Search This Blog

Wednesday 22 March 2023

NITAKUUA MWENYEWE - 1

  

IMEANDIKWA NA : SULTAN UWEZO

***********************************************

Simulizi : Nitakuua Mwenyewe 

Sehemu Ya : Kwanza (1)




Robinson aliamka asubuhi na mapema kuelekea shambani akiwaacha wazazi wake wakiwa bado wamelala, lengo likiwa kwenda kumalizia kieneo kidogo ambacho walikibakiza kulima kwenye shamba lao la mihogo.


Alichukua panga lake na jembe lake begani na kuianza safari ya Kuelekea shambani.


Kutoka nyumbani mpaka shambani kwao kulikuwa na kama kilometa kumi hivi na eneo hili lilionekana kuwa na rutuba kiasi chake na walilitegemea tofauti na eneo la upande wa milimani lilikuwa na kokoto nyingi sana hivyo halikuwa rafiki kwa kilimo.


Eneo la mzee Kaaya halikuwa kubwa sana ni kama viplot vitatu tu.


Alipofika shambani alianza moja kwa moja kulima eneo lile, ilipotimia saa nne asubuhi jua lilikuwa kali hivyo kumfanya aache kulima na Kuelekea bondeni ambako kulikuwa na kijito kidogo lakini kilichotiririsha maji mwaka mzima.


Alivua nguo zake na kuanza kuoga kwa kuogelea kwenye kisehemu ambacho maji hujikusanya na kuwa kama kibwawa hivi, aliogelea na alipomaliza alivaa nguo zake na kuondoka zake lakini akiwa njiani aliamua Kupitia kwenye migomba ili akatafute ndizi zilizoiva walau atulize njaa ambayo tayari ilikuwa imeanza kuchukua nafasi.


Aliizunguka migomba yote lakini hakukuwa na dalili yoyote ya uwepo hata wa chembe moja ya ndizi, alijilaumu sana.

"Ona sasa migomba yote hii inakosaje ndizi?"


Baada kujiridhisha kuwa hakukuwa na ndizi aliondoka zake kurudi shambani.


"Kwa njaa hii sijui nitafanikisha kumaliza eneo lililobaki." Alijisemea mwenyewe.

Mungu ni mwema alimaliza kulima kisehemu kile na kuchukua zana zake na kurejea nyumbani.


"Habari yako kaka!"


Ilikuwa ni salamu iliyomshtua Robinson akiwa njiani kurudi nyumbani. Aligeuka na kumuangalia aliyetoa salamu hiyo.

Alikutana na sura ya mtoto wa kike mrembo mwenye wingi wa tabasamu usoni.

Robinson aliangaza huku na kule kujua dada huyu katokea wapi na kama ni nyuma yake mbona alipokuwa anaingia kwenye barabara hiyo hakuona mtu.


"Kaka vipi nimekusalimia mbona hujibu?" Mrembo huyo aliuliza baada ya kuona Robinson hajibu salamu yake.

Na swali hili lilimtoa mawazoni.


"Salama dada, samahani kwa kuchelewa kujibu salamu yako nadhani ni uchovu tu." Alitetea.


"OK, naitwa Jackline." Mrembo huyu alijitambulisha.


"Naitwa Robinson."


"Nafurahi kukufahamu Robby."


"Siyo Robby, naitwa Robinson dada."


"Aah ok Robinson."


"Samahani Robinson naomba msaada wako, Gari langu limenizimia pale bondeni nimetoka mjini nilikuwa naelekea kijijini kwa mzee Fikirini na kabla sijafika mafuta yameniishia."


"Du pole sana, nakusaidiaje dada yangu?"


"Naomba msaada wa mafuta kijijini."


"Ni mbali sana kutoka hapa mpaka kijijini,lakini ngoja nijaribu."


"Asante sana kaka yangu, ngoja nikupe hela ila kidumu utaomba huko huko."


"Bila shaka, so wewe unabaki huku huku?"


"Inabidi nibaki mpaka utakaporudi ila utanikuta ndani ya gari."


"OK, basi ngoja niwahi."


Robinson alikimbia haraka kufuata mafuta ya gari la mgeni wake. Alishika vizuri panga na jembe ili visiweze kumkwaza kwa mbio zake. Aliwaza sana juu ya yule binti,


"Inakuwaje mrembo kama yule anatembea porini peke anajiamini nini? "


Ndani ya muda mfupi alikuwa nyumbani kwao akiweka zana zake za kazi na kisha kuingia kwenye kichumba cha kutunzia vyombo na kuchukua kidumu cha lita 5 na kutoka mbio.


"Robinson, Robinson." Mama yake aliita baada ya kumuona yuko juu juu na ghafla akitoka na kidumu. Lakini alikuwa kuchelewa kwani tayari alikuwa akikata kona ya mtaa wa tatu.


"Sijui anaharakia wapi mtoto huyu chakula chenyewe hajala." Aliwaza mama yake.


Alifika na kumuomba muuza petroli pale vibandani ampimie ya lita 5 kwani anaharaka sana.


"Samahani kaka nifanyie haraka niwahi ninasafari ya mbali." Aliongea Robinson.


"OK, dakika chache tu mdogo wangu."


Baada ya kulipa na kuridishiwa chenji yake alichukua dumu lile na kuanza kuondoka kwa kasi yake Kuelekea kule porini. Japo jua lilikuwa kali halikumzuia kutembea haraka ili kumuwahi mgeni wake akiamini binti kama yule kukaa porini kwa muda mrefu ni hatari.

Alifika na kumkuta Jackline akiwa kalala fofofo akiwa kalaza kiti cha mbele lakini kioo akiwa kakishusha.


"Jackline, Jackline, Jackline."

Alimuamsha kwa dakika kadhaa ndipo aliposhtuka kutoka usingizini.


"Niache Siyo mimi, siyo mimi."


"Siyo wewe nini Jackline?"


"Oogh sorry Robby, nilikuwa naota ndoto ya ajabu sana. Umeenda haraka sana ee mara hii au siyo mbali."

Jackline alijibu kwa swali.


"Sema njia yenyewe nimeizoea sana."


"Aisee, uko fasta sana Robinson."


Baada ya kuweka mafuta aliiwasha gari ikawaka, Jackline alifurahi sana kuona gari imekubali kusonga mbele.


"Robinson panda twende zetu hapa imepona."

Aliongea Jackline.


Robinson alipanda gari hiyo aina ya Honda na safari Kuelekea kijijini ilianza.


"Unatelemkia wapi Robinson." Aliuliza Jackline.


"Kwenye ile nyumba ya yenye bati kuu kuu."


"Ndo kwenu pale ee."


"Hapana, nyuma ya ile nyumba."


"Ok, nitafika nipafahamu."


"Karibu sana dada Jackline."


"Usijali."


Gari ilisogea taratibu kabisa na ikaacha Njia na kuelekea chini ya mti mkubwa wa mwarobaini uliokuwa nje ya nyumba yenye bati kuu kuu na kupaki. Jackline aliteremka kwa madaha na Kuelekea upande ule wa kushoto na kumfungulia Robinson mlango si unajua tena "MASHIKORO MAGHENI" kisha akalock milango na kumfuata Robinson.


"Twende zetu Robby." Aliongea Jackline.


"Njia ni huku kwenye hiki kiuchochoro."


"Ok."


Walitembea Kuelekea kwenye kiuchochoro hicho huku Robinson akiongoza njia.

Jackline aliwaacha watu wa mtaani hapo kuacha kazi zao na kumkodolea macho Robinson na mgeni wake huku wakimkazia macho zaidi Jackline kutokana na mavazi ambayo aliyavaa.


"We mama umemuona yule dada."


"Jamani jamani, sasa ndiyo nguo gani zile yaani suruwale imembana vile akitaka kuivua anafanyaje mwe." Aliongea mama huyu aliyepigwa butwaa.


"Hivi hata chooni anaendaga kweli maana kule nyuma nako kaaa!" Alichombeza mama mwingine aliyekuwa akitokea kuchota maji.


"We mama Joi hivi huyu binti ndiyo mke wa Robinson?" Aliuliza Mama muuza nyanya.


"Atambe na umaskini alionao atamuoa nani, mtoto wa mama Mashaka mwenyewe alimshinda kwenye uchumba tu baada ya kutajiwa ng'ombe watatu sembuse huyu mkanyaga lami?" Alijibu mama Joyce.


Robinson na mgeni wake walikata mtaa na hatimaye kufika nyumbani kwa kina Robinson.


" Karibu sana Jackline hapa ndo nyumbani."


"Ooh Asante Robinson ni pazuri." Alijibu Jackline.


Robinson aliingia ndani na kutoka na kiti kidogo cha miguu mitatu maarufu kama KIGODA na kumkabidhi mgeni wake, kisha kuingia tena ndani.


"Mama, mama!"


"Rabeka mwanangu, hivi ulikuwa unakimbilia wapi muda ule nakuita."


"Shikamoo mama."


"Marhaba, jibu swali langu kwanza."


"Mama nitakujibu tu lakini kwa muda huu njoo huku nje kuna mgeni."


"Katokea wapi?"


"Utajua hapo hapo nje."


Walitoka nje na kumkuta mgeni ambaye alionekana ni mgeni kijijini hapo.


"Mama Shikamoo." Alisalimia Jackline.


"Marahaba mwanangu, karibu kwetuu."


"Asante mama."


"Mama, huyu ni Jackline anatokea mjini kaja hapa kijijini kwetu na huyu ndie aliniomba nije huku kumnunulia mafuta ya petrol kwa ajili ya Gari lake ambalo liliishiwa."


"Aaa karibu sana mwanangu."


"Asante mama."


"Robinson au ndiye mkwe wangu nini maana nyinyi vijana mhh."


"Hapana mama nilikutana naye tu kule shambani."


Baada ya kutambulishana huko Jackline aliomba aende kwani bado anakasafari kidogo kwani alikuwa akielekea mwisho wa kijiji.


"Mama naomba mniruhusu niende, maana bado nina kasafari kidogo."


"Si usubiri baba yako aje umsalimie na umfahamu?"


"Wakati mwingine mama yangu nitamuona tu." Aliongea huku akiingiza mkono ndani ya pochi yake na kutoa noti tatu za elfu kumi. Na kumkabidhi mama Robinson.


"Asante Sana mwanangu Mungu akubaliki weweee."


"Kidogo mama."


"Karibu sana dada Jackline."


"Usijali Robinson."


Baada ya hapo walimsindikiza mgeni wao mpaka kwenye gari lake na kufungua mlango na kuingia ndani. Aliwasha gari na kulisogeza barabarani na kulipaki na kumwita Robinson.


"Hii ni namba yangu ya simu tusipoonana utanitafuta kwa mawasiliano. Na hii itakusaidia kwa mishe za hapa na pale."


"Asante sana nashukuru!"


Kisha gari liliondolewa kwa kasi na kutokomea. Huku nyuma Robinson hakuamini alichokiona mkononi mwake kwani alikuwa na kitita cha shillingi elfu sabini. Mama Robinson alimfuata mtoto wake na kumwambia kitu hiki.


ALIMWAMBIA NINI MTOTO WAKE, NA JACKLINE ANAELEKEA WAPI?

UNGANA NAMI KATIKA SEHEMU INAYOFUATA.



Mzee Fikirini alifurahi sana kumuona binti yake Jackline tena ambaye waliachana kwa kipindi cha miaka ishirini na tano.


Jackline ni mtoto wa kaka yake mzee Fikirini ambaye alijulikana kwa jina la Joachim. Joachim na mke wake walifariki muda mrefu sana katika ajali ya gari ambayo ilitokea katika mlima Sekenke mkoani Singida walipokuwa katika ziara ya mapumziko katika kisiwa cha Ukerewe na katika ajali hiyo alinusurika binti yao wa pekee Jackline, ambaye baada ya taratibu zote kufuatwa alikabidhiwa mzee Fikirini kipindi hicho Jackline alikuwa na umri wa mwaka mmoja tu.


Kutokana na urafiki uliopitiliza baina ya mzee Joachim na mzee Jonathan Ubao. Ilibidi mzee Jonathan Ubao amuombe Jackline kutoka kwa mzee Fikirini ili akaishi naye nyumbani kwake mkoani Tabora ikiwa ni pamoja na kumpatia mahitaji yake ya muhimu kama vile Elimu kama asante yake kwa rafiki yake Joachim kwa msaada ambao alimsaidia kipindi alichokuwa amefirisika.


Mzee Joachim alimsaidia kiasi cha shilingi milioni nne ili imsaidie kumrudisha kwenye mstari, na hapo ndipo alipoamua kufanya biashara ya mazao hasa mchele ambapo alikuwa akinunua mpunga kutoka wilaya za Nzega na Igunga na kisha kukoboa na mchele kuusafirisha mpaka mkoani Singida ambako aliwauzia wafanyabiashara kutoka Arusha na Zanzibar kwa bei ya jumla. Biashara hii ilimfanya kuwa maarufu ndani ya miaka miwili, kwani kwa kipindi hicho cha miaka miwili tayari alikuwa na mtaji uliofikia milioni 30 kwa kipindi hicho na kumfanya kuwa na mashine yake ya kukoboa mpunga mkoani Singida.


Hii ilimrudisha kwa rafiki yake Joachim na kumshukuru kwa msaada wake na hakusita kumfahamisha maendeleo ya biashara zake.

Miaka kadhaa baadaye alisikitishwa na taarifa ambazo zilimfikia juu ya ajali mbaya ya rafiki yake. Ilimuuma sana Mr. Jonathan kutokana na maisha ambayo waliyapitia yeye na rafiki yake na mpaka kufikia hatua ya Kupokea msaada wa shilingi milioni nne kama mtaji na sasa alikuwa milionea.


Hivyo jukumu lake baada ya kukamilisha shughuli za mazishi ya mzee Joachim na mkewe ikabidi achukue jukumu la kumlea Jackline na kumsomesha mpaka pale atakapofikia. Na hilo ndilo alilifanya kwa Moyo wake wote.


Na leo hii binti huyu alikuwa kwenye ardhi ya baba yake mdogo mzee Fikirini pale kijijini Lupa Wilayani Chunya ambako mzee huyu alijishughulisha na kilimo cha mihogo, ndizi, mahindi pamoja na zao la Tumbaku ambalo kwa wakati huu wakulima walilazimika kutumia mtaji na hii iliwafanya wengi washindwe kulimudu zao hili na kuegemea kwenye mazao mengine na kuwaacha wakina Fikirini wakipambana na zao hilo kwa Kupitia migongo ya wakulima wakubwa pale kijijini.


"Hivi ni wewe mwanangu Jackline kweli?" Aliuliza mzee Fikirini.


"Baba ni mimi ndiye, kwani vipi?"

Alijibu Jackline.


"Yaani bado siamini kama ni wewe maana ni muda mrefu sana."


"Ni kweli kabisa baba lakini ramani uliyokuwa umenielekeza kuanzia pale madukani haikunisumbua sana japo nilipokuwa nimekaribia maeneo yale ya Kaea kwa chini kabla ya kuvuka daraja lile dogo mafuta yaliniishia, lakini nimshukuru sana yule kijana anaitwa Robinson alinisaidia sana."


"Aaa yule kijana nampenda sana kwa tabia yake, ni mtulivu, mwelewa, asiye na majivuno kama wenzake waliopo mtaani hapa. Kwanza bidii yake shambani wee acha tu mzee Kaaya kalamba dume."


Maneno yale ya mzee Fikirini yalipenya vilivyo masikioni mwa Jackline na kumfanya afikirie kuendelea kumfuatilia zaidi huyu Robinson.


Mbali na hayo lakini Jackline alimsimulia baba yake safari nzima ya kimasomo pale Tabora mpaka mkoani Tanga na kisha nchini Afrika Kusini.


Kifupi baada ya kumaliza shule ya msingi alijiunga na Sekondari ya Nanga iliyoko Wilayani Igunga na baadaye kujiunga na Sekondari ya juu ya Umoja iliyo karibu kama kilometa kadhaa kutoka Kijiji cha Ndala-Nzega kwa elimu ya kidato cha tano na Sita.


Kwa kuwa shule ile ya Umoja ni ya kidini iliweza kuwadhamini wanafunzi ambao walifanya vizuri kwenye mitihani ya mwisho kidato cha Sita na Jackline akiwemo kwa elimu ya juu ya Chuo Kikuu na hapo ndipo Jackline alipata nafasi ya kuingia ndani ya Chuo Kikuu cha Soweto nchini Afrika ya Kusini.


"Kwa hiyo huko Afrika ya Kusini uliwahi kuonana na Mandela mwanangu." mzee Fikirini Aliuliza.


"Halafu na wewe baba bwana, kwani wewe mpaka umefika umri huo ni raisi gani wa Tanzania umewahi kuonana nae?"


"Mhh, tuachane na stori hizo za Mandela, maisha yalikuwaje kuanzia kwa mzee Jonathan mpaka Chuoni Afrika ya Kusini?"


"Kwanza kabla ya yote mama na wadogo zangu wako wapi baba, maana toka nimefika sijawaona."


"Mama yako yuko msibani sehemu moja umeipita inaitwa Bitimanyanga kuna rafiki yake alihamia huko miaka kadhaa nyuma ndo ambaye kafariki juzi baada ya kupigwa na radi akiwa shambani kwenye Matumbaku yetu haya, na mdogo wako Shamimu anasoma kidato cha tatu hapa hapa Lupa Sekondari na kaka yako Athuman anaishi jijini Mbeya akifanya biashara ya mitumba huko."


Wakati baba na mwana wakiendelea na mazungumzo baada ya kuachana kwa muda mrefu wakati huo wakiwa Wilayani Manyoni kabla ya mzee huyo kuhamishia makazi yake kijijini hapo. Alifika Shamimu kutoka shule na ndipo mzee Fikirini alipomtambulisha kwa Jackline na baada ya utambulisho huo Jackline na Shamimu walikumbatiana kwa furaha.


***


"Baba Robinson yaani Leo mwanetu katuletea neema hapa acha kabisa yaani toto tulizaaa."


"Mbona sikuelewi mke wangu kuna nini tena kuhusiana na hiyo neema?"


"Leo nikiwa nawaza hili na hili juu ya nini tutapika jioni hii, mara Robinson huyo kaongozana na mgeni wake, mgeni mwenyewe toto, toto kweli baba Robinson sijui walikitana wapi huko mimi nikajua ni mkwe wangu kumbe la hasha ni mtoto wa mzee wa kule juu uwanja wa ndege kwa mzee Fikirini."


"Mzee Fikirini, mtoto gani mbona huyu Shamimu bado anasoma hapa hapa Lupa ni nani huyo?"


"Mhh, we Robinson yule binti uliyekuja nae jina lake nani?"


"Anaitwa Jackline mama."


"Basi huyo ni mgeni wao tu kutoka mjini huko." Aliongea mzee Kaaya.


"Inawezekana lakini yote kwa yote mume wangu alichotufanyia yule binti acha tu mimi minoti, mwanao minoti yaani wiki hii ni mwendo wa kunikia msosi wa maana."


"Pendeni vya bure na mwanao angalieni mtaolewa ooh." Maneno ya mzee Kaaya.


"Yule si mwanamke? atatuoaje mimi na mwanangu labda mwanao Robinson. Na mwanangu ukifanikiwa kuwa na yule binti Hatareee tutanuka minoti na mihogo atabaki analima baba yako sisi wengine tunabadili magari tu."


"Wee nani alime mihogo peke yake na mimi si nitahama kutoka komoni mpaka bia."


Hizo zilikuwa ni tambo za Hawa wazazi wa Robinson iwapo angebahatika kuoana na Jackline na hatujui iwapo hilo litatokea kwenye hizi familia mbili.


***


Shamimu alikuwa na furaha kubwa wikendi hii baada ya dada yake kumbeba ndani ya gari yake na Kuelekea mjini Makongolosi kwa ajili ya kwenda kufanya manunuzi, wakiwa sheli ya mafuta wanajaza mafuta akatokea Robinson akiwa na rafiki yake kuja kununua petrol ya bodaboda ya rafiki huyo Awadh tayari kwa safari Kuelekea Mpirani Isangawana.


"Robby."


Robinson aligeuka kuangalia sauti ilitokea wapi lakini alipoangalia pembeni akawa ameifahamu ile gari, akakumbuka siku moja iliyopita gari ile aliipanda. Akiwa bado anaendelea kuishangaa ndipo mlango wa gari ile ulifunguliwa na msichana aliyechanua vilivyo akashuka na kuwafuata pale walipokuwa wamesimama.


"Mambo Robby!"


"Poa Jackline, hivi hapa nilikuwa naangalia anayeniita ni nani?"


"Ni mimi bwana."


"OK, kutana na rafiki yangu Awadh."


"Mambo Awadh, na ninafurahi kukufahamu."


"Awadh, huyu ni rafiki yangu anaitwa Jackline nimekutana naye jana kule Kaea baada ya gari yake kukata Wese."


"OK, Jackline karibu sana Lupa."


"Nishafika Awadh."


"Wapi sasa Jackline muda huu."


"Na ndo maana nimekufuata nilipokuona hapa, naelekea Makongolosi niko na mdogo wangu Shamimu lakini Njia yeye anadai haifahamu vizuri unaonaje ukaungana nasi kwenye hii safari utupe kampani!" Aliomba Jackline.


"Mbona sisi tun.......!


"Mbona nini si umsindikize Jackline bwana kwani kule unakwenda kucheza wewe, mpira tuachie sisi Robby." Awadh alimkatisha Robinson.


Hakuwa na jinsi zaidi ya kumkubalia Jackline ombi lake lakini kwa sharti la kwenda kwanza nyumbani kwao akaombe ruhusa. Hilo halikuwa Shida sana kwa Jackline alikubali na kuingia kwenye usukani na kugeuza gari Kuelekea maeneo ya misheni ya Lupa kwa nyuma ambako ndiyo nyumbani kwa kina Robinson.

Kutokana na hili Awadh Ilibidi aondoke peke yake Kuelekea mpirani.


"Sijaamini kama baba anaweza kuniruhusu kirahisi rahisi namna ile maana wazazi wangu ni watata balaa." Aliongea Robinson.


"Wanakupenda na ndiyo maana wanakuchunga sana, na hii imekufanya kuwa kivutio kwa kila mzazi pale kijijini."


"Kivutio namna gani Jack."


"Si ni upole na utulivu ulionao bwana. Kila mzazi anakusifia kwa hilo."


"Sasa ushaanza kuwa muongo, wewe umefika jana tu umeyajuaje haya?"


"Tukiwa njiani tukitokea nyumbani kuna sehemu ina kiduka tukiwa pale niliwasikia wazee fulani wakikujadili."


"Hata mimi niliwasikia dada, halafu wao wanadhani wewe dada ni mke wa Robinson." Aliongeza Shamimu.


"Mhhh." Robinson aliguna tu.


"Vipi Robby mbona unaguna kwani uongo mimi siyo mke wako?"


"Nitaanzia wapi mtoto wa mzee Kaaya na umaskini wetu."


"Usiseme hivyo Robby huwezi jua Mungu kaandaa nini mbele yako."


Safari iliendelea kuwa nzuri ndani ya hii gari ambayo tayari ilikuwa inaichungulia Makongolosi na safari ilikuwa fupi kutokana na utani wa hapa na pale na hapa ndipo Jackline alipogundua kuwa Robinson ni muongeaji sana.

Na kimoyomoyo akajisemea mwenyewe.


"Lazima nitampata tu Robinson."


Safari yao ikaishia nje ya geti la Hotel maarufu mjini Makongolosi inayojulikana kama PM HOTEL na kupaki gari nje ya hotel hiyo na kutelemka.


Waliposhuka aliwaongoza Robinson na Shamimu Kuelekea ndani ya hotel hiyo kutokana na ugeni uliokuwa umejionesha mbele yake. Wakaongoza mpaka kwenye moja ya mwamvuli na kukaa.


Mhudumu mmoja wa hotel hiyo aliwafuata wateja wake.


"Habari zenu, naitwa Magreth ni Mhudumu ndani ya hotel hii. Karibuni niwahudumie." Aliongea hayo na kuonesha kitambulisho chake kisha akawakabidhi menyu.


"Ok, tunashukuru kwa utambulisho wako ngoja tuipitie menyu hii kisha tutakuita dada eee." Jackline alimjibu.


Wakati hayo yote yakiendelea upande wa Robinson na Shamimu ilikuwa ni giza totoro hawakujua chochote kilichokuwa kikiendelea pale.


"Hii karatasi ina huduma zote zinazopatikana hapa kuanzia Chakula mpaka kulala, hivyo kila mmoja aangalie kinachomfaa kuweka tumboni."


Aliongea Jackline akimkabidhi Robinson ile menyu.


"Vitu vya wazungu hivi mimi sijavizoea hata kidogo, mimi naomba waniletee Wali maharage. Alijibu Robinson.


" Dada si uagize tu chochote kinachotufaa hapa badala ya haya makaratasi. "

Majibu ya Shamimu yaliwafanya wote waangue kicheko.


" Ni kweli kabisa Shamimu." Alijazia Robinson.


"Acheni hizo nyie chagueni vyakula ohh." Jackline aliongea akisimama na kumfuata Magreth.


Huku nyuma Shamimu na Robinson waliendelea kuchekana kutokana na kushindwa kuagiza vyakula walivyoambiwa waagize.


"Mbona hata wewe umechemka bwana usinishushue hapa." Shamimu alimwambia Robinson.


"Mimi hata Sekondari sijagusa ni kweli nina kaushamba, sasa wewe mwenzangu msomi kabisa." Alisema Robinson.


"Bwana ee kwenye misosi hakuna cha usomi wala nini, wote hollaaaaa."


"Ila dogo tumetia aibu balaa." Aliongea Robinson.


"Bwana eee." Maneno ya Shamimu.


"Halafu nimekumbuka, hebu weka namba yako ya simu hapa kwenye kimeo changu." Aliongea Robinson.


"Mambo ya namba yameanza hapa Mhhh usiharibu hali ya hewa Robby."


"Usihofu ni kwa ajili ya kuchati tu."


"Maana nikimuangalia dada ni kama tayari kakufia kifuani tayari."


"Acha hizo amekuambia?"


"Dalili zinaonekana tu."


Shamimu alirudisha simu haraka baada ya kumuona dada yake anarejea kuungana nao pale mezani.

Muda mfupi Magreth alifika akiwa na kuku watatu waliokwa vizuri na chupa kubwa ya soda aina ya koka kola. Hali ile iliwaacha macho kodo Robinson na Shamimu.


" Mbona mnashangaa si mlinipa kazi, kazi kwenu kuendeleza umafya kwenye hao kuku."

Aliongea Jackline.


"Kwa kweli, umetuweza na sisi ngoja tukuoneshe kazi ya mdomo." Aliweka utani Shamimu.


"Jamani baada ya kula tutaelekea kule madukani kila mmoja akang'ae kimjini mjini mnasemaje?"

Aliuliza Jackline.


"Si la kuuliza hilo dada." Alijibu Shamimu.


"Mimi mtanikuta hapa hapa naangalia televisheni." Aliongea Robinson.


"Kwa ajili ya nini, utanikwaza Robby.Hii safari tuko wangapi?"


"Robinson acha kumkwaza dada ndo nini sasa si ungebaki Lupa." Aliongea Sh


amimu kuonesha nae kutofurahishwa na kauli ya Robinson.


"Naombeni mnisamehe kama nimewakwaza jamani."


"Ok, ila siyo vizuri kujitenga tenga wakati tumekuja Pamoja."

Aliongea Jackline akionekana kukubali kumsamehe Robinson.


Waliendelea kukishambulia Chakula kile huku Robinson akiwa anawachekesha pale mezani.


"Niwe mkweli tu, toka kuzaliwa kwangu mwenzenu sikuwahi kula mkuku mzima kama leo da Asante sana mgeni kwa kuja."


Wote waliangua kicheko mpaka kupelekea Shamimu kupaliwa na soda iliyohama njia na kutokea puani.


"Robinson utasababisha Matatizo hapa bwana aaa." Aliongea Jackline.


"Hata yeye Shamimu kashindwa kuongea tu ni mwenzangu tu na ndiyo maana kakutwa na tukio hilo."

Aliongeza Robinson.


Kauli ile ya Robinson ilimkwaza sana Shamimu na kuondoka kwa hasira akitoka nje ya hotel.


"Unaona sasa Maneno yako Robinson."


"Naomba mnisamehe jamani ilikuwa ni utani tu na sikujua kama nitamkwaza mtu." Alijitetea Robinson.


Aliinuka Robinson na kumfukuzia Shamimu kule nje na kumkuta akiwa katulia kwenye viunga vya nje. Alimsogelea na kumuomba msamaha.


***


"Pole na yote mke wangu kuanzia msibani na njiani pia." Aliongea Mzee Fikirini


"Asante sana mume wangu, namshukuru Mungu tumesafiri salama mpaka kufika salama."

Alijibu mama Shamimu.


"Ni jambo la kumshukuru Mungu mke wangu."


"Ni kweli kabisa."


Mzee Fikirini alimsimulia mke wake ujio wa mtoto wa marehemu kaka yake Jackline. Na kueleza namna alivyokuwa mkubwa.


"Unasema kweli mume wangu kuwa Jackline kaja??"


"Amini sasa kaja na mimi nilishikwa na mshangao kama wewe mke wangu."


"Kama ndoto Vile jamani."


"Kafika hapa na gari lake mizawadi kibao iko jikoni huko yaani ndani ya muda mfupi tumekuwa wengine kabisa."


"Kaja na gari?"


"Basi ana mihela huyo Jackline ee."


"Unashangaa gari wakati mwenzako alikuwa anaishi Afrika ya Kusini wee."


"Haa, ndio kile kipindi ulichokuwa humpati kwenye simu na kwanini mzee Jonathan alikuficha."


"Tuache hayo kikubwa amerudi nyumbani."


"Yuko wapi sasa."


"Wameelekea Makongolosi na mdogo wake kuna vitu amefuatilia huko sijui vitu gani hivyo."


"Waangalie wasijeibiwa gari lao."


"Hawawezi bwana."


Mama Shamimu aliingia jikoni kwa ajili ya maandalizi ya Chakula cha jioni. Alipofika huko jikoni vitu alivyokutana navyo hakuamini macho yake kwani baada ya kukuta mchele, Viazi, Ndizi, sukari, Chumvi, mafuta ya kupikia na vingine vingi.


" We baba Shamimu mavitu yooote haya si tutafungua duka sisi."


"Unashangaa hivyo njoo uchukue begi lako la manguo."


Alipokabidhiwa lile begi la nguo alipigwa na mshangao kwa alichokutana nacho ndani yake maana kulikuwa na kila aina ya nguo ya mwanamke kuanzia za ndani na hata nyingine nyingi kama Vile vitenge, kanga na Waksi za kutosha hakika ilikuwa furaha ndani ya nyumba hii.


Tukutane katika sehemu ifuatayo kujua safari ya Jackline, Robinson na Shamimu kule MAKONGOLOSI.




"We baba Shamimu nakuomba huku ndani mara moja."


"Nakuja mke wangu ngoja niondoe gogo hili njiani."


"Utaliondoa tu mume si mazungumzo marefu sana bwana."


"Ok, nambie mke wangu."


"Mhhh, mzee Fikirini utasimameje mlangoni utafikiri unafukuzwa ingia bwana uketi kitako hapa kwenye kiti."


"Haya bwana nishaketi hivyo, lete nongwa."


"Wala si nongwa bwana bali ni mazungumzo juu ya huyu mtoto wetu wa kumlea Jackline."


"Enhee, kafanya nini tena Jackline?"


"Nisikilize basi mbona unamshawasha mapema hivyo."


"Haya endelea mke wangu."


"Kama unavyojua mume wangu maisha yetu yalivyo na umaskini huu...."


"Ndiyo najua mke wangu."


"Nikiangalia naona kabisa mwisho wa tabu umefika ni muda wa kuponda raha sasa, si unakumbuka dokomendi za Mali ya marehemu kaka yako mzee Joachim unazo wewe na zilikuwa zinamngoja mwanae Jackline akue ndipo umkabidhi nyaraka zote na utajiri uwe mikononi mwake na sisi kubaki mafukara wa kutupwa mume wangu."


Maneno ya mke wake yaligonga ngoma za masikio yake mzee wa watu lakini ni kama hakujua mke wake alimaanisha nini kwa kauli ile na kujikuta akimuuliza swali.


"Unamaana gani mke wangu kwa maelezo hayo."


"Nina maana gani tena mume wangu? Chemsha kichwa hicho wewe ni mwanaume hodari sana nakumbuka miaka ile ulipokuwa ukinitafuta uliamua kumwaga damu ya Hassan aliyekuwa akishindana nawe kunitafuta mrembo mimi. Nitashangaa kwenye hii vita ya kitoto kama itakushinda."


"Unamaanisha kuitoa roho ya Jackline ili tubaki na Mali zote mke wangu?"


"Kumbe nini sasa, unamuonea huruma umemzaa yule? Waliyemzaa wanamsubiri huko waliko."


"Mmhh, mke wangu Jambo ni kubwa hebu nipe muda wa kulifikiria mara mbili."


"Nakupa siku mbili tu kila kitu kiwe saaafi, nimemaliza unaweza kwenda mimi niendelee na mapishi."


"Sawa mke wangu."


Maneno yale yalimtoa jasho hasa ukizingatia hakutegemea kuyasikia maneno kutoka kwenye kinywa cha mke wake. Hii ilimfanya alipofika nje alijikuta jasho jembamba likimtembea Mwilini mwake. Aligeuka na kumwangalia mke wake aliyekuwa bize jikoni akiendelea kuandaa Chakula huku karoho kake kakiwa kwatuu.


"Hivi mke wangu karogwa au kalishwa maneno mazito kama haya. Eti nimuue Jackline eti kisa mali mmhh kweli mbele ya pesa hakuna mwenye roho safi." Alijisemea mzee Fikirini.


Mzee Fikirini aliondoka na Kuelekea kilabuni angalau akapumzike kwa kuungana na wazee wenzake kwenye unywaji wa pombe ya asali wenyewe wakiita WANZUKI, pombe iliyotengenezwa kwa kutumia asali ya nyuki wakubwa au Sukari na kwa wenyeji wa eneo hili la Lupa na viunga vyake wanaipenda sana pombe hii ambayo huhifadhiwa ndani ya chupa za soda.


***


Baada ya kufanya manunuzi ya nguo zao ndani ya maduka ya nguo Makongolosi walirudi kwenye gari lao pale PM HOTEL na kuziweka ndani gari. Hakika hii ilikuwa ni siku nzuri sana kwa Robinson na Shamimu kwa shopping ya NGUVU waliyofanyiwa na Jackline ambaye muda wote alikuwa akichati na simu yake janja.

Watu waliokuwa wanawafuatilia walibaki kuwashangaa kwa namna walivyokuwa wakifanya matanuzi, na mbaya zaidi hawakujua hawa vijana wametokea wapi.


"Mengo umewaona watoto hao?" Alijikuta kijana mmoja akiropoka.


"Aise lile jamaa sijui linawamiliki hawa watoto? Kama ni wake zake daa mshikaji namuonea wivu sana maana warembo wameumbika Hatareee." Alijazia Mengo.


"Hebu mcheki yule twiga alivyofungasha, mtoto mkali yule daa mimi mpaka natamani niwateke wote." Aliongea yule kijana.


"Halafu mbona sura zao ni ngeni hapa mjini, wametokea wapi?" Aliuliza Mengo.


"Warembo wa taipu hizi hutokea sana Mkwajuni si unajua kule ni kiwanda cha kutengenezea watoto wazuri." Aliendelea kuwasifia yule kijana.


Walipohakikisha kila kitu kiko Sawa waliingia ndani ya gari tayari kwa kuianza safari ya Kuelekea Lupa. Jackline alikaa nyuma ya usukani na kuuzungusha na kuigeuza kwa kasi ikatimua vumbi jingi na kusimama kama mita tano mbele.


"Wee, weee fyuuuuuu bado hawajaona dada rudia tenaaaaaaa wakuoneeeee." Zilikuwa ni kelele na ndulu za Muosha magari pale nje ya hoteli.


"Huyu binti ni mwathirika nini? Vurugu gani hizi hajui haya ni mavyuma tu hayazoeleki." Aliongea bibi mmoja aliyekuwa akipita eneo na mzigo wake wa kuni kichwani.


"Bibiii hao ndo watoto wa mjini, enzi zenu mambo kama hayo hayakuwepo." Alimjibu kijana mmoja mshona viatu karibu na kontena la mtandao wa simu wa airtel.


Baada ya kulizungusha na kusababisha kelele na vumbi kubwa ajabu Jackline alishuka na kuelekea kwenye lile kontena na kupanda ngazi na kuzama ndani yake.


" Habari yako dada!"


"Safi, karibu dada."


"Asante, nipatie hizo Sumsung SX. Naomba hiyo ya silver na hiyo nyeusi."


"OK, ngoja nikuchukulie huku stoo."


"Fanya haraka nina safari ndefu Ndugu yangu."


"Bila shaka."


Mhudumu aliingia kuzichukua zile simu stoo ambako huzihifadhi huko kwa kuhofia wizi, japo kuna nyepesi nyepesi zinasema hiyo ni njia ya kukwepa mapato.


"Hizi hapa dada."


"Kiasi gani kwa zote."


"Zikague kwanza ili kujiridhisha."


"Dada ee hujiamini, nikiona zimezingua si nitakurudishia?"


"Ilikuwa ni ushauri tu dada."


"Ondoa shaka."


"Kwa zote utanipa shilingi milioni moja kwa maana ya shilingi laki tano kwa kila moja dada."


Jackline anaonekana kutawaliwa na Uzungu zaidi, nafikiri kuishi kwa muda mrefu Afrika Kusini kumemfanya kuyaishi maisha ya WAZUNGU kwani kiasi alichotajiwa hakubisha hata kidogo zaidi ya kutoa kitita hicho kutoka kwenye pochi yake na kumlipa. Hapa angekuwa Mbongo ninayemfahamu mimi angelia kwenye bei na muuzaji mpaka wangeishia kwenye shilingi laki nane kwa zote. Kitendo hiki kilimfanya huyu dada muuzaji wa simu kutoamini Macho yake, kwani toka aajiriwe kwenye duka hilo miaka miwili iliyopita ndiyo mteja wa kwanza kutobishia bei.


"Kazi njema."


"Asante sana dada, karibu sana wakati mwingine."


"Nashukuru sana."


Alishuka ngazi haraka haraka na kuvuka barabara na kulifuata HONDA JET5 lake gari la kifahari ambalo ukiliangalia kwa juu juu waweza Sema ni gari la kawaida sana lakini huwezi amini thamani ya gari hili ni shilingi za kibongo milioni tisini na tano (95ml).

Gari ambalo Jackline alilinunua nchini Afrika Kusini wakati akiwa huko masomoni.


"Robinson, zawadi yako hii hapa nadhani kuhusu kuitumia unajua. Na wewe Shamimu ya kwako hii hapa, hapa ni mwendo wa kuchati kila mmoja."


"Ooough My God, Jackline umeninunulia simu ya gharama hivi! Nitakulipa nini kwa wema wako huu."


"Lazima uwaze hivyo Robinson, lakini kumbuka kuwa bila wewe siku ile ningeumbuka pale baada ya gari kuishiwa mafuta."


"Sina neno jingine zaidi ya asante. Nashukuru sana."


"Bila shaka Robinson."


"Dada Jack nashukuru kwa kuninunulia simu hili nadhani Shuleni watapata tabu sasa dude kama hili hakuna anayemiliki kuanzia Shuleni mpaka mtaani zaidi yetu sisi. Asante sana dada."


"Shamy wewe ni mdogo wangu ni wajibu wangu kukupa furaha."


"Shemeji tutawakimbiza pale Lupa kwa misimu hii mpaka waturoge." Shamimu alimnong'oneza Robinson aliyekaa kiti cha mbele na Jackline.


"Umeanza maneno yako Shamimu." Alimjibu huku akitabasamu, tabasamu hili nadhani lilikuwa linaashiria Jambo kuwa ikitokea zali analiachaje.


"Shamy unasemaje hapo?" Aliuliza Jackline aliyeshtukia mchezo.


"Hamna kitu dada."


"Mhh, haya bwana siwawezi kwa vituko vyenu."


Muda huu maongezi yanaendelea gari hili aina ya HONDA JET5 lenye muonekano maridhawa kama wa Harrier Mayai lilikuwa linahamisha vumbi kutoka barabarani na kulitupa nyuma na pembeni maeneo ya kijiji cha Upendo huku muziki ukiendelea kuburudisha ngoma zao za masikio na alikuwa si mwingine zaidi ya msanii wa nyimbo za Injili aitwaye Magreth Magenda akiimba wimbo wake wa NASHUKURU MUNGU.


"Dada nikwambie kitu."


"Niambie mdogo wangu mwenyewe."


"Na sisi siku moja moja uwe unatufundisha gari."


"Hilo tu, labda kama kuna jingine."


"Lingine lipo."


"Lipi hilo Shamimu."


"Natamani siku moja Robinson awe Shemeji yangu maana hapo mbele mmependeza sana."


"Jackline aligeuka akamtazama Robinson kisha Shamimu, akaishia kumtupia swali Robinson."


"Robinson unamsikia Shamimu anachokiwaza."


"Aaa nimemzoea kwa sasa Shamimu na maneno yake." Alijibu Robinson ambaye kiuhalisia kimoyo kilikuwa si chake.


"Mdogo wangu nakushukuru kwa ushauri wako lakini zingatia Masomo haya mengine waachie Wajuvi wa mambo


." Alijibu Jackline ambaye kiuhalisia kwa Robinson katua anashindwa aanzie wapi hivyo kwa maneno ya mdogo wake anashukuru amepata pa kuanzia.


Mpaka muda huo miguu ya Jackline ilikuwa ikipishana kwenye peda za breki na moto maeneo ya Mamba 'A' kilometa chache kuikaribia Lupa.


Nini kitaendelea,

Tukutane sehemu ijayo




Honda jet5 lilitia nanga yake nyumbani kwa akina Robinson na wakashuka garini, wakati Robinson na Shamimu wakishusha mizigo garini yeye Jackline aliongoza mpaka kwa mama Robinson na kumkumbatia hali iliyosababisha mama huyu kushindwa la kufanya lakini ilibidi naye afanye hivyo hivyo japo kwa uoga, hebu fikiria kwa familia ya kimaskini na inayoishi kijijini kukumbana na mtoto kutoka kwenye familia ya kitajiri inakuwaje, na ndiyo maana walijaribu kumkanya mtoto wao Robinson kuacha kuambatana na binti huyo asije waletea Matatizo lakini mwisho wa siku binti huyo (Jackline) hufika nyumbani hapo na kumuomba Robinson na tendo hilo huwafanya wazazi hawa kumkubalia tu kwa shingo upande.


"Mama samahani kwa kuchelewa kurudi ilitubidi tulale kutokana na giza lililotukuta tukiwa bado Makongolosi." Aliomba msamaha Jackline.


"Mwanangu ondoa shaka, japo tuliingia hofu juu ya hili lakini tukajipa Moyo kuwa ninyi ni watu wazima. Nimewasamehe kabisa." Unafikiri mama wa watu angejibu nini mbele ya binti Tajiri.


"Halafu mama naomba mnichukulie kama mwanenu na mimi, kwani najisikia faraja sana nikiwa na Robinson." Aliongeza Jackline.


"Mmhh, vipi kuhusu mzee Fikirini atatufikiriaje sisi kama lilivyo jina lake maana ni korofi yule mzee!!"


"Kuhusu wazazi wangu niachieni mimi nitashughulika nalo."


Wakati wakizungumza hayo tayari Shamimu alikuwa karibu na dada yake na alisikia kila kitu pale huku Robinson akiwa kaegemea mlango asijue ni nini kinaongelewa pale na moja kwa moja akajua Jackline anamchongea kwa mama yake juu ya mtafaruku ambao ulijitokeza kati yake na Shamimu kule Makongolosi.


Alitamani asogee pale ili akaombe msamaha lakini hakujua anatumia njia gani.


"Robinson siye tunakwenda, bye bye." Aliongea Jackline akimpungia Mkono.


"We mama si uwaandalie Chakula wageni mbona wanaondoka na njaa." Robinson alimwambia mama yake.


"Kweli wanangu, tupike kwanza mle ndiyo muondoke mnaharaka gani ilhali na Chuma mnacho?"


"Mama tunashukuru sana, siku nyingine tutakula itakuwa ni siku maalum ya kuja hapa."


"Karibuni sana lakini na leo pia mngekula wanangu jamani."


"Mama sisi hapa ni nyumbani muda wowote na wakati wowote tunakuja bila wasiwasi tunaomba uturuhusu tuende." Shamimu aliongea baada ya kuona ngonjera zimezidi.


"Karibuni sana japo mmekataa kula Chakula, ila mkifika nijulisheni si mnajua tena Robinson kwa hewaaaaa." Kauli hiyo ikapelekea wote kucheka huku Jackline na Shamimu wakiingia garini na kuondoka.


"Wee mwanangu hebu njoo huku ndani hivi unajua hatukuelewi na hawa mabinti?"


"Kuhusu nini mama?"


"Kuhusu nini, hujui mmetoka wapi na toka lini mlipokwenda huko shauri yako si unamfahamu yule mzee Fikirini lakini."


"Mamaaa, unachofikiria walaaa sisi ni marafiki tu na kama ujuavyo mimi ndo mtu wa kwanza kufahamiana naye."


"Pamoja na hayo shauri yako, baba yako jana kawaka hapa balaa, nikakusaidia."


"Na mimi nilijua kuna jembe huku nyuma na ndiyo maana sikuwa na wasiwasi wowote ule, kwanza njoo uone vitu huku mama."


"Vitu gani hivyo, Umeona utumie gia zako kupoteza lengo, haya tuone hivyo vitu."


"Yaani mama mpaka nashindwa kumuelewa Jackline, kwanza pale alikuwa anakuambia nini?"


"Mambo ya wanawake wayatakia nini wewe mtoto wa kiume?"


"Mmhh, haya nimeacha. Angalia mambo aliyonifanyia Jackline, cheki simu hii ya bei mbaya Lupa nzima hakuna ni mimi na mdogo wake Shamy tu inauzwa laki tano mama, cheki hii saa umewahi iona wapi, hapo sijagusa pamba zenyewe humo Hatareee na lazima waturoge mwaka huu japo lambalamba walipita. Haya chukua mfuko huu una vitu vyenu na mume wako."


"Wee Robinson wewe utasababisha tufe kabla ya muda wetu. Simu ya laki tano kweli si ungemwambia akununulie ya shilingi elfu thelasini Halafu iyo nyingine ungetuletea tununulie mahindi hapa nyumbani."


"Mama chakupewa hakina maswali, wewe chukua weka mfukoni mengine yafuate."


"Ila mwanangu huyu mwanamke anakupenda si bure kabisa haiwezekani mavitu yote haya gharama yake shilingi ngapi?"


"Haiwezekani anipende mimi mtoto wa fukara mzee Kaaya."


"Na uzuri ni mzuri mwanangu unawakimbiza mtaani na ndiyo maana mtoto wa tajiri katua mwenyewe kwenye kidonda cha fukara, chezea kazi ambayo tuliifanya na baba yako?"


"Mara aah mara eeh familia gani choka mbaya ile, wana nini wale. Wananiita mpaka majina mabaya mimi eti Robinson Marapurapu. Sasa wataniita Robinson handsome chezea."


"Sasa mwanangu tuachane na hayo watajibeba wenyewe hawajui kila mchuma janga hula na wa kwao acha tule vitu vya Jackline siye ila angalia mwanangu utaolewa wewe."


"Mama, mimi kidume naolewa vipi kumbuka natokea bara si wa Mombasa mimi oohh."


Wakati wakiendelea na majigambo yao mara alifika jirani yao mama Kaundime na hii ni baada ya kuona lile gari likitokea pale na hiyo haikuwa mara moja kuliona.


"Jirani hodi, hodi."


"Karibu, karibu."


"Asante jamani, habari ya hapa."


"Robinson mbona hatuambizani kama umeoa?"


"Nimeoa toka lini mama yangu? Mbona unaniletea mikosi ya ajabu hivi."


"Mwanangu hajaoa, ila najua udenda umekutoka ulipoliona gari lile likitoka hapa, yule ni rafiki yake tu."


"Mhh makubwa marafiki wa jinsi mbili tofauti, inawezekana?"


Mambo ya kijijini wao hawaamini kuwa mtoto wa kike na wa kiume wanaweza kuwa marafiki zaidi ya kuwa na mahusiano. Ukaribu wa Robinson na Jackline uliendelea kuwa gumzo mtaani mpaka Watu wakaanza kumuonea wivu Robinson.


" Umetoa mimacho ya nini, wewe si ulisema huwezi kuolewa na mtu kama Robinson sasa nini?"


"Yaani mama we acha tu, Robinson kawa handsome utafikiri kazaliwa leo. Na nimeamini usimdharau mtu chini ya jua."


"Yamekushuka, shuuuuu mwanangu."


Yalikuwa ni mazungumzo kati ya Mwahija na Mama yake. Mwahija ni miongoni mwa wasichana ambao walimtolea maneno mbofu mbofu Robinson alipokuwa akitafuta fursa kwao.


***


Mzee Fikirini alijaa kwenye mawazo ya mke wake ambapo mwanzo alionekana kutoungana naye kwenye wazo lake la kupora Mali za marehemu shemeji yake ambazo kwa sasa walitakiwa kumkabidhi Jackline ambaye alikuwa amekuwa.


Mzee Fikirini aliamua kumuweka sawa Jackline ambaye usiku wa siku aliyotoka Makongolosi alimueleza kuwa nyaraka zote za usimamizi wa Mali za baba yake alikuwa nazo na alimkabidhi usiku ule ule, lakini akaenda mbali zaidi kwa kumwambia Jackline kuwa kutokana na ugeni wake kusimamia mali hizo ilibidi aombe msaada kwa rafiki wa marehemu Ndugu yake mzee Jonathan ambaye ni mlezi wa Jackline kwa kipindi chote hicho kuanzia utoto wake mpaka sasa.


Na suala ambalo lilikuwa mbele yake ilikuwa ni Kuelekea mjini Tabora kwa mzee Jonathan kwa ajili ya kumkabidhi rasmi ofisi Jackline ili azisimamie vizuri biashara zake.


Jackline aliwashukuru sana walezi wake kwa kulitambua hilo japo alionyesha masikitiko yake juu ya mlezi wake mzee Jonathan ambaye kwa kipindi chote hicho hakuwahi kumwambia kama mali alizonazo ndani yake zipo zao.


Akakumbuka siku aliyohitimu chuo alimweleza mzee huyo juu ya mipango yote ya safari yake itakavyokuwa.

Lakini cha ajabu anasema siku moja kabla ya safari yake mzee Jonathan alimpigia simu na kumweleza kuwa amepata dharura yeye na familia yake wanaelekea nchini China watakuwa huko kwa Muda wa miaka miwili.


"Unafikiri mali hizi tutazipata mzee wangu?"


"Mhh, kwa hiyo unataka kuniambia mzee Jonathan hayupo nchini kwa sasa?"


"Ndiyo baba."


"Hapa tunakazi kubwa ya kufanya, maana naona kengele ya kutapeliwa inanigonga."


"Jackline, unachoongea una uhakika nacho kweli?"

Aliuliza mama Shamimu, mama wa mipango ambaye taarifa hizi zilimchoma Moyo moja kwa moja japo hakuna aliyejua zaidi ya bwana yake mzee Fikirini.


"Mama ni kweli kabisa, na hata namba zao za simu hazipatikani. Mimi nilijua wameamua kunifukuza kisomi na ndiyo maana kwenye ujumbe wa mwisho ulikuwa na namba ya simu ya kwako baba na ndiyo tukawa tunawasiliana mpaka nilipofika hapa."


"Mhh mbona naona giza mbele mimi jamani." Aliongea mzee Fikirini.


"Giza la nini mume wangu haya yote uliyasababisha wewe kwanini ulichukua jukumu la kumuamini mtu na kumkabidhi utajiri mtu huku sisi tukiendelea kula mlenda?"


"Mke wangu leo unaniruka kabisa."


"We ee ishia hapo hapo nikuruke kwa lipi ambalo tulipanga Pamoja?"


"Sawa tu lakini kufikia asubuhi nitawapa jawabu la utata huu na kila mtu atalifurahia


naomba tukapumzike. Jackline tutaangalia asubuhi tufanye nini lakini suluhisho nitakuja nalo."


Jackline aliitikia kwa kichwa kwani muda huo wote alikuwa akilia tu asijue afanye nini? Na lililokuwa likimpa tabu kwanini mzee ambaye alimuamini kwa kila kitu tena rafiki mkubwa wa marehemu baba yake mzee Joachim, na aliyechukua jukumu la kumsomesha kumbe alisomeshwa kwa fedha halali za baba yake. Pia akamfikiria mzee Fikirini kwa nini alimuamini mzee Jonathan?

Lakini baadaye akapata jibu ilikuwa ni uoga wa kusimamia mali ambazo hajawahi kuwa nazo.

Mpaka anakwenda Kulala Macho yalikuwa mekundu.


"Nasema haiwezekani, haiwezekani nitakutafuta popote duniani mzee wangu Jonathan." Alijikuta akiropoka kwa Sauti ambayo ilipenya moja kwa moja mpaka chumbani kwa mzee Fikirini ambaye alisikia maneno hayo.


***


Usiku ulikuwa mrefu kwa mzee Fikirini ambaye aliwaza sana juu ya alichosikia kwa Jackline kama kina ukweli ndani yake. Na pia akamfikiria mzee Jonathan alichokifanya kama ni kweli kwa nini aliamua kuwafanyia hivyo lakini. Alienda mbali zaidi na kufikiria jinsi ambavyo alimwambia ile siku alipokuwa akimkabidhi miradi na kufikia kumuahidi kuwa angezisimamia kama zake. Na sasa alikuwa nchini China sehemu ambayo hafahamu iko wapi na Watu wake wakoje na wanaishije. Hili lilimuumiza sana kichwa Akakumbuka namna ambavyo mke wake alimshawishi wamuue Jackline ili warithi mali zile. Akawaza mwisho wa siku jamii itakwenda kumtazama vipi kwenye hili si watajua ameshiriki kuhujumu mali za binti yao Jackline.


"Itabidi nifanye Jambo kabla ya asubuhi ili kujiweka mbali na hili." Aliwaza mzee Fikirini..


Katikati ya usiku mzee aliingia chooni akakikagua vizuri akauona mwamba uko imara. Akaurudisha mlango na kuchukua kamba ya katani ambayo ilikuwa nje kwenye mti aliyokuwa akiitumia kufungia nguruwe akaifunga vizuri kwenye mwamba wa Choo kisha akatengeneza kitanzi na kukivaa shingoni.


Kwanini mzee Jonathan katorokea nchini China, je ni kweli yuko huko?


Na mzee Fikirini anavaa kitanzi kwa lengo la kufanya nini?




Mzee Jonathan Ubao ni mfanyabiashara maarufu sana kwa Kanda ya kati, Magharibi na Kanda ya Ziwa.


Umaarufu huu uliongezeka zaidi mara baada ya kuongeza mara dufu miradi mingine ambayo ilikuwa chini ya kampuni aliyoianzisha iliyofahamika kwa jina la UBAO INTERNATIONAL TRADE.


Kampuni hii inahusika na uagizaji wa vipuri, mitambo na magari kutoka nje ya nchi.


Pia kampuni hii inasafirisha Maua kwenye nchi za Kanada na India hizo ni kimataifa na kwa upande wa ndani ya nchi inahusika na uandaaji wa mchele na kuupaki kwenye uzito tofauti tofauti na kupeleka mikoa ya Dar na Arusha.


Pamoja na yote hayo kitu pekee ambacho kilikuwa kinamuumiza kichwa ilikuwa ni juu ya familia ya mzee Joachim yaani mzee Fikirini na Jackline.


Aliumiza kichwa chake usiku na mchana, na Kiukweli alikuwa nchini katika mkoa wa Mwanza na si nchini China kama ambavyo alimwambia Jackline alidanganya lengo likiwa ni kujiweka mbali na mtoto huyo ambaye asilimia kubwa ya mtaji wote wa kampuni yake umetokana na mali za marehemu mzee Joachim na sasa Jackline alikuwa kahitimu Masomo yake nchini SA hivyo kurudi kwake tafsiri ni kuwa anakuja kuchukua mali za mzee wake ili azisimamie mwenyewe kwa ushirikiano mkubwa na baba yake aliyebaki mzee Fikirini.


Hili hakuwa tayari kuona linatokea mbele yake na alikuwa tayari kumwaga damu za Watu watakaoonesha dalili za kumfuatilia na ndiyo maana kitu cha kwanza kukifanya ilikuwa ni kuuza makazi yake na kuhamisha makazi yake na kutimkia sehemu ambayo Jackline ingemchukua karne na karne kujua na ndiyo maana alibadilisha na jina kabisa la kampuni.


Baada ya kutafakari kwa muda akamkumbuka rafiki yake ambaye miaka kadhaa nyuma alikuwa nyuma ya nondo pale gereza kuu la Dodoma.

Huyu jamaa issue zake ni kukodiwa kwa shughuli mbalimbali iwe kuteka, kuua na kadhalika, hivyo akaona amtafute kwenye namba yake ya zamani ili kujua kama alishatoka ili amshawishi kwenye mpango wake mpya.


"Griiii, Griiii, Griiii, kumbe yupo hewani alitoka nini gerezani?" Aliwaza mzee Ubao.


"Halooo." Iliita upande wa pili.


"Naongea na Abuu Surambaya."


"Ndo mwenyewe kaka upo Ndugu yangu."


"Niende wapi bwana, ila Kwa sasa naishi mkoani Mwanza."


"Ulinitenga kabisa kaka, hata kunitembelea pale gerezani?"


"Ndugu yangu kwanza naomba unisamehe kwa hilo lakini nadhani unafahamu maisha niliyoyapitia."


"Wewe tena, nakufahamu kama njaa. Lete mpya lakini."


"Mambo yako vipi bado unaendelea au umeacha?"


"Kaka nilikunywa damu ya kiapo hiyo ni mpaka kaburini, wewe kama una kazi Nambie."


Mzee Jonathan Ubao alimueleza kila kit rafiki yake huyo Abuu Surambaya. Na kumueleza nini lengo lake.

Abuu alimuelewa mzee Jonathan na kumwambia kuwa kuna vitu anavihitaji kwa muda huo navyo ni picha za wahusika, eneo wanakopatikana na mkwanja wa awali kama milioni hamsini.

Mzee Ubao alifurahi kusikia hivyo akiamini tayari wabaya wake mzee Fikirini na Jackline wanakwenda kulamba mchanga na kumuacha yeye akiendelea kutanua maisha na kushamiri zaidi kwenye biashara zake.


"Wamekwisha hawa." Aliwaza mzee Jonathan.


Alifanya maandalizi ya fedha alizohitaji Surambaya Pamoja na picha zao hivyo vyote alivituma Kupitia simu janja yake ya MACX, simu anayoipenda kupita kiasi, Hivyo Alifanya miamala yote kwa njia ya APPLICATION YA BENKI Fulani nchini. Baada ya kukamilika alitumiwa ujumbe.


"Nimepata, subiri majibu ndani ya siku tatu kaka." Aliandika Abuu.


***


Mji mzima wa Lupa ulizizima kwa vilio, kila kona ya mji safari ilikuwa ni moja tu nyumbani kwa mzee Fikirini ambaye alizua taharuki kwa kifo chake cha kujinyonga.

Na kilichopelekea watu kuacha shughuli zao na Kuelekea kwenye mji huu haikuwa tu kujinyonga kwa mzee Fikirini la hasha bali ni pamoja na kifo cha mke wake, mama Shamimu ambaye alikutwa na umauti baada ya kukuta mume wake kaning'inia chooni akiwa tayari kafariki hali iliyomkuta ni mshangao mkubwa uliomuangusha chini na kupelekea umauti wake.

Hivyo kwenye mji huu kulikuwa na misiba miwili ya hawa wazee.


Na kila aliyefika kwenye msiba huu alitokwa na machozi kutokana na namna ambavyo hawa mabinti wawili walikuwa wakilia kwa NGUVU kupelekea Sauti zao kukauka.


Vijana wengi walikuwa na kazi kubwa ya kumnyamazisha kijana mwenzao Robinson ambaye kwa wakati huu alikuwa ni familia moja na hii ya mzee Fikirini.


Na wengi walijua huyu Robinson alikuwa tayari ni mchumba wa Jackline.

Wanafunzi wa Sekondari ya Lupa, walifurika kwenye msiba huu kumpa Moyo mwenzao Shamimu.


Wakina mama wengi waliokuwa kwenye huu msiba walilia sana kutokana na kumpoteza mzee Fikirini aliyekuwa mcheshi zaidi popote pale ambapo alikuwepo lakini swali lilikuwa ni kwa nini wamejitoa uhai hawa wazee?


Mzee Kaaya na wazee wenzake waliandaa mazingira ya namna ya kuisitiri miili ya marehemu hawa wawili.


"Da, hili toto kweli limeumbika aise cheki linavyolia, Pamoja na kulia kote huko lakini bado litamu. Robinson analifaidi kweli." Yalikuwa ni maneno ya dogo mmoja fundi pikipiki.


"Robinson si bure, hapa kizizi kimetumika hawes mtoto mwenye sifa zote, mzuri, tajiri na msomi lakini kaangukia kwa kijana Fukara lakini handsome asiyekuwa na matunzo. Ina maana hakuwaona vijana na wazee wenye mtonyo hapa kati?" Alijibu kijana mmoja aliyejulikana kwa Jina la Chawa.


Wakati Utitiri huu ukiendelea kumiminika kwenye mji huu wa mzee Fikirini. Kati yao ni mtu mmoja ambaye aliungana na Watu wengine kwenye msiba huu.


Kila mmoja alikuwa akimtazama sana mtu huyu kwani alifika hapo akiwa na pikipiki aina ya XR450-KAWASAKI alifika hapo akiwa na begi lake mgongoni na akiwa na full black clothes (rainclothes).


Aliungana na wengine kwenye hatua zote za kusitiri miili ya hawa wazee.


"Huu msiba umebeba Watu wengi sana wanaojulikana na wasiojulikana mfano huyo jamaa hapo ni mgeni kabisa halafu cheki huo mpikipiki wake sasa." Aliongea kijana mmoja aliyekuwa pembeni ya mgeni huyo.


Baada ya mazishi kufanyika kila mmoja alitawanyika kurudi kwake kutokana na tangazo la mwenyekiti wa kijiji kuwa kutokana na msiba huu kuondokewa na wazazi wote wawili na kubaki na watoto tu tena mabinti, hivyo hakuna msiba utakaoendelea hapo na kuwaacha hawa watoto kutafakari juu ya misiba hii.


"Hivi Robinson huyu mtoto umewahi kummega?" Aliuliza rafiki yake Awadh.


"Awadh, maswali gani unayouliza hapa, unafikiri ni mahali Sahihi kwa swali lako?"


"Sorry boy, samahani bwana ilikuwa ni joke tu."


Mzee Kaaya alimfuata mtoto wake Robinson na kumnong'oneza kitu sikioni. Kitendo kilichomfanya Robinson kuinuka na kumfuata Jackline ndani.


"Pole Jack."


"Asante Robinson, ndo hivyo tena wazazi wametuacha wakiwa."


"Baba na Mama wanakupa pole sana na wanasema msijione wapweke kwani kwa wema uliotenda kwetu amedai Wapo kwa ajili yenu."


"Waambie nawapenda sana wazazi wako maana wao ndiyo wazaa chema, nakupenda sana Robinson ungana na mimi kwenye kipindi hiki kigumu nimeona nikueleze ukweli muda huu wa majonzi."


Jackline aliamua kueleza ukweli toka moyoni kwake namna ambavyo anampenda Robinson. Na Robinson alivyoambiwa hayo alibaki mdomo wazi japo hakuonesha wazi.


" Nakupenda pia Jack, nakuahidi sitakuumiza milele. "

Alijitahidi kuongea Robinson.


" Nashukuru sana Robinson, kuna mpango ambao baada ya siku nne tunatakiwa kuufanya."

Bila shaka.


Pamoja na kuwa kwenye majonzi lakini Jackline alikuwa bado kwenye mkakati ya kuhakikisha anamnasa mzee Jonathan akiwa Hai au amekufa.

Aliamini msiba huo ni zao la utapeli wa mzee huyu.


Baada ya kuondoka kwenye msiba huu, Abuu Surambaya alipaki pikipiki lake eneo la kijiji cha Upendo na kutoa simu yake.


"Boss...."


"Nakusikia Abuu.". "


"" Hawa watu nimewakuta tayari wanakoishi, lakini yule mzee Fikirini na mke wake wamekufa kicho cha ghafla, ambapo mzee Fikirini alijinyonga sababu haijulikani na mke wake alikufa kwa mshtuko wa kifo cha mume wake."


"Duuu, inakuwaje sasa!"


"Kale kabinti nimekakuta kapo pale."


"Lini unakapoteza hako maana ndiyo kamwiba."


"Ngoja kwanza msiba huu umalizike kwanza then nitaleta mshtuko mwingine kwenye familia hii na hivi sasa niko njiani naelekea jijini Mbeya kukutana na mchizi wangu Hasara niliyekuwa naye gerezani Dodoma."


"Mimi nakutegemea wewe Abuu."


"Bila shaka kaka."


Kisha akakata simu yake Na kuiweka mfukoni mwake na kuiwasha pikipiki yake na kuendelea na safari yake.



***


Jackline alifika mapema Shuleni kwa Shamimu pale Lupa Sekondari kwa lengo la kwenda kumuaga.


Hii ilikuwa ni lazima aondoke kijijini hapo na kusafiri Kuelekea mkoani Dodoma kuanza maisha mapya lakini kichwani aliamini hii ni sehemu muhimu sana ya kufanikisha mpango wake wa kumnasa mzee Jonathan Ubao.


Na ambacho kilimvutia zaidi ni kuweza kumnasa Robinson kijana ambaye alimpenda mara baada ya kufika tu Lupa na hali hii ilimshangaza sana kwani kwa kipindi chote alichokuwa masomoni Afrika ya Kusini hakuwahi kuwa kwenye mahusiano ya kimapenzi zaidi ya kuwa na urafiki tu na kijana mmoja kutoka nchini Botswana waliyekuwa darasa moja.


Na kitu ambacho kilimvutia kutoka kwa kijana huyu wa Kiswana si kingine bali ilikuwa ni mazoezi na mapigano ya karate na judo ambayo aliyamudu sana chuoni hapo na kupelekea Jackline kupenda michezo hiyo na hivyo ikawa ni suala la kumuomba Simbozya amfundishe michezo hiyo.


Simbozya hakuwa mjivuni alikubali kumfundisha hivyo Jackline aliungana na wasichana wengine wanne kwenye mafunzo hayo ambayo waliweza kuyamudu vilivyo na kupelekea kukiwakilisha chuo kwenye mashindano mbalimbali ya Olympics duniani.


Miongoni mwa mashindano ambayo alifanya vizuri Jackline yalikuwa ni yale yaliyokwenda kwa jina la SOWETO INTERNATIONAL OLYMPICS 006 ambayo alishinda kwa kumpiga mwanadada wa Afrika Kusini aliyefahamika kwa jina la Malosa na kupeleka medali ya dhahabu chuoni hapo.


Hivyo katika suala la mapenzi alijikuta akiangukia mikononi mwa shamba boy (Robinson) ambaye naye hakulaza damu juu yake.

Alifika Shuleni na kumkuta mwalimu mmoja anaongea na simu akatulia pembeni kumsubiri amalize kwanza ndipo amweleze shida yake.


Mwalimu alipoona kuna mtu pembeni yake ilibidi akatishe maongezi yake kwenye simu.


"Naomba kukusaidia binti."


"Naitwa Jack." Alijitambulisha.


"Naitwa mwalimu Costantine, naomba nikusaidie Jack."


"Samahani mwalimu, ninamomba Shamimu."


"Uhusiano naye."


"Ni mdogo wangu."


"Ooh, wewe ndo yule mwenye ile Honda?"


"Haujakosea mwalimu."


"OK, ngoja nikakuitie mdogo wako."


Mwalimu Costantine aliondoka Kuelekea madarasani kumfuata Shamimu na dakika kadhaa akaja akiwa kaongozana naye.


"Jack mdogo wako huyo ila maongezi yawe mafupi nimemtoa kwenye kipindi."


"Dakika chache mwalimu." Jackline alijibu akimvuta Shamimu pembeni ambapo aliongea naye mambo kadhaa ikiwemo kukazania masomo zaidi ya chochote pia ilikuwa ni kumuachia fedha kidogo ambazo zingemsaidia kipindi ambacho yeye Jackline atakuwa mbali na mdogo wake huyo ambaye kwa muda huu ndiye mlezi wake.


"Dada nitakumis sana na sijui kwenye masomo kama nitafanya vizuri."


"Usiseme hivyo mdogo wangu mimi ninaimani utafanya vizuri sana kikubwa amini kuwa nitarudi baada ya kufanikisha suala nililokueleza ambalo itakuwa ndiyo dira yetu." Jackline alimfafanulia mdogo wake.


"Vipi kuhusu Robinson amekubali kukusindikiza?"


"Mdogo wangu hii siyo sehemu muafaka kwa mazungumzo haya, rudi darasani kaendeleze kitabu."


"Ila mimi bado nina kinyongo na kaka yangu kwanini afanye vile dada?"



"Mdogo wangu msamehe bure tu kuna siku ataelewa maana, mwache aendelee na maisha yake anayoamini ndiyo kila kitu kwake."


"Sawa dada nikutakie safari njema na mkafanikiwe na kurudi salama kuungana nami."


"Bila shaka mdogo wangu najua mpaka likizo ifike tutakuwa tumerudi."

Baada ya mazungumzo ya dakika kadhaa waliweza kurudi pale kwa mwalimu na kumkabidhi.


"Nashukuru mwalimu nimemaliza na naomba niwaache muendelee na kazi."


"OK, karibu tena Jack." Alijibu mwalimu Costantine.


Jackline aliondoka taratibu na kumuacha mwalimu Costantine akiyashibisha macho yake kwa nyuma kukitolea macho kichuguu ambacho alikifungasha Jack kwa nyuma. Ni kweli Jackline kaumbika kiasi cha kumtoa mate mwanaume yeyote ambaye ni lijali. Jackline aliondoka zake pale shuleni na kurudi zake nyumbani kwa ajili ya kuianza safari.


Tukutane katika sehemu inayofuata ya Hadithi hii.




"Hallow boss."


"Lete habari mpya Abuu."


"Unahitaji habari mpya?"


"Abuu unauliza nini tena?"


"Boss hapa ninapoongea niko ndani ya shimo hapa porini, sisimizi wamezingira hili eneo wananitafuta."


"Buuu shiiiit! Umefanya nini sasa na hapo ni wapi?"


"Nilipofika hapa Makongolosi, nilitulia sehemu moja hivi nikamfuata pusha mmoja hivi kununua kitu cha Jamaica ili kuweka Sawa akili na wakati pusha yule ananishughulikia wewe ndo ulipiga tena kujua nitalala wapi si ndo nikajichanganya kuanza kukupa mchakato mzima na namna ya kuongeza vijana watatu kwa zoezi Zima. Kisha nikapewa changu nikalipa na kusepa nikilenga kulala sehemu moja inaitwa Matundasi. Nikiwa spidi kwa nyuma si nikaona kuna pikipiki kama tatu zikija kwa kasi."


"Kwa hiyo walikukamata?"


"Hapana boss ila nikiwa nakanyaga mafuta zaidi ghafla dude likazima kucheki nyuma jamaa hawa hapa ikabidi nichumpe pembeni na kutokomea porini na kuiacha pikipiki hapo, hivyo jamaa wameichukua na kulizingira eneo hili sijui kama nasalimika. Ila nikipona tu kutoka salama eneo hili lazima nirudi pale kati na kumsaka yule pusha hanijui mimi ni nani Mchawi yule."


Wakati Abuu Surambaya akiwa anawasiliana na mzee Jonathan juu ya janga lililomkuta katika eneo la Manyanya, ghafla akasikia sauti kwa juu ikitoa amri.


"Washa moto eneo lote hili kwanini tupoteze muda kwa mtu mmoja mpumbavu kama huyu ilmradi tumepata pikipiki lake na hili begi lake tukalikague tujue kuna nini ndani yake na haya ndo Majambazi yanayokimbia huko na Kuja kujificha huku machimboni."


"Sawa Afande."


Kweli moto uliwashwa eneo lote lile na moto ulikubali sheria, kwani ulisambaa kila eneo na kwa moto ule sidhani kama hata sisimizi watapona.

Kiufupi kila kitu kiliteketea kwenye msitu ule na mpaka kuleta hofu karibu na makazi ya Watu kwenye kijiji kile cha Manyanya.

Baada ya kuona moto umekolea vilivyo wale Askari Doria waliondoka eneo lile na kurudi kituoni wakiamini mtuhumiwa wao wameshamuangamiza pale.


***


"Huyu mshenzi mbona hapatikani hewani?" Aliwaza mzee Jonathan baada ya kupiga simu ya Abuu karibu mara sita pasipo kumpata hewani.


"Mume wangu mbona unaongea peke yako, kulikoni?" Aliuliza mke wake.


"Si mshenzi huyu hapatikani hewani?"


"Kwanini sasa."


"Dakika kadhaa nyuma aliniambia kajificha shimoni jamaa wametanda kila kona wanamsaka na pikipiki imenaswa baada ya kuzima wakifukuzana, sasa sijui wamemkamata?"


"Tutafanya nini sasa Mume wangu, nilikuonya lakini kuwa achana na mali za udhulumaji unaona sasa tumekuwa Wakimbizi ndani ya nchi yetu."


"Keleleeee....... Nitausambaza ubongo wako wewe, unafikiri akikamatwa kwa uzembe wake na mimi nitakamatwa la hasha zaidi nitaingia mtaani mwenyewe mpaka nimtie mkononi Jackline hawezi ishi katika dunia hii labda dunia nyingine pambafuuuu toka hapa."

Alimfokea mke wake akiwa kauma meno yake kuonesha kachukia sana na haitaji kusikia lolote tofauti na alivyopanga yeye.


Anachokiamini yeye ni kuuondoa uhai wa Jackline na ili apate fursa ya kuikuza kampuni yake Kupitia mihela ya marehemu rafiki yake mzee Joachim.


Aliumiza kichwa usiku huu pasi na kupata jibu zaidi ya kuona jasho likiendelea kumtiririka Mwilini wakati kwa muda huu jiji la Mwanza lilikuwa na baridi kali sana lakini mwili wa mzee Jonathan haukuliona.


"Au huyu mtoto ni mchawi nini?"

Aliwaza mzee Jonathan huku akijipiga piga kichwani kwa kutumia Mkono wa kisu chake.


"Griiiiiiiiiii, griiiiiiiii, griiiiiiiii."

Simu yake mzee Jonathan iliita na haraka sana akaitoa simu mfukoni na kuipokea haraka pasipo kuangalia ni nani mpigaji.


"Hivi wewe una akili zote kwanini bado umeuweka hapo si uwakimbie hao Askari wewe." Aliongea mzee Jonathan.


"Unasemaje shemeji mbona sikuelewi?"

Alijibu Mwanaheri, huyu ni mdogo wa mke wake akiwa Dodoma chuo cha Mipango aliamua kumpigia shemeji yake kumjulia hali lakini alichokutana nacho ni janga.


"Mhh, shabashi........." Alipoangalia kioo cha simu yake akagundua amechanganya madensa baada ya kugundua ni shemeji yake ndiye aliyempigia kabla ya kumjibu alikata simu hiyo haraka na kuzima simu yake.


***


"Niwashukuru sana wazee wangu kwa kukubali kukaa mdogo wangu kwa kipindi chote cha Masomo yake."


"Bila shaka Jackline ninyi ni wanangu ni jukumu letu kuhakikisha mnazifikia ndoto zenu pasipo kuathiriwa na Matatizo yaliyopita." Alijibu mzee Kaaya


"Nashukuru sana tena sana." Aliongeza Jackline huku akitokwa na machozi.


"Baby, punguza kulia hapa ni kwetu kila kitu kitakuwa vizuri pasi na shaka kabisa."

Robinson Alimbembeleza Jackline.


"Nimekuekewa baby, ila roho inaumaa, naumia mimi........"

Huku akilia kwa kwikwi.


Robinson ilibidi atumie akili ya ziada kumbembeleza mpenzi wake.

Huu ulikuwa ni muda wa Jackline kuondoka na mpenzi wake Robinson kuelekea jijini Dodoma kwa ajili ya kuanza maisha lakini tageti kubwa ilikuwa ni kuwatafuta marafiki wa karibu na mzee Jonathan ili wampe ukweli aliko baba yake huyo mlezi japo alijua itakuwa ni ngumu, alijipa matumaini ya kumpata popote pale iwe ni huko China au kwingineko.


Na kilichokuwa kina muumiza kichwa ilikuwa kwanini asipatikane hewani? Na kwanini hakufika hata kwenye msiba wa walezi wake? Na kwanini huyu kaka Athuman afanye kitendo kile mbele ya watu? Ni maswali ambayo alijiuliza Jackline bila majibu yoyote. Athuman mtoto wa kwanza wa mzee Fikirini anaishi Mbeya akifanya biashara ya mitumba na baada ya kufika kijijini kuwazika wazazi wake alitoa ya mpya ya mwaka baada ya kuwatuhumu majirani zao kuwa wamewatoa kafara wazazi wake ili wakatumike kwenye mashamba ya tumbaku kitu ambacho kiliwaudhi sana wale majirani na laiti kama ingekuwa siyo busara za Jackline kumuombea msamaha kaka yao huyo bila shaka majirani wangeondoka lakini walibaki kutokana na busara za mtoto wa kike. Baada ya mazishi kukamilika Athuman hakusubiri kukamilisha taratibu zote za msiba aliondoka siku ile ile tena bila kuaga kitendo kilichotafsiriwa kuwa alimaanisha maneno yake.


Safari ya kuelekea Dodoma ilianza kwa kupitia barabara ya Singida na hii ilikuwa ni baada ya kupata baraka zote za wazazi wa Robinson na ambao walichukua jukumu la kuishi na mdogo wake Jackline kwa kipindi chote ambacho wao hawatakuwepo.


Wakiwa njiani maeneo ya Rungwa kuitafuta Singida Jackline aliona ampigie simu rafiki yake Simbozya kuomba ushauri katika hili.

Kama utakumbuka huyu ni Mbotswana ambaye walisoma pamoja kule Afrika kusini na huyu ndiye aliyekuwa mwalimu wake wa mapigano ambayo yalipelekea kujizolea umaarufu mkubwa ndani na nje ya chuo chao kwa kushinda kwenye michuano mbalimbali.


"Jackline hili si jambo dogo rafiki yangu na si la kuliendea kichwa kichwa huwezi jua mpaka kafanya hivyo kajiandaaje." Simbozya alimtahadharisha Jackline juu ya kukabiliana na mzee Jonathan.


"Nifanyaje sasa, naomba ushauri wako mwamba."


"Kama hutojali fanya maandalizi ya kuja huku BONDENI kisha tufanye mpango wa kukutana na yule rafiki yangu ambaye alikuwa ananitumia vipande vya video za mafunzo ya mapigano bwana Santana."


"Yupi huyo mbona kama nimemsahau vile?"


"Jackline, umemsahau Santana ambaye nilikutana naye kwenye mtandao wa Instagram?"


"Okay, nimemkumbuka mshikaji wangu."


"Ndiyo huyo sasa najua baada ya kujifua vilivyo ndipo tutamtafuta popote pale duniani huyo mzee na kisha kumuonesha namna dunia inavyotaka tuishi."


Maongezi yake na Simbozya yalimwingia zaidi Jackline na hapo akawa amepata wazo jipya la kufika Dodoma na kuanza maandalizi mapya ya safari ya kuelekea Afrika ya kusini.


"Itakuwaje sasa Jackline hili jambo mbona ni la ghafla sana." Robinson alimuuliza Jackline baada ya kuambiwa wanatakiwa kuelekea nchini Afrika Kusini kuongeza ujuzi wa mapigano ili kuja kumkabili mzee Jonathan ambaye inasemekana yuko nchini China.


"Kivipi Robinson?"


"Si kama hivyo unavyosema tunatakiwa kuelekea nje ya nchi ilhali wazazi wangu na mdogo wako wanajua tunakwenda Dodoma."


"Ni kweli mpenzi lakini tambua kuwa katika hili tukisema tukaombe ridhaa yao hawatakubali hata kidogo hivyo unaonaje kama tukiondoka kimya kimya bila kuwapa taarifa na mpaka waje wajue ukweli tutakuwa tumerudi na zoezi litakuwa limekwisha."


"Hapana Jackline haiwezekani hata kidogo, yaani niende nje ya nchi bila ridhaa ya wazazi?"


"Kwa hiyo unasemaje katika hili?"


"Mimi siwezi kwenda huko Jackline."


"Okay sawa, basi wewe itabidi ushukie Manyoni kwa kuwa tunakaribia kufika kisha utarudi nyumbani na mimi nitaendelea na safari yangu kamwe siwezi kurudi nyuma."


Na kweli baada ya kufika Manyoni Jackline alishuka na kwenda kumkatia tiketi Robinson ya kurudi Chunya, alirudi akiwa na tiketi mkononi lakini ajabu ni kwamba Robinson alibadili mawazo yake na kuigomea tiketi ile na kumsihi airudishe ile tiketi hata kwa kuiuza kwa nusu bei. Kwa namna ambavyo Jackline alifurahi alimwambia Robinson haina haja ya kuirudisha itabaki kwenye kumbukumbu zetu tuondoke zetu mpenzi, na safari ikaanza.


Nini kitatokea?

Tukutane katika sehemu ya saba ya kigongo hiki.




Jackline na Robinson wako ndani ya msitu mnene wa San Antonio ulioko nchini Brazil. Msitu huu unapakana na Ufukwe wa Marigezh kwenye mji wa Belem.


Imekuwaje waingie Brazil haraka kiasi hiki badala ya kuelekea Afrika Kusini kama walivyokubaliana na mwenyeji wao.


Safari hii ilikuja ghafla mara baada ya kupata taarifa kuwa kuna mtu ameuawa kwa kuchomwa moto katika msitu wa manyanya ndani ya Makongolosi.


Na inasemekana pikipiki Pamoja nyaraka nyingine zilikamatwa na kuhifadhiwa kituoni kwao.


Ndani ya nyaraka hizo kulikutwa picha za Jackline, mzee Fikirini na vitambulisho vya jambazi huyo aitwaye Surambaya.


Hivyo jeshi hilo la polisi lilipanga kuwatafuta watu hawa popote pale ili kupata maelezo ni kwa namna gani picha zao zimekutwa kwenye fuko la mtuhumiwa. Taarifa zilisambaa kila kona ya maeneo yale na hivyo zilimfikia baba mzazi wa Robinson mzee Kaaya ambaye moja kwa moja aliwataarifu wakina Jackline na Robinson.


Jackline alimuomba mzee Kaaya aende polisi kuripoti na ikiwezekana amuunganishe na mkuu wa kituo ili aweze kujua ikoje hiyo taarifa mpaka picha zao kukutwa kwenye begi la marehemu. Na kweli alifika pale na kupata maelezo ya kutosha juu ya tukio lilivyotokea na ndipo mzee Kaaya naye akatoa maelezo yake kwa namna anavyoijua stori hiyo na kisha akamuunganisha na Jackline ambaye muda huo alikuwa mkoani Dodoma.


Jackline aliweza kuelezea kila kitu kuanzia vifo vya wazazi wake na namna walivyodhulumiwa mali zao na mzee Jonathan Ubao na kutoa hisia zake kuwa huyu mzee anahusika na hili.


Hivyo kuahidiwa kuwa jeshi la polisi litakuwa bega kwa bega naye katika kuhakikisha mzee Jonathan anapatikana kutokana na kuangalia namba ya mwisho iliyowasiliana na marehemu ilikuwa ni ya Jonathan ambaye baada ya kufanya mawasiliano na mamlaka ya mawasiliano kuikagua namba ile inaonekana ipo ndani ya nchi na wala si nje ya nchi bali anapatikana Kanda ya Ziwa.


Hivyo baada ya kuhakikishiwa na jeshi la polisi kuwa mtuhumiwa atatiwa mikononi muda si mrefu lakini Jackline alifanya mawasiliano na Simbozya kumueleza kilichotokea na hivyo Simbozya akafanya mawasiliano na Santana juu ya mkasa wa rafiki yake akashauri wamfuate Brazil ndani ya siku hizi tano ili mchakato ufanyike mapema kama ujuavyo jeshi la polisi linaweza lisiifanye kazi yake ipasavyo hivyo ilikuwa ni bora wajiandae ili kumkabili adui yao.


Hivyo moja kwa moja wakakubaliana kuwa badala ya kwenda Afrika ya Kusini ni bora waunganishe safari kuelekea Brazil na kisha Simbozya naye ataungana nao huko huko.


Na mwenyeji wao bwana Santana anaishi ndani ya mji huu wa Belem ambako anafanya shughuli zake mbalimbali, pamoja na shughuli hizo lakini pia Santana hukodiwa na Matajiri wakubwa wa eneo hilo katika shughuli zao fichivu mbele ya serikali.


"Mnaionaje hali ya hewa hapa Belem?" Aliuliza Santana.


"Si mbaya sana kwani inafanana na hali ya hewa ya nchini kwetu Tanzania." Alijibu Jackline.


"Naomba mpango wako ili niufanyie kazi usiku wa leo ili ikiwezekana kesho tuanze na program fupi fupi katika kuiweka miili Sawa."


Jackline alitoa laptop yake na kumkabidhi Santana na alipoipokea aliifungua na kuanza kuangalia baadhi ya vitu ambavyo vitamsaidia katika kuanza mazoezi yao.


" OK, iko vizuri sana nadhani itakuwa kazi ndogo sana kwa upande wako labda kwa Robbie ndo itachukua muda mrefu kidogo kwa kuwa yeye bado kabisa Hana kitu."


"Tutashukuru sana Santana kwani nina hasira sana na mzee Jonathan Ubao."


"Ondoa shaka hili limekwisha labda kama kuna jingine Jack?"


"Hakuna."


"Ila mawasiliano yenu namaanisha simu zenu hazitakuwa hewani ndani ya mwezi mzima mpaka tumalize programu na hivyo mtanikabidhi kesho OK."


"Brother kwanini?" Aliuliza Robinson.


"Robinson utaelewa maana baadaye na si kwa sasa." Alijibu Santana.


Baada ya maongezi hayo Santana aliwachukua wageni wake na kuwapeleka kwenye jumba ambalo wataishi kwa kipindi chote ambacho watakuwepo nchini Brazil.


Jumba hili lilikuwa ni zuri na la kuvutia sana lakini kilichomshangaza Jackline na kumuacha na mshangao Robinson ni juu ya jumba hilo kujengwa katika ya msitu huu wa Caratons karibu zaidi na mto wa Rio Amazonas.


"Kaka Santana ilikuwaje mjengo wa kifahari Kama huu ukajengwa msituni huku na si mjini?" Aliuliza Robinson.


"Brazil ni miongoni mwa nchi ambazo biashara ya madawa ya kulevya inafanyika sana na kushika kasi duniani japo haiongelewi sana. Na hili jumba lilijengwa na bilionea maarufu kwenye biashara ya madawa ya kulevya NduguTuyilagezi mwenye asili ya Bara la Afrika nchini Burundi."


"Haaa, yaani karibu na nyumbani kwetu Tanzania, alipenya vipi na kufika huku kufanya biashara hii?" Aliuliza Jackline.


"Familia yake yaani wazazi wake ndo walikimbilia huku mwanzoni mwa miaka ya 1886 na hivyo tunaweza kusema ni mwenyeji wa huku."


"Yuko wapi sasa huyu bilionea Tuyilagezi?" Aliuliza Robinson.


"Kwa leo pumzikeni kisha kesho nitawapeleka kwenye jengo lile pale juu ya kilima kwa ajili ya kutambua vizuri bilionea huyu au mnasemaje?"


"Bila shaka kaka Santana." Alijibu Jackline.


Baada ya kuwakabidhi sehemu ya kupumzika wenyeji wake aliondoka na kuelekea mtoni Rio Amazonas kwa ajili ya kuendelea na shughuli yake ya uvuvi.

Huyu Santana katika historia yake ni miongoni mwa wanajeshi walioacha kazi yake na kuamua kuwekeza katika shughuli ya uvuvi kama kivuli cha kazi lakini akiwa ni mfanya biashara wa madawa ya kulevya lakini yeye akiifanya kwa kificho sana.


***


Taarifa zake kuonekana kwenye magazeti karibia yote nchini Tanzania zilimtisha sana kwani wakati anaamua kufanya umafya huu hakutegemea kama hili lingetokea. Hii ilikuja baada ya vitambulisho vyake, picha zake na business card yake kukutwa kwenye begi la Surambaya na hivyo ikawa ni rahisi kwa waandishi wa habari kuzichapisha mbele ya magazeti yao huku gazeti mojawapo kuwa na kichwa hiki kilichokolezwa kwa maandishi meusi..."PICHA ZA BILIONEA JONATHAN ZAKUTWA KWENYE BEGI LA JAMBAZI SUGU NCHINI, JE NI MIONGONI MWA WAFADHILI WA MAGENGE YA UJAMBAZI?"


"Mume wangu utakuwa mgeni wa nani katika hili?"


"Yaani hapa mke wangu kichwa hakifanyi kazi na sijui nifanye nini da Surambaya Surambaya umeniachia msala mimi." Alilalamika mzee Jonathan.


"Mimi nadhani tulia lala nadhani mpaka kufikia kesho utakuwa umepata jibu Mume wangu."


"Ni kweli mke wangu lakini tayari picha na jina viko gazetini jamani."


Mara simu yake mke wa mzee Jonathan iliita na Mama huyu aliipokea simu hii baada ya kugundua ni shoga yake Shufaa wa Nzega.


"Mhhh, wa kwanza huyu hapa! Halloo."


"Halloo shoga yangu wa ukweli, pole na majukumu."


"Asante wangu, lete stori uko pande zipi?"


"Nipo tu nyumbani naangalia TV hapa, lakini kuna taarifa kutoka mkoani Mbeya inamhusu shemeji kulikoni?"


"Mimi sijaiona hiyo ni taarifa mbaya au nzuri?"


"Mhhh, washa TV uone lakini hata kwenye magazeti ya leo zimesambaa sana na ndiyo habari ya mjini."


"Basi ngoja niangalie kama nitaiwahi, Mume wangu nini kimemkuta jamani?"


"Haya shoga mimi nikuache, ila mwambie Shem kama Zina ukweli ateleze mapema."


HAYA SASA UHONDO NDIYO HUO.

TUKUTANE KATIKA SEHEMU INAYOFUATA



Katikati ya usiku wa manane Robinson alishtushwa na sauti za watu waliokuwa wakisikika nyuma ya chumba walicholala. Aliamka na kuelekea kwenye dirisha lile la nyuma ili abaini ni wakina nani.Alipolifikia alilifungua kidogo na kuchungulia kule chini, kwa mbali aliona watu wanne wakibishana Jambo fulani. Na kwa kuwa ilikuwa ni usiku na mwanga wa taa za jengo lile haukuwafikia vizuri hivyo ikawa ni tatizo kuona vizuri.


Robinson alianza kupata hofu baada ya kuona kuna muda walikuwa wakimulika taa zao usawa chumba chao.


Alirudi mpaka kitandani na kumuamsha Jackline aliyekuwa kalala fofofo hajui kinachoendelea duniani zaidi ya ndoto tamu aliyokuwa akiiota muda huo.


"Jack, Jack, Jack."


"Mhhhh."


"Amka baby haraka uone."


"Niache nilale bwanaa..."


"Baby amka bwana uone kule nje kuna sintofahamu." Aliendelea kumuamsha huku akimvuta.


Jackline alijivuta vuta kivivu kutoka pale kitandani huku akimlaumu mpenzi wake kwa kumkatisha ndoto yake. Robinson hakujali hizo lawama zake aliendelea kumvuta mpaka dirishani na kumfunulia pazia kidogo na kumtaka aangalie nje.


"Angalia kule nje unaona nini?"


"Ni kama kuna watu hivi."


"Endelea kuwafuatilia wanafanya nini pale."


"Robinson, tumekwisha wale si watu wazuri kwetu inavyoonesha wanataka kutuvamia maana naona wanaoneshana huku na wanamulika mulika huku pia."


"Baby, inamaana ndio mwisho wetu umefika? Tunafia ugenini bila hata miili yetu kuonwa na wazazi, ndugu jamaa na marafiki? Mungu wangu."

Robinson alianza kulia kwa kwikwi kwani taswira ya wazazi wake ilimjia kichwani na kuwaona walivyokuwa wakihangaika bila msaada wowote na yeye ndiyo alikuwa mkombozi wao na sasa alijiona mfu ndani ya ardhi ya ugenini, kilimuuma sana.


"Robinson acha kulia kama mtoto, wewe ni mwanaume shupavu mbele ya mtoto wa kike na tena mrembo simama na tuchukue hatua."


Maneno yale ya Jackline yalimtoa kwenye mawazo ambayo yaliuteka mfumo mzima wa fahamu na ghafla alijiona yeye ndiye kidume mle ndani na mwenye nguvu hivyo alisimama na kuanza kuvaa nguo zake na katika muda Jackline alikuwa tayari kajiandaa alikuwa akimngoja Robinson na alirudi pale dirishani kuchungulia nje tena.


"Kunja hilo blanket kwa urefu liwe jembamba, na kisha chukua hilo shuka na funika juu yake na kwa juu huo mto uweke tengeneza kama kichwa kisha funika shuka hilo jingine."


Robinson alifanya kama alivyoagizwa na Jackline na baada ya kumaliza alimwambia aangalie kama kapatia.


" Baby cheki kama nimepatia."


"Umepatia, lakini nilisahau huoni kama hapo kalala mtu mmoja, hilo blanket jingine fanya kama hilo kisha shuka lililobaki funika miili yote miwili."


Na baada ya Maelekezo yale kutoka kwa Jackline, Robinson akafanya kama alivyoambiwa.


"Waoo, umepatia baby." Jackline aliongea kwa sauti ya chini huku akiwa Mwilini mwa Robinson kwani alimrukia na kumaliza na bonge la kisss."


Robinson alibaki katoa tu mimacho akimshangaa Jackline ambaye alionekana mwenye furaha ilhali nje kulikuwa na Hatari.Na mwisho akajistukia baada ya kuona Jackline kamkazia macho.


" Asante sana baby." Alijikuta maneno yenye umombo ndani yake yakimtoka.


"Nifuate." Jackline alitoa amri.


Walitoka na kuubana mlango na kisha waliongoza mpaka kwenye sebule ya nyumba ile na kumwambia Robinson alale nyuma ya sofa kubwa lililo upande wa kushoto wa sebule ile. Robinson alifanya kama alivyoagizwa, Jackline aliondoka na kulifuata dirisha la pale sebuleni na kuchungulia kule nyuma tena.


Baada ya kuangalia kwa muda pale dirishani aliondoka haraka na kuelekea nyuma ya kabati na kujificha nyuma yake.


Ndani ya dakika chache walisikia kitasa cha mlango kikichezewa na kunyongwanyongwa.


Huwezi amini Robinson aliyekuwa nyuma ya sofa gimba lilikuwa linagonga na kurudi. Akiwa bado kautolea mlango ule uliokuwa ukichezewa ghafla ulifunguka na kuwafanya wale watu wenye nia ovu kuingia na moja kwa moja kuongoza mpaka kwenye kile chumba

Na walipofika pale mlangoni hawakuwa na la kusubiri zaidi ya mmoja wao kuupiga teke na mlango na ukakubali wakajaa ndani.


"Paaaaaaaa, pa pa papaaaaaaa." Milio ya risasi kutoka chumbani kule ilisikika,

Ghafla wale jamaa Walitoka na kukimbia kuelekea nje pasipo hata kurudisha mlango.


Tendo lile liliwashangaza Jackline na Robinson kwani hawakujua nini maana ya tendo lile na kwanini waliongoza chumbani kwao.


Jackline ambaye alionekana ni jasiri kuliko Robinson alinyata na kuufuata mlango na kutoka nje, lakini alirudi na kumfuata Robinson.


Alipofika pale nyuma ya sofa alichokikuta kilimshangaza sana kwani Robinson alikuwa keshazimia muda mrefu.


"Roby don't do that, utani wako si nzuri bwana hebu amka tuondoke."


Lakini Robinson hakuonesha dalili yoyote ya kushtuka na hapo Jackline akajua tukio lile limemshtua mpenzi wake na kupelekea kuzimia.


Alimfanyia huduma ya kwanza kwa muda wa takribani dakika ishirini na ndipo aliamka.


" Nimekufa tayari?"


Lilikuwa ni swali la kwanza la Robinson baada ya kuamka.


"Haujafa bado, na hauwezi kufa na kama ungekuwa umekufa ungeongea wewe?"


Jackline alimjibu huku akimuinua na kicheko kama chote kwa alichokingea Robinson.


"Baby tuondoke hawa jamaa watarudi tena."


"La msingi kaoge kisha badilisha hizo nguo kisha tuondoke."


Baada ya kauli ile ya Jackline, Robinson alipojikagua akagundua gimba lilikuwa limetua kwenye jinsi yake na kusababisha harufu mbaya mle ndani. Alijisikia aibu sana na akaongoza ndani haraka, na haikuchukua muda mrefu akarejea pale sebuleni.


" Pole sana mpenzi wangu, najua hali hii ni kwasababu ya ugeni wako kwenye matukio kama haya."


"Ni kweli kabisa, toka nizaliwe sijawahi sikia mlio wa risasi zaidi ya kwenye video."


"Kwa sasa utazoea tu, mwenzako tayari nina uzoefu na misukosuko kama hii."


Hesabu zikaanza kupigwa kwamba wakitoka wataelekea wapi wakati huko nje wao bado ni wageni kabisa. Lakini kilichowachanganya ni nani yuko nyuma ya mchezo huu mchafu,au ni Majambazi lakini kwanini wameongoza chumbani kwao moja kwa moja na kushambulia na kisha kuondoka? Hawakupata majibu ya maswali yao.


"Mbona hapa kama sielewi elewi hivi?"

Robinson aliuliza.


"Si wewe tu hata mimi mpenzi hili tukio limenichanganya sana kwani sifahamu ni nani anatufanyia mchezo huu."


"Mpenzi naweza kukuuliza swali dogo?"


"Uko huru mpenzi niulize tu."


"Hivi huyu mwenyeji wetu unamfahamu kwa undani kabisa?"


"Ngoja kwanza."

Jackline alifungua mlango na kutoka nje na baada ya dakika chache alirejea tena.


"Nilihisi kama kuna minyato ya mtu hivi lakini ni salama, kiukweli simfahamu hata kidogo nimemwamini tu kwa kuwa yuko karibu na mshikaji wangu yule msauzi."


"Hauoni kama tumekifuata kifo chetu wenyewe huku? Badala ya kuja kujifunza namna ya kukabiliana na adui yetu tumejaa wazima wazima kwenye mdomo wa Mamba."


Robinson aliongea hayo akiingia kwenye chumba ambacho walilala.


"Haa ile plani imefanya kazi yake mpenzi, huwezi amini risasi zote zimeishia kwenye mablanketi watu tuliyoyatengeneza."


"Hiyo nilijua tu, kwani siku zote wavamizi hufanya kazi kulingana na akili zao zilivyowatuma hivyo hawakuweza kujiridhisha kama waliowamiminia ni walengwa au la?"


"Hisia zangu zinanituma wanaweza kurudi kuhakikisha kama kazi imekamilika ili malipo yafanywe kama walikodiwa na katika hili nina hofu na mwenyeji wetu Santana."


"Siwezi kukupinga katika hili mpenzi kwani hata mimi akili yangu inaniambia hivyo hivyo, hebu tufanye tuondoke huko nje akili itatukaa sawa."


Walifungua mlango taratibu na kutoka kwa kunyata, kama walivyokubaliana kuwa wakifika nje itafahamika ni wapi waelekee.


JE, NINI KITATOKEA?


TUKUTANE KATIKA SEHEMU INAYOFUATA.



Jackline na Robinson walifanikiwa kutoka ndani ya lile jumba na zoezi lililokuwa mbele yao ilikuwa ni namna gani wataivuka fensi ya jumba hilo ambayo ilikuwa umbali wa mita kama 20 kulizunguka jumba na kwa haraka haraka ilionekana kuwa na ulinzi mkali sana.


Jackline na Robinson walifanikiwa kutoka ndani ya lile jumba na zoezi lililokuwa mbele yao ilikuwa ni namna gani wataivuka fensi ya jumba hilo ambayo ilikuwa umbali wa mita kama 20 kulizunguka jumba na kwa haraka haraka ilionekana kuwa na ulinzi mkali sana.


Hiyo haikuwapa tabu sana kuendelea kutafuta uchochoro wa kupenya.

Walifika kwenye majumba mengine ambayo kwa haraka haraka yalionesha ni kama vile yalikuwa yamehifadhi vitu ndani yake kwani yalikuwa karibu zaidi na fensi upande wa Kuelekea kwenye ufukwe wa Typhons.


Hapo ilibidi Jackline amzuie Robinson kwenye ile kona ya jengo mojawapo ya Yale mengine lengo ni kusogea mbele ili kujua kama kuna usalama ama la.


"Robbie jibane hapo kwenye hayo mabati usiondoke, nikaangalie usalama kule mbele."


"Jack tutatoka salama kweli humu ndani, angalia hatuna Silaha hata moja ya kujihami kweli?"


"Umeelewa nilikuambia Robbie?" Jack alimkatisha kwa swali.


"Nimekuelewa Jack, lakini......"


"Tekeleza hakuna cha lakini hapa."


"Sawa."


Jackline alisonga mpaka kwenye kona ya ghala lile na kuangalia kwa mbele kuna nini, alipotazama vizuri akaona kuna kajumba kadogo kama ka vyumba viwili hivi ila kana madirisha makubwa ya vioo katikati ya maghala mawili.


Kwa tahadhari kubwa alisogea mpaka kwenye kajumba kale na kujiviringisha kwa chini ili asionwe na yeyote aliye ndani yake.


Lakini Mazungu wa unga si watu wa mchezo hata kidogo na ndiyo maana hata serikali huwa hawaendi kichwa kichwa kwenye makazi yao hata siku moja.


Pale pale kwenye kijumba kile kabla ya kuinuka akaguswa kisogoni na kitu cha baridi ambacho kwa utaalam wake katika masuala ya mapigano alijua ameotewa na huo ulikuwa ni mdomo wa bunduki, jasho jembamba lilimtiririka Jackline.


"Unaonekana ni mzuri sana kwenye sanaa ya uchunguzi eee, hivyo hivyo ulivyo inuka taratibu huku mikono yako ikiwa juu ukileta jeuri nakupasua kichwa."


Jackline hakuwa na jeuri zaidi ya kutii amri, lakini akacheza na akili yake akakumbuka siku moja wakiwa ndani ya jiji la Pretoria nchini Afrika ya Kusini walivamiwa na kundi la vijana Mateja akiwa na mwalimu wake wa mapigano, akakumbuka namna walivyowapa kichapo wale vijana ambao walikimbia kila mmoja njia yake na wengine wakibaki pale hoi.


Mwalimu wake akamwambia Teja ujanja wake ni Silaha ukifanikiwa tu kumdhibiti hana jeuri.

Maneno yale yalipita kichwani kwa Jackline haraka na hapo akatabasamu mikono ikiwa juu.


Lakini kwa haraka ya ajabu kama umeme Jack alijipingua kama paka na kumgonga mlinzi yule teke la mkono, na mbaya zaidi mkono uliopigwa ni ule wenye Silaha na kuifanya bastola kuanguka pembeni.


Na hapo Jackline alimgonga yule mlinzi mateke ya sehemu za siri na kumfanya yule mlinzi kuishia kuanguka huku akitokwa na kilio kikali, hali ile ikampa ishara mbaya Jackline na haraka akamrukia na kumkata pumzi yule mlinzi na hapo akajua lazima kuna mwingine angekuja upande ule kuangalia nini kimempata mwenzake hivyo akajibana kwenye kona pale pale.


Kama vile aliotea, alitokea jamaa mmoja, huyu alikuja kichwa kichwa na kukutana na teke matata almaarufu kama Waving Cut na kumkuta usoni yule mlinzi na kumtupa chini na kwa kutopoteza muda alimrukia akampiga ngumi nzito ya pua iliyopelekea kumwaga damu nyingi pale chini na kwa kutopoteza muda akamnyonga shingo.


Akachukua ile bunduki yake na kurudi nyuma mpaka kwa Robinson na kumpa ishara ya kumfuata.

Jackline alikuwa tayari kachemkwa na damu kwani tayari alikuwa kawaweka chini watu wawili na alichokuwa akiwaza muda huo ilikuwa ni kumwaga damu tu.


Kifupi hali ilikuwa imechafuka na ilimfanya Robinson abaki kumshangaa tu Jack ambaye hakuwa yule aliyemfahamu kabla kwani huyu alikuwa katapakaa damu kifuani na mikononi.


"Robbie uwe mwepesi wa kusoma kila ishara ninayokupa tuko eneo hatari ukileta mchezo linarudi jina Tanzania."


"Niko makini Jack."

Alijibu Robinson na hii ni kama alilopoka tu kwani uhalisia suruali yake ya jinsi tayari ilikuwa imeshaloa.


Walitembea kwa mwendo wa kunyata Kuelekea kwenye kijumba kile tena ili kuweza kuangalia upande ule na mle ndani kulikuwa na nini na kwa nini ulinzi uliimarishwa Tofauti na walikotoka.


Walipokuwa wamechuchumaa chini ya dirisha, Jack aliinua kichwa kwa tahadhari kubwa ili kuchungulia ndani.


"Tobaaaa."


Sijui ulikuwa ni mshangao au nini kwani alijikuta akitokwa na neno hilo kimoyo moyo na ilikuwa ni kwa sababu ya kile alichokiona mle ndani.


Alirudisha kichwa chini na kumnong'oneza kitu Robinson na haraka wakajivuta mpaka mlangoni na kugusa kitasa na cha ajabu mlango ulikubali sheria ukafunguka.


Jackline akampa ishara Robinson aingie ndani kwa kujiviringisha kama tairi, haikuchukua muda Robinson akafanya kama alivyoambiwa na baada ya kuangalia huku na kule naye akaingia ndani ya kijumba kile.


"Jack mbona huyu yuko kwenye hali hii au ni tahila?"


Swali lile lilikuwa Sahihi kwa Robinson kwani hakuwahi kukutana na mtu ambaye ametopea kwenye utumiaji wa madawa ya kulevya.


Na mbele yao alikuwepo dada mmoja aliyefungwa kamba mwili mzima na kuzungusha kwenye kiti huku mate mepesi yakitiririka kutoka mdomoni na kufanya tisheti yake ilowe kwa mbele.


"Huyu ni mateka na hapo kapewa madawa ya kulevya na si hivi hivi kuna sababu."


"Sababu gani hiyo Jack?"


"Tulia utajua tu Robinson mbona muziki ndo umeanza tu."


Wakiwa pale kwa yule dada wakimfungua zile kamba, akawa kama anaonesha ishara fulani kwa mbele.


Jack alipoangalia kule anakooneshwa akaona kuna mlango uko wazi ikabidi aufuate kwa kunyata, na alipofika mlangoni pale alijiviringisha na kutua ndani ya kile kichumba, hali aliyoikuta kule ni hatari kwani alimkuta msichana mwingine akiwa naye kafungwa kitambaa cheusi usoni na kamba miguuni na mikononi lakini huyu alikuwa hajavutishwa unga.


Alimfungua zile kamba Pamoja na kile kitambaa usoni haraka na kabla hajammaliza vizuri akashtukia akipigwa ngumi nzito kutoka kwa yule dada. Jack akajua ameingia sehemu mbaya lakini akajitahidi akamuweka Sawa.


"Wewe ni nani, au umetumwa na Watu wa Santana uje utuchukue?"


"Watu wa Santana?"


"Ndiyo, unajidai huwafahamu eti ee na mshukuru dada mmempa madawa bila hivyo wala msingetuweza hata kidogo."


Jackline akagundua hapo kuna stori juu ya madawa, Santana na hawa wasichana hivyo akajidai haelewi chochote zaidi ya kumwambia yeye kaja kuwaokoa wao.


"Umekuja kutuokoa sisi wewe, unajidanganya ndugu unafikiri utatoka salama humu Ngomeni. Elewa wewe na sisi wote ni punda."


Wakiwa wanatoka pale sebuleni, Jackline akauliza punda kivipi na walifikaje pale. Yule dada aliyejitambulisha kwa jina la Jessica na dada yake ni Jasmine ni raia wa Tanzania katika mkoa wa Mbeya ndani ya wilaya ya Rungwe na akasema walifikaje pale si sehemu yake bali muda huo waangalie wanatokaje pale kama kweli kaja kuwaokoa.


"Kwa hiyo nini maana ya punda?"


"Kweli wewe ni mgeni huku mpaka hujui maana ya punda, Punda ni binadamu wanaotumiwa kusafirisha madawa ya kulevya kwa kupenda ama kutopenda."


"Tufanye mchakato wa kutoka humu ndani na tutoke nje kabisa ya ngome hii na huko tutajua la kufanya.Najua hawa jamaa wakirudi tumekwisha maana nimeua wenzao wawili tayari." Aliwaambia wenzake Jackline.


"Twende huku nyuma kwanza kuna jambazi moja ndilo linatulinda sisi na ni litumiaji likubwa la madawa kwa vyovyote limelala."

Aliongea Jessica.


Kweli walipofungua mlango wa nyuma ya nyumba hiyo wakamkuta yule mlinzi akiwa kalala kwenye viunga vya maua huku pembeni kukiwa na bunduki aina ya SMG na kisu kikiwa kiunoni mwake.


Kwa haraka Jessica alimkata pumzi kwa kumziba pua na mdomo kisha wakachukua zile Silaha na kurudi ndani. Mle Jessica akachukua dawa fulani hivi kutoka kwenye mfuko wa suruali ya Jasmine na kumuwekea puani na nyingine akamlisha mdomoni na ndani ya muda mfupi Jasmine alipiga chafya na kufumbua macho na ndani ya dakika kadhaa akawa kwenye hali yake ya kawaida.


Kitendo hicho kilimshangaza sana Jackline na Robinson ambaye muda wote alihisi alikuwa ndotoni maana kila kilichokuwa kikitokea mbele yake kilikuwa kigeni.


"Hapa ninafanya nini tena?"

Jasmine Aliuliza.


Swali hilo peke yake lilitosha kuamini Jasmine alikuwa katika lindi Zito la usingizi mzito uliotokana na madawa.

Wakiwa kwenye mchakato waanzie wapi katika harakati za kutoka mle ndani.


Ghafla walisikia mlio wa Helikopta ambao kwa vyovyote ilikuwa ikijiandaa kutua ndani ya Ngome.

Walipoangalia dirishani wakaiona ikiwa inaelekea kutua.


"Santana kaja, tumekwisha!!!!!"

Alitamka kwa hamaki Jessica.


Kundi jipya limezaliwa ndani ya jumba lile la Santana ambao ni Jackline, Jessica, Jasmine na Robinson.


Kundi hili linakwenda kufanya nini?

Ni kweli Santana yuko ndani ya Helicopter?


TUKUTANE KATIKA SEHEMU YA KUMI YA KIGONGO HIKI.



Jasmine aliangalia kule ndege ilikoelekea akajua huyo si mwingine ni Santana na ndege ilikuwa ndiyo inaelekea kutua kwenye Uwanja wake.


Moja kwa moja alijua nini kinakwenda kutokea muda mfupi uliofuata sababu anamfahamu vizuri sana Santana kwani kaishi naye muda mrefu zaidi ya miezi saba kama wapenzi hivyo anamfahamu ndani nje.


Na kilichosaidia baada ya kupewa dawa ile iliweza kumsaidia Jasmine kwani kila muda ulivyokuwa ukienda ndivyo hali yake ilikuwa ikitengamaa.


"Ndugu zangu Santana kafika hivyo naombeni mnifuate huku kuna Njia moja ni ya ardhini inayokwenda kutokea katikati ya msitu mnene wa San Antonio."


Hapo hapakuwa na mjadala zaidi ya wote kumfuata Jasmine kule alikowaambia wamfuate.


Ni kweli kwa kupitia mlango wa nyuma ya kijumba kile walitoka mbio na kuelekea kwenye kijumba kingine kidogo zaidi ambacho ukikiangalia kwa haraka unaweza dhani ni kijumba cha mbwa.


Humo ndani walikutana na mfuniko wenye ukubwa wa pipa la maji katikati ya kibanda hicho.


Jasmine aliufungua mfuniko huo na kuwaambia wazame ndani yake na kwa mazingira Yale yalionesha alikuwa ni mwenyeji wa mazingira yale.


Waliingia ndani ya lile shimo na cha ajabu mle ndani kulikuwa na nyumba nzuri sana ambayo ilikuwa na vyumba vya kutosha lakini hiyo haikuwafanya waduwaye pale bali haraka sana aliwaongoza wenzake mpaka kwenye chumba kimoja ambacho kilionekana kama bafu na humo kulikuwa na mlango ambao waliufungua na kuingia ndani yake, baada ya kuingia walikutana na pikipiki zilizopaki humo na kabla ya yote Jasmine alirudi nje ya chumba kile na kung'oa system ya umeme na kufanya eneo lile lote kuwa giza na akarudi ndani na kuwasha pikipiki ya kwanza ikawaka na akaifuata ya pili ikakubali.


"Nani anaweza kuendesha pikipiki kati yenu?"

Jasmine Aliuliza.


"Naendesha mimi dada naomba maelekezo ya wapi tunaelekea." Alijibu Jackline.


Kiukweli mle ndani kulikuwa na giza nene muda ule zaidi ya mwanga wa pikipiki zile ambazo zilikuwa tayari kwa msafara.


"Sasa mimi natangulia mbele wewe utakuwa unanifuata."


"Bila shaka."


Baada ya hapo Jasmine na Jessica walipanda pikipiki moja huku Jackline na Robinson wakapanda ya kwao na safari ikaanza mara moja.


Wote watatu walikuwa gizani hawakujua wanaelekea wapi, aliyekuwa akiijua njia ile ni Jasmine peke yake kwani waliitumia mara nyingi njia ile ya siri kipindi wakiwa kwenye mapenzi mazito na Santana na ilitumika kutorokea kipindi ambacho walivamiwa na Mazungu ya Unga toka Columbia.


***


"Wako wapi washenzi hawa, wanaleta kujuana hapa eti kaka Santana tufundishe mapigano tukaokoe mali zetu. Wananijua mimi." Aliongea Santana


"Wako chumba kile kile ambacho walilala." Alijibu msaidizi wake.


"Mzee Marhindo kutoka India kanipigia simu jana kadai tuhakikishe Figo na Mioyo hii tunaihifadhi vizuri mpaka watu wake watakapokuja ni bonge la dili." Aliongea Santana kwa kujiamini zaidi mbele ya watu wake.


Kumbe nje ya madawa ya kulevya, lakini pia Santana alijishughulisha na biashara ya viungo vya watu hasa Moyo na Figo.


Watu wake hawa walikuwa makini sana kwani walikuwa wakitumwa kuvamia walionywa wasiue na wasipige sehemu nyingine zaidi ya mapajani na miguuni tu na si vinginevyo.


"Chude hamkuwaua kweli?"


"Hapana boss tuliingia tukawatageti kwenye miguu na kufanya yetu na baada ya hapo hatukuwa na la ziada zaidi ya kutokomea gizani." Alijibu Chude msaidizi wa Santana.


Waliongoza moja kwa moja mpaka chumbani kule na kukifikia chumba kile na baada ya kukifikia, Chude kwa kujiamini kabisa mbele ya boss wake alifunua lile blanketi.


Lahaula, kitanda kulikuwa tupu, Chude alishangaa na kujiongelesha mwenyewe. "Hawapo?"


"Mbona siwaelewi, kuna nini hapo?"


"Boss mimi mwenyewe nashangaa walikuwepo hapa."


"Noo men, haiwezekani katika hili mmehongwa siyo?"

Aliuliza Santana akichomoa bastola kiunoni, na kwa kitendo kile kila mmoja mle ndani alijua nini kinakwenda kutokea.


"Hapana boss hatuja......" kabla mlinzi wa Chude hajamalizia sentensi yake risasi iliongea naye.


"Paaa, Paaa."

Sipendagi utani kazini miiiimiiiii aliongea kwa hasira kali Santana huku akijipiga kwa kitako cha bastola kifuani.


Muda huo yule mlinzi alikuwa tayari sakafuni akibubujikwa na damu.


"Nitoleee uchafu huu peleka kwenye mapipa ya takataka haraka."


Haraka sana walimbeba na kumtoa nje na kumpeleka kwenye mapipa ambayo huhifadhia Chakula cha samaki.


Huku nyuma alitoa visho vya kufa mtu.


"Na haki ya Mungu wasipoonekana tu nyinyi ndo nitawatoa kwa mkono wangu Figo zenu na Mioyo yenu nimuuzie Mhindi.Pumbavu potea haraka sana kuwatafuta kabla hawajafika popote."


"Sawa boss." Alijibu Chude.


Walitoka haraka sana na kuelekea nje kuwatafuta Robinson na Jackline ambao kwa wakati huo walikuwa ndani ya handaki wakiendelea Kupokea.


Wakiwa wanaendelea na msako kila kona wakashtuka kukutana na miili ya walinzi wa kijumba ambacho walihifadhiwa Jasmine na Jessica.


"Ooog my God, wameuwawa?"


Alijisemea mwenyewe Chude baada ya kukuta miili ya wenzao ikiwa imelalia damu.


"Hawa watu wanaonekana si wa kawaida hata kidogo." Aliongea mwenzake na Chude.


"Mfuate boss haraka mwambie hali si shwari kuna wenzetu watatu wameuwawa."


Taarifa hizi zilimchanganya Santana kwani ni tukio la ajabu kwenye ngome yake ambayo haijawahi angusha tone la damu ya wafanyakazi wake.


Haraka sana alikimbia Kuelekea kwenye kijumba kile ambacho walihifadhiwa Jasmine na Jessica na kumuacha yule mlinzi kaduaa pale pale.


"Oops, wamefanikiwa kutoroka? Mbona imekuwa rahisi hivi na huyu ni Jasmine tu."


Akijiuliza maswali yasiyo na majibu na baada ya kubaini mateka wake wametoroka wote alichanganyikiwa sana kwani Jasmine anamfahamu ni Mtukutu sana kwani kamfundisha yeye mwenyewe na mafunzo mengine alimpeleka nchini Columbia kujifunza zaidi kipindi ambacho aliamini wataowana lakini baadaye aliamua kuzika mawazo hayo baada kushindana kukubaliana juu ya kumgeuza punda Jessica, apeleke mzigo nchini China na asafirishe mzigo huo akiwa maiti.


Kila kitu kilienda sawa lakini mwishoni Jasmin alibadilisha uamuzi kwani hakutaka kumuona mdogo wake akitolewa uhai mbele yake kisa hela na ndipo alipomshindilia madawa ya kutosha kama adhabu.

Ni kama alikumbuka kitu alitoka ndani ya kijumba kile na kumfuata Chude.


"Tumekwisha Chude, wametoroka wote na huu ni uzembe wako. Hebu nenda control room kaangalie uelekeo wao."


"Sawa boss."


Chude aliingia control room na kuifuata Kompyuta ambayo iliunganishwa na system ya kambi nzima lakini ilikuwa nyeusi tu alipoangalia juu akagundua umeme umekata na hii ni baada ya kuona sensor imeganda na mwisho akaenda ukutani na kuwasha taa lakini wapi.


"Shabashi, umekata?"


Alitoka na kumfuata boss wake Santana ili kumpa taarifa hii ambayo haikuwa nzuri hata kidogo.


Taarifa hii baada ya kumfikia Santana alichanganyikiwa sana na hapo akajua kazi hiyo imefanywa na Jasmine ambaye asilimia kubwa alikuwa anafahamu kila kitu.


HAYA SASA MAMBO NDIYO HAYO, THE JAYS NA ROBINSON WAMEFANIKIWA KUTOROKA JE WATAFANIKIWA KUTOKA?

(THE JAYS NI JACKLINE, JASMINE NA JESSICA)


Nini kinaenda kufanywa na Santana?


Tukutane sehemu inayofuata





"Habari ya mihangaiko dada yangu." Mwanaheri alimtumia ujumbe mfupi dada yake.


"Nzuri mdogo wangu japo si sana." Aliujibu ujumbe huo wa mdogo wake.


"Si sana kivipi? Halafu dada mbona hata shemeji nilipompigia simu vitu alivyokuwa akiviongea sikuvielewa hata kidogo na mbaya zaidi alinizimia simu. Dada kuna nini?"


"Mdogo wangu ina maana hujasikia chochote kumhusu shemeji yako?"


"Sijui chochote dada kafanya nini mbona unazidi kunichanganya?"


"Mwanaheri mdogo wangu shemeji yako ni wanted' tafuta magazeti ya hivi karibuni yana kila kitu."


"Mmhh, ngoja nitafute tuone kuna nini humo."


Wakati akiwa anaendelea kuchati na dada yake mara akaingia rafiki yake Johari akiwa anahema kama vile kakimbia umbali mrefu bila kupumzika.


"My shemeji yako Jonathan Ubao ni Jambazi."


"Nini wewe?"


"Kama ulivyonisikia Mwanaheri kwani naamini huna matatizo ya kusikia na ukweli ndiyo huo."


"Shemeji yangu ni Jambazi? Wewe hizi taarifa umezitoa wapi?"


Badala ya kujibu swali Johari alichokifanya ni kumrushia gazeti alilokuwa amelishika kwa nyuma ili asome mwenyewe kilichomo humo kwenye gazeti. Mwanaheri hakuamini macho yake baada ya kukutana na maandishi makubwa meusi yaliyokolezwa vizuri yakiwa yameambatana na picha za mzee Jonathan yaliyosomeka hivi "MFANYABIASHARA MAARUFU NCHINI AUMBUKA"


Ikabidi aifuatilie taarifa hiyo kwenye ukurasa uliofuata kutaka kujua kilichomkuta shemeji yake na baada ya kuisoma alibaki mdomo wazi hasa baada ya kubaini kuwa mbwembwe zote za shemeji yake zinatokana na mali ya dhuluma na mbaya zaidi alilenga kuiangamiza familia hiyo ili awe huru. Na hapo hapo alichukua simu yake akatafuta namba ya shemeji yake na kumpigia.


"Makubwa!"


Alijikuta akitokwa na neno hilo baada ya kuona namba ile haipo kabisa hewani.


"Vipi kulikoni?"

Johari aliuliza.


"Nashangaa shemeji hayupo hewani."


"Atakuwa amebadilisha namba huyo, kwa skendo hii atakuwa hewani kufanya nini lazima ashuke chini na kujificha huko mapangoni, hivi shoga unataka kuniambia hili kwako ni geni kweli?"

Johari alimtupia swali rafiki yake Mwanaheri.


"Naomba niache kwanza nipumzike tutaongea baadaye shoga yangu."


"Okay sawa." Johari alichukua gazeti lake na kutoka nje na kumuacha Mwanaheri.


Mwanaheri alitafakari kwa muda juu ya alichokiona kwenye gazeti na akavuta taswira ya shemeji yake alivyo mpole, mcheshi mpenda kusaidia wenye matatizo hata yeye kufika chuo cha mipango bila mkopo ni nguvu ya shemeji yake huyu sasa iweje ahusishwe na matukio hayo hili likawa gumu kwake ikabidi ampigie simu dada yake.


Akaingia kwenye kitabu cha namba ndani ya simu yake akaitafuta namba ya dada yake na kumpigia.


"Ehee niambie mdogo wangu?"


"Hivi mimi ni mdogo wako kweli?"


"Ndiyo wewe ni mdogo wangu kwani kuna nini mdogo wangu?"


"Yaani unauliza kabisa, kwani kuna nini? Nahisi sisi si ndugu kabisa."


"Naomba nisikilize mdogo wangu, unajua nini? Baada ya kupata taarifa hii nilichanganyikiwa kwa kweli mpaka kujikuta nashindwa hata kuwapa taarifa ndugu zangu na huwezi amini kwa sasa tuko mafichoni Mwanza tukijiandaa kutorokea nje ya nchi."


"Unaona sasa mpaka mmehamia Mwanza, mnapanga kuondoka nchini kimya kimya dada yangu okay nimebaini sisi wote ni maadui zenu." Mwanaheri akakata simu na kuizima kabisa kwani hata dada yake alipojaribu kumpigia hakumpata.

Kitendo kile kilimuuma sana dada yake akainuka pale sebuleni na kumfuata bwana yake chumbani.


" Na hiki ndicho ulichokuwa unakitafuta siyo?"


" Kuna nini mke wangu?"


"Unauliza, haya maisha gani?"


"Sikuwahi kuwaza kama kuna siku nitaishi maisha ya kidigidigi kama haya mume wangu!"


"Ni kweli mke wangu uyasemayo lakini kumbuka pia chanzo cha haya yote ni nani?"


"Si mali za mzee Joachim?"


"Ndiyo lakini wewe ndiyo chanzo cha haya yote kumbuka ulivyonishawishi nimdhulumu mali binti yetu wa kumlea Jackline na ikiwezekana tumpoteze kabisa juu ya uso wa dunia yeye pamoja na familia ya mzee Fikirini kisha tuishi kama wafalme hapa duniani ila sikulaumu kwa maamuzi yako mke wangu najua ulitaka maisha mazuri ambayo tayari tunayo, kuhusu kutafutwa na hivi vyombo vya dola niachie mimi."


"Utafanya nini kwao mume wangu?"


"Mbwa chakula chake makombo akiona nyama huchanganyikiwa."


"Unataka kuniambia kuwa utapenyeza rupia katikati yao?"


"Unauliza juu ya hilo mke wangu kumbuka mimi ndiyo Jonathan Ubao kutoka kwenye maisha duni mpaka ku-take over ' kwenye vyombo vyote vya habari."


"Unafurahia, unaandikwa kwa mazuri?"


"Haijalishi katika hilo, ni matajiri wangapi duniani hukutwa na tuhuma kama hizi tena wengine kubwa zaidi ambazo hukumu ya haki huwa ni kunyongwa lakini hugeuza kibao na kumtafuta mbuzi wa kafara na kumtoa sadaka, na mimi napanga kufanya hivyo tu."


"Sijui ila kuwa makini mume wangu sitaki nikupoteze mapema kiasi hiki."


"Ondoa shaka kabisa mke wangu na hata hivyo leo usiku nitaianza safari kuelekea wilayani Chunya kwa ajili ya kulimaliza hili."


"Mume wangu utapita wapi ambako sura yako haipo? Usiniletee majanga mimi, tafuta njia nyingine na si wewe kwenda huko."

Wakati mke wake akiwa na wasiwasi juu ya safari ya mume wake lakini Jonathan ni mzee wa mipango tayari alikuwa amesha panga kubadili muonekano wake kwa kusuka rasta na kisha kuanza kutumia mavazi ya jinsi full kuanzia juu mpaka chini na kupigilia Raba au maviatu ya makubwa ya Ngozi na kuzipa likizo suti zake na briefcase na kutumia mabegi ya mgongoni.


"Mke wangu kuna mwanamitindo mmoja hapa mjini amelipwa kiasi kikubwa cha fedha kwa ajili ya kuubadili muonekano wangu hivyo atafika mahali fulani tulipokubaliana kukutana na kufanya kazi hiyo na baada ya hapo ndiyo utaamua uniruhusu au unikataze."


"Unamwamini mtu huyo?"


"Sana tu mke wangu."


"Okay but be careful."


Alijiandaa na kumuaga mke wake kuwa ndiyo mida yenyewe alitoka na kuelekea kwenye sehemu ya kukutana na mwanamitindo huyo ambako ni karibu kabisa na jengo la Rock City Mall kwenye kijumba kinachotumiwa na genge la kihuni na uhalifu linaloitwa TIA CHATA likiongozwa na huyu mwanamitindo aitwaye Rogers.


"Niko hapa kwenye viunga vya jengo la Rock City Mall."

Jonathan alitambulisha eneo.


"Okay sawa, hata mimi niko hapa hapa geuka nyuma na mfuate huyo chizi unayemuona."

Jonathan alichanganyikiwa kwani sehemu aliyokuwa akielekea huyo chizi ilikuwa ndogo sana kiasi kwamba gari yake isingepita. Na kingine alichojiuliza kwanini huyu chizi ahusike kwenye mpango huu, hakupata jibu na hata hivyo akaona ni mambo yasiyomhusu.


" Sasa gari niipaki wapi?"

Aliuliza baada ya kupigiwa simu na Rogers.


"Hiyo gari toka nayo nje ya jengo hilo ipaki kwenye Gereji iliyo hapo nimeongea na mwenye gereji kuwa kuna mgeni wangu atakuja na kupaki gari yake hapo kisha utafuata njia ile ile aliyopita chizi."


"Okay sawa."


Jonathan alifanya kama alivyoelekezwa na Rogers na baada ya kutoka pale ni kweli alikutana na gereji moja ambayo ni kama huwa haitumiki hivi hapo alipaki gari akapandisha vioo vizuri akajitengeneza na kuvaa kofia yake ya Mzula akashuka na kufunga milango vizuri kisha akarudi kule Rock City Mall na kufuata ule uchochoro kama alivyoelekezwa na mwenyeji wake.


***


Zile pikipiki zilikuwa zikitembea kule chini kama vile siyo chini ya ardhi na Jasmine alionekana kuzimudu zile njia barabara kwa namna alivyokuwa akikata mbuga huwezi amini na baada ya umbali fulani walifika sehemu moja hivi ambayo ilikuwa na barabara nyingine hivyo Jasmine akawaambia wasonge mbele kama hatua kadhaa kisha waziachie pikipiki zikiwa kwenye moto kisha wao waruke.


Hivyo Robinson na Jessica waliambiwa wabaki pale kisha yeye na Jackline waliondoka kasi na baada ya kama kilometa moja walifanya kama walivyokubaliana waliruka na kushika kushika Bomba zilizokuwa juu yao ambazo zimepitisha nyaya za umeme kule chini ila Jackline kabla ya kulidaka lile bomba aliteleza na kuanguka chini ilikuwa hatari kwani alijipigiza kwenye moja ya kingo za underground road ile.


"Mamaaaa........"


Alipiga ukelele ambao ulimshtua sana Jasmine haraka alikuja kumuangalia.


"Vipi besti kuna usalama kweli?"


"Usalama upo ila tu nilipigiza mkono kama unavyouona."


Alimuonesha alivyokuwa ameumia damu zilivyokuwa zinamtoka kila mmoja kati yao aliogopa ikabidi Jasmine aufute kwa kitambaa ambacho alijifunga kichwani na alipoona hakukuwa na mvunjiko alishukuru Mungu, Akakichukua kile kimbaa na kumfunga eneo lile haraka.


"Ashukuriwe Mungu haujavunjika Jackline."


Aliongea akimfunga kile kitambaa kwenye eneo lililokuwa likitoa damu.


"Afadhali maana nilikuwa nawaza itakuwaje sasa kwenye mpango wangu na ndoto zangu za baadaye."


Wakati wakiwa wanatiana moyo pale waliona moto mkubwa mbele yao, kumbe zile pikipiki kufika kule zilifika na kugonga kuta za ile njia ambazo zilisababisha msuguano uliozaa mlipuko.


" Jackline tuondoke haraka hii ni hatari."


Jasmine alipiga kelele na kuushika mkono ule ule wenye hitilafu na kuanza kumvuta mbio zikaanza. Huwezi amini Jackline alikimbia kumshinda mzima. Walikimbia na kuwakuta wenzao Jessica na Robinson wakiwa wanawasubiri walipowaacha.


" Ninyi kimbieni kuna hatari huku tunel imekamata moto hivyo kule kama waliunga umeme tumekwisha." Jasmine alionesha hofu.


"Mungu wangu tumekwisha."


Jessica naye alionesha hofu ya moja kwa moja baada ya kupata taarifa hiyo mbaya lakini kwa upande wa Robinson hakutaka kusubiri ushahidi wa Tomaso yeye alishika njia na kutimua mbio ndefu na kwa namna alivyokuwa akiwaacha wenzake ni dhahiri ana asili ya nchi jirani ambayo wenzetu kwenye suala mbio asikwambie mtu wako vyema.


"Robinson wewe ni kiboko unatimua mbio kiasi hicho hata kugeuka nyuma kuangalia dada zako tuko sambamba na wewe ama vipi?" Jasmine alimtania Robinson mara baada ya kumfikia na kupumzika kwenye kijengo fulani ambacho walikikuta kwenye uelekeo ule.


"Hivi hili andaki alijenga Santana kwa lengo gani?"


"Wala si Santana ni boss wake ambaye yeye Santana alikuwa akimfanyia kazi kama ujuavyo Mazungu ya Unga kuzungukana ni jambo la kawaida hivyo Santana alimuua bosi wake na kuchukua miliki yote pamoja na utajiri wake."


"Aliitwa nani huyo bosi wake?"

Aliuliza Robinson.


"Ni mzee mmoja mwenye asili ya Afrika kule Afrika Mashariki katika nchi ya Burundi alikuwa anaitwa Tuyilagezi."


"Hebu acheni stori zenu bwana mmejiachia kama vile tumetoka ngomeni kumbe bado kabisa."

Jessica aliwakumbusha.


Na kweli waliinuka na kuendelea na safari kuitafuta njia ambayo itawapeleka nje kabisa ya ngome ya Santana kwani kuna baadhi ya njia mle zinawapeleka kwenye majumba yaliyo ndani ya Ngome ya Santana.


JE NI NINI KITATOKEA?


TUKUTANE KATIKA SEHEMU INAYOFUATA.




Walitembea kwa muda mrefu sana, maana kutoboa mwisho wa safari haikuwa mchezo kwani usiku wa siku ya pili uliingia wakiwa bado kabisa ndani ya ile barabara ambayo ilikuwa ikielekea katikati ya mji Belem kwenye nyumba moja ya Santana ambayo huitumia kuhifadhia vitu vyake mbalimbali kama vile silaha, fedha, vito vya thamani pamoja na vyombo vya moto ambavyo ni magari,pikipiki nk kifupi ni kama ghala ambalo kwa nje ukiliona ni kama jengo la vyuma chakavu vilivyotelekezwa na familia fulani lakini huko ndani kulikuwa na ulinzi wa kufa mtu. Na kwa kuwa walikuwa wamechoka sana ilibidi wajipumzishe na kutafuta uwezekano wa kupata chakula kutoka kwenye vijumba vidogo vya mle ndani ambavyo Santana huhifadhia vyakula vyake ili kila apitapo asipate tatizo la njaa hivyo vijumba hivyo vilisheheni vyakula vya kila aina vilivyosindikwa kwenye makopo na biskuti za kila aina bila kusahau vinywaji. Ila kumbuka haya ni makazi ya wauza madawa ya kulevya hivyo usipokuwa makini unaweza fakamia vilivyochanganywa na madawa hayo ila kuwa Jasmine alikuwepo hakuna ambacho kingeshindikana kwani anafahamu kila kitu mle ndani kwa sababu vyakula na vinywaji vyenye madawa ya kulevya vina alama maalum ya fuvu.

Hivyo Jasmine na Jessica waliwaacha akina Jackline na Robinson kwenda kufuatilia chakula na sababu ya kumuacha Jackline ilikuwa ni jeraha ambalo alilipata kwenye ajali ya pikipiki wakati akijaribu kuruka.


"Sasa ninyi bakini hapa hapa kwenye hili chuma msitoke kwani huku tuliko kwa sasa kuna ulinzi mkali na doria hufanywa mara kwa mara ni miongoni mwa maeneo ambayo Santana huhifadhi nyaraka na baadhi ya vitu vyake vya thamani tuombe Mungu mpaka tunatoka humu wasiwe wameiwasha Underground Security System (uss) ambayo ndiyo huonesha kila chembe ya vitu vilivyo huku chini."


"Sasa Jasmine unajuaje kama hawajawasha?"

Jackline aliuliza kwa uoga aliposikia kuna security system na wanaweza kuonwa.


"Wakiwasha tu kuna kuna taa za blue ziko hapo juu huwaka na kumbuka mpaka sasa ni giza hii ni ishara bado hawajajua ni wapi nilikatia umeme."


"Jasmine tufanye fasta tuondoke huku chini watatuua hawa watu siyo wazuri kabisa."

Jessica alimsihi dada yake ambaye hakuwa na hofu hata kidogo.


"Usihofu mdogo wangu kwenye kidole changu hiki cha mwisho hapa ukiangalia hii ni Pete lakini matumizi yake hata Santana mwenyewe hajawahi jua, hii Pete imeunganishwa na mfumo wa hili jengo lote hivyo ninauwezo wa kuzuia system kutofanya kazi mpaka tutoke."


" Uliipata wapi sasa?"

Robinson aliuliza.


"Nilipokuwa namalizia mafunzo yangu ya mwisho kule Columbia nilizawadiwa hii Pete na Rolling Fante aliyekuwa mmoja wa wakufunzi wangu na aliniambia kuwa wauza madawa hawana ndugu hivyo hii itakuwa silaha yangu na ndivyo ilivyo mpaka sasa."


"Kweli duniani kuna mambo tembea uyaone na leo nayaona sikuwahi fikiria haya mambo kama yapo zaidi ya kuyasoma kwenye vitabu vya hadithi vya Kijasusi vya akina Willy Gamba."

Robinson aliongea akitokwa na machozi huku akimkumbatia mpenzi wake Jackline. Na Jasmine na mdogo wake waliondoka kwenda kufuatilia chakula wakiwaacha wapendanao wakiangusha chozi.

Haikuwa kazi nyepesi kama walivyodhani kwani kuvizunguka vibanda vyote waliona walinzi wakirandaranda japo kulikuwa na giza lakini waliweza kuwaona vizuri.


"Mdogo wangu hili giza litasaidia kuwaangamiza hawa walinzi mmoja baada ya mwingine."


"Tutafanyaje dada ilhali wenyewe wana silaha na sisi hatuna?"


"Sikiliza wewe baki hapa kisha shuhudia kazi ambayo dada yako ninakwenda kuwafanyia hao vikaragosi."


Jasmine aliondoka na kumuacha mdogo wake pale kwenye kona ya moja ya banda lililokuwa karibu yao. Jessica hakuamini anachokiona kwa dada yake na alichokuwa anajiuliza huu ujasiri kautoa wapi na hii roho ya kinyama ilimuingiaje kwani anakumbuka miaka kadhaa nyuma wakiwa wadogo walikuwa wafuasi wakubwa wa kwaya kanisani kwao na dada yake alipenda sana huduma za kidini mpaka siku moja alipanga akiwa mkubwa anatamani kuja kuwa mtawa na si vinginevyo lakini leo hii anamshuhudia akiingia katikati ya mianaume mikatili na yenye silaha eti kupambana nayo hii ilimshangaza sana Jessica pale alipokuwa.

Alimshuhudia dada yake akimtandika teke kali la kisogo mmoja wa wale walinzi na kwenda chini na hapo hapo akamshuhudia akimvua nguo zake na kisha kumvutia kwenye mapipa ya takataka kisha alirudi mpaka kwa mdogo wake na kumkabidhi zile sare.


"Jessica vaa hizi sare za jeshi la Ulinzi la Santana zitakusaidia kupambana nao bila wao kushtukia."


"Dada haitakuwa hatari, huoni mimi ni mwanamke na asilimia kubwa ya walinzi ni wanaume?"


"Mdogo wangu amka, fumbua macho iruhusu akili yako ifanye kazi haraka. Mdogo wangu jiangalie kisha tafakari."


Baada ya kuambiwa maneno yale Jessica alizichukua sare zile na kuzivaa kisha akazitengeneza nywele zake vizuri na kutupia na kofia kichwani. Japo mwanga ulikuwa ni hafifu lakini Jasmine aliweza kumuona mdogo wake vizuri.


" Waoo mdogo wangu si umeona sasa ni nani atakushuku kuwa ni mwanamke?"


"Nimetokea kidume dume eti eee?"


"Yaap, twenzetu mdogo wangu kazi ndo imeanza hivyo." Aliongea akimpigapiga bega mdogo wake. Walisonga mbele mpaka karibu kabisa na kile kibanda kilichokuwa kikilindwa sana na kumtuma mdogo wake aende karibu na lile banda kisha afanye yake.


"Lakini sina silaha dada."


"Okay, nilisahau ufuate huo ukuta karibu na hilo dirisha kuna silaha ya huyo bwege mwenye hayo mavazi niliiegesha wakati namvua nguo zake."


Jessica alifanya kama alivyoelekezwa na dada yake na baada ya kuiona haraka sana alijongea mbele kulingana na maelekezo ya dada yake. Ile anaukaribia tu mlango wa kile kibanda alitokea mlinzi upande wa pili wa kibanda kile.


" Mwamba umesahau maagizo ya bosi unaelekea wapi huko au unataka kubipu kifo ee shauri yako dogo."


Baada ya kusema hivyo aliwasha sigara yake na kuanza kuivuta, kufanya vile ilikuwa kosa sana kwani siku nyingi Jasmine alikuwa maeneo yale alimbana pumzi yule mlinzi na kumvutia nyuma ya kile kibanda. Jessica alimfuata na kumpongeza dada yake kwa kitendo alichokifanya.


"Hakika wewe ni zaidi ya Komando Kipensi yaani unawaminya mdogo mdogo na muda si mrefu tutakuwa ndani ya kijengo hiki."


"Na ndiyo maana nilikuambia vaa sura ya ujasiri mdogo wangu sasa unaona maana yake."


Alimueleza mdogo huku akimvua sare yule mlinzi na kuzivaa. Baada ya kumaliza kuzivaa alimuuliza mdogo wake.


"Nimependeza na mimi Jessica?"


"Sana dada yangu, yaani hapa najiona katikati ya GIRLS IN ACTION."


"Tusonge mbele sasa." Walisogea mbele na silaha zao wakiwa ndani ya mavazi yao ya kijeshi. Na kwa sasa hata wale walinzi ambao walikuwa wakiendelea kucheza karata kwenye gari ya wazi na mbovu iliyokuwa mbele yao kwa kutumia mwanga wa tochi hawakuwashuku hata kidogo kwani walipowamulika waliona ni wenzao wakiwa doria tu.



***


Baada ya kutembea kwa muda kidogo alikutana na yule chizi kisha akampa kikaratasi chenye maandishi kisha yule chizi akaondoka zake. Kikaratasi kile kilikuwa kina maandishi yaliyosomeka hivi,


"KABLA YA KUFIKA KWENYE LANGO KUU LILILO MBELE YAKO TOA SILAHA YAKO NA IACHE HAPO HAPO TOFAUTI NA HAPO UTAKUWA RAFIKI WA GIZA LA MILELE."


Baada ya kusoma kile kikaratasi aliangalia mbele na kuona geti chakavu lenye rangi ya bluu na pembeni yake kulikuwa na walinzi wawili wenye silaha. Alipogeuka nyuma alishangaa kumuona yule chizi akiwa na silaha aliyomuelekezea kichwani.


" Tii amri mjomba vinginevyo nitausambaratisha ubongo wako mzee."


"Mbona sielewi kinachoendelea huku?"


"Si muda wa maswali na majibu hapa dingi hayo tunawaachia wapiga suti huko Mjengoni Dodoma lakini hapa ni kutii amri tu."


Hapo mzee Jonathan Ubao akajua tayari kanasa kwenye kundi la wahuni wa jiji na hivyo hakuwa na jinsi zaidi ya kutoa bastola yake na kisu na kuviweka chini huku mikono mkono wake mmoja ukiwa juu.


" Tulia hivyo hivyo dingi ukileta kujua umekwisha." Yule mtu aliyedhani ni chizi kumbe hakuwa bali ilikuwa ni mbinu ya kumnasa Jonathan.

Alimsogelea na kumfunga kitambaa cheusi machoni na kisha kumuamuru ainuke na baada ya kuinuka aliwaita wale walinzi wakambeba na kumpeleka moja kwa moja kwa bosi wao aliyekuwa ndani ya jengo lile.


"Karibu sana bwana Jonathan Ubao."


"Asante sana, mbona unanifanyia hivi?"


"Hii ni ngome kuu ya kihalifu mzee, mfungueni kitambaa."


Amri ilitolewa na akafunguliwa kitambaa na baada ya kufunguliwa alishangaa kukutana na sura za vijana wadogo wakiwa wamemuweka mtu kati. Na kwa jinsi walivyoonekana ni kama waliopitia mateso makali sana na sasa waliamua kufanya Umafia.


" Mzee hili ni kundi linaloitwa FINGA PRINTI kazi yetu ni kucheza na silaha tu na baada ya kusoma magazeti yaliyochapisha habari yako tuliapa kukutafuta kwa udi na uvumba ili tulambe bingo."


"Mshenzi mkubwa wewe dogo yaani mwili wako hauendani na matendo yako."


"Nimekuwa mshenzi toka nilipotelekezwa na wazazi wangu hivyo kuniita jina hilo mzee wangu ni kama unakitukuza cheo changu, kwetu sisi Mkwanja ni kila kitu hivyo utatoka hapa iwapo tu utatii amri ya kundi."


Mzee Jonathan Ubao hakuamini alichokutana nacho kwani kimekuwa ni tofauti na matarajio yake.


MZEE JONATHAN MIKONONI MWA FINGA PRINTI, JACKLINE NA WENZAKE NGOMA NZITO PIA.

NINI KITATOKEA?


Sehemu ijayo inakuhusu msomaji.






"Mzee Jonathan karibu sana kwetu wapenda mpunga aka Ngawila, kama ulivyosikia na kuona dau lililotangazwa kwa yeyote atakayetoa taarifa zako na kupelekea kukamatwa hapa tumepanga kukukabidhi mikononi mwa jeshi la polisi ukajibu mashtaka yanayokukabili mzee."


"Kwanini mmenifanyia hivyo lakini ninyi vijana?"


"Hakuna kitu kingine zaidi ya mkwanja mzee na tunavyoongea hapa tayari gari lako liko mikononi mwetu pale ulipolipaki halipo mzee wangu."


"Kwa hiyo mnataka niwafanyie nini ili kuniachia na kushiriki kwenye kazi yangu?"


"Kwanza kabisa weka mezani kiasi cha shilingi milioni mia nne keshi na baada ya hapo tuzungumze biashara nyingine."


"Wadogo zangu mimi ni bilionea maarufu nchini hivyo mnatakiwa mjivunie kufanya kazi na mimi ila tu kwa upande wa kiwango mlichopendekeza ni kikubwa sana hebu rekebisheni kidogo walau mia moja hamsini milioni inawezekana kabisa."

Mzee Jonathan ilibidi aanze kuwapanga watekaji ili wapunguze kiwango ili waende sawa.


" Mzee Jonathan haitawezekana kutoa hata chembe na ujue kuwa hapo ulipo hautatoka salama."

Mzee Jonathan alichanganyikiwa baada ya kuambiwa hayo tofauti na yeye ambavyo alijua kuwa anakuja kubadili muonekano wake ili apate kusafiri kwenda mkoani Mbeya katika wilaya Chunya kwa ajili ya kuiangamiza familia ya Jackline ili akifanikiwa aweze kuwa huru na Mali za rafiki yake Joachim.


"Basi isiwe tabu mwanangu naomba niongee na mke wangu aweze kuleta kiasi hicho cha fedha ili mambo mengine yasonge mbele."

Ilibidi mzee Jonathan ashuke chini na kukubali kutoa kiasi hicho cha hela ili kuinusuru pumzi yake hivyo akaomba awasiliane na mke wake alete kiasi hicho.


" Utatumia simu yako mwenyewe ila ukileta jeuri naondoka na kamoyo kako kwenye presha kwa sasa."


"Siwezi fanya hivyo ndugu zangu hata mimi mwenyewe nina akili zangu za kunitosha unafikiri siupendi ugali?"


"Okay mpigie sasa hivyo ukimuagiza tu maelezo mengine utaniachia mimi nimuelekeze namna ya kuzifikisha hapa."


Mzee Jonathan alitoa simu yake na kubonyeza namba akapiga na kuiweka simu sikioni lakini kabla hajaipokea alishtukia simu haiko mikononi mwake, alipogeuka alishangaa kuona imeshikwa na yule Nyemela mkuu akiangalia simu ilipigwa wapi na baada ya kujiridhisha aliiweka loud speaker ili wote wapate kusikia maongezi yale.


"Mbona hivyo vijana wangu ina maana hatuaminiani?"

Jonathan Ubao aliuliza.


"Nani akuamini wewe mzee mzazi wangu mwenyewe simuamini sembuse wewe? Wewe ongea na waifu wako kapokea simu tayari."


"Halo mke wangu."


"Ndiyo mume wangu nakupata, vipi umefanikisha zoezi lako?"


Alipoulizwa swali hilo na mke wake ilibidi amuangalie kwanza mkuu wa kosi la watekaji kuona atasemaje lakini Nyemela alitikisa kichwa kumuashilia akubali na ndipo alipoendelea.


"Huku mambo yanakwenda kama nilivyopanga na tuko katika hatua za mwisho na Mungu akijalia tu nategemea safari itakuwa kesho lakini nitarudi nyumbani kwanza kwa maandalizi ya safari."


"Hongera mume wangu kwa hatua hiyo ila uwe makini na kila hatua unayopiga."


"Niko makini sana mke wangu, sasa nakuomba uende kule ofisini kaonane na mhasibu mwambie akutolee kiasi cha shilingi milioni mia nne na kikiwa tayari nipigie simu nikuelekeze kwa kuzipekeka maana kuna mtambo mmoja niliuagiza kutoka nje sasa nimetumiwa ujumbe kuwa kila kitu kiko tayari na mzigo umewasili."


"Sawa mume wangu ngoja nielekee huko mara moja lakini unaonaje kama ukimpigia kabisa umpe taarifa ili nikifika nisichukue muda mrefu na si unamfahamu ndugu yako yule alivyo kauzu kama wewe?"


"Basi ngoja nimtaarifu sasa hivi." Baada ya kumalizana na mke wake alikata simu na kumgeukia Mtekaji.


"Naomba tafuta jina lililoandikwa Tariq nimuelekeze."


Jamaa hakuongea chochote zaidi ya kuchukua simu na kulitafuta jina hilo na baada ya kulipata akapiga na kumkabidhi hakusahau kuiweka loud speaker. Baada ya kupokewa upande wa pili mzee Jonathan alitoa maelezo ambapo hakukuwa na pingamizi lolote lile kisha simu ilikatwa na kuwekwa mfukoni.


"Mnaonaje zoezi la pili likiendelea tunaposubiri mzigo?"


"Haraka yako ya nini mzee wewe tulia hapa mzigo ufike mengine yafuate na si vinginevyo hapa."


Mzee Jonathan aliishiwa pozi akatoa kitambaa kwenye suruali na kufuta jasho maana ilikuwa ni dakika chache tu toka awasili lakini jamba jamba aliyokutana nayo ilikuwa ni shidaa.

Simu ya mzee Jonathan iliita na alipoangalia mpigaji alikuta ni mke wake akaipokea haraka.


"Tayari mzigo ninao kwenye gari naupeleka wapi sasa?"


"Okay Safi mke wangu, sasa njoo moja kwa moja mpaka hapa Rock City Mall kisha nitakupa maelekezo mengine."


"Sawa mume wangu ngoja nijongee nikifika nitakujulisha."


Alikata simu na kuiweka pembeni yake na pale alipokuwa kakaa nadhani ni kuepuka usumbufu wa weka toa.


"Mzee Jonathan una akili sana kwa maelezo uliyompa mke wako."

Mtekaji alimsifia mzee Jonathan japo mwenyewe alikuwa kafura kwa hasira ila alishindwa afanye nini mbele ya mtekaji huyo mwenye ulinzi kila kona na katika maisha yake Jonathan hakuwahi amini kama kuna kitu kinaitwa kushindwa mbele ya mkwanja au kutoa kiasi kikubwa namna hiyo. Maana kwake ilikuwa akikupa kiasi chochote kile jua zitarudi tu kwa namna yoyote ile ila kwa hawa hakuwa na ujanja kwani yeye ndiye mwenye shida na anatafutwa kila kona.


"Ndivyo nilivyo bwana mdogo kuna nyakati huwa natumia akili ya ziada kupanga na kufanikisha mipango yangu. Na kwa namna mlivyo nimefurahishwa sana mpaka nimefikiria baada ya masuala yangu kuisha ningefanya kazi na ninyi kama hamtojali."


"Ni wewe tu mzee, sasa ni hivi akifika tu tutatoka wote huku mpaka pale Mall na wewe ndiye utakayekutana naye na kupokea mpunga wetu na kuuleta isipokuwa tu ukileta jeuri majibu atayapata mkeo."


"Ondoeni shaka juu yangu kila kitu kitakwenda kama kilivyopangwa."


Wakati wakiendelea kupangana na kuwekeana vitisho simu iliita tena.


***


"Chude hivi hawa wapuuzi haijafahamika tu ni wapi walielekea? Na ninaapa iwapo hawataonekana hawa nitawafanyia kitu mbaya ninyi ambacho hamtokisahau maishani mwenu."


Santana alikuwa akilalamika wakiwa bado wanawatafuta wakina Jasmine kwenye maeneo mbalimbali ya Ngome yake.


" Bosi nimepata wazo jipya hapa."

Chude aliongea muda huo akiwa anakichezea chezea kisu chake na muda huo Santana jasho lilikuwa likimtoka japo ilikuwa ni alfajiri kukiwa na kibaridi kikali lakini kwa Santana ilikuwa tofauti kabisa.


"Wazo gani hilo Chude, kumbuka mimi sihitaji mawazo hapa nawahitaji wale wajaa laana."


"Najua bosi lakini kwenye hili la system kukata na kupelekea kila kitu kuwa off huoni kama shemeji Jasmine anahusika hapa?"


"Yote yanawezekana Chude, unataka kusemaje?"


"Nahisi kuna sehemu aliingia na kublock system kisha kuwapa nafasi wenyewe kushuka kwenye kambi zetu za chini."


"Yes, yes ni kweli kabisa Chude maeneo mengi Jasmine anayafahamu na kwa vyovyote vile lazima alikwenda kublock ile main switch ya chini ambayo ndiyo roho ya kambi nzima. Hebu nendeni kule haraka mkakague."


Chude na wenzake walitoka na kuelekea kule iliko main switch kuangalia walichohisi kina ukweli ndani yake? Na huku Santana akiwa kachanganyikiwa kweli kweli akiwa hataki kuamini kilichotokea.


" Hivi hawa Kenge wamepitia wapi lakini hawawezi kuikimbia Ngome hii hata kidogo."

Santana alikuwa akiongea peke yake wakati wenzake wakielekea kule chini.

Walifika na kuichunguza main switch na kugundua kuwa ni kweli ilikuwa imechezewa haraka sana bila kuchelewa waliirekebisha na kuiwasha na papo hapo ngome yote ilirudi kwenye system na kila kitu kikawa sawa, Chude na wenzake wakarejea kwa bosi wao na kwa kuwa kila kitu kilikuwa tayari hakukuwa na haja ya taarifa kwani Santana alikuwa Ofisini akiifuatilia security system yake kuona kama anaweza ambulia chochote kitu.


"Huwezi ona chochote hapo Jasmine ni jeuri sana unaonaje tuelekee kule chini na wengine wabaki huku juu sana sana main gate kwa usalama zaidi."


"Okay uko sahihi maana toka nianze kuangalia hapa sioni chochote zaidi ya kuona walinzi wote wako kwenye maeneo yao ya ulinzi japo kuna eneo hapa sioni walinzi wake. Shukeni haraka mkaanze na eneo hilo mimi nitakuwa hapa kufuatilia na ngoja nimpigie Sharon kumuuliza kuna nini pale." Baada ya kumpigia simu hakuweza kupatikana hewani Sharon na hii iliendelea kumchanganya


Santana asijue nini kimetokea, lakini hakuwa na wa kumlaumu zaidi ya yeye mwenyewe kujilaumu kwa kumzalisha Jasusi hatari wa kike Jasmine anayekutana na mtoto wa kike mwingine hatari kuliko hata Jasmine ambaye kajeruhiwa zaidi ambaye ni Jackline.


Na kumbuka kuwa kule chini Jasmine na wenzake tayari wamefanikiwa kuvalia mavazi ya kikosi cha ulinzi cha Santana na wakati huo huo Jasmine kashaharibu mfumo mzima wa mawasiliano mle ndani hivyo ni ngumu kwa Santana na vikosi vyake kuwasiliana zaidi ya kufanikiwa kurudisha mwanga tu.

Santana alipogundua hilo la kutopata mawasiliano yoyote na yeye aliamua kwenda kule kule chini kuwatafuta adui zake mpaka kieleweke. Na kwa kuwa chemba zote anazijua vilivyo haikuwa shida kwake kuwakuta wakina Chude wakiwa wanazikagua pikipiki ambazo zilikuwa zimebakia mabati tu.


"Kuna nini kimetokea hapo Chude?"


"Bosi hapa kuna mabaki ya zile pikipiki zako ambazo huzipaki first room, na nikiangalia eneo hili hapa inaonekana zilitumiwa na wakina Jasmine lakini ziliwashinda na kupata ajali."


"Unataka kuniambia na wao watakuwa wamekufa?"

Santana aliuliza swali akiwa kamtolea macho kijana wake Chude.


"Sina uhakika bosi lakini yote yanawezekana."


"Hebu kagueni eneo hili lote kuona kama tunaweza kuona chochote cha kutusaidia iwapo wapo hai au la."


"Sawa bosi nimekuelewa."

Chude alimjibu Santana ambaye aliondoka pale na kuifuata alama fulani ambayo aliiona pembeni kidogo na pale kwenye mabaki ya pikipiki.


UNAFIKIRI NINI KITATOKEA?


TUKUTANE KATIKA SEHEMU INAYOFUATA.





Santana aliendelea kulikagua lile eneo na kisha kubaini kitu pale kwani aliona matone kadhaa ya damu ambayo hiyo ilimpa ishara kuwa wakina Jasmine hawajafa ni wazima hivyo haraka sana akawageukia wakina Chude pale walipokuwa wakiendelea kukagua mabaki ya pikipiki.


"Chude!"

"Naamu bosi."

"Msijidanganye kuwa wamekufa si kweli ni wazima hapa kuna matone ya damu ni dhahiri wamenusurika."

"Tufanyaje bosi?"

"Mfanyaje tena? Ni kusambaa kila kona kuhakikisha wanapatikana wakiwa hai ili zoezi langu likamilike."

"Sawa bosi." Chude aliwageukia wenzake na kuwataka kusambaa kwenye chemba zote kuhakikisha wanawatia hatiani wakina Jasmine.

"Chude sitaki mchezo katika hili endapo mtacheza faulo nawaangamiza ninyi."

Santana aliwachimba mkwara wakina Chude.

Ambao kama hawakusikia vile walikuwa bize kuingia kwenye njia zile zote wakiamini watawakuta kwenye eneo mojawapo.


"Chude wameelekea huku hebu angalia hapa." Mwenzake na Chude alimwita kuangalia sehemu ile ambayo ilikuwa na vumbi sana lakini kuna alama za mtu kugusa na kuacha alama kama ya kupukuta hivi.

"Shenzi taipu, wako huku mbele songeni mbele kwa tahadhari."

"Lakini kwa unavyomfahamu Jasmine atakuwa amekaa tu anatusubiri sisi kweli?"

"Nonda unaongea nini wewe maneno ya bosi ni amri wawe wapo au hawapo sisi letu jukumu ni kuwatafuta popote walipo."

"Sawa Chude lakini nilikuwa nauliza tu."

"Ndiyo hivyo Nonda unatakiwa kuchunga domo lako na unatakiwa kuangalia ni muda gani wa kubwabwaja."

Walisonga mbele kukagua ni wapi wanaweza kuwapata watu wao. Wakiwa wanapangua kona moja baada ya nyingine walifika eneo moja ambalo liliwatatiza kwani walikuta vitu vimesambaa sana na baada ya kuangalia pembeni kidogo Nonda aliona kuna silaha imelazwa chini.

"We Chude njoo uone huku."

"Kuna nini Nonda?"

"Kuna bunduki hapa na ni yetu lakini mhusika haonekani."

"Ohho kuweni makini hawa Mbilikimo hawako mbali." Chude alitoa tahadhari kwa wenzake.

"Jamani Antony huyu huku kapigwa risasi."


"Amepigwa risasi?"

"Ndiyo bosi na mwili umepoa kabisa inaonekana ni masaa kadhaa yaliyopita."

"Shiiit, wapumbavu sana hawa watakuwa wapi?" Chude alifoka baada ya kupewa taarifa za kuuwawa kwake Antony.

Wao wakiwa kwenye taharuki ya kifo cha Antony mara wakishtukia mwenzao mmoja anaanguka chini na baada ya kumkagua alikuwa anavuja damu.

"Hee kafa tayari naye?"

"Chude hawa watu ni hatari sana inaonekana wanatumia silaha zenye viwambo vya kuzuia sauti."

"Muacheni Antony jificheni hovyo hovyo tunakufa wote hapa....." Kabla Chude hajamaliza kuongea akashuhudia mwenzake mwingine akianguka chini, aliangalia huku na kule hakuna kitu.

"Mijusi hii imejificha wapi?"

Chude aliendelea kuwaza pale alipokuwa kajificha.


Wakati wakiamini kuwa Jasmine na wenzake bado wako kule chini wakiwa bado wanahangaika kutoka lakini ukweli haukuwa hivyo kwani tayari walikuwa kwenye chemba ya mwisho kuelekea kutoka nje. Na kutokana na mavazi yao ambayo walivalia ilikuwa ni rahisi kuwafikia walinzi na kuwaua kwa sababu yalifanana.


"Jackline jikaze mkombozi wetu hapa ndipo tunapotokea."

Jasmine alimjulisha Jackline ambaye alikuwa hoi kutokana na maumivu ya mkono.


"Afadhali jamani Mungu amekuwa upande wetu." Jessica alishukuru kwa kuifikia pointi ya mwisho.


"Baby jikaze ndo tunatoka hivyo Andakini." Robinson alimwambia Jackline ajikaze kwani alimuona anazidi kuumia zaidi.


"Baby hivi nitapona kweli mbona mkono naona kama unawaka moto?"


"Jackline utapona tu hapa cha msingi tukuwahishe hospital." Jessica alikazia na kumpa tumaini jipya Jackline.


"Mshikeni mshikeni mimi huku tayari." Robinson aliongea akiwa kambeba shingoni Jackline huku wakina Jasmine wakiwa nje wakijitahidi kumvuta.


"Mungu ni mwema jamani tumeliona jua tena." Robinson aliongea baada ya kuushuhudia mwanga wa jua.


"Hatuna muda wa kupoteza hapa tuondokeni eneo hili kwani nalo ni miongoni mwa miliki za Santana lile jengo pale ni lake hivyo tujitahidi kuvuka fensi ile pale ili tuifikie barabara ambayo tutaitumia kufika hospital."

Jasmine aliwataarifu wenzake ambao tayari walishajisahau.


" Na uzuri tuko ndani ya mavazi yao itakuwa rahisi kuvuka ngome yao." Jessica aliongea kwa kujidai kabisa.


" Acha ujinga mdogo wangu haya mavazi hutumiwa na vikosi vya ulinzi vya ardhini vya Santana hivyo tunatakiwa tuondoke eneo hili kabla hawajatushtukia." Jasmine alifafanua zaidi.


" Twendeni jamani, mwenzenu mkono unawaka moto." Jackline aliona afunue kinywa kuwaeleza namna anavyopata maumivu.

Papo hapo wakainuka na kuanza safari kuielekea fensi ambayo haikuwa mbali sana na pale walipokuwa. Jackline alijikongoja mwenyewe akiwa pamoja na wenzake.


" Dada pale kuna mavazi yameanikwa unaonaje tukayaibe kisha tuyavae na haya tuyatupilie mbali." Jessica alitoa wazo kwa wenzake.


"Achana na plani hiyo Jessica hapa bado tunazunguka kwenye mikono ya Santana hivyo msione kuwa tuko huru la hasha." Jasmine aliwang'ata sikio wenzake.


Ndipo wakaifikia fensi kabla ya kuonwa na mtu yeyote kwenye eneo lile. Na baada ya kutoka nje tu na kuifikia barabara ambayo ilikuwa ni ya vumbi. Na kwa bahati nzuri walipofika tu ilitokea gari ambayo Robinson aliisimamisha ikasimama na dereva akashusha kioo cha gari hiyo aina 110 defender (land lover).

"Niwasaidie nini?"

Aliuliza dereva huyo ambaye alikuwa amevalia kofia almaarufu kama Marlboro huku macho yake yakiwa ndani ya miwani ya jua myeusi.

"Mzee samahani tunaomba msaada wa lifti tufike mjini."

Aliomba Jackline akiwa kauweka nyuma mkono wake uliofungwa na kitambaa.


"Huwa sipakii watu nisiowajua kama nyinyi." Alipandisha kioo na kutaka kuondoka lakini alikuwa kachelewa kwani tayari risasi ilishapenya kupitia kioo na kwenda kumtandika eneo la singo, hakuwa mwingine zaidi ya Jasmine ambaye siku zote maamuzi yake huwa ni ya hatari sana.


" Mvuteni nje huyo anatuletea mashairi yasiyo fahamika ni ya nchi gani?"

Aliagiza Jasmine huku yeye akifungua mlango upande wa kulia kumtaka Jackline aingie.

Baada ya Robinson kumvuta nje yule mzee mwenye gari alimvutia kando ya barabara na kuja kupanda gari. Jasmine alipiiga mafuta gari na kupotelea mjini Belem na tageti yao ikiwa ni kumfikisha kwanza Jackline kwenye matibabu.


"Tukifika umbali wa kama kilometa moja hivi nyuma ya hospital ya Belem tutaiacha hii gari hapo na kutembea kwa mguu ili kuwapoteza boya maadui zetu."

Jasmine aliwapa taarifa wenzake namna watakavyoingia hospital.


"Plani hiyo imekwenda shule na lazima wapotee na ninajua lazima watatufuata baada ya kuiona maiti ya mzee hapo pembeni." Robinson aliunga mkono hoja ya Jasmine.


"Robinson naomba washa simu yangu na mtafute diga diga wa South Africa bwana Simbozya niongee naye."

Sawa baby ngoja nifanye hivyo.

Na baada ya kuipata alipiga na baada ya kupokelewa alimpa Jackline.


"Nambie Jacky hali ya huko ikoje?"


"Simbozya huku kwa kweli nashukuru bado tunapumua kwa sababu Santana ni bonge la Mafia lakini ndo hivyo."


"Mko wapi muda huu?"

Swali hilo lilimfanya Jackline atulie kwanza kujua ajibu vipi swali hilo kutokana na sababu kwamba hata yeye hawamuamini.


"Bado tuko ndani ya Ngome ya Santana tumejificha kwenye moja ya nyumba yake."


"Poleni sana na ndiyo maana nimewatafuta sana bila mafanikio kumbe mlikumbwa na janga? Poleni sana kikubwa ni uzima, ngoja nifanye mchakato wa kuona naweza kufanya nini kuwaokoa."


"Asante sana Mungu ni mwema kwetu."


"Kwa hiyo ni...."


Jackline hakutaka kuendelea kumsikiliza alikata simu na kumpa Robinson. Gari muda huo lilikuwa likipaki kwenye uchochoro mmoja ambao ndiyo walipanga kulitelekeza gari hilo kisha kutembea kwa miguu mpaka hospital na kisha kutokomea chimbo jingine.


***


Walipotokea kwenye uso wa jengo la Rock City Mal mzee aliambiwa ajongee mbele ili kukutana na mke wake.


"Narudia tena mzee ukienda tofauti jua mkeo hutamuona na wewe mwenyewe utajutia."


"Niache niende kisha mtaona iwapo nitawageukeni ama vipi?"

Mzee Jonathan aliongea akilisogelea gari la mke wake.

Watekaji wakiwa wametulia wakiusoma mchezo ambao anakwenda kuucheza mzee Jonathan iwapo utawapa matokeo au hautawapa matokeo.

Mke wake aliteremka kwenye gari huku akiwa na begi mkononi.


" Mume wangu uko salama lakini?"


"Niko salama mke wangu."


"Mzigo uko kamili kama ulivyoagiza mume wangu."


"Usihofu ngoja nimpelekee jamaa ili mzigo wangu usipate vikwazo vyovyote vile."


"Naweza kuongozana na wewe huko kwa huyo jamaa?"


"Hapana mke wangu wewe rudi tu nyumbani nadhani nikikamilisha mchakato nitageuka kwenda kwa dogo wa kunibadili muonekano kisha nitarejea nyumbani japo itakuwa kwa kuchelewa."


"Sawa mume wangu basi nikutakie mafanikio mema kwenye kila ulifanyalo."


Mzee Jonathan alikumbatiana na mke wake kisha wakaagana na mke kuingia garini na mume wake kuondoka na lile begi la hela kuelekea kule uchochoroni anakoshikiliwa.


"Mzee Jonathan umekomaa kivita kwa namna ulivyolicheza gemu ni hatari." Kiongozi wa watekaji alimsifia.


"Unanisifia au unaninanga?"

Mzee Jonathan aliuliza swali.


"Nakueleza ukweli mzee."

Alimjibu akimpokea lile begi na kuondoka nalo kuelekea kambini. Walifika kambini na kuliingiza ndani lile begi bila hata kuhakiki kwani kwa kiasi kile hawakuwa na haja hiyo kutokana na sababu kwamba hawana mashine ya kuhesabu hela.


" Mzee Jonathan nikuhakikishie zoezi lako la kuubadili muonekano wako litaanza kesho asubuhi na pia baada ya kukamilika utaungana na vijana wangu wanne kuongozana nawe kuelekea Chunya kuhitimisha kazi yako."


"Una uhakika kwa uyasemayo kweli?"


"Mimi ndiyo ninayeongea naomba amini hilo na kwa kuwa umetupa mzigo huu tunakuhakikishia kuwa hutatoa kiasi kingine mpaka ushindi upatikane ndipo utatupa Asante."


"Nitashukuru sana kama itakuwa hivyo."


Baada ya kukubaliana na kila walichokiongea kiongozi wa Genge lile la Kihuni mzee Jonathan aliomba apate sehemu ya kupumzika kutokana na akili yake kutokuwa vizuri na hii bila shaka ni kutokana na kutoa kiasi kikubwa cha fedha ambacho mpaka kuja kukirejesha si leo wala kesho. Na wakati wakiwa bado wanaangalia sehemu ya kumlaza mzee Jonathan kama alivyoomba, mara yule mfanyakazi anayekuwaga kama chizi hivi aliingia tena ndani akiwa anahema sana.


NINI KITAENDELEA?


TUKUTANE KATIKA SEHEMU INAYOFUATA.





"Mbona fasta kuna nini Majaliwa?"

Aliuliza kiongozi wao baada ya kumuona Majaliwa ambaye huigiza kama chizi mtaani kumbe ni shushu wa genge hili.


"Nimewaona askari watatu wakiingia mtaani kwetu kiongozi tunatakiwa kuwa makini usiku huu."


"Usihofu Majaliwa tutakuwa makini kikubwa endelea kuwafuatilia kujua wanasaka nini mtaani kwetu usiku huu kisha utanipigia simu siyo lazima uje."


"Sawa mkuu nimefanya hivi baada ya kugundua kifurushi kimekata."


"Okay nitakutumia salio ili ununue kifurushi cha wiki Majaliwa."


"Nitashukuru mkuu." Majaliwa alijibu akitoka nje na kurudi kijiweni kwake akiwa kwenye mavazi yale yale ya kichizi.


"Masanja muingizie Majaliwa kiasi cha shilingi elfu hamsini afanye mambo yake si unajua tena hatakiwi kuonekana madukani akifanya manunuzi ilhali yeye ni chizi."


"Dakika sifuri kiongozi atakuwa kapata kiasi hicho."


Masanja alijibu na kutoa simu yake na kuhakikisha anamfanyia ingizo la hela Majaliwa. Na ndani ya dakika kadhaa zoezi likawa limekamilika tayari.


"Mkuu tayari nishatuma."


"Okay sawa na ndiyo maana nakuaminia sana Masanja."


"Ni majukumu yetu hayo kiongozi."

Baada ya kuhakikisha mzee Jonathan amelala wao waliingia kwenye chumba chao cha vinywaji na kuanza kupiga vyupa kwa kusheherekea mkwanja walioupata siku hiyo.


"Majembe yangu mimi kama Karatu achana na cheo nilichonacho nina furaha kubwa sana hamuwezi amini ndugu zanguni kudaka shilingi milioni mia nne kwa kutumia maneno na si nguvu na pia ndani ya muda mfupi tu aaa kwanini tusifurahi?"

Kiongozi wao aliyejitambulisha kwa jina la Karatu alifungua sherehe.


" Mkuu na mimi kwa upande wangu niseme tu iwapo tutawapata watu waoga kama huyu mzee na kutii amri itakuwa poa sana."

Masanja alielezea hisia zake.


" Mimi mwenzenu nimepata wazo lililozaliwa kutokana na fedha tulizoingiza leo."


"Wazo gani hilo BlackMaster?"

Karatu aliuliza baada ya kumsikia injinia wao akitaka kutoa.


"Mnaonaje tuanze mradi mpya wa kuteka watoto na wake za matajiri na kisha kuwapigia simu kuwataka watoe kiasi fulani cha fedha tutakachohitaji na kisha wakitimiza tunawaachia watu wao."


"Jamani mmemsikia mwenzetu kaweka zoezi mezani kazi kwetu kulijadili."

Lakini wakiwa wanajiandaa kuanza mjadala wao mara simu ya Majaliwa iliingia kwa Karatu.


"Sorry jamani ngoja nimsikilize Majaliwa kwanza, nakusikia Majaliwa."


"Mkuu wale askari walikuwa wanakwenda kumkamata yule mama Nyangoro muuza gongo maarufu mtaani kwetu hivyo kwetu ni salama."


"Hongera sana Majaliwa kwa taarifa hii nzuri, sisi tunasherehekea ushindi wetu wa mamilioni wewe tutakuongeza kiasi kingine cha fedha walau uongeze sumu mwilini kama sisi."


"Nitashukuru mkuu ikiwa hivyo."


"Pamoja." Kisha alikata simu na kuendelea na majadiliano yao.


"Jamani Majaliwa anasema nje ni salama ila tu huzuni ni kwa bwana BlackMaster ambaye mtengeneza sumu wake mama Nyangoro katiwa bangili na wafunga buti."


"Duu sasa hii tabu tena tutafanyaje sisi wapenda gongo?"


"Tuendelee na majadiliano yetu jamani kingine nilitaka kuwajuza kuwa kesho asubuhi naanza zoezi la kumsokota dredi mzee Jonathan na kisha kumtafutia nguo za jinsi full juu mpaka chini na kadeti pia t-shirts za kutosha ili akiingia mtaani asishtukiwe na mtu yoyote."


"Kwa kazi hiyo nafikiri imepata wenyewe kwa ushauri wangu upande wa mavazi kazi hiyo akabidhiwe Masanja na kwenye muonekano hiyo yako kiongozi."


"Hiyo imepita Black ila sasa wewe pamoja na Kennedy mtaongozana na mzee Jonathan kwenye safari yake huko Chunya kumsaidia kazi yake."


"Maneno yako ni amri imepita hiyo, ila vipi juu ya hela ya kununulia vitu vyote hivi tunapanga sisi Je mzee mwenyewe awe hana salio?"


"Okay, jamani kwenye hili tutatumia fedha zetu ili kuendelea kumvuta zaidi mzee Jonathan aendelee kutuamini na ninyi wakina Kenedy ndiyo mtatuongezea fedha kwani iwapo mtafanikiwa huko ni hakika tutakunja mpunga mwingine tena kutoka kwake."


"Tunakuhakikishia mambo yatakuwa kama tulivyopanga kiongozi."

Kenedy alimhakikishia kiongozi wao kufanya vizuri.


Baada ya hapo vyupa viliendelea mpaka usiku mnene ambapo kila mmoja alikwenda kuutafuta usingizi.



***


Waliingia kwanza kwenye duka moja la mavazi ya kike na kununua nguo za bei poa kwanza ili wafanikiwe kuingia hospital na kutoka salama na kisha kutokomea sehemu nyingine ambako wataendelea na mikakati yao.


"Dada vipi kwa zote hizi gharama yake itakuwa shilingi ngapi?"

Jasmine alimuuliza muuza nguo zile za mtumba.


"Kwa zote itakuwa shilingi laki sita na sabini."


"Okay chukua kadi hii."

Jasmine alitoa kadi yake na kumkabidhi muuza achanje fedha yake.


"Tunaomba nguo zetu zibaki hapa tutazipitia tunaingia mara moja kati kwenye mambo fulani."


"Bila tatizo mtazikuta wekeni hapo kwenye hilo boksi pembeni."

Nguo zile ambazo ni sare ya Santana walizitelekeza pale dukani na kuishia zao hospital.

Waliingia na kuongoza moja kwa moja mpaka kwa Daktari wa mifupa na kumuelekeza tatizo ambapo alimkagua Jackline na kisha akamfanyia tiba na baada ya kumaliza walitoka, ila wakiwa eneo la OPD kuna taarifa ilikuwa ikirushwa na kituo kimoja cha TV maarufu kwa kama WORLD NEWS TELEVISION na taarifa iliyokuwa ikirushwa muda huo iliwashangaza kidogo.


"Mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la Nelson Murphy ambaye ni mkulima wa Karoti kutoka kijiji cha Naruto amekutwa kando ya barabara akiwa kauwawa na watu wasiojulikana, na inasemekana wauaji walipora gari lake ambalo waliliterekeza mtaa wa Wens. Tutaendelea kuwapa taarifa za tukio hilo ambalo mpaka sasa watuhumiwa hawajatiwa mbaroni."

Hawakutaka kupoteza muda eneo hilo haraka sana waliondoka kabla hawajabambwa na askari. Walipita mitaa kadhaa kisha wakakodi taxi ambayo walimtaka dereva huyo awakimbize mji wa Antonios. Dereva aliwataka walipie kabisa kiasi cha shilingi laki moja ndipo safari ianze na baada ya kulipwa safari ilianza. Walikwenda umbali wa kilometa kadhaa wakaona kuna Chek point mbele yao.


"Jamani ee mbele kuna kimeo tunafanyaje?" Jasmine aliyekuwa mbele aliwauliza wenzake.


"Dereva simamisha gari kwanza." Jackline alimtaka dereva asimamishe gari.


"Kati yetu kuna mwenye vitambulisho au vielelezo vya kuwepo mjini hapa kutoka uhamiaji?"

Jackline aliuliza wenzake.


"Sijajua ninyi lakini sisi tunazo."

Jessica alijibu haraka na Jasmine alipojikagua mfukoni hakuona kitu.


"We Jessica na vyetu tumeviacha kule chini chembani kwenye nguo zetu sijui tunafanyaje?"


Jackline akamfuata dereva taxi nafikiri alitaka kuongea naye kitu.


"Brother hakuna njia ya pembeni unayoijua ya kuwakwepa hawa askari?"


"Ipo ila ni ya mzunguko sana mtaongeza hela mara mbili ya makubaliano."


"Anasemaje dereva?"

Jasmine aliuliza.


"Anadai tudabo malipo kwani njia inayotakiwa tupite ni ya mzunguko sana."


"Haina shida twendeni jamani kikubwa tufike Antonios."


Dereva aligeuza gari na kuingia njia ya vumbi na kukanyaga mafuta ipasavyo. Kimya kilitawala kila mmoja akiwaza lake huku Jessica yeye akikoroma tu siti ya pale mbele na ikawa kama kituko kwani kuna muda alikuwa anamlalia dereva.


" Suka tunaweza kutumia masaa mangapi kufika Antonios?"


"Ni kama masaa saba hivi kama hakutakuwa na tatizo njiani."


"Duuu mpaka hapo tutaingia usiku si ndiyo?"


"Ndiyo maana yake dada yangu, mbona mmeogopa kupita pale Kituo cha Ukaguzi au ninyi ni Wazamiaji?"

Dereva akiwa anawaangalia kupitia kioo cha pale juu yake sijui ndiyo backview mirror' kinaitwa hivyo sijui aliwatupia swali.


"Wala si Wazamiaji sisi ni wanafunzi tunasoma hapo Belem chuo cha utafiti wa Mimea hivyo tumeona kwa kuwa leo ni wikendi tukawatembelee wenzetu wanaosoma Antonios University of Technology."


"Sasa si tungewaeleza tu kuwa ninyi ni wanafunzi wa Chuo jamani mpaka tumejihangaisha kupita huku?"


"Kwa kuwa tumeshaianza safari twende zetu kaka."


"Okay sawa."


Gari iliendelea kuchanja mbuga na muda walikuwa ndani ya eneo oevu ambalo lilikuwa limejaa maji.


"Sijui kama hii mbuga tutafanikiwa kupita salama maana udongo wake ni wa mnato sana na iwapo tutapita salama tu tutakuwa na kama dakika arobaini tu za kuingia Antonios."


"Jaribu tu kwa ufundi wako wote ikishindikana tutajua la kufanya hapo hapo."

Wakiwa wanaendelea kupeana taarifa za namna ya kupambana na eneo lile mara redio ya gari ambayo ilikuwa ikiwatumbuiza ilitoa taarifa ambayo ilikuwa ni breaking news' na hapo mazungumzo yakakoma kila mmoja akatega sikio lake.


"Taarifa iliyotufikia hivi punde inasema kuna mavazi ya kampuni moja ya ulinzi inayomilikiwa na Santana Group of Companies yamekutwa kwenye duka moja la nguo na muuza nguo huyo kasema Wenye hizo nguo ambao ni wasichana watatu na mvulana mmoja waliacha hapo kwa maombi kuwa watayarudia baada ya pilika zao hapo mjini kumalizika lakini mpaka sasa hawajaonekana na kulingana na taarifa ya jeshi la Ulinzi iliyotolewa inasema kwa eneo ulipokutwa mwili wa marehemu na eneo yalipo makao makuu ya Kampuni ya Ulinzi ya Santana ni dhahiri hao walioterekeza mavazi hayo wanahusika na tukio hilo hivyo Juhudi za kumsaka mmiliki wa kampuni hiyo zinaendelea, na kwa atakayekuwa na taarifa ya watu hao donge nono litamuhusu."

Walitazamana Jackline na Jasmine kisha Robinson wakajua issue ishakuwa mbovu na Jackline akamsogelea Jasmine na kumnong'oneza jambo sikioni.


" Tunatakiwa kufanya jambo hapa kabla hatujashtukiwa na huyu nyani."


Kabla hawajajua wafanye nini yule dereva akawaomba wamsubiri akajisaidie mara moja na kisha safari iendelee.


"Unaonaje twende pamoja maana hata mimi nimebanwa Suka?"

Robinson akawa amemshtukia tayari dereva kwanini abanwe baada ya kusikia taarifa ile?


"Okay tunaweza kwenda wote bila shaka."


Robinson akaongozana naye kuelekea porini na baada ya kufika kule vichakani dereva akaingia kwenye kichaka cha kwanza na Robinson akasogea mbele kama anakifuata kinachofuata lakini alivyochungulia mbele akamuona yule dereva katokea mbele akikimbia huku simu ikiwa sikioni na hapo akajua anatoa taarifa ikabidi amfukuzie haraka kabla hajafanya chochote na bahati alimuwahi na kumkata mtama uliompeleka chini na huku simu ikiangukia mbali naye.


"Ulijiona jeuri siyo, kwamba wewe ni ripota wa mambo ya watu siyo?"


"Hapana brother naomba nisamehe sirudii tena."


"Umechelewa brother wewe ni snichi."

Robinson alimpiga na kigongo kichwani kilichosababisha damu kuanza kutiririka kama bomba la maji lililokosa nguvu hivi. Jamaa alibaki kukoroma tu huku roho ikihangaika kujinasua kutoka kwenye mwili wa dereva huyo. Robinson alimuinua na kumbeba begani akaichukua na simu yake na kurudi naye kule kwenye gari.


"Well done my baby, sasa umekwiva."


"Nilijua tu lazima angecheza gemu la kitoto hili."


"Kuna nini tena jamani hapa si tuendelee na safari?"

Jessica aliyekuwa kalala alishtuka na kuona yuko peke yake garini akashusha kioo na kutoa kichwa nje.


"Cha kufanya ni kumtumia kwenye maji huko na hiyo simu yake chomoa laini nayo tupa kule."

Jackline alitoa wazo ambalo halikupingwa walifanya kama ilivyoshauriwa na Jackline na kisha walirudi kwenye gari na safari hii Jasmine alikuwa nyuma ya usukani kujaribu kupambana na tope lile.


" Zile bunduki tulizokuwa tumezihifadhi ndani ya ile gari watakuwa hawajaziona eti?"

Robinson aliuliza wenzake.


"Si tuliziweka chini ya siti ya nyuma?"

Jackline aliuliza.


"Ndiyo tuliziweka kwenye siti za nyuma japo nahisi itawachukua muda kugundua kama kuna silaha chini ya siti yawezekana na sisi tutakuwa mbali na msala huu ataubeba Santana tu."

Jasmine aliwatoa hofu wenzake na muda huo ilikuwa imebaki kidogo avuke eneo la tope.


Nini kitaendelea?


TUKUTANE KATIKA SEHEMU INAYOFUATA YA HADITHI HII.




Zoezi la kupita na gari ile kwenye tope liliweza kufanikiwa na safari iliweza kusonga mbele huku hofu ikitawala kwa kila mmoja kwani kwa muda huu walikuwa wakielekea Antonios pasipo kuwa na mwenyeji wa kuwaonesha baada ya dereva wa taxi ile kujidai mjuaji na kuambulia kifo. Lakini kwa kuwa tayari walikuwa wameyavulia nguo maji walijipa moyo na kuamini watasonga na kufika mwisho wa safari na hatimaye kupaa angani kuelekea Afrika salama kabisa.


"Hivi tutafika town bila kukutana na kikwazo njiani kweli?"

Robinson aliwauliza wenzake.


"Kwa maelezo ya yule dereva ni kwamba barabara hii huwa haifuatiliwi sana hivyo tunaweza kutoboa bila tatizo."

Jackline alimjibu huku gia zikiendelea kukanyagwa na Jasmine.


"Ila tunatakiwa kuwa na tahadhari." Robinson aliwatahadharisha wenzake.


"Ni kweli kabisa na ninafikiri hiki kigari tutakiacha mara baada ya kuingia tu mjini na uzuri itakuwa bado usiku itakuwa afueni kwetu."

Jackline alitoa wazo ambalo kila mmoja alilikubali.

Hivyo safari iliendelea na muda huu baridi nayo ilianza kuwa kali zaidi hali ambayo ilianza kuwatisha kwani kulikuwa na kila dalili ya mvua au ukungu na giza lilikuwa ni la saa tisa.

Mara wakiwa wameanza kuyaona mataa ya mji wa Antonios gari ilizima ghafla.


"Vipi mbona unasimamisha gari eneo hili?"


"Nahisi ni wese maana limekata moto lenyewe ghafla."

Jasmine aliwaeleza wenzake na hapo ndipo wakajua muda wa kudakwa umefika maana walipoangalia mbele waliweza kuona jiji la Antonios kwa mbali kiasi kwamba namna ya kulifikia ikawa ndiyo mtihani.


"Jamani ndiyo hivyo tena mafuta yamekwisha na hakuna ya ziada tunafanyaje hapa?"

Jackline aliwauliza wenzake juu ya kilichowakuta.


"Mimi nafikiri hakuna cha ziada zaidi ya kulitelekeza hili gari hapa hapa na tuanze mdogo mdogo mpaka tutakapofika mjini."

Jasmine aliwataka wenzake waianze safari pasipo kuangalia kuna umbali gani kutoka pale walipo.


"Najua tutachoka lakini hatuna jinsi jamani safari ianze au?"

Jessica aliona kama vile muda unachelewa akaona awatake safari ianze mara moja.


"Ni kweli jamani tunatakiwa kuanza safari maana mwenzenu nina hofu na hao jamaa wakitufuma hapa sijui itakuwaje?" Robinson alionesha hofu yake.


Safari ilianza na wakaona ili wafike salama inatakiwa wapite porini nje kidogo ya barabara kikubwa wasiiache barabara. Na msitu ulikuwa ni mnene kiasi kwamba kama ni muogaoga huwezi pita pori hilo.


"Mungu wangu hivi tutatoka salama kweli kwenye hili pori?"

Robinson aliuliza swali.


"Jamani tupunguze hofu kwanza ili tuweze kuvuka hili pori ila tukitanguliza hofu tu tutaishia humu."

Jasmine aliwataka wenzake waondoe hofu kwanza ili kuvuka msitu huo.


"Tukazeni buti jamani kwani hofu yangu mwenzenu ni juu ya maadui zetu."

Jessica aliona atoe lile linalomtia hofu katika safari yao.


Waliendelea na safari ya kupambana na msitu huo ambao walikuwa wakiangalia mbele ilikuwa ikiwatia moyo kutokana na mji wa Antonios kuonekana japo ilikuwa bado ni mbali kwa mguu. Wakiwa wanapita kwenye miti fulani ambayo ni mirefu sana karibu kabisa na barabara mara waliona gari likija nyuma yao, na hapo Jessica akatoa pendekezo la kulipiga mkono gari hilo walau liwasogeze kilometa kadhaa mbele.


"Gari hiyo inakuja mnaonaje tuisimamishe tuombe msaada wa kusogezwa walau umbali fulani."


"Tusijiingize kwenye mdomo wa Mamba hapa kumbukeni tunatafutwa kila kona na hofu yangu hata Santana atakuwa hajakata tamaa juu yetu hivyo umakini unatakiwa." Jackline alishauri wawe makini na maamuzi yao.


Lakini wakati wanaendelea kushauriana juu ya kuchukua tahadhari kwa kila wanaloamua. Ila waliposikiliza vizuri mlio wa hilo gari wakabaini kuwa halikuwa gari la kawaida bali lilikuwa ni gari kubwa.


" Jamani hilo ni gari kubwa la mizigo mnaonaje tulisimamishe?"

Robinson aliwauliza wenzake.


"Kama ni Lori tujitokezeni hilo ni salama ila lingekuwa ni gari dogo ingekuwa shida."

Jasmine aliunga mkono na hivyo walijivuta mpaka barabarani na kukaa kandokando wakisubiri hilo gari lifike waombe msaada.


"Hivi itakuwaje iwapo tutalisimamisha hilo Lori kumbe ni la Wanajeshi?"

Jackline aliwauliza wenzake japo ilikuwa kama utani hivi.


"Hivi Jackline mkono kwa sasa unauonaje?" Ilibidi Jasmine apotezee kwa swali maana aliamini kuacha swali hilo lijadiliwe lingeleta hofu kati yao na kupelekea kurudi porini wakati naye alikuwa anajikaza tu ila alikuwa kachoka.


"Kiukweli nashukuru Mungu naendelea vizuri tofauti na mwanzo ilivyokuwa."


"Jambo jema hilo na la kuangalia hapo ni kutokuugongesha na kuibua upya tatizo." Robinson alishauri.


Gari lilifika na Jessica aliibuka barabarani na kusimama katikati na kupunga mikono kuashiria kulisimamisha na lilipofika kama bahati lilisimama na ndipo Jessica alizunguka upande wa dereva ili kuongea naye.


" Habari yako kiongozi? "


"Salama binti mbona porini muda huu?"


"Sisi ni wanafunzi wa Chuo tulikuwa kwenye utalii katika mapango ya Nangiz na huko tukakutana na majinamizi yaliyopelekea kila mmoja kushika njia yake na sisi tuliokimbilia eneo moja ndiyo tunatokea barabarani muda huu."


"Poleni sana mko wangapi?"


"Tuko watu wanne tu."


"Okay hebu waite wenzako pandeni twende japo mimi sifiki mjini."


"Tutashukuru hata kwa hapo utakapotufikisha mzee wangu."


Hivyo Jessica aliwaita wenzake na kupanda nyuma kwenye magogo kwani mbele isingewezekana kutokana na gari hilo kuwa na siti ya dereva tu. Walipopanda dereva alishuka na kuja kuwaangalia kama tayari.


" Vipi tayari wote mmepanda?"


" Ndiyo mzee tayari." Jessica alijibu.


Na ndipo dereva huyo akiwa na sigara yake mdomoni alirudi kwenye usukani na kung'oa nanga.


"Kasema yeye hafiki mjini kuna sehemu atachepuka inaonekana kuna sehemu nje ya mji anajishughulisha na shughuli fulani hivi kutokana na magogo aliyobeba." Jessica alifungua mjadala kwa wenzake.


"Hapa tuwe makini sana na tena ikiwezekana kabla ya hajatushtukia inatakiwa turuke na kupotea zetu atakapokuja kuangalia hakuna watu."

Jackline aliwatahadharisha wenzake.


"Hiyo ni plani nzuri sana ila tatizo ni wapi anachepukia hatujui hivyo bado tu itakuwa ngumu kwenye mpango huo."

Jasmine alikubaliana nao lakini akaonesha hofu kutokana na kwamba si wenyeji na maeneo hayo na hawajui huyo mzee anachepukia wapi.


"Kwa hapo hatuna ujanja inatakiwa tuwe wapole tu liwalo na likawe kikubwa ni kujiandaa kukabiliana na lolote ndugu zangu." Jessica aliongea.


Baada ya umbali fulani hivi mwanga wa mashariki ulianza kuonekana kwa mbali kuashiria tayari jua linakaribia kutoka na kulitaka giza kuupisha mwanga nao uweze kutawala. Na hapo wakaona gari linapaki pembeni hali hiyo iliwapa hofu na kutaka kuruka na kukimbia lakini wakashauriana kutulia kwanza kujua kuna nini na walipochungulia chini walimuona dereva akipata haja ndogo na kisha akawa anakuja kule nyuma.


"Inawezekana kafika sehemu ya kuchepukia."

Jessica aliongea alipoona anakuja kule nyuma.


"Ngoja tumsikilize mwenyewe."

Robinson aliwauliza wenzake.

Na baada ya kufika pale nyuma dereva aliwataka washuke chini, na waliteremka na kumfuata alipokuwa. Aliwaangalia kwa muda kisha akageuka kuangalia pande zote kama vile ana hofu na kitu fulani hivi. Kitu kilichowapa hofu wakina Robinson kwamba kuna nini au mzee huyu amewatambua na anataka kuwakamatisha kwa maadui, hapo ikabidi Jackline ajitose kuuliza kabla mzee hajafanya lolote.


"Mzee vipi umefika sehemu ambayo unatakiwa kuchepukia?"


"Hapana bado kabisa."


"Kwa hiyo kuna nini mbona umetushusha na unatuangalia tu kama kuna kitu unasubiri hivi."


"Ni kweli kabisa binti nimefanya hivi baada ya kugundua utambulisho wenu kuwa ninyi si wanachuo bali ni watu hatari sana mnaotafutwa na jeshi la Ulinzi la Belem. Na muda si mrefu wametoka kuongeza zawadi kwa atakayefanikisha kuwatia nguvuni."


Maneno hayo ya mzee yaliingia vilivyo kwenye ngoma za masikio ya akina Jessica wakatazamana usoni kwamba nini kifanyike kwa mzee huyo na kabla hawajajua wamfanye nini dereva huyo, walikuwa wamechelewa kwani tayari alikuwa ameshamkata mtama mzee wa watu na kutua chini kama furushi la pamba.


"Mzee hujakosea kabisa sisi ni watu hatari sana na kwa kuwa umetufahamu lazima ufe."

Robinson aliongea naye akiwa ameshamtia kabali takatifu iliyomfanya mzee kutoa macho kama vile kamfumania mke wake.


"Lakini mzee bado una nafasi ya kutusikiliza kwanza inawezekana ukawa umepata taarifa zisizo sahihi juu yetu mzee hivyo ni wewe kutusikiliza yaliyotusibu kwanza kabla ya kutukabidhi kwa hawa wanaotutafuta au na sisi tukuue katika kujitetea mbele ya mkono wa sheria."

Jackline alikuwa kapiga magoti kumuelekea mzee pale alipokuwa kalazwa na Robinson.


" Naombeni mnisamehe bado napenda kuishi, kuna familia inanitegemea naombeni muongozane nami kwangu huko nadhani mtanieleza kila kitu kilichowakuta na ikiwezekana tutaangalia tunafanyaje maana hamuwezi kwenda kokote kule mnasakwa kama rupia wanangu."


"Tutakuamini vipi kwa haya uyasemayo?"

Jasmine alimuuliza.


"Niliwatambua toka mliposimamisha gari lakini niliamua kuwasaidia tu ila hapa nilitaka kujiridhisha kama ni ninyi kweli."


"Haya inuka utakuwa na mmoja wetu kule mbele japo hakuna siti atasimama."

Robinson aliongea kwa ujasiri mpaka Jackline alitabasamu kitu ambacho hakuamini kutokana na uoga aliokuwa akiuonesha siku za mwanzo.


"Nitakaa naye mimi ninyi pandeni, mzee twende."

Jackline aliona yeye ndiyo akakaye naye kule mbele ili akileta kujua aweze kumfundisha adabu. Walipanda na safari ikaanza tena baada ya kupata jamu isiyo rasmi.


Nini kitaendelea?


TUKUTANE KATIKA SEHEMU INAYOFUATA.




Baada ya masaa kadhaa waliwasili kwenye kambi moja ambayo ndani yake ilionekana kama kulikuwa na shughuli nyingi kama vile ni uzalishaji nguvu fulani au ni machimbo ya madini fulani hivi, kifupi lilikuwa ni eneo ambalo ni kama kambi fulani yenye kila aina ya mateso ndani yake. Lililowashangaza wakina Jackline ni wakati wakiingia ndani ndani ya Ngome watu wote waliacha shughuli zao na kukimbilia kwenye eneo ambalo lilionekana ni paredi hivi maana walijipanga kama vile wanajiandaa kuimba wimbo wa Taifa. Na mara gari liliposimama tu lile kundi lilipanga mstari mmoja kutoka kwenye gari lile na kuelekea ndani ya jengo fulani lililokuwa likitoa moshi kwa juu.


"Mwanangu tumefika tayari ngomeni tushuke sasa."


"Mbona kuko hivi na hawa watu mbona wamejipanga hapo chini?"


"Ni tayari kwa ajili ya kushusha magogo hayo tuliyobeba."


"Wote hawa ni wafanyakazi wako mzee?"


"Ndiyo mwanangu na hao unaowaona ni wachache tu kwani wengine wako mashambani huko wakilima."


"Unawalipaje wote hawa mzee mbona ni kundi kubwa sana?"


Mzee yule alimpigapiga bega Jackline na kumwambia asiwe na haraka sana kwani kuna mambo mengi sana na ya kustaajabisha sana ambayo akitaka kuyajua yatachukua miaka kadhaa kupata ufafanuzi wake. Hivyo alimtaka washuke chini ili kutoa nafasi kwa wafanyakazi kushusha magogo kwani walikuwa wakisubiri oda yake. Walishuka chini na mzee aliwasalimu kwa kuinua kofia yake na kundi lote liliinamisha vichwa chini ikiwa ni ishara ya kutoa heshima kwa mkuu wao.

Tendo lile kumbe hata wakina Jessica, Jasmine pamoja na mbabe wa vita Robinson liliwashangaza sana mpaka kuanza kuhisi kuwa walikuwa wamejipeleka wenyewe kwenye kambi ya mateso bila kujua.


"Hali ya humu ndani mnaionaje wenzangu?"

Jasmine aliwauliza wenzake baada ya kumuona Jackline akiwa sambamba na mzee yule kama kuna kitu anadadisi hivi.


"Hapa sielewi chochote kile maana kama vile niko ndotoni labda tumsubiri Jackline atuambie kinachoendelea humu."

Jessica alijibu huku akionekana kama kupata hofu hivi na hii ni kutokana na watu waliokuwa wakipita mbele yao na magogo mabegani afya zao zilikuwa zimedhoofu sana huku harufu mbaya ikitembea nao. Hapa walihisi hatari iliyokuwa mbele yao kwani hawakuona upenyo ambao unaweza kuwatoa mle ndani. Na mara alikuja kijana mmoja ambaye alikuwa kashiba sawa sawa akiwa na silaha begani ambayo ilifanana na old gun' maarufu kwa jina la Gobore.


"Habari yenu wakubwa!!"


"Kama utuonavyo." Alijibu Robinson.


"Karibuni ngomeni."


"Tumekaribia." Jasmine alimjibu kwa mkato.


"Okay sawa, mkuu anawaita kule juu." Aliwajulisha kuwa wanaitwa na mkuu wao huku akionesha uelekeo aliko huyo mkuu wao lakini kilichowashangaza ilikuwa ni kule kule alikoelekea Jackline na yule mzee. Walitazamana wote kisha yule mlinzi na ndipo Jessica alipomjibu.


" Okay tunashukuru, tunaelekea."


Yule mlinzi aliondoka na kuwaacha wakiwa hawajui waanzie wapi kuliepuka eneo lile ambalo lilionekana si rafiki kwao.


"Jamani hapa naanza kuihisi harufu ya ngome ya mateso kama ya Santana."

Robinson aliendelea kuelezea hofu yake.


"Si wewe tu hata sisi ni hivyo hivyo kwani mazingira yanaongea yenyewe hayahitaji mwalimu wa kutoa ufafanuzi."

Jasmine naye aliungana na Robinson.


"Hebu twendeni kule juu tusionyeshe hali hii kiasi cha kuwafanya kutustukia mapema."

Jessica aliwasihi wenzake kuwa wapande ngazi kuelekea kule juu ili kumsikiliza huyo mkuu wao ana jambo gani kwao. Na hivyo moja kwa moja waliongoza walikoelekezwa lakini cha ajabu wakiwa wanapandisha kule juu ambako ni ghorofa la miti na ni jengo ambalo liko juu kuliko majengo yote pale na yote yakiwa yamejengwa kwa miti na kukandikwa kwa udongo waliona kundi la walinzi wenye silaha kama yule wa mwanzo wakiwa nyuma yao na hapo wakajua yamewafika kooni. Walianza kupandisha ngazi kuelekea juu na hapo ndipo wale walinzi walibaki wamesimama hapo huku silaha zile zikiwa zimeelekezwa kwao. Walipandisha mpaka juu ambako walikutana na kama ofisi hivi kwani ilikuwa imesheheni kila kitu kinachotakiwa kwenye ofisi yoyote na kingine kilichowashangaza ilikuwa ni uzuri wa ofisi hiyo isiyofanana na muonekano wa nje ambako imekandikwa na matope tu lakini ndani ilikuwa imesakafiwa vizuri kwa saruji na kufuatiwa na rangi ya maziwa iliyong'aza zaidi ofisi hiyo ambayo ukitaka kujua uzuri wake unaweza kujaza maelfu ya karatasi.

Na nyuma ya meza kulikuwa na mzee yule aliyekuwa akiendesha gari na waliyemfanyia vurugu.


"Karibuni vijana wangu kwenye ngome ambayo kuingia kama hivi ni rahisi lakini kutoka ndiyo ngoma nzito."


Hakuna aliyeitikia ukaribisho huo ulioonekana ni wa dharau kwao, hicho mzee yule alikiona na hivyo kuendelea na maelezo yake.


"Nimewaita huku juu maalum kwa ajili ya kuwasikiliza kile ambacho mliniambia kuwa kiliwasibu huko mlikotoka mpaka kupelekea kufanya mauaji na kisha nitayachekecha kuona nawasaidiaje au ndo nawaripotisha ili nivute kiasi hicho cha mpunga (hela) ambacho kitasaidia katika kuukuza mradi wangu huu ambao ni maarufu hapa nchini."


Baada ya maelezo marefu ya mkuu huyo aliyetaka kujua kilichowasibu na ndipo aliposimama Jackline na kuanza kutoa historia ya safari yao mpaka pale alipowakuta.


" Mzee kwanza kabisa tuko chini ya miguu yako kwa kitendo tulichokifanya kwako bila kujua wewe ni nani lakini ilikuwa ni moja ya hofu yetu tusamehe sana."

Kisha aliinamisha kichwa kuashilia ombi lile linatoka moyoni mwake.


"Lile lilipita mwanangu endelea na kipya nisichokijua kutoka kwenu."


"Okey sawa, kifupi hapa tuko katika makundi mawili yaliyoungana ugenini namaanisha mimi na huyu hapa tumekuja hivi karibuni kutoka Tanzania na hawa wenzetu tumekutana nao huku huku lakini nao ni watanzania pia na ilikuwaje ikawa kama ilivyo ni kwamba mimi naitwa Jackline Joachim na huyu hapa ni Robinson Kaaya ambao tulikutana wilayani Chunya katika mji mdogo wa Lupa huko nilikwenda kumfuata baba mdogo aitwaye mzee Fikirini na hii ni baada ya kupoteza mawasiliano na rafiki wa marehemu baba yangu mzee Jonathan ambaye alifanya hivyo kwa makusudi baada ya kujua kuwa nilisha maliza masomo yangu ya chuo pale Soweto University cha Afrika ya Kusini ningechukua Mali za wazazi wangu ambazo alikabidhiwa na baba mdogo aziendeleze nafikiri ni kutokana na upeo mdogo wa elimu na yeye lengo lilikuwa ni kudhurumu na mpango wake ukiwa ni kutuangamiza na ndipo nilipoamua kukimbilia huku kwa ajili ya kuja kupata mafunzo ya kupambana ili nikiiva nirudi kupambana naye na kuzikomboa Mali zetu na ndipo nilipoongozana na huyu rafiki yangu Robinson."


"Na wazazi wako wako wapi mpaka Mali zenu ziwe kwa mtu mwingine ambaye ni rafiki tu."

Mkuu yule aliuliza swali baada ya kuonekana kuvutiwa na Simulizi ya Jackline.


"Wazazi wangu walifariki katika ajali mbaya gari wakiwa njiani kuelekea kisiwa cha Ukerewe mkoani Mwanza nikiwa bado mdogo n...." Alishindwa kujizuia akaanza kulia kutokana na kumbukumbu ya wazazi wake.


"Jack pole sana, nyamaza basi endelea na Simulizi yako."

Mkuu aliinuka kitini na kumfuata Jackline kumtuliza wakati akilia.


"Hivyo safari yetu ya kuja huku tuliunganishwa na mtu mmoja wa Afrika ya kusini aitwaye Simbozya kuwa kuna rafiki yake ambaye huwa ana chati naye mtandaoni akijitambulisha kama mwalimu wa mapigano na anamiliki shule nyingi za mapigano hivyo pasipo kufanya uchunguzi tukaunganisha safari na ndipo tukafikia katika mji wa Belem.. "


" Anaitwa nani huyo mwalimu pale Belem?"

Mkuu yule alimkatisha kwa swali.


" Anaitwa Santana."


"My God, my God ninyi watoto mna balaa hivi mnamfahamu Santana? Yule si mtu hapa Brazil ni nani asiyemfahamu, ni Zungu la Unga lile lina miliki kampuni lililoichukua kutoka kwa mzee Tuyilagezi Mrundi wa Afrika. Poleni sana na kwa ninavyomfahamu lazima hajatulia nina uhakika anawatafuta kila kona yule, eeh ikawaje sasa?"


" Baada ya kufika alitupokea yeye mwenyewe na kutupeleka kambini kwake na hapo ndipo alipoandaa mpango wa kutuangamiza lakini kama bahati hivi mchezo ule tuliusoma na kutoka kwenye chumba kile huku tukishuhudia wakiingia na kumimina risasi pale tulipokuwa tumelala na wakati tukihangaika ni wapi tupite ndipo tulipenya na kukuta kichumba ambacho ndani yake kulikuwa na hawa wenzetu na kutokana na walivyokuwa wamefungwa mle ilibidi

kuwaokoa na kutoa huduma ya kwanza kwani hali zao zilikuwa sio nzuri na kisha ndipo tulipoongozwa na dada hapo aitwaye Jasmine na mdogo wake Jessica. Jasmine akiwa mke wa Santana na mdogo wake akiwa kaja kumtembelea na ndipo walipokutana na mateso baada ya Santana kuchukizwa na kitendo cha mke wake kukataa kumtoa mdogo wake Jessica kuuawa na kubeba madawa. Na wakati tunapambana kutoka tukipita kwenye njia za chini ambako tuliua walinzi wake na tulipotoka tuliomba lifti kwa mzee fulani ambaye alikataa na kutaka kupambana na sisi ndipo tulipomuua na kuondoka na gari lake na kulitelekeza mjini Belem na ndipo siri ya sisi kufanya mauaji hayo kubainika na mpaka sasa tunatafutwa mzee kwa ufupi iko hivyo tunaomba msaada wako tufanikishe zoezi letu na turejee Tanzania kulipa kisasi.. "

Jackline alianza kulia tena na tendo hilo lilipelekea wote kuanza kulia huku mzee akibaki kufuta machozi asijue afanye nini kutokana na historia ya vijana aliokuwa nao mle ndani kwani umri wao hauendani na makubwa waliyopitia na wanayoendelea kuyapitia.


Nini kitaendelea ndani ya Ngome ambayo bado hatujaifahamu jina lake?


TUKUTANE KATIKA SEHEMU INAYOFUATA.






"Nimewaelewa vizuri sana na pia niwape pole kwa yote mliyopitia inawezekana ni mpango wa Mungu katika kuwafanya muweze kuwajua maadui zenu."


"Asante mzee tunamshukuru kwa kutuelewa." Jasmine alishukuru.


"Bila shaka, niwakaribishe katika Ngome yetu na pia nianze kwa kuwajulisha kuwa huu ni mgodi wa kuzalisha kokoto ni mgodi mkubwa sana ndani ya Brazil mengine mtaendelea kuyajua kwa muda mtakaokuwepo hapa. Na mimi ndiye msimamizi mkuu na miongoni mwa wamiliki wa Mgodi kwa majina naitwa Bruno Gautier.Karibuni sana."


"Asante mkuu, ila nilikuwa naomba kuuliza kidogo kama hutojali."


"Uliza tu binti."


"Tutakuwepo hapa kwa muda gani?"

Jessica aliuliza.


"Hapa mtakuwa nasi kwa kipindi hiki chote ambacho mnatafutwa mpaka pale hali utakapokuwa sawa mtaondoka tu."


"Hawawezi kubaini kama tuko ndani ya mgodi huu? Kama ulivyosema kuwa ni mgodi mkubwa."

Robinson aliuliza swali jingine.


"Vijana wangu niwatoe hofu kuwa eneo hili huwa haliingiwi hovyo na watu wasiohusika kwani mgodi huu una eneo la kiwanda cha kuziboresha kokoto huko ndiko wateja wetu huishia." Alifafanua mzee huyo.


"Tutashukuru sana mzee na bila shaka tukiwa humu tutaweza kujifua zaidi na mazoezi ikiwa tutapata eneo."


"Hilo ni jambo dogo sana kwangu tegemeeni makubaliano kutoka kwangu."


Baada ya kikao hicho kisicho rasmi mzee Bruno aliwaacha ndani ya ofisi yake na yeye kushuka chini ambako alimwita mmoja wa walinzi wake na kuongea naye mambo fulani kisha yeye akaingia ndani ya Lori lake la kubebea magogo na kutoka zake na kitendo hicho kilionwa na Robinson aliyekuwa akichungulia kule chini kupitia dirishani na kupata wasiwasi kwanini aondoke na kuwaacha mle ofisini mwake?


"Mmhh jamani kuna sintofahamu hapa."


"Ipi hiyo Robinson?" Jasmine alimuuliza.


"Mzee Bruno kaondoka na mgari wake na pia kuna maelekezo alikuwa akimpa mmoja wa walinzi wake."


"Hakuna haja ya kupata hofu kwani mzee Bruno kama alivyosema ndiye mmiliki wa eneo hili na kiongozi pia hivyo hawezi kukaa tu humu ofisini ilhali kuna kazi zinatakiwa kuendelea." Jackline alimtoa wasiwasi mpenzi wake Robinson.


"Ni kweli kabisa Jackie lakini eneo hili bado nina mashaka nalo kutokana na namna mambo yanavyokwenda hatuwezi kusema ni salama hebu angalia kule chini namna wafanyakazi wanavyopata adhabu." Jasmine alionesha hofu yake ya wazi kwa mzee Bruno na Ngome yake.


" Ni kweli Jasmine hebu angalia kule namna yule mfanyakazi anavyokula mijeredi moja kwa moja hawa ni watumwa hawalipwi chochote kutokana na kazi wanazofanya humu ndani." Jessica alimuunga mkono dada yake.


"Kikubwa jamani tuwe makini hawa si ndugu zetu lolote linaweza kutokea."

Jackline aliwatahadharisha wenzake.


Wakiwa kwenye mjadala mle ofisini mara mlango ulifunguliwa na akaingia yule mlinzi aliyekuwa akipokea maagizo kutoka kwa mzee Bruno Gautier.


"Samahani naitwa James Martin ni mkuu wa kitengo cha ulinzi hapa GAUTIER MINING LTD."


Walitazamana wakina Jackline baada ya kusikia jina la mgodi huo hapo wakabaini kuwa asilimia mia moja mzee Bruno Gautier ndiye mmiliki mkuu.


"Okay asante ndugu." Robinson alijibu kwa ufupi.


"Hivyo basi kabla ya kuondoka kaniagiza niwachukue na kuwapeleka kwenye vyumba ambavyo mtakuwa mnakaa."


"Ok sawa brother hakuna tatizo tunaweza kwenda tu."

Jackline alijibu na kuwaonesha ishara ya shingo wenzake kuashiria kumfuata mlinzi.


Walishuka na kuongozana na mlinzi huyo mpaka kwenye vyumba vilivyoandaliwa kwa ajili yao. Na wakiwa njiani kuelekea huko walipishana na mmoja wa wafanyakazi aliyekuwa akiwaangalia huku akitikisa kichwa kuonesha ishara ya kuwasikitikia wageni hao. Hilo Jasmine alibahatika kuliona na hapo akajua si salama kwao. Walifika na mlinzi aliwaonesha makazi yao ila tu hofu iliongezeka pale walipoambiwa kuwa chumba kimoja kwa mtu mmoja.


"Brother sisi ni ndugu tunaweza kukaa chumba kimoja tu bila shaka yoyote." Robinson alimfuata mlinzi na kumuelekeza kwa sauti na ishara za mikono.


"Unaweza kuwa sawa lakini kulingana na kanuni zetu humu ndani ziko hivyo na hii ni kulingana na vitanda vyetu vilivyotengenezwa."


"Mbona hii mpya sasa." Jessica


alijisemea huku akichungulia ndani ya chumba alichooneshwa kuwa kitatumiwa naye.


"Brother sasa mbona hata hivyo vitanda sivioni humo ndani?"


"Jamani mimi natekeleza maagizo ya mkuu na si vinginevyo na kama hamjaridhishwa basi mtaongea naye alirudi jioni."


"Jamani ee tuingieni tu humu tumejaa wenyewe hivyo hatuna jinsi." Jasmine alionekana kupaniki akaongea hayo na kuingia zake chumbani kwake. Kitendo hicho kilikuwa kama ni ishara kwa wenzake kwani nao ilibidi waingie vyumbani mwao. Na kilichowathibitishia kuwa wamedakwa ni baada ya wao kuingia tu milango ilipigwa lock.

Mle ndani kwa kuwa mlikandikwa kwa tope haikuwa tabu kwao kuendelea kuwasiliana kwa kuwa juu kwenye ukuta wa kutenganisha vyomba hivyo kulikuwa wazi hivyo sauti zao zilikuwa zikisafiri vizuri.


"Jamani ee hakuna kufanya chochote kile mpaka tuusome mchezo kisha tufanye yetu."

Jackline aliwatahadharisha wenzake.


"Ni kweli kabisa jamani kwani kufanyiwa hivi inawezekana ni kutokuwa na imani nasi na matukio tuliyotoka kuyafanya."

Jasmine akakubaliana na Jackline.


"Hatuna jinsi yoyote ila tu niwaombe simu zenu tafuteni sehemu ambayo ni salama ficheni hali inaweza kubadilika ukashangaa tunafanyiwa ukaguzi." Robinson alishauri wenzake.


"Brother umesomeka." Jessica alijibu.


"Robinson umetenganishwa na sukari yako itakuwaje sasa?"

Jasmine alimtania Robinson.


"Ni mapito tu dada yangu yatakwisha na maisha mengine yataendelea."


"Kabisa mpenzi wangu." Jackline alimuunga mkono mpenzi wake.


Huku nje mlinzi yule aliyetambulisha kwa jina la James Martin na mkuu wa kitengo cha ulinzi alimpigia simu mkuu wake kumjulisha kuwa tayari kawabania vyumbani mwao.


"Mkuu kama ulivyoagiza ndivyo nilivyotekeleza."


"Vizuri sana sasa cha kufanya andaeni kile chumba cha mateso ili nikifika niwaoneshe mimi ni mtu wa namna gani."


"Kama ulivyoagiza bosi wangu."


"Hakikisha kila kona ya Ngome kuna ulinzi wa kutosha maana hao si watu wazuri hata kidogo James."


"Sawa bosi kila kitu kitakwenda vizuri."


"Okay, tunamalizia kupakia magogo na baada ya masaa kadhaa tutakuwa hapo."


"Sawa mkuu."


Bruno alikata simu na kumfanya mlinzi wake kuyapitia mageti yote kuimarisha ulinzi kisha akapenya mpaka kwenye kuta zote na chemba kuu ambayo ndiyo kokoto hupitishwa huko kwa njia ya viberenge kupeleka upande wa pili wa mgodi ambako kuna kiwanda cha kuziongeza thamani kokoto na kuzitenga kwenye madaraja huko kote alihakikisha ulinzi uko sawa.



***


"Haloo nani mwenzangu?"

Mke wa mzee Jonathan aliuliza baada ya kupokea simu ambayo alipigiwa na mtu asiyemfahamu.


"Samahani shemeji mzee Jonathan bado hajarudiwa na fahamu zake lakini jambo la kumshukuru Allah ni kwamba tumefanikiwa zoezi lake."


"Okay nashukuru sana kwa hilo vipi itamchukua muda gani mpaka kurejewa na fahamu?"


"Ondoa shaka hata dakika ishirini hazitafika atakuwa tayari kazinduka."


"Nawategemea sana ndugu zangu katika hili."


"Ondoa shaka mama ila sasa samahani kuna kijana wetu atakuwa maeneo Bismarck Coffee Table maeneo ya Nyakato jitahidi uonane naye kuna maagizo atakupatia."


"Muda gani itakuwa ili na mimi nielekee huko?"


"Hata sasa unaweza kwenda kwani yeye muda mrefu yuko huko tayari."


"Okay basi ngoja niende nikaonane naye."


"Sawa mama."


Simu ilikatwa na mama Jonathan haraka aliinuka kutoka pale alipokuwa akiandaa chakula na kuweka mchele pembeni na kuingia chumbani ambako alifanya maandalizi ya kuoga haraka katika kuondoa jasho la jikoni na kisha kupigilia viwalo vyake kisha akaliwasha gari lake na kuelekea alikoelekezwa.


"Hivi hawezi kunishtukia kweli kumbukeni yule ni mke wangu?"

Mzee Jonathan alionyesha hofu.


"Mzee huu ni mtihani iwapo atakutambua basi tunaanza upya maana yake kila mmoja huko mtaani atakutambua."


"Okay ngoja tusubiri basi tuone itakuwaje."

Mzee Jonathan aliendelea kutojiamini katika zoezi hilo.


"Mzee kikubwa fanya kama tulivyokueleza na si vinginevyo."


"Sawa sawa kijana wangu."


Wakiwa wanaendelea kuwekana sawa mara kuna gari lilikuwa linaingia pale Bismarck Coffee Table na hapo wenzake wakaondoka na kumuacha pale mzee Jonathan akutane na mke wake.

Mke wake baada ya kuteremka kwenye gari aliongoza moja kwa moja mpaka ndani na kuanza kuangalia huku na kule kuona kama anaweza kumuona mwenyeji wake na mara aliweza kumuona baada ya kuona mtu kwenye kona moja akimpungia mkono kumuonesha kuwa ni yeye mwenyeji wake.


"Habari yako Anti naitwa Ras Migo nimeagizwa na kijana mmoja anayeitwa Nyashiko kaniambia nikupe hii bahasha."


"Okay asante sana."


"Basi Anti naomba uniruhusu niweze kuondoka maana nilikuwa nakusubiri wewe tu."


"Upate hata kinywaji tu kijana wangu ndipo uende."


"Nashukuru sana siku nyingine nitakunywa."


Wakati wakiendelea na mazungumzo yao mara simu ya mke wa Jonathan iliita akaipokea.


"Ndiyo kijana wangu mzigo nimeupata tayari."


"Sawa mama hiyo bahasha utaihifadhi ndani ni documents za mtambo ambao mzee ameununua hivi karibuni."


Kisha simu ilikatwa na mke Jonathan aliiweka kwenye pochi yake na alipogeuka kumtazama mwenyeji wake hakuona kitu zaidi ya kiti. Aliangaza huku na kule hakuona mtu.

Kwa zoezi hili iliwapa matumaini kuwa muonekano mpya wa mzee Jonathan utawapa wakati mgumu sana maadui kumtambua.







"Ninyi ni hatari aise yaani mke wangu mimi anayenifahamu mpaka alama iliyo kwenye utumbo leo hii hajanitambua? Maskini weee Dorothy wangu."

Mzee Jonathan aliwamwagia sifa vijana waliobadili muonekano wake uliopelekea mpaka mke wake kumsahau baada ya kukutana pale Bismarck Coffee Table.


" Nilikwambia mzee hutaamini kazi ikikamilika hivyo basi kilichobakia hapa ni kuanza safari ukiongozana na vijana wangu wawili ambao watakusaidia mambo yako huko ukirudi na ushindi unatupa chetu." Aliongea kiongozi yule ambaye ndiye aliyefanya kazi ile ya kisanaa.


" Nashukuru sana kijana wangu naamini kila kitu kitakwenda kama kilivyopangwa maana sipate usingizi kabisa juu ya ile familia."


"Wale ni sawa na kuku walio ndani ya banda unaamua tu umkamate yupi na kwa staili gani mzee hawana ujanja waleeee." Alisisitiza kiongozi.


"Basi sawa nadhani mimi sasa nielekee nyumbani kwanza nikafanye maandalizi ya safari ili ifikapo saa nane mchana tuanze safari yetu."


"Bila shaka mzee."


Mzee Jonathan aliondoka pale kupitia uchochoro wa nyuma wa kingome kile na kutokea eneo moja hivi la wazi huko aliikuta gari yake ikiwa inamsubiri, ilimshtua kidogo kwani alipoikuta ni tofauti na pale alipoiacha lakini hakutaka kuonesha hofu hiyo mbele ya kijana aliyemsindikiza pale. Waliagana kisha mzee Jonathan akaondoka zake na baada ya dakika kadhaa alikuwa getini kwake akipiga honi. Geti lilifunguliwa na gari ilijaa ndani na mzee Jonathan alishuka garini, akiwa anafunga mlango wa gari mke wake aliyekuwa akitoka pale getini akashtuka kumuona tena yule mtu waliyekutana na kisha kupotea kule Bismarck.


"Vipi tena? Wewe si ulinikimbia bila kuagana?"


"Naomba unisamehe Anti kulitokea dharura na nimeona nije nikuombe radhi."


"Okay limekwisha hilo nambie lakini?"


"Naitwa Jonathan Ubao mumeo halali kabisaaa."


Baada ya utambulisho huo mke wake hakuamini macho yake na hapo hapo alidondosha machozi ambayo alijua mwenyewe kama ni ya furaha au ya mshangao.


"Mume wangu umebadilika hivyo?"


"Ndicho nilichokuwa nakihitaji hiki mke wangu nimekuja mara moja kufanya maandalizi ya safari nategemea mchana kuanza safari."


"Kwa muonekano huo kila apitaye mbele yako ni risasi tu."

Mke wake alimtania.


Waliingia ndani na mke wake alimuandalia maji ya kuoga na kisha wakapata chakula. Na kila kitu kilipokuwa tayari waliagana na kisha Kulga iliwashwa na kuondoka.


"Waambie wakina Black nawapitia wajiandae."


"Wajiandae nini tena mzee hawa kama Wajeda wako tayari muda wote wewe njoo muondoke."


"Okay sawa kiongozi."


Alifika pale na kuwakuta vijana wale wakimsubiri hivyo aliisimamisha gari na kisha wakapanda na gari ikang'oa nanga na nyuma ya usukani akiwa ni Black na huku mzee Jonathan akiwa pembeni yake.



***


Mzee Bruno aliingia ndani ya Ngome yake na kupaki gari lake lililokuwa limejaa magogo tena na kama ilivyokawaida kundi lile la watumwa walifika pale kwa mstari na kuanza kushusha huku mzee yeye akiwa sambamba na James kuelekea walikofungiwa wageni wake.


"Vipi wanasemaje hawa paka?"


"Hawana usemi ila tu walilalamikia kitendo cha kufunga mlango na kuwatenganisha vyumba."


"Wanatuletea sheria zao hapa ni kwangu lazima wafuate sheria zangu, kwanza niletee na vifaa vya kutolea wenge ili niwakaribishe rasmi ndani ya Ngome kuu."


"Kama ulivyoagiza mkuu."


Mlinzi yule aliondoka na kwenda kuleta vitendea kazi na kumuacha mzee Bruno akiliendea jengo lile walilofungiwa wakina Robinson. Baada ya kufika alikwenda moja kwa moja kwenye eneo la wazi ambalo ni ghala fulani likiwa na baadhi ya magunia kadhaa ya nafaka. Alikagua kagua magunia yale na mara kamanda wake James aliingia na kuweka chini vifaa vile ambavyo vilikuwa ni beseni la moto na baadhi ya vyuma pamoja na maji yaliyokuwa ndani ya kontena lenye barafu.


"Kawafungulie na uwalete hapa."


"Sawa mkuu."


Aliondoka na kwenda kuwafungulia wakina wakina Jackline ambao mpaka muda huo walikuwa gizani hawajui ni nini lengo la kufungiwa mle vyumbani tena kila mmoja na chake.


"Vipi mzee karudi?"

Robinson aliuliza baada ya kufunguliwa.


"Ndiyo na ndiye aliyeniagiza niwafungulie.


Yuko kule mwisho kwenye lile jengo lenye mlango mkubwa anawahitaji."


Bila wasiwasi wowote waliongoza kule walikoelekezwa na hapo hapo James akawaamuru walinzi zaidi ya kumi na tano kuwafuata nyuma.


" Karibuni sana vijana wangu kwenye jengo hili ambalo mara nyingi watu huwa hawatoki salama."


"Mzee kwani kosa letu ni lipi kwako?"

Jasmine aliuliza.


"Wala hamjanikosea lolote ila tu sina imani na ninyi kwani kwa namna Ngome ya Santana ilivyo na ulinzi mkali lakini ninyi mkatoka na kumchanganya Santana hivyo ni mjinga gani ambaye awaamini kirahisi rahisi uongo wenu? Ila hapa ni sehemu pekee ambapo wenye roho ngumu huweza kulainika."


"Ina maana mzee hujatuamini kwa tulichokuelezea?"


"Ndiyo na sitaki niwaamini kirahisi ila kupitia eneo hili najua mtanieleza ninyi ni wakina nani na mmefuata nini Brazil na mmetokea wapi na ni nani aliye nyuma yenu."


"Mzee si...."

Kabla hajamaliza kuongea Robinson alikutana na ngumi nzito kutoka kwa mzee Bruno.


"Halafu wewe dogo unaongea sana, nafikiri sasa ni muda wenu wa kuongea."


"Hatuna tunalolijua jingine."

Jackline alijibu.


"James waite vitasa wafanye kazi yao mara moja."


Alimtaka James awaite vijana ambao hufanya kazi chumba cha mateso. Na muda mfupi baadaye waliingia vijana wenye miraba minne wakiwa na minyororo mikononi na miguuni na kisha walifunguliwa ile minyororo na kisha waliwafuata wakina Jackline.


" Anzeni kazi yenu mpaka walainike hao si mnaona walivyo strong' hao."


Hapo hapo walikamatwa wakina Robinson na kufungwa minyororo na kisha yale majitu yalianza kuwashushia vichapo.

Hali ya mle ndani ilibadilika kwani sakafu ilianza kutapakaa damu ikiwa ni dalili vijana walianza kuiva.


NIKUOMBE USIKAE MBALI NA SEHEMU YA ISHIRINI KUJUA NINI KITAENDELEA NDANI YA NGOME.




"Kwa-ni-ni m-nat-ufa-nyia hiiiiviiiii?"

Robinson aliongea kwa taabu sana kwani muda alikuwa akitokwa na damu kila sehemu ilipitiwa na mingumi ya wale majitu.


"Tuk...o wap.."

Jackline alishindwa kumalizia sentensi akazimia tena na alikuwa hatamaniki hata kidogo kwani nguo zake tu zilikuwa kama vile zilikuwa zikitobolewa na misumari upande wa Jasmine na mdogo wake ndiyo kabisa hawakuwa wanajua kinachoendelea walikuwa wamezimia muda mrefu.


"Mtajuta kuitambua Kambi hii kichapo kidogo tu mnazimia? James waondoe wenge hao haraka."

Mzee Bruno aliagiza.


James alichukua lile kontena lenye maji ya barafu na kuwamwagia kila mmoja. Walizinduka lakini walikuwa walikuwa bado wanamaumivu makali mwilini kwani kila mmoja alikuwa akilalamika kivyake.


"Bila shaka bado hawajitambui vizuri hebu niletee lile beseni niwaweke nembo ambayo wataikumbuka maishani mwao."


Alisogezewa beseni lile ambalo lilikuwa na visu ndani yake na kisha kuanza kuwapiga chapa ya moto kwa kila mmoja.


"Mamaaaaa nakufaa mzee mbona unatufanyia hivyo?"

Robinson alilalamika baada ya kisu cha moto kupita kifuani kwake.


"Kumbe mnaweza kuongea vizuri ee mbona mwanzo mlikuwa mnakatakata maneno?"


"Nakuahidi mzee tukitoka kwenye jengo hili tutakachokifanya Ulimwengu wote utatushangaa."

Jackline aliongea huku kisu cha moto kikikatisha taratibu mgongoni lakini badala ya kulia kama wenzake yeye alimkazia macho mzee Bruno na kuongea hayo na mwisho alimtemea mate usoni yenye mchanganyiko na damu.


" Unanifanyia nini wewe binti? Kumbe hunijui eee."

Mzee Bruno alimuwakia baada ya tendo la kutemewa mate.


"Thubutuuuu kumbe hunijui wewe mzee, sasa ukitaka kujua mimi ni wa namna gani fungua hii minyororo nikuoneshe na kwa kuanza naanza na hawa wakosa sura."

Jackline alichafukwa kiasi cha kuwashangaza wenzake hasa Jasmine ambaye muda wote aliamini yeye ni zaidi ya wote kutokana na mafunzo aliyopitia na muda wote kutokana na ukimya wa Jackline alijua hajui chochote.


" Jackline achana na mawazo hayo kumbuka kuwa tuko gizani na hatujui itakuja nuru itakuja saa ngapi tuwe wapole love."

Robinson aliona amshauri mpenzi wake kwani anamfahamu akipaniaga jambo huwa harudi nyuma.


"Muache yeye si ameamua kuvimba kifua mbele ya wanaume sasa ngoja apewe somo. James mfungulie minyororo hiyo huyo bwege kisha kaandaeni lile eneo la machinjio."

Mzee Bruno Gautier alitoa maagizo ambayo yaliwatisha wakina Jasmine, Jessica pamoja na Robinson ambao walianza kulia wakimuonea huruma mwenzao.


"Kama ulivyoagiza bosi."

James Martin aliitikia maagizo ya mkuu wake na kumfuata Jackline kumfungua minyororo, lakini kabla hajafanya hivyo Robinson alimrukia James na kumpiga na minyororo ya mkononi.


"Unanigonga na minyororo ee unataka shida brother?"


"Hapana ni bahati mbaya tu ila nilitaka kukuzuia usimfungue huyo bahati mbaya minyororo ikatangulia please nisamehe."


Haikusaidia kitu kwani James alimtandika teke la tumboni lililopelekea Robinson kuangukia kwenye magunia ya nafaka.


"Jiangalie kijana utakufa kabla ya wakati wako ohhohh shauri yako."


"Ha ha ha ha ha safi sana mjeshi wangu ndiyo maana kila siku napenda kukupandisha mavyeo kama yote fanya kazi yako achana na kelele za huyo pimbi."


"Sawa mkuu."


"Jackline please usifanye hivyo tutashindwa kufanikisha zoezi letu."

Jasmine alimnong'oneza Jackline sikioni akiamini atamuelewa lakini haikuwa hivyo.


"Jasmine wacha niwaoneshe kazi hawa washenzi maana tukiwakalia kimya watatupanda kichwani."


Sauti ile ya juu ilimfanya Jasmine ajivute pembeni na kubaki mtazamaji tu kama ambavyo Jessica alifanya.

Baada ya kufunguliwa tu Jackline alisimama kwa kasi ya kimbunga na kumkata mtama James ambaye bila kutarajia alijikuta chini karibu na beseni la moto. Alijikaza akainuka kwa kupepesuka ili kukabiliana na Jackline ambaye muda huo alikuwa kavimba akimsubiri ainuke ampe kichapo kingine.

Bahati haikuwa kwa James kwani alikutana na kichapo kingine na mbaya zaidi lile teke la mdomoni lilimpeleka chini tena James na kushuhudia meno kadhaa yakienda chini na kabla hajafanya chochote alimfuata na kumkaba na ile minyororo kiasi cha kuwafanya yale majitu kumrukia Jackline na kuanza kumtandika mangumi.


"Heeey kaa pembeni nani aliyewaambia huu ni ukumbi wa mapambano, haya bila shaka ulingo uko tayari twendeni nje tukashuhudie mpambano, wafungulie na hao wapuuzi wakashuhudie mwenzao akiagana na dunia."


"Unafikiri nawaogopa twendeni fasta kabla shetani mnyonya damu hajatoka mwilini mwangu." Jackline aliendelea kuwaduwaza mle ndani.

Walifunguliwa ile minyororo na wote wakatolewa nje mpaka kwenye eneo ambalo liliandaliwa kwa ajili ya pambano na kwa namna eneo lilivyokuwa liliashiria hapo hufanyika michezo kama hiyo kila wakati. Mzee Bruno alichukua kipaza na kutoa tangazo lililopenya kwenye kila sikio la aliyekuwa mle ndani.


"Watu wote mnatakiwa kufika kwenye machinjio kushuhudia mtu aliyechoka maisha akichinjwa kama kuku, wote acheni kazi zenu wahini ukingoni haraka."


Baada ya tangazo hilo kupita kila mmoja aliacha shughuli yake na kukimbilia eneo la tukio huku kila mmoja akijiuliza ni nani tena huyo aliyeamua kuchafua siku mle ngomeni.


" Kijana wangu hivi ni nani huyo aliyeamua kujitoa mhanga? "

Mzee mmoja aliyekuwa akifua vyuma alimuuliza kijana anayefanya naye kazi kule chini.


"Mzee wangu hata sijui ni nani mimi nadha twende tukashuhudie huko huko tutajua tukifika."


Watu zaidi ya mia tatu walikuwa wamelizunguka eneo la ulingo ambao ulikuwa umemwagwa tope ambalo kwa mtu asiyekuwa mzoefu nalo basi asingeweza kurusha hata teke moja kutokana na kuteleza. Miongoni mwao wakina Jasmine nao walikuwa karibu kabisa na ulingo chini ya ulinzi mkali huku wakimshuhudia Jackline alivyokuwa akijinyooshanyoosha kujiandaa na mpambano huo.


"Namuonea huruma Jackline kwa maamuzi aliyochukua sijui itakuwaje."

Jessica aliongea akiwa kashika shavu lake.


"Huyo ndiye Jackline mrembo wangu ambaye huwa akiamua jambo huwa harudi nyuma hata siku moja." Robinson alijibu huku akijifuta machozi.


Ndani ya ulingo mtu aliyekuwa akiingia kufungua mpambano hakuwa mwingine bali James ambaye alioshwa vya kutosha kule ndani. Na baada ya kuingia tu James kengele iligongwa na mpambano ulianza.

Jackline alikuwa ameshausoma ule ulingo hivyo alichokifanya ilikuwa ni kuruka juu na kumgonga kichwa kwa kiwiko na kumpeleka chini James na kisha Jackline alimfuata juu yake na kumnyonga kichwa. Tendo lile lilimshangaza sana mzee Bruno kwani kwa namna alivyoruka juu na kutua na kiwiko juu ya kichwa cha James hakutegemea kutokea.


"Mzee Bruno naomba nikwambie kitu, huu ni moto wa petroli ukigusa lazima uwake..."


"Weee kaa kimya hapo hujashinda kwa kumnyonga James, Brown muoneshe kazi huyo haraka."


Kama mshale Brown alitua ulingoni tayari kwa mpambano na baada ya filimbi tu, alimvamia Jackline miguuni na kumchota mzima mzima. Jackline aliangukia matope kwa kutanguliza mgongo.


" Yessss maliza kazi Brown, watu wote shangilieni kumpa nguvu kijana wetu."

Kweli shangwe liliongezeka na kumfanya Brown ahisi ameshinda mchezo alimfuata Jackline pale chini ili amuinue lakini hakujua kama ulikuwa mtego kwani alishtukia akipigwa teke la sehemu za siri.


" Ooishhhhh Mungu wangu weee nafwaaaaaa.... "

Brown alitoa kilio kwa maumivu makali aliyopata.


Na hapo hapo mzee Bruno aliinuka na kutoa tamko kali ambalo lilitokana na hasira baada ya watu wake wawili kupigwa na mwanamke hicho kilimkera sana Bruno.


"Askari mfunzeni adabu huyo ibilisi haraka."


"Ndiyo mkuu."


Askari kama nane waliingia ulingoni na kuanza kumshambulia kwa mafimbo yaliyotua kwenye kila kiungo cha Jackline, alijitahidi kujizuia lakini hakuweza kwani hawa walinzi walikuwa hawana chuguo la wapi wapige na hii ni kutokana na kifo cha kiongozi wao wa ulinzi bwana James Martin.

Hakika Jackline aliiva na ukizingatia lile eneo lilikuwa na matope usingeweza kumtambua Jackline aliyekuwa kama mfu hivi. Mwisho nguvu zilimwisha alianguka chini na kutulia kimya lakini juu yake kichapo kiliendelea. Hali hiyo iliinua hasira kwa Jasmine aliyepaza sauti yake.


"Mijanaume mizima msio na hata chembe ya huruma yaone, kama mna nguvu za kupambana si angeingia mmoja mmoja mbona mlimvamia na mafimbo? Si mngepanga mkono kama wenzenu? Mtu ameanguka bado bado mnaendelea kumshambulia tu nyinyi vipi? "


"Kweli, kweli, kweli...."

Sauti za wote waliojitokeza kushuhudia mpambano walipaza sauti zao kitendo ambacho kilimsimamisha mzee Bruno.


"Keleleeeeeee shwaini nyinyi nadhani mmenisahau eeehh."


"Wakukumbuke wewe kama nani bwana waache wapaze sauti zao mbona wakati Jackline akipigwa ulitoa amri washangilie vipi tena?"

Robinson aliinuka na kupaza sauti yake.


"Hee kila mtu aende sehemu yake ya kazi mara moja na ninyi walinzi peleka ndani hao pimbi kabla sijaamsha hasira zangu za urithi na huyo aliyeniulia kamanda wangu namsubiri si anajidai kafa tutaona."


Watu wote walikimbia kwenye maeneo yao kuendelea na shughuli zao huku wakina Jasmine wakirudishwa ndani na mara hii waliingizwa chumba kimoja wote pamoja na mgonjwa wao Jackline ambaye hatujui mzima au kafariki. Watu walikuwa wakiongea kila mmoja lake wengine wakimsifia Jackline kwa alichokifanya kwani haijawahi kutokea mmoja wa walinzi wa Ngome ile kuuawa mbele ya macho ya mzee Bruno na wengine walikuwa wakiwaonea huruma tu wakina Jasmine.


"Kale kadada kamenikumbusha mbali sana enzi zile naonesha video za kina Jetlee, Donnien ilikuwa shida mpaka mimi mwenyewe niliiga mapigo yake na baadaye kuanza kuyatumia mtaani, kuna siku niliotewa na mbishi mmoja aliyeingia bila kulipa kiingilio acha ndo hili pengo na mpaka leo sipendi ngumi ila kuangalia tu."


"Babu mimi nakupendeaga hapo tu kwenye saundi zako za uongo yaani umesahau kama hilo pengo ulipigwa ngumi na marehemu James ile siku ulipomtongoza mrembo wake Stella?"


"Haa hivi kweli eti na wewe hausahau tu, napo si kafa chezea kale kadada pigo moja tu mavi kuleee na sasa Stella wangu."


"Ninyi hapo bado mnashangaa nini potea?"

Mlinzi aliwatimua baada ya kuona wako bize na stori.



***


"Kijana habari yako."


"Salama mzee shikamoo!"


"Samahani naomba kuuliza."


"Ndiyo uliza tu mzee wangu."


"Sijui unamfahamu mzee fulani hivi anaitwa Fikirini?"


"Ndiyo namfahamu vizuri sana."


"Sijui unaweza kunipeleka kwake au kunielekeza kwake."


"Hata kukupeleka pia naweza mzee."


"Litakuwa jambo jema hilo kijana wangu."


Basi yule kijana aliwapeleka moja kwa moja mpaka sehemu moja hivi karibu na makaburini kisha akamtaka asimamishe gari.


"Kaka yangu bwana yaani aliamua kuja kuishi karibu na makaburini?"

Mzee Jonathan aliongea huku akionekana kushangaa


"Kwa maeneo ya vijijini haya mambo ya kawaida sana."

Black alidakia naye.


Muda huo wanatembea kuelekea eneo hilo la makaburi, yule kijana alikuwa anatuma ujumbe fulani sijui kwa nani.


"MWENYEKITI KAMA AMBAVYO ULIAGIZA KUILINDA FAMILIA YA MZEE FIKIRINI TAYARI KUNA RASTA MMOJA YUKO WENZAKE WAWILI WANAMUULIZIA MAREHEMU MZEE FIKIRINI TUKO MAKABURINI NJOONI."


"Kijana mbona hatufiki tu huko kwa mzee Fikirini?"

Mzee Jonathan aliona aulize baada ya kuona wanazidi kuyakatisha tu makaburi.


"Nataka tupitie huku nyumba yenyewe ni ile pale sasa njia ya kule juu imefungwa kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha zimepelekea korongo kubwa sana na hivyo kusababisha wakazi wa kieneo hiki kutumia hii njia ya makaburini."


"Okay, ila hii mvua imekuja na majanga mengi sana sijui mpaka mwisho itakuwaje?"

Black aliuliza baada ya kupata ufafanuzi kwanini walipita ile njia.


"Nisubirini hapa kwanza nimgongee mlango."

Aliwataka wabaki pale nje ya fensi ya matete na kisha kijana huyo kuingia ndani ya ile nyumba.


"Wenyewe mpo, wenyewe, wenyeweee, mzee nimekuletea wageni wako bwana."

Yule kijana aliongea hivyo kuwaaminisha wanaomsubiri kisha akazunguka nyuma ya ile nyumba na kukimbia. Wao Wakabaki pale wanasubiria.


"Unajua nini taarifa ambazo nilipataga ni kwamba mzee huyu alifariki kipindi kidogo sasa mbona huyu dogo kasema yupo na huko ndani anaita jina hilo hilo la Mzee Fikirini."


"Yawezekana ulidanganywa tu na aliyekupa taarifa."


"Mmhh ni mtu niliyekuwa namuamini sana Black."


"Amka mzee chini ya jua hakuna wa kuaminiwa hata mmoja."


"We Black mbona kimya huko ndani hebu nenda kawaangalie bwana tunakwenda na muda eti."


Black aliingia mpaka ndani lakini alishangaa kukuta kufuli mlangoni na nje kuna nguo tu kambani kuashiria


kuwa wenyeji wapo lakini muda huo hawakuwepo.


"Mzee huyu dogo hayupo huku ndani."


"Whaaaaaat, unamaanisha nini Black?


USIKOSE KATIKA SEHEMU INAYOFUATA KUJUA NINI KILIENDELEA.





"Ndiyo hivyo mzee sijui kaelekea wapi?"


"Ninyi tuondokeni eneo nahisi harufu ya damu mwenzenu."

Masanja aliwataka waondoke baada ya kijana waliyekuwa naye kutoweka.


"Hili picha mbona silielewi hivi?"

Mzee Jonathan aliuliza huku wakiondoka eneo hilo kurudi walikoacha gari.


"Au amekutambua nini mzee Jonathan?"

Black alimuuliza mzee Jonathan.


"Siyo rahisi nadhani ni ushamba wake tu si uliona hata mle kwenye gari alivyokuwa akitetemeka?" Ajibu mzee Jonathan.


"Hee oneni kule!!"

Masanja aliwashtua baada ya kuona kitu.


"Wapi dogo Masanja?"

Black aliuliza baada ya kuona Masanja kama kapigwa butwaa.


"Kule kwenye gari kuna nini?"


"Mungu wangu tumejulikana tayari, tufanye nini sasa?"


ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog