Search This Blog

Wednesday 22 March 2023

UKURASA WA GAIDI - 5

 

Simulizi : Ukurasa Wa Gaidi 

Sehemu Ya : Tano (5)


Kutokana na maelezo ya Makassy,Mick alijua nini cha kufanya.

"Wewe jifiche hapa chukua na hii bastola yangu.Mimi naenda kupambana nao ana kwa ana.Yeyote atakayenipita akija huku mtwange risasi afe.Wala usihangaike kutaka kumtafuta."Mick alimwambia Clara na kumkabidhi silaha yake huku yeye akienda kupambana akiwa na visu vidogo vidogo kadhaa vilivyofutikwa katika mkanda maalum aliovaa kiunoni mwake.Clara alibaki amejificha akiwa na silaha mbili yaani bunduki aliyokuwa nayo tangia mwanzo pamoja na bastola aliyopewa na Mick.

Mick alianza kitembea kwa kunyata kurudi kule walikomaadui kadri alivyokuwa anapata maelekezo kutoka kwa Mkurugenzi wa idara ya C.T.I kupitia kifaa cha mawasiliano alichokivaa sikioni.

Mick alitembea kimachale machale kwa mita kadhaa kisha akasimama ghafla.Aliwaona adui wawili wakiwa na bastola wakija upande wake.Mick alianza kuwakimbilia adui wale kwa utaalamu wa hali ya juu bila kuweka kishindo.

Alipowafikia, kwa kasi ya ajabu Mick aliruka juu katikati yao na kuchanua miguu hewani na kuwatandika mateke yaliyowakuta kwa pamoja na kuwapeleka chini.Waliposimama mmoja alikutana na kisu cha shhingo kilichorushwa kiustadi na Mick huku mwenzie akikutana na teke aina ya 'round kick' lililopigwa kiustadi na Mick huku akijizungusha hewani.Teke lile lilitua katika shingo na kuvunja kabisa shingo ya adui yule.Adui hawa wawili wakawa marehemu.

"Wawili tayari".Aliongea Mick.

Wakati huo huo akamuona adui mwingine akija upande wa kushoto.Mick akaruka sarakasi kwa kujiviringisha hewani na kisha akatua mbele ya adui yake yule.Yule adui akashtuka lakini akaanzisha mapambano mara moja kwa kurusha ngumi kwa mkono wa kulia.Mick akaiona na kuipangua huku akimtegua kiwiko cha mkono.Adui akasikia maumivu lakini akajikaza na kurusha ngumi nyingine kuelekea usoni mwa Mick. Mick aliiona hiyo pia.Akaipangua huku akitegua kiwiko cha mkono kama alivyofanya kwa mkono wa kwanza. Kisha Mick akaanza kumrushia ngumi kwa kasi kubwa kama ile ya sindano ya cherehani wakati wa kushona nguo adui yule ambazo zilitua kifuani,tumboni na kwenye mbavu.Hapo adui alivunjwa mbavu kadhaa kisha akakatishwa pumzi kwa ngumi iliyotua shingoni na kumvunja kabisa mifupa na mishipa ya shingo.Akawa marehemu pale pale.

Kisha Mick akarusha visu viwili kwa ustadi wa hali ya juu sana.Kisu kimoja kikaenda kutua kifuani upande wa kushoto usawa wa moyo na kingine kikatua shingoni katika koromeo la adui wawili ambao walikuwa wakimjia kasi kutoka kulia kwake.Wakakata roho papo hapo.

"Watano tayari".Aliongea Mick tena.Kwa kupitia kifaa cha mawasiliano alichokivaa sikioni akasikia sauti inasema "Bado watano sasa."

"Sawa ngoja niwaoneshe kazi".Aliongea Mick

Kisha akaona mahindi yakicheza cheza .Mick akachuchumaa chini kwa kujificha.Akawaona adui zake wote watano wakiwa na bunduki au bastola mikononi huku wakizunngumza kwa sauti ya chini.

"Oya,nimesikia purukushani kisha kukawa kimya upande ambao Sam na Dennis walielekea."Mmoja alisikika akiongea huku sauti ikiwa na kama kitetemeshi hivi.

"Acha woga wewe Devi.Hawa vibaraka wa serikali watakuwa wamekimbia."Ilisikika sauti nyingine ikijibu kwa majivuno.

Ghafla kwa kasi kama ya mzimu,Mick-Reuben alipita kati kati yao huku akitoa kichapo.Yaani ndani ya sekunde chache, mmoja alichomwa kisu kifuani,mwingine alipigwa ngumi ya kuvunja shingo, mwingine alipigwa teke chini kidogo ya kisogo na mwingine akakabwa na kuvunjwa shingo haraka sana.Sekunde tano tu zilitumika hapa.Watu wanne walikuwa tayari wameenda ahera ama kuzimu.

Mick alimbakiza adui mmoja tu kwa ajili ya kazi maalum ambayo ni Mick tu aliyeijua kichwani mwake.Ni yule ambaye wenzie walimuita kwa jina la Devi,ambaye pia alionekana kuwa mwoga zaidi ya wenzake.

"Nimemaliza kazi waweza kujitokeza". Aliongea Mick.Dakika chache baadae Clara aliungana naye pale alipokuwa.

Ajenti Mick akamfunga pingu yule adui(Devi) kisha wote pamoja na Clara wakaingia katika gari aina ya Landrover walilokuja nalo wale adui. Clara akakamata usukani huku Mick na mateka wake wakikaa kiti cha nyuma.

"Twende viwandani.Kuna jengo moja zamani lilikuwa kiwanda cha sabuni siku hizi hakuna kazi yoyote.Jengo limebaki kama gofu tu.Nadhani litatufaa sana leo hii"Aliongea Mick,Clara akakanyaga mafuta na kuondoa gari kwa kasi kelekea huko alikoelekeza Mick.Wakati huo Devi alikuwa kama anaelekea kujikojolea kwa woga.

**************************************************************************************************

Kiwanda cha sabuni zilizokuwa maarufu sana miaka zaidi ya kumi iliyopita mkoani Mbeya, kilikuwa eneo la viwanda huko Iwambi.Sabuni hizi ziliitwa 'Hisoap' na zilisifika kwa kuwa zilitengenezwa katika miche mipana mipana sana na kwa povu jingi zilizotoa huku zikiuzwa bei rahisi sana.Sabuni hizi zilikuwa msaada sana kwa wana Mbeya waliokuwa na maisha ya chini,kwa kuwa zilisaidia kupunguza bajeti kwa upande wa sabuni.Hata kiwanda chake kiliitwa kwa jina la sabuni yaani ' kiwanda cha hisoap'.

Mara ya mwisho kwa sabuni hizi kuonekana ilikuwa miaka zaidi ya kumi iliyopita.Hii ilitokana na kufa kwa kiwanda hiki,ukiwa ni muendelezo wa kufa kwa viwanda mbalimbali mkoani Mbeya na hata nchini.Watu wengi sana walipoteza ajira mbali mbali ambazo zilisababishwa na uwepo wa viwanda hivi.Kwa kilichobaki katika eneo hilo ni mashine zisizofanya kazi na vyuma vikubwa vikubwa vilivyo na uhisiano na mashine hizo.

Ndani jengo moja wapo kati ya majengo kadhaa yaliyopo katika mahali hapo,palikuwapo na ugeni wa ghafla siku hiyo. Ugeni huu ulijumuisha jumla ya watu watatu, yaani Mick,Clara na yule kijana ambaye sasa aitambulika kwa jina la Devi.

Devi alikuwa amefungwa kwa kamba za waya ambazo zilikutwa humo ndani.Alifungwa katika kiti kimoja kichakavu cha chuma ambacho nacho kilikutwa ndani ya chumba hiki kilichotawaliwa na vumbi pamoja na utando wa bui bui chungu nzima.

Mahojiano yalikuwa yakiendelea wakati huu na sasa, mahojiano hayo yalikuwa yamepiga hatua kadhaa mbele.

Tangu masaa mawili yaliyopita, mara tu walipoingia katika eneo hili tulivu kabisa ambako si kawaida kwa watu kupita pita,Mick aliongoza mahojiano hayo. Katika hatua za awali, Devi alipewa muda wa kujibu kwa hiari yake swali moja tu ambalo Mick aliuliza tangu wameingia ndani ya chumba hiki.Devi aliahidiwa kuwa iwapo angejibu basi angepata faida ambazo ziko katika makundi mawili.

Kwanza kabisa angeepuka kushtakiwa na kupewa uhuru.Pili angesaidiwa na serikali kwa kupewa pesa nyingi ambazo zingemfanya aweze kuishi maisha ya raha kwa muda wote wa maisha yake.

Hili lilithibitishwa kwa mawasiliano ya kompyuta ya 'skype' katika kompyuta mpakato ya ajenti Clara kati ya Devi na Rais George ambayo yalifanikishwa na mkurugenzi wa idara ya C.T.I, Eliakim Makassy.Lakini pamoja na kupewa ahadi nyingi zingine ambazo zilikuwa za uhakika na ambazo zilimuhakikishia Devi kuwa atakuwa salama na kufaidi maisha iwapo ataonesha ushirikiano,lakini Devi alionesha kutokuwa tayari kuonesha ushirikiano.

Hakika kama Mick na Clara walidhani kwamba Devi ni mwoga san kwa hiyo itakuwa rahisi kupata ushirikiano kutoka kwake, basi walikosea sana.Devi alikiwa mgumu sana kutoa ushirikiano.Yaani ni kama hakuwa tayari kumsaliti ama kuwasaliti watu waliomtuma ambao Mick ndiyo alihoji kuwahusu.Alionekana kama mambo ya kihalifu yalikwisha kumwingia moyoni.

Ubishi wake ndiyo ulisababisha Mick kuamua kutumia njia zilizoboreshwa zaidi ambazo kwa kawaida husababisha adui atoe ushirikiano bila kupenda. Daima Mick alikumbuka msemo usemao "Diplomasia inaposhindikana, vita huchukua nafasi".Kwa wakati huu,msemo huu ulikuwa unaelekea kufanya kazi.

"Nakuuliza swali lile lile , ni nani aliyewatuma kujaribu kutuua."Ilikuwa sauti isiyo na masihala, sauti ya Mick. Kama ilivyokuwa tangu mwanzo hakuna ushirikiano kutoka kwa Devi ambao Mick aliupata.

Mick alitoka nje kisha akaenda hadi katika gari walilokuja nalo.Akaingia nakuondoa gari kwa mwendo wa kasi sana.

Dakika kumi baadaye alirudi tena katika jengi hilo.Safari hii hakuja mikono mitupu.Kutoka katika gari lile, Mick alishusha madumu manne yaliyo jaa maji safi ya kunywa yaliyokuwa katika ujazo wa lita kumi kila moja ambayo alitoka kuyanunua dukani.Begani mwake pia alitundika taulo zito jeupe ambalo pia lilikuwa jipya.

Mara tu baada ya kuingia ndani ya jengo hilo tena,Mick alikibinua kiti ambacho Devi alifungwa na kukiegemeza katika meza na kukifanya kiti kile kusimamia kiguu miwili huku egemeo la kiti likitegemea meza hiyo ili kutoanguka.Kufanya hivi kulimfanya Devi akae mkao wa kuegama kwa kuangalia juu.

Mick aliongeza kamba nyingine ambayo hii ilimfunga shingoni na kumuunganisha zaidi na egemeo la kiti na meza na kumfanya asiweze kutikisika kabisa.

Baada ya hapo, Mick alimfunika Devi na taulo lile zito usoni.Kisha akamwangalia Clara.Clara akaelewa kitu.Akaenda kushikilia taulo lile ili lisiweze kudondoka huku akihakikisha eneo la taulo lililofunika usoni likiwa mahala pale pale.

Mick alifungua dumu moja la maji na kulinyenyua juu kisha kuanza kuyaamwaga maji yale pole pole juu ya taulo lile katika eneo ambalo limefunika uso wa Devi.Zoezi hilo alilifanya kwa dakika moja na maji yakawa yamekwasha katika dumu lile.Kisha Clara akalitoa taulo lile mara moja nakumuacha Devi avute hewa mara moja tu.Kabla hata hajatoa hewa tena nje Clara akarudisha taulo lile usoji tena kama lilivyokuwa mwanzo na Mick akafungua Dumu lingine na kuyamimina maji yale juu ya lile taulo kama mwanzo.

Dumu lile la pili lilipoisha maji,Clara akalitoa taulo like usoni mwa Devi.Mara tu taulo lilipotolewa, Devi alikohoa kikohozi kilichoambatana na maji mengi sana.Rangi yake nyeupe ilikuwa imebadilikavna kuwa nyekundu.Machozi, mate mazito na kamasi zilizochanganyikana na damu ziliuchafua uso wake. Kama kuna mtu ambaye alimuona dakika kadhaa kabla ya zoezi hili kuanza kufanyika, basi angeweza kusema siye yeye.

Kabla hata hajamaliza kukohoa maji ambayo yalimuingiaa katika mapafu na kumtesa, na kabla hata ya kuweza kuzungumza tena taulo likarudishwa tena usoni. Mick akafungua dumu la tatu na kumimina maji juu ya taulo lile kama mwanzo. Safari hii alimimina nusu yaa dumu tu kisha akamwambia Clara atoe taulo lile.

Safari hii Devi alikohoa hadi akatapika.

"Mwekee taulo tena tuendelee na kazi sisi.Madumu mengine kumi bado yapo kwenye gari yanasubiri kufanya kazi hii".Mick alimwambia Clara kwa sauti isiyo na masihala mara tu baada ya kuona Devi amekohoa kwa muda na sasa anaweza kuongea.

Clara naye bila kuchelewa akainua taulo ili aliweke usoni mwa Devi kama hapo awali.

"Su.....bbbiri na..sse..mmaaaa."Devi aliwahi kuongea kabla taulo like halijarudi usoni mwake.Sauti aliyoitoa, waweza kudhani ni mtu aliyebebeshwa mzigo wa kilo mia mbili wakati uwezo wake ni kubeba kilo kumi.

"Ongea sasa.Ukizingua tu zoezi litaendelea hadi utakapoongea ukweli.Na sitakuua ila safari hii nitatumia maji yaliyo na pilipili kali kufanya zoezi hili.Kufa huta kufa ila nitakupa mateso ambayo utaomba mwenyewe nikuue"Aliongea Mick kwa kumaanisha.

"Braza nitakwambia ukweli wote". Aliongea Devi. Sasa kwa sauti nzuri angalau kukiko mara ya kwanza.Kisha akaendelea kuongea;

"Jina langu naitwa David Sanga.Ni mzaliwa wa Iringa. Kiukweli mimi simfahamu mkubwa wetu ila ninamfahamu tu kijana anayemtuma kwetu kuja kutupa 'odder' za kazi mbali mbali."Aliongea Devi.

Mick akamuangalia kwa muda Devi. Ni kama alikuwa akimkagua usoni kama anachoongea ndicho anachomaanisha.

"Anaitwa nani kijana huyo". Alihoji Mick.

"Namtambua kwa jina la Juma Nkya."Alijibu Devi.

"Tunaweza kumpata wapi yeye au hata picha yake."Alihoji Mick

"Kwa bahati mbaya huwa tunakutana maeneo tofauti tofauti na hata picha yake sina" Alijibu Devi.

Mick akafikiria kidogo.Lakini kabla hajawaza zaidi Clara naye akauliza,"Unaweza ukamuelezea muonekano wake vizuri"

"Ndiyo naweza.Tumekutana naye mara nyingi tu.Ninaweza kumuelezea vizuri".Alijibu Devi huku akionekana kuvuta hisia kichwani mwake.

Clara akawasha programu fulani katika kompyuta mpakato yake ambayo daima alikuwa nayo wakati wote. Kisha akaanza kumuuliza maswali Devi kuhusu mtu huyo.Alimuuliza kuhusu muonekano wa macho yake,pua,mdomo,kichwa na mambo mengine mengi. Kila alipojibiwa,Clara alibonyeza hap na pale katika kompyuta na kutengeneza sura yya mtu.Alipomaliza , Clara akamuonesha Devi picha aliyoitengeneza katika kompyuta yake.

"Ndiye yeye huyo.! Yaani ni yeye kabisa.Huyi ndiye aliyetuagiza sisi kuwaueni nyinyi."Aliongea Devi mara baada ya kuona picha ambayo Clara aliyoitengenezakwa kufuata maelezo yake.

"Aliwaambia sababu ya kutuua?".Aliuliza Mick,swali ambalo ni kama alijua jibu lake .

"Hapana.Alisema tu mnaingilia maslahi ya bosi wake".Alijibu Devi.

"Umewahi kuhisi bosi wake ni Mtanzania au anatoka nje ya nchi".Alihoji Mick.

"Siyo kuhisi tu.Nimewahi hata kusikia sauti yake akiwa anaongea na huyu jamaa(huku akioneshea picha iliyotengenezwa na Clara katika kompyuta). Ana sauti nzito sana na anaongea taratibu kwa pozi sana."Alijibu Devi.

Hapo Mick akashituka kidogo.Maneno"Ana sauti nzito sana. Anaongea kwa pozi na taratibu sana"yalimwingia sana kichwani na kufanya kengere ya hatari kulia kichwani mwake.

Mick aliigeuzia kompyuta mpakato ya Clara upande wake na kuitazama tena picha iliyotengenezwa na Clara.

"Ndiyo mwenyewe."Aliongea kwa kuhamaki Mick.

"Mwenyewe nani tena ". Aliongea Clara kwa kuhoji

"Unawafahamu walinzi wa waziri wa ulinzi?."Mick alijibu swali kwa kuuliza swali.

Clara naye akawa ni kama ndiyo anaamka kutoka usingizini.Naye akaitazama picha ile tena ambayo ameitengeneza mwenyewe.

"Kweli.Anaitwa James Peter ama kwa majina anayotumia katika mitandao ya kijamii anajulikana kama Juma Nkya.Moja kati ya vijana wanaoaminiwa sana na waziri wa ulinzi."Aliongea Clara.Kisha akawa kama ameshtuka kwa mara ya pili.

"Haaa...Mick uko sawa kabisa....WAZIRI WA ULINZI ANA SAUTI NZITO NA ANAONGEA TARATIBU SANA."Aliongea tena kwa kushtuka Clara.

"Rais anatakiwa kujulishwa haraka sana. Kwa namna anavyowaamini mawaziri wake, nadhani maisha ya rais yako hatarini iwapo ataendelea kutojua". Alijibu Mick.

Wakati huo ndipo Mick alipofanya mawasiliano na mkuu wa idara ya C.T.I ,Makassy na kumueleza yote aliyoweza kuyagundua. Makassy naye akawasiliana na Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzana bwana George Katumba.

**************************************************************************************************

Ama kweli umdhaniaye ndiye kumbe siye.Huyu huyu waziri aliyewachochea wabunge kutaka ulinzi wa nchi upewe kipaumbele miaka kadhaa nyuma.Aliye sababisha maeneo mbalimbali yaliyoainishwa na na wabunge kuwekewa kamera za ulinzi na kuingizwa kwa silaha za kijeshi za kisasa sana ambazo baadhi hutumiwa hata na mataifa ya ulimwengu wa kwanza. Huyu ndiye waziri aliyemshawishi hata rais kuweza kuzisuka idara za kiusalama nchini.Mambo mengi ya usalama wa nchi ambayo waziri huyu alikuwa amehusika,ndiyoyalisababisha hata wachunguzi wa mambo kutoka nje ya nchi kushangaa na kujiuliza kwamba kwa nini Tanzania inajijenga katika nyanja za usalama wa nchi kwa kiasi hiki.Waziri wa ulinzi alikuwa na ushawishi na alikuwa na uwezo mkubwa sana wa kushawishi na kukubaliwa kwa mambo mengi hasa yahusuyo usalama wa nchi na kusababisha asilimia kubwa ya wananchi kumsema kuwa ni mmoja wa viongozi muhimu na mwenye mchango mkubwa kwa maendeleo ya taifa hili.

Lakini kumbe nyuma ya Pazia waziri huyu alifanya mema mengi ili tu aweze kuficha makucha yake.Ndiyo.Kwa mazuri aliyoyafanya isingekuwa rahisi kwa mtu yeyote mwenye ufikiri wa kawaida kudhani kwamba ndiyo mtu mbaya zaidi na hatari zaidi katika nchi hii. Rais alimuweka karibu pasipo kujua kuwa ana mipango ya kuvuruga amani ya nchi kabisa.Kumbe kila jema alilolifanya nyuma yake kulikuwa na nia ovu na hila na ulaghai.Kumbe alikuwa anaandaa mazimgira kwa ajili ya kutekeleza mambo maovu ambayo mwanzoni hakuna mtu ambaye angeweza kumdhaniya kuwa amehusika.

"Lakini hivi ni kweli waziri ambaye mimi nilimuamini sana na amesifiwa sana kwa mema anaweza kunifanyia mimi hivi ?Ni kweli alitaka kuisaliti nchi?Hapana. Ngoja kwanza achunguzwe labda amesingiziwa.Labda kuna mtu alitaka kumtegeshea ili kum 'frame'.Au labda kijana yule mlinzi waziri alihusika peke yake bila waziri kujua.Lakini si ndiyo kijana ambaye waziri anamuamini sana kwa ulinzi.Si ndiyo anapatana sana na waziri."Rais George Katumba alijiuliza maswali mengi pasipo kupata jibu la uhakika.Wakati fulani akili yake ilipinga kuwa waziri wa ulinzi alihusika na mambo ya ugaidi.Wakati mwingine aliunga mkono kuwa pengine ni kweli waziri wa ulinzi alihusika na mambo haya.Yaani moja haikukaavwala mbili nayo haikukaa.

Wakati huo huo simu ya mezani ililia.Rais alishtuka kutoka katika lindi la mawazo na kuipokea simu ile.

"Hallow George Katumba hapa naongea."Aliongea Rais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania.

"Makassy wa C.T.I hapa.Mheshimiwa Rais nimekupigia nikueleze yaliyojiri masaa mawili yalopita.Kikosi maalum kikiongozwa na 'Field agent' Paul, kilikwenda ofisini kwa waziri wa ulinzi Dar es salaam kumkamata kama ulivyotupa maagizo.Lakini walipofika wakakuta taarifa ya kuwa waziri aliondoka ofisini masaa mawili kabla ya kikosi kile maalum kufika.Kikosi kile kikaenda hadi nyumbani kwake Masaki na kukuta nyumba yake iko tupu. Katika kupeleleza, ikagundulika kuwa huenda waziri ametorokea nje ya nchi pamoja na familia yake. Na baada ya muda ndipo taarifa za kiintelijensia zikatufikia kwamba waziri ametorokea Somalia pamoja na familia yake kwa kupitia ndege ndogo ya kukodi.Haya yote yametupa uhakika kuwa waziri wa ulinzi hajasingiziwa. Ni kweli amehusika na maovu haya."Alimaliza kuongea Makassy, mkuu wa idara ya C.T.I.

"Kuanzia sasa namtangaza Michael Joseph Magombe kuwa siyo waziri tena na ni adui namba moja kwa taifa letu."Aliongea Rais George.

"Lakini nina ombi moja muheshimiwa.Naomba hili suala liwe siri sana,lisitangazwe kwa wananchi lisijevuruga upelelezi wetu.Pia ule wasiwasi wangu kuwa kuna uvujishaji wa siri kutoka ndani ya idara ya C.T.I ni ukweli wa uhakika.Kwa sababu suala la waziri wa ulinzi tulilijua wachache,lakini kuna mtu ambaye nadhani anatega sikio kwa kificho na kutoa siri kabla ya muda wake.Lakini namuwekea mtego na nitamkamata tu."Aliongea Makassy.

"Sawa kama ni hivyo.Ila kuweni makini sana na kazi njema".Aliongea Rais na kukata simu



Mick alipachika darubini machoni na kutazama upande ule wa ngome. Ndani ya ngome,vijana walionekana wamepanga mistari wakipiga gwaride za kijeshi.Kisha mkuu aliyekuwa akiamrisha siku hiyo akaitisha rokoo.Haya yote Mick aliyaona kupitia darubini yake iliyokuwa na uwezo wa hali ya juu. Japokuwa hakusikia kutokana na umbali lakini aliweza kitafsiri vyema kile alichokiona.

Kwa kadri Mick alivyoyashuhudia yote haya, aliweza kukadiria uwepo wa vijana wapiganaji zaidi ya elfu mbili na mia tano ndani ya ngome hiyo. Pengine kulikuwa na uwezekano wa kuwapo vijana wengi zaidi kwa kuwa wengine hawakuonekana machoni pake.

Mara baada ya rokoo kuisha, vijana wale walitawanyika na kwenda katika viwanja vya mazoezi mbali mbali ya kimapigano.Wengine walifanya mazoezi ya shabaha huku wengine wakifanya mazoezi ya mapigano ya ana kwa ana , yaani mkono kwa mkono.

Wakati huo huo Mick alisikia muungurumo wa magari kutokea upande wa nyuma kutoka pale juu ya mlima alipokuwapo.Magari manne aina ya VAN yalikuwa yakija upande wake. Ubavuni na juu ya magari yale kulikuwa na nembo imeandikwa 'the squad'.Kilikuwani kikosi cha mapambano cha E.C.S kimewasili.

Magari yale yalikuwa yakipita pori kwa pori bila kufuata bara bara.Mbele ya magari haya kulikuwa na gari aina ya 'SUBARU' lililokuwa linaendeshwa na ajenti Clara.Mick akashuka kutoka mlimani.Dakika tano tangu Mick aliposhuka,vikosi vile vikamfikia mahali alipo na askari wote wakashuka na kumpigia saluti Mick.

"Karibuni vijana.Nadhani tuzunguke upande wa kushoto wa mlima ili tuwe katika kificho zaidi.Huko kuna miti mingi na kivuli cha kutosha kinachofaa kwa vijana kupumzika hadi saa kumi na mbili.Kisha tutapanga mashambulizi ili ikifika saa nne usiku tukaanze mapambano. Natumaini wote tuko katika hali nzuri hivyo natumaini leo tutashinda vita hii."Alizungumza Mick na Vijana wote waliitikia na kufanya kadri ya maelekezo.

SAA KUMI NA MBILI JIONI.

Kwa siku nzima tangu kuwasili kwa kikosi maalum cha E.C.S, Ajenti Mick, Ajenti Paul(alikuja na kikosi hiki), Kamanda Joshua(kamanda wa kikosi cha E.C.S) pamoja na Ajenti Clara, walikuwa wakiendelea kukusanya taarifa za intelijensia kuhusiana na ngome ile ya maadui. Walifanya 'surveilance' kwa vifaa vya kitaalam pasipo kushtukiwa na adui zao. Hadi kufika jioni hii, walikuwa wamegundua mengi sana.

Ilipofika jioni hiyo, askari wa weledi wa E.C.S walikusanyika pamoja sehemu fulani ili kupata maelekezo na mipangilio ya jinsi mapambano yatakavyoendeshwa.Maelekezo na amri zote zilitegemea utashi wa ajenti Mick, ambaye katika uwanja wa intelijensia ,yeye (Mick) alikuwa ndiye 'head of field operations'(kiongozi mkuu katika mapambano ya kimapigano).

Mick aliwapangilia askari wote wa weledi kwa kuwagawa katika makundi manne.Kundi la kwanza lingeongozwa na yeye(Mick) mwenyewe likiwa na askari kumi, Kundi la pili lingeongozwa na ajenti Paul likiwa na askari kumi, kundi la tatu lingeongozwa na kamanda Joshua likiwa na askari ishirini na kundi la nne ni la askari wa weledi waliobobea katika udunguaji(snipers) ambao wangekaa pande nne tofauti juu ya milima ili kutoa msaada wa kumdungua adui yeyote ambaye angehatarisha opesheni ile.Pia zaidi ya hao kulikuwa na askari sita ambao hawakuwapo hapo.Hawa walitegemewa kuja na helkopta tatu za mapigano aina ya 'Chinok' wakati ambao vita ingepamba moto sana.

Askari wote walipewa silaha na vifaa vya kisasa vya kutosha vitakavyowasaidia katika mapambano haya ya usiku.Kisha Mick akawapa maelekezo na mipango yote na majukumu ya vikosi vyote pamoja na eneo ambalo kila kikosi kitahusika.

Pia ajenti Clara naye alipewa majukumu ya kuwa tayari kutoa usaidizi wa ki-kompyuta pale ambapo atahitajika namajukumu mengine mengi. Baada ya hapo vikosi vikaondoka hapo na kwenda kujipanga tayari kwa mapambano.

**********************************

Ajenti Jackline, mwanadada mrembo kuliko urembo wenyewe alikuwa ndani ya helkopta aliyokuwa akiiongoza mwenyewe kuelekea uwanja wa mapambano.Ni dakika kadhaa nyuma zilikuwa zimepita tangu alipopewa maagizo na mkuu wake wa C.T.I, mkurugenzi Makassy. Makassy alimueleza kila kilichokuwa kikifanyika kwa siri ambayo hata Jackline hakujua na kumueleza kwa nini siri ilifichwa.

Jukumu kubwa la Jackline lilikuwa ni kwenda hadi umbali wa kilomita moja toka uwanja wa mapambano.Huko angekutana na askari wa kikosi maalum cha jeshi la polisi na jeshi la wananchi miambili.Ajenti Jackline alitakiwa kuongoza vikosi hivyo kimapigano wakati ambao angehitajika.Sasa ilikuwa ni dakika tano kabla hajatua na helkopta yake mahali ambapo angekutana na askari wale.


Ajenti Mick na kikosi chake cha askari wa weledi wa E.C.S, walikuwa wamejipanga kwa stail ya kuchuchumaa na kupiga goti moja chini.Hapo walikuwa nje ya wigo wa ngome.Askari wote wakiwa katika vazi la gwanda nyeusi na kofia ngumu nyeusi yenye uwezo wa kuzuia risasi pamoja na vifaa na silaha kede kede,walikuwa wakisubiri amri ya ajenti Mick ili waruke uwigo mrefu wa ngome hiyo na kuianza kazi.

Hakika ngome ile ilikuwa kubwa.Kadri ya makadirio ya ajenti Mick-Reuben, ilikuwa ni mraba wa kilometa mbili na nusu.Ngome hii ilizungushiwa ukuta ilio na urefu wa mita tatu,uliojengwa kwa mawe makubwa.Mbele ya ngome kulikuwa na mageti matatu ambayo yalikuwa na ulinzi wa kutosha kabisa. Kwa upande wa ndani,pembezoni mwa ngome, kulikuwa na minara ya mlinzi ishirini iliyokuwa mirefu sana na walinzi wake walikuwa na vifaa vya kuona mbali sana pamoja na bunduki kubwa za udunguaji zilizo na uwezo wa kumdungua mtu aliye mbali.

Ajenti Mick naye alikuwa akisubiri maelekezo ya ajenti Clara ambaye alitumia kompyuta yake kuiongoza ndege ndogo yaani 'drone' kufanya 'surveilance' upande wa ndani ya ngome.Lakini pia si kwamba magaidi walikuwa ndani ya ngome tu, bali hata nje ya ngome,hasa upande wa mbele wa ngome,magaidi wale walitapakaa umbali wa nusu kilomita.Wapo walioonekana wakiranda randa,na wengine ambao walikuwa maeneo ya maficho muda wote hukubwote wakiwa na silaha nzito.

Hiyo ndiyo sababu wale wadunguaji wanne wa kikosi cha E.C.S, walikaa katika milima iliyozunguka ngome hiyo, umbali wa mita mia saba kutoka katika kuta za ngome. Kila mdunguaji alikuwa na bunduki ya kisasa ikiwa imefungwa kiona mbali ambacho kina uwezo wa kuoja hata gizani.

Kazi nyingine kubwa ya wadunguaji hawa ilikuwa ni kuhakikisha wanawadungua maadui wote waliokuwa katika minara ya mlinzi ngomeni. Walikuwa na muda wa dakika ishirini tu kuhakikisha askari wote waliokuwa katika minara ile ni marehemu.

"Kunguru wote wako chini".Mick alisikia sauti kutoka katika kifaa cha mawasiliano alichokivaa sikioni.Ulikuwa ni ujumbe wa neno fumbo uliomaanisha kuwa walinzi wote waliokuwa katika minara wamekwisha kufa.

"Ok.Endeleeni kutulindia mkia.Wengine wakishtuka tu mtuambie."Aliongea Mick.

"Tumekupata."Sauti kutoka kwa wadunguaji zilisikika.

Mick na kikosi chake walikuwa bado wakisubiri taarifa nyingine kutoka kwa ajenti Clara ili waweze kuanza ooeresheni.

"Ok.Sasa mnaweza kuingia.Ndani ya dakika kumi adui watapita hapo kufanya 'patrol' hivyo inatakiwa muwe mmekwishatoweka hapo". Ilikuwa ni sauti ya Ajenti Clara ambayo Mick aliisikia kupitia kifaa cha mawasiliano alichokivaa sikioni.

"Ok nimekupata madam."Mick alijibu kisha akatoa ishara fulani kwa kikosi chake.Wanakikosi wote wakaendelea kutulia kimya kama mwanzo.

Mick akatoa kamba kutoka katika begi lililokuwa mgongoni mwake.Kamba yenyewe ilikuwa na urefu wa mita nne,ikiwa nene na ngumu sana.Pia ilikuwa imefungwa mafundo mafundo mengi sana.Muisho mmoja wa kamba hii ulikuwa umeunganishwa na ndoano moja imara sana.Mick alirusha kamba ile kiustadi sana, ndoano ya kamba ile ikadaka vizuri eneo la juu kabisa la ukuta ule wa ngome.Kisha Mick akaukwea ukuta ule hadi juu kabisa. Kwa umakini mkubwa, Mick akazikwepa nyaya za umeme za ulinzi zilizozungushwa juu ya ukuta ule na kurukia upande wa ndani pasipo kufanya kishindo.

Mick alitembea kwa kunyata kuelekea upande ambao alihisi kunaweza kukawapo waya mkubwa unaopeleka umeme katika uwigo huo wa ngome.Hapo akatoa kijembe kidogo kutoka katika begi lake,kisha akachimba hadi alipoufikia waya huo.Kwa umakini wa hali ya juu,Mick alikata waya huo kwa kifaa kingine na kutenganisha kabisa.

Baada ya kukata waya,Mick alirudi hadi pale alipoingilia,kisha akapiga mbinja kidogo.Sekunde chache baadaye, wana timu wote wa kikosi cha E.C.S waliruka ukuta na kuingia ndani.

Katika wigo wa ngome ile,kuliwekwa ulinzi wa umeme ambao ulipelekwa kwa kupitia nyaya nyingi sana.Nyaya hizi nyingi zilikuwa zimechimbiwa chini ardhini. Yaani kwa maana nyingine, ule waya mkubwa alioukata Mick, ulikuwa unapeleka umeme katika eneo dogo tu la wigo. Hii ilikuwa ni kwa sababu za kiusalama kwa upande wa magaidi. Ili kukata umeme wa ulinzi katika wigo wa ngome yote, Mick angehitaji kung'amua, kuchimbua na kuzikata nyaya nyingine tisini na tisa ili kutimiza nyaya mia, kitu ambacho ni sawa kusema hakiwezekani kabisa kukifanya bila kushtukiwa na magaidi.

Na wakati huo huo ajenti Paul alikuwa akisubiri maelekezo kutoka kwa Mick ili aweze kuruka ukuta na kuingia ndani ya ngome hiyo.Kwa hiyo ili kuwawezesha Paul na kikosi chake kuingia, ilitakiwa Mick aende kuharibu chanzo cha umeme cha ngome hiyo.Hii ilitokana na kuwa upande aliokuwapo Paul na kikosi chake bado umeme wa ulinzi katika wigo ulikuwa unafanya kazi.

Ili kuweza kuharibu kabisa vyanzo vya umeme,Mick alitakiwa kufika katika jengo lililokuwa na vyanzo vya kufua umeme yaani 'power plant'.Ndani ya jengo hilo kulikuwa na transfoma na jenereta .

"Chumba mnachokiendea kipo umbali wa mita sabini kutoka hapo mlipo kuelekea kulia.Nje kuna walinzi wanne, ndani sifahamu." Ilisikika sauti ya mtaalamu wa kompyuta, ajenti Clara.

"Ok". Mick alijibu.

Mara baada ya kupewa maelekezo hayo, Mick alikiongoza kikosi chake kuelekea katika jengo hilo kwa mwendo wa tahadhari na kwa kujificha.Mara baada ya kufika, Mick na kikosi chake wakajificha kwa tahadhari kubwa sana. Mick alichunguza kwa makini na kugundua kuwa kulikuwa na walinzi wawili walikuwa wakija upande wao na wawili wengine wamebaki mlangoni.

Mick akamuonesha kwa ishara askari mmoja wa weledi wa E.C.S aliyekuwa karibu yake,kwamba "utashughulika na wa kushoto mimi nitashughulika na wa kulia."Yule askari akamuelewa.

Wale adui walikuwa wanaenda kujisaidia haja ndogo karibu na pale Mick na kikosi kizima walikuwapo.Kwa ustadi wa hali ya juu, Mick na yule askari,wakawanyatia adui wale na kuwakaba shingo na kisha wakazinyonga shingo zao kwa namna ya kuvunja koromeo.

"Sniper namba moja unaweza ukamuangusha kunguru mmoja?"Mick aliuliza kupitia kifaa cha mawasiliano alichokuwa amekivaa sikioni.

"Ndiyo niko kwenye 'position' nzuri kabisa."Upande wa pili ulijibu.

"Basi nahesabu hadi tatu(huku akichomoa kisu chake kutoka katika ala na kukishika vizuri mkononi) ushughulike na huyo anayesinzia.Moja, mbili, tat......."Alipofika tatu,adui mmoja kati ya wale wawili alipasuliwa kichwa kwa risasi kutoka kwa mdunguaji namba moja wa E.C.S, huku mwingine akikutana na kisu kikali kilichorushwa kwa ustadi na Mick na kutua katika koromeo wakati huo huo.

Kisha Mick akatoa ishara na hapo askari wanne wa E.C.S wakamfuata.Akaenda nao katika mlango wa jengo lile.Hapo akakuta makufuli makubwa mawili yamefunga chumba kile. Kwa kutumia bastola yake aina ya 'beretta' iliyofungwa kiwambo cha kuzuia sauti,Mick alipiga risasi moja kwa kila kufuli na kusambaratisha kabisa makufuli hayo.

Kisha Mick na askari wale wanne wakaingia ndani kwa tahadhari ya hali ya juu.Lakini kwa bahati nzuri hawakukuta mtu mule ndani.Ndani ya chumba hicho kulikuwa na mashine kede kede zilizohusika na mambo ya umeme. Pia kulikuw na jenereta kubwa pamoja na transfoma moja kubwa.

Mick aliweza kuiona swichi kubwa ya umeme wa ngome yote.Akaizima na kuiharibu kabisa. Ngome yote ikawa giza.

"Timu namba mbili mnaweza kuendelea na operesheni." Mick alizungumza kupitia kifaa cha mawasiliano.

"Poa tumekupata."Sauti ya ajenti Paul ikasikika kutoka katika upande wa pili.Kisha ajenti Paul na kikosi chake nao wakakwea ukuta na kuingia ndani.

Mara tu ajenti Paul na timu yake walipokwea ukuta,wakaanza kukutana na upinzani wa maadui wachache waliokuwepo eneo hilo hivyo mapambano yakaanza mara moja kwa kutumia bunduki zilizofungwa viwambo vya kuzuia sauti.Kwa weledi wa hali ya juu, Paul na kikosi chake walifanikiwa kuwaua adui wale kwa risasi kwa kuwawahi kabla hata hawajajibu mashambulizi.Kwa kuwa bunduki za vijana hawa wa E.C.S pamoja na ajenti Paul mwenyewe zilifungwa viwambo vya kuzuia sauti,hakuna risasi iliyosikika.

Upande wa ajenti Mick na kikosi chake,mara tu baada ya kuzima umeme,walivaa miwani maalum ya kuonea gizani.Kisha kwa tahadhari ya hali ya juu wakaanza kutembea umbali wa kilomita moja kuelekea katika nyumba ambayo , Mick na Clara walifanya 'surveilance' jana yake kwa kutumia 'drone' na kugundua kuwa ndimo walipo adui zao.

"Kuna mtu anaonekana ni fundi umeme anakuja huku kwenye 'power plant'(kule kuliko na chanzo cha umeme ambacho Mick alikwisha haribu)."Ilisikika sauti ya mdunguaji(sniper) namba moja katika kifaa cha mawasiliano cha Mick.

"Huyo ataona maiti za walinzi wa pale kisha atawashtua adui.Akikaribia tu mmalize."Sauti ya Mick ilisikika ikijibu.

Dakika ishirini baadaye, Mick na kikosi chake walikuwa wamejibana upenuni mwa nyumba ile ambayo ndiyo ilikuwa 'mlengwa mkuu' wa operesheni ile.Kikosi kizima kilichoambatana na Mick,walikuwa kimya unaweza dhani hakuna hata panya eneo hilo.

"Madam angusha moto kwenye mzinga wa nyuki."Mick alimuagiza Clara kupitia vifa vya mawasiliano.

Clara alitumia kompyuta kuongoza 'drone' nyingine iliyokuwa imebeba bomu lenye uzito na uwezo mkubwa wa kusambaratisha hata adui aliye chini ya ardhi.Clara aliiongoza ndege hiyo isiyo na rubani hadi mahali ambapo,katika 'surveilance' ambayo ilifanyika jana,waligundua ndiko ambako kuna vyumba vya kulala askari wa magaidi wale ambavyo viko chini ya ardhi.Mara baada ya kuifikisha 'drone' hiyo eneo husika,Clara alitumia kompyuta yake kufyatua bomu hilo ambalo lilisambaratisha kila kitu na kuwazika kabisa ambao walikuwamo katika eneo hilo na kutoa kishindo kikubwa sana na sauti kubwa ya mlipuko.



Mara baada ya kushuka kutoka katika gari, Mick alitembea kuelekea kule aliko James Omolo.Alikwenda kwa namna ambayo hakuna aliyedhani kuwa kuna mtu anamfuata.Alipokuwa umbali wa hatua tatu kutoka alipo James Omolo ndipo alipoanza kuzungumza kwa sauti ya juu na kuwafanya watu wasiopenda shari wasogee pembeni.

inaendelea.........


"James Omolo, gaidi uliyesumbua sana Afrika na dunia kiujumla,uko chini ya ulinzi kuanzia sasa.Ukijaribu kubisha nina ruhusa ya kukumaliza hapahapa."

Baadhi ya watu walidhani ni utani na kama ilivyo jadi ya watanzania,baadhi hata walisogea kushangaa ni nini kilichoendelea.Ghafla Omolo alisimama na kutoa vitu vyote vya bandia alivyovivaa na kufanya aonekane katika uhalisia wake.Mara baadaa ya watu kumtambua, hawakujiuliza mara mbili.Walikimbia na kwenda kusimama mbali kabisa na eneo hilo.Kila mtu ndani na nje ya Afrika alimjua vizuri Omolo na matukio yake ya kigaidi na kikatili aliyowahi kuhusika nayo.

Mara baada ya kusimama, Omolo alianza kushuka ngazi na kumfanya Mick arudi chini kwa kushuka ngazi kinyume nyume hadi walipofika mwasho wa ngazi, mahali palipo na uwanja uliotengenezwa na lami.

Sasa hata watu waliopitaa barabarani walipaki magari yao pembeni na kuendelea kushuhudia mambo haya.

" I once heard that you are number one agent in your agency with the highest capability.But i'm yet to see what you got to be given such high position. I think your government is stupid and dumb.And your agency is useless.To day is your last day to breath.(Niliwahi kusikia kuwa wewe ni mpelelezi namba moja na mwenye uwezo wa juu katika idara yenu.Lakini sijaona bado ni kwa nini ulipewa nafasi hiyo ya juu.Nadhani serikali yako ni pumbavu.Na idara yako haina maana yoyote. Na leo nadhani ndiyo itakuwa ndiyo siku yako ya mwisho kuishi duniani)." Aliongea James Omolo kwa kejeli akiwa na lafudhi ya watu wa Afrika Magharibi.

"Fare well Mr. Omolo(Kwa heri bwana Omolo)."Aliongea Mick huku akitabasamu na kujiweka tayari kwa mapigano.

Omolo ndiye aliyeanzisha mapigano kwa kurusha makonde na mateke mazito mazito kwa ghafla.Lakini Mick aliyaona yote hayo.Aliyapangua kwa ustadi sana,japo baadhi yalimpata kutokana na ughafla alioanza nao Omolo.

Baada ya kujiweka sawa Mick naye akamshambulia Omolo kwa mapigo ambayo Omolo aliyaona na kuyakwepa na kupangua baadhi.Mapigano haya yaliendelea huku kila mmoja akibadili mitindo adhimu zaidi ya mapigano na bado hakuna aliyedondoshwa chini.

"Mr.Mick, i told you that you are useless.Say hello to the hell(Bwana Mick nilikwambia wewe huna lolote.Sasa wasalimie kuzimu).James Omolo alizungumza kwa kejeli.

Mick hakujibu kitu.Alitabasamu kwa muda kisha akaamua kuonesha sura ya kazi.Sasa alitambua kuwa muda wa maneno matupu umekwisha. Akajiweka katika mpangilio wa mapigano kisha akamuita James Omolo kwa ishara ya mkono.James akamfuata Mick kwa kasi ya ajabu huku akirusha ngumi na mateke kwa namna ya mchezo wa kung-fu. Mick aliyaona yote hayo na kuyakwepa huku akijibu mashambulizi kwa kuibia.

Mtindo huu alioutumia sasa Mick ulizaa matunda haraka.Mtu yeyote ambaye angemshuhudia Mick akipambana asingesita kutambua kuwa Mick alikuwa anajua anachokifanya kwa hali ya juu sana.Kila wakati ambao James Omollo alijaribu kurusha ngumi moja,alijikuta imekingwa kiustadi na kushambuliwa na ngumi mbili au tatu za haraka.Kama alidhani yeye ni mjuaji,basi leo alikutana na mjuvi wa mambo wa hali ya juu.

James Omollo alijaribu kutumia ujuzi wake na ujanja wake wote hata ule ambao kwa kawaida huwa anauweka akiba,lakini Mick alikuwa mbele yake hatua kadhaa kila wakati.Hakuwahi kukutana na upinzani kama huu tangu kuzaliwa kwake.Mara ya kwanza wakati wanaanza kupambana, James alidhani Mick alikuwa anapambana kwa uwezo wake wote na ndiyo kaana alimkejeli.Lakini sasa alitambua kuwa ule wa mwanzo haukufaa hata kuitwa uwezo mbele ya Mick. Kejeli na dharau zilikuwa zimemponza.

Sasa James Omolo alionekana dhahiri kuwa amezidiwa ubavu japo aliendelea kujikakamua.Lakini bado aliendelea kutoa matusi na kauliza dharau kwa Mick na nchi ya Tanzania kiujumla hukuakisema kuwa Tanzania haitaweza kushinda vita ya ugaidi ambayo imeichokonoa kamwe.Na badala yake,Tanzania itajutia kuanzisha vita hii.

Sasa Mick aliamua kummaliza kabisa.Kwanza akamuhadaa kama anataka kumpiga teke.James alipolikinga teke lile akajikuta amepigwa kwa ngumi nzito sana mbili za haraka za kifuani huku akimaliziwa na teke lililomvunja mbavu upande wa kulia.Kisha akapigwa ngwala na kuanguka chini.Kila alipojaribu kuamka akakutana na teke la mbavu tena.Mara apigwe kifuani.Mara akaanza kutapika damu Kwa wingi.Hapo Mick akaona haina haja ya kumkawiza, akamkaba shingoni kwa kiwiko.Kila Omolo alipojaribu kujinasua alishindwa kabisa.Mara akaanza kupoteza pumzi pole pole.

"Kawasalimie kuzimu."Mick aliongea kisha akamnyonga shingo hadi aliposikia sauti ya mvunjiko.Gaidi la kimataifa James Omolo alikuwa ni marehemu tayari.

Watu waliokuwapo eneo hilo bado walikuwa katika mshangao mkubwa sana.Walikuwa wameshuhudia mapambano haya ya ana kwa ana kwa muda wa nusu saa sasa.Walimshangaa kijana huyu aliyevalia nadhifu na akiwa na haiba na mvuto sana,namna alivyo mmaliza gaidi huyo kwa mapigano ya ana kwa ana. Muda wote walikuwa wakishangaa namna alivyopigana kwa ufundi mkali namna ile.Ilikuwa ni zaidi ya muvi kali sana ya mapigano.

Mara Mick alipommaliza James Omolo, aliubeba mwili wake na kuuweka katika gari aina ya Range rover ambalo alikuja nalo kisha akaondoa gari kwa kasi sana.Alikuwa anaelekea katika kambi la jeshi la JWTZ Mbalizi.

Alifika Mbalizi dakika chache sana baadaye. Taarifa za kufika kwa Mick zilikwisha fika kabla.Jina lililotambulika kwa sasa ni Luteni Juma Ahmedi.Askari wa Pale kambini wakamsaidia kutoa mwili na kuubeba kuupeleka maabara ambako maiti ingefanyiwa utafiti zaidi.

MASAA MAWILI NYUMA

Wakati ambao Mick alikuwa bado amepaki gari nje ya hospitali ya Meta, alipata kuwasiliana na ajenti Paul.Ajenti Paul alikuwa ana Taarifa Muhimu sana kwa Mick.

"Oya, tumembana James Peter kwa mbinu zilizoboreshwa na tumefanikiwa kumtapisha mambo mengi sana.Moja wapo ni kuhusu 'book of codes'. Ametuambia kuwa 'book of codes' ni mali ya James Omolo na ameificha mahali ambako hakuna anayejua.Ila pia ametuambia kuwa huwa mara zote alipo Omolo ndipo ilipo 'book of codes'."Ajenti Paul alitoa taarifa.

"Ok,bado niko katika harakati za kumpata huyo mwanaharamu.Nikimtia mikononi nitahakikisha kwanza nang'amua wapi alikoficha 'book of codes'."Mick alijibu.

Mara Mick alipokutana na Omolo nje ya jengo la TAZARA na kabla hata hawajaanza kupambana,Mick aligundua kitu tayari.Katika mkono wa kushoto juu kidogo ya kiwiko cha mkono,James Omolo alikuwa na kovu la jeraha lililoonekanakuwahi kushonwa.Mick alipolitazama kwa umakini wa kuibia,aligundua kuwa halikuwa kovu la jeraha lililotokea kiajali ajali.Kwa namna lilivyonyooka,Mick aligundua haraka kuwa inawezekana Omolo aliwahi kujikata kwa makusudi mahali hapo na kisha kujishona. Kwa uzoefu wa kazi ya kupambana na wahalifu kama hawa,Mick alijua kuwa inawezekana kabla ya kujishona mara baada ya kujikata kwa makusudi, James Omolo alificha kitu fulani kidogo mahali hapo alipojikata kisha akashonea kwa juu.Labda alishonea kitu ambacho ni cha siri sana au kingemuelekeza kuelekea kwenye kitu kilichofichwa kwa siri sana.Na labda kuna uhusiano na 'book of codes'.

Hata hivyo,Mick alitambua kuwa asingeweza kumtapisha siri yoyote James Omolo,hivyo akaamua kumuua kisha aendelee kutafuta 'book of codes' mwenyewe.

******************************

Maabara ndogo, Hospitali ya jeshi-JWTZ Mbalizi.

Mick alikuwa mbele ya mwili wa James Omolo ndani ya maabara hii.Macho yake yalikuwa yakiangalia katika mkono wa kulia juu kidogo ya kiwiko.Alikuwa akiangalia tena kile alichokiona kwa mara ya kwanza wakati akipambana naye nje ya jengo la ukumbi wa abiria TAZARA.

Wakati huu alikuwa ameshika kiwembe cha kufanyia operesheni mbele ya mwili huo. Mick aliushika mkono wa kulia wa marehemu James Omolo,kisha akauchana katika eneo lile la kovu lililokuwa na rangi nyeusi.Kisha akaingiza vidole vyake viwili katika sehemu ile alipopakata.Hapo alihisi ameshika kitu kigumu. Akakivuta na kukitoa.Kilikuwa ni kikasha kidogo cha plastiki ambacho kilijaa damu kwa nje.Mick alikifuta kikasha hicho kwa pamba safi iliyokuwa pembeni yake.Hapo kikasha kile kikaangaza kuonesha ndani kilikuwa na kitu.

Mick akakifungua kikasha kile.Ndani akakutana na kikadi kidogo cha kutunza kumbukumbu(Memory chip).Mick akatoa 'memory chip' na kuipachika katika simu yake ya kisasa kabisa kisha akajaribu kuminya hapa na pale ili kuifungua 'memory chip' ile. 'Memory chip' ikataka neno siri ili iweze kufunguka.Mick akaona isiwe shida.Alipanda gari lake na kuanza kuliendesha kwa kasi kuelekea Iringa,katika ofisi ya idara ya C.T.I ya muda.

MASAA MANNE BAADAYE.

Wataalamu wa kompyuta wa C.T.I walikwishafanyakazi yao. Morris na Clara walikwishafanikiwa kuifungua 'memory chip' iliyoletwa na ajenti Mick kwa ujanja ujanja wa udukuzi wa data na taarifa.

Mara baada ya kuifungua 'memory chip' ile,nyuso za tabasamu zilitawala ghafla katika nyusi zao.

"Bingo. 'Book of codes' .Sasa kilichobaki ni kumalizia kazi hii." Alizungumza Mick kwa furaha ya kukamilisha kazi hiyo kwa mafanikio mengi japo siyo yote.

Ndiyo.Mafanikio hayakufikia asilimia mia mbele ya dunia nzima kwa kuwa mlengwa mkuu wa mtafutano huu tangu mwanzo, Omar Al-Mahmood alikuwa bado hajakamatwa na kutiwa nguvuni kaa ambavyo ilitakiwa.Lakini kwa upande wa Tanzania,mtafutano huu uliibua maovu mengi yaliyowahi kufanyika na ambayo yalitarajia kufanyika.

Wataalamu wa kompyuta wa C.T.I sasa walibakisha kazi moja ili kuhakikisha mafanikio makubwa ya operesheni hii.Ilikuwa ni kutumia 'book of codes' kuyatambua majina ya wahusika wa uovu huu uliokuwa unatarajiwa kutimizwa, ambao ilisemekana walikiwa wako nddaniya serikali na baadhi ya watu maarufu zaidi nchini.Walikuwa katika kuhitimisha.

SOMALIA

Hali ya hewa ilikuwa ni upepo mkali sana na mvua za rasha rasha katika mtaa wa Madina jijini Mogadishu.Ndani ya jyumba moja ,baba mmoja pamoja na familia yake walikuwa katika wakati mgumu sana. Dakika chache zilizopita,familia hii ilipata ugeni ambao hawakuutarajia.Ugeni huu uliwahusisha watu wawili warefu, wembamba huku mikononi wakiwa wameshika bunduki aina ya AK 47.

"Jamani nisameheni,naahidi sitakamatwa na hata nikikamatwa sitatoa siri hadi siku nitakapokufa."Baba huyu wa familia aliyebeba tumbo kubwa lililotokana na kutumbua mali wakati alipokuwa madarakani nchini kwake kabla ya kutorokea katika nchi hii,alijaribu kujitetea.

"Wewe ako jinga sana.Sisi habana wesa achia wewe.Umesababisha mupango ya bosi yetu kuharibika kabisa.Wewe ametoroka ameacha makabrasha mengi muhimu yenye siri nyingi na sasa ako mikononi mwa serikali na amesha weza kutafsiri siri zetu.Sisi habana mucheso.Tutakachokusaidia tutakuua wewe peke ako.Hii ni nadra sana.Kawaida sisi alitakiwa kuua familia ote."Alijibu mmoja kwa kiswahili kibovu kilicho na lafudhi ya kisomali.

Baba yule hakuwa na la kusema zaidi ya kujutia kushirikiana na watu hawa ili kujineemesha na hata kutaka kuhusika kuiangamiza nchi yake kwa faida zake binafsi. Familia yote ililia sana lakini watu wale walitoka nje pamoja na mzee yule kisha wakafunga mlango nyuma yao.

Risasi nane zilimiminwa katika kifua cha baba yule wa familia na huo ndiyo ukawa mwisho wa maisha yake. Waziri wa ulinzi wa Tanzania ambaye aliisaliti nchi yake,alikiwa amepata hukumu ya kifo kutoka kwa watu wabaya ambao alishirikiana nao hapo awali.

*************************************

IKULU-Magogoni, Dar es salaam.

Rais George Katumba alikuwa katika kikao cha siri na mkurugenzi wa C.T.I pamoja na wanausalama wote kutoka ndani ya idara hii.Mkurugenzi wa C.T.I , alikuwa anakabidhi majina ya wasaliti waliotaka kuiuza serikali ya nchi mikononi mwa Magaidi wa Al-shabaab.Majina maarufu yalikuwa mengi.Yalijumuisha mawaziri,manaibu waziri,Wakuu wa mikoa,wafanyabiashara wakubwa na hata wakuu wa vyombo vya usalama.Mnyororo ulikuwa mrefu sana na ulihusisha wengi sana.

"Mumefanya kazi nzuri sana.Nimepigiwa simu kutoka Marekani,wamewapa sifa sana.Japokuwa hamjamkamata Omar Al-Mahmood, lakini mumemkamata Abdallah Yusoof,mtubaliyemfanikisha sana Omar Al-Mahmood.Pia mumefanikiwa kumuangamiza James Omolo, gaidi aliyesumbua dunia kwa muda mrefu.Mumeteketeza vikosi vya kigaidi ambavyo vingeweza kuja kuwa mwiba mchungu kwa serikali na nchi kiujumla.Mumefanikiwa kuwatambua wasaliti wa nchi hii. Ninawahakikishia kuwa ninawaamini sana.Waliopo katika majina haya watafilisiwa hadi senti ya mwisho na kisha watahukumiwa kwa mujibu wa sheria na watajuta kujihusisha na ugaidi wakati dunia nzima inaupinga."

"Sasa najua magaidi wataleta chokochoko nyingi huko mbeleni.Mimi ninawaahidi kuwa ofisi maalum ya rais itawasaidia na itawaboresha zaidi na zaidi kuliko hivi sasa."Alimaliza kuzungumza Rais George Katumba.

Wanausalama wa C.T.I nao waliongea mambo mbalimbali yanayohusu mipango ya usalama ya mbeleni hasa kwa upande wa vita dhidi ya ugaidi.Baada ya hapo kulifanyika tafrija ya siri ndani ya ikulu hiyo.Hakika ilikuwa siku ya furaha.

*************************************

"Mick unakwenda wapi kipindi hiki cha likizo?"Aliuliza Mkurugenzi wa C.T.I bwana Eliakim Makassy.Wakati huu maajenti wa C.T.I waalikiwa wakila chakula cha jioni katika hoteli moja kubwa ya kitalii ndani ya jiji la Dar es salaam.

"Narudi Ibiza kula bata na watoto wazuri mzee.Si unakumbuka ulikatisha likizo yangu."Alijibu Mick kwa masihara.

"Acha uhuni wewe.Inabidi uoe sasa.Vinginevyoutakufa kwa ngoma."Alidakia Paul.Naye aliongea kwa masihara.

"Amenishindwa mtu hatari Omolo,ngoma itaniwezea wapi babuuu"

"Alikushindwa wapi wakati alikuonea huruma ulivyokuwa unalialia."Aliongea Paul

"Nyie bakini hapa nchini.Omar Al-Mahmood akija tena mjiandae kukatwa vichwa."Mick aliongea kwa kucheka.

"Hahaaaaaa." Wote wakacheka kwa sauti huku wakigonganisha viganja.

**TAMATI**


Mwisho wa stori hii ni mwanzo wa stori nyingine.....stori inayofuata itakuwa na muendelezo wa mtafutano kati ya idara matata ya C.T.I na magaidi akiwamo Omar ambaye bado hajakamatwa...


MWISHO

0 comments:

Post a Comment

Blog