine yaliyokuwa nyuma ya lile gari la Mr. Oduya yalianza kupiga honi ya kumtaka dereva aondoe gari.


Dereva wa Mr. Oduya aliangalia nyuma kupitia kioo cha gari cha katikati na kuyaona yale magari yaliyokuwa nyuma yake yakimuwashia taa kumuashiria aondoe gari, alitii na kukanyaga pedeli ya mafuta, magurudumu ya gari yakaserereka kwenye lami huku gari likiondoka kwa kasi.


Wakati lile gari likiondoka kwa kasi eneo lile Mr. Oduya aligeuza shingo yake kutazama kule alikokuwa amekimbilia Sammy, lakini hakumuona.




Mr. Oduya alibaki akiwa mtulivu huku akitazama kule alikokuwa amekimbilia Sammy huku akiendelea kutabasamu, muda huo huo magari mengine yaliyokuwa nyuma ya lile gari la Mr. Oduya yalianza kupiga honi ya kumtaka dereva aondoe gari.


Dereva wa Mr. Oduya aliangalia nyuma kupitia kioo cha gari cha katikati na kuyaona yale magari yaliyokuwa nyuma yake yakimuwashia taa kumuashiria aondoe gari, alitii na kukanyaga pedeli ya mafuta, magurudumu ya gari yakaserereka kwenye lami huku gari likiondoka kwa kasi.


Wakati lile gari likiondoka kwa kasi eneo lile Mr. Oduya aligeuza shingo yake kutazama kule alikokuwa amekimbilia Sammy, lakini hakumuona.


Sasa endelea...


* * * * *


Saa 1:00 jioni gari aina ya Toyota Lexus RX la rangi nyeupe lililokuwa na vioo vya ‘tinted’ nyeusi isiyomruhusu mtu kuona waliokuwemo ndani lilikuwa linaukaribia uzio wa hoteli ya Udzungwa Beach Resort katika barabara ya Ufukweni, eneo la Oysterbay.


Lilikata na kuingia kulia likishika barabara iliyoelekea nyuma ya majengo ya hoteli ya Udzungwa Beach Resort, kisha liliingia kushoto na kuishika barabara maalumu iliyoelekea Paradise Club.


Eneo lile lilikuwa na ulinzi mkali nje na ndani ya uzio, na walioruhusiwa kuingia ndani ya Paradise Club ni wanachama waliosajiliwa tu au wageni wao maalumu, lakini kwa utambulisho maalumu.


Barabara ile ilipambwa na maua mazuri ya ‘Magnolia grandiflora’ yaliyokuwa na rangi ya maziwa na maua mengine aina ya ‘lotus’ yaliyokuwa na rangi mchanganyiko nyeupe, pinki na zambarau, pia ilikuwa imezungukwa na taa nzuri za rangi mbalimbali na maua ya kupendeza.


Lile gari lililokuwa likiendeshwa na Spoiler lilikaribia kwenye kizuizi cha barabarani kilichokuwa na maandishi makubwa yaliyoandikwa kwa lugha ya Kiingereza: ‘Security Check Point’, na kwenye kizuizi hicho kulikuwa na askari maalumu watano wa kampuni ya ulinzi ya Spark K7, watatu kati yao walikuwa na silaha.


Spoiler alikanyaga breki na kupunguza mwendo na hatimaye kusimamisha gari lake umbali wa mita kumi kutoka kilipokuwa kizuizi huku walinzi wenye silaha wakiwa wamenyoosha silaha zao kumuelekea. Walinzi wawili kati yao walianza kupiga hatua zao kulisogelea lile gari huku wakiwa wameshika vyema bunduki zao wakizielekeza kwenye lile gari.


Mlinzi mmoja alielekea kwenye dirisha la Mafuru, akamsalimia kwa adabu sana na kumuomba kadi yake. Wakati huo huo mlinzi mwingine alizunguka akaelekea upande wa nyuma wa lile gari huku akiwa analichunguza kwa jicho la hadhari.


“Mgeni wa PC.008.19, nadhani taarifa zote mnazo!” Mafuru alimwambia yule mlinzi huku akionesha kadi maalumu ambayo walipewa wageni, kisha aliachia tabasamu.


Yule mlinzi aliwapa ishara walinzi wengine waliokuwa wamesimama kwenye kile kizuizi kuondoa kile kizuizi, wale walinzi walitii na kuondoa kizuizi wakimruhusu Spoiler kupita.


“Madame, hivi sasa Tanzania imeendelea sana tofauti na ulivyoiacha, unaona kama hapa kuna ulinzi mkali sana, kwa kuwa wanaokuja hapa ni mabilionea na watu wenye nyadhifa kubwa serikalini,” Mafuru alimwambia Zainab aliyekuwa kimya muda wote akionekana kushangaa sana.


Baada ya mita hamsini walikutana na kizuizi kingine kilichokuwa na askari maalumu watano wa kampuni ya ulinzi ya Spark K7 huku wawili wakiwa na silaha. Spoiler alisimamisha gari lake na Mafuru akatoa kichwa chake nje.


Alitaja tena namba ya utambulisho huku akiwaonesha ile kadi na wale walinzi walimruhusu kupita, walikwenda mita therathini tu mbele wakakutana na kizuizi cha tatu, ambacho pia kulikuwa na askari maalumu watano wa kampuni ya ulinzi ya Spark K7 huku watatu wakiwa na silaha.


Mafuru alitaja tena namba ya utambulisho huku akionesha ile kadi na mara mlinzi mmoja alibonyeza kitufe fulani, geti kubwa likajifungua na kuwaruhusu kuingia ndani. Walijikuta wametokea katika eneo zuri mno lenye bustani nzuri ya nyasi laini aina ya ‘Citronella’ na mandhari ya kuvutia sana yaliyopambwa na mazuri aina ya ‘Magnolia grandiflora’ na ‘lotus’.


Waliegesha gari lao kwenye maegesho maalumu ya magari, na kulikuwa na magari mengine kadhaa ya kifahari yaliyokuwa yamejipanga.


“Madame, tumefika,” Mafuru alimwambia Zainab huku akishuka na kumfungulia mlango wa gari kisha alishusha begi lake.


Zainab alishuka na mara moja akatokea mwanadada mmoja mrembo sana aliyekuwa amevaa gauni zuri lililochanganywa kitenge cha fabric na kitambaa cha rangi ya pinki ndani ya kitenge, lenye mshono mzuri wa kisasa. Nywele zake ndefu nyeusi alikuwa amezisuka mtindo wa mkia wa pweza.


Midomo yake alikuwa ameipaka rangi ya pinki na macho yake alikuwa ameyatia wanja mzito na kumfanya aonekane kama malkia wa uzuri katika njozi ya alfajiri.


“Naitwa Lilian Japhet, sina shaka ni Madame Suzanne Ross wa PC.008.19…” yule mrembo alijitambulisha kwa kina Mafuru huku akiachia tabasamu pana na kusalimia kwa adabu.


“Yeah, ni mgeni wa PC.008.19,” Mafuru alisema huku akimtambulisha Zainab kwa Lilian. Mara moja Lilian aliachia tabasamu na kupokea begi la Zainab.


“Karibu sana Madame, mimi ndiye nitakayekuhudumia muda wote utakaokuwepo hapa, naomba nifuate,” Lilian alisema na kupiga hatua zake taratibu na kwa madaha akitangulia mbele huku akiburuta begi.


Zainab alimfuata nyuma taratibu hadi kwenye mlango mkubwa wa mbele wa Paradise Club, Lilian akausukuma taratibu na kumruhusu Zainab aingie ndani. Lilian akaurudisha ule mlango nyuma yake kisha taratibu akaanza kupiga hatua zake kwa utulivu huku akifuatwa na Zainab, wakakatisha katikati ya ukumbi.


Zainabu alitembea huku akiyatembeza macho yake taratibu kutazama huku na huko, mazingira aliyoyaona yalimuashiria kuwa eneo lile lilikuwa ni klabu ya kisasa kabisa yenye vionjo vyote vya burudani kwa watu wenye ukwasi wa daraja la kimataifa, walikuwa wakipishana na sura zilizoonekana za watu wenye ukwasi mkubwa na kulikuwa na burudani ya kila aina.


Kisha walikatisha kwenye korido pana iliyopita kwenye ukumbi mkubwa wa baa ya kisasa uliokuwa na viti vizuri vya sofa vyenye foronya laini pamoja na meza fupi na pana zenye umbo duara. Zainab aliyatembeza macho yake taratibu kuwatazama mabilionea wachache, wengi wakiwa wageni wa kutoka nje ya nchi ya Tanzania, na zaidi kabisa nje ya bara la Afrika, waliokuwa mle ndani na wenzi wao.


Kisha waliufikia mlango mwingine mkubwa uliokuwa na maandishi makubwa ya ‘VVIP’, nje ya ule mlango kulikuwa na walinzi watatu wa kampuni ya Spark K7 waliokuwa nje ya ule mlango, wawili kati yao walikuwa wameshika silaha.



Lilian alimtambulisha mgeni wake. Wale walinzi walimsalimia Zainab kwa adabu na mmoja wao alichukua kifaa cha kukagulia na kuwakagua Zainab na Lilian kuona kama yeyote kati yao alikuwa na silaha yoyote. Kisha walilichukua lile begi lake na kulipitisha kwenye mtambo maalumu na walipohakikisha kwamba hana silaha yoyote, waliufungua mlango na kuwaruhusu waingie.


Lilian na Zainab wakaingia na kutokea kwenye korido pana iliyokuwa ikielekea kwenye vyumba vya VVIP, wao waliifuata korido nyingine fupi kushoto kwao na kukuta vyumba viwili vya lifti upande wa kushoto na upande wao wa kulia kulikuwa na ngazi za kuelekea juu.


Lilian alibonyeza kitufe chenye alama za mshale unaotazama juu na mwingine ukitazama chini kilichokuwa pembeni ya milango ya lifti na mara milango ya kile chumba cha lifti ikafunguka na kuwaruhusu kuingia ndani.


Walipoingia Lilian akabonyeza nambari mbili kwenye kitufe fulani kilichokuwa humo ndani kikiwa na namba kadhaa pembeni ya mlango, milango ya kile chumba cha lifti ikajifunga kisha lifti ikaanza kupanda juu taratibu na ilipofika katika ghorofa ya pili ikasimama na milango ikajifungua yenyewe.


Walipotoka tu wakakuta korido nyingine pana na mlango mkubwa wenye maandishi ya ‘Presidential Suites’. Hapo waliwakuta walinzi wengine watatu wa kampuni ya Spark K7 waliokuwa nje ya ule mlango, wawili kati yao walikuwa wameshika silaha.


Lilian alimtambulisha tena mgeni wa PC.008.19. Wale walinzi walimsalimia Zainab kwa adabu na kuwafanyia ukaguzi. Waliporidhika kuwa hawakuwa na silaha waliwaruhusu kuingia ndani


Lilian alimuongoza Zainab, wakafuata korido nyingine pana iliyopita katikati ya vyumba kadhaa, mbele yao wakaingia kushoto wakiifuata korido nyingine fupi iliyowapeleka hadi mbele ya mlango madhubuti wa mbao uliokuwa na maandishi: PC.19.


Lilian aliufungua ule mlango kwa kadi maalumu ya kielektroniki aliyoigusisha juu ya kitasa cha mlango kisha wakaingia na kutokea kwenye sebule pana. Lilian alibonyeza swichi zilizokuwa ukutani na kuwasha taa na kiyoyozi kilichokuwa sehemu fulani kwenye kona ya kile chumba, na hapo hewa safi ya ubaridi ilianza kusambaa mle ndani.


Sakafuni kulikuwa na zulia nene la rangi nyekundu na upande wa kushoto kulikuwa na runinga pana aina ya Sony iliyofungwa ukutani na chini yake kulikuwa na meza fupi nyeusi yenye kisimbusi chenye chaneli nyingi za kimataifa.


Upande wa kulia kwenye kona kulikuwa na meza fupi ya mapambo na jokofu na ukumbi mdogo wa chakula wenye meza ya umbo duara ya chakula iliyokuwa imezungukwa na viti vinne nadhifu vyenye foronya laini.


Jirani na ule ukumbi wa chakula kulikuwa na mlango ulioelekea kwenye chumba cha kulala. Lilian alimwelekeza Zainab ule mlango huku akiufungua, wakatokea kwenye chumba kikubwa cha kifahari chenye nafasi ya kutosha na kilichokuwa na kitanda kikubwa cha samadari katikati.


Mbele ya kitanda kulikuwa na seti nzuri ya runinga pana aina ya Sony na chini ya ile runinga kulikuwa na meza fupi nyeusi ya kioo, na juu ya meza kulikuwa na simu ya mezani na kitabu chenye orodha ya majina ya watu na kampuni zilizotumia huduma ya simu hiyo ya mezani.


Pia kulikuwa na kabati kubwa la kisasa la nguo lililokuwa ukutani, kando yake kulikuwa na meza ya vipodozi yenye kioo kirefu cha kujitazama na kochi moja kubwa la sofa.


Kulikuwa na madirisha mawili mapana ya vioo yaliyokuwa yamefunikwa kwa mapazia mazito na marefu yenye nakshi za kupendeza. Kwa kutokea kwenye lile dirisha mtu angeweza kuona mandhari nzuri ya kuvutia, na kwenye kona ya chumba kile upande wa kushoto kulikuwa na mlango wa kuelekea kwenye maliwato.


* * * * *


Sammy alifika nyumbani kwake muda wa saa moja na ushee za jioni akiwa amebeba mkoba wake mdogo wa kiofisi aina ya Pad & Quill wa rangi ya hudhurungi aliokuwa ameusahau pub ya Barakuda usiku wa siku iliyokuwa imetangulia.


Aliupitia baada ya kukumbuka, na alipoingia ndani ya nyumba yake alimkuta Joyce akiwa mwenye furaha mno, Sammy alimtazama kwa makini huku mshangao wa wazi ukijitokeza usoni kwake, kisha aliwatupia macho watu wengine waliokuwepo pale sebuleni.


Pale sebuleni walikuwepo Joyce, Pendo na Winifrida waliokuwa wanafuatilia marudio ya mchezo maarufu wa kuigiza wa runinga ulioitwa ‘Gereza la Kifo’ kutoka kwa mtunzi mahiri wa michezo ya kuigiza, Hamisi Kibari.


Hata hivyo, mawazo ya Joyce hayakuwa kwenye ule mchezo wa kuigiza bali alikuwa anawaza kuhusu ahadi yake ya kwenda kuonana na Madame Norah, huku akianza kuiona njia ya kuelekea kwenye mafanikio makubwa kimataifa. Muda ule alikuwa amejiegemeza kwenye sofa huku uso wake ukiwa umepambwa na tabasamu muda wote.


Joyce alimuona Sammy na kuinuka, akamkaribisha huku akiupokea mkoba wake, hata hivyo tabasamu pana usoni kwake lilishindwa kabisa kwenda likizo. Sammy aliguna huku akimkazia macho Joyce kwa umakini zaidi.


“Mwenzetu vipi, mbona naona leo una furaha kupita maelezo, au umeshinda jackpot?” Sammy aliuliza kwa shauku huku akimkazia macho Joyce.


“Kapigiwa simu, kipindi chake cha mitindo kimekubaliwa,” Winifrida alidakia huku akiachia tabasamu.


“Kapigiwa simu na nani?” Sammy aliuliza huku akiwa bado ana mshangao, alimkodolea macho Joyce huku akiwa na maswali lukuki kichwani kwake. Joyce alibaki kimya, lakini sasa hakuwa anatabasamu tena!


“Kapigiwa na Madam Norah…” Winifrida alisema bila wasiwasi wowote huku akionesha kufurahishwa sana na hatua ya Madam Norah kumpigia simu Joyce.


Sammy alishtuka kidogo, alibana taya za midomo yake akionekana kuzuia hasira huku akimkazia macho Joyce. Hakuonesha kufurahishwa kabisa na zile taarifa.


“Madam Norah ndiyo habari ya mjini… anamiliki vituo vya radio na televisheni na ana kipindi cha “Madame Norah Show” cha kuhamasisha harakati za wanawake,” Winifrida alizidi kuongea kama ametiwa ufunguo na kumfanya Sammy akunje sura yake, kisha aliondoka taratibu na kuelekea chumbani kwake bila kusema neno.


Joyce alimsindikiza Sammy kwa macho na kushusha pumzi za ndani kwa ndani, kisha aligeuka kumtazama Winifrida huku akiwa amekunja sura yake, alitaka kusema neno lakini akasita.




Joyce alimsindikiza Sammy kwa macho na kushusha pumzi za ndani kwa ndani, kisha aligeuka kumtazama Winifrida huku akiwa amekunja sura yake, alitaka kusema neno lakini akasita.


* * * * *


Saa 2:30 usiku ilimkuta Mr. Oduya akiwa amesimama chumbani kwake mbele ya meza nzuri ya kisasa ya vipodozi maarufu kama ‘dressing table’ iliyokuwa na vioo virefu vitatu vilivyowekwa kuizunguka ile meza na kumfanya mtu ajione mara tatu, alionekana yupo katika harakati za kujiandaa ili atoke.


Mr. Oduya alikuwa amevaa suti ya bei ghali nyeusi aina ya Kenzo, shati jeupe la mikono mirefu na viatu vyeusi vya ngozi, alikuwa anachana nywele zake taratibu huku akijitazama kwenye vile vioo, kisha mikono yake ilianza kurekebisha tai yake ya rangi nyekundu shingoni.


Alionekana kuwa mtulivu sana huku akiwa amezama katika lindi la fikra, hata hivyo, alikuwa makini akimtupia jicho la wizi mkewe, Dk. Salma Oduya aliyekuwa amesimama kando yake akimtazama kwa makini huku amekunja sura yake.


Dk. Oduya alikuwa mwanamke mnene wa wastani, hakuwa mfupi wala mrefu bali alikuwa na kimo cha wastani na rangi ya maji ya kunde iliyokuwa ina mng’aro wa aina yake.


Akiwa na umri wa miaka hamsini na tano, alikuwa Mhadhiri Mwandamizi wa Sheria katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na mama wa watoto wawili: Omari Oduya aliyekuwa na miaka 30 na kwa wakati huo alikuwa anaishi nchini Marekani, na Zuhura Oduya aliyekuwa na miaka 26 na wakati huo alikuwa anachukua Shahada ya Umahili ya Maendeleo ya Uchumi wa Kimataifa nchini Uingereza.


Usiku ule Dk. Oduya alikuwa amevaa nguo nyepesi ya kulalia maarufu kama ‘night dress’ ya rangi ya samawati na alijifunga kitenge kiunoni, juu alivaa sweta la mikono mirefu na kichwani alikuwa amevaa kofia laini maalumu kwa kukinga nywele.


Muda ule wa saa mbili na nusu usiku upepo ulikuwa unavuma na kutengeneza sauti ya mvumo wa kustaajabisha kwenye matawi ya miti mikubwa ya kivuli iliyozunguka jumba la kifahari la Mr. Oduya, kadiri matawi ya miti yalivyocheza huku na kule kwa utulivu ndivyo mvumo ule ulivyosikika na kutengeneza sauti kama ya chatu mkali aliyehisi hatari kichakani.


Upepo ulivuma ukayasonga songa mapazia marefu yaliyokuwa yamefunika madirisha mawili makubwa mle chumbani.


Jumba la Mr. Oduya ambalo lilistahili kuitwa kasri, lilikuwa katika eneo la ufukweni mwa Bahari ya Hindi, Mbezi Beach, eneo lililokuwa na makazi ya watu wenye ukwasi mkubwa au viongozi wa ngazi za juu wa serikali ya Tanzania. Katika eneo lile tulivu yalionekana majumba kadhaa ya kifahari yaliyozungukwa na kuta ndefu na mageti makubwa mbele yake.


Lilikuwa jumba kubwa la ghorofa mbili lenye vyumba saba vya kulala kila kimoja kikiwa na maliwato yake, sebule tatu kubwa, kumbi mbili za chakula, majiko mawili ya kisasa, kaunta ya baa iliyokuwa katika sehemu ya chini ya jengo na sehemu mbili za ghorofani za kubarizi zenye kochi safi za sofa.


Eneo lile lilikuwa na barabara pana ya lami yenye usafi wa hali ya juu, iliyopandwa miti mizuri ya kivuli kando ya barabara. Muda ule wa usiku eneo lile lilikuwa na utulivu mkubwa sana huku likimulikwa na taa nzuri zenye mwanga mkali. Ni sauti kali za mbwa waliokuwa wakibweka eneo lile bila sababu za msingi ndizo zilizokuwa zinasikika kwa mbali na magari machache sana yalipita barabarani.


Ndani ya lile jumba waliishi watu kumi, watu wazima wanane na watoto wawili: Mr. Oduya mwenyewe na mkewe Dk. Oduya, ndugu watatu wa familia ya mkewe na watoto wao wawili, wahudumu wawili wa kike wa ndani na mhudumu mmoja wa kiume aliyesaidia shughuli za mifugo na shamba. Pia kulikuwa na walinzi watatu waliolinda kwa kupokezana, lakini hawakuwa wakiishi pale.


Hata hivyo, lile jumba lilikuwa na ulinzi madhubuti kwa kujengewa ukuta mrefu uliofungwa mfumo maalumu wa umeme wa kuzuia wezi juu yake na usiomwezesha mtu yeyote kuona mle ndani.


“Hivi wewe mwanamume, unajua mimi sikuelewi kabisa!” sauti ya Dk. Oduya ilimgutusha Mr. Oduya kutoka kwenye lindi la mawazo.


Muda wote Dk. Oduya alikuwa anamwangalia mumewe akionesha wazi kuwa alikuwa na hasira na sura yake alikuwa kaikunja na kutengeneza matuta madogo usoni.


“Kwa nini hunielewi?” Mr. Oduya alimwuliza mkewe bila kugeuka ingawa alikuwa akimtazama kupitia vioo vya kwenye meza ya vipodozi.


“Eti eeh! Unajifanya huelewi ninachomaanisha!” Dk. Oduya aliongea kwa hasira huku sasa akiwa ameshika kiuno chake kwa mikono yote miwili na kumkazia macho mumewe.


“Hapana naelewa,” Mr. Oduya alimjibu huku akigeuza shingo yake kumtazama kwa makini.


“Unaelewa nini?” Dk. Oduya alihoji huku macho yake yakiwa hayabanduki usoni kwa mumewe.


“Naelewa kwamba hunielewi kabisa!” Mr. Oduya alijibu huku hasira zikianza kuchipua ndani yake.


“Haya wewe endelea tu… huo umalaya wako wa uzeeni utakugharimu siku moja… ila usisahau kutumia condom usije ukaniletea maradhi,” Dk. Oduya alisema huku akishusha pumzi za ndani kwa ndani.


“Naomba tusianze kuharibiana siku, unaropoka tu wala hujui naenda kukutana na kina nani saa hizi, hivi kwa mwendo huu nitaweza kweli kushinda uchaguzi wa urais kama hata kwenda kukutana na washirika muhimu wa kisiasa inakuwa nongwa!” Mr. Oduya alianza kulalamika.


“Wadau gani wa kisiasa? Hivi unaniona mimi mtoto mdogo siyo! Wewe si umetoka huko huko muda huu! Hata hujapumzika vizuri unataka kuondoka tena, eti kuwaona wadau wa kisiasa, ni wadau gani wasiokupa hata muda wa kupumzika na familia yako?” Dk. Oduya alizidi kuhoji,


Mr. Oduya alimtazama kwa makini, akataka kumjibu lakini alisita na kuamua kumpuuza, ni mwanamke aliyeishi naye katika ndoa kwa miaka therathini na moja. Alimchukulia kama mwanamke wa kawaida tu ambaye hakuwa na jipya zaidi ya maneno mengi mithili ya chiriku kila uchao.


Badala yake Mr. Oduya alichukua mkoba wake wa kiofisi na kugeuka, akaanza kupiga hatua za taratibu kuondoka, aliazimia kwenda kuumaliza usiku wa siku ile akiwa na Zainab, mwanadada mtundu mno na aliyekuwa amemuonesha ulimwengu mpya wa mapenzi, pamoja na umri wake mkubwa, alikiri kuwa hakuwa mjuzi kabisa.





Zainab Semaya, mtoto wa ki-Tanga, alikuwa binti mwenye busu za kusisimua sana na kila mara walipomaliza mchezo alimwachia Mr. Oduya maswali kibao na kubaki akijiuliza alijifunzia wapi yale mahaba! Kwani Zainab alikuwa wa aina ya pekee, mwenye majibu yote ya maswali yahusuyo mapenzi.


Hivyo, Mr. Oduya aliona kuwa hakutakiwa kumpa nafasi mkewe aharibu utaratibu mzima wa siku ile wa kwenda kufurahia penzi la mrembo asiyechuja, bibie Zainab, kwani lingekuwa kosa kubwa sana kumwacha alale peke yake wakati alikuja kwa ajili yake.


“Sawa bwana, endelea kunidharau… lakini nakwambia mbio za sakafuni huishia ukingoni,” Dk. Oduya alisema huku akiwa bado kakunja uso wake kwa hasira, alikuwa anamsindikiza mumewe kwa macho.


Mr. Oduya hakugeuka wala kusema neno bali alitoka nje ya chumba kile na kuufunga mlango nyuma yake kisha alizifuata ngazi za kuelekea sehemu ya chini ya lile jumba la kifahari huku akiwa amechefukwa kweli kweli.


Asingeweza kuahirisha safari yake ya kwenda Paradise Club kufurahia maisha na kipenzi cha moyo wake, hakuwa na shaka kuwa suala la mkewe angelimaliza kiutu-uzima kwani alijua namna nzuri ya kumdhibiti.


* * * * *


Saa tatu na ushee usiku Joyce alikuwa amekaa kwenye kona ya kitanda chumbani kwao, alikuwa amevaa nguo nyepesi nyeupe ya kulalia iliyolichora vizuri umbo lake zuri na kuifichua nguo yake nyeusi ya ndani.


Joyce alikuwa ameketi akimtazama mumewe Sammy kwa wasiwasi lakini kwa macho yaliyojaa ubembe wa huba huku akihisi moyo wake ukienda mbio kama saa mbovu! Hata hivyo, moyoni alionekana wazi kusimamia kile alichopanga kufanya na hakuwa tayari kuyumbishwa, kwani aliamini kuwa bahati kama iliyomtokea siku ile haiji mara mbili!


Ni kweli alimpenda sana na kumheshimu Sammy, lakini isingekuwa rahisi kwake kuachana na mpango wake wa kwenda kumuona Madame Norah.


Kilipita kitambo kirefu cha ukimya, Joyce alikuwa akimwangalia Sammy kwa makini. Macho yake yalishatoa taswira ya kilichokuwa moyoni mwake. Alishajua kabisa kuwa mwenzake alikuwa katika hasira, alikasirishwa na jambo ambalo lilikuwa na faida, si kwao wawili bali kwa familia nzima.


Tangu Sammy aliporudi nyumbani na kuelezwa na Winifrida kuhusu simu ya Madame Norah aliyompigia Joyce, alionekana kutokufurahia jambo hilo, kwani siku zote hakukubaliana na mkewe kutaka kuonana na Madame Norah. Alikuwa na wasiwasi kuwa Madame Norah angeweza kumwambukiza tabia zake Joyce.


Muda ule kila mmoja alikuwa na mawazo yake, Sammy alikuwa amejiegemeza ukutani pale kitandani alipokaa na kutazama juu ya dari kwa muda mrefu. Joyce naye alikuwa na mawazo yake, alijaribu kufikiria ni kwa namna gani angemlainisha Sammy akubali kumruhusu kwenda kuonana na Madame Norah.


Kwa hakika ilikuwa kazi ngumu, tena ngumu kweli kweli! Pengine ingekuwa rahisi kwa ngamia kupenya kwenye tundu la sindano kuliko kumlainisha Sammy, maana alikuwa na msimamo thabiti! Sammy alimtazama Joyce kwa makini na kushusha pumzi za ndani kwa ndani.


“Sijakuelewa kabisa, Baba Pendo! Kwa nini hutaki niende kuonana na Madame Norah?” Joyce alimwuliza Sammy kwa mara nyingine tena baada ya kitambo kirefu cha ukimya na kushusha pumzi za ndani kwa ndani.


“Kwani hujaelewa nini katika yote niliyosema?” Sammy aliuliza huku akipitisha ulimi wake kulamba midomo yake iliyoanza kukauka.


“Yote uliyosema ni uvumi tu, hayana ukweli wowote. Mambo mengi dhidi ya Madame Norah ni ya kuzushwa tu, tena yanazushwa na watu wenye wivu, wasiopenda maendeleo yake,” Joyce alisema.


“Ya kuzushwa ki-vipi wakati kila kitu kinajionesha?” Sammy alihoji huku akimtazama Joyce kwa mshangao.


“Mimi siamini! Isitoshe mimi siyo mtoto mdogo useme kwamba naweza kushikiwa akili, ninatambua mabaya na mazuri,” Joyce alisema huku akitingisha kichwa chake taratibu.


“Hata kama huamini lakini kumbuka kuwa hakuna moshi bila moto!” Sammy alisema kwa sauti tulivu akijitahidi kuizuia hasira iliyokuwa imechipua ndani yake.


Joyce alimtazama Sammy kwa makini kwa kitambo kifupi na kushusha pumzi za ndani kwa ndani.


“Usidhani kuwa nazuia maendeleo yako bali nafanya hivi kwa sababu nakupenda…” Sammy alisema huku akijiweka vizuri pale kitandani.


“Unafanya hivi kwa sababu una wivu. Kwa sababu Madame Norah ana misimamo juu ya wanaume na anaelimisha wanawake!” Joyce alisema kwa unyonge huku akiinamisha kichwa chake kutazama chini. Sammy alishtuka sana, hakutegemea jibu kama lile kutoka kwa mkewe.


“Sijawahi kukudharau hata siku moja na wala sifikirii kuja kukudharau, lakini nalazimika kufuata ndoto zangu,” Joyce alisema na kuinua uso wake kumtazama Sammy.


Sammy alionekana kuchukizwa sana na ile kauli, alikunja sura yake na hasira ikaanza kuibuka upya ndani yake. Alikunja ngumi ya mkono wa kushoto na kwa kutumia vidole viwili; kidole gumba na kidole cha shahada akaibana pua yake na kuvuta hewa ndani kama aliyekuwa anavuta kamasi.


Joyce aligundua kuwa alikuwa amemuudhi sana mumewe, aliamua kumsogelea na hapo hapo mikono yake yote miwili ikaanza kufanya ziara kwenye mwili wa Sammy, huku mkono wa kulia ukienda moja kwa moja kwenye kifua chake na kuanza kukipapasa kile kifua chenye vinyweleo vingi.


“Can you please stop this?” Sammy alisema kwa sauti iliyoonesha hasira huku akikunja sura yake, pumzi zake zilianza kumpaa.


“Stop what?” Joyce aliuliza huku akimwangalia Sammy moja kwa moja machoni.


“Niangalie machoni,” Joyce alisema kwa sauti ya upole na kwa utulivu mkubwa huku akiendelea kumpapasa kifuani kwake. Sammy akamwangalia. Wakaangaliana kwa sekunde kadhaa, Sammy akakiona kile ambacho hakutarajia kukiona katika macho ya Joyce.


“Nisamehe sana mume wangu, sikukusudia kukukwaza wala kukuhuzunisha, unajua ni kiasi gani nakupenda sana na kukuheshimu, lakini sijui kwa nini wewe hutaki kuniamini!” Joyce alisema kwa sauti ya mhemo huku mikono yake ikiendelea kujivinjari kwenye mwili wa Sammy.


Sammy hakusema neno bali alibaki kimya huku akifumba macho yake kuusikilizia ule mpapaso wa mikono ya Joyce kwa makini. Hata hivyo, Joyce hakusubiri jibu la Sammy, alipeleka mkono wake wa kushoto ndani ya bukta ya Sammy na kuanza kuvinjari eneo la ikulu huku mkono wa pili ukienda moja kwa moja mgongoni.




“Niangalie machoni,” Joyce alisema kwa sauti ya upole na kwa utulivu mkubwa huku akiendelea kumpapasa kifuani kwake. Sammy akamwangalia. Wakaangaliana kwa sekunde kadhaa, Sammy akakiona kile ambacho hakutarajia kukiona katika macho ya Joyce.


“Nisamehe sana mume wangu, sikukusudia kukukwaza wala kukuhuzunisha, unajua ni kiasi gani nakupenda sana na kukuheshimu, lakini sijui kwa nini wewe hutaki kuniamini!” Joyce alisema kwa sauti ya mhemo huku mikono yake ikiendelea kujivinjari kwenye mwili wa Sammy.


Sammy hakusema neno bali alibaki kimya huku akifumba macho yake kuusikilizia ule mpapaso wa mikono ya Joyce kwa makini. Hata hivyo, Joyce hakusubiri jibu la Sammy, alipeleka mkono wake wa kushoto ndani ya bukta ya Sammy na kuanza kuvinjari eneo la ikulu huku mkono wa pili ukienda moja kwa moja mgongoni.


Sasa endelea...


Wakati akiendelea kumpapasa, Sammy aliamua kuvunja ukimya huku akimtazama Joyce usoni.


“Joyce!” Sammy aliita kwa sauti tulivu.


“Abee, mume wangu,” Joyce aliitikia kwa sauti laini iliyokuwa na kila aina ya kiashiria cha kuhemkwa na tamaa za kimwili.


“Nimekuelewa,” Sammy alisema huku akihema kwa nguvu.


“Kweli?”


“Ndiyo.”


Joyce alitabasamu, mikono yake iliendelea kujivinjari kwenye mwili wa Sammy, macho yake bado yalikuwa usoni kwa Sammy yakimwangalia kwa makini, Sammy naye alikuwa akimwangalia Joyce kwa makini. Macho ya Joyce yalipepesa, kope zikacheza kidogo kuruhusu usafi wa macho yake. Kisha taratibu alianza kufumba macho yake.


“Nenda kazime taa,” Sammy alimwambia Joyce huku akijinyoosha na kujilaza chali kitandani, alionekana kusubiri kile ambacho kila mmoja wao alikihitaji kwa wakati huo. Joyce aliinuka haraka na kwenda kuzima taa.


Muda mfupi uliofuata walikuwa wamehama kabisa kutoka katika sayari hii, wakajikuta wakiwa katika sayari nyingine ya mbali, sayari ya mahaba mazito yenye kila aina ya vionjo vya kumtoa nyoka pangoni.


_____


Ilikuwa imetimu saa sita na nusu za usiku, Sammy na Joyce walikuwa wamelala kitandani na kupitiwa na usingizi mtamu wa uchovu baada ya kwenda mizunguko miwili iliyowafanya washindwe hata kujimudu, wote walikuwa hoi.


Sammy alikuwa amelala chali na Joyce alikuwa amelala kifuani kwake kama kifaranga cha kuku kilichokuwa kimekumbatiwa na mama yake. Mguu wake mmoja ulikuwa katikati ya mapaja ya Sammy huku mkono wake mmoja akiwa ameuzungusha shingoni kwa Sammy na alikuwa akikoroma kwa sauti hafifu ya uchovu.


Mara mlango wa chumba chao ulianza kugongwa taratibu, Joyce alishtuka na kufumbua macho yake kivivuvivu, alimtazama Sammy usoni kisha alinyanyua kichwa chake na kugeuza shingo yake kutazama kule kwenye mlango huku akipiga miayo ya uchovu.


Alijaribu kumpuuza mgongaji wa mlango na kukilaza tena kichwa chake kifuani kwa Sammy, lakini mlango ulizidi kugongwa, safari hii uligongwa kwa nguvu zaidi na kusababisha kero masikioni mwake. Joyce aliposikiliza kwa makini aliweza kuisikia sauti ya Winifrida nje ya mlango ikiita kwa hofu.


Kabla hajajua cha kufanya, yeye na Sammy kwa apamoja walijikuta wakikurupuka kutoka pale kitandani na kusimama kwa wasiwasi huku wakilitupa shuka walilokuwa wamejifunika. Walitazamana lakini hakuna aliyekuwa na jibu.


Winifrida aliendelea kugonga mlango huku akiwaita kwa nguvu, Joyce alichukua haraka khanga yake akajifunga kifuani na kuelekea mlangoni akiwa na wasiwasi, wakati huo Sammy alikuwa 

ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog