Search This Blog

Monday 27 March 2023

HADI LINI - 2

  


Simulizi : Hadi Lini

Sehemu Ya Pili (2)


“Na macho ya watu wengi wanaotuangalia nayo pia yanasababisha madhara, twen’zetu!” Ibrahim alisema huku akimshika mkono na kuanza kumuongoza kutoka katika eneo lile.




Kama aliyekumbuka kitu, Ibrahim aligeuka kuwatazama wale watu waliokuwa wamejazana eneo lile na kuwashukuru sana kwa msaada walioutoa kwao.

Kisha Ibrahim alimuongoza Bélise hadi nje kabisa ya lile jengo kwenye eneo la maegesho ya magari alikokuwa ameegesha gari lake la kifahari aina ya Toyota Landcruiser GX V8 la rangi nyeusi. Bila kujali macho ya watu waliosogea eneo lile Ibrahim alimfungulia Bélise mlango wa mbele wa upande wa kulia, kisha alikwenda upande wa kushoto, pasipo kuwajali watu akaingia.

Ibrahim aliliondoa lile gari kwa mwendo wa kasi na kuyafanya magurudumu yachimbe ardhi, akaingia katika barabara ya Ave De Luxembourg na kuelekea uelekeo wa ya uwanja wa mpira wa miguu wa Prince Rwegasore Stadium kama alivyokuwa ameelekezwa na Bélise. Aliyavuka makutano ya barabara za Ave De Luxembourg, Ave De France na Ave De Portugal akaendelea na ile barabara ya Ave De Luxembourg hadi alipoifikia barabara pana ya Boulevard de I?ndependence, Bélise akamuelekeza kuwa akunje kushoto na kuifuata ile barabara ya Boulevard de I?ndependence iliyokuwa ikipita mbele ya ule uwanja wa mpira wa miguu wa Prince Rwegasore Stadium.

Muda mwingi Bélise alionekana mtulivu sana huku akitafakari hili na lile. Ibrahim alimtupia jicho la matamanio mara kwa mara wakati lile gari lake likichanja mbuga kukatiza mitaa na kuipita Aroma Sambicoffee, kisha uwanda mpana uliokuwa na majengo ya Shule ya Kifaransa kulia kwao.

Baadaye wakakuta barabara pana ya Boulevard de I’Uprona iliyokuwa ikikatiza mbele yao ikitokea Ubalozi wa Ufaransa. Bélise akamwelekeza Ibrahim kuingia upande wa kulia akiiacha ile barabara ya Boulevard de I?ndependence na kufuata barabara ya Boulevard de I’Uprona.

Ibrahim akaingia katika ile barabara ya Boulevard de I’Uprona akiendelea kuambaa kando kando ya uwanda mpana wa majengo ya Shule ya Kifaransa kulia kwake, na alipofika mwisho wa eneo la ile shule ya Kifaransa Bélise alimuelekeza tena Ibrahim kuingia kulia kwake kuifuata barabara ya Ave Muyinga.

Ibrahim aliongeza mwendo huku akiipita barabara ya Ave de lax Paix iliyokuwa inaingia upande wake wa kushoto na kwenda mbele zaidi kisha akaifikia barabara ya Ave des Patriotes, ambayo pia ilikuwa inaingia upande wake wa kushoto, kisha Bélise akamuonesha jengo moja la ghorofa lililokuwa jirani na baa ya Bunga Bunga, nyuma ya ule uwanja wa mpira wa Rwagasore.

Ibrahim akafunga breki na kuliegesha gari lake kando ya ile barabara ya Ave Muyinga huku akilitazama lile jengo kwa makini.

“Hapo ndipo ninapoishi, bwana mkubwa! Karibu ndani… karibu kwetu tafadhali” Bélise alimwambia Ibrahim kwa sauti laini na tulivu ya nyenyekevu.

Ibrahim alimtazama Bélise na kuachia tabasamu pana, “Je, ninaweza kuruhusiwa kukaribia kwako siku nyingine baada ya leo?” alimuuliza huku akiyatulizia macho yake kwenye uso wa Bélise.

Bélise alimtupia jicho la wizi akimtazama Ibrahim kwa udadisi huku akionesha wasiwasi kidogo, “Sawa… unaruhusiwa wakati wowote,” Bélise alijibu huku akishusha pumzi.

Muda ule ule Ibrahim aliteremka na kuwahi kuzunguka upande wa pili, akamfungulia Bélise mlango huku akimpisha ashuke kutoka kwenye gari. Bélise aliposhuka akanyoosha mkono wake kumpa Ibrahim huku akiachia tabasamu pana na laini lililozidi kumkoroga ibrahim, kisha akainamisha kidogo kichwa chake kwa adabu.

“Uende salama bwana mkubwa… kwa heri,” Bélise alisema kisha alianza kupiga hatua kuanza kuondoka lakini akasita na kugeuka baada ya kusikia Ibrahim akiongea.

“Naitwa Ibrahim Bigirimana…” Ibrahim alisema kwa sauti tulivu huku akimtazama Bélise kwa makini na kutoa business card moja, akanyoosha mkono wake kumpa Bélise. “Mawasiliano yangu yote yapo humo).

Bélise aliipokea ile kadi huku akimtupia jicho la wizi Ibrahim, kisha macho yake akayapeleka kwenye ile kadi aliyopewa na kuitazama kwa makini.

“Asante, bwana mkubwa, mimi naitwa Bélise Gatete, nitawasiliana nawe kwa vile umenipa namba zako… kwa heri bwana Bigirimana,” Bélise alisema huku akimtazama Ibrahim akionekana kusubiri ruhusa ya kuondoka.

“Kusema ukweli, natamani sana tufahamiane zaidi ya hivi, Ee... ninachojaribu kusema... ni... ee, kwa nini tusiwe ee ... labda tuseme marafiki?” Ibrahim alisema kwa sauti tulivu huku akimtazama Bélise kwa makini.

“Kwa hali inavyoonekana, sisi tayari tu marafiki, au ni urafiki gani unaoutaka?” Bélise alisema huku akiangalia kando na kuachia tabasamu la aibu.

“Urafiki kama ulivyo… nadhani wewe si mtoto mdogo unaelewa nikisema hivyo!” Ibrahim alisema huku akiangua kicheko hafifu.

Bélise alimmtazama Ibrahim kwa udadisi zaidi huku akishusha pumzi.

“Sawa, nadhani tutaelewana zaidi kadri tutakavyokuwa pamoja, au siyo?”

Ibrahim alishusha pumzi kwa nguvu huku akijilegeza na kuegema gari lake. Akaonekana kuwaza kidogo kwa sekunde chache huku akizungusha macho yake kuyatazama mazingira ya eneo lile.

“Unaweza kupata nafasi Jumamosi ya wiki hii? Ningependa tuonane kwa maongezi zaidi ya kufahamiana, maana ni kweli tumeshakuwa marafiki,” hatimaye Ibrahim alisema huku akiilamba midomo yake iliyoanza kukauka.

“Wapi?” Bélise alimuuliza Ibrahim baada ya kufikiria kidogo huku akimtazama kwa makini.

“Hotel Club Du Lac Tanganyika, saa kumi na mbili na nusu jioni. Nadhani panafaa zaidi,” Ibrahim alisema pasipo hata kufikiri.

“Sawa…” Bélise alisema huku akibetua kichwa chake baada ya kufikiria kidogo…

______

“Bwana, una matatizo gani mbona hujibu?” sauti ya Bélise ilimzindua Ibrahim kutoka kwenye mawazo pale Bélise alipoulizwa swali.. Ibrahim alimtazama Bélise na kushusha pumzi za ndani kwa ndani huku akilazimisha tabasamu.

“Ah, usijali! Karibu ukae,” Ibrahim alisema huku akimuonesha Bélise sehemu ya kuketi, huku akijiweka vizuri kwenye kiti chake.

“Ahsante, samahani kwa kuchelewa,” Bélise alijaribu kujitetea huku akimtumbulia macho Ibrahim.

“Bila samahani,” Ibrahim alimjibu Bélise kumtoa shaka huku akiitazama saa yake ya mkononi na kuongeza, “…hukuchelewa, ni saa kumi na mbili na dakika therathini na tano tu. Bado ahadi yako ni ya Kizungu.”

Bélise aliketi kwenye kiti alichoelekezwa na ibrahim huku akijitahidi kuyakwepa macho ya Ibrahim yaliyokuwa yanamtazama kwa makini. Muda huo huo mhudumu wa ule ukumbi alifika na kusimama mbele ya meza yao huku akimtazama Bélise kwa tabasamu pana la kibiashara lililokuwa likivinjari usoni pake.

“Karibu dada, sijui ungependa kuagiza nini?” yule Mhudumu alimuuliza Bélise kwa sauti tulivu huku macho yake yakiweka kituo kwenye uso wa Bélise.

Bélise alimtazama yule mhudumu kwa makini huku akizungusha macho yake kujaribu kufikiria, alivuta pumzi ndefu za ndani kwa ndani kisha akazishusha taratibu huku akiminya midomo yake yenye maki.

“Niletee chipsi na nusu kuku,” hatimaye Bélise aliongea baada ya kufikiria kidogo kisha aligeuka kumtazama Ibrahim huku akiachia tabasamu la haya.

“Ongeza na glasi nyingine ya Navette de Marseille,” Ibrahim alimwambia yule mhudumu kisha alimtupia jicho Bélise.

Yule mhudumu aligeuka na kuanza kuondoka eneo hilo, lakini Ibrahim alionekana kukumbuka jambo na kumwita. Yule mhudumu akarudi huku akiyatuliza macho yake kumtazama Ibrahim kwa makini.





“Kuna kingine chochote?” yule mhudumu alimuuliza Ibrahim akiwa bado kamkazia macho yake.

“Ndiyo,” Ibrahim alijibu yule mhudumu huku akimtupia jicho Bélise, kisha anaongeza, “Vitu tulivyoagiza vipeleke kwenye kile chumba maalumu, sawa?”

“Ondoa shaka,” alisema yule mhudumu huku akimtupia jicho la wizi Bélise na kuachia tabasamu pana. Kisha aligeuka na kuondoka haraka kutoka eneo lile na kuelekea kwenye kaunta ya jikoni ya ukumbi wa maakuli.

Ibrahim alishusha pumzi huku akimtupia jicho Bélise na kuachia tabasamu, “Chakula cha hapa kizuri sana,” alismema huku akiendelea kutabasamu.

* * * * *

Saa tatu usiku, kwenye chumba kizuri cha kifahari cha Hotel Club du Lac Tanganyika, taa mbili za rangi ya bluu zilikuwa zinatoa mwanga hafifu wenye mg’ao na kufanya nusu ya chumba kile kuwa kizani.

Kilikuwa chumba kikubwa chenye kitanda kikubwa cha samadari kilichokuwa katikati ya chumba, kitanda kile kilikuwa cha futi sita kwa sita, cha mbao ngumu za mninga na chenye droo mbili kila upande, na juu ya zile droo kulikuwa na zile taa mbili za rangi ya bluu.

Mbele ya kile kitanda kulikuwa na seti nzuri ya runinga pana aina ya LG ya inchi hamsini na mbili na chini ya ile runinga kulikuwa na meza nzuri nyeusi ya kioo, ambayo juu ya meza kulikuwa na simu mbili kubwa za kisasa za Smartphone na kando ya meza ile kulikuwa na briefcase nzuri nyeusi iliyokuwa imeegamishwa kwenye ukuta.

Upande wa kushoto wa kile chumba kulikuwa na jokofu la vinywaji lililokuwa kwenye kona, na hatua chache kutoka kwenye lile jokofu kulikuwa na dirisha pana la kioo lililokuwa limefunikwa kwa pazia zito na refu lenye nakshi za michoro ya maua yaliyodariziwa vizuri na kuyafanya yapendeze.

Kwa kutokea juu kwenye lile dirisha la chumba kile mtu angeweza kuona mandhari nzuri yenye nyasi nzuri za rangi ya kijani kibichi zilizopakana na maua ya rangi tofauti ya kuvutia na bwawa ambalo lilikuwa limezungukwa na nyasi zilizopandwa katika hoteli ile.

Pia mle ndani kulikuwa na kabati kubwa la kisasa la nguo ambalo hata hivyo lilikuwa limefungwa. Na pembeni ya lile kabati kulikuwa na kochi moja kubwa la sofa na meza ya kioo iliyokuwa mbele yake iliyokuwa na bilauri mbili ndefu, chupa kubwa ya mvinyo mwekundu wa Navette de Marseille na vyombo vilivyokuwa na mabaki ya chakula, vyote vikiwa juu ya ile meza.

Kando ya lile sofa kulikuwa na meza fupi ya mbao iliyokuwa na simu ya mezani na kitabu kidogo kilichokuwa ba orodha ya majina ya watu na kampuni zilizotumia huduma ya simu hiyo ya mezani. Kwenye kona ya chumba kile upande wa kulia kabisa kulikuwa na mlango wa kuelekea kwenye chumba kidogo cha maliwato na bafu.

Ukutani kulikuwa na picha mbili kubwa nzuri za kuchorwa zilizokuwa zimetundikwa sehemu mbili tofauti. Moja ilikuwa ni picha ya wanyama wa porini na picha nyingine ilikuwa ya ua zuri la rangi nyekundu na bluu lililochorwa kwa ustadi wa hali ya juu.

Picha zote mbili zilikuwa zimewekwa ndani ya fremu nzuri za kioo na kuzifanya zionekane vizuri katika hizo kuta nyeupe na safi za chumba kile. Chini sakafuni kulikuwa na zulia zuri lenye mchanganyiko wa maua ya rangi ya njano, bluu na kijani kibichi.

Hapo sakafuni zilionekana nguo za Ibrahim na Bélise zilizokuwa zimetupwa tupwa na kusambaa ovyo, na juu ya kile kitanda kikubwa cha kifahari walionekana Ibrahim na Bélise waliokuwa wamemezwa na ulimwengu wa anasa.

Muda ule Bélise alikuwa anajitahidi kumwonesha Ibrahim ufundi sanaa ya aina yake na kumfanya kutoa miguno kwa raha aliyojisikia huku akimimina ahadi nyingi ambazo aliapa kuwa angezitekeleza.

Ibrahim alimbusu mzinzi mwenzie na kumpapasa nyama za mgongo huku akihema kwa nguvu. Bélise naye alikuwa anatweta kwa mchoko lakini akionekana kuhisi faraja kubwa iliyokuwa inapenya kwenye mishipa yake ya damu, akajikuta akilia kilio kilichokosa tafsiri inayoweza kukubalika kwa haraka.

Akiwa anakaribia kumaliza safari yake ya kufika kileleni, Ibrahim alianza kutapatapa kama mtu aliyetaka kukata roho, jambo hilo likamfanya Bélise kupitisha vidole vyake laini ambavyo vilikuwa na kucha ndefu kwenye masikio ya Ibrahim. Kitendo hicho kikamfanya Ibrahim kuvunja dafu huku akilia kama mtoto mdogo.

Alitweta huku akionekana kuwa hoi na mapigo ya moyo wake yalikuwa yakimuenda mbio isivyo kawaida.

Bélise alijiinua taratibu kutoka pale kitandani na kumwacha Ibrahim akiwa bado amejilaza kwa uchovu aliokuwa nao, kisha aliingia bafuni na kujimwagia maji, na alipotoka alichukua taulo na kujifunga juu yake kupitia kifuani na kufanya lile taulo liache mapaja yake wazi, kisha alirudi tena katandani, akaketi juu ya kitanda huku akimtazama Ibrahim kwa aibu. Ibrahim alikuwa bado amejilaza huku akiwa amefumba macho yake kwa uchovu.

Mara simu ya Ibrahim ikaanza kuita na kumshtua Ibrahim. Alifumbua macho yake na kuinua kichwa chake kutazama mahali zilipo zile simu zake. Bélise aliinuka na kuichukua ile simu iliyokuwa inaita huku akipitisha macho yake kuiangalia namba ya mpigaji kabla hajampa Ibrahim.

Ibrahim aliitazama kwa makini ile namba iliyokuwa inampigia na kuguna huku akikunja sura yake. Aliipokea ile simu kwa shauku kubwa na kuiweka kwenye sikio lake la upande wa kushoto huku akiminya midomo yake.

“Hallo… unasema!” Ibrahim anamaka kwa mshtuko huku akijichomoa haraka kutoka pale kitandani.

Alimkodolea macho Bélise huku akiwa makini kusikiliza kile alichokuwa anaelezwa na mtu aliyekuwa upande wa pili wa ile simu. Akashusha pumzi ndefu huku aakiuma mdomo wake wa chini.

“Una uhakika? Okay, okay… nakuja sasa hivi…” Ibrahim alisema na kuamka kutoka pale kitandania akakimbilia bafuni bila hata kukata simu, kule bafuni alijimwagia maji chap chap na alipomaliza akaokota zile nguo zake pale sakafuni na kuanza kuvaa haraka.

Muda huo Bélise alikuwa anamtazama kwa mshangao uliokuwa umechanganyika na wivu, macho yake yalionesha wazi kumuonea Ibrahim.

Ibrahim alipomaliza kuvaa alichukua briefcase yake na kuanza kutoka nje haraka kabla hata hajamaliza kuvaa shati lake vizuri, mara akakatizwa na sauti kali ya Bélise kabla hata hajafungua mlango na kutokomea.

“Mpenzi!”

Ibrahim aligeuza shingo yake kumtazama Bélise kwa mshangao, alionekana kukerwa kidogo.

“Unasemaje? Nachelewa!” Ibrahim alisema huku akimtazama Bélise kwa makini zaidi.

Bélise alikuwa amezishika mkononi zile simu mbili za Ibrahim na kumwonesha huku akimkazia macho.

“Sawa, lakini umesahau simu zako,” alimwambia huku akiminya midomo yake akionesha dhahiri kuingiwa na wivu.



Ibrahim alionekana kushtuka na kurudi haraka hadi alipokuwa amesimama Bélise, akanyoosha mkono wake kutaka kuzichukua simu zake akionekana kuwa na haraka.

“Asante, mpenzi wangu…” Ibrahim alisema huku akiachia tabasamu laini.

Bélise akaurudisha nyuma mkono wake uliokuwa umeshika zile simu huku akimkazia macho Ibrahim, kitendo kile kikamfanya Ibrahim ashike kiuno chake huku akimtazama Bélise kwa mshangao uliochanganyika na hasira.

“Kuna shida yoyote?” Ibrahim aliuliza kwa sauti iliyokuwa imebeba hasira.

”Ndiyo, kwa nini unanifanyia hivi?” Bélise alisema huku sauti yake ikionesha kubeba hasira kidogo. Wivu wa mapenzi ulikuwa unajionesha waziwazi kwenye uso wake.

Ibrahim alimwangalia Bélise kwa kitambo kifupi akionekana kutoelewa maana yake, akakunja sura yake na kutengeneza matuta madogo usoni huku akijaribu kufikiria.

“Nimekufanyia nini, mbona sikuelewi!”

“Unaniachaje?” Bélise alimuuliza Ibrahim huku akiongea kwa hasira, alimeza funda la mate kutowesha donge kubwa la hasira lililokuwa limemnasa kooni.

Ibrahim alimwangalia Bélise kwa mshangao zaidi, akakunja sura yake huku akimsogelea taratibu lakini Bélise alibetua midomo yake huku akikunja uso wake kwa hasira na kuanza kurudi nyuma.

“Kama uliona mkeo mali, kwa nini ulinitafuta?” Bélise alisema huku akirudi nyuma.

Ibrahim akazidi kushangaa, akamkazia macho Bélise na kushusha pumzi ndefu huku akijaribu kufikiria kidogo.

“Funguka, acha kuongea kwa mafumbo.”

“Usijitie hamnazo. Kama vipi nenda na usinitafute tena uone kama nitababaika!”

“Nipe basi simu zangu niende, mbona unanifanyia hivi lakini?” Ibrahim alionekana kulalamika.

“Sikupi mpaka kieleweke,” Bélise alisema na kuketi juu ya kile kitanda huku akiendelea kumkazia macho Ibrahim..

Ibrahim alisimama akamtazama Bélise kwa makini huku akionekana kukerwa, hata hivyo, alijitahidi sana kuzuia hasira yake. Kikapita kitambo kifupi cha ukimya huku kila mmoja akijitahidi kuidhibiti vyema hasira iliyokuwa inafukuta nafsini mwake. Ibrahim akatingisha kichwa chake kwa huzuni huku akimtazama Bélise kwa utulivu kama aliyekuwa akijaribu kuyasoma mawazo yake.

“Nipe changu nikupe simu zako, ulivyokuwa unaniahidi ulidhani nini!” Bélise aliongea huku akimkazia macho Ibrahim, alionekana kumaanisha kile alichokuwa anakiongea.

Ibrahim aliiweka briefcase yake sakafuni na kujipapasa mifukoni, akatoa wallet, akaifungua na kuhesabu kitita cha fedha haraka haraka, faranga laki moja kisha akanyoosha mkono wake kumpa Bélise. Bélise alizitazama zile fedha bila kuzipokea, kisha alinyanyua mabega yake kukataa.

Ibrahim alimtazama kwa mshangao, akataka kuondoka na zile fedha lakini akasita na kunyanyua mabega yake juu huku akibetua midomo yake.

“Unataka faranga ngapi?” Ibrahim alimuuliza huku akijishika kiuno.

“Laki tatu” Bélise alijibu huku akimkazia macho Ibrahim.

Ibrahim alivuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu, akauma midomo yake huku akiyatuliza macho yake kwenye uso wa Bélise, alionekana kufikiria kidogo na kuitupia jicho saa yake ya mkononi kisha akasonya. Alionekana kushtuka kidogo na kuamua kuongezea faranga zingine kama laki moja kwenye kile kitita cha faranga laki mbili, kisha anazitupa juu ya kitanda.

Bélise alionekana kuzihesabu zile fedha kwa macho pasipo kuzishika kisha akanyanyua uso wake kumtazama Ibrahim kwa mshangao.

“Hazitoshi!”

“Basi kesho nitakutumia zingine.”

Bélise alionekana kufikiria kidogo kama mtu aliyekuwa akijishauri jambo, kisha akanyoosha mkono wake kumpa Ibrahim zile simu. Ibrahim alizipokea na kuondoka haraka bila hata kuaga, akaufunga ule mlango nyuma yake.

Alipotoka ndani ya kile chumba alitokea kwenye korido pana na kushika uelekeo wa upande wa kulia wa ile korido pana, akaifuata korido iliyokuwa inatazamana na milango minne na upande wa kushoto kulikuwa na mlango mkubwa uliokuwa wazi.

Akaifuata korido hiyo hadi mwisho kabisa, upande wa kushoto kulikuwa na lifti, akafika na kubonyeza kitufe kilichokuwa kando ya ule mlango akijaribu kuiita ile lifti. Alisimama hapo kusubiri kwa dakika kadhaa lakini akagundua kuwa kile chumba cha lifti kilikuwa bado kipo ghorofa ya juu zaidi na kilikuwa kimekwama huko kwa muda mrefu. Huenda labda kulikuwa na mtu aliyeamua kuizuia ile lifti.

Ibrahim alisonya na kuondoka haraka akiufuata mlango mkubwa uliokuwa wazi, hapo akanza kuziparamia ngazi za kuelekea sehemu ya chini ya lile jengo la hoteli. Aliteremka ngazi mbili mbili kwa mwendo wa mbio mbio.

Baada ya kushuka hadi ghorofa ya kwanza aliufuata mshale mdogo mweupe uliokuwa umechorwa ukutani ukielekeza upande wa kushoto na kutokea kwenye ukumbi mdogo ambao kulikuwa na milango mitatu.

Mlango mmoja ulikuwa unaelekea kwenye ukumbi wa mazoezi, na juu ya mlango ule kulikuwa na kibao cheusi kilichokuwa na maandishi meupe yaliyokuwa yameandikwa kwa lugha ya Kifaransa ‘Salle de gymnastique’ yaani Ukumbi wa mazoezi (Gym).

Kwenye mlango wa pili kulikuwa na kibao juu yake kilichokuwa na maandishi yaliyosomeka kwa lugha ya Kifaransa ‘Magasin’ yaani Stoo. Na mlango wa tatu uliokuwa wazi ukiwa umefunikwa kwa pazia zuri na jepesi ulikuwa na kibao cheusi juu yake kilichokuwa na maandishi meupe ‘Sortie’ au ‘Exit’ kwa lugha ya Kiingereza, au mlango wa kutokea kwa Kiswahili.

Ibrahim alielekea moja kwa moja kwenye ule mlango uliokuwa na maandishi ‘Sortie’ juu yake na kuzikuta ngazi, akaziparamia zile ngazi kushuka chini hadi alipoukuta mlango mwingine uliokuwa na kibao juu yake chenye maandishi ‘Sortie’.

Ibrahim aliufuata ule mlango na kuvuka, wakati alipokuwa anapita akatazama upande wake wa kulia na kuona mlango mwingine ambao juu yake kulikuwa na maandishi yakisomeka ‘Sauna’, au ‘Bafu la mvuke’ kwa Kiswahili.

Sauna kilikuwa chumba maalumu kilichobuniwa kama sehemu ya kupata joto la mvuke ambalo huipa hewa ya chumba hicho joto na kisha hewa kusambaa katika chumba na kuipasha ngozi ya mtu aliyeingia humo. Joto lake huwa linategemea mtumiaji alihitaji liwe la kiasi gani na lilitumika zaidi kwenye nchi zenye baridi.

Ibrahim aliupita ule mlango uliokuwa na maandishi ‘Sauna’ na kwenda kutokea kwenye ukumbi mwingine wa baa, akaendelea mbele akiipita kaunta ya vinywaji iliyokuwa upande wake wa kulia na kukuta mlango mkubwa uliokuwa wazi. Juu ya ule mlango kulikuwa na kibao cheusi kilichokuwa na maandishi meupe yaliyosomeka kwa lugha ya kifaransa ‘Salle à manger’ yaliyokuwa na maana ya Ukumbi wa chakula kwa lugha ya Kiswahili.

Kwenye ukumbi ule wa baa kulikuwa na seti nzuri za runinga pana zilizokuwa zimetundikwa ukutani zikirusha burudani mbalimbali. Ndani ya ukumbi ule kulikuwa na watu kadhaa waliokuwa wameketi kwa utulivu huku wakijipatia vinywaji na wakati huo huo sauti ya muziki laini ilisikika taratibu ndani ya ukumbi ule na kuzikonga vizuri nyoyo za watu waliokuwemo ndani ya ule ukumbi.





Katika eneo hilo kulikuwa na wazungu wengi na Waafrika wachache sana, labda kutokana na gharama za juu za huduma zilizokuwa zinatolewa humo ndani, wote hawa walikuwa wanajipatia vinywaji na vyakula huku wakiendelea na maongezi yao.

Ibrahim aliwapita bila kusema neno kama vile hajawaona japo kuna mwanamume mmoja alionekana kumwita. Ibrahim hakuitika, hakugeuka wala hakusimama bali alizidisha mwendo akijifanya hajamsikia yule mwanamume na kuwafanya watu wengine mle ukumbini kugeuka kumtazama kw mshangao, kisha wakampuuza na kuendelea na hamsini zao.

Ibrahim aliongeza mwendo wake ili kulivuka eneo lile kwani alikuwa hapendi kutazamwa Aliufikia mlango wa mbele kabisa wa Hotel Club du Lac Tanganyika na kuusukuma, akatoka nje na kujikuta akikabiliana na macho ya watu wachache, hasa madereva wa teksi waliokuwa wanaosubiri wateja ili kuwapeleka sehemu mbalimbali za mji.

Wale madereva na watu wengine wachache waliokuwa wamesimama pale nje walikuwa wakipiga soga. Mara madereva wawili kati yao wakamuona Ibrahim na kumchangamkia huku wakimwita kila aina ya majina kama “Boss”, “Tajiri”, “Afisa”, “Mkubwa” n.k. ili kumvutia apande gari zao.

Ibrahim alitingisha kichwa chake kukataa huku akiwapita bila kuwatilia maanani na kuendelea na hamsini zake.

Alitembea haraka hadi alipolifikia gari yake la kifahari aina ya Toyota Lexus RX la rangi nyeupe na kufungua mlango, akaingia ndani ya lile gari na kufunga mlango, alionekana akiwa hana muda wa kupoteza. Alivaa mkanda wa siti haraka na kuliondoa gari lake taratibu kutoka kwenye yale maegesho ya magari ya Hotel Club du Lac Tanganyika akizunguka kuelekea kwenye geti kubwa la mbele la jengo lile la Hotel Club du Lac Tanganyika.

Bélise akatokea kwenye mlango wa mbele wa Hotel Club du Lac Tanganyika na kulikimbilia gari la Ibrahim lililokuwa linalifikia geti kubwa la mbele la hoteli lakini akasita, alikuwa anampungia mkono Ibrahim kwa nguvu kumwashiria asimame lakini Ibrahim aliliondoa gari lake pasipo hata kumjali na kukata kona upande wa kulia akiingia katika barabara ya Chausse d'Uvira.

Bélise alilisindikiza lile gari kwa macho akionekana kukata tamaa, lile gari liliongeza mwendo na kupotelea mtaani. Bélise akashusha pumzi za ndani kwa ndani huku akiminya midomo yake na kushika kiuno.

Kijana mmoja mtanashati, mwembamba na mrefu aliyekuwa amevaa suti maridadi ambaye alikuwa mmoja kati ya watu wachache waliokuwa wamesimama pale nje ya Hotel Club du Lac Tanganyika alimtazama Bélise kwa makini kama aliyekuwa akimfananisha, kisha akamsogelea huku akiendelea kumtazama kwa makini. Bélise alishtuka na kugeuza shingo yake kumtazama Sylvere na kujikuta akipigwa butwaa.

“Hey, Sylvere!” Bélise alimaka kwa mshangao mkubwa huku akimtazama Sylvere usoni. Sylvere aliachia tabasamu pana huku akimkazia macho Bélise kwa makini.

“Bélise, unafanya nini hapa?” Sylvere alimtupia swali Bélise huku akimtazama kwa acho ya udadisi.

Bélise alishindwa kujibu, alimtazama Sylvere kwa makini kisha akatandaza mikono yake kumkumbatia. Walikumbatiana kwa mahaba huku wakibusiana. Sylvere alizungusha mikono yake kwenye kiuno cha Bélise huku akimkazia macho kumtazama usoni.

“Mbona ulikuwa hupokei simu yangu?” Sylvere alisema huku akiendelea kumkazia macho Bélise.

“Ngoja tutaongea,” Bélise alisema huku akitazama kando kuyakwepa macho ya Sylvere.

Katika barabara ya Chausse d'Uvira Ibrahim aliendelea kuendesha gari kwa mwendo wa kasi na kuyafikia makutano ya barabara za Chausse d'Uvira na barabara ya RN 5 Boulevard du 1er Novembre iliyokuwa inatokea katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Bujumbura.

Muda ule wa usiku jiji la Bujumbura lilikuwa limemezwa na utulivu wa aina yake. Kulikuwa hakuna pilika pilika zozote zilizokuwa zinaonekana barabarani wala mitaani bali magari machache tu yaliyokuwa yakikatisha barabarani, hasa magari ya Jeshi la Serikali ya Burundi.

Ibrahim aliifuata ile barabara pana ya Boulevard du 1er Novembre akizidi kuelekea katikati ya mji akiwa bado katika mwendo wa kasi, akalivuka eneo la viwanda, na mbele akakutana na pikipiki aina ya Boxer iliyokuwa na watu wawili ikiwa katika mwendo wa kasi ikitokea mjini kwenda maeneo ya viwandani, ile pikipiki ikaonekana kuingia upande ule lilipoku gari la Ibrahim.

Ibrahim aliiona ile pikipiki akakanyaga breki kwa nguvu, gari lake likasota na kuyumba kwenye barabara hiyo pana, bahati nzuri gari halikutoka nje ya barabara. Ibrahim akasonya na kukunja ngumi huku akiinua juu kidole chake cha kati kumuonesha yule dereva wa pikipiki katika hali iliyoashiria hasira alizokuwa nazo.

Pikipiki ile liserereka kisha dereva wa pikipiki akaiweka sawa na kuongeza mwendo pasipo kusimama. Mtu aliyekuwa amepakiwa nyuma kwenye ile pikipiki aliinua juu mkono wake wa kushoto huku kidole cha kati kikining’inia hewani utadhani kilikuwa kimepigiliwa msumari katika staili ya kumzodoa Ibrahim.

Ibrahim alisonya kwa hasira na kukanyaga pedeli ya mafuta, gari likajivuta na kufanya magurudumu yake kuchimba ardhi, kisha likaondoka kwa mwendo wa kasi. Ibrahim aliendesha gari lake kwa kasi huku akiendelea kusonya kwa hasira kisha akakata kona kuingia upande wa kushoto akiingia katika barabara ya Avenue de I'OUA.

Katika ile barabara ya Avenue de I'OUA Ibrahim alipishana na magari mawili matatu likiwemo lori moja la Jeshi la Serikali ya Burundi ambalo lilikuwa limewabeba wanajeshi wengi waliokuwa wamevaa sare za jeshi na bunduki zao mikononi, wakiwa kwenye doria kuhakikisha usalama wa nchi, hasa kwa sababu kulikuwa na tishio la waasi waliotaka kufanya mapinduzi mengine ya kutaka kuing’oa madarakani Serikali ya Rais Pierre Nkurunziza.

Wanajeshi waliokuwa kwenye lile lori waligeuka kumtazama Ibrahim kwa mshangao wakati gari lake likipishana na gari la jeshi kwa mwendo wa kasi utadhani labda alikuwa kwenye mashindano ya magari, hata hivyo wale wanajeshi hawakusimama wala kumfuatilia, waliendelea na safari yao.

Ibrahim aliendesha akiwa mwingi wa mawazo, akaupita mgahawa maarufu wa Parquet de la Mairie de Bujumbura na mbele yake, kabla hajakifikia kituo cha mafuta cha ANS Station mara akakuta kizuizi cha barabarani ambacho kilikuwa kimeandikwa kwa lugha ya Kifaransa POLICE CONTROLE au POLICE CHECK POINT kwa lugha ya Kiingereza, na kwenye kizuizi hicho kulikuwa na askari polisi na wanajeshi kadhaa wa serikali ya Rais Pierre Nkurunziza.

Ibrahim alikanyaga breki na kupunguza mwendo na hatimaye kusimamisha gari lake umbali wa mita kama therathini hivi kutoka kilipokuwa kizuizi kile kando ya barabara ya Avenue de I'OUA. Alisonya huku akaiitazama saa yake ya mkononi, hakuwa na muda wa kupoteza kwani alikuwa anatakiwa awe amefika Avenue de I’Hopital ambako alipigiwa simu akitakiwa kufika haraka ndani ya dakika ishirini! Laiti angejua kuwa barabara ile ilikuwa na kizuizi cha barabarani asingepita kabisa barabara hiyo.




Askari wawili, Major Ferdinand Niyongabo na Koplo Diomede Sinzumusi walianza kupiga hatua zao kulisogelea gari la Ibrahim huku wakiwa wameshika vyema bunduki zao aina ya SMG wakizielekeza kwenye lile gari. Koplo Diomede Sinzumusi alilifikia lile gari na kumuuliza Ibrahim kwa sauti ya ukali.

“Unatoka wapi na unaelekea wapi saa hizi?”

“Natoka kwenye miradi yangu naelekea nyumbani… Vipi kuna tatizo lolote?” Ibrahim alimuuliza yule askari kwa kujiamini huku akimkazia macho.

Wakati huo huo Major Ferdinand Niyongabo akalifikia lile gari la Ibrahim na kuzunguka akielekea upande wa nyuma wa lile gari huku akiwa analichunguza kwa jicho la hadhari.

“Nipe leseni yako ya udereva,” Koplo Diomede Sinzumusi aliongea kwa sauti kali akimwamuru Ibrahim huku akimkazia macho yake.

Ibrahim alitoa leseni yake na kumpa Koplo Diomede Sinzumusi huku naye akimkazia macho bila kupepesa. Koplo Diomede Sinzumusi aliipokea ile leseni ya udereva ya Ibrahim na kuanza kuikagua. Kitambo kifupi cha ukimya kikapita wakati yule askari akiendelea kuikagua ile leseni ya Ibrahim na wakati akifanya hivyo Major Ferdinand Niyongabo akawa anazunguka gari na kwenda mbele kwenye mlango wa dereva.

“Umebeba nini ndani ya gari yako?” Koplo Diomede Sinzumusi alimuuliza tena Ibrahim kwa ukali akiwa bado kaishikilia mkononi ile leseni ya udereva ya Ibrahim.

Ibrahim alimtazama Koplo Diomede Sinzumusi kwa makini huku donge la hasira likianza kumkaba kooni, maana aliona kuwa alikuwa anamchelewesha kuendelea na safari yake pasipo sababu za maana. Alitafakari kidogo akitafuta jibu la kumpa yule askari lakini kabla hajajibu, Major Ferdinand Niyongabo akamfikia na kumtazama kwa makini usoni.

“Hey, Bigirimana! Mambo vipi?” Major Ferdinand Niyongabo alisema huku akiachia tabasamu pana usoni kwake.

“Salama afande, vipi kuna tatizo?” Ibrahim alijibu huku naye akiachia tabasamu pana usoni kwake.

“Ni katika kuhakikisha tu kuwa nchi na wananchi wake wanakuwa salama kabisa,” Major Ferdinand Niyongabo alisema huku akiinama kidogo na kuegesha mkono wake kwenye dirisha la mlango wa gari.

Ibrahim alibetua kichwa chake akionesha kukubaliana na Major Ferdinand Niyongabo. Muda huo huo Koplo Diomede Sinzumusi aligeuka kumtazama Major Ferdinand Niyongabo kwa makini kisha akamgeukia tena Ibrahim na kuonekana kunywea kidogo, baada ya kuona kuwa mtu aliyekuwa anataka kumkagua alikuwa anafahamiana na bosi wake.

Koplo Diomede Sinzumusi hakuna na namna nyingine isipokuwa kumrudishia Ibrahim ile leseni yake ya udereva. Ibrahim aliipokea ile leseni na kushukuru.

ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog