Search This Blog

Thursday 23 March 2023

MSAKO WA MWEHU - 2

 


Simulizi : Msako Wa Mwehu

Sehemu Ya : Pili (2)


Ilipofika saa kumi alasiri, shangwe, hoihoi, nderemo na vigeregere vikaibuka kisha watu wakatulia vitini raha mustarehe kama Sultan bin Jerehe. Nderemo hizo zilikuwa ni kuashiria kuwasili kwa Waziri wa Mambo ya Ndani Mheshimiwa Ngaiza Jacob Ngaiza akiwa ameambatana sambamba na wageni wake watukufu Mabalozi wa Marekani na Canada. Wakakaribishwa meza kuu huku viongozi wengine wa chama na serikali wakiwa wameshachukua viti vyao. Zikaanza hotuba mbalimbali za wageni hao wakiwa wameambatana na Maofisa wao wa kutoka Ubalozini. Kisha ukafika wakati adhimu wa kukabidhiana vifaa hivyo. Wakaitwa mbele ya kadamnasi wageni wa heshima wote wakasogelea yale magari na kompyuta. Wakaanza kuzungukwa na wanahabari kwa ajili ya kuchukuliwa picha na video za kutosha kwa ajili ya vyombo vyao vya habari.
Balozi wa Marekani na Balozi wa Canada wakapanda kwenye magari pamoja na Waziri wa Mambo ya Ndani kwa ajili ya kuyajaribisha. Waziri wa Mambo ya Ndani, Mheshimiwa Ngaiza, alipopachika funguo kwenye swichi ili awashe gari alipowasha tu, gari linataka kuwaka kisha likagoma kwa kuzimika. Ghafla moshi mzito ukaanza kufuka mbele ya boneti la gari, kabla hawajafahamu kinachendelea ukalipuka mlipuko mkubwa wa bomu kwenye lile gari haujapata kusikika tokea Jiji la Dar es salaam ligeuzwe jina kutoka kuitwa Mizizima. Kishindo kikubwa hicho kikazusha taharuki na tafrani eneo zima la Posta Mpya kila mtu akawa anakimbilia upande wake kuokoa roho yake. Ajali nyingi zilitokea barabarani siku hiyo kwa magari kugongana yenyewe kwa yenyewe na watu kugongwa kwa sababu ya hofu iliyotokana mlipuko huo uliotokea jioni hiyo.


Jumamosi nyeusi iliyotanda huzuni
Kulipokucha kila kona ya nchi katika siku hiyo ya Jumamosi gumzo lilikuwa ni tukio la mlipuko wa jana yake kwenye jengo la Wizara ya Mambo ya Ndani. Magazeti yote yalitoa taarifa ya tukio hilo kwa ufasaha kabisa. Televisheni zote za ndani ya nchi zilisitisha vipindi vya burudani na michezo wakawa wanaripoti juu ya tukio hilo la kishenzi na kinyama mfululizo.
Mpaka kufikia saa sita mchana wa siku hiyo ya Jumamosi ilithibitika watu 50 walifariki dunia huku zaidi ya 100 wakilazwa hospitalini Muhimbili kama wahanga wa kisanga hiko cha kigaidi. Miongoni mwa waliofariki dunia walikuwa ni Mabalozi wote wawili wa Marekani na Canada, pamoja na Waziri wa Mambo ya Ndani. Pia Wabunge 10 nao walipoteza maisha yao, hivyo ilikuwa ni misiba iliyogusa Tanzania nzima. Kama hukufiwa na Mbunge wako, basi utakuwa umepoteza Mjomba, Shangazi, Rafiki, Baba, au Mama ili mradi kila mtu aliguswa kwa namna moja au ingine.
Amiri Jeshi Mkuu, Rais wa Nchi alizungumza mubashara na wananchi kupitia vyombo vya habari vya redio, televisheni na mitandao ya kijamii. Alitangaza maombolezo ya kitaifa ya wiki moja na bendera ya taifa itapepea nusu mlingoti. Pia aliwataka wananchi kuwa watulivu wakati vyombo vya usalama vinawasaka wahusika ili wafikishwe mahakama. Akawahakikishia kuwa serikali yao ipo makini kuhakikisha inavitumia vyombo vyake vya ulinzi na usalama na wananchi kukabiliana na tishio la makundi ya kigaidi dhidi ya Tanzania.
Ikapangwa Ijumaa ijayo kuwa ni ya mazishi ya kitaifa. Ambapo Wabunge waliofariki watapelekwa Dodoma Bungeni kuagwa kwa heshima zote kisha maiti zao zitapelekwa Majimboni kwao kwenda kuzikwa. Miili ya Mabalozi wa Marekani Na Canada ilisafirishwa kwenda nchini kwao kuzikwa. Pia serikali ya Marekani ikawataka raia wake wote waliopo Tanzania warejee nyumbani mara moja mpaka tishio la kigaidi dhidi yao litakapokoma. Wingu jeusi lilitanda katika nchi ya Tanzania kwa upande wa kidiplomasia. Ilishachafuka kimataifa sifa yake ya kuwa kisiwa cha amani na usalama, ikapotea na kuanza kuonekana kuwa sio sehemu salama tena bali ni kisiwa cha mauti na machafuko.
Vyombo vya usalama vilikuwa sasa vinaanza mkesha wa usiku na mchana kwa ajili ya kuwasaka wahusika wa tukio hilo la kigaidi.

SURA YA NNE
"Magaidi wajianika dhahiri shahiri"
Vyombo vya Dola vilichanganyikiwa havikufahamu lengo la magaidi kufanya shambulio hilo kwa nchi ya Tanzania. Mashushushu wakatawanywa kila mtaa wanahaha na kunusanusa kutafuta penyenye za watu waliokula njama za kulipua mabomu kwenye Jengo la Wizara ya Mambo ya Ndani, Ijumaa iliyopita.
Ilipofika siku ya Jumapili asubuhi fumbo la makusudio ya shambulio hilo likateguka, likawa hadharani kweupe. Vipeperushi viliokotwa vimesambazwa mitaani maeneo yote ya Jijini kuanzia Posta Mpya mpaka Kariakoo. Mbagala kuu mpaka Bunju, hakuna kichochoro, wala kinjia ambacho vipeperushi hivyo havikufika. Kipeperushi hicho kilisomeka kama ifuatavyo :
"TUNATAKA NCHI YA TANZANIA IKATE MAHUSIANO YA KIDIPLOMASIA NA MAADUI ZETU NCHI YA KENYA MARA MOJA. TUNATOA MUDA WA SIKU TATU TU BALOZI WA TANZANIA AWE AMERUDISHWA TANZANIA, MWISHO JUMATANO IJAYO, VINGINEVYO KISHINDO KINGINE KIKUBWA KINAKUJA MJIANDAE KUCHIMBA MAKABURI MENGI ZAIDI"
??? ????? ?????
Ujumbe huo ulioishia na chata ya maandishi ya lugha ya kiarabu ulizusha kizaa upya na kupandikiza hofu mpya miongoni mwa wananchi. Hapo kila mtu akawa anajiuliza "hao walioandaa kipeperushi ni watu gani, mbona hawajajitaja!". Wale watu waoga wenzangu na mimi wakaanza wakakacha kwenda Mjini tena, na wengine wakarudi Mikoani kwao kabisa kupisha upepo mbaya upite.
Magaidi walishafanikisha walichokikusudia, nacho ni kupandikiza hofu na taharuki miongoni mwa wananchi na kudhoofisha uchumi wa nchi. Pia watalii wakaanza kuogopa kuitembelea Tanzania. Kwa watu wa usalama kwao haikuwa shida kutambua kuwa hivyo ni vitisho toka kundi la kigaidi la "Al-shabaab", walihitaji muda tu kuthibitisha dhana yao hiyo. Adui aliyetangaza vita ya hadharani na nchi ya Kenya ni kundi la kigaidi la "Al-shabaab". Kundi hilo lilikuwa linaendesha mapambano ya ulipizaji kisasi dhidi ya Jeshi la Kenya ambalo katika miaka michache iliyopita lilijiunga na "Vikosi vya Umoja wa Afrika" (AMISON) kwa lengo la kuwaondoa wapiganaji wa kundi hilo katika Miji mikubwa na midogo nchini Somalia. Hivyo vipeperushi hivyo sasa vilionyesha "Al-shabaab" wanakusudia kuifanya Kenya ni kisiwa, iwe nchi iliyotengwa na majirani zake wa Afrika Mashariki. Mipango ambayo walijua fika kama itafanikiwa itadhoofisha Umoja wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Afrika kwa ujumla. Hivyo kuzima ndoto za viongozi waasisi wa Afrika akina Kwame Nkurumah wa Ghana na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere wa Tanzania. Ndoto yao ya kutamani uwepo wa Umoja wa Afrika wenye nguvu ya kisiasa, kiuchumi, kiutamaduni na kila nyanja ya kimaendeleo. Magaidi tayari walileta kishindo cha mtego kilichowanasa wakazi wa Tanzania.


Vibaraka wa Al-shabaab wakabidhiwa mikononi mwa Kachero Manu

Ofisi za Usalama wa Taifa kitengo maalumu cha Ujasusi, zilikuwa zipo katika jengo la "Benjamin William Mkapa Pension Tower" roshani ya tano katika mtaa wa Azikwe. Zamani jengo hili lilikuwa linaitwa "Mafuta House". Zilikuwa ni ofisi za siri ambazo mtu wa kawaida huwezi kujua kazi wanazofanya watu hao. Ilikuwa ni Ofisi yenye Makachero bobezi wasiozidi watano, pamoja na Mkuu wao wa kazi mpya Bwana Omega Mtanika na Katibu Muhtasi wao dada Kokunawa.

Siku hiyo ya Jumatatu asubuhi Makachero wawili 'Manuel Yosepu maarufu kama "Kachero Manu" na Kachero wa kike Yasmine Abeid walikuwa wameitwa ofisini kwa Mudiru wao wa kazi Bwana Omega Mtanika ili wapewe jukumu jipya la kikazi.
Kachero Manu alikuwa ndio kwanza bado mpya mpya hajamaliza hata fungate lake la ndoa aliyoifunga hivi karibuni na mpenzi wake wa siku nyingi, tokea akiwa Chuo Kikuu, Bi Faith Magayane. Alipigiwa simu jana yake Jumapili saa sita mchana, akiwa yupo "Hotel Verde", Zanzibari na Katibu Muhtasi wa Mudiru wake kuwa anatakiwa arudi ofisini mara moja.

Mara baada ya vipeperushi vya magaidi wa "Al-shabaab" kusambazwa kwenye kila kona ya Jiji. Idara ya Usalama wa Taifa ikaona kuna haja ya Jeshi la Polisi kupigwa jeki na Kachero Manu, ambaye ametabahari katika fani ya Ukachero. Maji yalishazidi unga kwa Jeshi la Polisi, mapambano dhidi ya magaidi walio na uthubutu wa kufanya shambulio katika Makao Makuu ya Wizara ya Mambo ya Ndani yalikuwa ni mapambano kabambe. Ilikuwa ni patashika ya nguo kuchanika, mtoto hatumwi dukani, ngoma inogile mpaka kieleweke.

Kachero Manu kumuelewesha mkewe kuwa anavunja fungate kwa sababu ameitwa ghafla kazini, ilikuwa ni kazi nzito kueleweka. "Kama kazi yenyewe hiyo ambayo inakukosesha hata muda wa kutulia na mke wako katika kipindi muhimu kama hiki cha fungate bora uache kazi tu. Huu ndio muda adhimu tuliotakiwa kama wanandoa wapya kujenga mustakabali wetu mpya wa namna ya kuendesha maisha yetu" yalikuwa ni maneno makali yaliyoropokwa na mke wa Kachero Manu akiwa amefungwa na joto la hasira kooni mwake.

"Sasa mke wangu nikiacha kazi hii nitafanya kazi gani? " aliuliza Kachero Manu swali la mtego kwa sauti ya kubembeleza huku amemkazia macho mkewe. "Utajiajiri tu, utafute shamba Bagamoyo unalima mbogamboga na matunda na huku unafuga ng'ombe na kuku maisha yatajipa tu" aliweka msisitizo kwa sauti ambayo inaonyesha anamaanisha kile anachokizungumza hatanii japo chembe.

"Mke wangu, uhondo wa ngoma ingia uicheze, usizuzuke na ile michanganuo ya kilimo sijui cha matikiti au ufugaji wa kuku inayokufikia mezani kwako pale benki kwenye idara yako ya mikopo ukajua basi kilimo na ufugaji kinalipa sana.

Michanganuo mingi inakolezwa matokeo kuliko uhalisia ulivyo, mie imani yangu naamini kila Mtanzania mkubwa kwa mtoto ana Diploma ya Usanii hata kama hajasomea sanaa kule chuo cha TASUBA, Bagamoyo. Utaletewa mchanganuo wa kilimo cha matikiti uelezwe ekari moja itakuzalishia milioni sita, lakini ukienda kukifanya hicho kilimo au kuangalia hali halisi ya uchumi wa wakulima hao wa matikiti hauendani na michanganuo yao uliyoisoma. Kilimo na ufugaji Tanzania bado kuna changamoto kubwa ya masoko, bei duni, pembejeo feki, na zinginezo kibao. Labda serikali yetu siku za mbele ije na sera ya kulinda bei ya wakulima wa mbogamboga na matunda na bidhaa za mifugo kama mayai, maziwa na nyama. Vinginevyo bado haujanishawishi mke wangu kucheza pata potea na ya kuacha kibarua changu kinachonipa jeuri Jijini" alimalizia maelezo yake Kachero Manu bila kupindisha maneno kwa mkewe ili kumuweka sawa.

"Mhhh....haya bana ngoja tukomae na ajira za mkoloni za maofisini, ambazo zinatubana mpaka tunashindwa kufurahia maisha ya kifamilia, muda wote tunatenganishwa na majukumu ya kikazi tu" alijisemesha kwa manung'uniko mke wake huku akionekana ameshakubaliana na maelezo ya mumewe kwa shingo upande.

"Magaidi wamelipua Wizara ya Mambo ya Ndani na kusababisha vifo vya viongozi kadhaa, hivyo hamna mtu anaweza kuwafunza adabu magaidi kama mimi serikali ndio imeona hivyo, ngoja nikatoe jasho na damu yangu kwa ajili ya nchi yangu. Nchi ikichezewa na magaidi wakafanya wanavyotaka wao watakuja kutupangia mpaka muda wa kulala na kuamka" aliendelea kukizalendo kwa mkewe ili kumjenga kuwa ameolewa na mpambanaji katika medani za kivita, ambaye anaweza hata kuiacha familia yake miaka miwili mtawalia anaipigania nchi. Alitaka atambue kabisa kuwa hajaolewa na mwanamuziki ambaye anabembeleza mpenziwe kwa nyimbo, vilio na chakula cha nyuki, zawadi ya mauaridi.

Kachero Yasmine Abeid nae alijumuishwa kwenye jukumu hili kutokana na sababu mbili kubwa. Kwanza yeye ndio aliyefanikiwa kuzima mashambulio ya mabomu yenye viashiria vya ugaidi yaliyokuwa yanarindima Zanzibar kila kukicha katika miaka ile ya 2012-2013. Pia alikuwa ni fasaha sana katika bahari ya lugha za Kiarabu na Kisomali, hivyo huenda kuna nyaraka zinaweza kupatikana za siri yeye ndio atakuwa mtarujumani wa lugha kwa Kachero Manu. Alihamishiwa kikazi kuja bara kutokea Zanzibar yapata mwaka na nusu sasa.


"Mbwa koko wamejileta wenyewe wapeni mfueni wa nguvu"
"Vijana wangu, nimewaiteni kikao kifupi sana cha kupeana majukumu ya kutekeleza. Sisi kazi yetu ni vitendo zaidi, kuupepeta mdomo tumewaachia Wanasiasa huko kwenye majukwaa yao na Wachungaji na Mashekhe huko kwenye nyumba zao za ibada. Nadhani mnafahamu tukio lililotokea Ijumaa iliyopita...!" alisimamisha maongezi yake kwa muda Bosi Omega Mtanika akavua miwani yake na kuwaangalia usoni kwa kuwakazia macho yake makali Kachero Yasmine Abeid na Kachero Manu. Wote kwa pamoja wakatikisa vichwa vyao kuashiria wanajua tukio lililotokea siku ya Ijumaa. Alipoona wameafikiana na alichowauliza, akavaa tena miwani yake na kuendelea na maongezi yake.
"Sasa nimekutupieni zigo hilo mlibebe, kama mie nilivyotupiwa na wanene huko juu, mzigo mzito wabebebeshe wanyamwezi, sasa sisi ndio tumebebeshwa. Ujumbe wangu kwenu upo wazi mbwa koko, vibaraka wa "Al-shabaab" wamejileta wenyewe wapeni mfueni wa nguvu, wakawasimulie vizuri Mabwana zao wanaowatuma huko Somalia, mfuasi wa nzi daima hula uvundo wameyataka wenyewe" akaonyesha kuwa kamaliza maongezi yake.
Ukapita ukimya wa dakika kadhaa, kisha Kachero Manu akavunja ukimya huo kwa swali. "Je ameshajulikana nani atakuwa Mgeni rasmi katika mazishi ya Kitaifa ya Wabunge wetu hiyo siku ya Ijumaa, Dodoma?".
"Makamu wa Rais anategemewa kuongoza mazishi hayo ya Kitaifa" alijibiwa kwa ufupi na Mudiru wake Bwana Omega Mtanika. "Mkuu tunakuahidi utendaji uliotukuka, wewe chapa usingizi kwa raha zote, tuachie kazi sisi" aliongea Kachero Yasmine baada ya kuwa kimya kwa muda mrefu. "Ha ha ha ha.....nimefurahi Kachero Yasmine unanipa matumaini mazuri, hasa nikipitia kazi yako nzuri uliyoifanya Zanzibar, ambayo ilibaki kidogo tu igeuke kuwa Somalia ndogo" alijibu Bwana Mtanika kwa kuanza na kicheko, akifurahishwa na ujasiri wa Kachero wake. "Ameacha kula urojo wa Zenji sasa yupo Bara anakula ugali wa dona kwa mandondo ndio maana amekuwa mkakamavu kila siku ananiambia mikono inamuwasha anatamani kazi " alitania Kachero Manu, wote kwa pamoja wakafa kwa kicheko.
Wakaagana na kutawanyika, huku Kachero Manu akifuata guu moja na Kachero Jasmine kwenda kujipanga kwa kazi nzito iliyopo mbele yao.

Hamna kulala Jogoo limewika kumekucha
Siku hiyo hiyo baada ya kikao chao kwisha tu, waligawana majukumu. Kachero Yasmine alitakiwa haraka atangulie Dodoma kuangalia mazingira ya usalama wa viongozi watakaohudhuria siku ya Ijumaa kwenye mazishi ya Kitaifa. Hasa ukichukulia kipeperushi cha "Al-shabaab" kilichimba mkwara mzito wa kuleta maafa mengine kwa Taifa.
Kachero Manu yeye akaelekea moja kwa moja Wizara ya Mambo ya Ndani sehemu lilipotokea tukio la mlipuko wa mabomu kwa ajili ya kuanza taftishi yake ya awali. Alipowasili alikuta kikosi cha mbwa wa kutegua mabomu wametawanywa wananusa eneo la tukio kama kuna mabomu yamebaki yaweze kuteguliwa kwa haraka. Pia kulikuwa na magari makubwa ya kubeba yale magari ya msaada ambayo yamethibitishwa kuwa yapo salama, hayakupata athari ya milipuko ili yaanze kusambazwa yakafanye kazi iliyokusudiwa. Hali aliyokuta mahalo hapoilikuwa inasikitisha sana. Zile picha za majengo ya kule Somalia, Afghanistan, Syria zinazoonyeshwa kila leo kwenye runinga, zilifanania na jengo hilo. Sehemu kubwa ya jengo hilo hasa upande wa kushoto ambao yale magari yaliegeshwa kuliharibika vibaya sana.
Mubashara akaingia Ofisi ya Mapokezi akajitambulisha na kutoa kitambulisho chake cha kazi. Akaomba kuonana na mhusika wa Usalama wa Jengo. "Karibu sana Kachero karibu ukae, nipo tayari kukupa ushirikiano unaouhitaji toka kwangu" yalikuwa ni maneno ya ukarimu toka kwa Inspekta Chacha kwa Kachero Manu, akiwa amekaa ofisini kwake. "Ahsante sana" akajibu huku anavuta kiti na kukaa. Akachomoa peni yake, peni ambayo inauwezo wa kurekodi kwenye mfuko wa shati lake akafungua kidaftari chake kidogo na kuanza mahojiano na Inspekta Chacha;
Kachero Manu: "Kwanza poleni na matatizo, unaweza kunielekeza ni uharibifu kiasi gani umetokea"?
Inspekta Chacha: "Tumepoa tayari, uharibifu kwa haraka haraka siwezi kutoa makadirio, lakini ni mkubwa baadhi ya majengo yameporomoka kama ulivyoona na samani za ofisi na nyaraka kuharibiwa"
Kachero Manu: "Kuna mtu yoyote wa ndani mnamshuku kuhusika na tukio hili na mmefikia wapi kwenye upelelezi wenu? "
Inspekta Chacha: "Hapana hamna mtu yoyote ninayemtuhumu kwa tukio hili. Mpaka sasa tumekamata watu zaidi ya 200 na tunawashikilia na kuwahoji lakini hamna matumaini yoyote ya kumpata mhusika. Tunawashikilia tu ili mradi wananchi huko nje waone tunashughulikia suala hilo la ugaidi lakini hatuna ushahidi wa kutosha kuwabandika tuhuma hizo"
Kachero Manu: "Je naweza kupata picha na video za CCTV-Kamera za siku ya tukio"?
Inspekta Chacha: "Kama nilivyokueleza kuna uharibifu mkubwa wa samani ikiwemo vifaa vya hizo kamera nazo zimeharibika vibaya hatukuambulia kitu"
Kachero Manu: Ahsante sana kwa ushirikiano wako, kama nitakuhitaji tena sitosita kuja tena kutaka msaada wako
Inspekta Chacha: "Karibu hamna shida tupo pamoja mkuu".
Wakapeana mikono na kuagana na mwenyeji wake. Kachero Manu wakati anaweka vizuri vitu vyake kwenye brifkesi lake dogo la rangi nyeusi ili aondoke zake, akaonyesha kuna kitu amesahau kuuliza. "Samahani kuna wafanyakazi wowote wa hapa hasa wa kwenye karakana ya magari ambao hawajafika kazini"? alitupa swali Kachero kwa Inspekta ambaye nae alionyesha dalili za kujiandaa kutoka nje ya ofisi. "Kwa haraka haraka siwezi kukujibu, ngoja niende idara ya rasilimali watu nikapate majibu, nipe kama robo saa, nisubiri hapo kitini" alijibu Inspekta Chacha huku akifanya haraka kuondoka kwenda kuchukua taarifa anayohitaji mwenyeji wake.
Baada ya kitambo cha dakika 10, Inspekta Chacha alirudi na orodha ikiwa na majina ya askari 5 ambao hawakufika kazini. Karatasi ilikuwa imeorodhesha majina yao, vyeo vyao, na majukumu yao ya kazi na sababu ya wao kutokufika kazini na maeneo wanapoishi. Ripoti hiyo Ilieleza kuwa wawili walikuwa akina mama ambao wapo likizo ya uzazi, na wawili akina baba walikuwa wapo likizo zao za mwaka na mmoja hakutokea kazini kwa utoro tu na hana sababu yoyote, na kwenye simu yake ya mkononi hapatikani hewani.
Kachero Manu akaisoma ile karatasi kwa umakini mkubwa kisha akatabasamu, akaisunda kwenye brifkesi yake ile karatasi akaaga tena kwa mara ya pili na kutokomea nje ya ofisi. Alipotoka nje ya geti tu akavuka barabara na kwenda pale kwenye kijiwe cha jirani na Wizara wanapokaa watu, maarufu kwa fundi viatu Peter. Alikumbuka hajanunua gazeti lolote la michezo tokea asubuhi. Kachero Manu alikuwa ni mdau na mpenzi sana wa kabumbu, akiwa ni shabiki wa kutupwa, tena yule kindakindaki. Akachagua magazeti yake kadhaa ya michezo anayoyataka akalipia kwa kutoa noti ya Sh.10,000/=. Akawa anasubiria chenji yake toka kwa muuzaji aliyekwenda kuitafuta chenji hiyo. Kama ujuavyo masikio hayana pazia, ndipo akasikia mazungumzo toka kijiweni kwa fundi viatu jirani na muuza magazeti.
Mazungumzo ambayo kwake aliyatilia umuhimu mkubwa sana kutokana na yanayozungumzwa kuvuta hisia zake. Walikuwa wanajadili tukio la mlipuko wa mabomu siku ya Ijumaa iliyopita. "Ebana eeeh....., kifo kinatisha sana, jamani yule mwehu "Maso Maso" anayependaga sana kukaaga pembeni ya kiduka cha Bwana Soni nae alitimka mbio, baada ya kishindo kile sikumuona tena" alisema mmoja wa wana kijiwe hapo huku akionyesha kusikitishwa na tukio hilo.
"Na tokea mlipuko ule hajakanyaga tena eneo hili, labda atafuata furushi lake analoliachaga hapo kwa Soni chini ya meza yake, usicheze na kifo wewe mpaka mwehu anakiogopa". Maongezi hayo ya mporoto yalisababisha mapigo ya moyo ya Kachero kwenda matiti. Tayari alishaanza kunusa harufu ya sehemu ya kuanzia upelelezi wake. Alipotupa macho yake pembeni ya hicho kiduka jirani na aliposimama akaona kweli kuna furushi linalozungumziwa lipo ndani ya eneo la mmiliki, ila duka limefungwa.


"Kachero Yasmine anawasoma kinagaubaga Al-shabaab"
Usiku wa siku ya Jumatatu kuamkia Jumanne Kachero Yasmine akiwa tayari ameshatia nanga Jijini Dodoma, alikesha kusoma lundo la nyaraka na vitabu mbalimbali vitakavyomsaidia kwenye jukumu lake la kuwatia mbaroni magaidi waliohusika na milipuko. Alibeba nyaraka za siri toka 'C.I.A" na "F.B.I" zinazoelezea kundi la Al-shabaab kiundani.
Humo akadurusu kuwa "Al-shabaab" ni kifupi cha neno la kiarabu "Harakat ash-Shabab al-Mujahidin" kifupisho "HSM"; kwa Kisomali, inatamkwa "Xarakada Mujaahidiinta Alshabaab" maana yake kwa Kiswahili ni "Tapo la Vijana wa Jihad". Ni kundi la waislamu wenye itikadi kali lililoanzishwa nchini Somalia mwaka 2006 kutoka kwenye kundi la Muungano wa Umoja wa Mahakama za Kiislamu "Islamic Courts Union" (ICU).
Mara baada ya kupinduliwa kwa Rais wa Somalia dikteta Mohammed Siad Barre, mwaka 1991, dikteta ambaye aliyedumu madarakani kwa muda wa miaka 22, Somalia ikaingia kwenye mzozo wa vita vya wenyewe kwa wenyewe.
Katika mapigano hayo ya wenyewe kwa wenyewe kikundi cha Muungano wa Umoja wa Mahakama za Kiislamu "ICU" kikafanikiwa kujipachika madarakani nchini Somalia tarehe 6/06/2006 na kuleta utulivu ya muda mfupi nchini Somalia. Utawala huo wa "ICU" haukudumu madarakani kwa zaidi ya miezi 6. Ilipofika tarehe 27/12/2006 wakafurushwa madarakani. Ulipoangushwa utawala huo wa Kundi la Muungano wa Mahakama za Kiislamu ndipo "Al-shabaab" wakaibuka kwa kasi wakijimegua kutoka kwenye kundi la "ICU" wakiongozwa na muasisi wao Bwana Ahmed Godane.
Mwaka 2012 kundi hilo lilijiunga na kundi kubwa la kigaidi la Al-Qaeda ili kuimarisha nguvu zake. Mpaka kufikia mwaka 2014, Wanamgambo wa Al-Shabaab walikadiriwa kuwa 7,000 - 9,000, wakiwemo wageni wengi, hasa kutoka Yemen, Sudan, Kenya, Tanzania, Afghanistan, Saudi Arabia, Malaysia, Pakistan na Bangladesh wote wakidai kuwa na lengo la kuigeuza Somalia kuwa nchi ya Kiislamu itakayoongozwa kwa sheria za Allah na sio za kutungwa na binadamu kwenye Bunge.
Alivyomaliza kujisomea taarifa za "Al-shabaab" akaanza kuandaa dhana na kuzitafutia majibu mepesi mepesi ili kuzipanua fikra zake katika uwanda mpana. Akatengeneza dhana ya kwanza "Kitu gani haswa kinamfanya kijana ajiunge na makundi hatari ya kigaidi?".
Akajipa majibu yeye mwenyewe, kuwa huenda ni sababu za kiuchumi, anashawishika kwa ndururu za kujikimu mahitaji yake kama kijana hasa ukichukulia kuna changamoto kubwa ya ukosefu wa ajira Afrika na duniani kwa ujumla. Wapo wanojiunga kwa sababu za kidini, wamepata mafundisho potovu yanayowahimiza wakubali kufa kwa ajili ya kutetea dini yao. Wapo pia wanaojiunga kwa kuchukizwa na vitendo vya kikatili wanavyofanyiwa watu wanyonge akina mama na watoto, huku mashirika ya haki za binadamu wamefungwa midomo kupaza sauti zao. Mfano mabomu yanayotupwa na jeshi la Marekani kule Syria, Afghanistan, Iraq na kwingineko duniani yanasababisha kuzalisha kizazi cha magaidi wenye lengo la kulipiza kisasi.
Na wapo wanaoingia kwa kulazimishwa kwa nguvu, wanakuwa hawana jinsi ya kukataa. Kwenye maeneo ambayo magaidi wamesimika utawala wao kila kijana anawajibishwa kujiunga na jeshi. Akaanza kutengeneza dhana mbalimbali za namna ya kuzuia ugaidi. Waswahili wanasema kinga ni bora kuliko tiba, hivyo ni vizuri ikaandaliwa mipango mkakati ya kuziba mianya ya ugaidi.
Kwanza watawala waumize vichwa kubuni miradi itakayozalisha ajira kwa vijana. Pia taasisi za dini na majumba ya ibada yote lazima yasajiliwe na viongozi wake pia watambulike kisheria na wafuatiliwe nini wanachokifundisha kwa wafuasi wao.
Baada ya kumaliza tafakuri yake, Kachero Yasmine akajisomea vitabu mbalimbali vya lugha ya kiarabu na kisomali vinavyowachambua vizuri sana "Al-shabaab". Akajikuta amepata mbinu mujarabu ya kuwatia mbaroni Al-shabaab kiulaini sana. "Hawa punda wa-al-shabaab kasoro mkia hawachomoki kwa mbinu hii ninayoiandaa kwao" aliwaza Kachero Yasmine huku akijiamini kwa kazi yake, huku akifunga makabrasha yake.

"Kigogo wa Polisi anayetumia PT3001 ni mshukiwa wa Ugaidi"
Kachero Manu alipotoka Mwananyamala Kisiwani alikanyaga mafuta kisawasawa kuendesha gari yake kuharakia mlo wa mchana maeneo ya Ferry, Kigamboni kwa Mama Nitilie maarufu kwa jina la Bi. Mwajuma, anayesifika kwa ujuzi wa mapishi na upimaji wake ni shazi la chakula cha kushiba.
Huyu Bi Mwajuma inasemekana kuwa wali wake akikupikia ulikuwa unakolea nazi vilivyo. Wateja wake walikuwa wanamtania kuwa "kwenye mchele kilo moja anatia nazi saba". Bi. Mwajuma alikuwa anamjulia mteja wake Kachero Manu chakula gani anachokipenda. "Mwanangu leo wali mchafu au mweupe, karibu sana" aliuliza Bi Mwajuma kwa uso wa bashasha mujarabu akimaanisha anataka kula pilau au wali mweupe. "Shusha wa kushiba mweupe kwa mchuzi wa samaki na mandondo ya nazi tafadhali".
Alipoletewa tu akaanza kukisokota chakula kutokana na njaa kali iliyomshika. Akala fyuu kisha akashushia na maji baridi ya kwenye mtungi, akalipa pesa Sh. 2,500/= tu, akaaga kwa ajili ya kurudi ofisini kuendelea na harakati za ujenzi wa taifa.
Alipofika ofisini akaandaa ripoti fupi ya alipofikia kwenye upelelezi wake mpaka sasa na anachotarajia kukifanya kukamilisha kazi yake. Akazama kwenye dimbwi la uandishi wa taarifa zake. Kisha baada ya hapo akaamua kutuma taarifa ya maombi rasmi ya picha na video za picha za CCTV-Kamera kutoka majengo ya jirani na Wizara ya Mambo ya Ndani iliyolipuliwa. Alituma maombi katika jengo la Tume ya Katiba ile ya Warioba, pia na jengo linalotumiwa na Tume ya Uchaguzi na pembeni yake kuna jengo la yalipo makao makuu ya "Exim Bank".
Kuja kuangalia saa yake ya mkononi baada ya kumaliza kazi zake zote, muda ukawa unasoma ni saa kumi na mbili kasorobo ikabidi akurupuke mbio mbio kushuka chini ili aelekee mtaa wa Ghana jirani na yalipo Makao Makuu ya Wizara ya Mambo ya Ndani.
Akaamua aache gari yake atembee tu kwa miguu kwa kupenya katikati ya majengo ya ofisi za Posta Mpya. Ilimchukua takribani dakika 10 tu kufika mpaka dukani kwa Soni, alipokaribia zaidi akatoa miwani yake yenye uwezo wa kurekodi matukio kwa njia ya video na sauti kwa muda usiozidi saa mbili.
Kwa bahati ile anafika tu ndio anamuona Soni anafungua geti la mbele la chuma la kiduka chake. "Mr.Soni habari yako, pole sana na matatizo ya msiba" aliwahi kusalimiwa na Kachero Manu. "Ahsante kaka yangu tumeshapoa tumezika salama, nashukuru". Alijibu Soni, huku anaharakisha kufungua walau apate riziki yake aliyopangiwa na Mola wake kwa jioni hiyo.
"Samahani, nataka nifanye mahojiano mafupi sana na wewe nikiwa kama Afisa Usalama" alijitambulisha Kachero Manu huku akivaa uso wa kazi. Soni alivyosikia ule utambulisho akaanza kutetema mpaka za funguo za geti zikamdondoka chini. Kachero Manu akamuokotea huku anatabasamu akamkabidhi kisha akamshika bega lake.
"Ondoa hofu, ni maswali ya kawaida tu kuhusiana na kadhia iliyotokea Ijumaa iliyopita" alimtoa wasiwasi ili apate ushirikiano. "Naogopa nimeshikwa na fadhaa unajua rafiki zangu hapa nimefika tu sasa hivi wananipa taarifa kuwa kuna kigogo mmoja wa polisi ananitafuta kwa udi na uvumba, wanasema anakuja mpaka hapa anaangalia kibanda changu kisha anaondoka kana kwamba ananitaka mimi" alijibu Soni huku uso wake ukinywea kwa uoga mkubwa uliomtawala.
"Yeah labda mpelelezi mwenzangu, je wanamfahamu kwa sura?" alizuga wanafahamiana na huyo kigogo wa polisi ili kumuondolea hofu Soni. "Walivyonielekeza hata mimi namfahamu sana wajihi wake, lakini gari anayoitumia leo ni gari binafsi hamna anayeifahamu, gari yake ya kazini anayotembelea ni rangi buluu 'v8' namba zake za gari ni PT 3001" alielekeza kwa ufasaha.
Wakazunguka nyuma ya kibanda kwenye maboksi na uchafu wa dukani na kilipo kifurushi cha mwehu "Maso Maso". Kachero Manu akakalia kiti cha mbao kichakavu huku Soni akikalia juu ya dumu tupu, lenye rangi ya manjano la lita 20 la mafuta ya kula. Mahojiano yakaanza kama ifuatavyo;
Kachero Manu: "Unamfahamu vipi Maso Maso?"
Soni: "Kumfahamu kivipi ningeomba ufafanuzi "
Kachero Manu: "Hivyo hivyo unavyomjua" alijibu Kachero Manu kwa sauti yenye hasira ila hakutaka kujijulisha.
Soni: "Maso Maso", ni mwehu ambaye amezoea kukaa hapa dukani kwangu, pembeni hapo ulipokaa ndio kikazi chake. Iwe mvua iwe jua hapo ndio maskani yake, wanasema watu kapigwa kipapai"
Kachero Manu: "Ana muda gani tokea awe anakita kambi dukani kwako hapa?"
Soni:"Sikumbuki vizuri sana ila haizidi miezi sita"
Kachero Manu: "Kuna vitu labda alikuwa anaongea ongea na wewe? "
Soni: "Hapana, mara nyingi alikuwa anautumia kuimbaimba nyimbo zake na kuandika andika kwenye kidaftari chake, mara chache ndio alikuwa anaongea lakini maongezi yasiyo na mtiririko maalumu ya kiwehuwehu"
Kachero Manu: "Unaweza kunionyesha hilo furushi lake nione hicho anachokiandika!". Soni akajibu swali kwa vitendo kwa kwenda kubeba fuko lenye vitu vya chizi "Maso Maso" akalibwaga mbele ya Kachero Manu. Kachero Manu akasitisha mahojiano kwa muda akaanza kazi ya kuchakurachakura kwenye lile fuko la mwehu. "Kweli hili fuko la chizi, mpaka chupa za mikojo zimo! " alijisemea kimoyomoyo Kachero Manu. Kulikuwa na vikorokoro vya simu mbovu, taa mbovu za kuchaji za Mchina, karatasi zilizochanika za aya za Qu'ran, viwembe vilivyotumika, mabakuli na vikombe na kila aina ya takataka zinazostahili kuwemo kwenye furushi la chizi.
Alipokuwa anakaribia kukata tamaa akashika kitu kigumu,




Wakazunguka nyuma ya kibanda kwenye maboksi na uchafu wa dukani na kilipo kifurushi cha mwehu "Maso Maso". Kachero Manu akakalia kiti cha mbao kichakavu huku Soni akikalia juu ya dumu tupu, lenye rangi ya manjano la lita 20 la mafuta ya kula. Mahojiano yakaanza kama ifuatavyo;
Kachero Manu: "Unamfahamu vipi Maso Maso?"
Soni: "Kumfahamu kivipi ningeomba ufafanuzi "
Kachero Manu: "Hivyo hivyo unavyomjua" alijibu Kachero Manu kwa sauti yenye hasira ila hakutaka kujijulisha.
Soni: "Maso Maso", ni mwehu ambaye amezoea kukaa hapa dukani kwangu, pembeni hapo ulipokaa ndio kikazi chake. Iwe mvua iwe jua hapo ndio maskani yake, wanasema watu kapigwa kipapai"
Kachero Manu: "Ana muda gani tokea awe anakita kambi dukani kwako hapa?"
Soni:"Sikumbuki vizuri sana ila haizidi miezi sita"
Kachero Manu: "Kuna vitu labda alikuwa anaongea ongea na wewe? "
Soni: "Hapana, mara nyingi alikuwa anautumia kuimbaimba nyimbo zake na kuandika andika kwenye kidaftari chake, mara chache ndio alikuwa anaongea lakini maongezi yasiyo na mtiririko maalumu ya kiwehuwehu"
Kachero Manu: "Unaweza kunionyesha hilo furushi lake nione hicho anachokiandika!". Soni akajibu swali kwa vitendo kwa kwenda kubeba fuko lenye vitu vya chizi "Maso Maso" akalibwaga mbele ya Kachero Manu. Kachero Manu akasitisha mahojiano kwa muda akaanza kazi ya kuchakurachakura kwenye lile fuko la mwehu. "Kweli hili fuko la chizi, mpaka chupa za mikojo zimo! " alijisemea kimoyomoyo Kachero Manu. Kulikuwa na vikorokoro vya simu mbovu, taa mbovu za kuchaji za Mchina, karatasi zilizochanika za aya za Qu'ran, viwembe vilivyotumika, mabakuli na vikombe na kila aina ya takataka zinazostahili kuwemo kwenye furushi la chizi.
Alipokuwa anakaribia kukata tamaa akashika kitu kigumu, alipokivuta akakuta ni daftari. Akashikwa na tashiwishi ya kulifungua na kujua kilichoandikwa. Ikadondoka kikaratasi chakavu cha maandishi ya Kiarabu, akakihifadhi sehemu salama. Kisha alipozidi kulifungua daftari hakuona chochote cha kumsaidia zaidi ya namba za simu kochokocho.
Kachero Manu: "Je siku ya mlipuko, Maso Maso alikuwepo au hakufika kabisa?". Akaendeleza mahojiano yake baada ya kulifunga furushi vizuri.
Soni: "Ndio alikuwepo alikaa hapo hapo, ila siku hiyo alikuwa kama mgonjwa hakuwa mchangamfu na hakula chochote tokea asubuhi, ulipotokea ule mlipuko, taharuki iliyokuwepo siku hiyo kila mtu aliingilia upande wake, na hajaonekana tena eneo hili mpaka tuna wasiwasi kama amesalimika na kifo"
Kachero Manu: "Ahsante sana kwa ushirikiano wako, nikikuhitaji tena nitakuja na samahani kwa kukuchelewesha na biashara yako"
Soni: "Hamna shida karibu tena, ngoja nifungue duka langu sitaki kula mate " aliongea kwa sauti ya hasira huku uso wake umebeba mawimbi ya ndita kuonyesha kuchukizwa kwa kuhojiwa muda wa biashara. Kachero Manu hakujali akaondoka zake huku akiwa amechukua kila kiratasi na kile kidaftari cha "Maso Maso" huku akishukuru kwa kupata majibu yaliyomkifu kifaya.
Muda sasa ulikuwa umeenda harijojo, ilikuwa imeshafika saa moja kasorobo magharibi. Akapitiliza moja kwa moja mpaka kwenye geti la Wizara ya Mambo ya Ndani kwenda kukagua namba za hiyo gari v8 PT3001 aliyotajiwa na Soni kuwa kigogo anayeitumia hiyo gari anamsaka .
Kachero Manu alikuwa tayari kasharuhusiwa na walinzi wa eneo hilo kufanya ukaguzi wake wa gari anayoitafuta. Alikuta v8 zaidi ya 18 rangi ya buluu zimejipanga. Hayo yote yalikuwa ni magari yanayotumiwa na Vigogo wa Wizara na Polisi Makao Makuu. Akaanza kufanya spenkesheni yake kwenye yale magari. Alirudia zaidi ya mara tatu halikuona lile gari alilotajiwa jina namba zake na Soni, PT3001.
Kijasho chembamba kikaanza kumvuja mpaka kwenye meno. Uso wake ukala debe akaanza kukata tamaa ya kuikosa gari hiyo. Akaamua awashe na mwangaza wa tochi ya simu yake ya mkononi kusaidia mwangaza wa eneo lile. Alipofika kwenye gari lenye namba 'PT1003' akasimama kwa muda akiikagua. "Namba hili zinafanana na zilizotajwa PT3001 tofauti ni mpangilio wa namba tu, labda zinachezewa" aliwaza Kachero Manu.
Akaanza kuchezea kile kibao namba za gari, akakikuta kibao kimeungwaungwa kiufundi mkubwa huwezi kugundua kwa haraka. Katika kupekenyua akakuta kuna nyaya zimepita kwenye namba tatu na moja. "Shabaaaashiii......kuna mchezo mchafu unafanyika, inaelekea gari ikitoka geti kuna kitufe kinabinywa kuzichezea namba za mwishoni zinapishana ndio maana mtaani linasoma PT3001, lakini humu ndani linasoma PT1003, kwisha kazi ujanja wake upo uchi" alijisemeza yeye mwenyewe.
Haraka haraka akawa anarudi pale getini kuulizia jina la kigogo anayetumia lile gari lenye namba za utata.
Alipofika wakati anaandikiwa jina la kigogo anayeitumia hiyo gari, tahamaki mtaani karibia na getini ikasikika milio ya risasi mbili zilizopigwa mtawalia, na kufuatiwa na risasi moja iliyobutuliwa juu, halafu ikasikika mseleleko mkali wa gari lenye kwenda kwa mchepuo wa kasi. Akajua mambo yameshaenda segemnege huko nje. Akafanya haraka kuchukua ile karatasi aliyopewa na kukimbilia nje ya geti huku mkononi tayari kachomoa bastola yake.

"Muuza duka Soni ameuliwa kinyama kibandani kwake"
Mamia ya watu walikuwa wamekusanyika karibia na kiduka cha Soni, huku giza lilikuwa tayari limeanza kushitadi angani katika usiku huo mbichi. Kila mmoja akijiuliza kulikoni mpaka muuza duka Soni ameuliwa kikatili namna ile. Hali ya hewa ilishachafuka kifo cha Soni kilizua tenge tahanani eneo hilo jirani na Wizara ya Mambo ya Ndani.
Maiti ya Soni ilikuwa imelala chali, damu zinamtiririka huku matundu ya risasi yakionekana dhahiri shahiri kwenye paji lake la uso na shingoni.
"Mie nimeshuhudia kila hatua ya tukio hili, walikuja watu wawili kwenye gari rangi ya kijivu aina ya "Brevis", mtu mmoja mrefu amevaa koti la kujikinga na mvua na kofia akashuka akaenda mubashara kwenye kiduka. Sikumfuatilia nikajua ni mteja wake tu anahitaji vitu vya dukani. Baadae nikaona kama kuna furushi kalibeba tokea kule anakohifadhia marehemu Soni takataka zake akalirusha ndani ya gari. Nae akaingia ndani ya gari kwa kuharakisha, lakini hawakuliondoa gari. Halafu baada ya kupita kitambo kama cha dakika 10 akashuka mmoja akakaribia tena kama meta 3 akanyanyua bastola yake na kumfyatulia risasi mbili za kichwani, ikabidi nijifiche nyuma ya kabati la fundi viatu jirani pale. Mpigaji akakimbilia kwenye gari kwa haraka. Alivyoona tumeanza kujikusanya wakadhani tunataka kuwapiga kipopo, mmoja wao akapiga risasi moja hewani, kisha wakatimka na gari lao wakala matu kwa umahiri mkubwa. Wakaingilia hiyo barabara ya mtaa wa Ohio na gari lao na kutokomea kusikojulikana" alielezea tukio hilo kwa ufasaha mkubwa mmoja wa mashuhuda wa tukio hilo.
Kachero Manu alivyoona umati wa watu umejikusanya akaamua kuirudisha silaha yake kwenye ala yake, akasogea karibu na eneo la tukio. Alikuwa ni mmoja wa wale waliosikiliza kwa umakini kabisa maelezo ya yule shuhuda. Baada ya hapo akaisogelea maiti ya Soni, akaona tayari kashaaga dunia, ameshaelekea jongomeo zamani.
Akajiona ni mtu mwenye bahati ya mtende kuwahi kuzungumza nae Soni muda mchache kabla hajapoteza maisha yake na kupata maelezo yaliyompa mwangaza wa upelelezi wake. Akatumia fursa ya watu kushuhudia mwili wa marehemu kuzunguka kule nyuma ya kiduka kwenye matakataka kuangalia kama furushi la chizi "Maso Maso" lipo au ndio limebebwa na wauaji!. Alipopiga jicho, akaona hamna kitu limepotea. "Kumbe furushi la mwehu, ni dili kama dhahabu linasakwa kwa udi na uvumba" alijiwazia peke yake Kachero Manu huku anatabasamu. Alishaanza kuunganisha matukio mbalimbali yatakayofanikisha upelelezi wake na hatimaye kuwatia mbaroni wahusika wa matukio ya ugaidi uliotekelezwa kwenye jengo la Wizara ya Mambo ya Ndani, Ijumaa iliyopita.
Askari kanzu wakawa wameshafika na kuanza kutawanya watu huku wakizungushia uzio eneo la tukio. Kachero Manu akaona isiwe tabu akaanza kuondoka mdogo mdogo kwa miguu kurejea ofisini, kufungasha vitu vyake arejee nyumbani kwake, tayari kwa safari ya Dodoma kesho kutwa yake.
Alipanga kwenda kumuongezea nguvu Kachero Yasmine. Lakini tukio la kuuliwa kwa kijana Soni kulimpa msongo wa mawazo wa kutaka kufahamu "je kuna uhusiano kati ya mauaji ya Soni na msako wa walipuaji wa jengo la Wizara? "


Kachero Manu uso na uso na Kigogo wa Polisi anayetumia gari PT3001
Siku ya Jumatano saa 12:00 asubuhi na mapema, kibaridi cha asubuhi kinapuliza, Kachero Manu alikuwa yupo ndani ya ndege ya shirika la ATCL aina ya Bombadia akielekea Jijini Dodoma. Alikuwa anahudhuria taazia ya marehemu waliokufa kwa mabomu yaliyolipuka katika jengo la Wizara ya Mambo ya Ndani, Ijumaa iliyopita. Alikuwa ametinga usoni miwani yake nyeusi na suti ya rangi buluu bahari, huku chini akiwa amevalia viatu vyake vyeusi. Muda wote wa safari alijifanya ametingwa na kusoma magazeti lako ila ilikuwa zuga tu.
Kila wakati alikuwa anamkodolea macho kwa kuibia, mbaya wake kigogo wa gari tata v8 PT1003 analohisi ndio mhusika wa mauaji ya Soni. Anamshuku kuwa anahusika kwa sababu ndio mtu wa mwisho kumtafuta Soni kutwa nzima na magharibi yake tu kijana wa watu akauliwa.
Yule Afisa alionekana ni mtu mwenye wasiwasi kama koo la kuku anayetaka kutaga. Uso ulionyesha kuwa ni mtu ambaye kichwani mwake ana mlima mzito wa mawazo ameubeba. Waliposhuka tu kwenye ndege, Kachero Yasmine alishakuja tayari uwanja wa ndege kumlaki Bosi wake. "Habari za asubuhi Bosi wangu, pole na safari... " zilikuwa ni salamu za Kachero Yasmine kwa Kachero Manu. "Fuata gari lile haraka sana" badala ya kujibu salamu, Kachero Manu akawa anatoa maagizo kwa mwenzake ya kumfuatilia kigogo huyo wa polisi. Kachero Yasmine akatekeleza amri ile kwa vitendo kwa kuitoa gari yake kwa haraka akiifuta taksi iliyombeba kigogo yule.
Kachero Yasmine alimjua vizuri sana Bosi wake kuwa akiwa ametingwa na jambo kuongea kwake ni tabu hata kula yake ni kwa manati. Baada ya dakika chache wakawa wapo nyuma yake mara walipotoka tu nje ya geti la uwanja wa ndege. Taksi ile iliyokuwa inafuatwa na Kachero Yasmine ilikuwa inaelekea barabara ya Arusha kama inaelekea njia ya ilipo kambi ya jeshi ya JKT-Makutupora.
"Inaonyesha anaenda Hoteli ya nje ya Jiji nadhani" alivunja ukimya Kachero Yasmine kwa kumzungumzisha Kachero Manu huku amemtupia jicho akitegemea kumsikia Bosi wake akitia neno. "Nadhani anatafuta eneo lenye utulivu " alijibu Kachero Manu kimkato. Ghafla gari wanayoifuatilia ikawasha indiketa ya taa ya kulia kuonyesha anaingia Simba Hoteli.
Ilikuwa ni Hoteli nzuri na tulivu iliyopendezeshwa kwa marumaru nyeupe kwa nje. Pia kulikuwa na bango kubwa kwa nje limeandikwa Simba Hoteli huku kukiwa na picha ya mnyama simba. "Sasa mie niache na huyu mjuba bado kuna vitu navihitaji kutoka kwake kabla sijamkamata, wewe endelea na yako" alisema Kachero Manu. "Sawa usisahau kunipa mzigo toka furushi la mwehu uliloniahidi toka juzi kuniletea" alijibu Kachero Yasmine na kukumbushia akabidhiwe karatasi iliyochukuliwa kutoka kwenye zigo la "Maso Maso".
"Hii hapa tena nashukuru kwa kunikumbusha, nilishasahau" alijibu Kachero Manu, huku mkononi amekamatia bahasha ya rangi ya kaki akimkabidhi. Kachero Yasmine hakuwa na simile pale pale akaipokea na akaitatua bahasha ile ya kaki na kukutana kikaratasi kidogo kichakavu kina maandishi ya lugha ya kiarabu. Akaanza kukisoma kiratasi hicho chenye maandishi yafuatayo ;
???? ?? ??? ??? ?????? ????? ??????"
???? ??????? ???? ????? ????????
???? ??????? ???? ????? ???????
????? ?????? ??? ????? ?????
????? ????? ???? ??? ??
ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog