Search This Blog

Monday 27 March 2023

GARI LA KUKODI (2) - 1

 

IMEANDIKWA NA : BISHOP HILUKA

*******************************************

Simulizi : Gari La Kukodi (2)

Sehemu Ya Kwanza (1)



Mr. Oduya alichukua simu yake na kutafuta namba za Dk. Masanja, meneja mkuu wa hoteli ya Udzungwa Beach Resort na kupiga ili kupata uhakika. Majibu aliyopewa yalimfanya ajihisi kukanganyikiwa, akili yake ilijaribu kukataa kabisa kukubaliana na taarifa ile na kile alichokishuhudia kwenye katika nyaraka zile za ununuzi wa gari.


Alijitahidi kuwa makini zaidi na akiishirikisha akili yake kikamilifu katika kumletea taarifa za kuaminika, kwani mambo yale hayakuwa yanamwingia kichwani kabisa! Ni vipi Sammy ameendelea kujitokeza katika harakati zake za kuusaka urais wa Tanzania na kugeuka kuwa kitisho?


Aliinua uso wake na kutazama juu akionekana kuwaza mbali. Wakati huo Spoiler na Dulla Mcomoro walikuwa kimya kabisa wakimtazama kwa wasiwasi. Akiwa katika hali ile mara hisia mbaya zikamjia na hapo mapigo ya moyo wake yakaanza kwenda kasi isivyo kawaida, hasa alipowaza kuwa huwenda wapinzani wake kisiasa walikuwa na fununu fulani kuhusiana na lile gari na wangeweza kulitumia kummaliza.


SASA ENDELEA...


Akiwa amezama kwenye tafakuri ile, akili yake ikaenda mbele zaidi katika kuunda hoja kichwani. Akaanza kuwaorodhesha washindani wake wakuu wa kisiasa bila kujali vyama walivyotokea, akianzia na wapinzani wake wakuu ndani ya Chama Cha Ukombozi, Benard Tumbo, Dk. Hussein Abbas na Anuary Kamba. Kisha akawafikiria wa kutoka vyama vingine walioonekana kukubalika zaidi, Zingo Kabwela na Tindua Luis.


Alipomaliza akaanza kutathmini vizuri nguvu na hali ya mahusiano yake kisiasa na viongozi wa nchi ikiwemo wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama. Tathmini yake ikamweleza kuwa mahusiano ya nyanja zote baina yake na viongozi wa nchi na wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama bado yalikuwa mazuri ingawa kulikuwa na misuguano ya kawaida ya hapa na pale kati yake na baadhi ya viongozi hao kutokana na tofauti za kimitazamo.


Alipotafakari kwa kina juu ya misuguano hiyo akajaribu kuwaza kama kulikuwepo mmojawapo wa wapinzani wake kisiasa au kiongozi ambaye angeweza kuwa na ukaribu na Sammy, bado haikuweza kumridhisha kuwa hata kama kusingekuwa na yeyote kati yao mwenye ukaribu na Sammy bado isingeweza kuwa sababu toshelevu ya kumfanya asichukue tahadhari.


Baada ya kimya cha kitambo fulani Mr. Oduya aliinua uso wake uliosawajika na kumtazama Spoiler. “Unamfahamu Samuel John Kambona?” alumuuliza kwa sauti tulivu.


“Sina hakika, lakini nadhani ni yule bwege aliyekuwa anafanya kazi hoteli ya Udzungwa Beach Resort,” Spoiler alisema baada ya kitambo kifupi cha kuvuta kumbukumbu. Mr. Oduya alibetua kichwa chake kukubali.


“Bado ni kizungumkuti kwani sina hakika kama hadi wakati huu hakuna yeyote kati ya wapinzani wangu kisiasa anayefahamu kuhusu hilo gari. Nimeshtuka sana kuona kuwa ni Sammy huyu huyu ndiye mmiliki wa gari ambalo siku zote nilidhani lilishateketezwa. Kwa kweli hizi ni taarifa za kustaajabisha na kuogofya sana,” Mr. Oduya alisema katika hali ya kukanganyikiwa huku taratibu akiviminyaminya vidole vyake vya mikononi katika hali ya kuupisha utulivu kichwani mwamke.


Kilipita tena kitambo fulani cha ukimya kila mmoja akijaribu kutafakari, kisha Mr. Oduya alishtuka akionekana kukumbuka jambo.


“Katika kufuatilia taarifa hizi mmehakikisha hamjaacha kielelezo?” Mr. Oduya alimuuliza Spoiler huku akimkazia macho.


“Hapana, hatujaacha kitu, tulichukua tahadhari zote, tulihakikisha tumebadili muonekano wetu, tukitumia gari lenye namba bandia na kuvaa glavu laini mikononi ambazo haikuwa rahisi mtu kutushtukia,” Spoiler alisema kwa uhakika.


“Silas, usichukulie kirahisi hivyo, kumbukeni kuwa hii ni vita. Mkifanya chochote hakikisheni hamuachi kitu tusije tukavuruga na kujipa kesi nyingine. Sawa?”


“Usijali, mkuu,” Spoiler na Dulla Mcomoro wakasema kwa pamoja.


“Okay, sasa mna kazi nyingine. Hakikisheni usiku huu huu huyu mtu anayeitwa Samuel John Kambona anapatikana kisha mpelekeni kwenye nyumba ya Kinondoni Makaburini na gari lake liteketezwe kabisa. Amenitafuta muda mrefu na sasa amenipata, I think he derseves to die,” Mr. Oduya alisema kwa sauti ya kitetemeshi kutokana na ghadhabu aliyokuwa nayo.


Spoiler na Dulla Mcomoro walikubali kwa kubetua kichwa, kisha wakanyanyuka na kuanza kuondoka wakifahamu kuwa kauli ile iliashiria kuwa maongezi kati yao mle ndani na Mr. Oduya yalikuwa yamefika tamati. Spoiler ndiye alikuwa wa kwanza kusimama sekunde chache kabla Dulla Mcomoro hajafanya hivyo.


“Tambueni kuwa nimewapa jukumu hili kwa sababu bado nawaamini sana, hivyo hakikisheni hamfanyi makosa,” Mr. Oduya aliongea kwa sauti tulivu ya kusihi na katika sauti yake kulikuwa na hali ya hofu iliyokuwa imejificha nafsini mwake. Alilazimisha tabasamu usoni mwake ingawa tabasamu hilo lilikataa kabisa kuumbika.


Spoiler na Dulla Mcomoro walibetua vichwa huku wakisimama kwa ukakamavu kama wanajeshi kisha wakaanza kuzitupa hatua zao taratibu kuondoka kwenye ofisi ile na kuufikia mlango, Spoiler aliufungua huku akiwa na hakika kuwa macho ya Mr. Oduya yalikuwa nyuma yao yakiwasindikiza.


Alipoufungua ule mlango akageuka na kumtazama tena Mr. Oduya aliyekuwa ameketi kwa utulivu kwenye kiti chake, alichokiona usoni kwa Mr. Oduya lilikuwa ni tabasamu lililohanikiza kila aina ya unyama. Bila kupoteza muda Spoiler akamtupia tabasamu la kuonesha kuwa alikuwa tayari kwa lolote, kisha wakatoka nje ya ofisi ile na kufunga mlango.


* * * * *


Saa mbili kasorobo usiku nyumbani kwa Sammy, Winifrida alikuwa anakatakata nyanya za kachumbari huku akimtupia jicho la wizi Joyce, ambaye muda huo alikuwa kafungua milango ya jokofu kubwa lililokuwa katika ukumbi wa chakula ila alionekana kuzama kwenye lindi la mawazo wala asichukue kitu alichokusudia.


Joyce alikuwa amesimama huku aking’ong’ona kucha zake, alikuwa amezama katika lindi la mawazo yaliyomfanya kuiona dunia yote ikiwa imemwelemea na kumkalia kichwani. Alijaribu kuwaza hili na lile katika namna ya kutafuta ni jinsi gani angeweza kuirejesha faraja na furaha iliyotoweka ghafla kwenye ndoa yake.


Donge la uchungu lilikuwa limemkaba kooni, alishindwa kuuzuia uchungu aliouhisi ukipenya moyoni mwake kutokana na mzozo uliokuwa umezuka kati yake na Sammy mchana wa siku ile. Tangu Sammy aliporudi nyumbani saa tano na ushee asubuhi hadi alipoondoka saa kumi na mbili jioni hawakuwa katika hali ya maelewano.


Siku nzima Sammy alikuwa akimpiga vijembe Joyce. Joyce hakuamini, alizoea utani wa mumewe lakini kila alipomtazama machoni hakuona dalili yoyote ya utani. Hakutaka kuamini kuwa ingetokea siku mumewe angemkasirikia kiasi kile. Ilifikia hatua alijiuliza kama yote hayo yalitokana na yeye kumweleza ukweli kuhusu kilichojitokeza kati yake na mwanamuziki Dynamo Plus au kulikuwa na jambo jingine lililojificha katikati.


“Nimekukosea nini kiasi hicho, mume wangu? Nilidhani yameisha kumbe bado unayo moyoni. Kwa hiyo uungwana wangu niliokuonesha kwa kukueleza ukweli ndiyo umeamua kuutumia kuniumiza?” Joyce alimuuliza Sammy kwa uchungu baada ya kuona hali ikizidi kuwa mbaya.


Sammy hakumjibu, alimtazama kama kinyago tu. Joyce alikuna kichwa aanzie wapi kusawazisha mambo. Hakuamini kama ile hasira ya mumewe ilikuwa imekuja ghafla tu. Bila shaka ilifugwa kwa muda mrefu na sasa ilikuwa imekomaa vya kutosha. Ilisubiri tu ipate mwanya ianze kujitawala badala ya kufugwa tu. Mwanya umeshapatikana, hasira imetoka na inaonesha makucha.


Joyce aliwaza kuwa hakupaswa kupuuzia, alitakiwa atafute njia ya kuidhibiti, aiangamize na kuitowesha kabisa kungali bado mapema. Kwa vipi sasa?


Muda huo Sammy alikuwa amekaa juu ya sofa, Joyce naye alikaa kwenye sofa lile lile ila hawakukaribiana. Kwa kitambo kirefu kimya kilitawala kati yao ingawa hali haikuwa tulivu katika vichwa vyao. Joyce alikohoa kidogo kutakasa koo lake kisha akaanza, “Mume wangu, naomba…” alisita baada ya kumwona Sammy akiinuka na kuondoka.


Kilikuwa kitendo cha dharau sana, Sammy alipotoka aliwasha gari lake na kuondoka zake bila hata kuaga alikuwa akienda wapi na hakuwa amerejea hadi muda ule, hivyo kichwa cha Joyce kilionekana kuzidiwa na uzito usiosemeka wa mawazo. Ni yeye tu labda na Mungu wake ndiye aliyejua kilichokuwa kikipita akilini mwake muda huo.


Mawazo juu ya mustakabali wa ndoa yao. Mawazo juu ya taaluma yake ya ubunifu wa mavazi na ndoto yake ya kutaka kuwa mbunifu bora barani Afrika. Mawazo juu ya wasiwasi wa kumpoteza mwanamume ampendaye, mwanamume wa aina na kariba yake ambaye ndiye chaguo la moyo wake. Mawazo juu ya… ah! Mambo yalikuwa mengi kichwani kiasi kwamba alijihisi kutaka kuchanganyikiwa.


Siku hiyo ilikuwa ndefu sana kwa Joyce kuliko kawaida, hadi muda ule hakuwa ameweka chochote tumboni na wala hakuhisi njaa kabisa. Ingawa amewahi kuwa na misuguano ya hapa na pale na Sammy lakini ilikuwa ya kawaida na mara nyingi iliisha kwa mazungumzo tu. Lakini lile lilikuwa jambo geni kabisa! Kwa miaka takriban nane waliyoishi hapakuwa na hata siku moja ya namna hiyo… Hata moja!


“Wifi, naona leo hauko sawa! Kwani kuna nini?” sauti ya Winifrida ilimzindua Joyce kutoka kwenye lindi la mawazo, alimtazama Winifrida kwa kitambo kidogo bila kusema neno, kisha akatabasamu kwa mbali na kushusha pumzi. Akanyanyua mabega yake juu na kuyashusha halafu akageuka tena, akafunga taratibu milango ya jokofu.


* * * * *


Kwenye jumba moja la kifahari la ghorofa moja lililojengwa katika eneo la Kinondoni Makaburini, Spoiler na Dulla Mcomoro walikuwa wanajiandaa ili kwenda kuifanya kazi waliyoagizwa na Mr. Oduya. Walikuwa wamefika hapo kujiandaa baada ya kutoka ofisini kwa Mr. Oduya.


Lilikuwa jumba la vyumba vitano vya kulala vilivyosheheni samani zote muhimu, sebule mbili kubwa chini na juu, ukumbi wa chakula, ofisi na maktaba ya siri, na chumba cha siri cha mateso. Hata hivyo, jumba lile lilikuwa halikaliwi na mtu yeyote, Mr. Oduya na watu wake waalifika kwenye jumba hilo pale walipokuwa na mission maalumu.


Spoiler aliandaa nguo maalumu na vifaa vya kazi. Nguo nyeusi, buti na barakoa. Akachukua bastola moja aina ya FNX 45 Tactical yenye kiwambo cha kuzuia sauti na kumpatia Dulla Mcomoro, kisha akachukua visu viwili vikubwa, kimoja akakiweka kwenye nyonga na kingine nyuma ya mguu kikifunikwa na suruali.


Alipomaliza alichukua chupa ya kemikali aina ya Chloroform inayotumika kumlegeza au kumzimisha mtu kiasi kwamba kushindwa kujitambua na kuhisi chochote na wahalifu wakafanya chochote wanachoweza kwa muda wa kutosha. Aliitazama kwa kitambo na kumpa Dulla Mcomoro ambaye aliitazama na kuachia tabasamu kisha akaiweka kwenye begi lake dogo aliloliweka mgongoni.


Walipoona kila kitu kipo sawa Spoiler alitoa simu na kupiga namba fulani, akaongea na mtu mmoja na kutoa maagizo kisha akakata simu na kumpa ishara Dulla Mcomoro amfuate. Walitoka na kujipaki kwenye pikipiki aina ya Boxer BM 150 na kuanza safari ya kuelekea kwenye mission yao.


* * * * *


Saa mbili na nusu usiku, katika mgahawa wa kisasa wa ELLI’S kulikuwa na pilikapilika za aina yake za kujistarehesha. Ndani ya ukumbi mkubwa wa chakula na vinywaji wa mgahawa ule wa kisasa sauti ya muziki laini wa taratibu ilikuwa ikisikika kutoka katika spika zilizokuwa sehemu fulani na kuzikonga nyoyo za watu waliofika kwa ajili ya chakula na vinywaji usiku ule.


Hakika usiku wa mjini haukuujua usiku kwa kuwa ulikuwa umejaa kila aina ya starehe na anasa. Giza lililozoeleka kutawala usiku maeneo ya vijijini na miji midogo halikuwa na nguvu wala uwezo katika maeneo ya starehe yasiyo na idadi jijini Dar es Salaam. Nuru za rangi mbalimbali toka katika majumba na taa za barabarani zilikuwa zikilidhihaki giza hilo kiasi cha kuufanya usiku kuwa mchana wa aina yake.


Katika ukumbi ule mkubwa wa chakula wa mgahawa wa kisasa wa ELLI’S, mwanadada Tunu alikuwa ameketi kwa utulivu kwenye kiti kifupi chenye foronya laini. Aliketi kwenye meza moja iliyokuwa imejitenga kwenye kona moja ya ukumbi ule akiwa mtulivu sana, mbele yake kulikuwa na chupa kubwa na bilauri ya mvinyo mwekundu aina ya Dodoma Wine na alikuwa akizungusha kidole chake cha shahada kwenye ile bilauri huku akitafakari na kuzungusha macho yake kuwachunguza watu walioketi mle ukumbini.


- (83)


Alikuwa anakunywa taratibu akishushia baada ya mlo mtamu aliomaliza kula muda mfupi kabla. Aliitazama saa yake na kugundua kuwa zilikuwa zimepita takriban dakika arobaini tangu alipoketi mle ukumbini, aliyekuwa amemfuata bado hajamtia machoni. Je, amedanganywa? Hapana, hawezi kuwa amekosea!


Wakati alipoingia katika mgahawa ule alikumbuka kuulizia na akahakikishia kuwa mtu aliyekuwa akimtafuta alikuwepo pale jioni hiyo na alitoka muda mfupi kabla yeye hajaingia na angerudi kwa kuwa kuna mizigo yake aliiacha na kuahidi kuifuata. Hivyo, Tunu hakuwa na shaka yoyote kuwa mtu huyo angerejea.


Hadi wakati ule alikuwa bado amevaa gauni la kitenge cha wax lililoshonwa kwa mtindo wa ‘Ankara midi tube dress’ likiishia juu kidogo ya magoti yake, likaushika vyema mwili wake na kulichora umbo lake maridhawa na viatu vyenye vikanyagio virefu vya mchuchumio. Miwani yake myeusi ya jua alikuwa ameiweka juu ya kichwa chake na mkoba wake mzuri wa kike ulikuwa juu ya meza.


Akiwa ameketi kwenye ile meza aliwatazama wateja wengine waliokuwa wameketi katika meza mbalimbali, kila mmoja alikuwa katika hali ya utulivu kama ambaye hakuwa na wasiwasi wowote duniani. Katika uchunguzi wake macho yake yalianza kutua kwenye meza moja mbele yake iliyokuwa na watu watatu, mwanamume mmoja wa kizungu aliyeonekana kubabaishwa na wasichana wawili wa Kibantu.


Wasichana wale walikuwa warembo kwelikweli wenye mavazi ya kileo yaliyowabana na kuonesha maungo yao yalivyoumbika, meza yao ilikuwa imechafuka kwa nyama choma na vinywaji vya bei mbaya, wao wakitoa oda kwa mhudumu na mzungu analipa. Walikuwa wanamchezea mapaja, kifua na kidevu kwa mahaba na yeye alikuwa anacheka, anaridhika.


Macho ya Tunu yakaiacha meza ile na kuhamia kwa watu wawili waliokuwa wameketi kwenye meza ya tatu tu kutoka pale alipoketi, kulikuwa na wanaume wawili walioonekana kumwangalia Tunu kwa matamanio. Wanaume hao walikuwa na umri wa kati ya miaka 35 na 40 na walikuwa wanakunywa pombe kali aina ya Grant’s Blended Scotch Whisky, muda wote walikuwa wanamchombeza Tunu kwa maneno haya na yale lakini hakuonekana kuwajali.


Mmoja alikuwa mfupi kiumbo lakini mkakamavu akiwa na mwili uliojengeka kwa mazoezi na sura yake ilionesha unyenyekevu mkubwa. Alivalia fulana nyeusi iliyombana na kulionesha vyema umbo lake lililojengeka kwa misuli na suruali nyeusi ya jeans, miguuni alivaa buti ngumu za ngozi. Alijulika kwa jina la Bob Chopa na hakuna aliyelijua jina lake halisi.


Mwanamume wa pili alikuwa mrefu aliyepanda hewani kisawasawa na mwenye mwili ulioshiba, alikuwa mweupe kiasi na kichwa chake kilikuwa kinang’ara kwa upara mpana, uso wake ulikuwa mpana na macho yake yalikuwa makubwa. Alivaa suti maridadi ya kijivu na viatu vyeusi vya ngozi.


Aliyaondoa macho yake kutoka kwa wale wanaume na kuyatembeza kuwaangalia watu wengine. Meza nyingine zilikuwa na watu ambao hawakumshawishi sana kuwatazama. Hakupata taabu kugundua kuwa waliokuwa wameketi katika meza hizo ni mtu na mkewe. Wengine wachumba na wale ni mtu na mchepuko wake mpya, kwa jinsi walivyokuwa wamekaa.


Meza mbili tatu zilikuwa zimekaliwa na wafanyabiashara wakubwa na viongozi wa kiserikali, wengine walionekana wazi kuwa ni mafisadi au wapiga dili na hapo walikuwa wanapanga harakati zao kwa sauti ya mnong’ono.


Kisha macho ya Tunu yakaangukia kwenye meza moja iliyokuwa jirani na mlango wa kuelekea maliwato, ambapo alikuwa ameketi mwanadada mmoja, peke yake kama yeye, alikuwa akinywa bia aina ya Heineken taratibu bila haraka. Tunu alishindwa kuyaondosha macho yake kutoka kwa yule mrembo, hakukumbuka ni wapi na lini aliwahi kumwona.


Alikuwa mrefu, mpana na alivaa sketi fupi nyeusi yenye miraba myeupe, blauzi nyeupe ya mikono mirefu na viatu vya flati. Mkononi alikuwa amevaa saa ghali ya kike na alipakata mkoba mzuri wa nguo ya pundamilia uliomgharimu fedha nyingi. Alionekana mtulivu sana akisubiri kitu au mtu muhimu sana, kwani mara kwa mara alikuwa akiitupia jicho saa yake ya mkononi na kukunja sura yake.


Kwa taabu sana Tunu aliyaondosha macho yake toka kumtazama yule mwanadada na kumgeukia mhudumu mmoja aliyekuwa anapita jirani na meza yake, akamwita, “Samahani, anti…”


Yule mhudumu alisimama na kumsogelea Tunu huku akimtazama kwa makini.


“Hivi, yule bwana anayeendesha lile gari la kizamani aina ya Cadillac DeVille atarudi kweli, maana nilikuwa nahitaji huduma yake lakini nashangaa hadi sasa sijamwona!” Tunu alimuuliza yule mhudumu huku akipitisha ulimi wake kulamba midomo yake.


“Sina uhakika, kwani huna namba yake ya simu umpigie?” yule mhudumu aliuliza huku akiyatupa macho yake kutazama kwenye meza aliyoketi mzungu na wanawake wawili wa kibantu waliokuwa wakimwita.


“Ningekuwa nayo wala nisingehangaika kukuuliza,” Tunu aliuliza ma kuminya midomo yake.


“Basi endelea kusubiri, maana subira yavuta heri,” yule mhudumu alisema na kuanza kupiga hatua kwenda kwenye ile meza alikoitwa. Tunu alishusha pumzi na kujiegemeza kwenye kiti chake na kuyatupa tena macho yake kwa yule mwanadada aliyeketi peke yake ambaye hakulijua jina lake.


Alimwona akiinamisha kichwa chake kama aliyeona kitu katika bilauri yake ya bia, alitazama ndani ya ile bilauri kwa kitambo kisha aliinua uso wake taratibu kwa madaha kana kwamba alikuwa anaigiza filamu, mara macho yao yakakutana. Kwa dakika nzima macho yao yalitulia yakitizamana kama ambao walikuwa wakisomana fikra zao, kisha yule mwanadada aliyahamisha macho yake na kutazama kando.


Mambo yanazidi kunoga ndani ya Bandari Salama, ingawa jiji hili si salama kama lilivyo jina lake. Nani ni nani katika jiji hili? Na nani anajua nani anafanya nini? Endelea kuifuatilia stori hii ya kusisimu ambayo kisa chake hakijapata kusimuliwa ili ujue hatma yake...

(84)


Muda huo huo simu yake ya mkononi ikaanza kuita, ilikuwa ni simu ghali ya kisasa aina ya Samsung Galaxy Fold. Yule msichana aliitazama kwa kitambo akionekana kama aliyekuwa akijishauri iwapo aipokee au aipotezee, akabana taya zake na kuipokea kisha akaipeleka moja kwa moja sikioni.


Alionekana kuwa mtulivu sana alipokuwa akiongea na simu, muda wote alipokuwa akiongea alikuwa akimtupia Tunu jicho la wizi na baada ya mazungumzo ya takriban dakika mbili alikata simu na kushusha pumzi za ndani kwa ndani.


Sasa alionekana kuanza kukosa uvumilivu, aliitazama tena saa yake na kukunja sura yake kisha akachukua chupa ya bia iliyokuwa juu ya meza na kumimina bia katika bilauri, bilauri ilijaa na bia kuanza kumwagika juu ya meza hali akiwa hana habari, alikuwa amezama kwenye lindo la mawazo.


Aliposhtuka bia ile ilikuwa imemlowesha kwenye sketi yake, akashtuka na kuruka huku akijaribu kuyaepuka macho ya watu yaliyokuwa yakimtazama kwa mshangao, alichukua tishu na kujifuta huku akisonya. Muda huo huo mhudumu alifika kwenye meza yake na kufuta meza huku akimpa pole.


Baada ya mhudumu kuondoka yule msichana alinyanyua bilauri yake na kuigida bia yote iliyokuwemo katika bilauri hiyo kisha akaikita ile bilauri juu ya meza na kunyanyuka, huku akimtazama Tunu kwa jicho la wizi akachukua simu yake na kuelekea maliwato.


Tunu alikuwa ametulia tuli akinywa mvinyo wake taratibu huku akijifanya kutoona kilichokuwa kikiendelea kwa yule msichana, alihisi kuwepo kwa jambo lisilo la kawaida na kujikuta akitamani kufuatilia ili ajue lakini hakufanya hivyo kwa kuhofia kuchanganya mambo, kwani hakuwepo pale kwa jambo jingine lolote isipokuwa lile lililompeleka hapo.


* * * * *


Saa tatu na ushee usiku, Joyce alikuwa kasimama barazani akionekana kutokuwa katika hali nzuri japo alijitahidi kuwa mtulivu sana. Alikuwa amevaa vazi la kulalia, kiunoni kajifunga khanga na kiganja cha mkono wake wa kushoto kakitumbukiza ndani ya khanga kwa mbele. Mkono wa kulia ulikuwa ameshika simu yake akiigongagonga kwenye shavu lake la kulia. Alionekana yuko mbali sana kimawazo.


Mtoto wake Pendo hakuwa amelala hadi muda huo, alikuwa amesimama kando yake akiwa ameng'ang'ania khanga ya mama yake. Joyce hakuonekana kumjali bali akili yake ilikuwa mbali, nje kabisa ya mahala pale aliposimama.


Joyce aliitazama ile simu aliyoishika, akashusha pumzi na kutafuta namba ya Sammy, akabofya ili kupiga lakini ghafla akaonekana kughairi na kuikata. Muda huo huo akasikia mvumo wa gari lililokuwa likisogea eneo lile. Joyce akatega vyema sikio lake kwa makini akijaribu kubaini sauti ya mvumo ule.


Gari lilipofika usawa wa nyumba yao likaongeza mwendo na kupitiliza na kumfanya Joyce aume meno yake kisha akayaachia, aliganda pale pale asijue la kufanya. Mara mvumo mwingine wa gari ukasikika tena ukisogea eneo lile na kupita. Joyce aliuma tena meno yake huku machozi yakimlengalenga.


Alishusha pumzi na kumtupia jicho Pendo aliyekuwa bado kamng’ang’ania khanga yake huku akimwangalia usoni kwa udadisi bila kusema jambo. Joyce alimtazama Pendo na kushtuka, akaufunika uso wake kwa khanga kujifuta machozi. Kisha aligeuka na kuingia sebuleni.


Hapo sebuleni alisimama karibu na kabati la vyombo. Pendo naye alimfuata kila aendako, pia alisimama huku akiendelea kumwangalia mama yake usoni kwa udadisi. Alikwisha hisi kuwepo kwa jambo lisilo la kawaida lakini hakuthubutu kuuliza.


Joyce alionekana kuzidiwa na mawazo, bila kufikiri akipiga ngumi ukutani kwa nguvu na kumshtua sana Pendo aliyemtazama mama yake kwa hofu. Joyce alishindwa kuvumilia, alichuchumaa pale alipokuwa amesimama, akajiegemeza na ukuta na kuanza kulia kimya kimya kwa uchungu huku uso akiwa kaufutika kwenye khanga aliyojifunga. Pendo alisogea pambeni kwa hofu.


Muda huo huo Winifrida alitokea sebuleni akiwa na uso wa mshangao, hofu na udadisi. Aliangaza macho yake na kumwona Joyce akiwa kajikunyata ukutani huku akilia kilo cha kwikwi. Winifrida alimtazama kwa wasiwasi na macho yake yakahamia kumtazama Pendo ambaye alikuwa amesimama kando akiwa ameduwaa, alikuwa anamshangaa mama yake huku machozi yakimlengalenga machoni.


Winifrida alifyatuka haraka toka pale alipokuwa amesimama na kumfuata Pendo, alimshika na kumnyanyua kisha akaelekea naye chumbani huku akimtuliza na kumwacha Joyce bado kajikunyata akilia kwa uchungu.


* * * * *


Tunu aliitazama saa yake kwa mara ya mia moja, dakika nyingine therathini na tano zilikuwa zimepita, zaidi ya muda aliokuwa ameukadiria. Alishusha pumzi za ndani kwa ndani na kunyanyua bilauri iliyokuwa na mvinyo, akapiga funda kubwa na kuunywa mvinyo wote uliokuwemo.


Uso wake ulionesha wasiwasi, alishusha pumzi na kumtupia jicho yule mwanadada aliyekuwa ameketi peke yake akinywa bia taratibu, akamwona sasa akiwa ameketi na mtu mwingine, mwanamume ambaye kwa mtazamo tu alionekana kunuka fedha. Uso wake ulikuwa umetulia akionekana hana wasiwasi na anacho kila kitu ambacho angeweza kukihitaji duniani.


Tunu hakutaka kuendelea kukaa hapo huku akiwa hajui mtu aliyekuwa akimsubiri angefika saa ngapi, alitaka kunyanyuka lakini akasita baada ya kumwona mwanamume mmoja mrefu na mweupe mithili ya chotara wa kizungu akiingia ndani ya ukumbi. Mwanamume huyo mwenye sura ya tabasamu muda wote alikuwa anatembea kwa madaha huku akizungusha macho yake kutazama watu walioketi mle ukumbini. Mkononi alikuwa ameshika funguo za gari lake akizungusha kwenye kidole chake cha shahada.


(85)


Mwanamume yule alikuwa amevaa suti ghali ya kijivu ya single button, brandi ya Piacenza kutoka nchini Italia, shati jeusi la mikono mirefu lenye kola ndogo, brandi ya Maria Santangelo kutoka Italia na viatu vyeusi vya ngozi halisi ya mamba.


Baadhi ya watu waliokuwa wameketi ndani ya ukumbi ule na wahudumu wa ule mgahawa walionekana kumchangamkia sana wakati akiwapita kiasi cha kumfanya Tunu ahisi labda alikuwa mtu mkubwa au mmiliki wa ule mgahawa. Alimtazama kwa makini huku akijaribu kuwaza, alihisi kumwona sehemu, si tu kwamba alimwona sehemu bali walionana.


Mwanamume yule ni Sammy na wakati akipiga hatua zake alionekana kusita kidogo baada ya kumwona Tunu, aliyatuliza macho yake kwenye uso wa Tunu huku akijaribu kuvuta kumbukumbu. Wakaangaliana kama waliokuwa wanasomana mawazo yao. Tunu akamkubuka na kuachia tabasamu. Alikumbuka kuwa alimwona kule Mzizima TV, walipishana mlangoni wakati akitoka na yeye Tunu akiingia. Bila shaka ndiye mmiliki wa lile gari la kizamani aina ya Cadillac DeVille.


Kwa upande wake, Sammy alijikuta akikihisi msisimko wa ajabu ambao hajawahi kuuhisi kwa mwanamke mwingine zaidi ya mkewe tangu alipofunga ndoa, msisimko ulikuwa ukimtambaa mwilini mwake na kuzifanya nywele zake kumsimama. Alishusha pumzi ndefu kama bata dume huku akiwa ameduwaa asipate cha kusema. Alianza kujishangaa, kwani alijikuta akibabaika kidogo kwa uzuri wa mwanadada yule kiasi kwamba moyo wake uliraruka kwa shauku ya kutaka kuongea naye.


Bila kujua alijikuta akipiga hatua kuelekea kwenye meza ya Tunu, akaketi huku akiendelea kuyatuliza macho yake kwenye uso wa Tunu, aliweka funguo za gari lake juu ya meza huku jicho lake likiwa halitoki kwenye uso wa Tunu. Alijikuta akimkodolea macho huku akiyasanifu mengi ya huba mbele ya hua aliyejitanashati kikweli kweli mbele ya macho yake!


Akiwa mbele yake alianza kujiuliza, mwanadada huyo ni nani na amewahi kumwona wapi! Kwenye televisheni? Kama ndiyo, je, ni mwigizaji? Mwanamuziki? Mwanamitindo? Hakupata jibu ingawa jambo moja ni kwamba alijua kuwa angeweza kuwa yeyote katika sanaa zote za maonesho, filamu ikitangulia.


Tunu aliuona mduwao katika uso wa Sammy. Yeye pia alikuwa na mshangao wake, hakutegemea kama mtu aliyemfanya kufunga safari kutoka mbali, kilometa zaidi ya elfu moja, kumfuata kisha akapata kibarua cha kusubiri kwa zaidi ya saa nne pasipo kuwa na uhakika wa kuongea naye, eti angeweza kujileta mwenyewe kwenye meza yake! Lakini, mbona kama wamewahi kukutana sehemu nyingine kabla ya siku hiyo? Walikutana wapi na lini? Walikuwa wanafanya nini?


“Gift!” Sammy aliita kwa sauti iliyoonesha wazi kuwa hakuwa na uhakika huku akiendelea kumkazia macho Tunu kwa makini, “Your name is Gift, right?” Sammy aliuliza kwa sauti iliyoonesha mshangao mkubwa.


Kwa sekunde chache Tunu alibaki amemkodolea macho Sammy akiwa hajui aseme nini, hakuweza kabisa kumjibu bali alimtazama kwa makini. Hakujua alilipata wapi jina hilo. Ni jina hilo ndilo lililomfanya aduwae kwani japo halikuwa jina lake halisi lakini kuna mtu mmoja tu alipenda kumwita hivyo. Alikuwa mwanamume wake wa kwanza ‘aliyemwondolea utoto’ wake na kumwingiza katika dunia ya wakubwa. Mwanamume yule alikuwa amelitafsiri jina la Tunu kwa Kiingereza akimwita ‘Gift’ kumaanisha tunu au zawadi.


Tunu akajiuliza, mwanamume huyu aliyeketi mbele yake alikuwa amelijuaje jina hilo? Alijaribu kuvuta kumbukumbu…


“Siwezi kuwa nimekufananisha! Pengine sikuwahi kuwa mtu muhimu kwako! Sikuwa kitu kwako, ndiyo maana ukaamua kutupa jongoo na mti wake!” Sammy alisema baada ya kuona Tunu akiwa bado anamtazama bila kusema neno lolote.


“Oh my God, Sammy!” Tunu alimaka kwa mshangao mkubwa baada ya kumkumbuka, alimtumbulia Sammy macho kwa mshangao na kushusha pumzi za ndani kwa ndani.


* * * * *


Takriban mita hamsini toka nyumba aliyokuwa akiishi Sammy, pikipiki lililowachukua Spoiler na Dulla Mcomoro lilisimama, hawakuwa na haraka, walibaki juu ya pikipiki na kusoma kwanza mazingira. Spoiler alizima taa za pikipiki na hata pikipiki yenyewe kisha wakaendelea kukaa hapo kwa takriban dakika tano hivi.


Kisha Spoiler akaiwasha tena pikipiki na kuiondoa taratibu akiivuka ile nyumba ya Sammy huku wakiichunguza kwa makini, wakazunguka na kutokea mtaa wa nyuma na kuiegesha pikipiki kwenye kichochoro kimoja cha nyumba jirani, si mbali sana kutoka nyumba ile ya Sammy.


Kwa tahadhari kuwa Spoiler na Dulla wakajongea hadi kwenye nyumba ya Sammy, Spoiler akadanda juu ya ukuta uliozungushwa katika ile nyumba na kuchungulia ndani, hakuona mtu. Kwa haraka akarukia ndani ya fensi ya ile nyumba na kutua bila kishindo kama paka.Alisimama pale kwa muda akihakikisha usalama, kisha akampa ishara Dulla aingie na kumwelekeza aelekee upande mwingine wa nyumba kulikokuwa na karo la kuhifadhi maji taka.


Spoiler akaelekea kwenye mlango wa jikoni uliounganishwa na dirisha la kioo na kukomea hapo, kisha akachungulia ndani, kulikuwa na mwanga hafifu uliokuwa unatokea kwenye korido na sebuleni, dirisha lilikuwa limefunikwa na pazia jepesi kwa ndani lakini kupitia uwazi mdogo pembeni ya dirisha lile Spoiler aliweza kuona ndani. Alitazama kwa makini, hakuona dalili ya kuwepo mtu eneo lile.


Alijaribu kukisukuma kile kioo cha dirisha upande mmoja lakini hakufanikiwa kwani kilikuwa kimefungwa kwa ndani na komeo. Akalivua begi lake na kutoa pini ndogo yenye kung’aa kama dhahabu, akaikunja kwa mikono yake iliyofunikwa na glavu halafu akaizamisha kwenye kitasa na kukorokochoa, mlango ukafunguka!



Akajitoma ndani kwa tahadhari huku akimpa ishara Dulla Mcomoro amlinde. Dula aliishika vyema bastola yake huku akiwa makini kumlinda Spoiler. Spoiler alitokea jikoni, akasimama kwa sekunde kadhaa akijaribu kuyatega masikio yake kusikiliza kama kungekuwa na sauti yoyote ambayo angeitilia shaka, hakusikia. Akaanza kutembea kwa tahadhari kuelekea kwenye korido pana ya kuelekea vyumbani.


Muda huo Dulla alikuwa ameingia jikoni na kubana kwenye ukuta akijaribu kuchunguza eneo lile kwa makini, akahisi kusikia sauti ya mtu upande wa sebuleni akishusha pumzi. Akachungulia na kumwona mwanamke mmoja akiwa amejiegemeza na ukuta sebuleni, amevaa vazi la kulalia na kiunoni alikuwa amejifunga khanga akiwa anatazama nje kupitia dirisha la sebuleni.


Dulla akainua kidole kimoja juu kumwashiria Spoiler aliyekuwa anataka kuelekea vyumbani kwamba kulikuwa na mtu mmoja.sebuleni.


Joyce alionekana kuwa na huzuni na machozi yalimlengalenga machoni. Alijaribu kuyazuia kwa kupepesa macho lakini yakadondoka. Akajifuta kwa viganja. Akiwa bado amesimama hapo mara akasikia sauti ya chombo kuanguka sakafuni, alisikiliza kwa makini na kugundua kuwa sauti ile ilitokea jikoni.


“Winnie! We Winnie kuna nini?” Joyce aliita kwa wasiwasi akidhani ni Winifrida alikuwa jikoni lakini kulikuwa kimya. Joyce akaamua kwenda jioni kuona kulikuwa na nini, alipokuwa hatua moja tu kutoka pale alipokuwa amebana Dulla akasita baada ya kuhisi kulikuwa na mtu kajificha. Moyo ulipiga kite baada ya kuona kivuli cha mtu aliyekuwa ameshika bastola mkononi akimwelekezea.


Joyce alitaka kupiga kelele lakini Spoiler aliyerudi haraka na kujificha nyuma yake akamuwahi na kumbana kisha akamvutia jikoni na kumbananisha na ukuta huku akimwekea kisu shingoni.


“Shhhhhh! Usijaribu kupiga kelele la sivyo tutakuua wewe na familia yako yote,” Spoiler alisema kwa sauti ya kunong’ona kwenye sikio la Joyce, Joyce aliogopa sana na kubaki akitetemeka.


“Sammy yupo wapi?” Spoiler alimuuliza Joyce kwa sauti ya chini huku akimkazia macho yaliyowaka kwa ghadhabu.


“Hajarudi bado,” Joyce alijibu huku jasho la woga likimtoka.


“Usinidanganye, naweza kukufanya kitu kibaya sana kama nitagundua kuwa umenidanganya,” Spoiler alimuuliza Joyce huku akizidi kumbana kwenye ukuta.


“Kweli hajarudi, siwezi kukudanganya,” Joyce alijitetea huku akikitazama kwa hofu kisu alichoshika Spoiler.


“Humu ndani mnaishi watu wangapi?” Spoiler alimuuliza Joyce huku akikipisha kisu chake kwenye shavu la Joyce katika namna ya kumwogofya.


“Wanne. Mimi, mume wangu na watoto wawili,” Joyce alisema kwa woga. Spoiler alimtazama machoni akayaamini maneno yake na kumtaka waelekee sebuleni, walipofika sebuleni wakamwamuru akae sakafuni huku Spoiler akimwekea kisu shingoni. Dulla alisimama kando, karibu na kabati la vyombo huku bastola yake ikimwelekea Joyce.


“Tafadhali naomba msiniue,” Joyce alisema kwa sauti ya kitetemeshi huku akiwa ameyatoa macho kwa woga.


Sauti yake ikapenya hadi kwenye chumba walichokuwa wamelala Winifrida na Pendo. Winifrida alifumbua macho yake na kusikiliza kwa makini huku akiyatupa macho yake dirishani. Hakuona kitu chochote cha kukitilia shaka. Akajiuliza ina maana alikuwa anaota? Hapana. Ile haikuwa ndoto kwani hakuwa amepitiwa usingizi japo alikuwa amelala kitandani.


Mara akakumbuka, kuna muda aliruhusu usingizi kumpitia na aliota ndoto ya kutatanisha iliyomfanya asipate tena usingizi. Katika ndoto hiyo aliota kwamba alikuwa analia, kilikuwa kilio cha msiba! Lakini hii haikuwa ndoto, alikuwa amemsikia wifi yake Joyce kwa masikio yake mawili. Je, ni nani alitaka kumuua Joyce? Sammy? Kwa nini amuue? Winifrida alijiuliza lakini akakosa jibu.


Alijiinua taratibu kutoka pale kitandani na kusimama huku akiwa na hofu, moyo wake ulikuwa unakwenda mbio isivyo kawaida. Akaanza kupiga hatua taratibu akisogea mlangoni kwa tahadhari kubwa huku akijaribu kuyatega masikio yake kama angeweza kusikia chochote. Mara akasikia sauti nzito ambayo hakuitambua, haikuwa sauti ya Sammy, ilikuwa sauti ngeni kabisa masikioni mwake, “Sema ukweli, Sammy kaenda wapi?”


“Mimi sijui, tangu alipoondoka hapa mchana sijui kaenda na wala hatujawasiliana,” Joyce alijibu kwa hofu.


Winifrida akashtuka sana na kujikunyata pale mlangoni kwa hofu, mara akaisikia tena ile sauti nzito ikisema, “Dee, cheki chumba kimoja kimoja na yeyote utakayemkuta huko mlete hapa.” Winifrida alihisi haja ndogo ikimtoka.


Dulla aliondoka haraka eneo lile na kuifuata korido pana iliyoelekea vyumbani, aliiona milango mitano, milango miwili ikiwa upande wa kulia na milango mingine mitatu upande wa kushoto. Dulla akaufuata mlango wa kwanza upande wa kulia na kugundua ulikuwa wa kuingia jikoni. Akauacha na kuufuata mlango wa pili.


Aliufikia na kukiminya kitasa cha mlango kisha akausukuma, mlango ukafunguka, chumba hakikuwa na mtu yeyote kwa kuwa kilikuwa chumba cha Sammy na mkewe Joyce. Akatoka na kuufuata mlango wa kwanza kushoto, kilikuwa chumba cha maliwato ya wote, mlango uliofuata pia hakukuwa na mtu yeyote, kilikuwa chumba cha wageni.


Sasa kilibaki chumba kimoja tu kilichokuwa mwisho upande ule wa kushoto ambacho aliamini kwamba kilikuwa chumba cha watoto. Dulla akafika na kushika kitasa cha mlango, akakiminya na kuusukuma lakini mlango ulikuwa umefungwa kwa funguo. Akakiminya kitasa kile mara tatu mfululizo na kukiachia, mlango ukafunguka.


Akaingia chumbani kwa tahadhari na kumkuta mtoto Pendo amelala. Dulla alisimama pale kwa kitambo akijaribu kujiuliza, mtoto mmoja, je, mwingine yuko wapi? Akahisi kuna jambo halikuwa sawa. Akaanza kupiga hatua taratibu huku akielekeza bastola yake pale kitandani, kisha akainama kuangalia uvunguni mwa kitanda, hakuona mtu. Akaguna na kugeuka kutazama kila sehemu, akaliona kabati la nguo la ukutani na kuachia tabasamu.


Akaanza kulisogelea lile kabati huku akielekeza bastola yake, kiza kilichokuwepo mle ndani hakikumzuia kuona kila kitu, alikuwa makini kusikiliza kila sauti aliyoitilia shaka, alizidi kulisogelea lile kabati kwa tahadhari, alipolifikia akafungua milango huku bastola ikiwa imeshikwa vyema mkononi ikiwa tayari kwa lolote. Hakuona mtu. Akachakura chakura nguo kuhakikisha lakini hakukuwa na mtu. Akatweta.




Akaanza kulisogelea lile kabati huku akielekeza bastola yake, kiza kilichokuwepo mle ndani hakikumzuia kuona kila kitu, alikuwa makini kusikiliza kila sauti aliyoitilia shaka, alizidi kulisogelea lile kabati kwa tahadhari, alipolifikia akafungua milango huku bastola ikiwa imeshikwa vyema mkononi ikiwa tayari kwa lolote. Hakuona mtu. Akachakura chakura nguo kuhakikisha lakini hakukuwa na mtu. Akatweta.


* * * * *


“Hivi, uliwezaje kunifanyia hivi? Labda sikuwa muhimu kwako…” Sammy alisema huku akimwangalia Tunu kwa utulivu.


“Shhhhh! I’m so sorry…” Tunu alisema kwa sauti ya chini.


“Sorry for what?” Sammmy aliuliza kwa sauti tulivu.


“For everything…”


“Hata siamini, hata baada ya miaka kumi na moja kupita bado unaonekana mrembo kwelikweli…” Sammy alichombeza baada ya kitambo kifupi cha ukimya. Tunu hakujibu, alibaki kimya huku tabasamu likiwa limeupamba uso ake.


Sammy alishusha pumzi, akajaribu kuvuta picha kukumbuka alivyokutana na Tunu miaka kumi na moja iliyokuwa imepita kwenye mahafali ya wanafunzi waliomaliza kidato cha sita ya Shule ya Wasichana ya Jangwani jijini Dar es Salaam, siku hiyo Tunu alikuwa mmoja wa wanafunzi wahitimu wa kidato cha sita.


Wakati huo Sammy alikuwa na umri wa miaka ishirini na nne tu na hakuwa na muda mrefu tangu ahitimu Shahada ya Kwanza ya Utalii na Biashara (Tourism With Business BA Honours) katika Chuo Kikuu cha Westminster nchini Uingereza.


Ilibakia kidogo tu angekufa kwa mshtuko wa moyo siku alipomwona Tunu kwa mara ya kwanza. Siku hiyo Sammy alikuwa ameambatana na Elli wakiwa wamepewa mwaliko wa Grace, dada wa Elli ambaye pia alikuwa mmoja wa wahitimu wa kidato cha sita. Wakiwa pale macho ya Sammy yalikuwa yakiangaza huku na huko. Wasichana walikuwa wamependeza kwelikweli, walikuwa wakicheza, wakicheka na kufurahi.


Mara Sammy akamwona msichana mmoja aliyekuwa ameketi kwa utulivu mno kuliko wasichana wengine. Alikuwa amemwona kabla lakini hakuwa amemtilia maanani, safari hii alimtulizia macho. Macho yao yakagongana. Sammy akashtuka sana. Huyu hakuwa msichana wa kawaida, alikuwa jamali aliyeumbika.


Sammy aliweza kuuona waziwazi urembo wa binti huyo japo alikuwa amevaa joho refu na pana lililokuwa limefunika maungo yake. Kwa nukta kadhaa alijikuta akiduwaa na kumkodolea macho. Pumzi zikampaa.


Akabaki kumtazama kuanzia miguuni hadi kichwani huku akijiambia kimoyomoyo, katika maisha yake hakupata kuhisi hali kama ile aliyoihisi muda ule kwa sababu ya msichana, tena kiumbe cha shani kama hicho! Amewahi kukutana na wasichana wengi warembo lakini alikiri kuwa hakuwahi kupatwa na hali kama ile iliyomtokea kwa mrembo huyo.


Muda wa kucheza muziki ulipowadia Sammy hakutaka kujivunga, alikwenda moja kwa moja hadi pale alipokuwa ameketi Tunu na kuinama kidogo kwa heshima huku akiweka mkono wake kifuani, “Naomba tucheze tafadhali. Kama utaniruhusu, wimbo mmoja tu.”


Tunu alimtazama kwa kitambo kama aliyekuwa akijishauri kisha bila kuongea neno wakaingia uwanjani na kuanza kulisakata. Kwanza kwa haya kidogo maana walikuwa hawafahamiani. Walicheza kimyakimya. Taratibu muziki ukaanza kuifukuza haya hiyo na miondoko yao ikaanza kurandana kiasi cha kuwavutia watu ambao hawakuwa wakicheza.


Watu wengi walijikuta wakiwaangalia wao tu, wengine kwa kuvutiwa na uchezaji wao, na wengine kwa husuda. Walipendeza mno wakawa kama pacha. Wimbo ule ukaisha na wimbo wa pili wa taratibu ukaanza, hawakuondoka. Walianza kuucheza huku wamekumbatiana. Kila mmoja alisahau kama kulikuwa na watu wengine wakiwaangalia. Hisia zao zilikuwa huru, wakiburudika mwili na roho, akili zao zikijiona kama waliofika safari yao baada ya kuvuka milima na mabonde.


“Unaitwa nani mrembo wangu?” Sammy alimuuliza Tunu huku mikono yake ikipapasa nyama za mgongo na kiuno chake.


“Naitwa Tunu,” Tunu alisema kwa sauti ya chini huku akiipitisha mikono yake nyuma ya shingo ya Sammy na kufanya chuchu za matiti yake kukitekenya kifua cha Sammy. Alisahau kabisa kama macho ya watu yaliyokuwa yakiwatazama. Sammy akajikuta akiwa na wakati mgumu wa kupambana na joto kali la mwili wa Tunu lililomfanya ajisikie faraja ya aina yake.


“Tunu nani?”


“Tunu Robin,” alinong’ona, “Na wewe?”


“Samuel Kambona, ila wewe niite Sammy…” Sammy alisita kidogo, kisha akaongeza, “Kwa kweli leo nimefurahi sana kukutana na wewe.”


“Kweli?” Tunu aliuliza kama mtoto mdogo.


“We unadhani nani asingefurahia kukutana na mrembo kama wewe? Au nani asingetamani kutaka kumkumbatia mrembo kama wewe? Hakika siku ya leo nitaikumbuka katika maisha yangu,” Sammy alisema huku akiupapasa mgongo wa Tunu. Tunu alifumba macho yake huku akiusikilizia mpapaso ule wa mikono ya Sammy.


“Najua kukutana kwetu hakukuwa kwa bahati mbaya, kila jambo huja kwa kusudi lake, na hii kwetu ndiyo nafasi nzuri. Unaonaje tukaifanya siku ya leo kuwa ya kukumbukwa zaidi kwenye maisha yetu,” Sammy alimwambia Tunu huku akimwangalia usoni.


“Ki vipi?” Tunu aliuliza huku akionesha mshangao kwa mbali, hakuonekana kuelewa maneno ya Sammy yalikuwa na maana gani.


“Sidhani kama nitaweza kuendelea kuishi kama sitapata penzi lako…” Sammy alisema kwa sauti ya kunong’ona.


“Ningetamani sana iwe hivyo lakini miye sijawahi kufanya mapenzi na mwanamume yeyote,” Tunu alisema huku akimtazama Sammy kwa aibu.


“Kweli!” Sammy aling’aka kwa mshangao uliochanganyika na shauku, shauku hiyo ikaipalilia hamu ya kutaka kumpata Tunu.


Mara wakashtuka baada ya kuhisi eneo lote lilikuwa limetawaliwa na ukimya. Kumbe muziki ulikuwa umekwisha kitambo! Ni wao wawili tu ndio waliokuwa wamebaki wima kwenye eneo la kuchezea muziki. Kwa aibu wakaondoka na kuongozana kwenda kukaa. Lakini huo haukuwa mwisho, walipanga na kukutana siku iliyofuata.


Sammy alimchukua Tunu hadi kwenye nyumba aliyokuwa amepanga eneo la Makumbusho, Kijitonyama. Siku hiyo Tunu alikuwa amevaa blauzi na kaptula ya kitenge. Kaptula ile iliishia juu ya magoti yake na kuifichua minofu ya miguu na mapaja yake yaliyonona.


“Nimekuja mara moja tu kukusalimia, sitakaa muda mrefu,” Tunu alisema huku akiitazama saa yake ya mkononi mara tu walipoingia ndani. Hata hivyo, Tunu alikuwa akimtazama Sammy kwa macho ya wizi, macho yake yalikuwa yamelegea kama aliyekuwa amekula kungu, sura yake ilionekana wazi kumsubiri Sammy afanye kitu.


Sammy aligundua kuwa Tunu alikuwa amekolea ingawa haikuwa rahisi kwake kukubali moja kwa moja, akamshika mkono. Hakuleta pingamizi lolote, kwani alionekana kutojiweza na uso wake aliuinamisha chini kwa aibu. Alimvutia kifuani kwake akamkumbatia. Tunu alijigandamiza kwenye mwili wa Sammy na kutulia huku akihema kwa nguvu.


Sammy hakuendelea kusubiri, alimbeba hadi kitandani, akamwangusha kama mzigo. Tunu pumzi zilimpaa! Kilichofuata baada ya hapo kilimfanya ahisi kuchanganyikiwa. Alijikuta akiwa taabani huku akiyashuhudia maumivu ya kupendeza yaliyokuwa yakimuua taratibu kama mgonjwa taabani. Yote yaliyotendeka kwenye mwili wake hakuwahi kuyaona ndotoni au hata kuyafikiria.


Mambo yanazidi kunoga, teksi inazidi kuzua mambo na sasa imewaunganisha tena Sammy na Tunu. Je, nini kitafuata baada ya hapo? Sammy atamsaliti Joyce? Je, Tunu hana mume? Na vpi kuhusu uvamizi nyumbani kwa Sammy, Winifrida yupo wapi? Usikose kufuatilia stori hii ya kusisimua... 




Sammy alimchukua Tunu hadi kwenye nyumba aliyokuwa amepanga eneo la Makumbusho, Kijitonyama. Siku hiyo Tunu alikuwa amevaa blauzi na kaptula ya kitenge. Kaptula ile iliishia juu ya magoti yake na kuifichua minofu ya miguu na mapaja yake yaliyonona.


“Nimekuja mara moja tu kukusalimia, sitakaa muda mrefu,” Tunu alisema huku akiitazama saa yake ya mkononi mara tu walipoingia ndani. Hata hivyo, Tunu alikuwa akimtazama Sammy kwa macho ya wizi, macho yake yalikuwa yamelegea kama aliyekuwa amekula kungu, sura yake ilionekana wazi kumsubiri Sammy afanye kitu.


Sammy aligundua kuwa Tunu alikuwa amekolea ingawa haikuwa rahisi kwake kukubali moja kwa moja, akamshika mkono. Hakuleta pingamizi lolote, kwani alionekana kutojiweza na uso wake aliuinamisha chini kwa aibu. Alimvutia kifuani kwake akamkumbatia. Tunu alijigandamiza kwenye mwili wa Sammy na kutulia huku akihema kwa nguvu.


Sammy hakuendelea kusubiri, alimbeba hadi kitandani, akamwangusha kama mzigo. Tunu pumzi zilimpaa! Kilichofuata baada ya hapo kilimfanya ahisi kuchanganyikiwa. Alijikuta akiwa taabani huku akiyashuhudia maumivu ya kupendeza yaliyokuwa yakimuua taratibu kama mgonjwa taabani. Yote yaliyotendeka kwenye mwili wake hakuwahi kuyaona ndotoni au hata kuyafikiria.


ENDELEA...


Hakujimudu na wala hakuweza kuvumilia, alitapatapa kama samaki anayekaangwa hai, akaanza kulia. Kilikuwa kilio cha faraja kilichotokana na adhabu aliyojitakia mwenyewe ambayo wala hakuijutia. Alilia na machozi yakamtoka, sauti ikamkauka. Ilikuwa ni siku ya aina yake kwake, siku ambayo kamwe isingepotea katika fikra zake.


Mechi ilipoisha Tunu hakuweza hata kumtazama Sammy machoni, alikuwa anatweta kama aliyemaliza mbio ndefu za kilomita arobaini na mbili baada ya kuvunja rekodi ya dunia. Aliyafuta machozi yake kwa kiganja cha mkono na kushusha pumzi ndefu.


“Pole mpenzi, pole sana…” Sammy alimpa pole Tunu huku akicheka kimoyomoyo, kilikuwa kicheko cha ushindi.


“Mmh, hakyamungu ungeniua,” Tunu alisema kwa sauti legevu ya chini huku akipiga miayo.


“Usijali, mpenzi wangu, utazoea tu. Hata hivyo, umenifurahisha sana, you’re a real gift to me. Kuanzia leo sitakuita Tunu bali wewe ni Gift…”


Tunu aliitazama saa yake na kushtuka, ilikuwa imeshatimu saa mbili na nusu usiku, akaamua kuaga na kuondoka, alikuwa hoi. Sammy alimsindikiza hadi kituo cha daladala, wakapeana mabusu motomoto ya kuagana kisha akampandisha daladala la kuelekea Sinza huku wakiahidiana kukutana baada ya siku tatu, lakini tangu siku hiyo Sammy hakuweza kumtia tena machoni Tunu! Bahati mbaya hakuwa akijua Tunu aliishi Sinza ipi, maana Sinza ni kubwa ati!


Sammy alikuwa kama mwehu, alizunguka mji mzima kumtafuta Tunu, alifika kila pembe ya Sinza na viunga vyake, aliuliza watu aliodhani wangeweza kuwa na taarifa za Tunu, lakini hakuna alichoambulia ambacho kingeweza kumsaidia kujua alipo. Alimfuata Grace, dada wa Elli ambaye alisoma darasa moja Tunu, lakini pia hakupata habari zake.


Kutokuonekana kwa Tunu katika maisha ya Sammy kulimwathiri sana kisaikolojia na hata kuathiri utendaji wake wa kazi za kila siku. Alijikuta akiwa na mwili wa mgonjwa akisubiri kifo ili arudi mavumbini, ubongo upo hospitali na nafsi kwa Mungu. Tabibu pekee wa kuutibu ugonjwa wake alikuwa mmoja tu, Gift!


Alimuwaza yeye tu muda wote. Mbele ya uzuri wa kiumbe aliyemwita Gift, Sammy alijiona kama limbukeni wa mapenzi. Gift alikuwa amemwachia shimo kubwa sana moyoni liitwalo mapenzi. Shimo ambalo hakukuwa na mtu mwingine wa kuliziba isipokuwa yeye tu. Kwa miaka miwili Sammy hakujiweza, kutwa kucha alimwaza Gift tu! Alishangaa, iweje mrembo yule apotee ghafla katika kipindi ambacho alimhitaji mno?


Katika kipindi cha miaka miwili tangu kutoweka kwa Tunu, Sammy alishindwa kabisa kumwondoa moyoni mwake, mawazo kuhusu Gift yalimpitia kila siku na kila alipolikumbuka jina lake moyo wake ulimwenda mbio kama mtu aliyekuwa na ugonjwa wa wasiwasi. Alijiuliza iwapo hali ile ilikuwa ni matokeo ya kumpenda sana Gift, ingekuwaje pindi angesikia kuwa ameolewa na mwanamume mwingine?


Yako wapi yale macho yake mazuri yenye mvuto wa ajabu yaliyomtia utumwani? Hivi iliwezekanaje kwa msichana kama Gift, aliyeamini ni zawadi yake kutoka kwa Mungu, kutoweka ghafla na kumwacha yeye katika kipindi kama kile? Kuachwa si kioja, laiti angelipewa nafasi ya miaka kadhaa kusema na roho yake pengine angeweza kuwa na uamuzi mzuri zaidi, ingawa ni ajabu sana kwa donda ndugu kupona!


Baada ya miaka miwili ya maisha ya mateso, Sammy alijiambia kuwa ilikuwa imetosha, huo sasa ulikuwa ni wakati mwafaka wa yeye kuanza maisha mapya kwani hakuweza kuendelea kumsubiri mtu ambaye hakujua yupo wapi, kama ni mzima au amekufa. Ni katika kipindi hicho ambacho Sammy alikutana na Joyce wakati akitoka Tanga kutembelea mapango ya Amboni. Kipindi ambacho Joyce alikuja kwenye maisha yake kama malaika mwokozi aliyeshushwa kumwondolea machungu ya kukimbiwa na Gift. Yote yaliyokuja kutokea baadaye yamebaki kuwa historia…


“Sammy!” sauti nyororo ya Tunu ilimzindua Sammy kutoka kwenye lindi la mawazo. Sammy alimtazama Tunu akamwona akiwa anamtazama kwa utulivu huku akitabasamu.


“Gift!” Sammy alimudu kusema huku akishusha pumzi za ndani kwa ndani. “Ninahitaji kujua ukweli na tafadhali naomba usiniongopee. Niambie ukweli hata kama ukweli huo utaniumiza sana,” Sammy alimwambia Tunu huku akimtazama usoni kwa makini.


“Unataka kujua nini, Sammy?” Tunu aliuliza huku akiwa makini kusikiliza alichotaka kuambiwa.


“Kwa nini ulinikimbia? How could you do this to me? ” Sammy aliuliza huku akimtazama Tunu kwa uchungu mkubwa. “Maybe I was not important to you at all,” aliongeza kabla Tunu hajasema neno.


Kwa sekunde chache Tunu alibaki kimya akimtumbulia macho Sammy akiwa hajui niseme nini, hakuweza kabisa kumjibu bali alibaki kimya huku akimtazama kwa makini. Kila alipotaka kujieleza alihisi kukosa ujasiri.


“Kwa nini ukaamua kutupa jongoo na mti wake! Tunu I need to know the truth,” Sammy alisema huku akiwa ameyatuliza macho yake kwenye uso wa Tunu.


“I’m so sorry…” Tunu alisema kwa sauti ya chini.


“Sorry? Baada ya miaka yote hii ya kunipa mateso leo unaniambia kirahisi rahisi tu, eti I’m so Sorry! Sorry for what? I’m disappointed, very disappointed,” Sammy alishindwa kuvumilia akaanza kuzungumza kwa sauti kubwa na kuwafanya watu wengine wageuze shingo zao kuwatazama kwa mshangao.


“Enough! Can you please stop blaming me?” Tunu naye alikuja juu na kusema kwa sauti ya ukali huku akikunja sura yake.


Kwa kitambo fulani hali ya mahali pale ilikuwa tete, walibaki kimya wakiwa wanaangaliana kama majogoo yaliyotaka kupigana. Tunu alishusha pumzi za ndani kwa ndani.


Inaendelea...

- (89)


“I’m sorry for everything, I’m real very sorry,” Tunu alimwambia Sammy huku akijitahidi kutengeneza tabasamu la kumlainisha Sammy.


Sammy alitaka kusema lakini akatishwa na simu yake iliyoanza kuita kwa fujo. Aliitazama kwa makini kisha akaitupia jicho saa yake na kushtuka. Akashusha pumzi.


“Mke wangu anapiga simu,” Sammy alisema huku akionekana kama aliyekuwa akijishauri iwapo aipokee au aipotezee.


Nyumbani kwa Sammy, Joyce alikuwa anapiga simu huku amewekewa kisu shingoni na Spoiler akimtishia kumchinja endapo angeshindwa kumshawishi Sammy arudi nyumbani. Spoiler alikuwa ameghadhabika kwelikweli.


“Na usijaribu kufanya jambo lolote la kipumbavu kumshtua, vinginevyo nitawaua wewe na mwanao…” Spoiler alisema kwa ghadhabu.


“Tafadhali naomba msimdhuru mwanangu…” Joyce alisema kwa woga huku akilia, alimkodolea macho Dulla aliyekuwa kamwelekezea Pendo bastola kichwani. Wakati huo Pendo alikuwa amebandikwa gundi maalumu ya karatasi mdomoni ili asiweze kupiga kelele.


Kwenye mgahawa wa ELLI’S, Sammy aliendelea kuiangalia ile simu huku akijiuliza angemjibu nini mkewe baada ya kupokea, simu iliita hadi ikakatika akiwa bado anaikodolea macho. Akashusha pumzi. Mara ikaanza kuita tena, hakusubiri akaipokea huku akimtupia jicho Tunu na kuipeleka moja kwa moja kwenye sikio lake. “Hallo!”


“Baba Pendo, njoo nyumbani haraka, hali ya Pendo ni mbaya sana,” Joyce alisema huku analia, sauti yake ilipenya kwenye ngoma ya sikio la Sammy na kumfanya ashtuke sana.


Sammy alisimama bila kujijua. Alibana pumzi huku akionekana kunyong’onyea sana kisha akashusha pumzi taratibu. Tatizo la Pendo lilionekana kumnyima raha.


“Baba Pendo! Mbona huongei, kwani uko wapi?” sauti ya Joyce ilimzindua tena kutoka kwenye mawazo.


“Fanya hivi, naomba chukua teksi tukutane hapo hospitali ya…”


“Siwezi, njoo nyumbani,” Joyce alimkatisha Sammy, alikuwa analia kilio cha kwikwi.


Sammy alitaka kusema neno lakini akagundua kuwa simu ilishakatwa. Aliogopa sana, alihisi mwili wake ukiishiwa nguvu na hakujua afanye nini. Tunu alionekana kuguswa sana na mabadiliko ya Sammy, alimtazama kwa makini akitaka kujua alichoambiwa na mkewe. Sammy alianza kukusanya vitu vyake, simu na funguo iliyokuwa juu ya meza huku akimtazama Tunu kwa huzuni kidogo.


“Samahani, Gift, nalazimika kuondoka, hali ya mwanangu nyumbani si nzuri kabisa,” Sammy alisema kwa huzuni na kuanza kuondoka lakini akakumbuka na kutoa kadi yake ya kibiashara, akampa Tunu, “Naomba tuwasiliane.”


Tunu aliitazama ile kadi kwa makini na alipoinua uso wake Sammy hakuwepo, akaduwaa asijue la kufanya. Muda huo huo aliwaona wale wanaume waliokuwa wameketi meza ya tatu kutoka meza yake, Bob Chopa na mwenzake wakiondoka haraka haraka kuelekea nje.


Huko nje, Sammy alilifikia gari lake na kufungua mlango, akaingia ndani ya gari na kuwasha injini ya gari, akasubiri kwa sekunde chache huku akiliacha gari likiunguruma taratibu. Simu yake ya mkononi ikaanza kuita, aliiangalia kwa makini na kugundua kuwa ilikuwa ni namba ngeni. Aliipokea kwa pupa huku moyo wake ukienda mbio kwa wasiwasi, “Hallo… Hallo!” alisema lakini upande wa pili wa simu ulikuwa kimya. Kimya kabisa! Sammy aliita tena lakini kimya kilitawala upande wa pili wa simu, mara simu ikakatwa.


Sammy alishangaa, akataka kupiga ili kujua ni nani aliyekuwa akimpigia halafu haongei, akaona kuwa ingempotezea muda na hivyo hakuipa umuhimu, akili yake ilikuwa mbali, alidhamiria kuwahi nyumbani kwake kwani hakujua kama Pendo alikuwa bado yu hai au amekufa. Akaachia breki taratibu na gari likaanza kuserereka. Wakati gari likianza kuyaacha maegesho, Sammy aliwaona wanaume wawili wakimsogelea huku wakipunga mikono yao juu kumsimamisha.


Alikanyaga breki na kuwatazama kwa makini, macho yake yakagongana na yao, Sammy akawatambua. Walikuwa ni wale wanaume waliokuwa wameketi meza ya tatu kutoka meza ya Tunu. Yule mwanamume mfupi alionekana kama aliyechoka sana au mgonjwa. Kila dalili ya kuomba msaada ilijionesha kwenye macho yake na alikuwa ameshikiliwa na mwenzake aliyekuwa mrefu mwenye mwili ulioshiba.


Wale wanaume waliangalina katika namna ya ‘nani aseme’ kisha wakamwangalia Sammy kwa unyonge. “Samahani, ndugu, unaweza kutuacha hapo mbele?” yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba alisema.


Sammy aliwatazama kwa makini akionekana kusita sana, akatingisha kichwa chake kukataa. “Samahani sichukui abiria sasa hivi, kuna sehemu natakiwa kuwahi.”


Wale jamaa wakageuka kuangaliana tena kwa namna ambayo Sammy hakuweza kuielewa. Hata hivyo, walionekana kukata tamaa. Bob Chopa, yule mwanamume mfupi akapandisha juu mabega yake na kuyashusha huku akimkabili Sammy. Aliikunjia kifuani mikono yake katika namna ya kuomba msaada.


“Basi unaweza kutuacha hapo mbele tu, halafu uendelee na safari yako, tafadhali sana…” alisema huku akionesha kwa kidole sehemu wanakotaka kuelekea.


Sammy hakuwa na muda wa kupoteza wala kujishauri, alishusha pumzi ndefu na kubetua kichwa chake kukubali huku akiwaashiria waingine. Walionesha furaha na kuingia, wakaketi kwenye siti ya nyuma ya gari.


Cadillac DeVille likaingia barabarani likiwa katika mwendo wa kasi. Sammy alikuwa anaendesha gari kama mtu aliyechanganyikiwa, ingawa alionekana kuwa makini barabarani.


* * * * *


Winifrida alikuwa amejikunyata kwa hofu kwenye eneo finyu lililokuwa juu ya kabati la nguo lililo ukutani. Alikuwa na mashaka makubwa na hakujua aliwezaje kunusurika mbele ya yule mtu aliyekuwa na uchu kama fisi aliyeona mzoga, hata hivyo aliamini kuwa bado hali haikuwa salama kwake, kwani yule mtu angeweza kurudi tena kule chumbani kumtafuta.


Winifrida alikuwa anaweweseka huku akijaribu kusikiliza kwa makini kama angeweza kusikia chochote kilichokuwa kinaendelea kule sebuleni, ambako wifi yake Joyce na Pendo walikuwa chini ya ulinzi wa majahili wasio na huruma.





Winifrida alikuwa ameponea kwenye tundu la sindano baada ya kupata wazo la kupanda kule juu na kujificha, lilikuwa eneo ambalo ingekuwa vigumu kwa mtu asiye mwenyeji wa chumba kile kufahamu kuwa kulikuwepo eneo finyu ambalo lingeweza hata kumficha mtu, hasa mwenye umbile dogo kama lake. Lile eneo lilikuwa limezibwa na mfuniko wa ubao mteke (plywood) uliopakwa rangi sawa na ile iliyopakwa ukutani na kupafanya paonekane kama sehemu ya ukuta.


Hakuwa na namna nyingine isipokuwa kujificha pale baada ya kuhisi kuwa angeonekana kama angetaka kutoka mle chumbani. Kilichomtisha zaidi ni kauli aliyoisikia baada ya wale watu kuelezana kuchunguza kila chumba ili kuwabaini wote waliokuwemo mle ndani. Bahati nzuri walianzia katika vyumba vingine na kile chumba kikawa cha mwisho. Hiyo ilimpa nafasi nzuri ya kujinusuru.


Alikuwa amefikiria kujificha pamoja na Pendo lakini akachelea kufanya hivyo kwa hofu kuwa eneo lile lisingetosha kuwaweka wote wawili na endapo wale watu wangeingia chumbani na wasikute hata mtu mmoja, wangepata shaka na matokeo yake ingekuwa rahisi kugundulika.


Winifrida alikuwa akiwaza afanye nini kuwanusuru Joyce na Pendo ilhali hofu nayo ilizidi kumtomasa maungoni na kumchachafya. Wakati akiwaza hayo, mwili nao ulikuwa unamuuma kama kidonda. Alishajikunyata pale juu kwa muda wa kutosha na sasa mwili wote ulikuwa umekufa ganzi. Pamoja na hayo bado hakuacha kuwaza. Alijiuliza wale watu ni akina nani na kwa nini walikuwa wanamtaka Sammy?


Pamoja na hofu aliyokuwa nayo lakini alikumbuka kumwona yule mtu aliyeingia mle chumbani, japo kwa taabu, kupitia upenyo mdogo. Aliweza hata kuiona sura yake wakati yule mtu alipogeuka na kuelekea upande ule wa kabati alikokuwa amejificha. Mavazi na umbile lake vilimjulisha Winifrida kuwa alikuwa kipande cha mtu. Winifrida alihisi kuwa aliwahi kumwona yule mtu sehemu fulani. Alimwona wapi?


Vinyweleo vya mwili vikamsimama baada ya kuikumbuka ile sura. Ilikuwa ni sura ile ile aliyoiona kwenye video ya mauaji aliyoikuta kwenye memory card aliyoitoa ndani ya gari la Sammy. Alihisi baridi kali ya hofu ikipenya hadi kwenye mifupa. Sasa aliamini kuwa lilikuwepo jambo lisilo la kawaida likiendelea ambalo hakulijua. Je, walikuwa wanaitafuta ile memory card aliyokuwa nayo? Alitishika. Tena alitishika si kidogo.


Hili lilimwongezea mashaka zaidi na kujiona kuwa hakuwa salama kabisa endapo ingegundulika kuwa ni yeye aliyeichukuwa ile memory card. Mapigo ya moyo wake yalikuwa yanakimbia kwa kasi ya ajabu. Alihisi yalikaribia kukitoboa kifua chake chenye mifupa miteke na kuchanja mbuga nje ya mwili wake.


Alianza kuweweseka kwa hofu na kufumba macho yake, akaanza kuomba Mungu ili amnusuru yeye na jamaa zake dhidi ya wale watu walioonekana kubobea kwa unyama ulioweza kumtisha hata ibilisi. Baada ya maombi mafupi ghafla alijikuta akiuvaa ujasiri. Akafumbua macho yake na kutazama pale alipokuwa amesimama yule mtu. Patupu!


Hakukuwa na mtu tena wala kivuli chake. Na hata Pendo hakuwepo kitandani! Amempeleka wapi? Alijikuta akiishiwa nguvu. Mara akamsikia yule mtu akimhoji Joyce ni wapi aliko mtoto mwingine kwa kuwa walikuwa wameambiwa mwanzoni kuwa mle ndani kuna watoto wawili.


Hata hivyo, Winifrida hakusikia Joyce alijibu nini, alichoweza kuambulia ni kuwasikia wale watu wakimlazimisha Joyce ampigie simu Sammy kumtaka arudi nyumbani haraka na kumwonya asifikirie kufanya ujanja ambao ungeyagharimu maisha yake na mtoto Pendo. Wakati huo Joyce alikuwa analia kilio cha kwikwi.


Winifrida alihamanika sana. Alipepesa macho yake pale alipokuwa amejikunyata huku akiwaza jinsi ya kufanya ili kuwanusuru Joyce na Pendo toka katika mikono ya wale majahili. Aliamua kufanya jambo la hatari lakini la kishujaa. Aliamua kumpigia simu Sammy na kumweleza ukweli wa kile kilichokuwa kinaendelea pale nyumbani. Lakini angeanzaje?


Bahati ilikuwa upande wake, simu yake ilikuwa imefichwa kule kule juu ya kabati alikokuwa amejikunyata. Ni kama vile Mungu alikuwa amemwongoza kuificha ile simu juu ya kabati. Kwa hofu kubwa aliichukua na kuitafuta namba ya Sammy, akapiga na kusikiliza, akasikia simu ikiita upande wa pili na mara ikapokelewa, kisha akaisikia sauti ya Sammy kutoka upande wa pili wa ile simu.


Winifrida akashikwa na kitete na kushindwa kuongea, hofu ilikuwa imemtawala na donge la fadhaa kumkaba kooni. Alimeza funda kubwa la mate kwa nguvu mithili ya mtu anayejaribu kukisukuma kipande cha mfupa kilichokwama kooni. Alitamani sana kupiga yowe lakini sauti yake ikamsaliti. Akajiuliza kwa nini apige yowe? Akili ilimhoji na kumtia ganzi.


Akajikuta akishindwa kabisa kuongea japo alimsikia Sammy akiendelea kuita upande wa pili wa simu. Alishindwa, si kwa sababu ya hofu ya kusikiwa, bali alijiuliza kuwa endapo Sammy angemuuliza simu ile aliitoa wapi angemjibu nini kwani hakuna yeyote aliyejua kama anamiliki simu. Akaikata.


Alianza kujilaumu kwa kutokuzungumza na Sammy, kwani ni hatari zaidi kumwacha Sammy arejee nyumbani na kukutana na wale watu hatari kuliko yeye kutafuta majibu ya wapi ameitoa ile simu. Majuto yalipita haraka kichwani mwake, yalipita kwa kasi mno kiasi cha kumwita Mungu na asimweleze alilotaka amfanyie.


Mara akapata wazo la kupiga tena simu. Lakini kwa wahaka aliokuwa nao, asingeweza kuzungumza na Sammy kwa kuchelea kusikiwa na wale watu. Alishusha pumzi huku akijaribu kusikiliza kwa makini akihofia kuingia kwenye mtego kwa kudhani mmoja wa watu wale, ambao hakujua idadi yao, angeweza kuwa amejificha mle chumbani kumsubiri. Alijitahidi kuangaza macho yake sehemu alizoweza kuzifikia lakini hakuona kitu cha kutilia shaka.


Usikose kufuatilia kila hatua ya kusisimua ambayo Taxi inapitia ili kuyajua yote yaliyojiri. Ciao...

Nb..kwa watakaotaka kuchangia vocha kidogo




Winifrida akashikwa na kitete na kushindwa kuongea, hofu ilikuwa imemtawala na donge la fadhaa kumkaba kooni. Alimeza funda kubwa la mate kwa nguvu mithili ya mtu anayejaribu kukisukuma kipande cha mfupa kilichokwama kooni. Alitamani sana kupiga yowe lakini sauti yake ikamsaliti. Akajiuliza kwa nini apige yowe? Akili ilimhoji na kumtia ganzi.


Akajikuta akishindwa kabisa kuongea japo alimsikia Sammy akiendelea kuita upande wa pili wa simu. Alishindwa, si kwa sababu ya hofu ya kusikiwa, bali alijiuliza kuwa endapo Sammy angemuuliza simu ile aliitoa wapi angemjibu nini kwani hakuna yeyote aliyejua kama anamiliki simu. Akaikata.


Alianza kujilaumu kwa kutokuzungumza na Sammy, kwani ni hatari zaidi kumwacha Sammy arejee nyumbani na kukutana na wale watu hatari kuliko yeye kutafuta majibu ya wapi ameitoa ile simu. Majuto yalipita haraka kichwani mwake, yalipita kwa kasi mno kiasi cha kumwita Mungu na asimweleze alilotaka amfanyie.


Mara akapata wazo la kupiga tena simu. Lakini kwa wahaka aliokuwa nao, asingeweza kuzungumza na Sammy kwa kuchelea kusikiwa na wale watu. Alishusha pumzi huku akijaribu kusikiliza kwa makini akihofia kuingia kwenye mtego kwa kudhani mmoja wa watu wale, ambao hakujua idadi yao, angeweza kuwa amejificha mle chumbani kumsubiri. Alijitahidi kuangaza macho yake sehemu alizoweza kuzifikia lakini hakuona kitu cha kutilia shaka.


ENDELEA...


Kisha akapata wazo jingine. Sasa alikata shauri, liwalo na lilwe lakini asingeweza kuendelea kujikunyata pale juu ilhali alikuwa na uwezo wa kunusuru ile hali. Aliazimia kupiga simu, kuwapigia polisi kwa kutumia ile namba yao ya dharura na kuwaleleza kilichokuwa kinaendelea kwenye nyumba yao.


* * * * *


Sammy aliendelea kuendesha gari lake katika barabara ya Uhuru kwa mwendo wa kasi akiyapita magari mengine. Sasa alikuwa anazivuka taa za kuongozea magari barabarani za Buguruni Shell na kuingia barabara ya Mnyamani, mara akaonekana kugutuka na kuwauliza wale watu aliokuwa amewapa msaada wa usafiri bila kugeuka wala kuwatazama. “Kwani mnashukia wapi? Mimi napitia barabara ya Mnayamani.”


Kimya!


Sammy akashangaa na kugeuza shingo yake kuwatazama. Akapigwa na butwaa na kushtuka sana. Akanywea. Yule mwanamume mrefu aliyepanda hewani kisawasawa na mwenye mwili ulioshiba alikuwa amemnyooshea bastola huku akiwa makini sana.


Uso wa Bob Chopa, yule mwanamume mfupi kiumbo lakini mkakamavu na mwenye sura ya unyenyekevu ulikuwa umepambwa na tabasamu la kifedhuli.


“Sasa sikiliza, utafuata maelekezo yangu,” yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba alisema kwa ukali.


Sammy alionekana kubabaika sana. Alishusha pumzi za ndani kwa ndani na kubana midomo yake, hakujua afanye nini.


“Ni nini mnakitaka toka kwangu?” Sammy aliuliza kwa sauti tulivu huku akipunguza mwendo wa gari kuwakwepa wapiti njia.


“Hatuna shida ya kukudhuru wala kuchukua gari lako ila kuna kitu tunakihitaji ndani ya hili gari, tukikipata tutakuacha uende zako,” yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba alimwambia Sammy.


“Na msipokipata?” Sammy aliuliza huku akipata shaka, hakuiamini ile kauli ya yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba.


“Tutajua cha kufanya…”


“Kwani kitu gani mnachokihitaji kwangu?” Sammy aliuliza huku akimtupia jicho la wizi yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba.


“Utajua baadaye, kwa sasa endesha gari hadi nitakapokwambia usimame,” yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba alimwambia na Sammy pasipo kubisha aliendesha gari lake pasipo kuhoji. Muda huo akili yake ilikuwa inafanya kazi haraka ili kujinusuru toka katika mikono ile ya watekaji.


Yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba aliikoki bastola yake na kuisogeza katika kichwa cha Sammy. Sammy alibana pumzi baada ya kuuhisi ubaridi wa bomba la bastola. Aliuma meno yake akionekana kuzuia donge la hasira lililoanza kumchonyota kooni. Waliivuka reli ya kuelekea Ubungo na hapo Sammy akataka kugeuza shingo yake kuwatazama.


“Endesha na usigeuze shingo yako kutazama nyuma,” yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba alimwambia Sammy kwa ukali.


Muda wote Bob Chopa alikuwa ameketi katika siti yake akiwa mtulivu mno, alikuwa anatabasamu kama ambaye hakuhusika na lile tukio. Alikuwa anashuhudia kila hatua, jinsi ambavyo yule mwenzake mrefu mwenye mwili ulioshiba alivyokuwa makini kuhakikisha Sammy hafanyi jambo lolote ambalo lingeweza kuwagharimu.


Maara simu yake ikaanza kuita, Bob Chopa aliitazama kwa makini na kupokea mara moja baada ya kuliona jina la mpigaji. “Hallo, boss,” alisema mara baada ya kuiweka sikioni.


“Vipi, Bob, mmefikia wapi?” sauti upande wa pili wa simu ilisikika ikiongea kwa wasiwasi.


“Bado, hatujafika eneo sahihi,” Bob Chopa alijibu na kushusha pumzi.


“Kuweni makini, nadhani kuna mtu anawafuatilia, pia hakikisheni huyo bwana haumii nitamhitaji baadaye kwa matumizi ya nyumbani, tumeelewana?”


“Sawa, boss,” Bob Chopa alisema huku akiachia kicheko hafifu, alikwisha fahamu nini maana yake. Akakata simu huku akimwangalia Sammy kwa makini na kusema. “Kazi kwelikweli!”


“Vipi, kamanda?” yule mwenzake mrefu mwenye mwili ulioshiba alimuuliza Bob Chopa kwa shauku.


“Disko limeingiliwa na Mmasai,” Bob Chopa alijibu huku akiendelea kutabasamu. “Ila usijali, nitacheza naye muziki wowote anaoutaka,” akaongeza huku akiendelea kutabasamu.


“Ongeza mwendo!” yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba alimwambia Sammy baada ya kuona mwendo wa gari umepungua, wakati huo walikuwa wanavuka eneo la Kidarajani.


Simu ya Sammy ikaanza kuita. Sammy akashtuka na kuitupia jicho katika hali ya kukata tamaa kwa kuwa alijua asingeweza kuipokea bila kuruhusiwa na wale watu. Simu yake ilikuwa imewekwa kwenye dashboard. Ilikuwa ni simu kutoka kwa Joyce aliyetaka kujua alikuwa amefika wapi.


Yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba aliitupia jicho la haraka ile simu kisha akayarudisha macho yake kumtazama Sammy kwa makini. Aliamua kuihamisha bastola yake toka kwenye kichwa cha Sammy na kuigandamiza kwenye mbavu zake. Hofu ilizidi kumsonga Sammy. Akaitupia tena jicho simu yake iliyoendelea kuita. Akaanza kuomba Mungu utokee muujiza.


Mara wakaliona gari moja likija kasi nyuma yao, lilikuwa ni gari aina ya Nissan Patrol la rangi nyeusi.Sammy akashusha pumzi za ahueni huku akiendelea kuomba Mungu. Bob Chopa alitoa bastola yake kutoka mafichoni na kujiweka tayari kwa lolote, macho yake aliyakaza kuliangalia kwa makini lile gari lililokuwa linawasogelea.


Wakati huo walikuwa wanalivuka soko la Vingunguti Kwa Simba. Lile gari aina ya Nissan Patrol jeusi likawafikia na kuanza kuwapita huku dereva wake akipiga honi kuonesha kuwa alikuwa na haraka. Wote walilitupia macho na kuyaona maandishi makubwa ya ‘POLISI’ ubavuni. Moyo wa Sammy ukapiga kite. Pah!


Bob Chopa akawa makini kuangalia ndani ya lile gari. Kulikuwa na maofisa wawili wa polisi. Sammy akataka kujaribu bahati yake, akaongeza mwendo ili kwenda sambasamba na lile gari la Polisi huku akigeuza shingo yake kuwatazama wale maofisa wa polisi kwa jicho la kuomba msaada.




Ofisa wa Polisi aliyekuwa ameketi upande wa kushoto aligeuza shingo yake kumtazama Sammy kwa macho ya kuuliza. Sammy akajaribu kuonesha hofu usoni kwake ili wale maofisa wa polisi waweze kubaini kuwa alihitaji msaada. Yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba aligundua ujanja wa Sammy, akazidi kuigandamiza bastola yake kwenye mbavu za Sammy.


“Usijaribu kufanya jambo lolote la kijinga. Utajutia uamuzi huo,” yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba alimtahadharisha Sammy kwa sauti ya chini. Kisha akachungulia nje kumtazama yule ofisa wa Polisi na kuachia tabasamu huku akimfanyia ishara ya dole gumba.


Yule ofisa wa polisi naye alionesha ishara ya dole gumba kwa yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba. Sammy hakuwa na ujanja tena, alitulia na kuendesha gari ilhali hofu ikizidi kumtambaa mwilini. Lile gari la Polisi likaongeza mwendo na kuwaacha.


Sammy akashusha pumzi huku akiwa amekata tamaa. Kisha akaonekana kupata wazo, lakini kabla hajafanya chochote simu yake ikaanza kuita tena. Sasa Bob Chopa alinyoosha mkono wake na kuichukua kisha akaitazama kwa makini na kuliona jila “My Wife’ likijitokeza kwenye kioo cha simu. Akaikata na kuizima kabisa.


Wakati huo gari lilikuwa limefika Vingunguti kwenye makutano ya barabara za Barakuda, iliyoelekea Fida na iliyokuwa inakwenda kutokea barabara ya Nyerere. Yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba akamuamru Sammy akunje kuelekea barabara ya Barakuda kupitia machinjioni.


* * * * *


Baada ya Sammy kutoka na hapo hapo Bob Chopa na mwenzake nao wakaondoka haraka kuelekea nje, Tunu alianza kupata hisia tofauti zilizoanza kuumbika kichwani mwake, moyo wake ulipiga kite kwa nguvu, hata hivyo aliendelea kutulia kwenye kiti chake.


Muda huo huo alimwona yule mrembo aliyekuwa ameketi kwenye meza iliyokuwa jirani na mlango wa kuelekea maliwato akiwa na wasiwasi huku akimtupia jicho la wizi Tunu. Tunu alianza kumtazama kwa udadisi huku akijaribu kukumbuka ni wapi na lini alimwona maana sura yake haikuwa ngeni sana kwake.


“Sijui nimemuona wapi huyu mdada?” Tunu alinong’ona kama bwege na

wakati huo zile kumbukumbu chache zilizosalia kichwani mwake kuhusu yule mrembo ziliyeyuka kabisa na kumwacha katika mduwao wa kizembe.


Yule mrembo alinyanyua mkono wake kuitazama saa yake ya mkononi na kisha akageuka na kutazama katika ule mlango wa kutokea mle ukumbini huku akionekana mwenye haraka na wasiwasi. Aliponyanyuka kutaka kuondoka, Tunu naye akanyanyuka. Yule mrembo akaonekana kusita kidogo na kumtupia Tunu jicho la wizi. Macho yao yakagongana.


Muda huo kulikuwa na watu waliokuwa wakiendelea kuingia mle ukumbini na vilevile walikuwepo wengine walioonekana kuondoka. Ulipita muda mfupi yule mrembo akijifanya kutazamatazama huku na kule mle ndani kama aliyekuwa akimtafuta mtu na alipoona kuwa kila mtu alikuwa akiendelea na hamsini zake alielekea maliwato ya wanawake.


Tunu alihisi kuwa huo ulikuwa ujanja tu wa yule mrembo ili kumhadaa kabla hajatoroka, naye akaamua kuelekea kule kule maliwato ya wanawake lakini akiwa na tahadhari kichwani. Alisimama kwa muda pale katika mlango wa kuingilia, baada ya kuhakikisha hali ni shwari akaingia akiwa na nia ya kumbana yule mrembo amweleze ukweli, yeye ni nani na alikuwepo pale kufanya nini.


Alipoingia alijikuta ametokea kwenye ukumbi mpana na msafi wa maliwato uliokuwa na masinki kadhaa ya kunawia mikono. Tunu aliyazungusha macho yake kutazama eneo lile na kuiona milango saba ya.vyumba vya maliwato. Akasubiri pale huku akiwa makini. Aliwaona wanawake wakitoka na wengine kuingia lakini yule mrembo hakumwona.


Alipochunguza vizuri akagundua kioo cha dirisha moja kilikuwa kimevunjwa. Yule msichana mrembo alikwishatoweka. Tunu hakutaka kusubiri, alitoka mbio na kuelekea ukumbini kisha akaufuata mlango mkubwa wa kutokea nje. Alishuka ngazi haraka haraka akiwa hataki kumpoteza yule mrembo. Alipotoka tu nje akagundua kuwa usiku ulikuwa umeshamiri.


Kulikuwa na giza zito lililoashiria kuwa mvua ilikuwa mbioni kunyesha tena hata hivyo kwa msaada wa taa za ule mgahawa na zile za barabarani zilizokuwa kando ya barabara kwenye nguzo ndefu, giza lile zito liligeuka mchana kwa baadhi ya sehemu.


Tunu alishangaa kutomuona yule msichana pale nje, akaamua kutoka kabisa katika eneo lile na kuvuka barabara, akaelekea upande wa pili uliotazamana na ule mgahawa, ambako kulikuwa na teksi kadhaa zimeegeshwa. Akumuona yule mrembo akiwa anatembea kwa mwendo wa haraka kama mwanamtindo aliyekuwa jukwaani katika mashindano ya urembo.


Wakati akitembea yule mrembo alikuwa anageuka kutazama nyuma mara kwa mara akionekana kuwa na wasiwasi. Muda huo alikuwa anaongea na simu. Tunu hakutaka kupoteza muda, akavuka tena ile barabara haraka na kuanza kumfuatilia kwa nyuma lakini katika namna ambayo alikuwa na uhakika kuwa asingeweza kushtukiwa.


Tunu alikuwa akijua namna ya kutembea haraka na alikuwa mwangalifu sana katika nyendo zake. Yule mrembo alikuwa takriban mita thelathini mbele yake, umbali uliomfanya Tunu aweze kujificha haraka kila yule mrembo alipokuwa akijiandaa kugeuka nyuma.


Yule mrembo alipofika mwisho wa barabara ya mtaa ule akaingia upande wa kulia akiifuata barabara nyingine ya lami iliyokuwa inakwenda kutokea barabara ya Uhuru ikikatisha katikati ya mtaa wenye migahawa na maduka kadhaa ya vyakula. Mara akasimama kwenye kioski kimoja cha vinywaji na kugeuka tena nyuma akitazama katika namna ya kujiridhisha kuwa hakukuwa na mtu yeyote aliyekuwa akimfuatilia nyuma yake. muda wote alikuwa anaongea na simu.




Aliporidhika kuwa hakukuwa na mtu nyuma yake akavuka barabara upande wa pili na wakati akifanya hivyo kuna gari dogo aina ya Toyota Verossa jeusi likatokea na kuufuata ule uelekeo wa yule mrembo. Lilisimama hatua chache pembeni na hapo yule mrembo akafungua mlango wa nyuma na kuingia ndani. Gari likaondoka kwa kasi. Lilikuwa tukio ambalo Tunu hakulitarajia.


* * * * *


Gari la Sammy lilikuwa likiyavuka machinjio ya Vingunguti katika barabara ile ya kuelekea Barakuda na kuanza kuteremsha kwenye mteremko mkali wa bonde la Mto Msimbazi, yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba akamtaka Sammy kuifuata njia nyembamba ya vumbi iliyoingia kushoto kabla hawajalivuka daraja la Mto Msimbazi. Sammy akatii, sasa wakawa wanaelekea eneo yalipo makaburi ya Vingunguti kando ya Mto Msimbazi.


Eneo lile lilikuwa kimya kabisa na mwanga eneo lile ulikuwa hafifu uliotoka kwenye taa za nyumba zilizokuwa ng’ambo ya Mto Msimbazi, mbali kidogo na eneo lile. Kiujumla eneo lile lilitisha mno kwa ukimya uliotawala. Yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba akamwelekeza Sammy eneo la kusimama.


Sammy hakubisha, alikanyaga breki na kulisimamisha gari lake eneo lile huku akimtupia jicho yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba kwa wasiwasi kidogo. Bastola yake ilikuwa bado imegusa mbavu zake.


“Zima injini, fungua mlango utoke nje na uinue mikono yako juu,” yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba aliamrisha.


Sammy alifanya kama alivyoelezwa, alizima injini ya gari lake, akachomoa ufunguo wa gari na kuushika mkononi. Lakini kabla hajafungua mlango Bob Chopa alishuka haraka na kuufuata mlango wa dereva, akashika kitasa na kuufungua huku akimtazama Sammy kwa makini kama simba jike anayewinda nyati.


Sammy alishuka na kutaka kuanza kuleta utata. Bob Chopa aliishika vyema bastola yake akiielekeza kwa Sammy, tayari kwa lolote. Wakati huo huo yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba alikuwa ameshashuka toka garini na kusimama akiielekeza bastola yake kwenye kichwa cha Sammy.


Sammy akagwaya. Alishusha pumzi huku akinyoosha mikono yake juu kama ishara ya kusalimu amri. Akaamuriwa kukaa chini akiwa ameweka mikono yake kichwani.


“Kamanda, hatuna muda wa kupoteza, pekua gari chapchap tusepe. Huyu fala niachie mimi,” Bob Chopa alimwambia yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba.


Yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba aliingia ndani ya gari, akavuta siti ya mbele ya abiria upande wa kushoto na kuinama. Akaangalia chini ya kile kiti. Patupu! Akamfuata Sammy aliyekuwa amedhibitiwa na Bob Chopa. “Umeiweka wapi?” alimuuliza Sammy huku akimkazia macho.


“Nini?” Sammy alimuuliza huku akimtazama kwa mshangao. Hakuelewa walichokuwa wanakitaka toka kwake.


“Kadi! Umeiweka wapi?” yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba akamuuliza kwa msisitizo.


“Kadi gani?” Sammy aliuliza huku akiendelea kushangaa.


“Memory card, umeiweka wapi?”


“Sijakuelewa, memory card ipi?” Sammy alizidi kushangaa.


Yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba alimtazama Sammy kwa kitambo kifupi pasipo kumjibu, kisha alirudi ndani ya gari na kuanza kufanya upekuzi wa haraka haraka kila mahali lakini akiwa makini. “Sioni kitu, huyu fala anajua alipoiweka!” alisema akionekana kukata tamaa.


Bob Chopa akiwa bado ameshika bastola yake kwa umakini alitoa simu yake ya mkononi na kubofya namba kadhaa, akaweka kwenye sikio lake na kusikiliza kidogo wakati ile simu ikiita. Muda mfupi baadaye simu ilipokelewa na upande wa pili.


“Bosi, hatujapata kitu…” Bob Chopa alisema huku akimkazia macho Sammy. Akasikiliza kwa kitambo kidogo na kubetua kichwa chake huku akitabasamu. “Okay! Nimekuelewa.” akakata simu.


“Hili gari umeanza kulimiliki lini?” Bob Chopa alimuuliza Sammy huku akiendelea kutabasamu lakini akiwa amemkazia macho.


“Kwani vipi?” Sammy aliuliza kwa mshangao huku naye akimkazia macho Bob Chopa.


“Jibu swali langu,” Bob Chopa alisema kwa ukali kidogo.


Sammy alibaki kimya akimtazama Bob Chopa kwa hasira, akili yake ilikuwa inajaribu kufanya kazi haraka haraka akijaribu kupanga namna ya kujinasua toka mikononi mwa wale watu.


“Umeanza kulimiliki lini hili gari?” Bob Chopa alirudia tena swali lake huku akimkazia macho Sammy.


“Sijui,” Sammy alijibu kwa mkato huku ghadhabu zikianza kumpanda. Donge la hasira lilikuwa limemkaba kooni na kumfanya aanze kupumua kwa shida. Aliona watu wale walikuwa wanamchelewesha kufika nyumbani kwake kuyaokoa maisha ya mtoto wake Pendo. Hakujua mtoto wake alikuwa na hali gani muda huo.


“Naona sasa anaanza kuwa jeuri,” alisema yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba na kumsogelea Sammy. Kufumba na kufumbua Sammy akawa amewekwa mtu kati na wale watu walioonekana kudhamiria kumuua. Walizishika vyema bastola zao na kumuelekea Sammy.


Sammy alitweta, ujanja wowote ule ambao angejaribu kuufanya mbele ya silaha zile ungeweza kumgharimu maisha yake kwa kuchakazwa vibaya kwa risasi jambo ambalo hakuwa tayari litokee. Hata hivyo, hakutaka kufa kibudu, aliamua kupambana. Alisimama akiwa tayari kwa lolote, aliamini kuwa hawakujua kama walikuwa wanacheza na mtu hatari ambaye hakutakiwa kufanyiwa mchezo.


Kitu alichokuwa anamshukuru Mungu mpaka wakati huo ni kumpa uwezo wa kufikiri na kufanya uamuzi sahihi na wa haraka. Ingawa hajawahi kukumbana na misukosuko mikubwa kama hiyo lakini kila alipojikuta katika sehemu hatari ambayo si rahisi kwa mtu wa kawaida kujiokoa aliweza kutumia uwezo wake wa kufikiri na kuamua kwa haraka ili kujiokoa.


Wakati wakiwa wanaangaliana kwa ghadhabu Sammy akashangaa kumwona Bob Chopa akiachia tabasamu kisha akashusha chini bastola yake.


“Tuondoke, tutatafuta namna nyingine ya kuipata,” Bob Chopa alimweleza yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba. Na hapo wakaanza kuondoka toka eneo lile wakimwacha Sammy katika mshangao.


Alisimama pale pale akiwatazama kwa makini akiwa haamini kama kweli waliamua kuondoka, alidhani ule ulikuwa mtego wao ili wapate kumdhuru lakini akashangaa kuwaona wakizidi kuyoyoma na kupotelea kizani, wala hakujua walikoelekea. Watu hawa ni akina nani? Walikuwa wanataka nini? Na nani aliyewatuma? Sammy alijiuliza bila kupata majibu.


Mambo yanazidi kunoga, usikose kuifuatilia stori hii ya kusisimua... 






Kufumba na kufumbua Sammy akawa amewekwa mtu kati na wale watu walioonekana kudhamiria kumuua. Walizishika vyema bastola zao na kumuelekea Sammy.


Sammy alitweta, ujanja wowote ule ambao angejaribu kuufanya mbele ya silaha zile ungeweza kumgharimu maisha yake kwa kuchakazwa vibaya kwa risasi jambo ambalo hakuwa tayari litokee. Hata hivyo, hakutaka kufa kibudu, alidhamiria kupambana. Alisimama akiwa tayari kwa lolote, aliamini kuwa hawakujua kama walikuwa wanacheza na mtu hatari ambaye hakutakiwa kufanyiwa mchezo.


Kitu alichokuwa anamshukuru Mungu mpaka wakati huo ni kumpa uwezo wa kufikiri na kufanya uamuzi sahihi na wa haraka. Ingawa hajawahi kukumbana na misukosuko mikubwa kama hiyo lakini kila alipojikuta katika sehemu hatari ambayo si rahisi kwa mtu wa kawaida kujiokoa aliweza kutumia uwezo wake wa kufikiri na kuamua kwa haraka ili kujiokoa.


Wakati wakiwa wanaangaliana kwa ghadhabu Sammy akashangaa kumwona Bob Chopa akiachia tabasamu kisha akashusha chini bastola yake.


“Tuondoke, tutatafuta namna nyingine ya kuipata,” Bob Chopa alimweleza yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba. Na hapo wakaanza kuondoka toka eneo lile wakimwacha Sammy katika mshangao.


Alisimama pale pale akiwatazama kwa makini akiwa haamini kama kweli waliamua kuondoka, alidhani ule ulikuwa mtego wao ili wapate kumdhuru lakini akashangaa kuwaona wakizidi kuyoyoma na kupotelea kizani, wala hakujua walikoelekea. Watu hawa ni akina nani? Walikuwa wanataka nini? Na nani aliyewatuma? Sammy alijiuliza bila kupata majibu.


ENDELEA...


Kitu kimoja tu alichokifahamu kwa wakati huo ni kwamba, eneo lile alilokuwa amesimama usiku huo halikuwa eneo salama hata kidogo, hivyo hakutakiwa kuendelea kuwepo pale. Bila kujali kama ule ulikuwa mtego au lah aliingia ndani ya gari lake na kuwasha injini kisha akaligeuza na kuondoka kwa kasi.


* * * * *


Ilikuwa inaelekea kutimia saa tano kamili usiku, gari dogo aina ya Land-Rover 110 jeupe la POLISI lilikuwa linaendeshwa kwa mwendo wa kasi mno kuelekea mtaa mmoja katika eneo la Tabata Chang’ombe, ndani ya gari lile mbele kulikuwa na askari wawili, mmoja akiwa ndiye dereva wa gari. Nyuma ya gari lile kulikuwa na askari sita waliokuwa wamebebelea bunduki na vifua vyao vimekingwa na mavazi maalumu yanayozuia risasi ‘bullet proof’. Askari hao walikuwa na sura ya kazi.


Jinsi walivyosimama nyuma ya gari lile ilionesha wazi kuwa mambo hayakuwa shwari kabisa huko walikokuwa wanaelekea.


Gari lile liliingia katika mtaa anaoishi Sammy na kupunguza mwendo baada ya kuikaribia nyumba ya Sammy, kitendo kile kikawafanya polisi watatu waruke kutoka nyuma ya lile gari katika mtindo wa kivita na kujiviringisha barabarani kama maninja kwa namna ya kuonesha kuwa kulikuwa na jambo la hatari, kisha kila mmoja akashika uelekeo wake kuizingira nyumba ile.


Mmoja alikwenda kujibanza mwanzo wa ukuta wa nyumba ya Sammy upande wa kushoto. Mwingine akakimbilia mbele ya geti kubwa la ile nyumba na kujibanza, na yule wa tatu alikwenda kujibanza kwenye kona ya ule ukuta iliyokuwa upande wa kulia. Lile gari Land-Rover 110 likaongeza mwendo na lilipofika mwisho wa mtaa ule likakata kona na kuuzunguka ule mtaa kwenda kutokea mtaa wa nyuma yake.


Kwenye ule mtaa wa nyuma lilipunguza tena mwendo na kuwaruhusu wale askari watatu waliobakia kule nyuma waruke na kujiviringisha barabarani kama maninja. Kisha lile gari Land-Rover 110 halikusimama badala yake likaongeza kasi mbele ya na kwenda kutokea tena katika mtaa lilioingilia, kisha likasimama mwisho kabisa wa ule mtaa.


Wale askari walioruka kutoka kwenye lile gari Land-Rover 110 kule mtaa wa nyuma wakaanza kuusogelea kwa tahadhari ukuta wa ile nyumba ya Sammy huku wakiwa wamezishika vyema bunduki zao mikononi. Watu wawili watatu katika mtaa ule wakaanza kujitokeza wakishangaa, wasijue kilichokuwa kinaendelea.


Dulla na Spoiler ambao walikuwa bado wanawashikilia mateka Joyce na Pendo waliisikia sauti ya gari lile nje ya nyumba lilipopita na kupunguza mwendo kisha vikafuatia vishindo vya watu walioruka. Haraka Dulla akajongea dirishani na kuchungulia nje lakini kwa sababu nyumba ilikuwa imezungukwa na ukuta hakuweza kuona mtu. Akayatega vizuri masikio yake kusikiliza kwa makini, akasikia sauti hafifu za vishindo vya watu waliokuwa wanakimbia sambamba na ukuta ulioizunguka ile nyumba.


Alishtuka sana na kumpa ishara Spoiler kuwa kulikuwa na watu nje ya nyumba kisha akatoka haraka akipitia mlango wa jikoni na kujibanza kwenye kibaraza kidogo cha upande wa jiko, akasubiri kwa dakika moja huku akiwa makini sana kuangalia eneo lote la ule uwa wa nyumba. Mara akawaona wanaume watatu walioshika bunduki na vifua vyao vimekingwa na bullet proof wakipanda ukuta haraka na kurukia ndani ya uwa bila vishindo. Dulla akashtuka sana na kurudi haraka ndani. “Askari!” alimwambia Spoiler kwa sauti ya chini huku akimwonesha vidole vitatu akimaanisha wapo watatu.


“Mafala hawa! Siwezi kukubali kukamatwa kijingajinga na hawa mabwege,” Spoiler alisema kwa hasira huku akielekea dirishani kuchungulia. Kabla hajafanikiwa kuchungulia dirishani kikatokea kitendo cha ghafla ambacho wote hawakukitegemea. Joyce alinyanyua stuli akampiga nayo Spoiler kichwani. Spoiler alianguka sakafuni huku damu zikianza kumtoka kichwani.


Wakati huo huo Joyce alimnyakua Pendo aliyekuwa amewekwa juu ya sofa na kuanza kukimbilia kule jikoni ilia toke nje lakini Dulla aliachia risasi mbili zilizompata mgongoni. Joyce akipiga yowe kubwa la maumivu na kudondoka sakafuni. Pendo aliangukia kando na kugugumia kwa maumivu. Hakuweza kutoa sauti kwa kuwa alikuwa bado amebandikwa gundi maalumu ya karatasi mdomoni.


Spoiler alinyanyuka haraka akiwa ameghadhabika sana, akatazama upande wa kushoto kwake na kulia akiwa makini, kisha akampa ishara fulani Dulla ambaye alikuwa ameshika bastola tayari kwa lolote. Kitendo bila kuchelewa, wakagawana njia, huyu akaelekea mlango wa jikoni akimruka Joyce na mwingine akaelekea mlango wa barazani.


Spoiler alielekea mlango wa barazani na kuufungua mlengo kwa tahadhari, akawaona askari wawili wakijongea kuelekea pale mlangoni kwa tahadhari, akabana pumzi na kukimbilia kwenda kuichukua ile stuli kisha akazima umeme kwenye swichi kubwa. Eneo lote la nyumba ile likawa kiza, kitendo ambacho wale askari hawakuwa wamekitegemea.


Kufumba na kufumbua Spoiler aliirusha ile stuli katikati ya wale askari wawili ambao walishtuka na kujaribu kuikwepa. Hiyo ilikuwa nafasi ambayo Spoiler alikuwa anaitarajia itokee. Alichomoka kama umeme wakati wale askari walipokuwa katika harakati za kuikwepa ile stuli na kukimbilia upande wa nyuma, akarukia juu ya ukuta wa uwa na kujirusha huku akitua salama nje. Aliusikia mvumo wa risasi zilizomkosakosa.


Alipotua chini aliangaza macho yake pande zote na hakuona mtu yeyote anayemfuatilia, akaanza kukimbia akiambaa na ule ukuta kuelekea kule walipokuwa wameacha pikipiki yao lakini akiwa na tahadhar kubwa, kisu chake kakishika mkononi tayari kwa lolote. Mara akaisikia milio ya risasi zikirindima kule ndani na muda huo huo akamshuhudia Dulla akirukia juu ya ukuta huku akijibu mashambulizi kwa kurusha risasi. Mara akapiga kelele na kuanguka chini baada ya kupigwa risasi kadhaa mgongoni.


Spoiler alishtuka sana na kugeuka nyuma yake, akamwona Dulla akiwa anagugumia kwa maumivu, mita chache tu toka pale alipokuwa amesimama, akamfuata na kumbeba kisha akakimbia naye na kumpandisha kwenye pikipiki akimlaza kifudifudi. Aliiwasha ile pikipiki na kuondoka kwa mwendo wa kasi huku akikoswakoswa na risasi. Mita therathini tu mbele yake akakutana na gari aina ya Cadillac DeVille la Sammy lililokuwa likija katika mwendo wa kasi na kuonekana likiingia upande wake.




Sammy aliiona ile pikipiki akakanyaga breki kwa nguvu, gari lake likasota na kuyumba na wakati huo huo ile pikipiki ile ilionekana kuserereka huku ikiyumba kulikwepa lile gari kisha Spoiler akaiweka sawa.


“Shit!” Spoiler alisema kwa hasira baada ya kugundua kuwa lilikuwa gari aina ya Cadillac DeVille na dereva wake ni Sammy, hata hivyo, hakuthubutu kusimama kwa kuhofia kukamatwa, aliongeza mwendo na pikipiki ikatokomea kizani huku watu wakishangaa.


* * * * *


Baada ya gari dogo aina ya Toyota Verossa jeusi kumchukua yule mrembo na kuondoka kwa kasi, Tunu hakutaka kukata tamaa mapema, alitoka mbio kukimbilia yalipo maegesho ya taxi mwisho wa mtaa ule. Dreva mmoja mjanja alikuwa amemwona Tunu tangu alipokuwa mbali akikimbilia kule, akawasha gari lake na kumfuata.


Alipomfikia alisimama na kumfungulia mlango wa mbele, “Twende zetu, sister!” yule dereva wa taxi alisema huku akimkazia macho Tunu.


“Una petroli ya kutosha?” Tunu alimuuliza yule dereva wa taxi kwa wasiwasi.


“Kwani unakwenda mbali, sister?”


“Itategemea,” Tunu alijibu huku akiingia ndani ya gari na kuketi. “Nataka ulifuate lile gari aina ya Toyota Verossa la rangi nyeusi lililoondoka maeneo haya muda mfupi uliopita.”


Yule dereva alielewa na muda uleule akayaacha yale maegesho ya teksi na kuingia barabarani akiufuata ule uelekeo wa lile gari Toyota Verossa jeusi.


“Ila naomba kuwa mwangalifu sana, wasijue kuwa wanafuatwa,” Tunu alimwonya yule dereva wakati ile taxi ikiingia katika barabara ya Uhuru kwa mwendo wa kasi.


Yule dereva wa teksi alionekana mjanja na mwerevu anayeitambua vyema kazi yake, alibetua kichwa chake kuonesha kuwa alimwelewa Tunu. Alikuwa kijana tu aliyekadiriwa kutozidi umri wa miaka therathini, alivaa suruali ya jeans rangi ya bluu na fulani nyekundu.


Katika muda ule wa usiku barabara ya Uhuru ilikuwa na msongamano wa magari, ikamlazimu yule dereva wa taxi atumie mbinu ya ziada kwa kupita pembeni hadi alipofika kwenye daraja la Malapa, jirani na kituo cha mafuta cha Lake Oil.


Alipenyapenya na kuvuka eneo la Malapa Hostel kisha akaiacha barabara ya Uhuru na kuingia upande wa kulia akiifuata barabara ya vumbi iliyopita nyuma ya makaburi ya Malapa.


“Una uhakika hawawezi kutupoteza?” Tunu aliuliza huku akionesha wasiwasi baada ya kuona dereva akipita njia nyingine.


“Sister, kwani shida yako si kulipata lile gari Toyota Verossa jeusi?” yule dereva alimuuliza Tunu, lakini akaendelea pasipo kusubiri jibu, “Toa wasiwasi, ninaijua vizuri kazi yangu.” alisema huku akiwa makini barabarani, taxi likakatiza mitaani kiasi cha kumchanganya kabisa Tunu.


Baada ya mwendo fulani wakatokea katika barabara ya Uhuru, katikia mtaa ambao ulikuwa ukitumika kama kituo cha daladala za kuelekea Muhimbili. Mara wakaliona lile gari Toyota Verossa jeusi likiwa mbele yao usawa wa ukuta wa Shule ya Msingi Hekima, eneo la Buguruni.


Muda ul ule askari wa usalama barabarani wakaanza kuyaruhusu magari yaliyopo katika barabara ya Uhuru kuvuka eneo la taa za barabarani za Buguruni. Dereva wa ile taxi aliyopanda Tunu alijitahidi kupenyapenya kwa kuyachomekea magari mawili matatu yaliyokuwa mbele yake na kujikuta akiwa nyuma ya lile gari Toyota Verossa.


Walipozivuka taa za kuongozea magari barabarani lile gari Toyota Verossa lilielekea barabara ya Mnyamani. Taxi nalo likaelekea barabara ileile ya Mnyamani wakilifuata lile gari Toyota Verossa. Hata hivyo, yule dereva wa taxi alikuwa mjanja, aliyaacha magari mawili yakawa katikati yao na lile gari Toyota Verossa.


Safari iliendelea hadi walipofika eneo la Vingunguti katika makutano ya barabara za Barakuda, Fida na ile inayokwenda kutokea barabara ya Nyerere, lile gari Toyota Verossa likanyoosha kuifuata barabara ya lami iliyokuwa inaelekea Fida. Yule dereva wa taxi naye akaifuata barabara ile akiwa nyuma huku gari moja likimtenganisha na lile Toyota Verossa.


Barabara ile haikuwa na msongamano, hivyo mwendo wao uliongezeka kidogo, wakakatiza katikati ya makazi ya watu wakikutana na kona kadhaa na hatimaye wakaanza kupita katika eneo la viwanda. Lile gari Toyota Verossa lilipofika mwisho wa barabara ile ya lami likakunja kona na kuingia kulia likiifuata barabara ya vumbi iliyoelekea eneo la Karakata.


Likaanza kushusha mteremko katika barabara ile ya vumbi likipita katikati ya makazi ya watu yenye nyumba mchanganyiko, za kawaida na za kisasa na baada ya mwendo wa dakika tano lile gari likakomea mbele ya nyumba moja kubwa ya kisasa iliyojitenga, ikiwa na uwanja mkubwa kwa mbele. Ilikuwa ni nyumba tulivu sana na mahala pa kifahari.


Ile taxi aliyopanda Tunu ilikuwa kwa mbali nayo ilikunja na kuelekea upande ule ikiifuata barabara ya vumbi na kwenda kusimama kwenye uwanja mpana wa mchanga uliokuwa mbele ya baa moja iliyokuwa inapiga muziki laini muda huo huku watu wakionekana kuburudika. Baa hiyo ilikuwa umbali wa mita mia moja toka pale ilipokuwa ile nyumba.


Tunu akamtaka dereva wake azime injini ya gari, yule dereva alikuwa mwepesi kuelewa, akafanya kama alivyoagizwa. Kisha Tunu akamuuliza kuhusu kiasi cha fedha alichokuwa anadai kama malipo ya umbali wa kutoka Ilala alikokodiwa hadi pale.


Yule dereva akamwambia kiasi cha fedha na bila kupoteza muda Tunu alimlipa na kumzidishia ili kujenga uaminifu kwa yule dereva. Yule dereva alizipokea zile fedha huku akishukuru sana. Tunu alitulia mle garini kwa muda akijaribu kulichunguza eneo lile kwa makini na mara akamwona yule mrembo akifungua mlango na kushuka toka kwenye lile gari Toyota Verossa, akaliendea geti la mbele la ile nyumba na kutoa ufungo, akafungua na kuzama ndani ya ile nyumba huku geti likifungwa haraka.


Muda huo huo lile gari Toyota Verossa likaonekana kugeuza na kuondoka likirudi lilikotoka na kuwapita kwa kasi, kisha likatokomea kizani. Tunu aliiangalia ile nyumba kwa shauku, akageuza shingo yake kumwangalia yule dereva wa taxi na kumwahidi kuwa angerudi baada ya dakika therathini ila endapo asingetokea katika muda huo basi angekuwa huru kuondoka zake.


Akiwa katikati ya udadisi na shauku alishuka toka ndani ya ile taxi, na kuanza kupiga hatua taratibu na kwa tahadhari kuelekea kwenye ile nyumba huku moyo wake ukienda mbio sana, hakuweza kuhisi nini ambacho kingemtokea mbele yake, hata hivyo, hilo halikumzuia kuendelea na harakati zake.


“Liwalo na liwe,’ Tunu aliwaza huku akizidi kujongea kwenye ile nyumba.


Sasa mambo ni ?????? kwelikweli! Kama ni gari ndiyo limeshakata breki likiwa linateremsha mteremko mkali wa Kitonga. Ili kujua kitakachoendelea usikose kufuatilia simulizi hii ya kusisimua ya 'Taxi





Tunu akamtaka dereva wake azime injini ya gari, yule dereva alikuwa mwepesi kuelewa, akafanya kama alivyoagizwa. Kisha Tunu akamuuliza kuhusu kiasi cha fedha alichokuwa anadai kama malipo ya umbali wa kutoka Ilala alikokodiwa hadi pale.


Yule dereva akamwambia kiasi cha fedha na bila kupoteza muda Tunu alimlipa na kumzidishia ili kujenga uaminifu kwa yule dereva. Yule dereva alizipokea zile fedha huku akishukuru sana. Tunu alitulia mle garini kwa muda akijaribu kulichunguza eneo lile kwa makini na mara akamwona yule mrembo akifungua mlango na kushuka toka kwenye lile gari Toyota Verossa, akaliendea geti la mbele la ile nyumba na kutoa ufungo, akafungua na kuzama ndani ya ile nyumba huku geti likifungwa haraka.


Muda huo huo lile gari Toyota Verossa likaonekana kugeuza na kuondoka likirudi lilikotoka na kuwapita kwa kasi, kisha likatokomea kizani. Tunu aliiangalia ile nyumba kwa shauku, akageuza shingo yake kumwangalia yule dereva wa taxi na kumwahidi kuwa angerudi baada ya dakika therathini ila endapo asingetokea katika muda huo basi angekuwa huru kuondoka zake.


Akiwa katikati ya udadisi na shauku alishuka toka ndani ya ile taxi, na kuanza kupiga hatua taratibu na kwa tahadhari kuelekea kwenye ile nyumba huku moyo wake ukienda mbio sana, hakuweza kuhisi nini ambacho kingemtokea mbele yake, hata hivyo, hilo halikumzuia kuendelea na harakati zake.


“Liwalo na liwe,” Tunu aliwaza huku akizidi kujongea kwenye ile nyumba.


SASA ENDELEA...


Kabla hajafika mbali akasikia sauti fulani ya tahadhari ikimwita nyuma yake, “Sister!” Alipogeuka akamwona yule dereva wa taxi iliyomleta akimjia haraka. Tunu alisimama akamtazama kwa mshangao. Yule dereva alikuwa akimjia haraka.


“Kuwa makini sana, Sister,” yule dereva alimwambia Tunu sentensi fupi yenye uzito kisha akaanza kurudi haraka kwenye gari lake. Tunu alibaini kuwa alikuwa anamaanisha anachokisema kwa namna alivyomtazama. Naye kwa kumwonesha kuwa wapo pamoja, alibetua kichwa chake kukubali kisha akaanza kuondoka.


Wakati akitembea, aligeuka tena kutazama nyuma, akamwona yule dereva akiwa ametulia kwenye gari lake lakini akiwa makini kufuatilia kule alikokuwa Tunu.


Tunu aligeuka kutazama pembeni yake, hakuweza kumwona mtu yeyote aliyemtilia shaka. Akashusha pumzi na kuendelea na safari yake bila kuonesha wasiwasi wowote akiwa kama mtu aliyekuwa anapita zake. Aliitupia jicho la wizi nyumba ile kuutathmini usalama wa eneo lile. Mwanga wa taa kubwa juu ya ukuta wa ile nyumba ulimwezesha kwa kiasi fulani kuyasoma mazingira ya eneo lile.


Aliziona kamera mbili zilizokuwa juu ya geti zenye uwezo wa kunasa picha ya kitu chochote mbele ya nyumba. Alipofika mwisho wa ule ukuta, akachepuka na kuzunguka upande wa nyuma ambako nyumba ile ilikuwa imezungukwa na miti mirefu na mikubwa ya kivuli ambayo matawi yake yalikuwa makubwa yaliyokuwa yametengeneza vichaka vilivyosababisha kiza fulani.


Alisimama kwenye kiza kwa tahadhari akaendelea kuitazama ile miti mikubwa kwa utulivu huku hisia zake zikimweleza kuwa mtu yeyote mwenye hila angeweza kujibanza nyuma ya miti ile na kuitimiza adhma yake mbaya.


Alipojiridhisha kuwa hali ilikuwa salama, akaukwea kwa tahadhari mti mmoja mkubwa na kufanikiwa kufika juu, akachungulia ndani. Akayaona mazingira mazuri ya nyumba ile. Ilikuwa nyumba ya kisasa iliyozungukwa kwa bustani nzuri ya maua na nyasi zilizokatwa vizuri. Kulikuwa na magari mawili yaliyokuwa ndani ya banda la wazi la kuegeshea magari.


Gari moja ni aina ya Mercedes Benz E-class limousine jeusi lililokuwa na milango sita na gari jingine ni Nissan Patrol jeupe. Akiwa pale juu alichagua tawi moja zuri lililokuwa limening’inia ndani ya ukuta wa ile nyumba kule nyuma ya nyumba. Alijilaza juu ya tawi lile na kuanza kusota kwa tumbo taratibu akishuka kuelekea mle ndani ya ule ukuta.


Kiza kilichosababishwa na matawi makubwa ya miti ya vivuli iliyoizunguka nyumba ile kilimpa nafasi nzuri ya kufanya mjongeo makini na wa utulivu akionekana kama kivuli kwani alitembea kwa tahadhari kubwa, akiwa na uhakika kuwa ingehitaji mtu makini sana kugundua uwepo wake.


Alifika kwenye varanda ndogo katika sehemu ya nyuma ya ile nyumba na kusimama huku macho yake yakiwa makini kuangaza huku na huko, varanda ile ilikuwa na mlango wa nyuma wa kuingilia jikoni. Aliusogelea mlango na kusimama kwa utulivu akitazama huku na kule katika namna ya kusikiliza kama angeweza kusikia kitu lakini hali bado ilikuwa ya ukimya mno.


Pembeni ya ule mlango kulikuwa na dirisha moja la sehemu ya jiko la ile nyumba upande wa kushoto. Tunu alilisogelea lile dirisha na kuchungulia ndani, japo dirisha lilikuwa limefunikwa na pazia kwa ndani lakini kupitia uwazi mdogo pembeni ya dirisha lile aliweza kuona mle ndani. Hakuona dalili ya kuwepo mtu yeyote.


Alijaribu kulifungua lile dirisha lakini hakufanikiwa kwani lile dirisha lilikuwa limefungwa ndani kwa komeo. Hakuona kama kulikuwa na namna nyingine yoyote ya kuweza kuingia mle ndani isipokuwa kuvunja sehemu ndogo ya kile kioo cha lile dirisha.


Mara akahisi uwepo wa kiumbe kingine eneo lile, akashtuka na kugeuka kutazama nyuma yake na macho yake yakakutana na macho ya yule mrembo akiwa ameshika bastola mkononi akimwelekezea. Tunu alishikwa na taharuki ambayo hakuitarajia kabisa.


Yule mrembo alikuwa bado amevaa nguo zilezile alizotoka nazo kule ELLI’S, sketi fupi nyeusi yenye miraba myeupe, blauzi nyeupe ya mikono mirefu na viatu vya flati, na alikuwa amekunja sura yake huku akimtazama Tunu kwa macho makali.


ITAENDELEA


0 comments:

Post a Comment

Blog