Search This Blog

Thursday 23 March 2023

MSAKO - 2

  

Simulizi : Msako

Sehemu Ya : Pili (2)


“Hii inaonesha kuwa huyu mwanamke aliyejiita Jo Mwa, ndiye aliyehusika na mpango wa kuvamia gereza maalumu. Hebu nipe hilo daftari nione!’’ Inspekta Lucas Mwenda akanyoosha mkono kupokea daftari kubwa lililokuwa na orodha ya majina ya wahalifu walioswekwa mahabusu ya pale kituo cha polisi cha Msimbazi. Alipopewa daftari hilo, akapitisha macho kwenye kurasa kadhaa kabla ya kuweka kituo kwenye ukurasa fulani. Hapo macho na akili yake, vikajenga shauku.

“Okay! Sasa nimeanza kupata picha. Japo mwandishi alijitahidi sana kuiga hati, lakini hili jina Joan Mwainunu halikuandikwa na mtu mmoja. Wino wa kalamu iliyotumika ni uleule isipokuwa helufi ‘Jo’ na helufi ‘an’ zimeandikwa na watu wawili tofauti. Kama ilivyo kwenye helufi ‘Mwa’ na helufi ‘inunu’. Inaonekana huyu msichana alikuwa akifanya mambo yake kwa mahesabu na umakini sana. Hivyo kutaja jina la Jo Mwa, alikuwa akijipa nafasi ya kubadilisha jina kama ingehitajika. Aliposikia kuwa watu wale wangegawanywa, wengine wangepelekwa Keko na wengine gereza maalumu. Ndiyo akaamua kuwe na Joan Mwainunu wawili, ili wakati majina ya mahabusu yakiitwa, achague kule alikotaka kwenda. Swali ni je! alibadilishaje jina wakati alikuwa mahabusu?’’ Inspekta Lucas, ambaye anasifika kwa umakini wa kuibua hoja, akamaliza uchambuzi wake kwa swali.

“Usiku ule baada ya kumaliza kuandika majina yao na kuwasweka mahabusu, kalamu niliyotumia kuandika sikuiona tena. Afande! Ndiyo maana utagundua kuwa majina yaliyofuatia nilitumia kalamu nyingine. Sasa ndiyo naelewa kuwa huenda yule msichana alichukua kalamu yangu kwa hila ili afanye atakacho. Kwa kweli hata mimi najiuliza swali kama lako afande. Alitokaje nje ya mahabusu na kwenda kaunta kubadilisha jina?’’ Sajini Halfan akaonesha mashaka yake.

“Labda alikuwa na ufunguo wa bandia. Anaonekana mwenye hila nyingi. Ukitathmini juu ya kile kilichofanyika kwenye gereza maalumu, utagundua huyu msichana ni mtu hatari sana.” Askari mmoja akachangia huku wengine wakiafiki kwa kutikisa vichwa.

“Lazima kuna zengwe limefanyika hapa!” Inspekta Lucas akasisitiza.



“Labda alikuwa na ufunguo wa bandia. Anaonekana mwenye hila nyingi. Ukitathmini juu ya kile kilichofanyika kwenye gereza maalumu, utagundua huyu msichana ni mtu hatari sana.” Askari mmoja akachangia huku wengine wakiafiki kwa kutikisa vichwa.

“Lazima kuna zengwe limefanyika hapa!” Inspekta Lucas akasisitiza.

* * *

Saa moja na robo jioni mitaa ya matajiri jijini Dar es Salaam.
Sabodo Msumari, aliendesha gari kwa mwendo wa taratibu huku akisikiliza muziki mtamu, uliokuwa ukizalishwa na spika zenye nguvu na ubora, za gari lake jipya la kifahari. Huku mluzi mwembamba ukimtoka kinywani kufuatisha muziki huo kwa furaha. Moyoni aliona ulimwengu wote ni wake, mambo yalikuwa yamemnyookea.

Kuwa Waziri wa Ulinzi na usalama kwenye nchi kama hii, halikuwa jambo dogo. Nyota yake ilikuwa imeng’aa sana. Kwa sababu hiyo akajikuta akifikiri zawadi ya kumpelekea mtaalamu wake wa mambo ya nyota kule Bagamoyo. Wakati akisikiliza muziki na mwendo huo wa taratibu, macho yake yalikuwa yakitalii kuangalia nyumba chache kubwa za kifahari zilizokuwa kando ya barabara hiyo eneo ya Masaki. Nyumba hizo zilijengwa kwa nafasi na hivyo kufanya mandhari nzuri ya kupendeza. Sabodo alikuwa anatoka ufukweni, alikokuwa amejipumzisha baada ya kupata dharura. Alikuwa akielekea nyumbani kwa mchepuko wake, umbali mfupi kutoka eneo alilokuwa amejipumzisha ufukweni. Mchupuko ulikuwa umemtaka afike haraka kwa vile hapo nyumbani wezi walikuwa wamevunja na kuiba.

Hivyo alikuwa ameitikia wito wa kwenda kuona athari za wizi aliopewa habari yake. Hakuwa na shida ya muda, kwani wakati huu alikuwa anatumia muda wa ziada, pesa za ziada, mapenzi ya ziada, kwa mtu wa ziada. Walikuwa wote ufukweni lakini kwa sababu ambazo bado hazikumwingia akilini, msichana huyo mchepuko alitaka kurejea nyumbani haraka kwa dharura. Sabodo hakuwa na kizuizi, penzi la binti huyo mrembo lilikwishamlevya, chochote ambacho angeambiwa alikuwa mwepesi kusikiliza na kutii. Alimradi penzi la mrembo huyo lisimponyoke. Hakupenda kumwekea mipaka wala kumchunga, alipenda uhuru kwani tabia hiyo hupendwa na wapenzi wengi. Hivyo alikuwa amemruhusu kimada huyo aende nyumbani kwa dharura kama alivyoomba, kwa maelewano kuwa angerudi ndani ya dakika chache baadaye. Sabodo akabaki ufukweni akibarizi kwa upepo mwanana wa bahari. Hata hivyo starehe hiyo haikudumu sana kwani muda mfupi baadaye, simu ya kimwana huyo aitwaye Nana Muhusin, ilimfanya akatishe alichokuwa akifanya na kumfuata nyumbani.

Aliendelea kuendesha gari, ambalo sasa lilikuwa na muda wa wiki mbili tangu alitoe bandarini kwa usajili wa jina la Nana Muhusin. Hakuwa na nguo nyingine mwilini zaidi ya chupi. Hakuona shida kwa hilo. Ulikuwa muda wa ziada, kufanya mambo ya ziada na mtu wa ziada, sehemu za ziada, kwa pesa ya ziada.

Wakati anakata kona kuingia mtaa ambao kulikuwa na nyumba aliyomjengea Nana, ghafla mambo mawili yakatokea kwa pamoja. Simu yake ya kiganjani ikaita. Wakati akiipokea, mara akasikia sauti ya kishindo cha mpasuko. Alipotanabahi kumbe lilikuwa jiwe kubwa limerushwa kwenye kioo cha mbele cha gari. Kioo kikapasuka. Kwa hamaki akageuka kutazama uelekeo wa jiwe hilo lilipotokea. Wakati huohuo akipokea simu.

“Baby! Mbona hufiki? Nasikia kuna watu wanagonga mlango wangu kwa nje.” Upande wa pili wa simu Nana alilalamika kwa hofu. Sabodo aliisikia sauti hiyo kwa makini lakini mawazo yake yalikinzana na kile alichokuwa akikiona mbele yake. Upande huo liliporushwa lile jiwe, alimwona kijana mmoja amesimama akimwonesha ishara ya kumtusi, kwa kunyoosha kidole cha kati cha mkono wake. Akasikia moyo wake ukisukuma damu kwa kasi na kupiga kite kwa nguvu. Akashikwa na hasira nusu ya kulipuka kwa jazba.

“Shenzi sana wewe kijana! Hivi unajua mimi ni nani?’’ Sabodo akafoka kwa hasira huku akishuka kwenye gari bila kulizima. Mkononi ameshika bastola, aliyoichukua kutoka chini ya kiti cha dereva. Alikuwa kama anayeenda kuogelea, mwilini amejisitiri kwa chupi nyeusi pekee. Akaanza kutimua mbio akielekea upande huo alipokuwa yule kijana. Kuona hivyo, yule kijana akashikwa na taharuki na kuanza kukimbia, akielekea upande ambao kulikuwa na nyumba ambayo haijamalizwa kujengwa. Mheshimiwa Sabodo akiwa amepandwa na hasira, akaendelea kutimua mbio akimfukuza yule kijana. Ilikuwa kama vichekesho, jinsi alivyokimbia huku amevaa chupi tu, na mtikisiko wa kitambi chake.

“Jitokeze uone! Ngedere weh!” Sabodo akafoka baada ya kufika kwenye ingo lisiloisha, alilokimbilia yule kijana. Akaanza kuangaza macho huku na kule, lakini kabla hajajikita kumtafuta yule kijana kwenye ingo hilo. Mara akasikia kishindo kutoka kule alikokuwa ameegesha gari lake. Alipogeuka kutazama hakuamini macho yake. Lori moja la taka, lililovurumishwa kwa kasi, lilifeli breki na kugonga gari lake kwa mbele. Moto mkubwa akalipuka.
“Shiiit…!” Akahamaki kwa kihoro, halafu akiwa katika mshtuko huo akaanza kuhisi kizunguzungu. Akabanwa na pumzi halafu akasikia sauti ya mtu akiongea nyuma yake.
“Jonas! Wewe sogeza gari pale barabarani, mimi na Luteni Misanya, tutambeba huyu fala.” Akasisitiza yule mtu mwenye nywele nyekundu.
“Mpigie Nana, amwambie mzee atukute La Grado Casino, saa nne na nusu usiku huu. Lazima tumalize kazi usiku huu ili kesho tukabidhi na kuondoka hapa jijini.” Luteni Misanya akasisitiza.
“Mzee ana roho ngumu yule!” Jonas akadakia.
“Mzee yupi?” Misanya akauliza kwa udadisi.
“Ngongoseke! Pamoja na lile jeraha la risasi la asubuhi kule gerezani, lakini bado yuko fiti tu!’’ Jonas akaongea kwa mshangao. Kisha akaondoka eneo hilo na kuwaacha wenzake watatu, wakimbeba Sabodo ambaye sasa alikuwa amelala chini hajitambui.

* * *

Fahamu zilipomrejea vizuri Sabodo, tayari ilikuwa imetimu saa tatu na robo usiku.
“Makadirio yangu yalikuwa sawia, tusingeweza kuwahi miadi kule La Grado Casino!” Luteni Misanya akawaza. Alikuwa mtaalamuu na mzoefu wa hali ya juu katika mambo haya. Sabodo Alipofumbua macho, hakupata shida kufahamu kuwa, alikuwa kwenye chumba alichokifahamu vyema. Alikuwa kwenye mojawapo ya vyumba vya nyumba aliyokuwa amempa kimada wake, Nana. Nyumba ambayo alikuwa mbioni kuifikia, kabla ya kukutana misukosuko iliyompelekea kupoteza fahamu. Hakuwa peke yake ndani ya chumba.

Ndani ya nyumba kulikuwa na jumla ya watu wane. Miongoni mwao aliwatambua, Nanalungu na mtu ambaye aliyerusha jiwe kwenye gari alilokuwa akiendesha. Hawa wengine; Luteni Misanya na mtu mfupi mwenye shingo nene, hakuwatambua. Alikuwa amefungwa kwenye kiti cha mbao, kwa namna ambayo watu hao walikuwa, ni kama wanaomsubiri arejewe na fahamu ili wamuhoji. Lakini mshangao mkubwa ulikuwa kwa Nana, ambaye alionekana kuwafahamu vyema wale watu.

“Nana! wewe unaweza kwenda, jamaa yako asije akarudi nyumbani na kukukosa na kuleta shida. Si unajua kuwa hata yeye tunamuhitaji sana! Hii kazi uliyofanya tangu jana, kwenye kituo cha polisi, kule gerezani na sasa kutusaidia kumpata huyu bwege, unastahili pongezi. Endelea kututumia taarifa zozote utakazopata kutoka kwa mumeo.” Luteni Misanya akaongea huku akitabasamu. Nana akatingisha kichwa kuafiki.

“Mkitoka mtanifungia nyumba yangu vizuri, hakikisheni haingii kwenye kumbukumbu zozote za mkasa huu. Hakikisheni mifupa yake mnaipeleka kwenye eneo la ajali, ili uchunguzi ukifanyika, ijulikane kuwa alifia kwenye gari kwa kuungua na moto. Misanya, nitakutumia namba ya nyumba ya Nana mwingine, ambaye ndiye ataonekana kuwa mmiliki wa gari hilo.” Nana akasisitiza wakati akiukaribia mlango wa kutoka nje ya chumba.

“Nana utalipa kwa haya unayofanya. Binti mdogo na mrembo kama wewe, kumbe upo kwenye mambo hatari kama haya. Natamani Inspekta Lucas Mwenda angejua kuwa hana mk, bali jangili tu. Shenzi na mwovu mkubwa weh!’’ Sabodo akafoka kwa hasira, lakini hakuna aliyemjali.

“Wewe na uzee wako hujui ule msemo usemao usione vyaelea ujue vimeundwa? Shenzi mwenyewe na usirudie tena kuniita mwovu! Hasa kwa vile wewe ni mwanaume. Waovu na wema hutoka kwenye tumbo la mwanamke, lakini wengi sana ukiwemo wewe Sabodo, husahau kuwa mwanaume ndiye anayeweka mtoto kwenye tumbo la mwanamke? Leo hii ndiyo unajua kuwa mimi ni malaya, sivyo? Nilivyokuwa nakupa raha hukuliona hilo? Kaa ukijua Lucas na wewe hamna tofauti. Unachomzidi ni pesa tu. Kwa vile yeye ni Inspekta wa kawaida wa jeshi la polisi, anayetegemea mshahara wa mwisho wa mwezi. Wewe na yeye ni walewale tu! Hata yeye nitammaliza hivi karibuni!” Nana akasema kwa dharau huku akichezesha kifua chake kilichokuwa na matiti ya ukubwa wastani.
“Utajutia kwa kitendo hiki. Subiri utaona.” Sabodo akafoka bila matumaini.
“Unajifariji tu kwani wakati huo utakuwa umekufa!’’ Nana akaongea kwa majigambo kisha akatoka kwa kukabamiza mlango nyuma yake.

Asanteni mnao like na ku-comment, maana mnaniwezesha kujua tuko pamoja



Imetungwa na kuandikwa na Japhet Nyang'oro Sudi

“Bwana Sabodo, una machaguo mawili tu. Kufanya kifo chako kiwe cha mateso makali au kije kwa urahisi sana. Naweza kukudunga sindano hii itakayokulaza usingizi wa milele. Au naweza kutumia nyundo hii kupondaponda viungo vyako mwilini hadi utakapokufa. Upi huru kuchagua, kwani kufa utakufa tu, tena leo hii hii. Hebu niambie, kile kikasha cheusi cha kurekodi taarifa ya safari ya ndege iliyoanguka na kuua watu juzi, kiko wapi? Pili, Judith Muga anaishi wapi?”
Kusikia swali, Sabodo macho yakamtoka kwa mshangao. Akiwa na wadhifa wa Waziri wa Ulinzi, mambo haya mawili yalikuwa kipaumbele cha juu katika ofisi yake, ndani ya siku hizi tatu. Hakuamini kuwa jambo aliloliona kama mzaha, sasa lilikuwa linaelekea kuwa hatari namna hiyo, kama ambavyo aliulizwa na huyo mtu. Akashusha pumzi. Kwa mara ya kwanza, akaona jinsi mambo yalivyomuwia magumu. Akajilaumu kwa kutochukua tahadhari ya kutosha.

**** ***** ***

ALITEMBEA taratibu kurudi pale alipokuwa amekaa hapo awali. Alipotaka kukaa ndipo akagundua kuwa kiti chake kilikuwa na damu mbichi. Macho yake yaliyosaidiwa na mwanga wa taa hafifu zilizowashwa ukumbini usiku huo, yaliweza kumtanabahisha kuwa kuna kitu cha tofauti pale kitini. Kwa kutumia ncha ya ufunguo wa gari, akagusa kile kitu na kukinusa puani. Harufu ya damu ikamgutusha. Akaangaza macho huku na kule, kuona kama kuna mtu yeyote aliyekuwa akifuatilia tukio hilo kwa makini. Akajiridhisha kuwa kila mtu alikuwa amezama kwenye starehe zilizokuwa zikiendelea La Grado Casino. Kasino ya watu matajiri na maarufu. Akatoa kitambaa kutoka mfuko wa suruali yake na kufuta damu hiyo, kisha kwa maumivu makali akaketi huku akifinya uso wake. Akiwa ameketi, akaingiza mkono wake wa kulia kwenye koti lake na kupapasa jeraha kubwa na bichi, lililokuwa likiendelea kuvuja damu mgongoni. Taratibu akalitomasa jeraha hilo kama vile muuguzi afanyavyo. Alipotazama majira kwenye saa yake ya mkononi, akagundua ilikwishatimu saa nne na dakika tano usiku. Zilisalia dakika ishirini na tano kabla ya kufika muda ambao Luteni Misanya, alimwahidi kuwa angekuwa pale na kundi lake ili kuleta taarifa ya kazi waliyopata kutoka kwa Sabodo Msumari. Kusubiri kwa muda wa saa moja na nusu, kwake ilikuwa sawa na mwaka. Alikuwa na shauku ya kupata taarifa aliyokuwa akiisubiri, kwani taarifa hiyo ingefanya mipango yake iende sawa kama alivyokuwa amekusudia hapo mwanzoni, wakati akianza kazi hii.
“Oh my God! Shiiit...!’’ Akafoka na kulaani kwa uchungu, pale kidole chake kilipopapasa tundu la risasi mwilini mwake. Akachukua simu yake ili ampigie mtu Fulani, lakini kabla hajatimiza azma yake, simu hiyo ikaanza kuita. Alipoitupia macho akaona jina la Dr. Kuselekwa lilijitokeza kwenye kioo cha simu yake.
“Vipi dokta?’’ Akauliza kwa hamasa. Sauti yake ilijawa na kitetemeshi cha maumivu makali ya jeraha.
“Nipe dakika kumi na tano, nitakuwa nimefika hapo, Bwana Ngongoseke.” Dr. Kuselekwa akasisitiza upande wa pili wa simu, huku sauti ya muungurumo wa injini ya gari lake ukihanikiza.
“Jitahidi kufika mapema, nazidi kupoteza damu kwenye jeraha. Saa sita nina kazi muhimu sana ambayo lazima niifanye. Haijalishi kama risasi hii mwilini itakuwa imetolewa au la!” Ngongoseke akasisitiza kwa sauti ya amri.
“Ondoa shaka. Kazi yangu unaifahamu vyema!” Dr. Kuselekwa akasisitiza upande wa pili wa simu.
“Halafu…’’ Ngongoseke akawa kama aliyekumbuka kitu.
“Sema mzee! Nakusikiliza.”
“Kama kawaida! Siri ndiyo ajenda kubwa hapa. Sawa…?’’
“Huna haja ya kunikumbusha hilo mzee. Mimi na wewe hatujaanza leo. Ili kuhakikisha hilo, ndiyo maana hata gari nimeamua kuendesha mwenyewe.’’ Dr. Kuselekwa akasisitiza.

Baada ya simu hiyo, Ngongoseke akaendelea kunywa taratibu huku akiyaacha macho yake yakistarehe kwa warembo waliokuwa wakijipitisha eneo hilo. Lengo lao likiwa; watamaniwe, waitwe, wasemeshwe, wasifiwe na hatimaye wapate pesa, ambazo wao waliziita malipo baada ya kuwaburudisha watu wa namna hiyo. Watu matajiri ambao akili yao haina raha, japo wanaishi sehemu zenye raha. Wanatumia vitu vyenye raha na kufanya vitu vyenye raha nyingi. Watu ambao wanajua kutumia pesa ili kupata pesa. Watu ambao hujua kuona fursa, watu ambao jamii ya kawaida huwaogopa na kuwaita matajiri. Watu ambao ni pale tu wanapomaliza shughuli ndipo hukumbuka kuwa wanahitaji kuburudishwa. Watu hao hupendelea kufika sehemu kama hizi na kukaa kwa saa nyingi. Wakiburudika kwa fahari ya macho, halafu dakika za mwisho hununua na kwenda kutumia. Japokuwa siyo watumiaji wazuri. Mfumo wa maisha yao umewafanya wasiwe watumiaji wazuri wa starehe hiyo. Kwa vile ni watafutaji wazuri wa pesa, vilevile ni wepesi wa matumizi na kuhonga. Tabia hiyo ndiyo huwavuta warembo, katika kucheza vyema turufu zao za kutafuta pesa.

Tofauti na siku nyingine, leo Ngongoseke alionekana mtu mwenye mawazo sana.
“Naona tajiri wetu leo hayuko poa!’’ Dada mmoja akimnong’oneza mwenzake.
“Kweli shoga, hata mimi nimemuona. Tangu ameingia naona ana chupa moja tu ya Whisky. Hajachangamka kabisa.’’ Mwenzake akachangia.

Saa nne na nusu ilipogonga, Ngongoseke akainua macho yake na kuyatembeza humo ukimbini. Akashangaa kuona kwenye meza yake kuliongezeka watu wengine wanne. Akashangaa kwamba hakuweza kusikia wala kuhisi, wakati watu hao walipofika na kuketi kwenye meza yake.

“Pole sana mzee, inaonekana jeraha limekuletea shida sana.” Luteni Misanya akaongea kwa utulivu.
“Acha tu, sina namna! Mtaka cha uvunguni sharti ainame!” Ngongoseke akaweka kituo, kabla ya kuendelea.
“Even in hell, there are rules. Haya hebu leta habari.”
“Tumemhoji Sabodo, amesema kisanduku cheusi kipo sehemu fulani inaitwa safe house. Ingawa yeye ni Waziri wa Ulinzi lakini hajui hiyo safe house iko wapi. Kuna watu wanne tu hapa nchini, wanaofahamu mahali ilipo hiyo safe house. Watu hao ni; Rais, Waziri Mkuu, Mkuu wa Majeshi na Mama mmoja anaitwa Bi. Anita. Ambaye ni mkuu wa kitengo cha kijasusi kiitwacho, Ofisi Fukuzi” Luteni Misanya akaongea kwa umakini.
“Good! Suala hilo niachieni mimi. Vipi kuhusu Judith Muga?” Ngongoseke akauliza huku akipisha tafakuri.
“Judith Muga amepanga nyumba namba 0713C, eneo la Masaki, Mtaa wa Chakechake.” Luteni Misanya akaongea kwa tabasamu hafifu. Kazi aliyopewa alikuwa ameikamilisha.
“Vizuri sana Luteni. Siku zote huwa nakwambia huko jeshini unapoteza muda! Wewe ulifaa ufanye kazi za kujitegemea tu. Usiku huu utakuwa na kazi gani ya kufanya? Ngongoseke akauliza kwa furaha.
“Nitakwenda kwa msichana mmoja huko Mbagala, kwa ajili ya kupandikiza zile karatasi za umiliki wa gari, iliyokuwa ikiendeshwa na Sabodo.” Luteni Misanya akaongea kwa majigambo.
“Kupandikiza…! Kivipi? Ngongoseke akahoji.
“Gari iliyokuwa ikitumiwa na Sabodo, ilikuwa imesajiriwa kwa jina la Naomi Nanalungu. Sasa kuna msichana mmoja kule Mbagala mwenye jina kama hilo. Nitaweka nyaraka za lile gari ndani ya nyumba ya huyo msichana na mambo yatakuwa sawa. Nana wetu atakuwa salama. Baada ya hapo nitarudi nyumbani kupumzika.” Luteni Misanya akaongea kwa utulivu.
“Badala ya kwenda kupumzika, nataka Judith Muga achukuliwe usiku huu. Yeye, kompyuta yake na makabrasha yake yote. Ni wazi kuwa, baada ya ile ndege kuanguka, ni yeye pekee ndiyo mwenye ule mkataba. Huko kwengine kote tumeshaondoa kumbukumbu. Kilichobaki ni kushughulika na yeye. Tukifanikiwa na malengo yetu yatakuwa yametimia.” Ngongoseke akaongea kwa hakika. Luteni Misanya akaitikia kuafiki. Kisha wakasimama na tayari kwa kuondoka.
“Vipi kuhusu hilo jeraha?’’ Luteni Misanya akauliza.
“Tangu lini ukanihurumia?’’ Ngongoseke akauliza kwa mshangao.
“Sijawahi kukuona katika hali hiyo. Wewe ni mtu wa vita ya akili na mipango. Haya mambo ya vita ya risasi na mapambano ya kutumia nguvu, hujayazoea. Haikuwa busara kulazimisha kuja kule gerezani, wakati tukimchukua Poka. Unajua ukidhurika na mpango mzima ndiyo umekufa?’’ Luteni Misanya akaongea huku akiwaonesha ishara vijana wake watangulie kutoka.
“Okay! Dr. Kuselekwa atakuwa hapa, ndani ya dakika tano zijazo. Bila shaka amewasaidia kumhoji Sabodo baada ya presha yake kupanda.’’ Ngongoseke akaongea kwa utulivu.
“Ametusaidia sana. Yule mtu anaifahamu vyema kazi yake.’’ Luteni Misanya akasisitiza.
“Kesho asubuhi nenda kafuatilie taarifa za akaunti yako benki. Utakuta tayari nimefanya mambo. Ukishamchukua Judith, mweke sehemu salama hadi nitakapokupa maagizo mengine.” Ngongoseke akapendekeza. Alitaka kusema kitu lakini akasita. Badala yake akainua kichwa kutazama huku na kule, kisha akainama. Luteni Misanya, naye akainama kusikiliza.
“Hawa vijana wako waliofanya kazi leo, wameshajua mambo mengi sana. Hawafai kuishi.”
“Unashauri vipi?”
“Kuna namna nzuri ya kuwaua. Nitakupigia kukupa maagizo ya namna ya kufanya. Nataka kifo chao kiwe cha kimyakimya.” Ngongoseke akapendekeza kwa sauti ya chini.
“Count it done, mzee. Lakini hujaniambia kuwa unataka kufanya nini na Poka Kingu?” Luteni Misanya akauliza huku akiondoka. Ngongoseke akapisha tabasamu la kifidhuli lenye uchungu ndani yake bila kutia neno. Ilikuwa ishara tosha kuwa, hakuwa tayari kuongelea mpango wake juu ya Poka Kingu.
Luteni Misanya alipofika mlangoni, akapishana na Dr. Kuselekwa aliyeingia kwa mwendo wa haraka. Nusura wakumbane kwa bahati mbaya. Walipotazamana, tabasamu jepesi likachomoza kwenye nyuso zao. Dr. Kuselekwa akaongeza mwendo kuelekea upande ambao Ngongoseke alikuwa amek

* * *

Wiki mbili baadaye...

WATU WAWILI walikuwa ndani ya nyumba moja, kati ya nyumba nyingi zinazotazamana na Slipway Hotel. Katika mtaa wa Ngomgoro, eneo la Msasani, jijini Dar es Salaam. Mawimbi ya bahari yalikuwa yakisikika kwa mbali, kutoka kwenye sebule waliyoketi. Sura zao na namna walivyoketi, ilikuwa dhahiri walikuwa kwenye mazungumzo magumu. Mmoja alikuwa mwanamke wa umri wa makamo. Mwingine alikuwa mwanaume wa kati ya miaka thelathini na nane na arobaini na mbili. Mwanamke alionekana mwenye siha njema na kipato cha kueleweka. Kwa namna ya mwonekano wake, vito vya thamani alivyovaa shingoni na masikioni, pamoja na mavazi yake ghali mwilini. Alikuwa amevaa suti nyeusi ya suruali na miwani nzuri ya kupendeza, iliyoyapelekea macho yake makali kuona vyema. Masikioni alitoga herini ndogo za almasi mfano wa punje ndogo za mchele. Kucha zake ziliwaka kwa rangi nyekundu ya kuvutia, miguuni alivaa viatu vyenye visigino virefu. Hakuwa mnene wala mwembamba. Kifua chake kilibeba matiti yenye ukubwa wa wastani na hivyo kusanifu vyema mwonekano wake. Huyo mwanamke aliitwa Bi. Anita, mkuu wa kitengo cha siri kinachoshughulika na masuala ya upelelezi na ujasusi. Kitengo hicho maalum ambacho hufanya kazi chini ya Rais, huitwa Ofisi Fukuzi.

Mwanaume aliyekuwa akizungumza naye humo ofisini, aliitwa Jacob Matata. Miongoni mwa wapelelezi mahiri wa kuaminiwa, katika idara hiyo ya kijasusi – Ofisi Fukuzi.
“Hadi sasa sielewi tatizo liko wapi?" Mpelelezi Jacob Matata akasema kwa mashaka.

Tuko pamoja? Asante kwa like na comment yako.



WATU WAWILI walikuwa ndani ya nyumba moja, kati ya nyumba nyingi zinazotazamana na Slipway Hotel. Katika mtaa wa Ngomgoro, eneo la Msasani, jijini Dar es Salaam. Mawimbi ya bahari yalikuwa yakisikika kwa mbali, kutoka kwenye sebule waliyoketi. Sura zao na namna walivyoketi, ilikuwa dhahiri walikuwa kwenye mazungumzo magumu. Mmoja alikuwa mwanamke wa umri wa makamo. Mwingine alikuwa mwanaume wa kati ya miaka thelathini na nane na arobaini na mbili. Mwanamke alionekana mwenye siha njema na kipato cha kueleweka. Kwa namna ya mwonekano wake, vito vya thamani alivyovaa shingoni na masikioni, pamoja na mavazi yake ghali mwilini. Alikuwa amevaa suti nyeusi ya suruali na miwani nzuri ya kupendeza, iliyoyapelekea macho yake makali kuona vyema. Masikioni alitoga herini ndogo za almasi mfano wa punje ndogo za mchele. Kucha zake ziliwaka kwa rangi nyekundu ya kuvutia, miguuni alivaa viatu vyenye visigino virefu. Hakuwa mnene wala mwembamba. Kifua chake kilibeba matiti yenye ukubwa wa wastani na hivyo kusanifu vyema mwonekano wake. Huyo mwanamke aliitwa Bi. Anita, mkuu wa kitengo cha siri kinachoshughulika na masuala ya upelelezi na ujasusi. Kitengo hicho maalum ambacho hufanya kazi chini ya Rais, huitwa Ofisi Fukuzi.

Mwanaume aliyekuwa akizungumza naye humo ofisini, aliitwa Jacob Matata. Miongoni mwa wapelelezi mahiri wa kuaminiwa, katika idara hiyo ya kijasusi – Ofisi Fukuzi.

“Hadi sasa sielewi tatizo liko wapi?" Mpelelezi Jacob Matata akasema kwa mashaka.

“Labda ngoja nikupe picha halisi ya jambo hili, ndiyo utaelewa mambo yalivyo.” Bi. Anita akadokeza.

“Nitashukuru sana, kwani bado nashindwa kuunganisha matukio.” Jacob Matata akapiga mwayo hafifu akijipa utulivu kichwani, tayari kusikiliza.

“Nyerere katika awamu ya mwisho ya utawala wake, alipata taarifa za za siri. Taarifa hizo zilibainisha kuwa, kulikuwa na uwezekano mkubwa wa Tanzania kuwa na hazina kubwa ya nishati ya gesi, huko pwani ya Mtwara. Zilikuwa habari za kutia hamasa kwa nchi hii masikini. Hususan kwa kiongozi ambaye alikuwa akipambana sana kutafuta vyanzo vipya vya pato la taifa, vitakavyoinua uchumi na hali duni za maisha ya raia wake.” Bi. Anita akaweka kituo kumeza mate, kisha akaendelea.

“Kwa jinsi Nyerere alivyokuwa kiongozi makini, haraka akaanza kuzifanyia kazi taarifa hizo. Uchunguzi ukafanyika na majibu yakapatikana. Hata hivyo, hakuwa tayari kupitisha mchakato wa kupima na kuanza kuchimba gesi hiyo.”

“Kwa sababu gani?” Jacob Matata akauliza kwa udadisi.
“Kwa sababu alijua kuwa ingechukua miaka mingi hadi utafiti juu ya gesi hiyo na uchimbaji wake kuanza.” Bi. Anita akaweka kituo na kuendelea. “Kwa vile nchi yetu ilivyokuwa masikini na nyuma kwa teknolojia. Katikati ya ulimwengu wenye ushindani na fitina nyingi. Hakutaka kukimbilia haraka suala hilo kama nafuu ya haraka ya uchumi wa nchi.”

“Ilikuwaje?” Jacob Matata akajenga shauku.

“Aliamua kwenda kwa hekima na mahesabu makali. Aliwaendea washirika wake muhimu wa wakati huo. Ambao ni China na Urusi, kuwaomba ushauri wa kitaalamu. Baada ya mashauriano, mwafaka ukapatikana.”

“Mwafaka upi?”

“Kabla ya uchimbaji wa gesi hiyo, ilishauriwa nchi yetu iwe kwanza na wataalamuu wake. Hivyo wakachaguliwa watanzania kumi na wawili wenye akili safi. Watu hao wakapelekwa nchini Urusi kusomea utaalamuu wa mambo ya gesi asilia. Kwa kuzingatia ushauri wa kijasusi na msaada mkubwa aliokuwa amepewa na rafiki zake hao wawili; China na Urusi. Kati ya watanzania hao, ilionekana wawili walipaswa kufanya mafunzo ya ziada. Hivyo watu hao wakaingizwa katika mpango wa mafunzo ya juu ya ujasusi.” Bi. Anita akaweka kituo.

“Kwanini ilionekana ni muhimu kuwapa watu hao wawili tu, mafunzo hayo hatari ya kijasusi?’’ Jacob Matata akauliza kwa udadisi.

“Kumbuka kuwa wakati huo dunia ilikuwa imegawanyika katika makundi mawili. Kundi la kwanza, lilifuata mrengo wa sera za nchi za magharibi, zilizokuwa zikiamini katika nadharia ya Ubepari. Kindi la pili, lilifuata mrengo wa sera za nchi za mashariki, zilizokuwa zikiamini katika nadharia ya Ujamaa. Kinara wa kundi la magharibi alikuwa ni nchi ya Marekani na uingereza. Wakati kinara wa kundi la mashariki ilikuwa ni nchi ya China na Urusi. Nyerere aliamini kwenye sera za kundi la mashariki. Huko ndiyo alipoibuka na sera yake ya Ujamaa na Kujitegemea.” Bi. Anita akaweka kituo akifikiri kabla ya kuendelea.

“Endelea, nakusikiliza vyema!” Jacob Matata akaendelea kutega sikio kwa makini.

“Kitu kimoja kilikuwa wazi. Kitu hicho ni kwamba, nishati nyingi na malighafi, vilikuwa kwenye nchi za mashariki. Hivyo nchi nyingi za Magharibi zikajikuta kwenye mkakati mzito wa kuhakikisha kuwa, zinatafuta namna yoyote ya kujenga mahusiano na nchi za kijamaa. Baada ya kufanikiwa kwa mpango huo, nchi hizo za kibepari ziliazimia kufyonza rasilimali za nchi za kijama na kuzisilimisha kwenye sera zao za kibepari. Hivyo ilitakiwa viongozi wa nchi za kijamaa waje na Plan B, au mpango mbadala wa kukabiliana na hila za nchi za magharibi. Ili ikitokea kuwa, mfumo wa dunia ukawalazimisha bila kupenda, kukubaliana na sera za uchumi wa magharibi, yaani Capitalist economy. Wawe na namna ya kuweza kwendana na sera hizo bila kutetereka.” Bi. Anita akaweka kituo kufikiri. Jacob Matata alikuwa amejenga umakini sana kufuatilia maelezo hayo. Bi. Anita akaendelea.

"Kwa vile Nyerere alikuwa rafiki wa karibu wa Rais wa China na Urusi wa wakati huo, akabahatika kuingia kwenye maandalizi ya mpango mbadala wa makabiliano hayo. Ili kama sera ya ujamaa ikishindwa, basi kuwe na uwezekano wa kuendana na sera za Ubepari. Hivyo China, Urusi na mataifa mengine ya kijamaa, yakawa yanawaandaa watu wao watakaoingia kwenye umoja wa mataifa. Watu hao walipaswa kuwa wenye taaluma kubwa za masuala mbalimbali, lakini ilikuwa ni lazima wawe na uwezo mkubwa wa kufanya ujasusi. Kwa namna nyingine naweza kusema walikuwa wanapandikiza majasusi ndani ya umoja wa mataifa.”

“Duh! Sasa ikawaje?”

“Wasiwasi wa Nyerere juu ya hatma ya gesi ya Mtwara, ulipewa uzito mkubwa na nchi marafiki. Hivyo wakati wa kupandikiza watu kwenye Umoja wa Mataifa, wale watanzania wawili waliopewa mafunzo ya ziada, walipewa nafasi ya kuingia kwenye kamati ya kudumu ya Umoja wa Mataifa, inayoshughulikia mambo ya nishati. Lakini kumbuka kuwa nchi masikini hazina uwezo wa kuwa na uwakilishi mkubwa na wa kudumu kwenye kamati hizo. Japokuwa nchi nyingi masikini ndiyo zenye rasilimali nyingi duniani."

"Ili kuwawezesha watanzania hao kuingia kwenye kamati ya kudumu ya Umoja wa Mataifa, mpango kamambe uliandaliwa. Wale watanzania wawili wakapewa uraia wa Urusi. Hilo lilifanikiwa. Si unajua tena, japokuwa kamati hizo husemwa kuwa ni za Umoja wa Mataifa, lakini nyuma ya pazia maamuzi na tafsiri ya mambo hufanywa kwa kutegemea nani anaegemea wapi.” Bi. Anita akafafanua."

ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog