Search This Blog

Thursday 23 March 2023

MATANGA YA ROHONI - 1

 

IMEANDIKWA NA :  BADI M. BAO
*********************************************

Simulizi : Matanga Ya Rohoni


Sehemu Ya : Kwanza (1)


SURA YA KWANZA.
Ilikuwa ni adhuhuri mwanana, ikichagizwa na upepo wenye kasi ya wastani ukivuma katika maeneo ya Posta Jijini Dar es Salaam. Kila mtu alikuwa ametingwa na mihangaiko yake ya kimaisha, watu wanakimbizana huku na kule ilimradi waweze kukamilisha makusudio na malengo yao ya siku ya kimaisha waliyojiwekea.

Wakati huo huo kulikuwa na kadamnasi ya watu walikuwa wamejikusanya wamejaa pomoni ndani ya kanisa la Mtakatifu Joseph 'St Joseph Cathedral church'. Hilo ni kanisa lililopo katika Mkoa wa Dar es Salaam, Wilaya ya Ilala. Kanisa hilo la kihistoria na la kuvutia kimandhari yake lipo mkabala na 'Sokoine drive' likiangalia 'Waterfront' karibu na geti la boti zinazoelekea Zanzibar.

Mkusanyiko wa umati huo wa watu ndani ya nyumba ya ibada kwa Wakristo wa Madhehebu ya Katoliki, ulikuwa na sababu yake maalumu. Haikuwa mkusanyiko wa bure bilashi tu wa kupiga porojo na soga siku iende. Motakaa kochokocho za aghali zilikuwa zimeegeshwa nje ya kanisa, kuashiria ni tukio la linalowahusu watu walalaheri.

Walikuja kushuhudia ndoa ya kifahari kati ya Dr. Trezguet na Bi Deborah iliyotarajiwa kufungwa muda mchache ujao ndani ya kanisa hilo. Wanandoa hao tarajaji waliwasili kanisani hapo kwa ngoma na matarumbeta hadi kanisani hapo huku sherehe kabambe ya kukata na shoka ikipangwa kuchukua nafasi yake ndani ya Hoteli ya kifahari ya 'Kempisky'. Wageni maarufu na mashuhuri wa ndani na nje ya nchi, kuanzia wanamichezo, wanamuziki, na wanasiasa nao walikuja kushuhudia ndoa hiyo kwa macho yao, hasa ukichukulia ukaribu wao na Dr.Trezguet ambaye kwa umaarufu wake hamna mtu ambaye alikuwa hamfahamu au hajapata kumsikia katika nchi hii ya Tanzania.

Umaarufu wake ulitokana na kuendesha vipindi vingi vya redio na televisheni akizungumzia masuala ya Afya na Saikolojia, huku akimiliki hospitali kubwa ya kisasa Jijini Dar es Salaam. Tetesi mitaani zilikuwa zinavuma kuwa sherehe yake hiyo ya ndoa ilitarajiwa kuteketeza zaidi ya nusu bilioni na ushee huku vyombo vya habari karibia vyote vikubwa vikiwa vimetingwa na harakati za kuhabarisha watazamaji na wasikilizaji hao hatua kwa hatua ya ndoa hiyo.

Taratibu zote za ndoa hiyo kufungwa zilishakamilika, misa ya ndoa hiyo ilikaribia kukamilika huku wakiwa wameshasimamishwa mbele ya Padre pale madhabahuni tayari kwa kuunganishwa na kuwa mwili mmoja.

Huo ulikuwa ndio wakati mgumu kuliko wakati wowote katika mioyo ya wana ndoa hao. Hapo ndio sehemu ambayo kama ni kitanzi mtu anajivika mwenyewe shingoni kujinyonga, haulazimishwi na mtu wala kushikiwa mtutu wa bunduki, unatakiwa ukubali agano hilo kwa hiari yako. Dr.Trez akiwa ameulamba vazi la suti nyeusi, akionekana yu nadhifu na maridadi kabisa uso wake muda wote ulikuwa na bashasha fokofoko kuonyesha furaha aliyonayo ya kumpata mwenza, mshirika wake wa kweli katika maisha, katika shida na raha, katika mvua na jua. Maisha ya ndoa ambayo yana pande mbili kama sarafu, pande moja ni tamu kama asali na ingine ni chungu kama shubiri.

Kanisa zima sasa muda huo lilikuwa lipo kimya, kama limemwagiwa maji ya baridi vile, kila mtu anawatazama wao tu wapendanao 'Love Birds' wanaosubiri kufunga ahadi takatifu. Hadhira ile mahadhuru kanisani mule kila mmoja kichwani mwake alikuwa ana mawazo yake, wapo waliokuwa wanajiuliza na kumlaumu na kumsengenya kimoyomoyo kuwa iweje mtu maarufu na tabaka a'ali kama Dr.Trez akaoe mwanamke ambaye sio wa hadhi yake, ambaye hata sio nyota, hajulikani vizuri na kuwaacha wasichana mastaa kibao ambao anaendana nao kihadhi.

Wengine wakawa wanampongeza kwa kupiga makofi ya pongezi mioyoni mwao kwa uamuzi wa kishujaa aliouchukua wa kuamua kuchukua jiko ambalo sio maarufu hasa wakiwa na mifano hai jinsi ndoa za mastaa kibao zinavyoshindwa kudumu. Hivyo wakawa wanamtakia kheri na fanaka katika safari yake ya maisha ya ndoa aliyoichagua kuianza.

Mawazo ya Dr.Trez pale mbele ya Padri mfungisha ndoa yakaanza kuvuka milima na mabonde, yanaisasambua ndoa kwa ujumla, akawa kama vile anasubiria maneno ya Padri atakapokamilisha ndoa kwa kutamka "kwenye ndoa za kanisani hakuna talaka hivyo kwa niaba ya Mungu Baba naifunga ndoa hii kwa kuwaunganisha kuwa mwili mmoja mpaka kifo kitakapo watenganisha na hapa chini ya jua hakuna mtu yoyote atakayekuwa na uwezo wa kuivunja ndoa hii hata mimi niliyeifunga sina mamlaka ya kuivunja nimeifunga na funguo nimeshazirejesha kwa Mungu Baba yeye ndiye pekee mwenye uwezo wa kuivunja kwa mmoja wenu kufa alichounganisha mungu mwanadamu asikitenganishe-Ameen".

Kitambo chote walichokuwa wamesimamishwa maharusi hao, Bi.Harusi Debora macho yake yalikuwa yanabubujikwa na mvua ya machozi yaliyoanza kutotesha shela lake alilojifunika kichwani mwake. Waliomshuhudia wakachukulia poa wakidhania ni machozi ya furaha ya kuolewa, hasa ukichukulia katika zama zetu hizi, wasichana wanadoda majumbani mwa wazazi wao kwa kukosa waoaji. Wanaume waonjaji ni wengi kuliko waoaji, hivyo watu kilio kile cha Debora wakakichukulia ni kilio cha furaha ya ndoa. Katu hawakung'amua kuwa kilikuwa ni kilio cha shari chenye uchuro ndani yake.

Swali kutoka kwa Padri lililotupwa kwa Dr. Trez la kuulizwa kama yupo tayari kuishi na Bi. Debora kwa shida na raha, katika uzima na ugonjwa, utajiri na umaskini katika maisha yake yote, lilijibiwa kwa haraka sana swali hilo na Dr Trez akiwa na furaha sheshe. Padri akamgeuzia kibao Bi Debora akamgeukia na kumtupia swali lile lile alilomuuliza mpenzi wake. Swali ambalo kama atalijibu vyema Padri ndio atapata fursa ya kuipasisha ndoa hiyo na kuendelea na sehemu ya pili ya misa inayohusiana na ekaristi takatifu.

Roho za wahudhuriaji zikawa zipo juu juu zinagonga kama saa mbovu, matarajio yao yakiwa ni jibu la ndio ili sherehe ya ndoa ya kifahari iliyopangwa iweze kufana. Macho yote yakakodoka kodo, yakamuelekea Bi.Debora alipoanza kuulizwa na Padri yule ambaye pembezoni yake kulikuwa na bakuli la pete za maharusi ambazo walitarajia kuvishana mara baada ya ndoa kupitishwa.

"Sipo tayari kuolewa na Dr.Trezguet.....I'm sorry Aaah...Aaah...yuuleee....!" Bi. Debora alishindwa kumalizia maelezo yake akiwa amemnyooshea kidole Bibi mmoja aliyekuwa amekaa benchi la mbele kabisa. Bi.Debora alijikuta anaanguka chini kwa kishindo na kuanza kurusharusha miguu kushoto na kulia, akifafaruka, anapiga kelele kama mwehu aliyevamiwa na mapepo anazungumza mambo yasiyoeleweka mpaka akapoteza fahamu.

Zogo na vurumai mtindo mmoja likaibuka mule kanisani kila mmoja akiingilia upande wake. Hamkani mambo si shwari tena, Debora kalitia tembo maji, mambo yamegeuka kuwa segemnege. Kikosi wa watoa huduma ya kwanza ambao nao walikuwa na mualiko rasmi wakafanya juhudi za kumtoa Debora kanisani pale madhabahuni alipokula mwereka na kumkimbiza katika Hospitali binafsi ya karibu ya 'Agakhan' ili kujaribu kuokoa uhai wake.

Kila mtu baada ya tukio hilo akaanza kuropoka jambo lake, vizabizabina ukawa ndio uwanja wao huru wa kujimwayamwaya kimaneno. Wao waliovumisha kuwa Debora karushiwa jini toka Pemba na mahasidi wake waliokuwa hawataki hata kuisikia ndoa hiyo. Hivyo wakapanga mipango ya kukomesha kwa kutumia njia za kimazingara.

Wapo waliozusha kuwa Debora kagundua usiku wa kuamkia siku ya ndoa yake kuwa Dr.Trezguet ana mke na watoto wa kizungu huko ng'ambo alipokuwa anadurusu na kuishu, hivyo kakasirika kutokana na kufichwa ukweli.

Wapo 'vidinga popo' na 'habari kauzwa' waliofika mbali zaidi na hata kumvunjia heshima mama mzazi wa Dr.Trezguet. Walileta madai kuwa huyo mama ni mwanga, mchawi wa kutupwa hataki kabisa mtoto wake aoe anahofia kushindwa kuzipochoa mali za mtoto wake vizuri kama akikaliwa kichwani na huyo mkewe. Wakaenda mbali zaidi kuthibitisha madai yao kuwa ndio maana Bi.Debora baada ya kuipiga chini ndoa alinyoosha kidole cha lawama kwa mama mzazi wa Dr.Trez. Ili mradi midomo yao, na hawailipii kodi yoyote walikuwa na khiyari ya kuzungumza tani yao, vyovyote watakavyo lakini ukweli halisi wa kwanini kaipanjua ndoa hadharani alikuwa anaujua yeye mwenyewe Bi.Debora na moyo wake.

Matukio hayo yote yanavyotokea Dr.Trezguet alikuwa ameganda kama sanamu haamini kilichotokea muda mfupi kama kweli Debora, chaguo la moyo wake, ambaye hawajawahi hata kukwaruzana hata siku moja tokea waanze mahusiano yao miaka mitatu iliyopita kuwa kweli amempiga kibuti mbele ya umati wa watu. Alikuwa anawaza aibu gani isiyomithilika mbele ya umati ule na Watanzania kwa ujumla, atauweka wapi uso wake.

Machozi yalikuwa yanamtiririka bila breki, huku anajitahidi kuyafuta kwa hanchifu yake. Waandishi wetu wa habari kama unavyowafahamu kwa kupenda habari tata, wakamfuata kumhoji kutaka kujua kulikoni mpaka anamwagwa kirahisi rahisi tena mbele ya madhabahu takatifu.

Aliwapa jibu moja tu, "She is suffering from Post-Traumatic Stress Disorder (PTSD), I will fight for my LOVE" huku akawa anaondolewa kwa nguvu na wapambe wake akiwa mnyonge kutoka pale madhabahuni na kumuingiza kwenye gari lake na kutokomea zake eneo lile.

Baadhi ya wadadisi wa mambo wakapatwa na matumaini huenda ni ugonjwa huo wa "PTSD" ndio umemfanya Debora aropoke jibu baya kuwa hataki ndoa, hivyo huenda akipona atakubali kuolewa tena. Huku wakishadidia nadharia yao kwa tafakari jadidi ya kuwa kama kweli Deborah angekuwa hamtaki Dr Trezguet tangu mwanzo asingekubali kumtia hasara na kumuaibisha hadharani hivyo mbele ya umati wa watu.

Wale wapenda manyamnyam na mapochopocho ya harusi hawakutaka kulaza damu wakayafungia safari mpaka 'Kempisky Hotel' kwenda kujisosomola nayo. Wakamalizia hasira za Debora kutibua sherehe kwenye maakuli hayo. Ila chakula kingi bado kilikosa walaji hasa kutokana na wahudhuriaji wa sherehe hiyo walikuwa ni walalaheri, wale nafasi zao kimaisha. Uhalisia wa mambo ni kuwa hapo kanisani ndio ukawa mwisho wa hadithi tamu ya penzi la kusisimua la Dr Trezguet na Bi. Debora lililodumu kwenye uchumba kwa zaidi ya miaka 3.



Kwa kawaida matanga ni mkusanyiko wa watu kwenye nyumba yenye msiba ili kuomboleza na kuwaliwaza wafiwa kwa siku tatu au zaidi baada ya kuzika. Baada ya matanga kwisha watu hurejea kwenye shughuli zao za kila siku na baada ya muda husahau kabisa msiba uliowapata. Hubakiwa na simulizi tu ya kuwa mwaka fulani, siku fulani tulifiwa tukazika.

Lakini yanayosahaulika hayo ni matanga ya mwili, ila matanga ya rohoni yakikusibu maombolezo yake ni milele mpaka siku unarejea jongomeo kwa Mola wako pale unapoingizwa kwenye mwanandani wa kaburi. Matanga hayo ya rohoni huwa yanakupa majonzi daima dawamu wewe ni mtu wa vilio vya kusaga meno na kujipiga vitefute. Debora alikuwa na matanga ya moyoni aliyoyahifadhi tokea utotoni mwake yaliyokuwa yanamtesa maishani mwake.

Matanga ambayo aliyarithi tokea kwa mama yake mzazi, daima wakawa ni watu wa masumbuko tu wote wawili, yeye na mama yake mzazi. Kwao wao kila kukicha madhira yanayowasibu wanaona ni afadhali ya jana. Ule msemo wa baada ya dhiki ni faraja kwao ulikuwa hauna mantiki yoyote. Wao walikuwa wanaona baada ya dhiki ni dhiki maradufu.

Debora Alikuwa amevikwa majonzi na huzuni ya rohoni kutokana na majanga yaliyomsibu. Ujio wake duniani kwanza haukuwa wa kawaida kama unavyokuwa ujio wa watoto wengine. Kuzaliwa kwake kulikuwa ni kwa nguvu za mizimu ya Mlima Kolelo. Mlima Kolelo ambao ni moja ya safu za Milima ya Uluguru unaovuma sana kwa imani za mizimu. Wasimuliaji wanaeleza kuwa katika mlima huo, mizimu ina uwezo wa kusemesha watu kwa sauti tu bila yenyewe kuonekana, au wakati mwingine hasa nyakati za usiku sana mizimu hiyo huwa inajitokeza kama viumbe fulani ambao wahusika wameshindwa kuwatambua.

Jina lake Debora Kunambi, kabila lake ni Mchaga. Alikuwa anapowatajia jina tu, watu wanampachika Uluguru ila akiwafungukia kuwa yeye ni Mchaga na sio Mluguru wanabakia midomo wazi wanastaajabu. Wengi walikuwa wanajiuliza ubini wa Kunambi na Uchaga wapi na wapi, wala haifananii, wakawa hawapati majibu. Uhalisia ni kuwa jina la Kunambi sio la baba yake mzazi Debora, hilo ni jina la babu yake mzaa mama. Baba yake mzazi alikuwa anajulikana kwa jina la Minja. Kwanini atumie ubini wa babu na sio wa baba yake mzazi, hiyo nayo ni hadithi ndefu.

Baba Debora alikuwa anajulikana kama la Mwalimu Minja alikuwa anafundisha shule ya sekondari Morogoro iliyopo katika Manispaa ya Morogoro. Alipomaliza masomo yake ya Chuo Kikuu Dar es Salaam na kujipatia shahada yake ya Ualimu mwaka 1976 akapangiwa kufundisha Morogoro Sekondari. Mama yake mzazi Bi.Mwenda alikuwa ni mhudumu wa usafi katika hospitali ya Mkoa ya Morogoro.

Mwaka 1978 wazazi wake wakafunga ndoa ya kanisani, na kuanza kuishi pamoja kama mke na mume katika nyumba ya kupanga eneo la Mafiga. Ndoa ya wazazi wake Deborah ilikuwa imetawaliwa na mikingamo na vigingi visivyokoma hasa kutoka upande wa wazazi wa baba Debora ambao hawakupendezwa na kijana wao kuoa Mluguru. Walikuwa na mitazamo duni ya kufadhilisha kabila la Wachaga fauka Waluguru. Lakini baba Debora alikuwa na misimamo thabiti isiyoyumba kama mwamba, ya kutokutaka kuingiliwa katika ndoa yake, mpaka wazazi wake wakanywea.Wakawa hawana jinsi, mtoto wao kageuka kisiki cha mpingo hachezewi ovyo kwenye maamuzi yake.

Aghalabu wapendanao wanapokuwa lao moja, hasidi hawezi kuwachezea asilani. Walipovuka mawimbi mazito ya kuwatenganisha kwa kigezo cha ukabila bila kuyumbishwa, kikaibuka kikwazo cha kutokupatikana mtoto kwenye ndoa yao. Katika malengo mama ya ndoa, mbali ya kuwakinga wanandoa na tabia ya uasherati pia ni kupata watoto ili kuendeleza kizazi. Watoto ni matunda ya ndoa, na ndio huchangia kuleta furaha na uwajibikaji katika ndoa. Kukosekana kwa watoto katika ndoa ni moja ya sababu kubwa sana inayochangia ndoa nyingi sana kusambaratika.

Miaka ikawa inayoyoma, mama Debora hapatwi na kichefuchefu wala kutapika kama dalili za kupata ujauzito. Wakaanza kuhangaika huku na kule kwa waganga na waganguzi, kwenye tiba za hospitali na za mitishamba lakini wapi, majibu hola.

Uzalendo ulishaanza kumshinda baba Debora, akaanza kuwa mtu wa kuutwika mtungi ili kupoteza mawazo ya kukosa mtoto. Akawa akitoka kushika chaki shuleni nyakati za jioni, kituo cha kwanza Baa kwenda kupata moja moto moja baridi. Mpaka kurudi nyumbani sasa akawa anachelewa sana, manane ya usiku ndio muda wake.

Mama Debora akijaribu kuhoji na kudodosa sababu ya mabadiliko hayo ya ghafla, baba Debora anakuwa mkali kama pilipili, na kumshambulia kwa maneno yenye kuchoma nyoyo kuwa asiulizwe muda wa kurudi anasaka mtoto, mrithi wake.

Mawifi nao walipoona ndoa ya kaka yao ipo tenge tehanani walikuwa na furaha sheshe, hasa wakichukulia mama Debora hawakupenda aolewe na kaka yao. Mama Debora katika kuhangaika huku na kule ndio akaumwa sikio na shoga yake mmoja kuwa kuna mtaalamu kiboko kwa kusaga mkungu yupo kijiji cha Mkuyuni, Wilaya ya Mvomero anaitwa Mzee Katimbwa.

Kijiji hicho ni zaidi ya kilomita 35 kutokea Morogoro Mjini. Kufika huko, ulitakiwa ufuate njia ya kuelekea mkoani Iringa, mpaka unafika eneo la SangaSanga, kisha unachepuka njia ya kushoto uelekeo wa kufuata Kijiji cha Mzumbe. Utapita vijiji vya Kipera, Mlali ndio mpaka unafika Mkuyuni, kwa mtaalamu Katimbwa.

Mama Debora akafanya maamuzi magumu ya kwenda huko akifuata ushauri wa shoga yake, chambilecho mgaagaa na upwa hali wali mkavu. Aliwasili majira ya alasiri, na kukuta halaiki ya watu mbalimbali wenye matatizo yao wamefurika katika upenuni mwa nyumba ya Babu Katimbwa.

Alikwenda kwa mganga huyo kwa baraka zote za mumewe, ambaye alishafanya maamuzi lilwalo na liwe bora kwao ni kupata mtoto kwa njia yoyote. Hali iliyompa matumaini kuwa huenda Babu Katimbwa ni kiboko yao ndio maana watu wamejaa upenuni mwake pomoni.

Katika maongezi na wenzake hapo, akakuta kila mtu kaja pale na tatizo lake linalomsibu. Wapo waliokuja kwa matatizo ya kusaka watoto kama yeye, wapo wanaotafuta waume wa kuwaoa, wapo wenye kutaka ajira na matatizo kedede anuwai mbalimbali.

Majira ya saa 1 usiku ndipo mama Debora akapata nafasi ya kuonana na Babu Katimbwa. "Ooh... Ooh... Woooh... arrr... arrr..karibu mama umeteseka muda mrefu huna mtoto, sawa sawa??? " alifungua mazungumzo yake Babu Katimbwa kwa kupiga ramli kuhusiana na matatizo yake mama Dendesha yaliyomleta pale. "Tawile Mganga tawile nimeteseka sana, ndoa yangu ipo kwenye ukingo, nisaidie Babu nisaidie.... " alijibu mama Debora kwa sauti ya majonzi iliyoambatana na kwikwi na kilio ndani yake. "Usilie mjukuu wangu tatizo naliona hapa kwenye kioo sio kubwa" aliongea kwa mbwembwe zote Babu Katimbwa.

"Nifanyaje mimi maskini nipate mtoto?" aliuza kwa shauku kubwa sasa akiwa na faraja ya tatizo lake kwisha. "Mizimu ya Kichaga kwa upande wa mumeo imekasirishwa na kitendo cha kijana wao kutowasikiliza wazazi wake wakati wa kuchagua mchumba. Walitaka akaoe nyumbani na sio ubakini. Hivyo mizimu wamefunga kizazi chako, inabidi uende kutambika kwenye mlima Kolelo, ufike mpaka ziwa Hengero, ueleze shida zako kuna kitu utapewa utakileta pindi utapopewa huko, shida yako itakuwa imekwisha" alizungumza Babu Katimbwa huku akionyesha ameshamaliza kazi yake.

Mama Deborah akatia kwenye kikapu pesa ya kusagia mkungu kwenye kikapu cha kuwekea pesa, kisha akanyanyuka na kutoka nje ya chumba tayari kwa kujipanga kuelekea mlimani.


Tarehe 02/03/1986, Mwalimu Minja ndio alipiga ripoti rasmi kwenye ofisi zake mpya. Ofisi zake mpya za "Peace Corps-Tanzania" zilikuwa zipo katika mtaa wa Uhuru, Jijini Arusha. Ofisi ambazo zilikuwa mkabala na ofisi za Mkuu wa Mkoa wa Arusha. Ilikuwa ni ofisi ndogo yenye chumba 3, ambazo ni ofisi ya Mratibu Mkuu, Katibu Muhtasi, Mhasibu na Ukumbi wa mdogo wa mikutano. Ofisi pia ilimpangishia nyumba ya kifahari yenye kila kitu muhimu ndani yake, katika mitaa ya 'Philips', huku ikimpa gari la kutembelea aina ya 'Mitsubishi Double Cabeen'. Kwa ufupi maisha ya Mwalimu Minja yalibadilika mno, kutoka kuitwa Mwalimu Minja mpaka Bosi Minja. Kutoka kuwa Mlalahoi wa kushinda darasani na kubugia vumbi la chaki kufundisha watoto mpaka kuwa Mlalaheri mwenye kupulizwa na feni ofisini muda wote.
Safari za ng'ambo kwake zikawa hazikauki kama chemchem ya maji, chakula chake ni cha kununua kwenye 'Masupamaketi' makubwa ndani ya muda mfupi akabadilika kwa umbile, muonekano, hali ya kiuchumi mpaka tabia zake. Mitaa yote ya Arusha alipata umaarufu wa ghafla kuanzia Njiro, Moshono, Kijenge, Philips, Sekei, Sanawari, Ungalimited na kwingineko kote, huku muonekano wake unaomtambulisha ni vazi la kaunda suti. Umaarufu wake ulianzia kwenye Baa kutokana na ofa anazotoa ovyo kwa wahudumu na walevi wenzake, kama ujuavyo masikini akipata makalio hulia mbwata. Mlio wa gari lake likipita tu mitaani kila mtu utaskia 'Bosi Minja Mlezi wa Wana huyooo anasepa zake'.
Pindi anaposafiri kikazi akakosekana kuonekana kwenye viwanja vya starehe na wadau wake, Jiji linaonekana limepooza vilivyo halina tena amsha amsha. Kwa ufupi ni kwamba ndani ya muda mfupi alishajitengenezea himaya yake ndani ya Jiji la Arusha. Licha ya mikikimikiki yake katika kukimbizana na starehe, lakini mnyonge mnyongeni haki yake mpeni, jambo zuri zaidi kwake lilikuwa ni ukaribu wake na binti yake wa pekee Debora. Alikuwa anahakikisha mwishoni mwa juma siku za mapumziko kazini, anashinda na binti yake muda mwingi. Debora nae alimzoea baba yake vilivyo hasa ukichukulia kuwa wakati wote alikuwa anamuona baba yake, mama yake hayupo, yupo masomoni kusini mwa Tanzania, mbali huko kutokea kaskazini.
Debora aliandikishwa shule bora ya Kimataifa inayofundisha kwa lugha ya Kiingereza, inayoitwa 'Arusha International School' kama mwanafunzi wa Chekechea. Ndani ya muda mfupi alikuwa anatema yai mdomoni kiufasaha utasema amezaliwa Uingereza kwa Malkia, kumbe wazazi wake ni waswahili, weusi tii wenye nywele koto.
Ilikuwa ni shule ya tabaka a'ali wanayosoma watoto wa Vigogo wa Balozi mbalimbali, Wafanyabiashara wakubwa na watoto wa Wakurugenzi na Mawaziri kutokana na ughali wa ada yake. Bosi Minja nae alijitutumua vilivyo Binti yake aweze kusoma shule bora, ili apate elimu bora na sio bora elimu.
Kwa upande wa mapenzi kwa mkewe Bi.Mwenda au Mama Debora, taratibu yalianza kupungua, kama maji ya mvuke yanavyopotea angani kidogo kidogo. Chambilecho 'kisicho machoni na moyoni hakipo' umbali baina yao ulianza kuwa kikwazo kikubwa kwa ndoa yao. Siku zote mawasiliano huimarisha mapenzi na hufanya wahusika kujihisi wapo pamoja hata kama wametenganishwa kwa maelfu kwa maelfu ya maili. Inapotokea kuwa na ufinyu wa mawasiliano ndipo hali ya mapenzi ya upande mmoja hupungua na kuhisi kwamba tayari mwanamke/mwanaume tayari ameshapata mwingine wakumfanya asifanye mawasiliano ya mara kwa mara.
Miaka hiyo ya 80's-90's hamna simu za mkononi, zaidi ya kutegemea mawasiliano kwa njia ya barua, au simu za mezani kwa baadhi ya watu wachache. Barua ambayo ukiandika leo basi kumfikia mhusika wako itachukua takribani wiki moja mpaka mbili kumfikia kutegemeaana na umbali wa mhusika. Miezi ya mwanzoni walikuwa na juhudi walau kwa mwezi mara moja kuandikiana barua lakini sasa ilishakatika miezi 6 hamna barua wala salamu. Mama Debora alikuwa hodari kwelikweli wa kuandika barua, lakini upande wa pili wa mumewe, Bosi Minja mikono ilikuwa mizito kujibu barua utasema imefungwa mawe vidoleni.
Mama Debora kiroho chake kikawa kinampigapiga, maana sasa hajui hali na usalama wa mumewe wala wa kinda wake Debora ambaye sasa alibakiza miezi michache atimize miaka 4. Masomo tena yakawa hayapandi kichwani, muda wote anamuwaza mumewe Bosi Minja. Chakula nacho kikawa hakipiti kooni kwa mawazo ya mumewe, mpaka akaanza kuwa kimbaumbau kama mwiko wa pilau. Alikuwa anapungua uzito kwa kasi mpaka wanachuo wenzake wakaanza kumlamba kisogo anaugua ugonjwa wa Juliana au AIDS, huo ulikuwa ni ugonjwa wa UKIMWI namna ulivyokuwa ukijulikana miaka hiyo. Unyanyapaa ulikuwa kwa kiwango cha juu sana, mpaka wakaanza kumtenga wakimuogopa atawaambukiza UKIMWI. Wagonjwa UKIMWI miaka hiyo walikuwa wanapachikwa majina ya ajabu ajabu mara mgonjwa Fire, Silimu, mdudu na mengineyo mengi. Vyombo vyake hamna aliyekuwa anavigusa tena, wakisalimiana hawapeani nae mikono tena kama zamani na vitendo vingi vya kumtenga. Hawakujua kama mwenzao anatafunwa na gonjwa la mapenzi, gonjwa ambalo ni hatari maradufu kuliko hata UKIMWI. Gonjwa ambalo lina uwezo wa kukutoa uhai kwa ugonjwa wa kiharusi, mshtuko wa moyo au hata sonono.
Mama Debora hakuwajali kitu, maadamu alikuwa hana mashaka na uzima wake, akajua tu watasema mchana usiku watalala. Akaweka azima na nia moyoni kuwa chuo kitakapofungwa likizo kubwa mwezi Disemba atapitiliza kimoja mpaka Jijini Arusha akajue mbivu na mbichi za mumewe nini kimemsibu mpaka anazembea kujibu barua.
Hisia zake zilikuwa zinamtuma kuwa kuna mwanamke mwenzake anamega penzi la mumewe sio bure. Alitaka aende ghafla bin vuu bila kutoa taarifa, amfumanie mwizi wa penzi lake, ama kweli adui wa mtu ni mtu, alikuwa haelewi inakuaje mwanamke kwa makusudi unaharibu ndoa ya mwanamke mwenzako. Mkuki kwa nguruwe mtamu lakini kwa binadamu mchungu, laiti wewe unayeharibu ndoa ya mwenzako yangekukuta wewe ungetoa kilio dunia nzima ifahamu. Lisemwalo lipo kama halipo linakuja, hisia zake zilikuwa sahihi mia fil-mia, Bosi Minja alinasa kwenye penzi jipya akawa hajiwezi wala hajitambui. Mzee mzima alinasa kwenye penzi jipya la binti wa Kimachame, aliyetumwa pesa kwao, hakuja Jijini Arusha kuuza sura.


'Recho Miondoko' alikuwa ni msichana wa rika la hirimu mwenye uzuri wa shani, mithili ya kipepeo kwenye bustani ya maua. Recho kama angekuwa ni ndege basi angefananishwa na tausi, na kama angekuwa ni moja katika anuwai za maua ya bustanini basi usingesita kummithilisha na uwaridi.
Alikuwa ni msichana aliyekamilika kila idara katika mwili wake kuanzia kichwani kwenye nywele zake mpaka kwenye kucha za vidole vya miguu yake, kila kiungo chake kilikuwa kinavutia. Alikuwa ni chotara wa baba Muitaliano kwa mama wa Kimachame, mchanyato wa wazazi ambao ulitoa Binti kisura wa kustaajabisha kwenye kila jicho litakalothubutu kumkodolea mlimbwende huyu. Binti huyu alilelewa na mamaye pekee, baba yake alikuwa anaishi nchini Italia. Alikutana na mama Recho alipokuja nchini Tanzania mwaka 1961 kwenye ziara ya Utalii wa kupanda Mlima Kilimanjaro. Mama yake alikuwa ni Kirukanjia mstaarabu mwenye kuzikamatia fursa za kutembea na watu Walalaheri, wenye ngwenje zao ambao ni mikono wazi wasio na mikono ya birika.
Vijana wengi walijitokeza kutaka kumchumbia mama Recho katika usichana wake lakini kwake kigezo cha kwanza alikuwa anaangalia unene wa pochi zao na kuwaona ni makapuku tu, wale wa mishahara tonge watamchakaza na kumzeesha huku wakimuacha solemba. Alitaka aolewe na mtu mwenye kipato na kama hatojitokeza aheri afe bila ndoa.
Alikuwa ni mtumishi katika kampuni ya kusafirisha na kutembeza Watalii kwenye vivutio mbalimbali vya kitalii nchini Tanzania. Hivyo kazi hiyo ikawa inamfanya anadaka madanga ya maana yaliyomrahisishia maisha yake kwa kumjengea nyumba ya kisasa, usafiri na kumfanya aishi maisha mazuri yanayozidi kipato chake cha mshahara. Katika harakati zake hizo za kujitafutia kipato cha haramu ndipo akapatikana Recho, akiwa ni mtoto wake wa kwanza. Jina lake halisi ni 'Rachel Francesco Gabriele', lakini hili jina la Recho Miondoko ni jina mpachiko alilopewa lakabu hiyo tokea skonga sekondari kule 'Machame Girls' na wanafunzi wenzake kutokana na mitembeo yake iliyojaa nakshinakshi na madahiro kama mlimbwende wa mashindano ya Miss Tanzania.
Alikuwa na miondoko ya njiwa, ukimuona jinsi anavyotembea lazima umtazame kwa muda. Maisha yake yote ya kielimu kuanzia shule ya msingi mpaka chuo, Recho alikuwa ni mtu wa kupatwa na visanga vya dhuluma za kingono. Uzuri wake ulikuwa ni karaha kwake, mpaka akazoea kuwa ni jambo la kawaida na kumbadilisha tabia yake. Manyanyaso hayo alikuwa anayapata kuanzia kwa wanafunzi wenzake, walimu mpaka na Mababa watu wazima wenye familia zao nyumbani.
Kipo kisanga kilimkuta wakati ndio anaripoti tu kidato cha kwanza 'Machame Girls', wanafunzi wakongwe wa kidato cha nne wale watukutu waliwahi kumteka usiku wa manane na kwenda kumchunguza kama matiti yake yaliyosimama kama mwiba aina ya mchongoma ni yake asilia au ni feki, anawachoresha tu. Imani zao zilikuwa zinawatuma matiti yake ni feki tu anapewa vifaa maalumu vya kuyanyoosha na baba yake mzungu, toka huko Utaliano. Bado wale wenye kumrushia matusi ya nipe nikupe tena yale ya nguoni bila sababu yoyote ya msingi wivu tu Bado dhuluma lukuki alizokuwa anafanyiwa na walimu wa kiume ambao wengine wana umri sawa na baba yake mzazi zikiwemo za kushikwa makalio yake na hata kutomaswatomaswa chuchu zake.
Kama sio usimamizi makini wa Mkuu wa shule ambaye alikuwa hana msalie Mtume kwa mwalimu yoyote atakayebainika kumnyanyasa kingono mwanafunzi, basi Recho hata kidato cha nne asingefanikiwa kumaliza shule, angekuwa ameshageuzwa asusa na walimu hao waroho wenye uchu wa fisi. Hali hiyo ya kuonekana ni mrembo na kusifiwa kila kona anayokatisha kuwa uzuri wake sio wa nchi hii ni wa kipekee, ikamjengea kiburi Recho na kumfanya ajione ni mwanamke wa sayari nyingine kabisa, asiyestahili kuishi kwenye dunia hii. Miluzi mingi anapopita walipokaa wanaume wakware wenye uchu wa fisi kwa vidosho warembo kama Recho na zile sauti za tsssssiiiiiitsssssiiiii apitapo vijiweni za kumuita zilimchanganya kabisa na kumtoa fahamu, akaanza kujiona ni kama malaika aliyepotelea duniani kimakosa.
Akajihisi yeye hadhi yake ni kuishi mbinguni anayakanyaga mawinguni, na sio duniani anayakanyaga matope. Hizo kelele zilizidi kumfanya azidishe mbwembwe zake za kutembea hivyo kusadifu kabisa jina lake la Recho Miondoko. Lifti lifti za gari anazopewa na Vibosile huko barabarani na kuchunguliwa kwenye kioo cha magari sight mirror pindi wakipishana nae na madereva vilizidi kumchanganya Recho na kumzuzua zuzu. Hali ambayo ilimpelekea asiwekeze nguvu zote kwenye masomo yake kwa kigezo kuwa ni mzuri sana hivyo atakuja kupata mume mwenye uwezo mkubwa wa kipesa, ambaye atamtengenezea maisha yake kiulaini.
Akaanza kula kuku kwa mrija bila kuvuja jasho katika umri mdogo kabisa. Wahenga wanasema Asiyefunzwa na mamaye, hufunzwa na ulimwengu, wanaume wakware walivyolitambua hilo hawakujivunga, waakaanza kumla Recho kama embe bichi linavyoliwa na chumvi bila kusubiria liwe bivu. Wakamgeuza kuwa ghashi wa mahonyo, ili mradi umemfuata na ngwenje sufufu tu unakula mzigo. Hakuna ladha ya pombe anuwai yoyote asiyowahi kuionja.
Recho alikuwa anapenda kuishi maisha ya fawaishi yaliyo nje ya umri na uwezo wake. Mpaka anakaribia kumaliza kidato cha nne alishanusurika mara kadhaa kufukuzwa shule kutokana na tabia zake mbovu.
Maisha ya shule ni kama mshumaa usio mkesha, ni matamu sana lakini ni mafupi sana, ukileta mchezo na shule, matokeo ya 'NECTA' yatakuumbua. Matokeo ya mitihani ya kumaliza kidato cha nne yalivyotoka, Recho alipata daraja la nne, chupuchupu azungushe sifuri, asipate cheti. Alivuna alichopanda shuleni, ukipanda bangi tegemea kuvuna bangi na sio vinginevyo. Ahsante kwa uwepo wa somo la Kiswahili na Siasa zama hizo, ndio masomo yaliyombeba Recho na kumpa daraja la 4. Hivyo hakuchaguliwa kuendelea na elimu ya kidato cha tano na sita Advance Level.
Hali hiyo ilimpelekea mama yake mzazi ahangaike huku na kule, kwa kutumia njia za panya kama kawaida yake anapolitaka jambo lake lifanikiwe, akafanikiwa kumpatia nafasi kwenye chuo cha Uhadhiri Tabora. Chuo ambacho kilikuwa chini ya Wizara ya Utumishi wa Umma kikiwa na malengo ya kuwaandaa Makatibu Muhtasi katika ofisi za umma. Huko nako chuoni, Recho hakuacha tabia zake za kuendekeza starehe. Kuna kipindi vigogo walikuwa wanamlipia nauli ya ndege na kumtorosha Chuoni kwa baadhi ya mwishoni mwa juma, kisha kwenda nae kula bata. Alishashirikishwa kwenye madili kibao ya utapeli wakimtumia Recho kama chambo cha uzuri wa kuwaingiza mkenge walengwa wao.
Hakuna marefu yasiyo na ncha, baada ya miaka mitatu akawa ameshahitimu kwa ngazi ya Diploma, akiwa sasa yupo tayari kwa kuajiriwa kwenye taasisi za umma na mashirika yake. Kimaadili Recho hakustahiki kabisa kuwa mtumishi wa serikali, alikuwa ni jambazi aliyejivika ngozi ya kondoo. Daima Recho alikuwa anawahadaa watu kwa uso wake wa udhu na adabu. Walikuwa wanamuona ni mstaarabu mwenye kujiheshimu. La hasha lillah wa audhu billahi Recho hakuwa mwema kiasi hicho kama wanavyomdhania, laiti wangemjua wasingediriki kutaka kumpa ajira kamwe. Unaambiwa siku ya sherehe ya kuhitimu Wanachuo wa Uhadhiri, Tabora, vigogo wa nchi enzi hizo kuanzia Wakurugenzi na Mameneja walikuwa wanajazana kwa pashau kubwa kuchagua Makatibu Muhtasi wa kuwaajiri kwenye Ofisi zao.
Wale warembo walikuwa wanagombaniwa kwa ahadi lukuki za mishahara minono na marupurupu. Nyuma ya pazia, vurugu hizo zote za vigogo, zilikuwa ni za kusaka vimada wao wapya. Walijiwekea utaratibu usio rasmi lakini uliozoeleka wa kuwageuza Makatibu Muhtasi wao kuwa ni mahawara wao, ambao wanajitanua nao na kujimwayamwaya nao vyovyote watakavyo, na wakati mwingine kusafiri nao kikazi popote wanapokwenda. Wasichana hao madhulumu wa kingono bila kujielewa walijiona ni watu muhimu sana katika nchi mpaka vigogo wa nchi nzima wanafunga safari toka pande mbalimbali za nchi kuja kuwafuata wao Tabora.
Kwa upande wa Recho mambo kwake yalikuwa ni kama moto wa gesi, vigogo baadhi yao walifikia hatua mpaka ya kutwangana masumbwi hadharani ili mradi kila mmoja aondoke na Recho kwa jino na ukucha ili akawe Katibu Muhtasi wake. Ile rangi yake ya uchotara ilizidi kuwakoroga nyoyo zao. Bahati yake Recho, mama yake mzazi tayari alishamuandalia mchongo wa ajira nono kwenye ofisi za "Peace Corps-Tanzania" tawi la Arusha. Alishaahidiwa mshahara mnono na marupurupu lukuki zikiwemo na safari za kutembelea ughaibuni. Hiyo ndio ikawa ponapona yake kutoka kwa mabazazi hao wenye ulaibu wa ngono.
Hivyo Recho alikuwa anapelekwa ofisini kwa Bosi Minja kwa kimemo cha kigogo mzito. Bosi Minja alikuwa anapelekewa kukumbatia mzinga wa nyuki bila kujua madhara yatakayokuja kumsibu.


Ilikuwa ni asubuhi yenye kibaridi cha wastani, huku juu kukiwa na mawingu ya kutosha dalili ya kutaka kunyesha mvua saa yoyote. Recho alikuwa ameshafika kwenye ofisi za Peace Corps Tanzania zilizopo Jijini Arusha. Alijihimu kwelikweli kimuhemuhe cha ajira mpya. Alikuwa amevalia suti zake za kike za rangi ya kijivu na chini kavaa viatu vyeusi. Alipendeza kwelikweli kwenye vazi lake la heshima alilovaa. Nywele zake nyingi na laini kama sufi alizifunga na kibanio mtindo wa mchicha.
"Habari za asubuhi, samahani nataka kuonana na Mratibu wa Ofisi ya 'Peace Corps-Tanzania'..!" aliuliza Recho kwa dada kibarua wa usafi. "Bila samahani ingia hapo ndani, utawakuta wenzako wapo foleni wenye shida kama yako..!!" alijibiwa na yule mhudumu wa usafi huku amempa mgongo Recho anadeki sakafu ya kibaraza. Alipoingia tu, alipotupa macho upande wa kulia, mbele ya ushoroba wa ukuta na ukuta, akaona chumba kimoja juu yake kuna kibao kimeandikwa "Coordinator-Peace Corps". Pembeni yake kuna msururu wa watu kama 8 wanaelekea huko, na yeye akawa wa 9. Akatafuta nafasi huru na kukaa, akisubiria zamu yake.
Shingo feni za wale aliowakuta zilizokuwa zinamuelekea yeye zikamjulisha kuwa kapendeza hana haja ya kutafuta kioo kujikagua. Baada ya kama dakika 35 hivi zamu yake ikafika. Akanyanyuka kwenye kiti akajongea mpaka mlangoni, akabisha hodi mara moja, akanyonga kitasa na kuingia ndani mubashara. "Shikamoo Bosi..!" alisalimia Recho wakati Bosi Minja amempa mgongo kuna faili alikuwa analitafuta kabatini mwake. "Marhabaa karibu sana binti....karibu kwenye kiti" aligeuka Bosi Minja, na kutokana uzuri aliouona kwa Recho, faili likamdondoka mpaka chini na kuyatawanya makaratasi chini ovyo. Recho akakimbilia kuinama kuyaokota makaratasi yale huku sketi yake imepanda juu ikiyaacha sehemu kubwa ya nyuma ya miguu yake ya kizungu kuelekea mapajani ikiwa wazi. Bosi Minja macho yalimkodoka kama mjusi aliyebanwa na mlango akiwa tayari kashapata mfadhaiko wa mwili. "Ahsante sana kwa kujali Binti karibia kiti" alipokea faili toka kwa Recho na kuvuta kiti chake akakaa.
Nae Recho akavuta kiti akakaa na kumkabidhi barua yake Bosi Minja. "Oooh....karibu sana kumbe ndio mtumishi mwenzetu mpya, nilipewa taarifa yako kuwa utakuja wewe baada ya kustaafu mama Pamba mwezi uliopita" aliongea Bosi Minja baada ya kumaliza kuisoma barua aliyokabidhiwa na Recho. "Ahsante Bosi wangu nimekaribia..!!" alijibu Recho huku anajitia kuinama chini kwa aibu. Baada ya mazungumzo mawili matatu wakanyanyuka na kwenda kuonyeshwa ofisi yake.
"Sasa umekuja kuanza kazi na mguu wa heri, jiandae kesho kutwa tuna safari ya kikazi Jijini Nairobi" aliongea Bosi Minja huku akiwa amemkazia macho Recho. Kusikia safari tena nje ya nchi, Recho alilipuka kwa furaha, "Ahsante Bosi wangu naahidi sitokuangusha katika uchapaji kazi wangu..!!". Tayari Bosi Minja alishaanza kumtupia chambo, ambacho kilikaribia kumnasa Recho. Bosi Minja alichokuwa hakijui ni kuwa Recho sio bwege mtozeni kama anavyomfikiria, na yeye anajitahidi kumuingiza kwenye mstari Bosi wake ili aanze kumchuna kwa kuanza kujilia mafao ya uzeeni kabla ya kustaafu. Recho alikuwa yupo tayari kwa chochote ili mradi kitampa pesa maridhawa.
Mipango yake Recho ilikuwa ndani ya miaka 5 asake pesa kwa udi na uvumba kisha aache kazi na kuanza kufanya biashara zake binafsi kabla hajavuka miaka 30. Mfano wao ulikuwa ni wa Pwagu na Pwaguzi, Bosi Minja anajiandaa kuuza cheni feki, na Recho anajiandaa kulipa kwa pesa bandia, hivyo ugali moto, mchuzi moto. "Je unayo hati ya kusafiria? " aliuliza Bosi Minja huku akiwa anajimiminia chai ya maziwa kwwnye kikombe chake, akaanza kukoroga sukari huku anasubiria jibu la Recho. "Hapana sina, sasa sijui itakuwaje na muda ni mfupi labda uende tu peke yako ili nianze kushughulikia hiyo hati ya kusafiria!" alijibu Recho huku akimpima upepo Bosi kwa kujifanya kama hana papara na safari vile.
"Oooh No...lazima uende, kuna majukumu mengi kama Katibu Muhtasi wangu unatakiwa uyatekeleze huko. Nitamwambia dereva akupeleke ofisi za uhamiaji ili upate hati ya dharura kwa haraka" mishipa ya shingo ilimtoka Bosi Minja akilazimisha lazima Recho asafiri nae jambo ambalo lilimfanya Recho achekee tumboni akijua tayari Bosi wake ameshamkamata hachomoki tena. Baada ya kumaliza maongezi yao na kukabidhiana majukumu ya kazi wakaagana huku akimuahidi kumpatia nyumba ya kulala ya ofisi, iliyokuwa inakaliwa na Katibu Muhtasi mstaafu ndani ya wiki mbili baada ya kuifanyia usafi na ukarabati.
Baada ya hapo akapelekwa kwenye ofisi za uhamiaji kwa ajili ya kukamilisha taratibu za kupata hati ya kusafiria ya dharura. Akatakiwa awasilishe kitambulisho chake cha kazi na picha mbili alizopiga hivi karibuni. Akahangaikia vitu hivyo kisha akalipia mpaka kufika alasiri akawa tayari ameshakamilisha kila kitu. Aliporudi ofisini kuleta mrejesho wa uhamiaji akakuta na tiketi yake tayari imeshaletwa akakabidhiwa mkononi. Furaha aliyokuwa nayo Recho ilikuwa haielezeki, na alishindwa kuizuia. Ilikuwa ndio mara yake ya kwanza kutaka kupanda ndege. Ilitakiwa wasafiri kwa ndege ya shirika la ndege la Tanzania ATC.
Aliporudi nyumbani Recho alikuwa anazunguka na tiketi ile kila anapokwenda mpaka chooni, huku akiona kesho kutwa mbali sana, masaa yanaenda taratibu mno, aweze kutimiza ndoto yake.
Siku iliyofuata hawenda kazini akijiandaa na safari hiyo kwa kufanya manunuzi ya nguo na vitu vidogo vidogo anavyohitaji safarini. Usiku wake hakulala kabisa, walitakiwa waripoti manane ya usiku na ndege inaondoka alfajiri. Chezea pipa wewe, kila alipojaribu kuuvuta usingizi uje ndio ulizidi kupaa akawa anajigagaza kitandani na tiketi yake ipo chini ya mto wa kitanda kila wakati anaiangalia kama ipo. Ilipofika saa 7:00 akaamka zake na kwenda kujimwagia maji tayari kujiandaa na safari.
Usiku huo alilijipodoa kama vile anaenda harusini, alijipamba akapambika. Ilipofika saa 8:05 akasikia honi ya gari iliyokuja kumchukua kumpeleka uwanja wa ndege. Akachomoka mbio mbio na begi lake dogo, tayari kuelekea kiwanjani. Baada ya nusu saa akawa ameshawasili uwanjani. Kwa bahati nzuri Bosi Minja alikuwa ameshawasili kitambo. Wakasalimiana kwa bashasha kwa mtindo wa kukumbatiana. Mara wakaanza ukaguzi wa kuingia ndani kwenda kusubiria ndege. Bosi Minja akapita salama kwenye ukaguzi, kimbembe kikamkuta Recho. "Samahani dada haturuhusu kuingia na manukato 'perfume' ndani ya ndege" alipewa hiyo taarifa na mkaguzi huku kwa vitendo akiitumbukiza kwenye pipa la taka. Recho aliumia mno kwa kitendo hicho, hasa ukichukulia kainunua jana yake tu tena kwa bei ya kupaa. "Ondoa shaka, Nairobi ni Jiji kubwa sana tena zaidi ya Dar es Salaam, nitakupeleka kufanya manunuzi mpaka utachoka wewe" aliongea Bosi Minja kwa sauti ya kumbembeleza Recho ili asijisikie vibaya. Recho akatabasamu na kujidekeza kwa Bosi wake kwa kumshukuru kwa kumkumbatia kwa nguvu bila kumuachia Bosi wake huku matiti yake machanga yakimchoma choma kifuani Bosi Minja.
Tendo ambalo lilichafua hali ya hewa, tayari Bosi Minja alianza kuhema juu juu kama mwanariadha. Recho akamuachia na kujitia kuna kitu anakitafuta kwenye pochi yake huku anamkata jicho pembe Bosi wake kumuona jinsi anavyohangaika kuirekebisha suruali yake ambayo maeneo ya sehemu za siri ilishatuna. Ikabidi Bosi Minja azuge kuaga anaenda msalani kujisaidia. Recho akaelewa mchezo mzima kuwa Mzee mzima anaenda kuweka mambo sawa vinginevyo ataadhirika mbele za watu. Kimoyomoyo Recho alikuwa anafurahia kuutema moyo wa Bosi wake ili aweze kumtafunia pesa zake ipasavyo. Ilipofika saa 10:30 usiku juu ya alama wakaingia kwenye ndege tayari kwa kuanza safari ya kuelekea Jijini Nairobi. Hawakukaa siti za jirani, walitenganishwa kwa sababu tiketi zilikatwa siku tofauti.
Safari hii Recho hakuwemo kwenye mahesabu, Bosi alilazimisha tu ili aweze kutekeleza ajenda yake ya siri ya kumgeuza Recho kuwa mpenzi wake rasmi, kama nyumba ndogo. Recho ujanja wote ulimuisha akiwa ndani ya ndege, mhudumu anatoa maelekezo ya kufunga mkanda, yeye hajui namna ya kufunga maana mwanzoni akidhania unafungwa kama mkanda wa kwenye gari. Ikabidi amuwiye mhudumu aje kumpa msaada wa kumfunga mkanda. Haikuchukua zaidi ya saa 2 wakawa tayari wameshawasili uwanja wa kimataifa wa Jomo Kenyatta 'Jomo Kenyatta International Airport'. Uwanja huo wa kimataifa upo eneo la Embakasi Jijini Nairobi, na zamani ulikuwa unajulikana kama 'Embakasi Airport' ila ulibadilishwa jina na kuitwa Jomo Kenyatta mwaka 1978 kwa heshima ya Rais wa kwanza wa Kenya Mzee Jomo Kenyatta.
Uwanja huo ni bonge la uwanja unahudumia abiria zaidi ya milioni 7 kwa mwaka huku ukishika namba 7 Afrika kwa kuhudumia wateja wengi. Ulikuwa unatoa huduma za kusafirisha abiria kwa zaidi ya nchi 50 duniani. Baada ya kukamilisha taratibu zote za uhamiaji pale uwanjani wakapanda taksi maalumu iliyotayarishwa kwa ajili yao na kuwapeleka kwenye Hoteli ya 'Villa Rosa Kempinski', hoteli ambayo ina hadhi ya nyota tano. Mwanzoni Bosi Minja akitaka kuleta ubazazi wake asubuhi na mapema kwa kumtaka Recho wachukue chumba kimoja, lakini Recho hakutaka kujionyesha yeye maharage ya Mbeya, maji mara moja akatia ngumu. Kijasho chembamba Bosi Minja kikamvuja akiona dalili za kuweza kumkosa Recho hivi hivi asipozichanga vyema karata zake. Walipofika wakapeana miadi ya kupumzika ila majira ya alasiri watoke mtoko wa kupita madukani kufanya manunuzi.
Hoteli hiyo waliyofikia kila kitu kilikuwa kinapatikana ndani yake kuanzia mkahawa wa chakula, baa ya kuuza vinywaji, mabwawa ya kuogelea, kumbi za mazoezi zilizoshiba vifaa, ilikuwa ni sehemu nzuri kwa mapumziko. Recho mchana hakwenda mkahawani, aliagiza huduma aletewe chumbani mwake 'room service'. Ilipofika saa 10:30 alasiri, taksi maalumu ikaja kuwachukua kwa ajili ya kuwatembeza madukani. Recho alitinga nguo matata zilizompendeza haswa, Bosi Minja alidata haswa akawa anajiapiza kimoyomoyo kuwa iwe isiwe, iwe mvua iwe jua lazima abebe jimbo kwa Recho.


Breki yao ya kwanza iikuwa mtaa wa Victoria, ambao miaka ya sasa umebadilishwa jina na kuitwa 'Tom Mboya Street'. Mtaa huo ukibeba jina la mwanasiasa maarufu nchini Kenya. Mtaa huo kama utakatisha Nairobi ya leo utakutana na majengo ya kibiashara kama 'Jade', 'Sasa Mall', 'Maduka Exhibition', 'World Business Centre', 'Domino Shopping Mall' na 'Imenti House'. Watu wa mataifa mbalimbali waliopo Jijini Nairobi, walikuwa wanamiminika kwenye maduka hayo kama kumbikumbi kufanya manunuzi ya vitu mbalimbali.
Recho akawa anapitishwa kwenye maduka ya nguo na vipodozi. Huko kote pochi nene ya Bosi Minja ilikuwa inatetema tu kufanya malipo. Kila alichokitamani Recho, Bosi Minja alimnunulia jioni ile. Alikuwa anamfanyia fadhila za kumlisha jogoo mchele mchana, kisha jioni unamchinja unamla kwenye wali. "Wewe chagua tu, tatizo sio pesa tatizo ni matumizi" alijitapa Bosi Minja mbele ya kidosho ambaye usoni anaonekana ni mwema kumbe ni jangili aliye na malengo maalumu ya kumfilisi Bosi Minja.
Mitaani kote walikuwa wameng'ang'aniana kama ruba, hata asiyewajua akiwaangalia tu, lugha ya ishara ilikuwa inaonyesha ni wapendanao. Wakapita kwenye maduka ya vifaa vya kieletroniki, Recho akavutika kuingia kwenye moja ya hayo maduka. "Nahitaji Kamera, nipate picha za kusimulia nyumbani kuwa siku moja niliwahi kukanyaga Jijini Nairobi..." aliomba Recho anunuliwe Kamera, wazo lililomjia ghafla njiani kuwa itamsaidia kwa matumizi yake binafsi. "Hamna shida, picha ni muhimu kwa ajili ya kumbukumbu unaweza kupiga picha za kuonyesha wajukuu miaka hiyoo ijayo..!" alitilia msisitizo wazo la kununuliwa Kamera hiyo.
Walipomaliza manunuzi yote wakapeleka vitu vyao walivyonunua kwenye Hoteli waliyofikia kisha wakarudi mtaani kwa mara nyingine tena kwa ajili ya kustarehe. Kamera ile ndogo ya kisasa Recho aliiweka kwenye mkoba wake wa mkononi, akiamua kutembea nayo ili kuweza kuchukua picha za matukio mbalimbali ya Jijini Nairobi. Magharibi hii sasa walielekea kiwanja cha kujirusha matata sana, kinaitwa 'Black Diamond Bar & Grill' kilichopo maeneo ya Mpaka road, Westlands. Vibopa na wenye pesa zao walikuwa wanatumbua maisha kwa nguvu za pesa zao nyingi kama mchanga. Huko sasa ikawa ni mtindo wa kula nyama choma kwa vinjwaji sampuli mbalimbali.
Recho alikuwa anapupia chakula walichoagiza kama nguruwe kutokana na njaa iliyokuwa inamtafuna. Kisha akaanza kushushia chakula kile kwa vinywaji. Mwanzoni Recho alizuga kuwa sio mzoefu wa pombe, kumbe ni jabali aliyekubuhu ana uwezo hata wa kumaliza sanduku zima la bia na macho yake ni makavu kabisa. Mchaga asiyekunywa pombe huyo basi ni mfiadini kwelikweli, lakini kwa kawaida pombe ni sehemu ya maisha yao. Burudani nyingine za muziki wa bendi mubashara 'Live Band' ilikuwa inatumbuiza, ili mradi kuleta mashamushamu eneo lile.
Wateja walikuwa wanaenda wanalipia kwa kuchagua nyimbo wanazozipenda wachezewe. "Ikifika saa 7 usiku juu ya alama tuondoke zetu, kesho kikao ndio kinaanza tusije tukashindwa kuwa makini kwenye kikao, tukaonekana watalii" aliongea Bosi Minja akimpa tahadhari Recho, kuwa wasijisahau. "Mmhhh....kama hivyo tuondoke sasa hivi, au mie sitokunywa tena pombe kuanzia sasa nitakuwa mpenzi mtazamaji tu... " aliongea Recho kwa kudeka, akitegesha jambo lake. "Aaaah....hiyo haiwezekani kabisa, lazima tunywe wote..!! " aliongea Bosi Minja kwa sauti ya kubembeleza huku akikichezea kiganja cha mkono cha Recho na akimimina pombe kwenye glasi ya Recho.
"Basi kama ni hivyo, tutafute sehemu ya kulala ingine ya dharura jirani na hapa, mie sipendi nirudi kule nimezima kama maiti, sipendi kabisa kuchafua hadhi yangu, ile ni Hoteli ya Kimataifa, kumbuka huo mkutano ni wa kimataifa, wasije kuondoka na taswira mbovu dhidi ya nchi yetu ya Tanzania..... ....! " aliongea Recho akiwa sasa amejiegemeza kwenye bega la Bosi Minja, huku nywele zake laini kama unyoya za uzungu koko zikiwa zinamtekenya na kumpa raha inayomsisimua mwili wake. Walikuwa wanaonekana ni wapenzi wapendanao kama ambari na zinduna. Ombi lake hilo likapita bila kupingwa, maana lengo la Bosi Minja ni Recho azidiwe na pombe iwe rahisi kwake kumfanya atakavyo yeye. Kumbe hakujua Recho nae ana malengo yake mabaya dhidi ya Bosi wake pia, ambayo kama akifanikiwa kuyakamilisha yatampa pesa nyingi sana za mkupuo.
Bosi Minja akanyanyuka kuelekea msalani akimuacha Recho peke yake kwenye meza na msitu wa vinywaji vimeizunguka meza yao. "Samahani dada una ujumbe wako huu toka kwa kaka yule...!" aliongea mhudumu huku anamkabidhi kikaratasi na kumuonyesha kwa ishara ya kidole alipokichukua kikaratasi hicho. "Ahsante....!" akashukuru akakifungua kile kikaratasi na kukisoma na kuanza kuangaza macho kutafuta wapi kilipotoka hicho kikaratasi. Mapigo ya moyo wake yalianza kwenda mbio mbio, akiwa haamini alichokisoma kwenye kikaratasi kile. Akafumba macho yake na kushusha pumzi ndefu. "Mungu wangu! Martin...Martin...ulipotelea wapi miaka yote hiyoo?? " aliwaza Recho bila kupata majibu kupata majibu. Jasho jekejeke likaanza kumvuja ingawa Jijini Nairobi usiku ule ni baridi ilikuwa inapuliza kama Ulaya.
Akamuona kijana mmoja shamsi matlai wa umbo, nadhifu, mrefu sana, ana kifua cha mataruma ya reli, hana hata alama ya kiriba tumbo, amesimama amevalia suti nyeusi na miwani akimpa ishara ya kumpungia mkono kuwa amfuate, kisha akaelekea uelekeo wa vyooni. Kipindi hicho hicho Bosi Minja akawa ndio anarejea, anatembea kwa kupepesuka toka msalani na kuvuta kiti kukaa. "Sasa zamu yangu mimi, na wewe ulinde vinywaji vyetu...!" aliongea Recho huku akisimama na kuelekea uelekeo wa chooni huku anaangaza huku na kule. Hey...Recho......u mrembo kama siku zote, karibia 5 years Waaaoooh...." aliongea kijana yule huku anamkumbatia Recho. "Oooh....My love... Martin Tenga, siamini macho yangu, ukatupa jongoo na mti wake...!! " akaongea Recho kwa sauti ya kitetemeshi kama mtu anayetaka kulia.
Wakapiga michapo ya haraka haraka, akamuambia aje kuwasalimia mezani kwao, huku Recho akimpanga kuwa wakitoka pale awafuate kwa gari nyuma nyuma mpaka watakapofikia na yule Bosi wake ili waweze kuongea vizuri zaidi kwa kina na mapana. Haraka haraka wakaagana na Recho kurejea tena kwa Bosi Minja. "Nilishaanza kuwa na wasiwasi umepatwa na masaibu gani nusra nikufuate....!!" akaongea Bosi Minja huku anajichekesha. Samahani ni ukweli nimechelewa nimekutana na kijana wa nyumbani kabisa anaishi hapa hapa Nairobi kitambo. "Yuko wapi huenda na mie ninamfahamu..." alijitutumua kumuulizia huku akiwa anaungua joto la wivu kindanindani, akiwa amefura kama hamira.
"Anasema atakuja kukusalimia, maana nimemuambia kuwa Bosi wangu nae ni mtu wa nyumbani, Moshi kafurahi sana...! Aliongea Recho kwa kujiamini akizidi kumtoa hofu Bosi wake. Kidogo Bosi Minja akatulizana, maana alishaanza kuwa na hofu kwanini huyo mgeni akaongelee vichochoroni na Recho...!. "Huyooo....anakuja kaka Martin..." alisema Recho kumwambia Bosi Minja wakati Martin anakuja kwenye meza yao. "Karibu sana kijana wangu, salama lakini?" alikaribishwa kijana Martin na Bosi Minja pindi tu alipokaribia meza ile. "Nimekaribia Mzee wangu, Nairobi tumeshaizoea tumeshakuwa wenyeji haitusumbui.. " alijibu makaribisho yale kijana Martin huku wanaangua kicheko na kupeana mikono. Martin akavuta kiti na kukaa huku wanaendelea soga, wanakichapa kichaga kama hawana akili nzuri vile. Martin alijitia kati katika mazungumzo hayo kama mchuzi wa ugali huku anaongea kama chiriku utasema wamezoeana kitambo kirefu.
"It's time to go now...call a tax driver please.. !" Bosi Minja aliongea kwa sauti ya kilevilevi kuonyesha pombe imeshamkolea. "Hapana, nitakupelekeni na gari yangu hamna shida...!" alijitutumua Martin huku akiwa anaelewa mchezo mzima. "OK..OK.....No Problem....tupeleke Lodge yoyote jirani hapa tukapumzike na mtoto huyu....!" aliongea Bosi Minja huku sasa anaanza kumshikashika hadharani Recho bila uwoga wowote. Wakatoka pale Baa na kupanda gari la Martin wakitafuta nyumba ya kulala wageni jirani na pale Baa. Iliwachukua dakika 5 kuifikia nyumba hiyo ya wageni. Wakauliza vyumba, wakajibiwa vipo ila masharti ya pale hairuhusiwi kulala mwanaume na mwanamke chumba kimoja kama sio wana ndoa. "Hamna shida... hamna shida.tupe vyumba...!" Bosi Minja aliongea akionyesha amezidiwa haswa na pombe. Alikuwa anakunywa mfululizo kwa zaidi ya saa 6. "Ila mie naogopa sifungi mlango wa chumba changu.... Uwe unakuja kuniangalia uzima wangu..! " alitania Recho huku anaagana na Bosi wake wakiwa wamepewa vyumba vinavyotazamana.
Bosi Minja alikuwa anayumba huku anaingia chumbani kwake. Recho alifahamu fika kwa uchu wa Bosi Minja lazima atakuja tu chumbani kwake ndio maana akamtia maneno ya shemere aje kweli atimize anachokitaka kukifanya. Kipindi hicho hicho alishaahidiana na Martin aende kisha arudi tena hapo nyumba ya kulala wageni wayajenge mambo yao kwa kina. Bosi Minja alipoingia chumbani kwake akaenda kujimwagia maji ili alale usingizi moromoro. Kidogo pombe ikampungua alipoangaza mule chumbani anajiona yupo peke yake na sio ile Hoteli yake aliyofikia mwanzoni alipowasili tokea Jijini Arusha. Akatanabahi kuwa walikubaliana na Recho wachukue vyumba kwenye Hoteli ingine. Bosi Minja akatulia kama nusu saa alivyoona sasa kunaweza kukawa kumetulia, akaanza kunyata nyata taratibu akaufungua mlango wake.
Huku roho ya tamaa ya kutaka ule mchezo ilikuwa ikimpelekesha. Taratibu kwa minyato alipiga hatua kuelekea chumba alichopo Recho nyatu nyatu mpaka kwenye mlango wa chumba cha Recho. Bila kuchelewa akanyonga kitasa, kikakubali kufungua mlango akashangazwa chumba hicho kutokufungwa. "Ila mie naogopa sifungi mlango wa chumba changu.... Uwe unakuja kuniangalia uzima wangu..! " sauti ya Recho wakati wanaagana ikajirudia kwa mbali kwenye masikio yake. Bosi Minja akatabasamu, "kumbe alikuwa anamaanisha kweli" aliwaza Bosi Minja.
Akaingia kwa kupenya kama chai kwenye mkate na kuurudisha mlango taratibu akauegamia mlango wa chumba kwa sekunde kadhaa. Chumba kilikuwa kinatoa harufu nzuri, Recho alikuwa ananukia kama ruhani. Taa ilikuwa inawaka, Recho alijilaza kihasara hasara pale kitandani bila kuvua viatu, huku akiwa amefanikiwa kuivua sketi yake tu na kubakia na taiti tu. "Huu ninaotaka kuufanya ni ubakaji, lakini hamna jinsi amezidi kuwa mrembo, inzi kufia kwenye kidonda ni haki yake, atanisamehe tu....! " aliwaza Bosi Minja huki roho yake ikiongezeka kujaa uwoga uliochanganyika na mawazo ya kuupata utamu wa Recho. Akavuta hatua mdogo mdogo mpaka akakifikia kitanda kile ambacho Recho alikuwa amekilalia huku rohoni Bosi Minja akiombea akimvamia asistuke usingizini vinginevyo mipango yake itaharibika. Alipozidi kumsogelea akagundua Recho amelala fefefe hajitambui.
"Shabaashi...pay back time....nimekulipia tiketi ya ndege nje ya bajeti, nimekufanyia shopping, ulidhani bure bure tu, No free lunch....!" alijikuta ananong'ona Bosi Minja huku akianza kuvua singlendi lake na kuacha kifua chake na kitambi chake kuwa wazi. Akaivua pajama yake ya kulalia. Kisha akachojoa kufuli lake na kubakia kama alivyozaliwa, Mzee wa watu na kuliweka pembeni huku tayari ameshapanda kitandani. Taratibu akaanza kuivua ile taiti yake Recho huku akiwa bado yu usingizini taratibu akaanza kuishusha, huku akiwa ana gusa gusa mpododo wake Recho wa kizungu. Aliendelea kuivuta taratibu, kuna sehemu iligoma kidogo alipojaribu kulazimisha tu alishangaa Recho akimtumbulia macho vyema akatabasamu na kumalizia sehemu ya taiti iliyobaki katika mwili wake yeye mwenyewe.
"Nilijua utakuja tu, Nakupenda sana My Boss....!" aliongea Recho kwa sauti nyororo ya wizi huku anamrembulia macho Bosi Minja. Bosi Minja hakujibu kitu zaidi ya kuwa na furaha sheshe na kupaparika utasema amepandwa na shetani. Katika maisha yake toka amezaliwa alikuwa hajawahi kupata mpenzi mwenye hadhi yake na vigezo vya urembo kama Recho. Akaanza kukurika kukuru kakara kwenye uwanja wa samadari, mpaka akaanza kupiga makelele kama mtu aliyepagawa. Haikupita hata robo dakika, Bosi Minja alikuwa ameshamaliza mzunguko wake mmoja na kujikuta amejitupa kitandani usingizi wa pono ukimpitia, huku anakoroma. Pombe sasa ilikuwa inafanya kazi yake mwilini mwa Bosi Minja, ilimlegeza rege rege.
Haikupita hata nusu saa mlango wa chumba cha Recho ukagongwa mara tatu. Recho akanyanyuka kitandani kwenda kufungua mlango. Alikuwa ni rafiki na mpenzi wake Recho wa toka anasoma shuleni Machame Girls. " Ripuripu!...Welcome...kwisha habari yake...!" aliongea Recho huku anamruhusu Martin aingie ndani ya chumba. "Ah, lo lo lo! Mwangalie tumbo lake kama pipa, tamaa zilimponza fisi..!" aliongea Martin akimkebehi Bosi Minja, kisha wakafa kicheko wote kwa pamoja. Huku wakivuta viti na Recho kuanza kumsomesha lengo la kumuita Martin usiku ule. Bosi Minja alikuwa yupo ulimwengu mwingine, kwenye usingizi mzito uliochagizwa na kugida kilevi kupita kiwango, hajui kinachoendelea ndani ya chumba cha Recho.


"Jamani msiniumizieeee Martin wangu Jamani.....nitalia mie jamani...." sauti nyororo ya msichana mrembo yenye uwezo wa kumtoa nyoka pangoni ilipenya kwenye masikio ya Martin Tenga mchezaji mahiri wa mpira wa kikapu. Martin akiwa amelala chini anaugulia maumivu ya mkono wake wa kushoto alioangukia kwa kusukumwa vibaya na mpinzani katika fainali za mashindano ya Umoja wa Michezo ya Shule za Sekondari (UMISETA).
Mashindano hayo kwa kawaida hukutanisha wachezaji bora waliochujwa kutoka shule mbalimbali. Mfumo wa mashindano yao ni kwa kanda, ambapo mikoa ya kusini, Lindi na Mtwara huunda timu moja, mikoa ya nyanda za juu kusini kama Ruvuma, Iringa na Mbeya nao huunda timu yao na kanda zingine mfanowe. UMISETA hushirikisha wanafunzi kwenye michezo ya Bao, Kikapu, Kurusha Tufe, Meza, Netiboli, Mikono, Riadha, Soka na Wavu.
Martin Tenga alikuja kwenye mashindano hayo akiwakilisha kanda ya Kaskazini inayojumuisha mikoa ya Tanga, Kilimanjaro na Arusha. Alikuwa ni mwanafunzi wa kidato cha tano katika shule ya sekondari 'Old Moshi' iliyopo mkoani Kilimanjaro. Alikuwa ni mchezaji mahiri mwenye vipaji vya kucheza michezo lukuki kwa ufasaha kabisa. Ulikuwa ukimpeleka kwenye mpira wa miguu atasaka kandanda safi litakalosuuza Roho za watazamaji huku wengi wakimfananisha uchezaji wake na mshambuliaji mahiri wa timu ya Taifa Stars wakati huo, Peter Tinno. Mshambuliaji ambaye alikuwa hakauki kutajwa katika vinywa vya wapenda soka hasa kutokana na kufunga goli lililoipeleka timu ya Taifa ya Tanzania kufuzu mashindo ya soka ya Mataifa Huru Barani Afrika.
Ilikuwa ukimpeleka kwenye mpira wa kikapu, alikuwa anafananishwa uchezaji wake namna ya mitindo ya urukaji wake hewani na 'Kareem Abdul Jabbar' mchezaji aliyechezea ligi kuu ya Marekani ya 'National Basketball Association' (NBA) kwa muda wa miaka 20 mfululizo. Kwenye mashindano ya UMISETA kuna wakati walimu wake wa michezo mbalimbali walikuwa wanagombana wenyewe kwa wenyewe kumtaka Martin aweke kipaumbele kwenye mchezo wake. Mwishoni wakafikia muafaka wamtumie wote kwa pamoja kwenye michezo kwa ajili ya manufaa ya kanda nzima ya kaskazini. Mashindano ya mwaka 1979 ya fainali za UMISETA yalikuwa yanafanyika katika viwanja vya Kibaha Sekondari katika mkoa wa Pwani. Siku ambayo Martin aliumizwa mkono kiwanjani ilikuwa ni mchuano mkali wa nusu fainali kati ya Kanda ya Mashariki na Kanda ya Kaskazini. Mpaka Martin anaaangushwa mpambano ulikuwa ni droo, wamefungana goli 87-87. Martin alikuwa anaugulia maumivu makali sana ambayo kwa vyovyote ilikuwa inaonekana kuwa angeshindwa kuendelea na mchezo huo.
Lakini sauti hiyo ya msichana mrembo chotara wa kizungu aliyevalia sare za bwelasuti rangi bluu maalumu kwa wanamichezo wa Kaskazini ilimgutusha Martin na kumsahaulisha maumivu kwa muda. Ilikuwa ni sauti ambayo ilipopenya kwenye masikio ya Martin na kutua kwenye ubongo wake na kuondosha maumivu moja kwa moja mwilini mwake. "Martin amkaaa...! Jamani Martin... Amka ukatupiganie tusipoteze huu mchezo watatunanga sana wajanja wa Dar es Salaam..!!" alizidi kulalama Recho huku machozi yanamtiririka machoni mwake. Macho ya Martin yakagongana na Recho, yakazalisha cheche za mapenzi na kuhurumiana baina yao. "Nifungeni bandeji najiskia vizuri kidogo nikapambane...!" alijitutumua Martin huku akinyanyuka kwa nguvu za ajabu.
Usicheze na nguvu ya mapenzi, ndio maana Mmasai anaweza kupambana na Simba mkali akahatarisha uhai wake ili mradi tu apewe mke aliyempenda. Daktari wa timu akajibu kwa vitendo ombi la Martin kwa kumchua na dawa ya kupunguza uvimbe kisha akamfunga na bandeji. Muda wote Martin yupo nje, timu ya kanda ya Mashariki ilikuwa inaongoza kwa bao 92-89. Dakika zilikuwa zinayoyoma zimebaki kama dakika 6 pambano liweze kwisha. Wanafunzi wa Dar es Salaam wajanja wajanja wakaanza nyimbo zao za kebehi, " Washamba toka Kishimundu wamelala doro...Ohi Ohi...Wakishimundu wamekalia..Ohi Ohi...". Shangwe, nderemo na vigeregere vilizidi kushamiri huku sauti za washabiki wa Kanda ya Mashariki vikitawala. Huku washabiki wa Kanda ya Kaskazini wakiwa wamezizima, wapo kama wamemwagiwa maji baridi mwilini. Mbaya zaidi mchezaji wao tegemeo Martin Tenga akiwa ameumia anatibiwa, hana matumaini ya kurejea kiwanjani.
"Hureeeeeeeeh....Weweeeeeeh......Woyowoyo... Woyowoyoooo.......Werawera Weraaaaaah...!" mayowe ya nguvu ya ushangiliaji yalilipuka kutoka kwa washabiki wa kanda ya Kaskazini baada ya kuona mchezaji wao mahiri Martin Tenga ameingia tena kiwanjani. Wachezaji wa kanda ya Mashariki kitendo cha kumuona Martin amerejea mchezoni kiliwanyong'onyesha nguvu na kuwafanya watepete kama chapati za maji. Ushangiliaji ule ulimchagiza Martin na kumpa ari na nguvu mpya ya kutumia kipaji chake kwa manufaa ya timu yake ya Kanda ya Kaskazini. Himahima ndani ya dakika chache za kumalizia akafunga pointi 7 peke yake kwa staili ya kudanki kimgongomgongo. "Tye.... Tye.... Tyeeeee......." kipenga cha kumaliza mchezo kilipulizwa huku washabiki wa Kaskazini wakiwa hawaamini kama wametinga fainali kwa kuwatoa wababe wa michezo ya UMISETA-Tanzania, kanda ya Mashariki. Shangwe, nderemo na vifijo vilitawala anga lile la Kibaha Sekondari. Kila mshabiki wa Kaskazini alikuwa na furaha fokofoko wakiwa wameshinda kwa pointi 96-94. Martin Tenga alikuwa amebebwa juu juu na wanafunzi wenzake anagombezwa kama mpira wa kona, huku uso wake umevaa tabasamu pana akijiona kama Mfalme aliyetawazwa kuongoza nchi.
Walimu kwa wanafunzi walikuwa wanamtuza zawadi mbalimbali za pesa kutokana na kukongwa na umahiri wake. Recho hakubaki nyuma muda wote alikuwa analia machozi ya furaha kwa ushindi ule huku akijipenyeza kwenye kadamnasi ile ya watu apate kufikisha ujumbe wake kwa Martin aliokuwa ameuandika kwenye kikaratasi kidogo. Martin akamuona Recho, macho yalipogongana tu, Recho akainamisha chini kwa aibu kubwa. Akajilazimisha kupenya na kufanikiwa kumkabidhi kikaratasi chake huku Martin bado akiwa juu ya mabega ya watu. Muda ulikuwa tayari umeshayoyoma, jua lilikuwa linaelekea kuzama. Filimbi ya chakula cha jioni ikaanza kupigwa, wanafunzi wakafanya hima kurejea mabwenini kwao ili wakajiandae na mlo wa chajio. Wanamichezo wasichana walikuwa wamepangiwa kuishi mabweni ya Nyanza na Pangani, wakati wavulana wao walikuwa wapo mabweni ya Skandia na Kibo.
Martin akaenda kujimwagia haraka haraka na kurudi bwenini kubeba sahani yake ya chakula. Alipofungua kabati lake la nguo ndipo akakumbuka kikaratasi na pesa alizopewa na Wanafunzi wenzake. Akakichukua kikaratasi alichopewa na Recho akaenda mpaka kitandani pake akakaa. Kiroho kilikuwa kinamdunda akiwa na kimuhemuhe cha kutaka kufahamu kuna ujumbe gani. Recho alikuwa ni msichana ambaye wanafunzi wenzake wote wake kwa waume wakimuona kama ana maringo na madahiro. Hakuna mvulana yoyote alithubutu kumtokea kwa kumtaka kimapenzi. Uzuri wake ulikuwa dhahiri shahiri, na weupe wake ulikuwa wa asili sio mikorogo ya dukani. Wenyewe wanafunzi walikuwa wanamsifia kuwa kwa jinsi anavyong'aa Recho, ukidondosha sindano kwenye kiza totoro cha usiku wa manane akipita Recho eneo hilo hiyo sindano utaiona tu. Wakaenda mbali zaidi kwa kumpamba kuwa ukiwa nae ndani ya nyumba moja ikifika usiku huna haja ya kumaliza umeme wako kwa kuwasha taa, kwani nuru inayotoka kwenye mwili wake kutokana na rangi yake ilikuwa mbalamwezi tosha ya kuangazia nyumba. Hivyo Martin kupokea kikaratasi cha msichana mrembo ambaye alikuwa ndio gumzo kwenye vijiwe vya mashindano hayo ya UMISETA alikuwa ana furaha sheshe.
"MARTIN KAMA UNANIPENDA KWELI KAMA NINAVYOKUPENDA MIMI, TAFADHALI NJOO BWENI LA NYANZA CHUMBA NO. 10 SAA 3:00 USIKU NAKUSUBIRIA" alipomaliza kukisoma alikuwa hayaamini macho yake juu ya kile alichokisoma. Akashusha pumzi nzito na kujiona ni binadamu wa kipekee kudondokewa na ngekewa ya kupendwa na mrembo wa hadhi yake kama Recho. Filimbi ya pili ya chakula ilipopigwa ikamkurupusha Martin na kuelekea bwaloni kwa ajili ya chakula.



Mapenzi ni kitu Fulani tofauti sana kwenye hii dunia na hata nje ya hii sayari. Kama uwendawazimu una matawi basi mapenzi ni moja ya hayo matawi ya ukichaa. Mapenzi kwa kiasi kikubwa sana yanasababisha hata mambo mengine kwenye hii dunia yaende sawa au yaende tofauti hata kama hayahusiani na mahusiano ya mapenzi.
Vifo vingi hutokana na mapenzi, kuna magonjwa watu wanaumwa kisa mapenzi, kuna mambo watu wanayafanya si ya kawaida kisa mapenzi. Ukiachilia mbali pesa, mapenzi huwa yana nafasi kubwa sana kwenye kitu chochote ndani ya hii dunia tunayoishi. Si masikini wala si tajiri, wote kwa pamoja wanahitaji mapenzi kutoka kwa wanaowapenda ili dunia iweze kwenda sawa kwa upande wao. Ukipata mpenzi anayekuelewa na kukupenda basi hata dunia iwe ya tabu vipi kwako utaiona inazunguka kama kawaida na maisha yatasonga mbele kwako kwa raha mustarehe, na hata matatizo mengine makubwa kwako huwa madogo kwa sababu tu unapenda na kupendwa kwa dhati.
Lakini ukiumizwa kwenye mapenzi au kutojaliwa kama wewe unavyojali basi hata dunia iwe na raha gani kwako utaiona chungu na hata raha ya maisha hutakuwa nayo hata kama una hela kiasi gani na hata kama una cheo kikubwa kama Mfalme au hata Rais.
Recho alijikuta amepatwa na kichaa cha ghafla cha mapenzi dhidi ya mwanamichezo mwenzake wa kanda ya Kaskazini Martin Tenga. Ndio mara yake ya kwanza tokea avunje ungo kujikuta anapatwa na hisia za kumpenda mtu ghafla tena bila kutarajia. Tena nguvu ya mapenzi hayo kwa Martin ilikuwa kubwa mpaka akashindwa kuvumilia kusubiri atongozwe yeye kama mila za Kiafrika zinavyotaka, akajikuta yeye ndio anamtongoza Martin Tenga.
Recho alikuwa na damu ya kizungu kwa baba huenda ndio ilikuwa inamuondolea uoga na kumvika ujasiri wa kumkabili Martin, ambaye ni mkubwa kwake kwa zaidi ya madarasa mawili, yeye akiwa kidato cha tatu na Martin akiwa kidato cha tano. Recho alishaamua liwalo na liwe lazima Martin usiku wa leo ajivinjari nae. Kwa bahati kwake, mwanamichezo mwenzake aliyepangwa kulala nae chumba kimoja alikuwa ni mgonjwa amelazwa Hospitali ya Tumbi akiwa na homa ya Malaria. Hivyo chumba kizima Recho alibaki peke yake anajimwayamwaya anavyojisikia.
Muda wa miadi ulikuwa unakaribia kufika huku hisia zake zikimtuma kwa vyovyote kama Martin atakuja kutimiza miadi ya mialiko wake lazima atapitia njia ya uwanja wa mpira ambao upo jirani na bweni hilo la Nyanza. Kila mwanafunzi alikuwa amejifungia chumbani kwake wanaongea wenyewe kwa wenyewe huku kukiwa na ulinzi mkali wa Matroni na mlinzi wa shule maarufu kwa jina la Babu Mshamu.
Ilikuwa ni amri wakishamaliza mlo wa jioni saa 1 usiku, kila Mwanafunzi anatakiwa abakie chumbani mwake, labda itokee dharura mahususi. Ilipofika saa tatu kasorobo Recho akatoka akiwa amejifunga kanga chini na kujifunika juu huku ndani yake amevaa bwelasuti za michezo, pia alibeba mto wa kitandani, sahani na bakuli yenye mfuniko na kijiko. Akajifanya kama anaenda choo cha nje akatokomea zake karibu na kiwanja akabana pembeni ya mti na vifaa vyake. Kadri muda ulivyokuwa unakaribia, kiroho kilikuwa kinamdunda huku anajiuliza kama Martin atajitokeza kweli. Saa 3:05 ghafla bin vuu akajitokeza mtu mmoja mrefu sana kama mlingoti, amejengeka mwili wa kimichezo nae amevaa suti za michezo. Alikuwa anatembea kwa wasiwasi anapiga mwendo halafu anasitasita kutembea kama vile kuna kitu anavizia.
"Martin.....Martin... nipo hapa njooo...it's me Recho... !" alinong'ona Recho baada ya kujihakikishia anayemuona ni Martin. "Wooh....Recho niambie nimekuitika kwa heshima yako tu Binti mrembo" aliongea Martin huku akimkumbatia Recho na kumchomekea utani. "Sasa twende 'room' tukayajenge, ila inabidi uweke huu mto kwenye makalio kisha ujifunge hizi kanga tupite kirahisi...!" aliongea Recho kwa haraka haraka huku Martin akiwa ameshaigundua mbinu inayopangwa na Recho.
Baada ya dakika kama 3, ulikuwa ukimuangalia Martin utasema ni mwanamke wa Kitusi kwa urembo wake. "Tufuatane mimi ndio nitaongea tukiulizwa kitu chochote na mlinzi..!!" aliongea Recho huku akijitutumua kwa kujivika ujasiri wakaanza kurejea bwenini. "Hey....nyie mbona hamuelewi lugha, mnatokea wapi hivi sasa, simameni hapo hapo mnieleze vizuri..." ilikuwa ni sauti ya kukwaruza ya mlinzi Babu Mshamu akiwachimba mkwara Recho na mwenzake, huku anazungusha kirungu chake kwa mbwembwe kuonyesha hana maskhara. "Tulipeleka chakula kwa mgonjwa Sikitu, Tumbi hospitali ndio tunarudi...!" alijitetea Recho kwa sauti ya puani ili kumtia shemere Babu wa watu.
"Haya nendeni haraka sana, siku nyingine msipite gizani huku mtakuja kubakwa bure, watu wenyewe mmeumbika na mawowowo yenu hayo" aliongea mlinzi Babu Mshamu huku analikodolea tako feki la Martin kwa uchu mkubwa. " Ahsante...Babu haturudii tena.." alijibu Recho huku wanaongeza kukaza mwendo. "Hey...simameni kwanza..." aliongea kwa sauti ya ukali ya kuamrisha mlinzi yule wakiwa tayari wameshamuacha hatua kadhaa. Martin akaanza kutetemeka, miguu inatetemeka huku anajishauri atoke mbio tu. Hata Recho alisikia tumbo lake linaunguruma kwa uoga, walijua Babu Mshamu kashtukia picha ya kihindi aliyochezewa. Kama angekuwa amewaacha umbali mrefu wangetimua mbio lakini alikuwa tayari ameshawafikia karibu, akija kwa mitembeo kama mwanajeshi na nguo zake za mgambo. Walijua hapo watachezea kipigo bure bila bilashi kama mwana wa kambo.
"Wewe unakaa chumba gani?.. Sijakuona mabweni ya huku? " aliongea huku anamkazia macho Martin. Martin akawa anapepesa macho kama mwizi, ikabidi ajiongeze aigize kama msichana kweli vile, kwa kuona aibu, akaanza kutafuna kucha na kuinamisha uso wake chini, huku akikosa raha na buraha. Alikuwa amesimama pwetepwete kinyonge kama sio mwanamichezo shupavu. "Namba 10..." alijibu Martin kiuoga huku anasubiria kuuumbuka. " Amehamishiwa 10 kutoka namba 8 baada ya Sikitu kuugua ghafla...sasa namba 8 wakilala wanafunzi 3 ,Matroni kamleta kwangu pale..." Recho alizidi kukazia uwongo huo ili kumtia ndimu na pilipili mlinzi yule. "Ahaaa....sawa, nendeni leo ni ofa kwenu mkipenda msizime taa nyie mna nidhamu sana, usiku mwema" aliongea Babu Mshamu kiunyonge huku anawasindikiza kwa jicho la matamanio akikosha macho yake kwa kuyatazama maumbile ya binti wale.
Mlinzi Babu Mshamu alichizika na makalio ya Martin, hivyo alitaka ajue chumba cha Martin ili akachungulie usiku. Mzee Mshamu moja ya marupurupu aliyokuwa anayapata ni kufaidika kuwachungulia wasichana hao wakiwa vyumbani kwao kwa kisingizio yupo kwenye speksheni ya usalama wao. Hivyo alitaka ajue chumba anachoenda kulala Martin na kujifanya kuwapa ofa wawashe taa kama wakipenda ili akauchungulie mpododo feki wa Martin mubashara. Bila kujua yule ni mvulana wamempiga tu chenga ya mwili. "Ahsante Babu usiku mwema....!" wakashukuru na kuanza kupanda ngazi fupi za kuelekea kwenye korido za vyumbani wakafungua chumba na kujifungia zao. Recho na Martin walikuwa wamejawa na tabasamu tele wanajimwashamwasha kwa kufanikiwa kumpiga chenga ya mwili Mlinzi yule mkuda.

ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog