Search This Blog

Thursday 23 March 2023

HUBA LA MISS TANZANIA - 2

  

Simulizi : Huba La Miss Tanzania

Sehemu Ya : Pili (2)


Waombolezaji toka pande mbalimbali za Tanzania na dunia kwa ujumla walijumuika. Watu maarufu katika jamii kuanzia Wanasiasa, Viongozi wa dini, Wafanyabiashara, Wanamichezo, na Wanamuziki nao walihudhuria msiba huo. Nyuso zao zilikuwa ni kioo cha kuonyesha kiwango cha huzuni kilichobebwa na nyoyo zao. "Mtume Muhammad...Mtume Muhammad...!!" alipayuka Sheikh Ayoub kwa sauti ya juu, waombolezaji wakawa wanamuitika "Swall-a-llahu Alaihi Wasalaam". Alikuwa anawatuliza waombolezaji wakae kimya, ili shughuli ya kuusitiri mwili wa marehemu ipate kuanza.

"Salaam Aleikum ndugu waombolezaji mliokuja kumsindikiza binti yetu Zabibu Bint Shamsi ambaye amerejea kwa Mola wake tokea jana asubuhi. Nafahamu nyote mna hamu kubwa ya kuingia kaburini, lakini hatuwezi kuingia wote kaburi ni finyu" akapumzika kuongea kumeza mate kidogo kisha akaendelea.na mazungumzo yake. "Sasa wafuatao ndio watakaoingia kaburini kuiwakilisha. Kila nitakayemtaja jina aporomokee kaburini, nao ni kaka wa marehemu Hilali Shamsi, mjomba wa marehemu Jumanne Kizinguto, Ustaadh Kalonji na Sheikh wetu Ayoub, ahsante sana" akashukuru mshereheshaji baada ya kuhakikisha wote waliohitajika kwenda kuingia kaburini wameshashuka tayari. Hekaheka za kuushusha mwili kaburini zikaanza huku kaburi likiwa limefunikwa shuka nzito kuzuia watu kuchungulia namna maiti inavyoswekwa ndani ya mwanandani, ambacho kina kichumba chembamba sana kilichopo ndani ya kaburi.

"Leteni ubao, miti na nyasi" ilisikika sauti ya Sheikh Ayoub ndani ya kaburi akiagiza vitu hivyo ili kuzibaziba upenyo ndani ya kaburini. Baada ya dakika kama 7 wakawa tayari wameuhifadhi mwili sasa ikabaki shughuli ya kushusha mchanga kaburini. Watu wakawa wanashindana kupokezana chepe ili kurushia mchanga kaburini. Baada ya kama robo saa kaburi likawa tayari limeshasawazishwa, huku mti maarufu kwa jina la mashahidi ukawa umechomekwa eneo la kichwani.



Jumamosi moja ambayo alikuja mapumzikoni nyumbani kwake toka shambani kwake alipanga atoke mtoko wa kwenda ufukweni mwa bahari. Kilipita kitambo kirefu bila kutia mguu kiwanja chochote kile cha starehe. Shebby alishang'amua na kupitishwa kwa vitendo jinsi mapenzi yanavyotesa, jinsi yanavyoweza kusababisha kifo, maziwa si msaada tena kwa sumu ya penzi. Pia alishajifunza moyo uliyojeruhiwa kwa mapenzi hauwezi kukingwa kwa vazi la chuma lililozunguka mwili mzima. Fauka ya hayo, kila aliyetambua hali yake anayopitia alikuwa anamfanyia maombi tu.

Ila watu wenye roho za kigaidi walikuwa wanamuona ni mwanaume tepetepe, mwenye mapenzi ya kihindi yenye maigizo ya nyimbo nyimbo na vilio vingi. Laiti hawa watu wakatili wangeonjeshwa walau suduthi ya maumivu yake Shebby, tungekuwa tumeshawazika tayari.


Siku hiyo akapatwa na mshawasha wa kwenda kujiburudisha ufukweni mwa bahari. Alijiandaa zake mapema mapema kwa usafi wa mwili wake, juu alivalia jezi ya buluu inayovaliwa na timu ya Chelsea ya nchini Uingereza, kuthibitisha yeye ni shabiki kindakindaki wa timu ya darajani pale Jijini London, Uingereza. Huku chini akivalia trakisuti rangi nyeusi ina mabaka ya buluu kuzunguka magotini, na raba zake za rangi ya maziwa chapa 'Adiddas'. Kwa kweli alipendeza vilivyo kimuonekano, nguo zilimkaa vilivyo mwilini hasa kutokana na umbo lake la kimazoezi.

Adhuhuri ilivyotimu akajisogeza kwenye kituo cha daladala, kuvizia usafiri wa umma, mkombozi wa wanyonge, daladala zinazoelekea stendi ya Makumbusho zikitokea Mbezi. Hakutaka kuganda kituoni kusubiria usafiri huo wa kibongo ambao hauna uhakika nao utafika saa ngapi. Akaamua atembee mdogomdogo usafiri umkute njiani ili nae anyooshe miguu. Hazikupita hata dakika tano akiwa ameshafika maeneo ya shule ya sekondari ya binafsi maarufu kwa jina la 'Libermann' akapata usafiri huo.

Kwa bahati ilikuwa ni mwishoni mwa juma daladala zinakuwa hazijazi nyomi ya kutisha, akabahatika kupata siti ya kuketi ya upande wa dirishani. Suka alikuwa fundi kwelikweli wa kulikamua gari lake alikuwa haliendeshi gari lake kwa mwendo wa mzofafa kama yupo harusini, alikuwa anajua abiria wanawahi kwenye pilikapilika zao za siku. Ghafla wakajikuta wameshafika kituo cha 'Massana Hospital' meta chache kutokea barabara ya 'Mwai Kibaki Road' au kwa jina la zamani 'Bagamoyo Road', Shebby Zoo akapatwa na mfadhaiko wa moyo na simanzi, akawa amejiinamia. Alitoneshwa donda la moyo baada ya kuitia machoni hospitali hiyo ilimpa kumbukizi mbaya sana maishani mwake aliyowahi kuipitia katika kipindi cha mapenzi yake na Zabibu.

"Sorry sana Bwana Shabani,mpenzi wako amepata miscarriage...mimba imeharibika, tutakaa nae kwa siku moja zaidi kumchunguza. Maana katuambia amekunywa soda ndipo dalili zikamuanza za maumivu.." alikuwa anafanya kumbukizi ya miaka minne iliyopita, majibu aliyopewa na daktari, siku alipomkimbiza kwa dharura mchumba wake Zabibu hospitalini hapo baada kuanza kutokwa na damu sehemu za siri. Maelezo ambayo yaliupasua moyo wake vipande vipande na kuzima ndoto yake ya kuitwa baba.

"Mwanangu angejaaliwa uhai sasa angekuwa na 4 years sasa angekuwa vidudu anahesabu tu kwa kimombo one..two..three!. Mwanangu angekuwa ni zawadi tosha niliyoachiwa na mpenzi wangu Zabibu, na angenipunguzia uchungu wa kifo cha mama yake" alizidi kuzama kwenye dimbwi la mawazo.

"Afrikana kituo...., Afrikana wa kushuka oyaaa...changamkeni, wa kupanda pandeni na wa kushuka fastaa msiuweke usiku, ni mwendo wa panda mti kata mti" maneno ya kondakta wa daladala ile ndio yalimuibua juu Shebby kutoka kwenye kina kirefu cha bahari ya mawazo alichokuwa anaogelea. Akajizoazoa kitini na kuharakia mlangoni kushuka.

"Oyaaaah...nauli mzee baba hamna stafu humu...hapa ni pesa tu" kondakta alimkumbusha Shebby Zoo ambaye kutokana na kutingwa na mawazo alishasahau kulipa nauli ya daladala. "Oooh...Samahani, nilipitiwa" akajibu Shebby huku anamfinyangia noti ya shilingi elfu tano. Akarudishiwa chenji yake ya shilingi elfu nne mia tano, kondakta akaruhusu gari kwa kupiga kofi bodi ya daladala, ikakitoa zake huku inafurumusha moshi angani.

Shebby Zoo akarudi nyuma kidogo ya barabara kulikuwa na bajaji zimepaki zinasubiri abiria huku pembeni ya bajaji hizo zilizojipanga kulikuwa na meza ya muuza magazeti, akaisogelea kushangaa magazeti ya siku hiyo. Baada ya kusoma vichwa vya habari akapendezewa na gazeti la michezo linaloitwa 'Kabumbu Uwanjani' akalilipia na kujinyakua pale mezani. "Broo...karibu hii hapa nikuhudumie tunapakia kwa zamu" alikaribishwa na mmoja wa waendesha bajaji. Shebby hakujibu kitu akaingia moja kwa moja, na kumpa maelekezo, "Nipeleke Jangwani Sea Breeze Resort tafadhali..". Muendesha bajaji akatii kwa vitendo ombi hilo.

Iliwachukua takribani dakika kumi na mbili na nusu mpaka kufika ufukweni hapo. Akamalizana nae malipo ya gharama za usafiri. Akawa anajongea kwa mwendo wa pole ndani ya hoteli ile. Akaingia ndani na kulipia kiingilio kisha moja kwa moja akaenda kwenye midule yenye kivuli cha makuti na kuketi. Mara moja mhudumu wa hoteli akamchangamkia kwa kumfuata pale alipokaa na kumuongelesha. "Kaka yangu karibu sana, nakusikiliza mahitaji yako". "Ahsante naomba hiyo karatasi ya orodha ya vyakula na vinywaji".

Akakabidhiwa na yule dada mhudumu ile karatasi ya Menu, akaanza kuisoma. huku ameiinamia kisha akanyanyuka na kumuongelesha yule dada mhudumu. "kinywaji Fanta Orange kisha niletee....Fried Chicken with Salads..". "Nimekuelewa, chakula itabidi usubirie kati ya dakika tano mpaka kumi" akasema yule dada huku Shebby akikubaliana nae kwa kuinamisha kichwa chake. Mhudumu yule alipoondoka zake,akalifungua gazeti lake la michezo na kuanza kuperuzi kurasa zake kujua kilichojiri katika ulimwengu wa soka Tanzania na duniani kwa ujumla.

Taratibu alishaanza kuizoea hali ya kutokuwa pamoja na mpenzi wake Zabibu. Zamani enzi za uhai wa mamsapu wake Zabibu walikuwa wanagandana kama luba, popote alipo Shebby na Zabibu yupo. Mpaka baadhi ya wanaowafahamu ambao wanawatakia heri wakawapachika lakabu ya 'Love Birds'. Mahasidi, wale wenye vijiba vya roho nao hawakuacha kuropoka maneno ya asidi dhidi yao, wapo waliowasimanga kuwa wanaishi maisha ya tamthilia ya kufikirika.

Wapo walioenda mbali zaidi na kusema kuwa Shebby Zoo amemloga Miss Tanzania, amemwendea kwa wataalamu wa mitishamba Zabibu ili tu amkubali kuwa mpenzi wake. Kigezo chao kikubwa kilikuwa haijawahi kutokea dereva taksi kama Shebby eti afaidi huba la Miss Tanzania mwenye viwango vyake kama Zabibu, ambaye Mapredeshee na Maofisa wenye milundi ya mali wanalizengea huba lake.

Akiwa amezama kwenye gazeti lake pendwa la michezo, akashtukia anagongwa begani. "Komredi upoo..!siamini kama nimekutia machoni, kitambo kirefu sana hujaonekana viwanja kama hivi. Pole sana na matatizo yaliyokupata ndio dunia ilivyo kikubwa subira tu" alizungumza huyo jamaa yake Shebby aliyevalia fulana nyeusi zenye na maandishi ya kijani kifuani yaliyoandikwa 'RAJA SAFARI TOURS'. "Ohooo...Kenny daah kitambo sana mzee wa pori hatujaonana ila ndio mbiringe mbiringe za maisha, mie nimeshapoa, yamepita" alijibu huku akiwa amesimama kumlaki mgeni yule wanayefahamiana kitambo.

Mhudumu akawa tayari ameshaleta chakula pale mezani. "Aisee...dada yangu msikilize na huyu anachotumia, bili zote juu yangu naomba Kenny usikatae ukarimu wangu kwako maana wewe moja haikai wala mbili pia haikai" alitoa angalizo Shebby huku wote wanakaa kwenye viti. "Sawa bwana umeshinda mie niletee Coca-cola bariiiidiii basi niisuuze roho yangu na joto hili la Bongo" aliagiza Kenny, huku anamsindikiza kwa macho yule mhudumu anavyotembea mzofafa.

"Bado tu Kenny...hujaacha tabia zako za kupenda totoooz..." alimchomekea baada ya kuona Kenny amekodolea macho kwenye miondoko ya yule dada. "Ng'ombe hazeeki maini afu si unajua kazi na dawa, sie watu wa pori hawa viumbe adimu sana kule ha...ha...ha... " alijisifia Kenny sifa yake ya ukware kwa akina dada. "Kulikoni mbona hapa tena na sare za kazi? " aliuliza Shebby baada ya kumuona hajavaa libasi za kuja kupumzika ufukweni. Maana juu alivaa hilo fulana yake, huku chini akivaa dangirizi ya buluu na safari buti nyeusi.

"Aaah...acha tu, nimekuja na wageni wangu Wataliano niliwapeleka mbuga ya Serengeti sasa nimerudi nao leo, wametaka wapate mlo mchana hapa kisha nawarudisha hotelini walipofika. Kesho wanaamsha kurejea kwao Itali" alieleza nia na madhumuni ya uwepo wake pale. "Daah...Waitali kavu sana, ni wababe na ni wabahili kuwa makini maana hata bakshishi zao ni kiini macho, anaweza kukupa tip ya dola 100 kumbe ni feki ha.. ha . ha... ha.." wakafa kwa kicheko wakichambua janja janja ya Waitali.

Kama ulikuwa hufahamu, Shebby na Kenny wamewahi kufanya kazi pamoja kwenye kampuni ya kuongoza watalii ya RAJA SAFARI TOURS kwa zaidi ya miaka 6, baadaye Shebby kibarua kikaota nyasi, akajiingiza kwenye taksi za UBBER huku Kenny akiendelea kulisongesha mpaka leo hii wanayokutana. " Unayosema ni kweli tupu hawa bwana kama Waswahili tu wana roho ya korosho. Watalii toka Swiss na nchi za Skandinavia kwa ujumla wapo poa sana, wale unaweza kuvuna mpaka bakshishi ya dola 1000 kwa safari moja" aliendeleza mada dereva Kenny huku wanashushia mazungumzo yao na vinywaji vyao waliyoagiza.

"Kuna safari moja bwana, nilienda watalii toka Norway, mbuga ya Mikumi basi kabla hatujatoka huku walianza kunitangazia dau langu la bakshishi. Wakaniambia nikiwaonyesha Simba watanipa dola 150, nikiwaonyesha Tembo dola 100, chui nae dola 150, na hawana longolongo hapo hapo wakiwaona wanakupa chako" alichagiza mazungumzo Shebby huku akiwa amemaliza chakula anachokonoa nyama zilizonasa kwenye meno yake kwa vijiti maalumu. Sasa ukiwabahatisha pale 'KIA Airport' halafu wakikuambia uwapeleke BOMA MASAI hapo ndio umekula bingo, maana huwa nawatia ndimu kuwa kuingia BOMA MASAI kushuhudia mila na tamaduni za kabila la Wamasai kila mtalii lazima alipe dola 20. Sasa ukiwa na vichwa 10 tayari unazo dola 200, kule kwa Wamasai wao tozo yao wanataka shilingi elfu ishirini na saba tu" alitoa siri namna waongoza watalii wanavyopata kipato cha ujanja ujanja kupitia watalii.

Wakiwa kwenye mazungumzo yao, wakikumbushiana michapo mbalimbali ya enzi wapo pamoja kazini, ghafla bin vuu simu ya Kenny ikaanza kuita. "Daaah..!tayari itakuwa wanataka kuondoka. Hellow..!OK...OK..i'm coming right now..!!" Ebana mie nawapeleka wazungu wangu wakapumzike. Ahsante kwa kuchati tutafutane bana usijitenge" wakaagana huku wakibadilishana namba za simu.

Akapiga hatua kama tatu tu, ghafla akageuka Kenny, "Mungu wangu weeeh...! Nikitaka kusahau jambo muhimu kwelikweli. Kuna barua yako, bahasha kubwa ilitumwa pale ofisini kwetu yapata miezi sita sasa. Kila nilipokutafuta kwenye simu sikukupata hewani, na nilishawahi kuja kwako Goba mara moja lakini hukuwepo sasa sijui tunafanyaje....?"

MAMBO YANANOGA SASA,BARUA INA MIEZI 6 INA NINI HIYO BARUA TENA????
ENDELEA KUFUATILIA HADITHI HII


Kila nilipokutafuta kwenye simu sikukupata hewani, na nilishawahi kuja kwako Goba mara moja lakini hukuwepo sasa sijui tunafanyaje....?" aliulizwa Shebby na rafikiye Kenny. "OK...vizuri ahsante wa taarifa nitaangalia namna ya kuipitia jumatatu ofisini kwenu kabla sijaenda shambani" alishukuru Shebby huku wakipeana mikono tena kwa mara ya pili. Shebby akawa anaendelea kula upepo mwanana wa bahari, sehemu ambayo feni haiwashwi labda uwe majinuni ndio utawasha feni ufukweni mwa bahari. Alivyochoka kukaa akaaanza kutembea pembezoni mwa bahari ili mradi lengo lake la kujipumzisha likatimia vilivyo. Ilipotimia muda wa magharibi akaanza harakati za kurejea nyumbani kwake. Mpaka kufika majira ya saa tatu kasoro usiku, akawa tayari kashawasili nyumbani kwake.

Ghorofa za ofisi ya RAJA SAFARI TOURS zilikuwa zipo katikati ya Jiji la Dar es Salaam, katika makutano ya mtaa wa Ohio na Sokoine Drive. Lilikuwa ni jengo lenye mvuto wa kipeke yake kwa jinsi lilivyosanifiwa kimaridadi likiwa na roshani tano. Ilimchukua takribani dakika 45 Shebby kufika ofisini hapo kutokea nyumbani kwake Goba. Alidamka asubuhi na mapema kwa malengo akishachukua hiyo barua aliyoambiwa jana afanye mipango ya kupitia sokoni Kariakoo kwa ajili ya kupata mahitaji ya shambani kwake kama madawa ya kudhibiti wadudu wa mazao shambani kisha ndio aelekee porini kwake Kiwangwa akajichimbie. Sasa Jiji alikuwa analiona halina thamani tena kwake bora ajichimbie porini tu kusakanya pesa za shambani ndio kazi iliyobakia kwake. Hakutilia uzito wowote barua hiyo anayoitiwa, alikuwa anajua ni barua tu kama zingine, ila alikuwa anadhania huenda barua hiyo inatoka wizara ya ardhi kukumbushia malipo ya kodi ya viwanja na nyumba ya familia yao iliyopo Kariakoo. Pia alipanga kama itakuwa ni barua ya ardhi, basi pia atapitia benki kabisa kulipia ili amalizane nao kabla hawajacharuka kutaka kuuza mjengo na viwanja vyao. Miaka nenda miaka rudi, alikuwa anatumia anuani ya posta ya kazini kwake kwa zamani kwa ajili ya mawasiliano yake ya barua. "Hellow...Sada za masiku upo bado... ? " alisalimia kwa uso wa bashasha Shebby huku anampa mkono dada huyo wa mapokezi ya wageni wenye kuhitaji kukodisha magari kwa ajili ya safari zao za kitalii na safari zingine zozote binafsi au za kiofisi katika kampuni hiyo ya RAJA SAFARI TOURS. "Aaah...Aaah...Aah..ni wewe kweli kaka yangu au mzimu wako... ! Siamini kaka yangu Shebby, umeamua kutupa jongoo na mti wake sawa bwana, Mungu anakuona ujue" alijibu salamu dada yule huku akiwa analalamikia kitendo cha Shebby kukata mguu ofisini kwao. "Afu nilisahau pole na matatizo ya msiba, sikuwa na taarifa kabisa za ndoa yako, ila habari nilizipata kwenye mitandao na magazeti, Mungu akupe faraja na subira kubwa" alizungumza Sada huku uso wake ukivaa huzuni kwa msiba wa mpenzi wake Zeddy. "Nimepoa kabisa sina hata kinyongo ndio mitihani ya duniani ingawa ni ngumu sana kukubaliana na kilichotokea. Halafu pia nisamehe nakiri sikutoa taarifa kwa watu wengi sana, sikutaka kukupeni takilifu ya kunichangia, kama ujuavyo kipato sasa hivi kimekuwa kigumu sana, unakuta mtu kwa mwezi ana mzigo wa kadi za harusi karibia tano na wote wanambananisha kwenye kona kuwa lazima awachangie" alishukuru na kujitetea kwanini hakuwapa taarifa za harusi yake. "Anyway... nina haraka kidogo sijui Kenny nimemkuta?" aliuliza Shebby akimjulisha kilichomleta pale ofisini. "Kenny katoka kidogo kaelekea uwanja wa ndege wa Mwalimu Nyerere kawapeleka wageni wake, ila kuna mzigo kaniachia kasema ukifika nikukabidhi" alijibu dada yule wa mapokezi huku akigeukia nyuma ya kabati lake kuchomoa hiyo bahasha aliyokabidhiwa, huku Shebby akiwa anaisubiria bahasha hiyo huku ametia mikono yake kwenye mifuko ya suruali yake anapiga mluzi. "Haya ahsante sana, tutaonana dada yangu usijali mambo ni tumbitumbi hayajatulia bado, wewe ni kama hirizi hapa kamwe huwezi kuacha kazi, mhindi kakurogezea" aliaga Shebby kwa utani wote wakafa kicheko na kupeana mikono ya kwaheri. Shebby akawa anatoka sasa ya ofisi hiyo iliyopo roshani ya pili, akaamua ashuke chini ya jengo kwa kutumia ngazi na sio lifti. Akatembea mpaka alipofika chini ya jengo akakutana na kibao kikubwa chenye nembo ya kampuni hiyo ya RAJA SAFARI TOURS, akawa anakumbukia siku yake aliyofutwa kazi pale ofisini. "Iko veve naendekeza sana mapenzi kuliko kazi, habari zako zote ninazo sitaki kukuona unakanyaga tena hapa ofisini kwangu, sitaki watu wavivu hapa, kabidhi kila kitu changu cha kiofisi" mwangi wa sauti ya mhindi yule Patel ulikuwa inajirudiarudia tukio la miaka sita iliyopita kila nilipoiangalia nembo ile. Akashukuru Mungu tukio lilipita na maisha yanasonga mbele kwa mbele sasa yupo Kiwangwa anakomaa na mananasi. IIlikuwa ni kampuni yenye uzoefu wa zaidi ya miaka 40 kwenye shughuli za usafirishaji hasa watalii katika mbuga mbalimbali za Tanzania. Ilikuwa ni kampuni ya familia ya Bwana Rajeev Patel iliyohamia Tanzania kutokea nchini India na kuamua kujikita kwenye shughuli hiyo. Ilikuwa na magari ya aina mbalimbali ya usafirishaji zaidi ya 200 kwa idadi. Wafanyakazi hapa walipapenda sana kufanya kazi kwa sababu alikuwa anawajali na kuwalea kama familia yake tofauti na tabia za wawekezaji wengi wa kihindi ambao wanawafanya wafanyakazi wao kama watumwa. Yeye Bwana Rajeev dereva yoyote alikuwa akiendesha gari miaka mitatu mfululizo bila kosa lolote la kinidhamu anakukopesha gari linakuwa lako kisha anakukata kidogo kidogo kwenye mshahara. Ilikuwa ni bahati mbaya sana kukuta dereva wa RAJA SAFARI TOURS kumkuta yupo choka mbaya kimaisha, apeche alolo, wengi wao walikuwa wanamiliki nyumba zao na magari yao wenyewe na Shebby alikuwa tayari ameshanunua kiwanja . Ndio maana siku Shebby anafukuzwa kazi kama mbwa kila mfanyakazi pale RAJA alishangaa sana, hawakujua kuna nini baina yao, siri ya mtungi aijuaye kata. Maana haikuwa kawaida ya Bwana Patel kumkoromea mtumishi wake namna hiyo, wakayaacha kama yalivyo. Alipofungua mlango wa gari lake tu kabla hajafunga mlango akapata kimuhemuhe cha kufungua bahasha hiyo kubwa ya rangi nyekundu ili kufahamu kuna ujumbe gani ndani yake. Mapigo ya moyo wake yalikuwa yanaenda kasi, alishaanza kuhisi sio barua ya kiserikali kama alivyodhania mwanzoni. Maana bahasha nyingi za serikalini ni za rangi ya kaki na wakati mwingine huwa zinakuwa na nembo ya taifa ya Adamu na Hawa, lakini hiyo ilikuwa ni bahasha ya rangi ya nyekundu mpauko, kutokana na kuwa ilishaanza kuchoka kwa kubadilika rangi kutokana na kupigwa vumbi muda mrefu. Vidole vilikuwa vinamtetemeka kama mlevi wa gongo wakati anachana gundi ya bahasha hiyo. Ule mwandiko wa juu ya bahasha ndio ulimuogopesha, ulikuwa ni mwandiko ambao karibia asilimia 99% anaujua mwandishi wake. Alichokuwa anatafuta ni uthibitisho tu kuwa ni kweli huyo huyo anayemjua ndio mwandishi wa barua hiyo au hati zao tu zimeshabihiana?. Kufungua tu ile bahasha na kutoa vilivyomo , Loooh Salalee weee.! ni yule yule mtu aliyekuwa anamhisi ndio mwandishi wa barua hiyo ndefu. Barua ambayo imekuja kutonesha kidonda chake cha huba katika moyo upya. Damu za kidonda hicho kilichokuwa kinakaribia kupona sasa kwa takribani muda wa miezi sita ya kukiuguza. Barua imekuja kuchubua upya majeraha ambayo kupona kwake hakuwezi kutibiwa na daktari bingwa wa upasuaji wa moyo, si kule hospitali ya Apollo, India wala sio Daktari bingwa Mohamed Janabi wa Jakaya Kikwete Cardiac Institute (JKCI), pale hospitali ya taifa Muhimbili. Bahasha ikamdondoka chini ya miguu yake ndani ya gari pale kwenye siti ya dereva. Akafanikiwa kuiokota bahasha huku jasho jekejeke likawa linamtiririka utasema yupo katikati ya jangwa huko Darfur, Sudani muda wa jua la mtikati ambapo joto la nje ni kali sana hufikia wakati mwingine mpaka sentigredi 40. La hasha...! hayupo Darfur, yupo Jijini, Dar es Salaam lakini kilichompandisha joto si kingine, bali ni joto la huba, huba la Miss Tanzania, mlimbwende wake, marehemu Zabibu. Alikuwa ameleta salamu za huba lao toka kuzimu. Alichofanikiwa Shebby ni kuifungia barua ile kwenye droo ya kuhifadhia nyaraka zake ndani ya gari na pia kupata nguvu za kumpigia simu dereva wake wa taksi yake ya UBBER anayoiendesha. Taksi ambayo kwa siku hiyo Shebby aliichukua kwa makubaliano kuwa afanyie misele yake ya mjini akimaliza mizunguko yake amkabidhi yeye arejee shambani kwenye kupiga jembe kama kawaida. "Hellow..Sheni, samahani nipo RAJA SAFARI TOURS njoo nifuate sijisikii vizuri kabisa kifua, mapigo ya moyo siyaelewi kabisa tafadhali njoo haraka! " akakata simu yake. Mapigo ya moyo yaakanza kupungua taratibu akaanza kujihisi kichwa kinauma na kizunguzungu kikali, akapoteza fahamu hapo hapo, hajui tena linaloendelea duniani. Barua toka kuzimu, yenye ujumbe tatanishi toka kwa mpenzi wake Zeddy ikawa imezua kasheshe upya.



Baada ya siku mbili za kulazwa katika hospitali ya Agakhan iliyopo jijini Dar es Salaam karibu na barabara ya Ufukoni, Shebby alikuwa tayari kupewa ruhusa. Afya yake iliimarika vilivyo hivyo alikuwa hana budi kuruhusiwa arejee nyumbani kuendelea na shughuli za ujenzi wa taifa. Uzuri wa mambo Daktari Shaqeel wa Agakhan ni mmoja wa Madaktari waliomhudumia kisaikolojia miezi sita Iliyopita alipoletwa toka Tanga akiwa hajitambui. Na ni daktari ambaye kwa kawaida ana maneno mengi kama kitabu mgonjwa akimsikiliza tu maneno yake anajiona amepona kabla ya kuanza matibabu. "Bwana Shabani, afya yako ipo mikononi mwako mwenyewe, ukiamua kujiua ni wewe mwenye na ukiamua kuishi kwa furaha ni wewe mwenyewe, kupanga ni kuchagua"aliongea Dr.Shaqeel kwa sauti ya huruma akionyesha hapendezwi na suala la kudorora tena kwa afya ya mgonjwa wake mara kwa mara. "Narudia tena, tatizo lako sio lenye kuhitaji kumeza vidonge vya kuondosha msongo wa mawazo, bali ni tatizo la kisaikolojia tu. Nakuomba ufuate kanuni zile nilizokuwa nakufundisha na ukaamua kuzifuata ipasavyo mpaka kwa muda wa miezi sita afya yako ikatengamaa na kuimarika vilivyo. Nitakupa na kitabu kipya kimetoka hivi karibuni tu kinaitwa 'A Widow’s Guide to Healing' kitakusaidia sana. Lakini nilipokufanyia vipimo leo kuna tatizo jipya nimeligundua kwako uniazime masikio yako" alisema Dr.Shaqeel huku anaweka miwani yake vizuri kisha akaanza kuuma kizibo cha peni yake ya kuandikia kana kwamba anasitasita kuendelea na kulieleza hilo tatizo. "Nipasulie ukweli tu Dr.Shaqeel, sasa nimeshakata shauri la kubadilika. Nimeshajifuma ujinga wa bure ninaoufanya, na tatizo la ujinga hauna kikomo hivyo nikiendelea na hii hali nitateseka mpaka siku naingia kaburini. Hivyo wewe Daktari wewe mwaga tu mchele kwenye kuku wengi moyo wangu upo tuli umetulizana raha mustarehe kama Sultani bin Jelebi" alizungumza Shebby kwa kujiamini, kwa sauti iliyokuwa inaonyesha kweli ameamua kubadilika. Alishatambua kukasirika au kuhuzunika ukiwa na tatizo wala haikusaidii kuondosha tatizo ulilo nalo bali mambo hayo yanaweza kuchochea matatizo mapya zaidi ambayo haukuyatarajia. Kama yeye Shebby tayari alikuwa kamkosa mpenzi wake walioshibana lakini akiendekeza msongo wa mawazo atakuja kuzalisha matatizo mapya kama shinikizo la damu, mshtuko wa moyo na hata kansa. "Mhh...Mhhiii..." alikohoa Dr.Shaqeel kuliweka sawa koo lake huku akishangazwa na ujasiri wa simba nyikani uliomvaa ghafla bin vuu mgonjwa wake Shebby. Kabla ya kuendelea na kitu kipya anachotaka kumuambia Shebby kuhusiana na tatizo jipya la kiafya lililoibuka kwake akafungua faili lililopo mezani kwake kisha akaanza kuongea "Tulipopima damu yako safari hii, tumekuta ni chafu....nikawaambia.....!" "Chafu kivipi sikuelewi ujue Bwana daktari.." alikatiza Shebby maongezi ya Dr.Shaqeel huku anapigapiga meza ngumi kwa kishindo. Maneno ya daktari yalipenya kama mshale wa sumu katikati ya moyo wake hasa baada ya kuona mambo yanazidi kuharibika kwa upande wake badala ya kupata tahfifu anazidishiwa uzito fauka uzito. "Punguza presha na munkari, Laa tahzani lazima nikuambie ukweli siwezi kukuficha na daima ukweli ndio utakuweka huru. Umegundulika kuwa na virusi vinavyosababisha ugonjwa wa UKIMWI baada ya vipimo vya damu kubwa. Ila kuishi na virusi ni jambo lingine na kuumwa ugonjwa wa UKIMWI ni jambo lingine. Ukizingatia kanuni bora za afya na lishe bora kama zinavyoshauriwa na washauri nasaha utaweza kuishi kwa matumaini raha mustarehe. Utaweza kutimiza ndoto zako mbalimbali ulizojipangia kimaisha kama kujiendeleza kwa kipato, elimu, kupata watoto, na mengineyo mengi tu kama wanayofanya wasio na virusi vya UKIMWI. Je una swali lolote kuhusiana na virusi vya UKIMWI?" aliulizwa Shebby na Dr.Shaqeel baada ya kuelezwa kinagaubaga namna ya kuishi kwa matumaini. Alishusha pumzi ndefu zilizotoa sauti, huku akikodoa macho yake kama bundi na kuyapepesa macho hayo kama mtu aliyebumburushwa usingizini, kuonyesha kapashwa habari mpya, ambayo ni nzito na mbaya sana aliyokuwa haitarajii. Kichwani mwake akiwaza namna wagonjwa UKIMWI wanavyokonda kama samaki ng'onda ndio na yeye atakuja kuwa hivyo. Pia akawa anafikiria namna watu wanavyo wanyanyapaa wagonjwa UKIMWI kama mtu mwenye ukoma. Kikapita kitambo kirefu kidogo huku akiwa Shebby amejiinamia kama kobe anayetunga sheria bila kuzungumza kitu chochote huku Dr.Shaqeel akiwa kajiweka tayari tayari kwa lolote. Maana taarifa za damu ya mtu kuwa chafu kila mmoja huipokea kivyake katika binaadamu. Wapo ambao wanataka kutembeza kipondo kwa daktari aliyempa taarifa hiyo na wapo ambao wanapoteza fahamu na hata kufa hapo hapo hivyo alijiandaa kukabiliana na lolote lile. Alishapigilia msumari mwingine kwenye moyo wa Shebby, ila ukweli wa mambo msumari uliomchoma mja hutokea pale pale ulipoingilia. Alishusha pumzi ndefu hufyu kijana Shebby huku akichegama mgongo wake kwenye kiti alichokalia akionyesha amechoka kutokana na ujumbe mzito aliopewa. Taarifa ya daktari ilimtingisha kichi kichi, alikuwa amepoa kama tangopepeta, kisha akafungua mdomo wake kuzungumza. "Nimepokea kwa masikitiko taarifa hii ya hali mpya ya afya yangu, moyo wangu umevunjika keche keche, lakini maji ukiyavulia nguo huna budi kuyaoga na hata hili jipya ulilonipa leo nitakabiliana nalo bila vikwazo vyovyote, sitotetereka tetere kama wafanyavyo wengine wakipata habari ya msiba ugongao moyo kama huu wa UKIMWI. Siwezi kusema taarifa hii haitonisumbua nitakuwa ni muongo, itanisumbua kimawazo lakini naamini baada ya muda nitakaa sawa sitoendelea kutepwereka tepwere la hasha!. Ila kinachonistaajabisha ni kuwa wiki moja kabla hatujataka kufunga ndoa na mke wangu tulipima vipimo vya UKIMWI katika moja ya hospitali kubwa tu ya binafsi hapa jijini Dar es Salaam na majibu tuliyopewa sote tuliyafurahia mimi na mchumba wangu mara tu tulipofahamu kuwa afya zetu ni njema. Sasa hapo ndipo ninapotatizika, ina maana vipimo vyao ni feki au nyie mmekosea? " aliulizwa Shebby swali gumu linalohitaji jibu gumu ili kumkinaisha vilivyo. "Vipimo vyako hata mimi vilinishtua sana, ikabidi nichukue damu upya mimi mwenyewe, kisha niingie maabara mimi mwenyewe kufanya vipimo. Majibu yangu na yale ya awali ya mtaalamu wa maabara yakalingana. Hivyo hospitali mliopima mara ya kwanza unaweza kuta wapo sahihi pia, kwa maana ukipima ukakuta hauna virusi vya UKIMWI unatakiwa urudie tena kupima baada ya kupita miezi mitatu" alimfafanulia vyema ili kumuondoa wasiwasi. Baada ya mazungumzo hayo yaliyogeuka kuwa ya kirafiki zaidi kuliko uadui, Dr.Shaqeel akaagana kwa kupeana mikono na mgonjwa wake kwa kumkabidhi kile kitabu cha kujisomea alichomuahidi. Uzuri wa Shebby kimombo kilikuwa hakimpigi chenga ingawa kaishia darasa la saba pale shule ya msingi Ilala, Boma lakini kukaa kwake muda mwingi na wazungu huko mbugani wakati wa kazi kulimnufaisha vilivyo kuijua lugha kiundani. Shebby akawa anatoka ofisini kwa Dr.Shaqeel huku yupo mnyonge haamini kama matatizo yote yanamuandama yeye, "ama kweli huu ni mwaka wa tabu kwangu" aliwaza Shebby huku akiwa tayari kashatoka nje ya jengo la hospitali, anajiandaa kuliita gari lake limrudishe nyumbani. Mawazo yalimjaa fori fori hajui ashike lipi na aache lipi.

Shebby alikuwa juu ya kitanda chake cha samadari, nje angani giza totoro nyumba nzima akiwa yupo peke yake anagaragara usingizini macho meupe pee hayana hata lepe la usingizi. Alikuwa anabingirika bingiri bingiri na kutangatanga kwenye kitanda kile kama kuku anayetaka kutaga. Barua yake iliyomsababishia kasheshe la kulazwa Agakhan alishaichukua kwenye gari na kuiweka nyumbani. Alipanga kesho yake akishapata staftahi ya asubuhi aisome ajue kuna ujumbe gani mahususi toka kwa Zabibu. "Lo masalala! Itakuwa ndani yake hiyo barua kaeleza chanzo chake cha kujiua. Itakuwa alijiandaa kumbe, akanicheza shere bure mtoto wa mwenziwe. Kesho Inshallah nitajua mbivu na mbichi za tukio zima lililosababisha ndoa yetu ikwame, ikanyorora nyororo" mawazo yalikuwa yanaendelea kumtafuna ila sasa kwa unafuu sio katika hali ya kumtetelesha afya yake. Afanalek! Huu UKIMWI nao mie nimeupataje? tokea nianze mahusiano na kipenzi changu Zabibu katu Yasin mkubwa! naapa sijawahi kuchepuka, Mwenyezi Mungu azizi na baswiru wa kila kitu ni shuhuda wa hilo" mkondo wa mawazo mbalimbali yalikuwa yanatiririka kichwani mwake. "Katika mahusiano yangu na Zabibu tulikuwa na utaratibu wa kupima mara kwa mara afya zetu sasa huyu mdumu kapitia wapi, au ndio uchawi tena wazee wataalamu wa fani ya mduni wamefanya yao dhidi yangu? Hawakupenda nimdhibiti mrembo mkali kama Zabibu wakaamua wanitumie makombora? Au labda umepitia kwenye mashine za kunyolea nywele kwa kinyozi mitaani? Mashine ambazo usafi wake ni tia maji tia maji! " maswali lukuki yasiyo na majibu ndio yalimfanya awe macho mpaka manane ya usiku. Fikra zake hazikutaka kabisa kupeleka tuhuma za kuambukizwa UKIMWI na mpenzi wake Zabibu, kwa sababu alikuwa anamjua fika uaminifu wake kwake ni wa kiwango cha kutukuka. Akaanza kuleta fikra na kumbukizi siku ya kwanza namna walivyokutana na mpenziwe Zabibu. Maana kila wapendanao wana sampuli ya peke yao iliyowakutanisha, kuna wanawake wengine waume zao ni makondakta wa daladala walikutaniana ndani ya daladala wakati wanakoromeana kurudiashiana chenji. Wengine wamefahamiana kwenye mitandao ya kijamii kupitia Facebook, Whatsapp, Instagram na mingineyo. Mbali ya hao, wengine wamekutana kwenye nyumba za ibada ili mradi kila binadamu wapendanao wamekutana kivyao vyao.
"Shebby iko kuja kazi hapa, takiwa wewe peleka warembo kule Saluu, nenda kwa keshia upate njuruku zako" alipewa maelezo Shebby akiwa ndani ya ofisi ya Mkurugenzi mkuu wa kampuni ya RAJA SAFARI TOURS alikuwa anapewa maagizo na Bosi wake mhindi mwenye kiswahili kibovukibovu utasema amekuja Tanzania wiki iliyopita, kumbe ni mzaliwa wa hapa hapa babu na babu zake. Tatizo la jamii ya kihindi linalowafanya washindwe kuongea kiswahili fasaha ni kujitenga na watu wa ngozi nyeusi, wao daima wanaambatana wao kwa wao. "Sawa nimekuelewa Bosi wangu ondoa shaka nitawafikisha salama Inshallah..." alijibu Shebby huku ananyanyuka kotini kuelekea ofisini kwa mhasibu kupewa masurufu ya safari. "Shebiiiii...iko tahadharisha wewe jiepushe, kaa mbali na hao wanawake..tafadhali tapata tatizo bure" alisikika Bosi mkuu akimuasa vilivyo? kujitenga na kuwatamani hao wateja wake, Shebby akiwa wakati ameshafungua mlango wa kutokea nje. "Ondoa shaka Bosi wangu, rekodi zangu unazijua vizuri, sina uhusiano usiohusu kazi na mteja wangu" alimtoa mashaka Shebby, Bosi wake. "Sawa...mimi aminia wewe ndio maana chagua wewe, safari njema" Bosi akaridhishwa na majibu ya Shebby wakaagana. Ofisi ya uhasibu na ya Mkurugenzi mkuu zilikuwa pua na mdomo, milango yao inatazamana. Alipotoka tu akapiga hatua kama tano tu akafungua mlango wa ofisi ya uhasibu


ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog