Search This Blog

Monday 27 March 2023

LAITI NINGEJUA - 3

  


Simulizi : Laiti Ningejua

Sehemu Ya Tatu (3)



Nilimtazama kwa mshangao akiwa ameishika vyema bunduki yake aina ya sub machine gun huku misuli ya shingo na mikono yake ikiwa imetuna kwa ukomavu. Mwonekano wake ukanitanabaisha kuwa alikuwa ni mtu hatari sana na aliyependa matata.


Yule muuaji akaendelea kutembea kwa tahadhari akikikaribia kile kichaka na wakati huo yule mwenzake alikwenda moja kwa moja hadi kwenye siti ya mbele kushoto kwa dereva alipokuwa ameketi yule mzee wa makamo mwenye suti maridadi, nikamuona akichukua kitu kutoka kwenye mikono ya yule marehemu.



Yule muuaji aliyekuwa akisogea pale kwenye kichaka tulichokuwa tumejibanza mimi na yule mrembo alisimama ghafla, kama aliyekuwa amehisi kitu nikamuona akijaribu kunusa nusa kama mbwa mwindaji aliyejaribu kubaini windo lake lilipo.


Kuona vile hofu ikazidi kutambaa kwenye mwili wangu, ikabidi nimzibe macho yule msichana mrembo ili asije akaona kilichokuwa kikitokea, kwani bila kufanya vile angeweza hata kukurupuka ili kukimbia na hivyo kusababisha balaa zaidi.


Pamoja na kumziba yule mrembo lakini nilihisi ujasiri ulikuwa ukinipotea taratibu na moyo wangu ulizidi kupoteza utulivu na kijasho chepesi kilikuwa kikinitoka sehemu zote za mwili wangu.


Yule muuaji aliinua ile bunduki yake na kuelekeza pale kichakani tulipokuwa tumejificha mimi na yule mrembo, kisha nikamshuhudia akiikoki tayari kwa lolote.


Kuona vile nami nikafumba macho yangu huku nikipoteza kabisa matumaini ya kuokoka katika tukio lile, mara nikamsikia yule muuaji mwenzake aliyekuwa amesimama kule kwenye lile gari akimwitwa huku akimwambia kuwa walipaswa waondoke haraka kabla jambo baya halijatokea na hawakutakiwa kupoteza muda wao katika eneo lile.


Kitendo kile kikamfanya muuaji ambaye alikuwa tayari kufyatua risasi katika kile kichaka tulichokuwa tumejificha asite kufyatua risasi na badala yake akakitazama kile kichaka kwa makini kama vile mtu aliyehisi kitu fulani ndani ya kile kichaka.


Hata hivyo nilimuona akishusha pumzi huku akiminya midomo yake akionekana kuwa hakuwa na namna nyingine ya kufanya, alionekana kama aliyekuwa akijishauri kama aondoke au aendelee na dhamira yake, mara akashusha bunduki yake na kugeuza kurudi haraka kule kwa mwenzake.


Yule muuaji mwenzake muda ule alikuwa ameshika mkononi ile brifukesi ya yule mzee abiria aliyekuwa ameketi siti ya mbele kushoto kwa dereva. Nilishusha pumzi za ndani kwa ndani huku nikishuhudia gari la wale wauaji likianza kuondoka taratibu kutoka eneo lile huku wale wauaji wakilikimbilia na kurukia nyuma, kisha liliondoka kwa mwendo wa kasi kutoka eneo lile kama lilivyokuja.


Baada ya sekunde chache hali ya mahala pale ikawa ya ukimya mno uliotisha katika eneo lote. Kwa sekunde kadhaa nikiwa bado nimemziba uso yule msichana mrembo nilijikuta nikiduwaa huku nikishindwa kabisa kuamini kuwa tulikuwa tumesalimika na mkasa ule hatari ulioyakatisha maisha ya abiria wenzetu pamoja na dereva wa lile gari letu.


Niliweza kuyashuhudia mambo yote ambayo yalikuwa yametokea ndani ya muda wa dakika zisizozidi tano. Sasa tulikuwa tumebaki wawili tu katika eneo lile, mimi na yule msichana mrembo. Mara kukaibuka hali ya utulivu mkubwa sana katika ile barabara na eneo lile lote kwa ujumla.


Sauti pekee zilizokuwa zikisika katika eneo lile zilikuwa ni sauti za wadudu wa porini na kwa mbali niliweza kusikia sauti za mbwa waliokuwa wakibweka kutoka makazi ya watu walioishi katika vijiji vilivyokuwa jirani na eneo lile.


Kwa hali ile niliweza kugundua kuwa kumbe hatukuwa mbali na eneo la makazi ya watu pale porini. Hata hivyo, sikuthubutu kabisa kuinuka na kutoka pale kwenye kichaka tulipokuwa tumejibanza bali niliendelea kujibanza kwenye kile kichaka huku nikiwa nimemshika yule mrembo kwa muda usiopungua dakika ishirini, wote tukiwa hatuamini kama tulikuwa salama.


Nilimeza funda kubwa la mate na kumshukuru Mungu kimoyomoyo kwa kutuepusha na ile mitutu ya bunduki kutoka kwa wale wauaji. Tukiwa bado tupo pale pale kichakani nilimtazama kwa makini yule mrembo ambaye muda huo alikuwa amejikunyata kwa hofu huku akitetemeka.


Nilijikuta nikimhurumia sana, nikazidi kumkumbatia katika namna ya kumfariji, na mara nikamuona akijilaza kwenye kifua changu huku akinikumbatia kwa hofu, alikuwa analia kilio cha kwikwi akiwa bado anatetemeka.


Japokuwa tulikuwa kwenye taharuki la aina yake na hali yangu ilikuwa ikizidi kuwa mbaya kadiri sekunde zilivyokuwa zikiyoyoma lakini nilijikuta nikijisikia faraja kubwa sana kukumbatiwa na msichana mrembo kama yule.


Mwili wangu wote ulikuwa unauma sana kama kidonda, na mguu wangu wa kushoto ulikuwa umepinda kidogo na kuvimba na nilipojaribu kuuinua ulikuwa mzito mno mfano wa kipande kizito cha chuma.


Nilitamani kumwambia yule msichana mrembo jinsi nilivyokuwa nikijisikia muda ule ili atafute msaada lakini nilisita kumwambia chochote kwa kuhofia kuwa endapo angegundua kuwa hali yangu ilikuwa mbaya ningemuogopesha zaidi.


Nikiwa bado katika hali ile mara nikasikia muungurumo wa gari lililokuwa likija eneo lile likitokea kule nyuma tulipotoka. Sauti ya muungurumo ule uliashiria kuwa mwendo wa lile gari ulikuwa wa kasi mno kiasi cha kunitahadharisha kuwa mambo bado hayakuwa shwari.


Moyo wangu ukashikwa na mfadhaiko huku ukianza kwenda mbio isivyo kawaida. Kwa sekunde chache nilijikuta nikiyasahau maumivu yangu na jasho jepesi likaanza kunitoka sehemu mbalimbali za mwili wangu. Wakati huo yule msichana mrembo alikuwa akizidi kujigandamiza kwenye mwili wangu akionekana kuogopa sana.


Nikalishuhudia lile gari likikaribia kabisa eneo lile na kupunguza mwendo, kitendo cha kupunguza mwendo kikawafanya watu watatu waliokuwa wamevaa kombati za kiaskari waruke kutoka nyuma ya lile gari na urukaji wao ulionesha kuwa walikuwa tayari kukabiliana na jambo lolote la hatari huku wakiwa wameshika vyema bunduki zao tayari kwa lolote.


Mara nikaliona lile gari likiongeza tena mwendo wake na kutupita kwa kasi, na mara tu lilipotupita nikagundua kuwa lilikuwa ni gari aina ya Nissan Patrol la rangi nyeusi lililokuwa na maandishi makubwa ya ‘POLISI’ ubavuni na nyuma yake kulikuwa na askari wengine watatu ambao mikononi walikuwa wameshika bunduki zao.


Lilikwenda umbali wa takriban mita ishirini au therathini mbele yetu kisha nikaliona likipunguza tena mwendo wake. Na hapo askari wale wengine watatu waliokuwa kule nyuma wakaruka kutoka nyuma ya lile gari wakiwa tayari kukabiliana na jambo lolote la hatari huku wakiwa wameshika bunduki zao tayari kwa lolote.


Niliwatazama wale askari huku nikijikuta nikianza kupata matumaini mapya ya kuokolewa. Hata hivyo, maumivu makali ya mwili wangu na mguu wa kushoto yalizidi kunitesa na mguu wangu ulikuwa mzito mno kama uliokuwa umefungwa mzigo mzito nisioweza kuumudu.


Niliwatazama wale askari wakati wakitawanyika haraka katika eneo lile nikatamani kufungua mdomo wangu ili nipige yowe la kuomba msaada kutoka kwao lakini nilipofungua mdomo sauti ikagoma kabisa kutoka.



Mara nikaliona lile gari likiongeza tena mwendo wake na kutupita kwa kasi, na mara tu lilipotupita nikagundua kuwa lilikuwa ni gari aina ya Nissan Patrol la rangi nyeusi lililokuwa na maandishi makubwa ya ‘POLISI’ ubavuni na nyuma yake kulikuwa na askari wengine watatu ambao mikononi walikuwa wameshika bunduki zao.


Lilikwenda umbali wa takriban mita ishirini au therathini mbele yetu kisha nikaliona likipunguza tena mwendo wake. Na hapo askari wale wengine watatu waliokuwa kule nyuma wakaruka kutoka nyuma ya lile gari wakiwa tayari kukabiliana na jambo lolote la hatari huku wakiwa wameshika bunduki zao tayari kwa lolote.


Niliwatazama wale askari huku nikijikuta nikianza kupata matumaini mapya ya kuokolewa. Hata hivyo, maumivu makali ya mwili wangu na mguu wa kushoto yalizidi kunitesa na mguu wangu ulikuwa mzito mno kama uliokuwa umefungwa mzigo mzito nisioweza kuumudu.


Niliwatazama wale askari wakati wakitawanyika haraka katika eneo lile nikatamani kufungua mdomo wangu ili nipige yowe la kuomba msaada kutoka kwao lakini nilipofungua mdomo sauti ikagoma kabisa kutoka.


Endelea...


Sikuona sababu ya kuendelea kujificha pale kwenye kichaka, hivyo niliamua kuinuka na kuanza kupiga hatua kuwafuata wale askari lakini maumivu makali sana ya mwili na kwenye mguu wangu wa kushoto yalinifanya nishindwe kutimiza azma yangu. Niliishiwa nguvu mwilini na kuanguka chini huku nikipiga kichwa changu kwenye kisiki cha mti mkubwa uliokuwa umekatwa na kutoa yowe dogo kwa sauti dhaifu.


Sasa moyo wangu ulikuwa unakwenda mbio isivyo kawaida na uliunguruma sana kama uliokuwa ukipambana na kazi isiyo ya kiasi chake, macho yangu nayo taratibu yakaanza kupoteza nguvu ya kuona. Hatimaye shughuli mbalimbali za mwili wangu nazo nikazihisi kuwa zilikuwa mbioni kusitisha utendaji wake.


Yule msichana mrembo alisimama akaniangalia kwa wasiwasi mkubwa, hakuweza kuvumilia akapiga kelele kubwa za hofu kuomba msaada. Muda ule ule nikasikia sauti za vishindo vya miguu za wale askari waliokuwa wakija mbio katika eneo lile tulilokuwepo.


Kufumba na kufumbua lile eneo lote likawa limezingirwa na wale askari wenye silaha. Muda huo nikatamani sana kuinuka au kufumbua macho yangu ili nione ni nini kilichokuwa kinaendelea katika eneo lile, na ikibidi kuongea nao ili niwaelezee kuhusu mkasa mzima ulivyokuwa lakini hilo halikuwezekana kabisa, kwani macho yangu yalizidi kuwa mazito sana.


Nikiwa bado nipo pale chini nikiwa sijielewi vizuri mara kwa mbali nikawa nasikia sauti za wale askari wakijaribu kumuuliza yule msichana mrembo kuhusu kilichotokea, lakini yule mrembo muda wote alikuwa analia kwa uchungu.


Nikataka nijiinue na kusimama lakini sikuweza, nikajikakamua kuinua lakini sikuweza na mara nikahisi fahamu zangu zilikuwa zikinitoka taratibu. Muda mfupi uliofuatia baadaye sikuweza tena kufahamu ni nini kilichoendelea pale.


Muda ule ule nilianza kujiona nikitumbukia kwa kasi ya ajabu kwenye shimo refu sana lilikokuwa na kiza kilichotisha. Kabla sijafika chini kuna ndege mkubwa alininyakua na kuanza kupaa juu kwa kasi ile ile ya ajabu hadi tulipotoka ndani ya lile shimo.


Na mara giza zito likatanda kwenye mboni zangu za macho huku taratibu nguvu zikianza kuniishia na mwili wangu ukilegea, mapigo yangu ya moyo nayo yakaanza kudorora, hata hivyo yule ndege alizidi kwenda juu zaidi na kuzifanya pumzi zangu zipae na kunifanya kuhema kwa shida. Nilijaribu kupiga kelele za kuomba msaada lakini sauti yangu ilikuwa haitoki na badala yake niliisikia ikitengenezwa mwangwi ndani ya kichwa changu.


_______


Nilikuja kuzinduka siku ya pili yake asubuhi na kujikuta nikiwa nimelala kitandani kwenye foronya laini na mto wa kuegemeza kichwa. Muda ule nilikuwa nimerudiwa na fahamu zangu, na hisia zangu zilinitanabaisha hivyo huku picha nzima ya tukio la mauaji kule porini Kibiti nikilikumbuka vizuri.


Nilipozinduka niliyazungusha macho yangu kutazama huku na kule na kugundua kuwa nilikuwa nipo hospitalini, sikuweza kufahamu nini kilikuwa kimenitokea wakati nilipoanguka na kupoteza fahamu zangu kule porini Kibiti tulipokuwa tumebaki wawili tu, mimi na yule mrembo ambaye hadi wakati huo sikuwa na taarifa zake na wala sikujua alikuwa wapi na nini kilimpata.


Hata hivyo, nilipiga moyo konde na kumshukuru Mungu kwa kuniokoa kutoka katika tukio lile la kutisha, nilijua kuwa aliniokoa na kuniweka hai hadi wakati ule kwa kuwa alikuwa na kusudi maalumu juu yangu, hivyo kitu muhimu kwangu kwa wakati huo ilikuwa ni kumshukuru yeye tu na mambo mengine nisiyoyajua hayakuwa na uzito kwa muda ule, kwani ningekuja kuyafahamu baadaye.


Nikayatembeza tena macho yangu huku na kule katika kutathmini vizuri mandhari ya mle ndani. Niliwaona vijana kadhaa waliokuwa wamelazwa wakiwa na majeraha mbalimbali kwenye miili yao na wengine miguu yao ilikuwa imetundikwa juu kwenye vyuma.


Jambo lile likanishtua kidogo na hapo nikagundua kuwa nilikuwa nimelazwa kwenye Taasisi ya Mifupa ya Muhimbili (MOI) ingawa sikujua nilifikaje pale Muhimbili!


Jambo lile likanifanya nitake kujua kwa nini nilikuwa nimelazwa kwenye Taasisi ya Mifupa Muhimbili (MOI) na si mahala pengine! Nikajaribu kujiinua pale kitandani lakini kichwa changu kilikuwa kizito mno, na nilihisi kizunguzungu na mwili wangu ulikuwa umechoka sana mithili ya mlevi aliyeamka na uchovu wa pombe baada ya kulewa sana jana yake.


Nilitulia kidogo huku nikishusha pumzi zangu kwa nguvu kisha nikataka niinuke tena ili nikae, nilipojivuta nikauhisi mguu wangu wa kushoto ulikuwa mzito sana kama kipande cha chuma na uliambatana na maumivu makali.


Hapo nikashawishika kufunua shuka nililokuwa nimefunikwa na kuutazama kwa makini ule mguu na ndipo nilipogundua kuwa ulikuwa umefungwa bandeji ngumu (P.O.P.), nikashtuka sana.


Nikiwa pale kitandani nikajikuta nikianza kukumbuka jinsi nilivyoanza kuhisi maumivu ya mguu yalivyokuwa makali wakati niliporuka kutoka kwenye lile gari tulilokuwa tumeopanda huku nikiwa nimembeba yule mrembo na kuangukia kwenye shimo.


Nikakumbuka picha nzima hadi pale nilipoinuka baada ya kuwaona polisi wa Kibiti wakilizingira eneo lile na mimi kuinuka lakini nikaanguka na kupiga kichwa changu kwenye mti, kabla sijapoteza fahamu zangu huku yule mrembo namna aliyekuwa ameziteka hisia zangu alipopiga kelele za hofu.


Nilipomkumbuka yule msichana mrembo nikahisi maumivu ya mwili wangu yakipungua, na sasa hamu ya kutaka kufahamu ni wapi alikokuwa yule mrembo na mambo mengi yaliyotokea baada ya mimi kupoteza fahamu. Hata hivyo, sikuwa na mtu wa kumuuliza maswali yale kwani katika ile wodi sikumuona mtu yeyote niliyedhani angeweza kufahamu kile kilichonitokea, japo hata kunijuza nilikuwa nimefikaje pale hospitali.


Hata hivyo, niliamini kuwa kwa vyovyote yule mrembo aliniokoa akishirikiana na wale polisi wa Kibiti, niliamini kuwa ni yeye aliyetoa maelezo kuhusu tukio lile la kutisha, ni yeye aliyesaidia kunifikisha pale hospitali na ndiye angeweza kunieleza vizuri nini kilichokuwa kimenitokea wakati nilipokuwa nimepoteza fahamu.


Lakini sikujua alikuwa wapi muda ule na sikuwa na namna nyingine yoyote ya kupata majibu isipokua kuvuta subira.


Nikiwa pale kitandani nikaendelea kuyatembeza macho yangu mle wodini taratibu huku nikiwatazama kwa makini wagonjwa wengine waliokuwa wamelazwa.


Wakati nikiwa bado nawatazama wale wagonjwa nikashtushwa na sauti ya upole kutoka kwa Muuguzi wa ile wodi aliyekuwa amesimama kwenye kitanda changu akiwa amebeba trei ndogo iliyokuwa na dawa mbalimbali za sindano, vidonge, bilauri ya maji na faili.


“Mr. Ibrahim, unajisikiaje sasa?” Aliniuliza yule muuguzi huku akiachia tabasamu pana usoni kwake.





Wakati nikiwa bado nawatazama wale wagonjwa nikashtushwa na sauti ya upole kutoka kwa Muuguzi wa ile wodi aliyekuwa amesimama kwenye kitanda changu akiwa amebeba trei ndogo iliyokuwa na dawa mbalimbali za sindano, vidonge, bilauri ya maji na faili.


“Mr. Ibrahim, unajisikiaje sasa?” Aliniuliza yule muuguzi huku akiachia tabasamu pana usoni kwake.


“Ah, kwa kweli hata sielewi, nahisi kizunguzungu na mwili wangu umechoka sana kama niliyeamka na hangover,” nilimwambia huku nikipeleka mkono wangu kichwani.


“Usijali, utapona… nilikuona ulipozinduka nikaona nikukuletee hivi vidonge vya kutuliza maumivu, ukimeza utapata nafuu kabisa,” aliniambia yule muuguzi kisha akanipa ile bilauri ya maji na vile vidonge vya kutuliza maumivu.


Bila kupoteza muda nilivitupia vile vidonge mdomoni na kugida mafunda kadhaa ya maji yaliyokuwa kwenye ile bilauri nikivisukumia ndani vidonge vile. Nilipoitoa ile bilauri mdomoni ilikuwa tupu, nikamrudishia yule muuguzi ile bilauri, naye aliipokea kutoka mikononi mwangu na kuachia tabasamu pana la kunifariji, “Pole sana, kaka…”


Nilibetua kichwa changu huku nikifumba macho yangu na kukunja sura wakati vidonge vile vya kuondoa maumivu vilivyokuwa na ladha mbaya vilipokuwa vikisafiri kwenda tumboni kupitia kwenye koo langu. Nilivisikia vikitua kwenye mfuko wa chakula, nikafumbua macho yangu na kutabasamu huku nikimtazama yule muuguzi kwa utulivu.


Nilimuona yule muuguzi akiweka rekodi sahihi kwenye lile faili alilokuja nalo kisha akaanza kupiga hatua taratibu akiondoka, sikutaka aondoke bila kunitegulia kitendawili changu.


“Samahani, dada, hivi ni nani aliyenileta hapa hospitali?” nilimuuliza yule muuguzi kwa sauti tulivu, nikamuona akigeuza shingo yake na kunitazama kwa makini kwa kitambo fulani.


“Sifahamu kwa kuwa mimi sikuwepo wakati ukiletwa, lakini nimeambiwa kwamba uliletwa hapa na polisi wa Kibiti,” aliniambia yule muuguzi huku akinitazama kwa utulivu.


“Walikuwa Polisi peke yao au waliambatana na msichana fulani hivi?” niliuliza kwa shauku nikitaka kujua kama yule msichana mrembo alifika pale hospitali akiongozana na wale polisi.


“Kama nilivyokwambia, sina jibu la kukupa kwa kuwa nimeingia zamu asubuhi hii hii na taarifa pekee kuhusu wewe niliyopewa ni ya kitabibu zaidi,” aliniambia yule muuguzi huku akitaka kuondoka.


“Halafu… samahani, hivi umejuaje jina langu?” nilimuuliza tena lakini nikamuona akinitazama kwa mshangao kana kwamba nilikuwa kichekesho, kwani nilikuwa nauliza swali ambalo jibu lake lilikuwa wazi kabisa.


“Hilo ni jina ambalo lipo kwenye faili lako, ni Polisi ndio waliosema kuwa unaitwa Bilali Ibrahim… kwani si jina lako?” aliniuliza yule muuguzi huku akiendelea kunitazama kwa mshangao.


“Ni jina langu, lakini…” nilisema lakini nikasita baada ya kugundua kuwa huenda polisi walikuwa wameliona jina kwenye vitambulisho vyangu ambavyo nilikuwa na kawaida ya kutembea navyo, na siku ile nilikuwa navyo kwenye mfuko wa suruali yangu.


Yule muuguzi alinitazama kwa makini kwa kitambo kidogo kisha nikamuona akishusha pumziz na kuondoka zake, akaelekea kwenye kitanda kingine akiendelea kugawa dawa kwa wagonjwa wengine.


Mara tu yule muuguzi alipoondoka nikaupisha utulivu kichwani mwangu huku nikigeuza tena shingo yangu kutazama huku na kule. Nilipoitazama saa yangu ya mkononi nikagundua kuwa ilikuwa ikielekea kutimia saa sita ya mchana na hapo fikra zangu zikahamia kutafakari juu ya jamaa zangu.


Sikujua kama jamaa zangu walikuwa wanazo taarifa kuhusu mkasa ule uliokuwa umenitokea kule porini Kibiti, hata hivyo, nilimuomba Mungu anipe unafuu haraka ili nitoke pale hospitali na kuendelee na harakati zangu za kuisaka shilingi.


Neno shilingi liliponijia tu akilini kwangu nikajikuta nikimkumbuka Yeriko, na hapo moyo wangu ukapiga kite. Sikujua Yeriko alikuwa wapi muda ule na sikujua kama alikuwa amekwisha pata taarifa kuhusu yale mauaji kule porini Kibiti. Pia sikujua simu yangu ilikuwa wapi, na kama alinitafuta kwenye simu.


______


Sikuweza kufahamu ni wakati gani nilipitiwa na usingizi ulioziteka fikra zangu pale kitandani wakati nilipokuwa nikiendelea kuwaza hili na lile, nilikuja kushtuka kutoka usingizini baada ya kuhisi mkono ukinigusa kwenye paji langu la uso.


Hivyo nikafumbua macho yangu na kugeuza taratibu shingo yangu huku nikitabasamu na kuyapeleka macho yangu kumtazama yule mtu aliyekuwa amenigusa kwenye paji langu la uso, akilini kwangu nilitarajia kumuona yule msichana mrembo niliyekuwa naye safarini kule Kibiti wakati tukivamiwa na wale wauaji.


Hata hivyo, hilo halikutokea na badala yake mbele yangu nilijikuta nikikabiliana na wanaume watatu waliokuwa wamesimama huku wakinitazama kwa makini. Wanaume wawili niliwatambua mara moja kuwa walikuwa ni Polisi kutokana na mavazi yao.


Kati yao, mmoja alikuwa na cheo cha Inspekta wa Polisi kutokana na alama mbili za nyota zilizokuwa kwenye mabega yake na yule mwingine alikuwa na cheo cha Koplo kutokana na alama ya “V” mbili.


Yule mwanamume wa tatu alikuwa ni daktari kutokana na mwonekano wa mavazi yake, kwani alikuwa amevaa shati la samawati, suruali ya bluu na koti refu jeupe juu ya shati, na alikuwa amening’iniza kifaa cheusi cha kupimia mapigo ya moyo kilichoitwa ‘Sphygmomanometer’ shingoni kwake.


“Vipi Bilali, unajisikiaje?” yule daktari aliniuliza huku akiendelea kunigusa kwenye paji la uso wangu kwa kiganja chake cha mkono.


“Nasikia maumivu makali ya mguu na kichwa changu ni kizito, halafu nina njaa,” nilisema kwa utulivu huku nikimtazama yule daktari kisha macho yangu yakahamia kwa wale maofisa wa polisi ambao muda wote walikuwa kimya wakinitazama kwa makini.


“Usijali utaletewa chakula muda si mrefu, sijui ungependelea kula chakula gani?” aliniuliza yule daktari huku akigeuza shingo yake kuwatazama wale maofisa wa polisi aliokuwa ameongozana nao.


“Chakula chochote kinachoweza kunipa nguvu, lakini kisiwe chakula kigumu,” nilisema kwa sauti tulivu huku nikifumba macho yangu.


“Okay! Hata hivyo, hawa maofisa wamekuja kukujulia hali ila kwa sasa unatakiwa kupumzika ila ukipata nafuu kidogo watahitaji kupata maelezo yako,” alisema yule daktari kwa utulivu huku akigeuka kumtazama yule Inspekta wa Polisi.


“Ni kweli, na usihofu chochote kwani hapa uko kwenye mikono salama,” alidakia yule Inspekta wa Polisi huku akiachia tabasamu la kunifariji.


“Nashukuru sana afande, lakini… mna taarifa zozote kuhusu wauaji?” nilimuuliza yule Inspekta wa Polisi kwa shauku kutaka kujua, ingawa ukweli nilihitaji sana kupata taarifa za yule msichana mrembo.


“Upelelezi bado unaendelea, tayari tumekwishapata maelezo ya awali kutoka kwa watu watatu walioshuhudia tukio lile na sisi tunajaribu kuangalia sababu za mauaji yale, maana kuna viashiria vya ulipizaji kisasi…” alisema yule ofisa wa polisi huku akishusha pumzi.


“Lakini tusingependa kuchosha sasa hivi, na kama ambavyo daktari ameshauri pumzika kwanza, kila kitu kitakuwa sawa, na tayari tumekwisha toa taarifa kwa jamaa zako ambao namba zao za simu tulizipata kutoka kwenye simu yako tuliyoiokota kwenye eneo la tukio. Daktari atakukabidhi baadaye,” yule ofisa wa polisi aliniambia huku akiachia tabasamu.




“Lakini tusingependa kuchosha sasa hivi, na kama ambavyo daktari ameshauri pumzika kwanza, kila kitu kitakuwa sawa, na tayari tumekwisha toa taarifa kwa jamaa zako ambao namba zao za simu tulizipata kutoka kwenye simu yako tuliyoiokota kwenye eneo la tukio. Daktari atakukabidhi baadaye,” yule ofisa wa polisi aliniambia huku akiachia tabasamu.


“Nashukuru sana, afande, hivi ni watu wangapi waliokufa katika tukio lile?” nilimuuliza yule ofisa wa polisi.


“Kwa taarifa tulizonazo ni watu sita ndio waliokufa,” aliniambia yule ofisa wa polisi.


Maelezo yale ya ofisa wa polisi yakanifanya nivute kumbukumbu zangu kujaribu kukumbuka kilichotokea katika lile tukio: nikakumbuka kumuona dereva wa lile gari akipiga yowe dogo na kuangukia usukani akiwa mfu, kisha yule abiria mtu wa makamo aliyekuwa ameketi kushoto kwa dereva.


Nikakumbuka kumshuhudia abiria mmoja aliyekuwa ameketi nyuma ya yule abiria mtu wa makamo, ambaye risasi zilipenya kutoka kwa abiria wa mbele na kumuingia kisha akafa papo hapo… halafu ilipotokea taharuki na abiria kuanza kukimbia ovyo, risasi zilizopigwa ziliwaua watu wengine watatu. Hivyo kufanya idadi ya waliokufa kufikia watu sita!


Dah, habari ile ikasababisha jasho jepesi lianze kunitoka mwilini huku nikihisi msisimko fulani wa hofu ya aina yake ukinitambaa mwilini! Wale maofisaz wa polisi waliniangalia kwa makini na kuangaliana, kisha wanageuka na kuanza kuondoka.


“Afande, naomba kujua jambo moja… kwani yule msichana niliyekuwa naye kule Kibiti wakati mauaji yanatokea yuko wapi?” nilimuuliza yule ofisa wa polisi nilipoona anaanza kuondoka.


“Ooh, yule alikuja kuchukuliwa na mzazi wake mara baada ya kufika hapa Dar es Salaam na yeye kutoa maelezo yake kwa polisi, kwani vipi?” yule ofisa wa polisi alinijibu huku akinitazama kwa udadisi zaidi.


“Aah… nilitaka tu kujua kama yu salama maana sina taarifa zozote na wala sijui anaendeleaje,” nilijibu kwa sauti ya utulivu.


“By the way, begi lako lipo limehifadhiwa mahala salama, yule msichana ndiye aliyetuonesha mzigo wako, utamwambia muuguzi akupatie wakati wowote utakapouhitaji,” alisema yule daktari na kugeuka kuwatazama wale maofisa wa polisi na kuwapa ishara ya kuondoka.


Niliwatazama kwa makini nikataka kuendelea kuuliza maswali kuhusu taarifa za yule msichana mrembo niliyekuwa naye kule Kibiti lakini nikasita kwa kuogopa kuwa wale maofisa wa polisi wangeweza kunifikiria vibaya, hivyo nikaamua kukaa kimya.


Nikawaona wakiondoka na kuniacha nikiwa nimenyong’onyea sana kwa kuwa hadi wakati ule sikuwa na taarifa zozote kumhusu yule msichana mrembo, ambaye hata jina lake sikuwa nalijua ingawa moyoni mwangu niliamua kumpachika jina la ‘the most wanted’.


Lakini pamoja na kutokufahamu mahali alipokuwa nilimshukuru Mungu baada ya kujua kuwa alikuwa salama akiwa na familia yake. Pia nilijisikia fahari kujua kuwa ni yeye aliyewaonesha maofisa wa polisi begi langu na simu yangu, hivyo nikaamini kuwa kwa namna fulani alikuwa ameguswa.


Dakika chache tu tangu walipoondoka wale maofisa wa polisi na yule daktari nikamuona muuguzi wa ile wodi akija moja kwa moja pale kitandani nilipokuwa nimelala akiwa amebeba begi langu dogo nililokuwa nalo siku ya tukio pamoja na simu yangu.


Pia alikuwa amebeba hotpot kubwa lililokuwa na maakuli, sahani, kijiko kikubwa cha kupakulia na kingine cha chakula, bilauri pamoja na chupa kubwa ya maji safi ya kunywa.


Niliipokea ile simu yangu kwa hamu na kujaribu kuangalia simu zilizokuwa zimepigwa lakini nikagundua kuwa ilikuwa imezimwa, nilipojaribu kuiwasha yule muuguzi aliniambia kuwa haikuwa na chaji.


Niliamua kumuomba anisaidie kuichaji ili baadaye niwasiliane na jamaa muhimu walioko nje ya nchi, akiwemo kaka yangu, ambao sikuwa na uhakika kama walikwisha pata zile taarifa.


Yule muuguzi aliipokea ile simu huku akinikaribisha chakula, kisha alilifungua lile hotpot lililokuwa na chakula. Niliinua kidogo shingo yangu kuchungulia dani ya lile hotpot nikaona mchemsho wa kuku wa kienyeji uliochanganywa na ndizi za Bukoba.


Kwa kuwa nilikuwa na njaa sana niliufakamia ule msosi bila kujali maumivu ya mwili na mguu niliyokuwa nayo. Niliposhiba nilianza kuwaza hili na lile kuhusu lile tukio la mauaji kule Kibiti huku nikijiambia kwamba ni wakati sasa niache kuzipuuza hisia zangu pale ambapo ningehisi kulikuwa na jambo baya.


Mara ikanijia tena sura ya yule msichana mrembo niliyemuokoa kule porini Kibiti wakati mauaji yanatokea. Nilitamani sana kujua alikuwa wapi muda ule na alikuwa na nani?


Nilitamani kujua alikuwa akifanya nini na kama alifahamu kuwa nililazwa pale Taasisi ya Mifupa Muhimbili. Nilitamani sana angekuja kuniona, hata hivyo, sikuwa na lolote la kufanya isipokuwa kusubiri majaaliwa ya Mungu.


Nikiwa pale kitandani fikra zangu ziliendelea kusumbuliwa na yule msichana mrembo ‘the most wanted’, niliwaza endapo angetokea pale hospitali kuja kuniona ningeweza kupona saa ile ile.


Wakati nikiwa bado nimezama kwenye tafakari ile mara nikashtuka baada ya kuhisi kulikuwa sauti ambazyo nilizifahamu zilizokuwa zikilitaja jina langu.


Niligeuza shingo yangu kutazama upande ule ambao sauti zile zilikuwa zikitokea na kuwaona watu watatu wakielekezwa na muuguzi wa ile wodi mahali nilipokuwa nimelala, kisha nikawaona wakija eneo lile nilipokuwa nimelala huku wakiangaza macho yao kwa makini kutazama kule nilikokuwa lakini wakiwa na nyuso zilizoonesha huzuni.


Nilipowatazama vizuri nikawatambu, walikuwa ni Jonas, Yeriko na Zubeda na walikuwa wamekuja kunijulia hali.


Yeriko alikuwa mfupi mwenye sura ya ucheshi muda wote na umbo la kawaida. Alikuwa na umri uliokaribia miaka arobaini na alivaa suti nadhifu ya rangi ya kijivu ya single button na shati jeupe ndani aina ya Levi’s lililokuwa limemkaa vyema na kumpendeza.


Jonas pia alikuwa mfupi lakini mnene mwenye misuli imara ya mikononi iliyotuna kikamilifu kwa namna iliyoonesha kuwa alikuwa akifanya mazoezi ya nguvu yasiyokuwa na kikomo.


Alikuwa na miaka therathini na tano na alivaa t-shirt nyekundu iliyombana na kulionesha vyema umbo lake lililojengeka kwa misuli na alivaa suruali ya jeans ya rangi ya bluu na buti ngumu za rangi nyeusi.


Kichwani alivaa kofia aina ya kapelo ya rangi nyekundu iliyokuwa imetuama vizuri kwenye kichwa chake cha mviringo kisicho na kisogo.


Zubeda alikuwa mwanadada wa umri wa miaka therathini na ushee na alikuwa mpangaji kwenye nyumba yetu, alikuwa mnene wa wastani, hakuwa mfupi wala mrefu bali alikuwa na kimo cha wastani na rangi ya maji ya kunde.


Alikuwa amevaa gauni fupi la kitenge lililoshonwa mtindo wa pencil dress na kumkaa vizuri mwilini likiuchora vyema mwili wake matata wenye umbo la kuvutia, kichwani alikuwa na nywele nyingi mfano wa mmanga, zilizosukwa kwa mtindo wa mkia wa pweza na kumwagika mgongoni.


Miguuni alikuwa amevaa sandozi ngumu za ngozi zilizokuwa zimeshikiliwa kwenye miguu yake mizuri kwa kamba.


Niliwatazama kwa makini walipokuwa wakizitupa hatua zao taratibu kusogea pale kitandani kwangu, na mara wakaniona na kuharakisha kuja pale kitandani.



“Mungu wangu, Bilali, kumbe ni kweli jambo hili limekutokea?” Jonas aliniuliza huku akinitazamana kwa mshangao. Zubeda alibaki kimya akinitazama kwa huzuni, macho yake yalikuwa yakilengwa lengwa na machozi.


“Nilipopigiwa simu na mtu aliyejitambulisha kuwa ni polisi, jambo la kwanza kujiuliza lilikuwa leo ni tarehe ngapi, maana nilidhani ni siku ya wajinga, baadaye Yeriko naye akanipigia simu kuwa amepigiwa na hao hao polisi,” aliongeza Jonas huku akiachia kicheko hafifu.


“Ndo hivyo kama mlivyoambiwa, ilikuwa hatari sana, ni bora usimuliwe tu,” niliwaambia huku nikiminya sura yangu kwa maumivu.


“Pole sana, kwani ilikuwaje hasa?” Yeriko alidakia kwa sauti ya chini huku akinitazama kwa mshangao na kuketi kando ya kitanda nilichokuwa nimelala.


“Ni hadithi ndefu…” nilimjibu Yeriko huku nikishusha pumzi za ndani kwa ndani.


Zubeda alishindwa kujizuia alisogea pale kitandani nilipokuwa nimelala na kunikumbatia kwa huzuni huku akishindwa kuyazuia machozi yake yaliyoanza kumtoka. Alinikumbatia huku akilia kilio cha kwikwi.


Hali ile ikanifanya nami nihisi uchungu mkubwa moyoni mwangu na kuanza kulengwa na machozi. Tuliendelea kukumbatiana kwa kitambo kirefu huku kila mmoja akionesha hisia za furaha na majonzi wakati huo huo kwa mwenzake.


Kisha Zubeda aliniachia na kusogea kando huku akinitazama kwa makini, aliendelea kunitazama akiwa kimya, tukatazamana usoni kwa kitambo huku kila mmoja akiendelea kutokwa machozi. Kwa kweli Zubeba alikuwa kama dada yangu wa tumbo moja na tulikuwa tukipatana sana.


“Kweli Mungu mkubwa, kaka Bilali, siamini macho yangu!” hatimaye Zubeba alisema, hata hivyo, uso wake ulishindwa kuficha huzuni aliyokuwa nayo na alikuwa akiendelea kutokwa na machozi.


“Ni kweli Mungu mkubwa, da’ Zubeda, huwezi kuamini kuwa nimeponea kwenye tundu la sindano,” nilimwambia Zubeda kwa furaha huku nikimtazama kwa makini.


Kisha tuliongea kwa kirefu kidogo, nikagundua kuwa kabla ya kupewa taarifa na polisi walikuwa wamesikia kuhusu za tukio lile la mauaji kule porini Kibiti kupitia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii.


Katika maongezi yetu pia niliweza kugundua kuwa nilikuwa nimelazwa katika wodi namba kumi na saba ya jengo la Sewa Haji pale Taasisi ya Mifupa Muhimbili.


Ilipotimia siku ya tatu tangu nilazwe pale Taasisi ya Mifupa Muhimbili Adnan na mke wake Ada walikuja kunitembelea. Walioneshwa kuguswa sana na lile tukio la mauaji ya watu sita kule Kibiti. Ada alinipa mfuko mweusi wa plastiki aliokuwa ameubeba, nilipoufungua nikakuta kulikuwa na matunda na juisi.


Adnan alinifikishia salamu kutoka kwa mama yake na kunieleza jinsi alivyoshtushwa na taarifa zile, kisha akasema kuwa wote walikuwa wakiniombea ili nipone haraka na niendelee na majukumu yangu kama kawaida.


Tuliongea mengi na muda wote wa maongezi yetu nilitamani sana kusikia habari za Jameela lakini haikuwa hivyo, Adnan hakutaja kabisa jina hilo na wala mimi sikumuuliza kwa kuwa niliogopa. Muda wa kutazama wagonjwa ulipokwisha Adnan na mkewe Ada waliniaga na kuondoka zao lakini waliahidi kuwa wangetafuta tena muda na siku nyingine ya kuja kunitembelea.


Kisha zilipita siku nyingine tatu tangu siku ambayo Adnan na mkewe Ada walipokuja hospitali kunitembelea, siku hii wale maofisa wa polisi walikuja tena na safari ile ya pili walikuwa wamekuja kuchukua maelezo yangu kuhusu kile nilichokifahamu juu ya lile sakata la mauaji kule Kibiti.


Waliniuliza maswali mengi huku wakiandika yale maelezo niliyokuwa nikiyatoa, nami nilielezea kila kitu nilichokumbuka, kuanzia nilivyoliona lile gari aina ya Toyota Land Cruiser Pick-up kule katika kituo cha kujazia mafuta cha Gapco Kibiti.


Nikawaleza kuhusu yule mwanamume alivyoshushwa pale kwenye kile kituo cha kujazia mafuta, jinsi nilivyopatwa na hisia mbaya juu yake pale alipokuja pale kwenye gari letu na kuonekana kama aliyekuwa anatuchunguza abiria tuliokuwa mle ndani ya gari. Jinsi tulivyolipita lile gari likiwa limeegeshwa kando ya barabara huku boneti la gari likiwa wazi, hadi walivyotufuata na kutuzuia kwa mbele.


Kisha nikaeleza nilivyouona mchezo mzima jinsi dereva wetu alipoamua kurudi nyuma na hapo ndipo mvua ya risasi ilipoanza kutunyeshea. Nikaendelea kueleza jinsi nilivyomuokoa yule binti mrembo, hadi walipofika polisi kisha nikapoteza fahamu…


Wale maofisa wa polisi waliandika maelezo yangu yote na kunishukuru sana wakionekana kuridhika, kisha waliniaga lakini kabla hawajaondoka niliwauliza nikitaka kujua kuhusu walipofikia kwenye upelelezi wao.


Yule Inspekta wa Polisi aliniambia kuwa walikuwa wamefanikiwa kuwakamata watu watatu na lile gari Toyota Land Cruiser Pick-up lililokuwa limetumika kwenye lile tukio lilikuwa linashikiliwa kituo cha polisi, baada ya watu kulitambua.


Pia waliniambia kwamba walikuwa bado wanaendelea na msako mkali wa kuwatafuta wahusika wengine amabao waliamini kuwa wamekimbilia Lindi au Mtwara.


“Hata hivyo, hatuwezi kusema zaidi jinsi tunavyopata taarifa zetu kwa sababu ni mambo ya ndani sana ya kiuchunguzi na kutokana na matukio yenyewe kuwa nyeti sana. Lakini pia tumegundua kuna ajenda fulani nyuma ya mauaji haya,” aliniambia yule Inspekta wa Polisi.


“Kwa kifupi, tunataka kila shambulio la umwagaji damu ya mtu yeyote uchunguzi wake uwe ni mkubwa zaidi kuliko matukio mengine tunayoyafanya kikawaida,” aliongeza yule ofisa wa polisi.


Nilibetua kichwa changu kukubaliana nao bila kuongeza neno lolote, nilishusha pumzi za ndani kwa ndani huku nikiegemeza kichwa changu vizuri kwenye mto. Wale maofisa wa polisi waliniaga na kuondoka zao. Nilipobaki peke yangu nikajikuta nikianza kumuwaza tena yule ‘the most wanted’ wangu. Kilichonisikitisha zaidi ni kwamba muda wote tangu nilipolazwa pale hospitali sikuwahi kumtia machoni hata siku moja, ingawa nilikuwa nimejitolea maisha yangu kumuokoa katika tukio lile baya la mauaji lakini alionekana kunisahau kabisa.


Nikiwa bado natafakari mara nikamuona Adnan akija upande ule niliokuwa nimelala, lakini safari hii hakuwa ameambatana na mtu mwingine bali alikuwa peke yake na alionekana kama mtu aliyekuwa na haraka.





“Kwa kifupi, tunataka kila shambulio la umwagaji damu ya mtu yeyote uchunguzi wake uwe ni mkubwa zaidi kuliko matukio mengine tunayoyafanya kikawaida,” aliongeza yule ofisa wa polisi.


Nilibetua kichwa changu kukubaliana nao bila kuongeza neno lolote, nilishusha pumzi za ndani kwa ndani huku nikiegemeza kichwa changu vizuri kwenye mto. Wale maofisa wa polisi waliniaga na kuondoka zao. Nilipobaki peke yangu nikajikuta nikianza kumuwaza tena yule ‘the most wanted’ wangu. Kilichonisikitisha zaidi ni kwamba muda wote tangu nilipolazwa pale hospitali sikuwahi kumtia machoni hata siku moja, ingawa nilikuwa nimejitolea maisha yangu kumuokoa katika tukio lile baya la mauaji lakini alionekana kunisahau kabisa.


Nikiwa bado natafakari mara nikamuona Adnan akija upande ule niliokuwa nimelala, lakini safari hii hakuwa ameambatana na mtu mwingine bali alikuwa peke yake na alionekana kama mtu aliyekuwa na haraka.


Endelea...


“Ooh, Adnan, habari za Kibiti?” nilimsalimia Adnan baada tu ya kuketi juu ya kitanda changu.


“Kibiti kwema kabisa, na wala hakuna jipya,” alisema Adnan huku akishusha pumzi ndefu.


Nilitabasamu lakini sikuongeza neno. Kisha kilipita kitambo kifupi cha ukimya, kila mmoja wetu alionekana kutafakari.


“Vipi kwa sasa, unaendeleaje?” Adnan alivunja ukimya huku akinitazama kwa makini.


“Naendelea vizuri, hata yale maumivu makali ya mwili na mguu yamepungua kidogo tofauti na ulivyonikuta mara ya kwanza ulipokuja, nadhani ukija tena safari nyingine utakuta nimesharuhusiwa kurudi nyumbani,” nilimwambia Adnan huku nikijiweka sawa pale kitandani.


Adnan aliachia tabasamu na kuinuka kutoka pale kitandani, alisimama akanitazama kwa makini huku akivuta pumzi ndefu kisha akazishusha taratibu.


“Leo mimi si mkaaji sana, nimekuja mara moja tu kukuona, nakwenda ofisi za uhamiaji kushughulikia hati zangu za kusafiria na kama Mungu akinijaalia basi nitasafiri kwenda Uarabuni,” alisema Adnan huku akipiga mwayo.


Sikuwa na cha kuongea bali nilimtazama tu Adnan. Kikapita tena kitambo kirefu cha ukimya tukiwa tumetazamana.

ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog