Search This Blog

Thursday 23 March 2023

MSAKO WA MWEHU - 1


IMEANDIKWA NA :  BADI M. BAO
*********************************************

Simulizi : Msako Wa Mwehu

Sehemu Ya : Kwanza (1)


SURA YA KWANZA

Idara ya magonjwa ya akili, Hospitali ya Taifa Muhimbili
Gangaganga ya mganga humwacha mgonjwa na matumaini, jitihada ya kutatua tatizo humpa mwenye tatizo tumaini. Bi Mwantumu Haji alikuwa amepatwa na maswahibu ya ulimwengu. Tatizo lililompata alijiona kama kaibeba dunia nzima mgongoni mwake. Ilikuwa ni majira ya saa tatu za asubuhi tulivu, iliyopambwa na mwangaza usioumiza wa jua ambalo lilikuwa tayari limeshachomoza upande wake wa mashariki, Bibi huyo alikuwa amekaa kwenye kiti na baadhi ya watu wengine akisubiria kuingia kwenye chumba cha daktari kilichopo kwenye bloku la hospitali ya Muhimbili, idara ya magonjwa ya akili.

Uso wake tu ukimuangalia ulionyesha ana jambo limemsibu, kwani daima dumu barua ya moyo husomwa juu ya panda la uso la mtu. Mtu akiwa na hali ya furaha au huzuni yote husomeka kwenye uso wake. Alikuwa amewasili katika hospitali ya taifa ya Muhimbili tokea muda wa jogoo la kwanza kuwika akimleta mtoto wake wa kiume anayeitwa "Masoud Masoud" maarufu kwa jina la Maso Maso” aliyerukwa na akili usiku huo wa manane uliopita.

Naam "Maso Maso" sasa kawa kichaa, mwehu, mwendawazimu, majinuni, akili zake zimetadathali, vyovyote utakavyopenda kutamka, lakini "Maso Maso" sasa akili zake ni maji kupwa na maji kujaa. Mgonjwa huyo alilazwa katika wodi ya wagonjwa wa afya ya akili katika Hospitali Taifa ya Muhimbili.

Mara ikasikika sauti toka kwenye kipaza sauti cha mhudumu wa zamu, mgonjwa mwenye kadi namba 10 aelekee kwa daktari chumba namba 02. Lilikuwa ni tangazo lililoleta faraja kwenye moyo wa Bi Mwantumu hasa ukichukulia yupo hapo hospitalini kwa zaidi ya saa sita tokea saa tisa za usiku na sasa saa tatu na dakika saba za asubuhi ndio anapata nafasi ya dhahabu aliyokuwa anaisubiria kwa hamu ya kuonana na daktari.

Bila simile, Bi. Mwantumu na uzee wake wa miaka 65 akajinyanyua kwa tabu pale kitini pake alipokuwa amejipweteka na kuingia kwenye chumba cha daktari bingwa wa Afya na Magonjwa ya Akili wa Hospitali ya Taifa Muhimbili. Alipokelewa kwa uso wa bashasha na tabasamu toka kwa Dokta "Alshad Mpenumbe". Alikuwa ni daktari wa hospitali hiyo mwenye uzoefu wa zaidi ya miaka 20 sasa, na umri wake alikuwa ndio anaingia kwenye rika la uzee wa makamo, wa miaka 55.

Karibu sana mama yangu, na pole na matatizo yalikuwa ni makaribisho ya Dokta Mpenumbe kwa Bi Mwantumu. Ahsante mwanangu nimeshapoa, matatizo tumeumbiwa wanadamu hatuna budi kuyapokea na kuyakabili kwa subira na stahamala kubwa alijibu kwa unyenyekevu Bi Mwantumu huku akijiweka vizuri kitini. Samahani naomba hiyo kadi yako alisema Dokta Mpenumbe. Bi Mwantumu akajibu kwa vitendo kwa kunyoosha mkono wake wa kulia kuikabidhi kadi kwa daktari apate kuisoma.

Ukapita muda kama wa rakaateni, muda ambao Dokta Mpenumbe alikuwa ametingwa na kuandika andika kwenye kompyuta yake ya mezani kisha, akamaliza akavua miwani yake akaiweka pembezoni mwa kompyuta yake, akaitoa hanchifu yake nyeupe kutoka kwenye koti lake jeupe alilovaa, akajifuta kwenye macho akajikohoza kidogo kulisafisha koo lake na kuanza mazungumzo na Bi Mwantumu.

Daktari: “Eheemwanao Masoud hili tatizo lake la akili limemuanza lini"?. Lilikuwa ni swali lililovunja ukimya uliopita baina yao kwa dakika kadhaa.

Bi Mwantumu: "Jana kuanzia saa mbili usiku alikuwa anazungumza mambo mchafukoge mara anasema kuna watu wapo nje ya nyumba wamekuja kumchukua. Wakati mwingine anasema amepigiwa simu na Rais kuwa ameteuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa. Ila ilipofika saa sita usiku, ndio akaanza kufanya fujo na kuvunja vitu vya ndani anataka tumruhusu atoke nje ya nyumba."

Daktari: "Kwenye ukoo wenu au familia yenu ameshawahi kutokea mgonjwa wa afya ya akili"? Bi Mwantumu: "Billahi wa Rasuli hakuna mtu huyo kwenye ukoo wetu, sio upande wangu wala upande wa marehemu mume wangu." alitoa kiapo kwa kutumia kidole chake cha shahada kukwangua juu ya koo lake kuweka msisitizo wa maneno yake.

Daktari: "Mwanao, ni Mwanachuo au Muajiriwa?"
Bi Mwantumu: "Mwanangu amemaliza Chuo mwaka juzi, Shahada ya Uhandisi huko nchini Uingereza, na mwaka huo huo akapata kismati cha kazi nchini Saudi-Arabia, lakini akaacha ghafla kazi, sasa ana miezi kama 6 yupo tu nyumbani, na wala hajatuambia kilichomsibu huko alipokuwa mpaka akaacha kazi."

Daktari: "Je mwanao, ni mtu wa kujichanganya na marafiki na je ameoa au kuwa na rafiki wa kike?"
Bi Mwantumu: "Zamani kabla hajasafiri kwenda masomoni Uingereza alikuwa mtu wa watu, mpenda marafiki. Nyumbani kwangu walikuwa hawakauki marafiki zake kama maji ya kisima, lakini tokea arejee masomoni akawa ni mtu wa kujitenga tu, hana marafiki na hata sijawahi kusikia wala kumuona yupo na rafiki wa kike tokea amebaleghe. Na nimemzaa akiwa ni mzima wa afya jogoo linapanda mtungi"

Daktari: (Akatabasamu kwa jibu la Bi Mwantumu akifurahishwa na msisitizo aliouonyesha kuthibitisha mtoto wake sio hanithi). "Sasa mama yangu, vipimo vya maabara vimerudi, mtoto wako hana malaria wala ugonjwa wowote ule. Maana mwanzoni nilihisi huenda malaria yamepanda kichwani, lakini hana malaria. Kutokana na maelezo yako, mtoto wako ana ugonjwa wa akili kitaalamu tunauita Schizophrenia. Huu ni miongoni mwa magonjwa makubwa ya akili. Jina hilo limetoholewa kutoka katika lugha ya Kilatini ambayo ni maneno mawili "Schizo" na "Phrenia". Mgonjwa anayeugua ugonjwa huo anakosa muunganiko kati yake na akili yake", akaweka kituo kidogo cha maelezo yake Dokta Mpenumbe kwa kumeza mate kisha akaendelea kuelezea.

"Kwa kawaida binadamu huwa na hisia tano muhimu, ambazo ni za kuona, kugusa, kuonja, kusikia na kunusa. Mtu aliyechanganyikiwa kutokana na ugonjwa huu anaweza kuona, kuhisi, kunusa, kugusa au kusikia vitu ambavyo wengine hawaoni, kuhisi wala kusikia. Mgonjwa anaweza kusema anaona simba anapita eneo ambalo mmekaa naye, lakini nyie msimuone au anasikia sauti na watu wanazungumza habari zake, wanamshurutisha au wanamtisha lakini nyie hamuoni wala hamsikii chochote". Machozi yalikuwa yanamchuruzika churururu bila kikomo Bi Mwantumu pindi alipokuwa anasikiliza maelezo ya daktari kwa umakini mkubwa.

Bi Mwantumu: "Sasa kitinda mimba wangu kweli atapona daktari"? Nieleze ukweli usinifiche kitu kabisa" alikatisha mazungumzo ya daktari kwa kuuliza swali kisha akaanza kutoa kilio cha sauti ya uchungu.
Daktari: "Mama, huwa tunatumia njia tatu kuwatibu wagonjwa wa akili ambazo ni za kibaiolojia, kisaikolojia na kijamii. Hivyo shaka ondoa mama yangu"

Bi Mwantumu: "Nashukuru sana Daktari, Mwenyezi Mungu akubariki na kukupa afya uendelee kutupa huduma wahitaji".
Daktari: "Sawa, mama yangu, tutajuzana kinachoendelea. Tutamlaza kwa siku kadhaa ili tuzidi kuangalia maendeleo yake".

Bi Mwatumu akanyanyuka na kutoka nje ya ofisi ya Daktari. Akaelekea kwa keshia kwenda kufuatilia bili yake ya matibabu ya mwana wake ili apate kufanya malipo.


"Mimi ndio "Maso Maso" msela toka Sinza kwa wajanja. Nyie Watanzania maboya tu, unakuta Mbunge anakuhonga buku tano umpigie kura, halafu unamchagua kwa miaka mitano, maana yake kila mwaka mmoja amekununua kwa buku". Ha..... Ha.....Ha.....Ha.......mazwazwa sana nyie watu tembeeni duniani mfunguke akili. Kutwa mnashindia "chips-dume" na maji, maziwa kwa watoto wenu hawanywi mpaka wanywe sumu, tokea wakiwa shule ya vidudu akili za kugundua ndege na magari kama wazungu mtapata wapi sasa, wakati watoto wa wenzenu Ulaya wanashiba baga kwa maziwa. Viongozi wenu nao ni janga la kitaifa, watoto wao wanawasomesha shule za kuzungumza "Yes... Yes.. Mzungu kala mafenesi" mpaka anamaliza chuo kikuu huko Ulaya mtoto kagharimu milioni mia tatu.

Afu anarudi 'Bongoland' kugombania ajira na watoto wa akina yahe waliosoma shule za kata. Ambao gharama zao mpaka chuo kikuu haifiki hata milioni moja. Hizo akili au matope!. Ukiwekeza kwa mtoto wako milioni mia tatu, basi muandalie mazingira ya kuja kuendeleza kampuni zako za mabilioni na sio kuja kuajiriwa kwa kamshahara cha laki nne na watoto wa walalahoi". Ha.... ha.... ha... ha.... sogeeni hapa mpate elimu kitaa bure, mupate rai tumbitumbi zenye mafundisho.

Wakulima wenu nao majanga tupu, shamba lake, mbegu za kwake, kupanda, palizi zote kwa gharama zake lakini akivuna mazao yake, serikali inaanza kumpangia sijui Ooh...usiuze nje ya nchi, huo ni unyonyaji mbona Wafanyabiashara hamuwazuii kuuza bidhaa zao nje ya nchi, mbona watumishi wa umma hamuwapangii matumizi ya ndururu zao za mwezi!.

Ningekuwa Rais wa nchi wagonjwa nyie mngekula bata tu, sio viporo mnavyoletewa na ndugu zenu. Dripu zingekuwa za juisi na sio za maji kwani nyie mmekuwa samaki... Ha...Ha..Ha....Ha....! "

Wakati Masoud anaendelea kubwabwaja mbovu, akasikika nesi mmoja anamuongelesha mwenzake, "Huyo ndio Masoud bana akianza kumwaga sera hapo ni usiku kucha mtakesha nae na kuna wakati anaongea vitu vya msingi hata sisi wenye akili timamu hatuwezi kuviwaza".

"Afu nasikia kasomea Uingereza ana Shahada ya Uhandisi, labda karogwa maana familia zetu za kiswahili nazo ni shida, wana roho ya tukose wote. Wanapenda wote tufanane hali zetu za maisha, wote tuwe wali deni mchuzi karadha. Babu dobi, Baba muuza kahawa, Mjomba fundi seremala, Shangazi kazi yake mchambaji kwenye "kitchen party", Mama mchoma vitumbua, hivyo ndivyo wanavyotaka. Akitokea mmoja tu anataka kujifanya msomi msomi wataanza kumpiga tunguri mpaka atakoma", nesi mwenzake nae alichangia kusherehesha mazungumzo yao.

"Madame Neesi eeh....Madame Neeesi....!, Nataka kwenda chooni kujisaidia, au nijisaidie hapa hapa wodini, mie sioni noma fumbeni macho tu nimtoe nyoka pangoni hadharani" ilikuwa ni sauti ya Masoud, alikatiza mazungumzo yao waliyokuwa wanateta wale manesi mawili.

"Aaaah.... hapana rafiki yangu Masoud usifanye hivyo, nenda chooni bana, tena leo simuiti mlinzi akusindikize nenda mwenyewe na urudi haraka rafiki" alisema nesi yule akimrai Masoud asijisaidie ndani ya wodi hiyo ya wagonjwa akili. Masoud alikuwa tayari ameanza kufungua mkanda wa suruali yake akitishia kujisaidia tayari.

Masoud akaondoka zake wodini kuelekea chooni kwa mwendo wa chapuchapu. Muda ulikuwa ni saa nne za usiku. Hiyo ndio ikawa ni kwaheri ya kuonana, kama vile kawapa mkono wa buriani, hawakumuona tena. Kwa ufupi Masoud alikuwa ametorokea mtaani kusikojulikana, alichoka maisha ya kufungiwa wodini kama ndege tunduni.


Masoud Masoud au "Maso Maso Mwehu" kama alivyojipachika mwenyewe, aliacha mambo wodini hamkani si shwari kwa kutoroka kwake. Alipoingia chooni alijifungia mlango kwa ndani na kupapachua dirisha dogo la kioo lililopo chooni kisha akavunja nondo zake.
Nesi wa zamu alisubiria arudi, akawa anaona amechelewa. "Huyu amezidiwa ugonjwa huko chooni au amejiua?" ni swali alilokuwa anajiuliza nesi huyo aliyetoa ruksa kwa hofu.
Ndipo alipotoa taarifa kwa walinzi wakaja kuvunja mlango wa chooni ndipo walipokuta kidirisha kimechomolewa. Kila mtu alishangaa na kustaajabishwa na namna alivyopenya dirishani baada ya kufanikiwa kukata vyuma vya dirishani.
"Huyu atakuwa na nguvu za ajabu sana mithili ya Samson wa kwenye Biblia, haiwezekani kwa kutumia mikono na vidole uweze kupindisha vyuma vya dirisha na kufanikiwa kutoroka" aliropoka mlinzi mmoja wapo akiwa ameshikwa na butwaa haamini kama binadamu wa kawaida anaweza kupachua dirisha lile madhubuti kwa kutumia mikono tu bila kifaa chochote.
Daktari wake anayemtibu alivyopita kuzungukia wagonjwa wake asubuhi na mapema ndio akakuta kaachiwa manyoya tu kitandani kwa Masoud. "Utaratibu upo wazi kabisa kuwa lazima asindikizwe popote anapokwenda, sasa ulishindwa nini kumpa taarifa mlinzi amsindikize chooni?" Dokta Mpenumbe alikuwa anaongea kwa hamaki huku anafoka.
Yule nesi wa watu masikini ya Mungu akawa hana cha kujitetea wala pakushikilia, amejiinamia kama zoba ulikuwa ni uzembe wake kazini.
"Sasa naomba uniandikie barua ya maelezo ya utetezi kwanini nisikufikishe kwenye vikao vya nidhamu uchukuliwe hatua haraka sana, kukomesha tabia hii mbaya iliyomea ya uzembe kazini" Daktari alitoa maagizo kwa nesi yule wa zamu, ambaye alionekana amegwaya na anajuta kwa uzembe wake lakini majuto daima ni mjukuu na maji yakishamwagika hayazoleki tena. Nesi yule alitamani muda urudi nyuma aweze kurekebisha kosa lake alilolifanya lakini alikuwa ameshachelewa, "Maso Maso" mwehu kashatimka zake mtaani.
Bi Mwantumu alijihimu alfajiri na mapema jogoo la pili akiwa ameambatana bega kwa bega na shoga yake Bi Mwazani wakiwa na kapu lao kubwa ndani yake kuna chupa yao kubwa ya chai ya maziwa na mapochopocho, michapalo kedekede kwa ajili ya mgonjwa. Wakiwa hawajui yaliyompata mtoto wao hospitalini usiku wa kuamkia leo yao. Walipofika nao wakakutana na taarifa za kutoweka kwa mtoto wao Masoud.
Bi Mwantumu alikuwa hashikiki kwa kilio cha kwikwi, "mwanangu eeeeeh.......Masooo mwanangu unateseka babaaaa...upo wapi babaaa eeeeeeh...unakula nini huko ulipo.... umelala wapi sasa mwanangu,..... nguo za kuvaa utapata wapi woooohi woooooohi.... uchungu mama tumbo la uzazi uchungu mamaaaaaa... Wooooh" kilio mtindo mmoja kama vile yupo msibani.
"Shoga nilikuambia hukunisikiza ukayataka matibabu ya kizungu, huyu katupiwa jini tu, tungewahi kwa mtaalamu sasa angekuwa mzima wa afya. Jisaidie Mungu akusaidie, mambo yenu ya kudharau mila zilizotulea ndio matokeo yake haya. Kiatu cha mtoto hakimponyi mama mbigili. Njia unazotumia kumponya mtoto wako haziendani na uhalisia shoga yangu, ulikuwa ni ushauri wa Bi Mwazani kwa shoga yake, huku akiongea kwa hisia kali na uchungu mkubwa.
"Shoga nimekuelewa sasa ama zao au ama zangu, wabaya wangu wamenibipu sasa mimi nina wapigia simu wakae mkao wa mapambano", tusiombane poo tu" Bi Mwantumu alijibu, majibu ya kukubaliana na ushauri wa shoga yake wa kufa na kuzikana, tokea utotoni na unyago wamechezwa na kungwi mmoja, huko kijijini kwao Utete, Rufiji.
Bi Mwantumu na rafiki yake waliondoka zao kurejea nyumbani kwao, baada ya kupewa taarifa na daktari kuwa juhudi zote za kumsaka mwehu "Maso Maso" kila kona zimegonga mwamba. "Mama tunasikitika kukutaarifu kuwa tumeshindwa kumpata, unaweza kwenda polisi upate msaada wa kumsaka mwanao Masoud" yalikuwa ni maneno yake kuaga ya Dokta Mpenumbe kwa Bi. Mwantumu.

Shekhe Abeid Mbonde alikuwa maarufu Rufiji nzima na vitongoji vyake kutokana na kazi ya upigaji ramli. Alikuwa anaishi kijiji cha Mkongo kilichopo kama makadirio ya umbali wa kilometa 4 kutoka mto Rufiji. Zamani kijiji hicho ndio ulikuwa Mji mkubwa wa Wilaya ya Rufiji. Kijiji hiki umaarufu wake unatokana na kuwa ndipo yalipo Makao Makuu ya Mamlaka ya Maendeleo ya Bonde la Mto Rufiji "Rufiji Basin Development Authority" (RUBADA).
Shekhe Mbonde kazi yake ya kupiga ramli au kusaga mkungu hiyo ndio kazi ambayo ilimpatia umaarufu mkubwa mpaka watu walifunga safari toka pande mbalimbali za dunia kuja kupata huduma yake. Umri wake sasa alikuwa ni shaibu wa miaka 80 na ushee. Alikuwa anaogopwa haswa ikisemekana anafuga Majini anaowatumia kwenye kazi zake za uganga.
Bi Mwantumu na shoga yake Bi Mwazani asubuhi ya saa nne iliwakuta wamekaa kwenye jamvi wakisubiria huduma ya Shekhe Mbonde. Walirauka alfajiri na mapema na basi linaloelekea Rufiji wakipandia Mbagala kuu. Bi Mwazani alijifunga kibwebwe kuhakikisha mtoto wa rafiki yake anayesakwa kwa hali na mali anarudi katika uzima wa afya yake ya akili.
Hawakupata tabu sana kufika nyumbani kwa Shekhe kwa sababu nao pia kwa asili ni Wandengereko walikuwa wanasikia sifa za Shekhe Mbonde tokea wakiwa wanawali wabichi kabisa. Walipofika walikuta kadamnasi ya watu wamejazana kwenye msambweni wa nyumba ya mtaalamu huyo.
"Shosti hapa kwa Shekhe Mbonde ndio Kigoma mwisho wa reli, kuwa na matumaini mwanetu Masoud amepatikana na amepona tayari ondoa mashaka atafanyiwa ruzuna atakuwa mzima wa afya" Bi Mwazani alivunja ukimya kwa kuanzisha mazungumzo kwa shoga yake. "Nashukuru sana shoga ama kweli akufaaye kwa dhiki ndio rafiki wa kweli, wengi wa marafiki ni mafarisayo ila wanajifanya wema machoni pa watu" alitoa shukrani za dhati Bi Mwantumu kwa shoga yake huku akiwapiga kijembe marafiki zake wengine
"Kikulacho kinguoni mwako, wapo majirani zetu hata kukujulia hali kwa matatizo haya uliyopata hawajaja, pengine ni wahusika wanaona haya kukuangalia usoni" Bi Mwazani alizidi kuchochea kuni za fitina kwa majirani wenzake ili yeye aonekane peke yake ndio mwema.
"Leo ndio fainali, hapa mganga akipiga bao akanionyesha fulani ndio mbaya wangu, sitosikia la mwadhini wala la mteka maji msikitini, tutagawana majengo ya serikali nakwambia mimi naenda Segerea yeye anaenda mochwari Muhimbili." alipandisha mzuka wa hasira Bi Mwantumu.
"Haya haya aliyebakia bado kutanguliza kishauzu cha Shekhe afanye haraka kabla hajafungua kazi" ilisikika sauti ya msaidizi wa mganga. Msaidizi huyo alikuwa anapigia debe advansi anayolipwa mganga kama sadaka, unatoa yoyote ile unayoguswa nayo.
Bi Mwantumu akatumbukiza elfu hamsini taslimu kwenye kapu la mganga lilipopitishwa usoni pake. Akabaki anasubiria kwa hamu zamu yake ifike aingie kwenye kilinge cha mganga akatapike yanayomsibu.

"Woooooh...wooooooh........woooooh....paachiiithhhh... chi...chi.... chi..... paraka parakata paaaah... pepo mchafu mama mwanao ametupiwa, amepatwa na shonga, amekuwa kichaa kweli si kweli? " aliulizwa Bi Mwantumu akiwa amekaa juu ya kinu cha Shekhe Mbonde aliyekuwa amekaa kwenye jamvi akizungumza maneno ya kurogonya baada ya kupandisha ruhani wake kichwani.
"Tawile mganga tawile" alijibu Bi Mwantumu huku anahema juu juu kwa huku fundo la hasira limejikusanya kooni kwake kwa wabaya wake. "Kapotelea mtaani hajulikani alipo sawa sawa mama?" aliendelea kuuliza ramli yake Shekhe Mbonde. "Tawile Shekhe tawile nimewakosea nini hawa walimwengu mimi jamani, unalala nao, unakula nao lakini kumbe ni wabaya wako" akawa analalamika Bi Mwantumu kwa sauti ya juu huku anamwaga mchozi wa nguvu.
"Usilie mama, hapa ndio mwisho wa matatizo umefika, wabaya wako mwisho wao umefika, ukisikia mwana wa Mbonde fimbo ya chuma kwa wachawi ndio mimi, viongozi wengi wa serikali mimi ndio kamati yao ya ufundi, ndio nawapangia nini cha kuvaa na siku gani, ndio nawapangia hotuba za kuzungumza mbele ya kadamnasi ya watu ha.... ha... ha... ha...." aliongea kwa sauti ya kujigamba huku anachezea tasbihi mkononi mwake. Shekhe Abeid Mbonde alikuwa tayari ameshamuingiza kwenye kumi na nane zake Bi Mwantumu hachomoki tena.
"Sasa chukua kipande cha kanga hiki, na hii sarafu ya Mjerumani uishike mkononi. Uende msalani kuoga, ukishaoga tu usijifute maji uivae mara moja hiyo kanga kisha uikumbate hiyo sarafu uanze kunuiza unayotaka kwa wabaya wako na kwa mema unayotaka kwa mtoto wako". Bi Mwantumu akawa ananyanyuka kwenye kinu na kuelekea bafuni, huku Shekhe Mbonde jicho limemsimama dede kukodolea mirindimo ya makalio ya Bi Mwantumu yanavyotikisika alikuwa amevalia vazi teketeke la dela.
Waswahili wanasema huba mwanzowe jicho, Shekhe moyo ulikuwa unamwenda mbio kama ametumia Mkuyati wa kuongeza nguvu za kiume au amekunywa kikombe cha Alkasusu.
"Afanalek! Mwenyezi Mungu ni fundi wa kuumba mashallah.....fatabaaraka llahu ahsanul-khaaliqiina" alijikuta Shekhe Mbonde anaropoka bila kujijua kusifia uumbaji kwa kutumia maneno ya kiarabu. Tayari alishachanganywa na umbo sotojo sotojo, laini laini la Bi Mwantumu ambaye licha ya umri wake kumtupa mkono wa miaka 65 lakini bado alikuwa ana mvuto.
Kwanini asiwe na mvuto wakati hajawahi kufanya kazi ngumu maishani mwake zaidi ya kuwa ndani kukatakata vitunguu na nyanya za kumpikia biriani na pilau marehemu mumewe ambaye alikuwa ni Mfanyabiashara mwenye pesa sufufu Jijini Dar es Salaam. Baada ya dakika kama 10 kupita, Bi Mwantumu akawa anarejea kutoka msalani huku akiwa amejifunga upande wa kanga kuu kuu iliyo nyepesi.
Ilikuwa imemgandia mwilini kanga hiyo vilivyo ikilichora umbo lake nene, akitembea huku nyonga zake zikijionyesha namna zilivyoumuka kama mikate iliyosusiwa hamira na mpishi.
Mganga Shekhe Mbonde udhaifu wake mkubwa ulikuwa wanawake vibonge, tipwatipwa, wenye miili laini. Wakeze wote kwenye ndoa yake ya mitara aliowafanyia nikaha ukiwaangalia nyuma wamejazia msondo wa nguvu. Hajawahi kuoa tokea ujanani mwake mpaka uzeeni, mwanamke kimbaumbau mwiko wa pilau.
Na wote aliwapata kupitia kazi yake ya uaguzi, "kuku hula sawa na mdomo wake", hivyo wateja wake wanawake ndio walikuwa mboga yake rahisi kuwinda. Tayari Bi Mwantumu alishajiingiza kwenye rada za Shekhe Mbonde ilikuwa ngumu kwake kuchomoka.




Mganga Shekhe Mbonde udhaifu wake mkubwa ulikuwa wanawake vibonge, tipwatipwa, wenye miili laini. Wakeze wote kwenye ndoa yake ya mitara aliowafanyia nikaha ukiwaangalia nyuma wamejazia msondo wa nguvu. Hajawahi kuoa tokea ujanani mwake mpaka uzeeni, mwanamke kimbaumbau mwiko wa pilau.
Na wote aliwapata kupitia kazi yake ya uaguzi, "kuku hula sawa na mdomo wake", hivyo wateja wake wanawake ndio walikuwa mboga yake rahisi kuwinda. Tayari Bi Mwantumu alishajiingiza kwenye rada za Shekhe Mbonde ilikuwa ngumu kwake kuchomoka.
"Sasa Bibie....njoo hapa karibu yangu, magoti yako yanatakiwa yaje yagusane na magoti yangu kisomo kiingie vizuri". Ilikuwa ni sauti ya kubembeleza ya mganga Shekhe Mbonde iliyobeba ulevi wa ngono uliotamalaki katika mishipa yake ya damu. Bi Mwantumu akawa anajongea huku anaogopa ogopa anatafuna kidole chake, huku macho yake anaangalia chini kama mwanamwali anayeletwa kutambulishwa kwa wakweze. Aibu ilimvaa hasa ukichukulia chumbani walikuwa wawili tu, na mlango umefungwa.
"Bibi acha uoga, utawakasirisha walimu wangu kichwani, hapa tupo kazini usiwaze mambo mengine, mimi umri wangu sasa miaka zaidi ya 80, mimi ni kisu kidugi hakina makali tena hakikati sina matamanio" aliongea kwa ukali Shekhe Mbonde kumtisha Bi Mwatumu. Bibi wa watu alinywea akawa mdogo hasa baada ya kusikia walimu wake mganga watakasirika, akajua majini hawana masihara watamteketeza, akajikalisha pwetepwete jirani na Shekhe Mbonde huku magoti yake yamegusana na magoti yake, mapaja yote nje.
"Sasa mahabubu tutaanza kuelewana maana ulishaanza kunikasirisha kwa kutonipa ushirikiano, walimu wameagiza ulete ngozi ya goromwe jike ukamkamate kwa mikono yako mwenyewe, ili tutengenezee hirizi utakayovaa kiunoni, na hirizi nyingine utaenda kuchimbia kwenye kizingiti cha mlango. Ukishachimbia saa nane za usiku utasimama kwenye kizingiti cha mlango na kuita jina la mwanao mara saba, atarudi baada ya muda mfupi" alitoa maelezo Shekhe Mbonde huku macho yake yamemtoka kama mjusi aliyebanwa na mlango kuchungulia matiti makubwa ya Bi Mwantumu yaliyojaza kifua mpaka yanataka kupasua sidiria yake ya mchina kutokana na kuelemewa na uzito. Bi Mwantumu alipigwa na taharuki mbili, kwanza kuitwa jina mahabubu, jina ambalo ni la kimahaba na pili ni ngozi ya goromwe huyo ndio mdudu gani!. Ikabidi aulize huyo goromwe ndio mdudu gani na atampata wapi.
"Ha... ha... ha....manti hofu manti hofu kidosho ondoa shaka, kula uliwe bibie, toa msaada usaidiwe, raha ya nyege kunyegezana. Huyo goromwe ni aina ya mjusi anayeishi mtini. Ila ukishindwa kumpata utasaidiwa na mwalimu, nawe utamsaidia anachokitaka" alitoa maelezo Shekhe Mbonde huku akionyesha kabisa lafudhi zake kuna ajenda ya siri ameikusudia kwa Bi Mwamtumu. Bibi wa watu masharti yalikuwa mlima mkubwa kwake kuupanda, kwanza huyo mende tu alikuwa anamuogopa kumuua sasa sembuse akamkamate mjusi tena juu ya mti na uzee wake, ni kutafuta kupanyuka msamba na kukiita kifo kwa makusudi.
Akaomba asaidiwe kupata hiyo malighafi adimu kwa ajili ya kushonewa hirizi itakayomrudisha mtoto wake kipenzi wa pekee mwanaume. Mganga akajitia amepandisha ruhani tena, kisha akatoa maelekezo hiyo ngozi ya goromwe wataipata makaburini saa saba za usiku watamletea. Hivyo ikabidi mipango ya kurejea Jijini Dar es Salaam siku hiyo ndio imekufa tena, inabidi alale hapo hapo kijiji cha Mkongo kusubiria kuletewa ngozi ya mjusi saa saba za usiku huko makaburini.

Ilipofika saa sita kamili juu ya alama, Bi Mwantumu aliamshwa na mpambe wa Shekhe Mbonde na kumpeleka makaburini kama alivyoelekezwa na Shekhe. "Sasa Bibi yangu, hapa masharti utatakiwa uende mpaka kwenye mbuyu ule pale, usaule nguo zote bila kubaki na chochote mwilini mwako, kisha unarudi kinyumenyume mpaka ufike kwenye kaburi lile pale la mtoto mdogo aliyezikwa jana, hapo sasa ukae kitako juu yake, ili mwanao nae afufuke upya. Utatakiwa ujifunike hili shuka jeupe ninalokukabidhi. Ufumbe macho usifungue kabisa baada ya nusu saa utasikia kivumo cha upepo hapo ndio ujue jini linalokuletea ngozi ya goromwe anakuja hivyo chochote atakachokufanyia kwako inatakiwa kuwa hewala tu, usimbishie, alitoa maelekezo na vitisho yule mpambe, huku Bi Mwantumu akitetemeka kwa uoga.
Moyo wake uligawanyika pande mbili, moja ya majuto, anajilaumu kwanini alikubali ushauri wa Bi Mwazani wa kuja kwa mganga. Hakutegemea kukuta masharti magumu namna hiyo yanayoendana kinyume na imani yake ya dini. Lakini upande wa pili wa moyo wake ukawa unamwambia nafasi pekee ya kumuokoa mtoto wake kipenzi "Maso Maso" na kujiokoa yeye mwenyewe ndio hii imewadia. Hivyo asilete masihara atajipoteza yeye mwenyewe na mtoto wake ndio atakuwa mwendawazimu nahaala wa laila.
Bi Mwantumu akafanya kama alivyoagizwa akawa sasa yupo juu ya lile kaburi jipya la mtoto mchanga, huku amejifunika gubigubi shuka nyeupe mithili ya sanda huku anatetemeka kwa uoga. Baada ya kupita kitambo cha takribani kama nusu saa tu, akaanza kusikia mvumo wa upepo mkali uliokuwa unatikisa miti yote ya pale makaburini. Upepo ambao ile shuka aliyojifunika ikawa kama inataka kupeperushwa na upepo.
Ghafla akashtukia kama kuna mtu anamfunua shuka yake anahema kwa nguvu, akaanza kumtomasa matiti yake. Akaanza kutaka kumlaza chini pale kwenye kaburi. Alikuwa hajafungua macho yake na hakumbishia kwa kuhofia kifo chake na kumpoteza mtoto wake Masoud. Wakati yule mtu anampapasa mapaja yake, akasikia kishindo kikubwa cha kama risasi iliyopigwa hewani. "Nyoosha mikono juu, upo chini ya ulinzi kibabu muasherati mkubwa wewe" ilikuwa ni sauti ya mmoja wa kundi la mapolisi, waliokuwa wamevamia makaburini saa saba za usiku kumkamata Shekhe Mbonde. Ilikuwa ni fedheha kubwa kwa Shekhe Mbonde na Bi Mwantumu.
"Wewe Bibi kavae nguo zako haraka sana, nawe upo chini ya ulinzi saa mbaya hizi za usiku makaburini unafanya nini, mpaka miaka hiyo yote uliyonayo na utu uzima bado tu unashinda kwa waganga. Huo ni umri wa kufanya toba kwa Mungu wewe unakuja kwa waganga ingebaki kidogo tu ungebakwa na huyu mganga. Kama hujui bibi huyu anaitwa jina la utani "kikaango", hakichagui mboga, uwe mke wa mtu, uwe bibi kizee maadamu umefungasha tu yeye twende kazi" aliongezea askari mwingine mwanamke, aliyekuwa anamuonea huruma Bi Mwantumu.
Bi Mwantumu akatamani ardhi ipasuke moja kwa moja aingie afukiwe, atoweke kwenye uso wa dunia hii tambara bovu, kukwepa aibu. Akajifananisha na hadithi ya punda kunyimwa pembe akapewa masikio, alipolia choyo akaongezewa mlio.
Ilikuwa ni aibu ya mwaka, habari zilisambaa kwa kasi kijiji kizima ndani ya muda mfupi umati wa watu ukafurika pale makaburini. Waandishi wa habari na makamera yao nao hawakubaki nyuma walikuwa wamefuatana na polisi wale waweze kuripoti tukio hilo. Wakiwa na hasira wananchi hao, wengine wakiwa wamebeba silaha za jadi kama mapanga, mashoka, mundu na zinginezo.
"Tuachieni hao walozi tumalizie kazi hapa hapa" alisikika mmoja wa wananchi mwenye hasira kali. "Biashara zetu haziendi vizuri, faida hatuzioni, hawa dawa yao ni kuchomwa moto tu, kijiji chetu ni kikongwe lakini tumebaki nyuma mithili ya koti, hatuna shule za maana hatuna hospitali bora, sababu ni hawa wanga wakubwa" alisikika mkuda mwingine. "Mke wangu Bi Chausiku alienda kutibiwa kwa hiki kibabu, tahamaki kumgeuza mke wake kimazingara ukimfata kumuhoji anatishia kukutupia majini" alilalama mwananchi mwingine.
Nchi nzima kulikuwa na kampeni ya kuwakamata waganga wa kienyeji wanaopiga ramli chonganishi katika jamii. Mbiu ya mgambo ilipigwa ikiwataka kila mwananchi mwenye taarifa za siri na za dhahiri za mganga anayejihusisha na kupiga ramli chonganishi ajitokeze kuleta taarifa. Serikali itampa ulinzi stahiki na itaficha majina na taarifa za wote walioleta taarifa hizo kulinda usalama wao. Jina la Shekhe Mbonde nalo likatajwa, hivyo akawa kwenye rada za wana usalama.
Bi Mwantumu baada ya kuhojiwa na kufanyiwa usaili wa kina alionekana hana hatia, ila alitakiwa awe shahidi namba katika kesi ya dhulma za kingono dhidi ya mganga feki Shekhe Abeid Mbonde. Baada ya kuachiwa yeye na shoga yake Bi Mwazani wakarejea Dar es salaam vichwa chini. Mambo yao yamekwenda mbagombago kinyume na walivyotarajia. Badala ya kupata faraja wamepata fedheha isiyoelezeka. Hadithi ya jipu kulipuka kugubua donda ikasadifu kwao.
Huku tukio lao zima likiwa limeripotiwa kwenye magazeti, redio na televisheni. Ilibidi amshukuru Mungu na akubaliane na matokeo tu kuwa mtoto wake Masoud Masoud ameshakuwa kichaa na amepotea. Hawezi tena kushindana na alilolikadiria Mola kwake, jitihada haiwezi kushinda kudura. Akawa ni mtu wa kujifungia ndani anaona aibu kutoka nje anahisi kila mmoja atakayeonana nae ameona picha zake za kukamatwa uchi makaburini usiku wa manane. Baada ya miezi kadhaa kupita akazoea akaanza maisha yake kama ya zamani siku zikaanza kusonga.

SURA YA PILI
"Maso Maso, mwehu mtaani"
"Maso Maso.....Msela toka Sinza kwa wajanja, nimezaliwa Ocean Road nitazikwa Kisutu inshallah..... sijaja Mjini kwa mbio za mwenge wala kwa ajili ya kufuata shule, mie ni "Born Town" bana, born here here ha..... ha......haa...teh.... teh....teh.. Haya haya tunaendelea elimu kitaa bila twisheni, nyie akina dada mnanunua magari mazuri sana lakini kila tatizo hata dogo tu unaita fundi, mnaliwa pesa zenu mnapunguza bajeti za pipi za wajomba zangu nyumbani.
Leo nawafundisha kudili na gari yako ikikataa kuwaka. Ukiona haiwaki kwanza kuna uwezekano mkubwa kwamba betri imekufa. Kuna sababu nyingi ya hii kutokea, zikiwemo, labda uliacha taa zikiwaka kwa muda mrefu. Sababu inaweza kuwa nguvu ya betri haiendani na nguvu gari, au betri imeingia maji. Wakati mwingine betri ni ya muda mrefu na imechoka. Woyo Woyo Woyoooooo.....! Huyo alikuwa ni Masoud Masoud mtoto wa Bi Mwantumu akiwa mitaa ya Posta, mwehu amekwisha kazi.
Ilishapita nusu mwaka sasa tokea atoroke wodi ya wagonjwa akili katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Mama yake alishakubali matokeo kuwa mwanawe ni kichaa sasa. Alikuwa amevaa shati lililoraruka kila kona, na suruali yake msurupwete wenye viraka vya kutosha. Mguuni amevalia ndula saizi kubwa kuliko miguu yake. Mkononi amebeba sanduku la chuma la mafundi gereji lililoshiba spana zote muhimu kwa fundi magari.
Kichwani nywele zake zikikuwa hazijapitishwa chanuo yapata miezi sita. Ulikuwa ukimuona tu hauhitaji kuuliza mtu kuhusiana na afya ya akili yake. Alikuwa amejipatia umaarufu maeneo ya Posta yote mpaka kijiwe chake mtaa wa Ghana. Hapo ndio palikuwa kijiwe chake jirani na Wizara ya Mambo ya Ndani pamoja na Makao Makuu ya Polisi.
"Unajua huyu kichaa anazungumza vitu vya ukweli kabisa kuhusu magari, mimi fundi magari nimemkubali sana muda mchache tu niliomsikiliza" alisema mmoja wa watu waliokaa kwenye benchi la fundi viatu karibu kabisa na aliposimama mwehu "Maso Maso" anapomwaga sera zake. "Huyu kijana ni balaa, akili zake zikitulia wanakujaga hapa mafundi magari wa gereji kubwa kubwa hapa mjini kumuuliza maswali" alichangia mada fundi viatu anayejulikana kwa jina la Peter huku akichapa kazi kwa kuvifua viatu vyake vya sabuni, kabla ya kuvipaka dawa ya viatu.
"Kwanini sasa ndugu zake wasimtafutie tiba apone, huyu kijana ni hazina kwa taifa akipona akafunguliwa gereji ataweza kuajiri mamia ya watu" alichangia mada muuza magazeti aliyekuwa anafuatilia mazungumzo yale.
"Nasikia wamehangaika bara na pwani, kwa waganga na waganguzi lakini wameambulia patupu, nasikia katupiwa jini mbaya sana" alizungumza fundi Peter ambaye alikuwa anapenda sana mada za kuchangamsha kijiwe chake ili pavutie wateja waje kupiga kiwi viatu vyao.
"Itakuwa kweli katupiwa jini, maana huyu kijana mie namfahamu vizuri sana tulikuwa tunakaa nae jirani Sinza-A. Huyu alifaulu vizuri sana katika mitihani yake ya kidato cha sita. Alikuwa anasoma shule ya watoto wenye vipaji maalumu vya akili, Mzumbe sekondari. Matokeo yake alipata daraja la kwanza pointi tatu, akaongoza nchi nzima. Alikuwa anasoma mchepuo wa Fizikia, Kemia na Hesabu. Kuna mwarabu mmoja nasikia alipopata taarifa za za kuwa ni yatima, amebaki na mama yake tu naye ni mtu mzima akampa ufadhili wa kusomea Uhandisi huko nchini Uingereza. Sasa toka amerudi huko ndio akaanza kuwa haeleweki eleweki" alichagiza mada hiyo mmoja wa wanunuzi wa magazeti aliyekuwa pia anamfuatilia majinuni "Maso Maso".
"Isijekuwa alitembea na mke wa mtu huko Arabuni wakamtengeneza, maana kuna wakati huwa akikaa hapa pembeni ya duka langu anaimba mashairi yake ya lugha ya kiarabu huwa naambulia ubeti anaourudia mara kwa mara utamsikia "Hoor-ain uhibukki Hoor-Ain I love you, Hoor Ain nakupenda.. " alichangia mada muuza duka anayeitwa Soni ambaye muda mwingi majinuni "Maso Maso" anaketi kivulini kwenye pembe ya kibanda lake la biashara. Mchango wa Soni katika kujadili mada ya uchizi wa "Maso Maso" uliamsha kicheko cha kikwakwa baraza zima, sasa likachangamka.
Wakati mjadala juu yake unaendelea ghafla geti la Wizara ya Mambo ya Ndani likawa linafunguliwa likatoka gari moja aina ya "Land Cruiser v8" rangi ya buluu yenye kibao cha namba za gari "PT" kujulisha ni gari ya polisi. "Maso Maso" alivyoliona tu lile gari akachomoka mbio mbio kulikimbilia, akalipiga mkono likatii amri na kusimama. Akaanza kuongea na yule kigogo wa polisi aliyekaa upande wa siti ya abiria, akachomoa noti ya elfu kumi akampa. "Maso Maso" alivyopewa tu hata hakuaga mbio mbio dukani kwa Soni hata hakukumbuka hata kushukuru. "Naomba mtindi paketi moja, Cocacola moja na maandazi matatu" alitoa oda "Maso Maso" uso wake ukiwa na bashasha.
Alivyopewa tu akachukua bakuli lake chafu chafu akachanganya soda yake, mtindi na akakatia maandazi akaanza kula bila kujali kunawa mikono wa kuosha sahani yake ya chakula. "Masooo..... wewe kiboko aisee mpaka vigogo wa polisi wanakupa saluti, nimeona umepigwa na msimbazi" alitania Soni kumtania mwehu "Maso Maso" baada ya kumpa mahitaji na kuanza kula.
"Wewe mimi sio wa nchi hii, hata Trump Rais wa Marekani atanipigia saluti, hata nyinyi bendera hufuata upepo mtaniimba sana tu tena huku mnalia, nitakuwa maarufu kwenye kila kinywa cha Mtanzania, jiandae tu kunipigia kura kwa hiari au kwa lazima" alijibu "Maso Maso" huku anashushia tumboni mwake mtindi uliochanganywa na soda.




"Wewe mimi sio wa nchi hii, hata Trump Rais wa Marekani atanipigia saluti, hata nyinyi bendera hufuata upepo mtaniimba sana tu tena huku mnalia, nitakuwa maarufu kwenye kila kinywa cha Mtanzania, jiandae tu kunipigia kura kwa hiari au kwa lazima" alijibu "Maso Maso" huku anashushia tumboni mwake mtindi uliochanganywa na soda.
" Unaambiwa yule Inspekta wa polisi anamheshimu sana "Maso Maso", ile gari aliyopanda "v8" wakati imefika ndio ina wiki tu ilipata hitilafu, mafundi wa jeshi la polisi wote walichemka. Ndio mwishoni wakamkumbuka "Maso" kuwa anajua ufundi magari. Walimfata hapa, aliwaletea madahiro kweli kweli maana baadhi ya polisi walikuwa na tabia ya kumpiga piga wakimuona hapa getini. Huyu Bosi wao aliyempa elfu kumi alimbembeleza mpaka akakubali ndani ya dakika 5 tu gari ikawaka na kupona kabisa. Tokea hapo wanamuacha afanye anavyotaka, siku akiamka vizuri anaweza kuingia mpaka kule karakana yao akawasaidia kutengeneza magari. Na siku kichaa chake kikimpanda atamwaga matusi, hamna anayeweza kumsogelea," alieleza fundi Peter tukio la ukaribu wa "Maso Maso" na kigogo wa polisi.
Soga za hapa na pale zikaendelea ili mradi siku imalizike kwa usalama. Mpaka jua likazama, hayo ndio yalikuwa maisha mapya ya Masoud Masoud, maisha ya kuwa punguwani wa akili asiyejua kesho yake itakuchaje, asiye na uhakika wa kula yake wala afya yake. Analala vibarazani, mbu wake, baridi yake. Wapo waliomsikitikia kwa tatizo lililompata na wapo waliompuuza na kumbeza kuwa kayataka mwenyewe kutembea na mke wa mtu, wakatoa hukumu bila kufahamu chanzo chake ni nini!.

Kikao kizito ofisini kwa Inspekta Haroub
Ofisini kwa Inspekta Haroub Farouq, mmoja wa vigogo wa Jeshi la Polisi kulikuwa na kikao kizito kinachoendelea baina ya maafisa wa ngazi za juu wa Polisi Makao Makuu na wale wa kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani na Ustawi wa Nchi. Ni kama kikao cha baba na mtoto kwa sababu hawa wote walikuwa ofisi zao zipo pua na mdomo na wanatumia geti moja na majukumu yao ya kikazi yanashabihiana. "Nimewaiteni kikao hiki kifupi cha kabla ya kuanza kazi, ili kukumbushana majukumu yetu mazito yalioyopo mbele yetu. Kama mnavyofahamu tunatarajia kupata ugeni mzito wa Mabalozi wawili toka Marekani na Canada." Akapumzika kidogo mazungumzo yake na kumeza mate kisha akaendelea. "Wanakuja kutukabidhi msaada wao wa vifaa walivyotoa kwa Jeshi la Polisi. Vifaa hivyo ni magari ya doria idadi yake 50, pamoja na kompyuta zaidi ya 1000. Ni msaada ambao umetufikia katika wakati muafaka hasa ukichukulia bado vituo vyetu vya Polisi Tanzania nzima tunaandaa mashauri ya watuhumiwa kwa kutumia mtindo wa karne za ujima wa peni na daftari.
Pia tuna uhaba mkubwa wa magari ya kufanya doria hasa nyakati za usiku. Huko nje ya Miji, majambazi yanajitawanya kwa mapana na marefu. Sio jambo zuri kwa Jeshi la Polisi, ni dalili ya kuwa tumeshindwa kwa kila njia na jiha kudhibiti uhalifu nchini Tanzania. Sasa anapotokea mhisani wa kutupa magari 50 ni jambo la kupongezwa sana.
Sasa maandalizi ya mkutano huo wa makabidhiano yapambe moto, kila mwenye jukumu lake alitekeleze kwa ufanisi mkubwa. Habari nilizopata ni kuwa mgeni rasmi atakuwa Waziri wa Mambo ya Ndani na Ustawi wa Nchi Mheshimiwa "Ngaiza Jacob Ngaiza", na pia baadhi ya vigogo wa serikali watahudhuria hafla hiyo wakiwemo Wabunge wetu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tengenezeni naizesheni yenu vizuri kabisa kila kitu kiende kama tulivyopanga. Uzembe wowote utakaosababisha aibu na izara mbele ya wageni wetu, tutahesabu ni uzembe kazini na unaweza kukupelekea kufukuzwa kazi, hivyo tekelezeni wajibu wenu, kumbukeni cheo ni dhamana, ahsanteni sana" akawa Inspekta Haroub ameshafunga kikao kifupi cha kulishana yamini ya utendaji kazi uliotukuka.
Kila Afisa akawa anatawanyikia ofisini kwako kichwa chini kwenda kujipanga vyema kutimiza majukumu yake. "Koplo Michael njoo hapa" ulikuwa ni wito wa Inspekta Haroub kwa fundi mkuu wa karakana ya Jeshi la Polisi. "Naam afande" aliitikia wito huku akigeuka na kupiga saluti maana tayari alishakishika na kunyonga kitasa cha mlango wakutokea. Ikabidi akiache kitasa na kupiga hatua mbili tatu za kurejea karibu na Bosi wake.
"Uzembe kama wa kipindi kile cha kushindwa kutengeneza v8 sitaki ujirudie tena mpaka anakuja kukusaidieni kichaa nyie wenye akili timamu mnaolipwa mishahara na posho mpo mpo tu mnapigwa ubwete! "alizungumza kwa kufoka Inspekta. "Samahani Afande kosa halitojirudia tena" alijibu Koplo Michael kwa unyenyekevu akiwa amekakamaa hatikisiki. "Kama mtamhitaji yule mwehu "Maso Maso" tena mie namuweza sana yule atakusaidieni hasa ukichukulia baadhi ya magari yamekaa bandarini muda mrefu na yatajaribiwa pale kama yanafanya kazi, sasa inaweza kuja aibu ya mwaka, au unasemaje"? aliuliza swali la mtego Inspekta Haroub.
"Itakuwa vizuri sana, unajua sasa pale karakana wenzetu wawili wapo likizo na mmoja amefiwa na mzazi wake sasa, ukaguzi wa magari yote ni shughuli pevu bora "Maso Maso" aje tu kama utamdhibiti asilete Ukichaa wake" akajibu Koplo Michael ili kumridhisha Bosi wake asije kukataa msaada likazuka la kuzuka akatimuliwa kazi.
"Haya niachie mimi hilo jukumu kesho tu utamuona karakana" akajibu Inspekta Haroub, wakaagana akaendelea na majukumu yake mengine.

SURA YA TATU
Hafla ya makabidhiano ya vifaa kwa Jeshi la Polisi
Ilikuwa ni siku ya Ijumaa majira ya kuanzia saa nane mchana jua lilikuwa bado linatoa miale yake yenye kuchoma mwili, kadamnasi ya watu ilikuwa imekusanyika mbele ya jengo la Wizara ya Mambo ya Ndani. Kulikuwa na hafla kubwa ya makabidhiano ya vifaa vya kazi vikiwemo magari na kompyuta kwa Jeshi la Polisi. Vifaa hivyo vilikuwa ni msaada kutoka nchi ya Marekani na Canada kwa ajili ya kuboresha utendaji wa jeshi hilo.
Bendi ya Jeshi la Polisi ilikuwa inatumbuiza nyimbo yao mpya ya kusifia ushirikiano mwema wa kidugu baina ya Tanzania na Marekani. Bendi hii ya "Polisi Jazz Band" ni moja ya bendi kongwe nchini iliyozoeleka miaka ya 70's-80's kwa mtindo wao wa "vangavanga". Pia wakaanza kuimba nyimbo zao zilipendwa kama "Naamua kurudi kijijini","Halima" na "Baba yupo wapi" nyimbo ambazo zilisuuza roho za watu wazima waliohudhuria ambao walikuwa wanakumbushwa enzi wapo vijana. Ilimradi hafla nzima ilikuwa imefana sana kila mtu alikuwa ana furaha sheshe.

ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog