Search This Blog

Thursday 23 March 2023

MSAKO - 5

  

Simulizi : Msako

Sehemu Ya : Tano (5)


“Janga jingine lililoongezeka jana ni kuibiwa kwa kisanduku cheusi kilichokuwa kwenye ndege iliyoanguka wiki na siku kadhaa zilizopita sasa. Hii inaamanisha idara nzima ya usalama iko gizani na haina usukani wa kile kinachoendelea sasa katika vita hii ambayo wengi wanaihusisha na hujuma dhidi ya kupatikana kwa gesi hapa nchini. Ambapo nchi kadhaa za kiarabu zinataka kushika soko ndani ya wiki au miezi michache ijayo hivyo wameona kuchelewesha Tanzania kuingia sokoni na pia kuyafanya makampuni ya Magharibi kuogopa kuja Tanzania kuwekeza kwa sababu za kiusalama”

“Jacob Matata ni kijana mwenye umri kati ya miaka 35 hadi 40. Ni mmoja kati ya wapelelezi bora kwa sasa waliopo Afrika. Mtu mwenye sifa zote za kuitwa Komandoo. Amehitimu kwa kiwango cha juu katika fani za karate, kung - fu, judo na mengineyo. Anadhaniwa ni kati ya watu wachache sana wenye uwezo wa hali ya juu katika kutumia silaha ya aina yoyote ile. Ni mtu hatari sana”.

“Tanzania imekuwa ikimtumia katika misheni mbalimbali za kipelelezi ambazo zilidhaniwa kuwa zilihitaji mtu mwenye mbinu za hali ya juu katika kukabiliana na ujasusi. Mara nyingi kitengo cha Usalama cha Umoja wa Mataifa (UUM), kimekuwa kikileta maombi ya kutaka kumtumia Jacob Matata katika pelelezi ambazo zilihitaji umakini na ufanisi wa hali ya juu. Hata hivyo kwa hapa nchini haijulikani anafanya kazi chini ya idara gani na hata ofisi yake haijulikani iliko. Jacob Matata anaishi Sinza. Mwisho wa taarifa.’’

"Makamanda, hiyo ndiyo taarifa iliyoandaliwa na wataalam wetu kutokana na vyanzo mbalimbali vya taarifa. Sasa labda tupate fursa ya kuijadili." Alisema afisa huyu huku akionyesha kuwa alikuwa amewapa fursa ya kuongea wenzie. Maafisa hawa wa ngazi za juu jeshini wote walikuwa wamevalia kiraia kabisa, ni tofauti na utaratibu, lakini walifanya hivyo makusudi kwa vile kikao hiki kilikuwa cha siri na hawakutaka kuvuta macho ya watu wengi. Hata kukutana kwao ilikuwa ni sehemu ambayo huwezi dhani kuwa maafisa wa usalama wa ngazi za juu kama hawa wangekutana.

Mjadala uliendelea kabla ya Luteni Frank Misanya kuongea. “Sijui kama ina uhusiano na hali, hii mnamkumbuka yule jamaa hatari sanaliyetingisha nchi wakati ule wa kashfa ya Loliondo (KL) aitwaye Poka Kingu, ambaye alikuwa amewekwa kwenye jela maalum, ametoweka siku kadhaa zilizopita huku walinzi kadhaa wa gereza hilo wakiwa wameuawa. Hivi jitihada za kumtafuta zimepamba moto. Uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa kuna watu walikuja kumchukua toka gerezani. Kwani nini na ni wakina nani? Hilo halijulikani.” Frank Misanya alisema na kuketi

“Hii ni ajabu sana, amewezaje kutoroka kwenye mazingira kama yale, lazima kuna mkono wa mtu hapa. Haiwezekani mtu hatari kama yule akawa ameingia mtaani. Nimjuavyo Poka Kingu ni wazi mji huu unaingia katika hekaheka kubwa sana. Yule si mtu wa kuwa huru, hafai kuitwa raia yule!’’ Kamanda mmoja alisema kwa jazba kuonyesha kuwa hiyo ilikuwa taarifa mbaya sana.

“Kwangu hii ni taarifa mbaya sana kuliko hata kutoweka kwa Jacob Matata. Poka Kingu ni mtu ambaye hata kikosi maalum kilimshindwa, mtu pekee ambaye alifanikiwa kumtia nguvuni kichaa yule ni Jacob Matata ambaye sasa hatujui yuko wapi na kama bado yu upande wa serikali. Hapa inabidi kuandaa kikosi cha makomandoo tayari kwa kukabiliana na Poka. Mshenzi sana yule, ile staili yake ya kupiga na kuua, natamani tungekuwa na watu kama yeye kwenye jeshi letu.” Alisema huyu afisa huku akitoa leso na kufuta kipaji chake cha uso.

“Mimi napendekeza atafutwe yeye na yeyote aliye nyuma ya kutoroka kwake.” Alisema mwenyekiti wa kikao, kisha akaongeza, “Je, kuna maendeleo yoyote kwenye uchunguzi wa kifo cha Mh. Sabodo?’’ Swali lake lilisababisha afisa mwingine atengeneze koo lake na kuanza kutoa maelezo.

“Uchunguzi ulikwenda vema sana lakini ulikatikia kwa msichana aitwaye Jo Mwa. Baada ya kupima na kujiridisha kuwa mabaki ya mifupa tuliyokuta kwenye gari lililoungua moto kule Masaki ilikuwa ya mheshimiwa Sabodo Sumari, upelelezi ukaanzia kwenye hilo gari ambalo mabaki ya mwili wake yalikutwa. Kwa kusoma namba za injini ya gari na kuwasiliana na TRA, tulikuja gundua kuwa gari lile lilikuwa likimilikiwa na msichana aitwaye Nanalungu. Upelelezi wa zaidi ukatuonyesha kuwa msichana huyo alinunuliwa gari hilo na Sabodo Sumari. Hivyo harakati za kumtafuta Nanalungu zikaanza, akapatikana akiwa maeneo ya Mbagala. Baada ya mahojiano naye ilikuja thibitika kuwa msichana huyo hakuwa anajua chochote kuhusu Sabodo Sumari, japo katika kupekua nyumba yake tulijikuta tumefanikiwa kupata kadi ya ya usajili wa gari lililoungua. Lakini ukimwangalia yule msichana kuna ishara zote kuwa hakuwa anajua chochote kuhusiana na Sabodo Sumari wala kifo chake. Kuna uwezekano kuwa zile nyaraka za gari zilipandikizwa kwenye nyumba yake bila yeye kujua. Tukaamua kuchukua alama za vidole zilizokuwa kwenye zile nyaraka. Hapo tukajiridhisha kuwa msichana yule hakuwahi kushika zile nyaraka”

“Tukajua yeyote aliyefanya vile alifanya kusudi kupoteza ushahidi. Sasa kazi ni kumtafuta msichana aliyehusika, maana alama za vidole zinaonyesha mtu wa mwisho kushika bahasha ile alikuwa ni msichana.” Afisa huyo alimalizia maelezo yake.

“Kazi nzuri, nadhani tukubaliane kimsingi kuwa kazi iwe kuwatafuta watu watatu; Jacob Matata, Poka Kingu na huyu msichana Nanalungu. Lakini labda pia, ni vema nikawaambia kuwa kuna msichana mwingine aitwaye Jo Mwa ambaye kwa mujibu wa Polisi ndiye aliyehusika kusuka mpango wa kumtorosha Poka Kingu toka gereza maalum. Katika ripoti hii nimeambatisha ripoti niliyokuwa nimeipata toka kwa marehemu Inspekta Lucas Mwenda. Hivyo ni vema huyu naye tukamwingiza kwenye mchakato wa kumtafuta. Kazi hii nampatia Luteni Frank Misanya.” Alimaliza maelezo yake. Minong’ono ilisikika huku kila mmoja akijaribu kuuliza na kuongea jambo na jirani yake.

“Tutakutana hapa baada ya siku mbili kwa kikao kingine muda kama huu wa leo.” Mwenyekiti wa kikao alisema na kikao kikawa kimefungwa.

“Tukajua yeyote aliyefanya vile alifanya kusudi kupoteza ushahidi. Sasa kazi ni kumtafuta msichana aliyehusika, maana alama za vidole zinaonyesha mtu wa mwisho kushika bahasha ile alikuwa ni msichana.” Afisa huyo alimalizia maelezo yake.

“Kazi nzuri, nadhani tukubaliane kimsingi kuwa kazi iwe kuwatafuta watu watatu; Jacob Matata, Poka Kingu na huyu msichana Nanalungu. Lakini labda pia, ni vema nikawaambia kuwa kuna msichana mwingine aitwaye Jo Mwa ambaye kwa mujibu wa Polisi ndiye aliyehusika kusuka mpango wa kumtorosha Poka Kingu toka gereza maalum. Katika ripoti hii nimeambatisha ripoti niliyokuwa nimeipata toka kwa marehemu Inspekta Lucas Mwenda. Hivyo ni vema huyu naye tukamwingiza kwenye mchakato wa kumtafuta. Kazi hii nampatia Luteni Frank Misanya.” Alimaliza maelezo yake. Minong’ono ilisikika huku kila mmoja akijaribu kuuliza na kuongea jambo na jirani yake.

“Tutakutana hapa baada ya siku mbili kwa kikao kingine muda kama huu wa leo.” Mwenyekiti wa kikao alisema na kikao kikawa kimefungwa.


**************


"Kuna jambo haliko sawa hapa mheshimiwa." Bi Anita alisema huku akimwangalia Rais wa Nchi (RN) Mhe. Jovin Sekendu kwa macho ya maswali.
"Sijakuita kwenye hii ofisi ili uniambie kuwa kitu kiko sawa au hakiko sawa Mkurugenzi." Mhe. Jovin Sekendu alifoka huku akionyesha kuwa mwenye hamaki sana. "Ninachosema kama hujashirikiana na Jacob kufanya yale yaliyofanyika safe house usiku wa kuamkia leo basi inabidi uanze kuelewa kuwa Jacob Matata amekuwa msaliti wa nchi. Na ndani ya saa chache, kama nisipopata maelezo ya kutosha toka kwako, nitatoa amri ya Jacob Matata kusakwa kama haini." Rais wa Nchi (RN) Mhe. Jovin Sekendu alisema huku akijimiminia kinywaji kikali kwenye glasi. Macho yake yalikuwa mekundu huku akionekana kuwa mwenye kuchoka sana.
Bi. Anita hakusema lolote, alikuwa akimsikiliza Rais wa Nchi (RN) Mhe. Jovin Sekendu na kubaki na maswali mengi kichwani jinsi mambo yalivyokuwa yakienda kwa mwendo wa kuruka.
“Lakini iko wazi kuwa kidole cha Waziri Mkuu (WM) ndicho kimetumika kufungulia. Maana taarifa ya uchunguzi inasema kwenye kioo ambapo ndipo mfunguaji anatakiwa kuweka kidole, zimekutwa alama za kidole cha Waziri Mkuu.” Bi. Anita alisema
“Waziri Mkuu (WM) alikatwa kidole cha kushoto na pale wameona cha kushoto, ila kidole chenye uwezo wa kufungua mlango ni cha kulia.” Mhe. Jovin Sekendu alisema huku akiichukua ripoti ile ya tukio la kuvamiwa safe house na kuipekua tena.
“Ina maana wanataka kumhusisha tu Waziri Mkuu (WM) na tukio halafu ili iweje?’’ Bi. Anita alihoji.
“Wewe mkuu wa shirika la kijasusi ndo unaniuliza miye badala ya miye kukuuliza wewe!’’ Rais alisema.
“Lakini ukweli unabaki kuwa wazi kuwa, mlango lazima ufunguliwe na mmoja wetu sisi watu watano. Hivyo kama si Waziri Mkuu basi mmoja wetu ametumika kwa kujua au kutojua.” Bi. Anita alisema kwa sauti ya chini kisha akaongeza, “Waziri Sabodo Sumari mwili wake umekutwa ukiwa na vidole vyote japo ilikuwa mabaki ya mifupa iliyoungua moto. Mwili huo wa Sabpdp ulipatikana hata kabla ya tukio la safe house. Hii ina maana hakuna namna yeye amehusika. Mheshimiwa, naomba unipe muda wa kufikiri na kujua nini cha kufanya...."
"Muda nimeshakupa, ukasema unamwamini Jacob Matata anaweza kutupatia ufumbuzi wa jambo hili. Lakini matokeo yake, yeye ndiye kawaua walinzi wote safe house na kutoweka kiasi kuwa hata wewe mkuu wake wa kazi unaniambia hujui alipo....." Mhe. Jovin Sekendu alisema huku safari hii akiwa anamwangalia Bi. Anita kwa macho makali mekundu yaliyokuwa yamelemewa na uchovu, pombe kali, fadhaa, hasira na woga.
"Bado nahitaji Muda, hata kama si muda mwingi lakini bado nahitaji muda. Halafu nahitaji unisaidie jambo moja. Nahitaji kumtumia tena Jacob Matata. Bado namwamini!’’ Bi. Anita alisema kwa msisitizo.
"Tukubaliane mambo mawili; moja nataka kujua Jacob Matata yuko wapi na kwa nini amewaua walinzi wote wale. Pili, nataka kujua nani yuko nyuma ya haya mambo. Usipoweza kufanya haya mambo mawili ndani ya siku nne basi kama nilivyosema, nitamtangaza Jacob Matata kama haini alafu wewe utawekwa chini ya uchunguzi mkali. Nadhani unajua maana ya kuwekwa chini ya uchunguzi." Mhe. Jovin Sekendu alisema huku akikuna kichwa chake. Bi. Anita, mkuu wa kitengo Ofisi Fukuzi aliminya midomo yake kwa vidole bila kujibu neno. alijua kauli hiyo ya Mhe. Jovin Sekendu ilikuwa na ukubwa na ukali gani. Katika historia ya kazi yake amewahi kukutana na mikasa mingi sana mikubwa kwa midogo, lakini safari hii aliona kuwa hii ilikuwa na ugumu wake. Hawakuwa akipambana na gaidi au kundi la majambazi bali msaliti toka ndani ya mfumo wa usalama wa nchi. Yeye kama mkurugenzi wa Ofisi Fukuzi, alijiona kama mtu mwenye dhamana kubwa. Kwani sura iliyopo sasa ilikuwa wazi kuwa ujasusi au majasusi walikuwa kazini ili kuchanganya hali ya mambo.

Muda wote ambao Mhe. Jovin Sekendu alikuwa akiongea na Bi. Anita, Waziri Mkuu, Mhe. Silas Kiondo alikuwa kimya kabisa ndani ya chumba hicho, ambacho walikuwepo watu watatu tu. Ilikuwa inagonga saa nne kasoro dakika kumi na tisa asubuhi.

* * *

"Afuatiliwe, nataka kujua mienendo yote na mawasiliano ya Bi. Anita tangu sasa" Mhe. Jovin Sekendu alisema mara baada ya Bi. Anita kuondoka. Mhe. Silas Kiondo ambaye ndiye Waziri Mkuu (WM) alitingisha kichwa kuitikia. Halafu aliminya namba kadhaa kwenye simu yake kisha akaiweka simu sikioni.
"Nyoso, hakikisha unajua kila kitu kinachofanywa na huyo mama anayetoka hapo getini. Namba yake ya simu naituma sasa hivi kwenye simu yako. Sitaki ujue ni nani na hutoweza kujua ila nataka ujue anaongea na nani na ameenda wapi. Utanipa taarifa kila baada ya saa tatu. Usimguse wala kumfanya chochote." Mhe. Silas Kiondo alitoa maelezo kisha akakata simu.
"Utaratibu wetu uwe ni uleule, zaidi yako wewe na Nyoso sitaki mipango na mawasiliano yetu yaende kwa mtu mwingine zaidi. Waache wakuu wengine waendelee na taratibu zao kama taratibu za mamlaka na mipaka zinavyotaka!’’ Mhe. Jovin Sekendu alisema huku akijiweka vema kitini.


Bi. Anita alitembea taratibu kuelekea ulipo mlango wa ofisi yake. Mawazo yake na akili ilikuwa ikitafakri maongezi yake na Rais. Ilikuwa wazi kuwa taaluma yake ilikuwa imeingia kwenye mtihani mkubwa sana ambao hajawahi kuupata tangu ameanza kazi hii. Mama huyu ambaye wengi walipenda kujua jina lake la pili lakini hakuna hata mmoja aliyefanikiwa. Vilevile hakukuwa na mtu aliyekuwa na uwezo wala kupata ujasiri wa kumwuliza mama huyu kuhusu jina lake la pili. Bi. Anita ni mtaalam wa juu katika masuala ya upelelezi na ujasusi. Sifa hizi ndizo zilizofanya mkuu wa nchi kutosita kumpa kazi ya kusuka na kusimamia kikosi cha siri kinachojihusisha na masuala ya ndani sana ya upelelezi na ujasusi. Kikosi hicho kinajulikana kwa jina la “Ofisi Fukuzi” Inasemekana kuwa mama huyu ni mwanamke pekee ambaye nchi ilimteua kuungana na kundi la wanaume kadhaa kwenda kuchukua mafunzo ya juu ya mambo hayo ya upelelezi na ujasusi enzi hizo, mara tu baada ya kupata uhuru miaka ile ya sitini. Ambapo nchi ilikuwa katika uhitaji mkubwa wa watu wa usalama ambao ni wazalendo na ambao hawakuwa wameathirika na fikra za kikoloni.

Safari yake kuchuma ujuzi huu ilimchukua miaka kadhaa. Katika miaka hiyo yote ilimlazimu kupita katika nchi nyingi zilizoendelea sana katika fani aliyokuwa akiihitaji. Ni katika miaka hiyo pia, ambapo ilimbidi kupitia katika mitihani mingi ya kazi za hatari na mateso makubwa. Mpaka aliporudi nchini, Bi. Anita alikuwa na sifa zote za kuitwa Komandoo.

Kwa miaka kadhaa tangu arejee nchini amekuwa akifanya kazi mbalimbali za kipelelezi na kijasusi, mpaka pale Serikali kwa sababu ambazo hazijulikani kwa hakika ilipoamua kuanzisha kitengo hiki cha Ofisi Fukuzi. Kitengo hiki ni maalum kwa masuala ya kijasusi ambayo si rahisi kutatuliwa na vyombo vingine vya usalama. Haikuwa kazi kumpata mtu wa kuweza kusimamia kazi hiyo ya siri sana. Jina la Bi. Anita lilijitokeza mara moja katika kumbukumbu za kichwa cha mkuu wa nchi wa wakati huo.

Kitengo hiki anachokiongoza kimesheheni vijana waliopikwa na kupikika katika masuala ya upelelezi. Nchi imekuwa ikitenga fungu maalum kama matumizi ya ofisi hii. Hali hii imesababisha, “Ofisi Fukuzi” kuwa na vifaa vya kisasa na vijana ambao wana mafunzo ya juu kabisa na kisasa toka nchi zilioendelea katika masuala ya ukachero.

Japo wataalam wa bajeti wamekuwa wakitaka kujua undani wa fungu linalotengwa kwa ajili ya Ofisi Fukuzi lakini walichoweza kujua na kuambulia ni, ‘ni kwa usalama wa nchi’. Wakanyamaza. Mawaziri wa Ulinzi walishajaribu mara kadhaa kujua undani wake lakini waliishia hewani. Ilikuwa ofisi ya siri yenye kufanya kazi moja kwa moja na Rais na kwa kiasi fulani Waziri Mkuu ambaye hata hivyo hakuwa na mamlaka ya moja kwa moja na ofisi hii. Ilikuwa ni nje ya mfumo wa kawaida wa madaraka na utawala.

Bi. Anita aliingia ofisini kwake kisha akaitisha kuonana na Jacob Matata. Jibu alilopewa ni kuwa Jacob Matata alikuwa hapo nusu saa iliyopita, amekwisha ondoka.
"Umeongea na Jacob alipokuja?" Bi. Anita alimuuliza Mkuu wa Ofisi, aitwaye mama Mbembela.
"Ndiyo, alivyofika tu aliuliza kama ulikuwepo ofisini nikamwambia hukuwepo. Basi akaenda ofisini kwake akajaza fomu ya dharula ya kuchukua silaha. Lakini pia, alikuja ofisini kwako, unajua kwa ngazi aliyopo anaweza kuingia ofisini kwako kwa dharula. Hakumaliza hata dakika tatu akawa ametoka. Akaondoka eneo hili, alionekana kuwa na haraka. Hilo halikuwa la ajabu kwangu, unajua Jacob Matata ni mtu mwenye majukumu mengi makubwa. Kwani kuna shida yoyote? Meneja wa Ofisi, Mama Mbembela alihoji baada ya kuona sura ya Bi. Anita iko katika hamaniko.
"Hakuna shida yoyote!’’ Bi. Anita alijibu huku akionyesha kuwa hakuwa na hamu kuendelea na maongezi, Mama Mbembela aliliona hilo, akasimama na kutoka mle chumbani, chumba cha ofisi ya Bi. Anita. Mama Mbembela alipoondoka, Bi. Anita aliingiza mkono kwenye uvungu wa meza moja kubwa iliyokuwa mbele yake.
"Shiiit!, Jacob anakusudia kufanya nini? What is going on?’’ Alisema baada ya kuwa amesoma kijikaratasi alichokikuta uvunguni mwa meza. Bi. Anita akiwa bosi wa Jacob Matata alikuwa anamjua vema Matata. Walikuwa wameshafanya kazi pamoja kwa muda mrefu na katika mazingira mbalimbali. Walikuwa na namna yao ya kufanya kazi, kuwasiliana, kuadhibiana na kutaniana ambayo hakuna mtu mwingine kwenye Ofisi Fukuzi alikuwa akijua japo wengi walijua fika kuwa Bi. Anita alikuwa akimpenda sana Jacob Matata. Hivyo baada ya kuwa ameambiwa mazingira ambayo Jacob Matata alikuwa ameondoka mara moja akahisi lazima Jacob atakuwa amemwachia ujumbe. Kweli alichokuwa akiangalia chini ya uvungu wa meza ilikuwa ni uwezekano wa kupata ujumbe wa Jacob Matata, hiyo ni moja ya sehemu ambazo hutumiwa na Jacob kumwachia ujumbe kukiwa na dharula. Ujumbe alioupata ulisomeka.
“Ruhusu mwindaji awe mwindwaji. I trust no one....” Ujumbe huu haukumshangaza Bi. Anita, kilichomshangaza na kujua kuwa wakati huu ofisi yake iko kwenye mtihani mzito ni zile nukta zilizofuata baada ya neno ‘one’. Jacob alikuwa ameweka nukta nne, yaani,(….) . Haikuwa bahati mbaya kwa Jacob Matata kuweka zile nukta nne , kwa mtu mwingine yeyote huo ungekuwa ujumbe wa kawaida ambao ulimaanisha kuwa Jacob Matata hamwamini mtu yeyote mpaka wakati huo. Katika utendaji wa Ofisi Fukuzi, mpelelezi wakati wote alikuwa na sehemu kuu nne muhimu, nazo ni Ofisi Fukuzi, Rais, Waziri Mkuu na Mpelelezi mwenyewe. Huo ndiyo uliitwa ‘mfungamano yakinifu’. Sasa Jacob Matata kuandika kuwa hamwamini mtu yeyote kisha akaweka nukta nne ilimaanisha kuwa hamwamini Rais, Waziri Mkuu, Ofisi Fukuzi na hata yeye mwenyewe! Hilo ndilo lililomshangaza Bi. Anita. Alielewa ilimaanisha nini mpelelezi anapokuambia kuwa, hajiamini hata yeye mwenyewe. Hi inamaanisha kuwa hana hakika kama anatumiwa au hatumiwi na adui. Ujumbe ulikuwa ni mmoja, mpelelezi alihitaji muda wa kuchanganua mambo. Tayari ilikuwa saa tano na dakika arobaini asubuhi.

* * *

Karatasi yenye ujumbe, “Ruhusu mwindaji awe mwindwaji. I trust no one....’’ iliweza kuoneka vema kwenye darubini ya Nyoso, aliyekuwa kwenye ghorofa iliyokuwa ikitazamana na majengo ya Ofisi Fukuzi. Alikuwa katika kutekeleza amri aliyopewa na Waziri Mkuu ambaye aliambiwa na Rais, "afuatilie, mienendo yote na mawasiliano ya Bi. Anita tangu sasa". Nyoso hakujua alikuwa akimfuatilia nani, wala maadili ya kazi yake hayakumtaka kujua ila alijua fika kuwa alitakiwa kumfuatilia mlengwa kwa ukaribu sana. Hivyo alipoona gari la Bi. Anita inaingia kwenye majengo hayo, yeye kwa haraka sana alitafuta namna ya kuingia kwenye jengo la ghorofa lililokuwa likipakana na jengo alilokuwa ameingia Bi. Anita. Kwa hila na mbinu za hapa na pale alifanikiwa kufika juu ghorofani na sasa alikuwa akichunguza kila kilichokuwa kikiendelea kwenye lile jengo. Darubini aliyokuwa nayo ilimwezesha kufanya hivyo. Mara moja alipiga picha ile karatasi, toka umbali ule na kwa kutumia ileile darubini. Kisha kwa kubonyeza vitufe vichache kwenye ile darubini, ile picha yenye ujumbe aliituma. Kisha akaisindikiza kwa ujumbe toka kwenye simu yake.

* * *

Haikuchukua Muda mrefu, dakika tano badaye yaani saa tano na dakika hamsini ujumbe uliingia kwenye simu ya Waziri Mkuu, Mhe. Silas Kiondo. Aliusoma, hakuelewa hadi pale ujumbe mfupi toka simu ya kiganjani ya Nyoso ulipoingia na kusomeka; “Mtu wako uliyesema nimfuatilie amekuta huo ujumbe kwenye meza yake.” Ndipo akaelewa haraka kuwa ujumbe huo ungekuwa umeandikwa na Jacob Matata kwenda kwa Bi. Anita. Mara moja akaufikisha ule ujumbe kwa Mhe. Jovin Sekendu, aliusoma kisha akaomba kuwa na nafasi ya peke yake. Kuna kitu alihisi kuwa alihitaji kuelewa. Katika mafunzo aliyopewa wakati ameingia madarakani, kulikuwa na kipengele cha usalama. Katika kipengele hicho alipata nafasi ya kufunzwa machache na Bi. Anita. Katika mada iitwayo ‘Kwa Wateule Wanne’, Bi Anita aliwahi kumweleza kwa kifupi juu ya zile nukta. Hivyo Mhe. Jovin Sekendu alipoziona kwenye ule ujumbe alitaka kujua zaidi.
"Naomba unikumbushe kidogo kuhusu nukta." Mhe. Jovin Sekendu, alisema mara baada ya kuwa kwenye simu na Bi. Anita.
"For your eyes only." Bi. Anita alisema.
"Okay, ila amri yangu inasimama palepale kama tulivyoongea asubuhi hii." Mhe. Jovin Sekendu alisema kwa mkazo.
"Nashauri Jacob Matata atafutwe kwa ajili ya nukta ya mwisho kama ulivyoona ujumbe!’’ Bi. Anita alisema.
"Sawa!’’ Mhe. Jovin Sekendu alisema kisha akakata simu. Mhe. Jovin Sekendu, alielewa lakini hakuelewa. Anakumbuka nukta zinasimama badala ya watu muhimu, lakini hakuelewa kama ujumbe umeandikwa na mtu kama Jacob Matata watu hao angekuwa nani na nani. Alichoelewa ni ‘for your eyes only.’ Hii ilimaanisha kuwa kuna kitu ambacho Bi. Anita hawezi kukisema toka kwenye ule ujumbe wa Jacob Matata, ila pia, inamaana na yeye Mhe. Jovin Sekendu, kama kuna kitu amekigundua asikiseme. Hivyo ‘for your eyes only’ ilikuwa ni lugha yao wawili ambayo Mhe. Jovin Sekendu aliielewa.
"Natoa agizo, Jacob Matata atafutwe kwa usalama wa nchi. Isitangazwe ila iwe kimyakimya. Namtaka akiwa hai." Mhe. Jovin Sekendu alimwambia Waziri Mkuu baada ya wawili hawa kuungana tena kwenye chumba kile cha awali.

* * *

Ngongoseke alitabasamu, kazi ilionekana kuwa nyepesi kuliko alivyokuwa ametazamia. Mamilioni ya dola yalikuwa yanaingia kwenye akaunti yake muda wowote, pale ambapo angeweza kutuma vithibitisho kuwa hakuna masalia ya ripoti ya gesi ya Mtwara na kuwa kile kisanduku cheusi cha ndege iliyoangushwa kuwa kimeshaharibiwa. Alikuwa karibu sana kuyatimiza hayo yote, lakini pia, alitaka kuhakikisha kuwa anakuwa karibu sana na Serikali kiasi kuwa kusiwe na hisia zozote kuwa ana mkono kwenye haya mambo. Kama kawaida sasa alikuwa kwenye jumba lake la kifahari, Bagamoyo.
Waliompa tenda hii ya kuvuruga mchakato wa gesi ya Mtwara, waliona ana kila sifa, hasa zile kuu mbili; ana sifa njema Serikalini na yuko jirani na viongozi halafu ya pili, anajua kuishi gizani bila taabu kana kwamba ndiko alikozaliwa, kukulia na ndiko atafia.

Hakuna anayekataa pesa, unaweza kunywa maji ukasema inatosha. Unaweza fanya chochote ukasema kinatosha, lakini kamwe huwezi sema pesa zinatosha. Hili linathibitika kwa Ngongoseke Amos Nkwija. Sasa alikuwa kwenye mipango yake tena. Na wakati huu alikuwa kwenye zile simu zake ambazo kila amalizapo kuongea huharibu kadi ya simu na hivyo kutumia mpya kila mara. Aliongea na Poka Kingu akaona mambo yako sehemu yake, alipoongea na Nyoso akahakikishiwa kuwa asiwe na wasiwasi. Frank Misanya yeye akasema ahesabu kila kitu kimeshakamilika. Akapiga simu nyingine mbili kwa vigogo. Halafu akapiga masafa marefu huko ughaibuni. Alipomaliza, alijuhusudu yeye mwenyewe; hakuna ambaye angeweza msifia kwa vile wachache waliokuwa wanajua alichokuwa anafanya. Na mbinu yake ni moja, kila aliyempa kazi alimpa kipande cha kazi, kazi kamili alikuwa akiijua yeye mwenyewe. Huyo ndiyo Ngongoseke Amos Nkwija.

Ungekuwa Jacob Matata au Bi. Anita ungefanya nini kwenye mazingira kama haya?




Frank Misanya yeye akasema ahesabu kila kitu kimeshakamilika. Akapiga simu nyingine mbili kwa vigogo. Halafu akapiga masafa marefu huko ughaibuni. Alipomaliza, alijuhusudu yeye mwenyewe; hakuna ambaye angeweza msifia kwa vile wachache waliokuwa wanajua alichokuwa anafanya. Na mbinu yake ni moja, kila aliyempa kazi alimpa kipande cha kazi, kazi kamili alikuwa akiijua yeye mwenyewe. Huyo ndiyo Ngongoseke Amos Nkwija.

*****Kitabu cha riwaya hii sasa kinachapwa kwa idadi ya wale walioweka ODA tu, kinatoka tarehe 15/6/2020. Weka ODA yako sasa 0762204166********

BAADA ya kutoka yalipo majengo ya Ofisi Fukuzi, mpelelezi Jacob Matata aliazimia kuanzia nyumbani kwa Afande Lucas. Kufutwafutwa kwa faili alilokuwa ameandaa kisha kuuawa ilikuwa dalili tosha kuwa kuna hatua alikuwa amepiga katika uchunguzi wake. Hivyo kwenda msibani na kuonana na mjane aliona kuwa lingekuwa wazo zuri. Afande Lucas alikuwa akiishi uraiani, Mwananyamala Komakoma jirani na Mwinjuma road.

Hakupata shida kuiona nyumba yenyewe, wamama wenye khanga tatu-tatu walionekana kufanya hili na lile. Upande wa kulia wa nyumba hiyo kulikuwa na turubai lililowekwa ili kuwapa watu kivuli. Aliangalia saa yake ya mkononi ilikuwa saa tano na dakika arobaini asubuhi. Kama utakumbuka wakati huu ndiyo Bi. Anita na yeye alikuwa ofisini kwake. Jacob Matata aliendesha taratibu kuliendea eneo lile. Hakukuwa na sehemu ya kuegesha gari hivyo alipitiliza kwa mwendo mdogo huku akijitahidi kutafuta sehemu ya kuegesha. Mbanano wa nyumba na ujenzi usio na mpangilio katika eneo hili ulifanya uzuri wa nyumba ambayo watu walikuwa wamejaa usionekane.

Aliiangalia ile nyumba ambayo aliamini kuwa ndiyo yalipo makazi ya marehemu Inspekta Lucas. Ilikuwa nyumba nzuri ya kisasa na thamani kubwa. Alishangaa kuona nyumba kama ile kujengwa eneo kama lile, maana nyumba kama hizo huonekana yale maeneo ya watu wazito. Kingine alichoshangaa ni kwa namna gani Askari Polisi alifanikiwa kujenga nyumba ya kifahari kama ile, ila alipokumbuka kuwa kwenye nchi yake mtu anaweza pata pesa kwa njia nyingi, alinyamaza. Kutafuta sehemu ya kuegesha kulimpeleka hadi mtaa wa nyuma ambapo kulikuwana kiwanja ambacho hakijajengwa. Hapo alikuta magari kadhaa yakiwa yameegeshwa. Kwa bahati nzuri aliona sehemu ambayo alipachika gari alilokuwa anatumia ambalo alikuwa amelikodisha. Hakuona busara kwenda nyumbani kwake baada ya yale yaliyokuwa yametokea usiku. Pia, isingekuwa akili nzuri kutumia gari lake analotumia siku zote. Hadhari lilikuwa jambo la msingi sana kwake wakati huu. Baada ya kuteremka na kufunga gari aliangaza kama anaweza pata kichochoro cha kumpeleka nyumbani kwa Afande Lucas, badala ya kuzunguka na barabara. Mara hii tena bahati ilikuwa upande wake, aliona kichochoro ambacho pia kilikuwa kikipitisha maji machafu. Haikuchukua muda alihisi yuko nyuma ya nyumba aliyokuwa akiiendea maana aliweza kusikia sauti za watu wakiongea katika hali ya kushirikiana kazi za upishi. Aliendelea mbele kidogo hadi alipokuwa usawa wa dirisha moja. Alipofika hapo alisita kidogo baada ya kusikia sauti ambayo haikustahili kusikika msibani. Alisimama kisha akajivuta ukutani jirani na lile dirishi ilikotokea ile sauti nzito ya amri.

“Kama akija mtu atakayejitambulisha kwa jina hilo tupe taarifa, maana mtu huyo ni hatari kwako na familia yako. Chukua simu hii, ukiminya tu hiki kidude utaongea na mimi moja kwa moja nami nitatuma askari wakusaidie. Pia, ukihitaji hela ziko kwenye akaunti yako ya benki.” Ilikuwa ni sehemu ya sauti hiyo nzito iliyoongea kwa amri. Jacob alitaka kuchungulia ili amwone aliyekuwa akiongea lakini kulikuwa na pazia zito hivyo hakufanikiwa. Aliharakisha kutembea ili awahi kuwaona watu hao kabla hawajatokomea. Akiwa na matumaini ya kufanikisha hilo mara uchochoro ule ukampeleka mbele ya dimbwi kubwa la maji machafu. Kwa mbele yake kulikuwa na choo ambacho kuta zake zilikuwa ni mabati na pembeni yake ambapo ndio kichochoro hiki kilipita lilichimbwa hilo shimo kubwa lililokuwa na maji machafu. Ilivyokuwa hakuwa na namna ya kuenedela na kichochoro hicho la sivyo ajitolee kutumbukia kwenye maji yale. Aliangalia kwa namna ya kukata tamaa, hii ilimaanisha asingeweza kuonana na yeyote aliyeongea kwa ile sauti. Alikata shauri kurudi na kuzunguka na barabara.

* * *

Wakati Jacob Matata akikwama kwenye kile kichochoro, Luteni Frank Misanya yeye alikuwa ndani ya gari lake akiendesha wakati simu ya Ngongoseke ilipoingia. Alipunguza mwendo wakati anakunja kushoto mbele ya Chuo cha Diplomasia akiiacha barabara ya Kilwa na kuingia Kurasini, mkono wa kushoto ulichukua simu hiyo iliyokuwa ikilia kwa fujo.
“Sema!’’ Alisema baada ya kuona namba asiyoifahamu “Ngongoseke hapa.” Alijitambulisha.
“Sema Mzee!’’ Luteni Misanya alisema.
“Nilikwambia wale vijana wamejua mengi kuhusu kazi zetu....” Ngongoseke alisema kabla hajakatizwa na Frank,
“Yaani umejuaje hapa ndio nakaribia nyumba wanayoishi, nataka nikawam...” Frank alisema lakini naye alikatishwa,“ Nilikwambia usiwaue wewe. Sasa sikiliza, sasa hivi wapeleke pale anapokaa Nanalungu, Jacob Matata, yuko hapo.” Ngongoseke alisema
“Aaaaah, aisee wewe Mzee ni kiboko!” Luteni Frank alisema, maana alishaelewa akili ya Ngongoseke.
“Ulikuwa hujui au unathibitisha tu?’’ Ngongoseke alisema kwa majivuni.
“Akili yako inafanya kazi kwa kiwango cha ajabu sana.” Frank alisema.
“Waende sasa hivi maana nimeambiwa Jacob yuko hapo muda huu. Yeye atatusaidia kuwaua.” Ngongoseke alisema.


* * *

Robo saa baada ya Ngongoseke kutoa maelekezo hayo kwa Luteni Frank Misanya, Jacob Matata yeye sasa alikuwa mbele ya mlango wa chumba alichoelekezwa kuwa mjane wa Afande Lucas alikuwemo. Kama alivyoiona kwa mbali, ilikuwa nyumba kubwa ambayo hukuhitaji elimu kubwa kuitaja kuwa ya kifahari japo ilikuwa maeneo yasiyoistahiki kuwepo. Alibisha na kukaribishwa. Aliangaza macho huku na huko. Kilikuwa chumba kilichojaa wanawake tu, ambao wengi wao macho yao yalikuwa mekundu na wengine yakiwa yamevimba. Mara alimwona msichana mmoja mrembo wa haja ambaye pembeni yake kulikuwa na kitu kama simu. Macho yake yakavutika na muundo wa ile simu, aliiangalia tena kwa makini na mara Jacob Matata akabaini kwa kilikuwa kinasa sauti. Akili ya Jacob Matata ilifanya kazi haraka, alijua yule mtu mwenye sauti ya amri ndiye aliyempatia huyo mwanamke kile kifaa akimdanganya kuwa ni simu ili aweze kurekodi mazungumzo yote ya yule Mjane wa Afande Lucas.

“Pole sana dadangu!” Jacob alisema baada ya kuwa ameinama alipokuwa ameketi yule dada. Alikuwa mwanamke, mzuri, mrembo wa umri wa kati, si mtoto si mtu mzima. Maana Jacob yeye anajua kuwa urembo na uzuri kwa manamke ni vitu viwili tofauti, lakini huyu alikuwa navyo vyote.

“Asante sana!” Alisema yule msichana kwa sauti kavu, huku akijitahidi kumwangalia Jacob Matata.

“Sijui unawe......” Kabla Jacob Matata hajamaliza alichotaka kusema, yule mwanamke haraka akaweka kidole katikati ya midomo yake kama ishara ya kumtaka Jacob Matata anyamaze. Kisha akasimama na kumwonyesha Jacob ishara kuwa amfuate.

“Bila shaka unaitwa Jacob Matata?’’ Msichana alihoji. “Kama ndiye?’’ Jacob alisema kwa mshangao.

“Ndiye wewe, maana hata jibu lako limekuwa sawa na nilivyoelekezwa na mume wangu. Naitwa Nana Lucas, marehemu mume wangu katika siku zake za mwisho alikuwa anakutafuta sana. Alijua maisha yake yako hatarini ila hakuona kama angeweza pata msaada toka kwa mtu yeyote yule mwingine zaidi yako. Juhudi zake za kukutafuta hazikuzaa matunda hadi alipouawa. Ila akawa amenielezea sifa zako akiwa na hakika kuwa kwa namna moja ama nyingine ungeingia kupeleleza kitu alichokuwa ameanza kupeleleza. Hivyo alikuwa na hakika kuwa ipo siku ungekuja kwangu. Hivyo nilivyokuona tu mara moja nikajua ndiye.” Alisema yule mwanamke huku sasa machozi yakiwa yanamtiririka. Jacob alimvuta na kuanza kumbembeleza.

“Je, unaweza kuniambia kama kuna lolote alitaka unifikishie?’’ Jacob alisema kwa sauti ya kubembeleza pia, huku akili yake ikiwa makini kabisa.

“Jumatatu wiki iliyopita ndiyo alikuja akiwa amebadilika sana. Nikamuuliza vipi, akaniambia kuna kazi amekuwa akifanya, anasema uchunguzi wake umemfikisha sehemu ambayo amegundua kuna watu wa usalama na viongozi wanahusika. Hilo halikumtisha sana, ila anasema alimtembelea Luten Frank Misanya, baada ya kuongea naye amemtishia maisha kama hatoachana na kazi hiyo. Hivyo akaniambia nikikuona nikuombe uanzie kwa Luten Frank Misanya.” Alisema yule msichana huku akilia kwa kwikwi.

“Je, kuna jingine Nana?’’ Jacob alihoji.

“Hapana Jacob, ila kuna watu walikuja wakijifanya wao ni Jacob Matata na kuniuliza kama kuna ujumbe wowote marehemu aliuacha kwa ajili yao. Lakini katika wote sikuona kama kuna mtu ana viashiria vya sifa ambazo mume wangu aliniambia. Hivyo sikusema lolote.’’

“Okay, bila shaka ndiyo waliyokupa hiyo simu ambayo pia ni kinasa sauti?’’ Jacob alihakiki.

“Ndiyo, nilipoiona niligundua. Wengi hudhani miye ni mwanamke wa kawaida tu, lakini si kweli. Ni mtu niliyepitia mafunzo mengi ya namna hiyo wafanyayo na mapenzi yangu kwa Lucas yaliyonifanya nijitulize kwake. Lakini hivi nilishapanga kama nisipokuona kesho nianze mikakati ya kisasi. Mazishi tumefanya jana, nilipanga kupumzika leo halafu kesho nianze mishe-mishe.” Nana alisema.

“Ulipanga ungeanzaje kulipa kisasi?’’ Jacob alihoji.

“Sina mpango kamili kwa sasa, ila kwa harakaharaka bila shaka ningeanza na waliokuja kunipa hii simu.” Nana alisema.

“Nadhani inaweza kuwa hatari kuliko unavyodhani.’’ Jacobo alisema kisha akamkumbatia yule Msichana ambaye sasa alianza kububujikwa na machozi.

“Nini kimekufanya uamini kuwa mimi ndiye Jacob Matata?’’ Swali hilo la Jacob lilimfanya yule msichana amsukume Jacob na kujitoa mikononi mwake. Akamwangalia kwa muda kana kwamba ndiyo kwanza anamwona. Kisha kwa sauti ya kutafakari akasema, “Wewe siyo kama askari wengine, askari ni wababe na wala siyo kama jambazi, una mvuto kwa mwanamke na ndiyo mume wangu alivyoniambia. Kitendo cha kupiga magoti pale wakati unanisalimia, muonekano wako na ulivyoitoa ile pole ilikuwa alama tosha kuwa wewe ndiye!’’ Alisema alafu akamkumbatia tena Jacob Matata huku, akilia kwa sauti na uchungu.
“Jacob, nisaidie kulipa kisasi kwa Mwenda wangu. Niko tayari kukusaidia kama ukitaka!’’ Alisema kwa uchungu, sauti yake kama iliingia kwenye masikio ya Jacob, haikuishia hapo tu bali iliingia kwenye nafsi na moyo wake. Matokeo yake akajikuta akisema,
“Tuombe uzima, Mungu atusaidie.”

"Kwa nini nisiwapigie halafu uje uwakamate Jacob?’’ Nana alihoji.

"Wazo zuri lakini sishauri ufanye hivyo. Watu hawa si wa kuwafanyia mzaha hata kidogo. Endelea kuwepo, ukiwa mtulivu na kufanikiwa kuwafanya wasijue kuwa umeonana na mimi hilo litatusaidia sana mbele ya safari tukiendelea kuwa hai. Lengo si kupata tawi bali mzizi wa mambo haya.’’ Jacob alisema huku macho yake yakiwa yametulia kifuani kwa Nanalungu. Alihusudu jinsi Afande Lucas alivyokuwa amefanikiwa kuchagua mwanamke mrembo.




Baada ya kutoka nyumbani kwa Afande Lucas, mpelelezi Jacob Matata alikanyaga mafuta hadi posta Mpya. Aliangalia saa yake ilikuwa saa sita na dakika hamsini na tatu asubuhi. Alipomaliza kuegesha gari lake maeneo fulani, aliingia Benki akachukua kiasi cha hela za kutosha. Safari hii hakutaka kutumia gari alilokuwa amekuja nalo, hivyo akachukua taxi hadi Tazara, Uchumi Super Market (USM) ndani ya Quality Plaza (QP). Hapo aliingia akanunua vitu vingi vya kula, lakini pia, akanunua kitabu cha riwaya Patashika, hakuwa amechukua kitabu hicho wakati anatoka safe house.

* * *

Saa nane kasoro dakika ishirini na tano mchana wa jua kali katika jiji la Dar es salaam, mpelelezi Jacob Matata anatembea kutoka jengo la Quality Plaza akiwa amebeba mfuko wenye vitu alivyonunua. Wakati yeye akitembea kutoka, kuna watu watatu walikuwa wanabishana ndani ya gari hatua chache toka pale alipokuwa.

“Wewe hebu mmalize bana tukafanye mambo mengine.” Mmoja alisema.

“Hapana, tumeambiwa kummaliza lakini natamani tummalize kwa namna ambayo itatupa sifa na majina makubwa baadaye. Unadhani kumuua mpelelezi hodari kama huyu ni nafasi ya kuchezea?’’ Mwingine alisema.

“Lakini kweli maana kesho unaweza jikuta umeingia kwenye orodha ya wauaji mashuhuri duniani.” Mwingine alisema kabla ya kuongeza, “Ila unadhani ni busara kupambana na Jacob Matata? Maana nasikia ni moto wa kuotea mbali!’’

“Sikiliza si unaona pale anatafuta taxi, twende halafu tumzoe kama mzoga na kuondoka naye. Napenda tuache majina yetu kwenye mwili wake ili watu wajue siye ndio tumemuua. Hiyo itatupa heshima sana!’’ Huyu alisema.

“Wazo zuri, haya naona anaelekea kwenye kile kijinjia pale. Akifika kwenye kile kibanda ndio tunaweza kumbana vema na kumzoa. Iwe kasi sana.” Mwingine alisema. Wakakubaliana.

* * *

Wakati hawa wanakubaliana, Poka Kingu yeye alikuwa akimwangalia Jacob Matata kwa husuda. Alikuwa ameshapewa maelekezo toka kwa Ngongoseke kuwa amwache kwanza kwa sasa. Hivyo japo alikuwa kwenye nafasi ya kummaliza Jacob Matata lakini aliheshimu uamuzi wa Ngogoseke. Alimwona Jacob Matata akiwa anakaribia kwenye kibanda fulani cha kuuzia vocha za simu.

* * *

Jacob aliendelea kutembea kueleke upande ambao kulikuwa na taxi za kukodisha. Wakati amekaribia kibanda cha simu mara akasikia gari likija kwa kasi nyuma yake.
Hakutaka kugeuka kuangalia ilikuwa nini, alijirusha na kuparamia mlango wa kile kibanda. Halafu akamwona mtu anamjia kwa kasi pale alipokuwa. Kwa kasi sana alijigeuza na kuachia teke kali ambalo lilimpata yule mtu kiunoni. Jamaa alijikakamua akanyanyuka kwa haraka wakati huo Jacob alikuwa ameshatoa bastola yake baada ya kuona gari lilikuwa limesimama. Hakuchelewa kujua nia ya wale watu kuwa ilikuwa ni kumteka nyara. Aliachia risasi mbili haraka zote zikampata yule Jamaa kifuani. Kuona hivyo Jamaa aliyekuwa kwenye gari aliliondoa gari kwa kasi kuelekea barabarani. Jacob Matata aliachia risasi kulenga taili za gari lile. Gari likaingia Kilwa road kwa fujo na kusababisha ajali mbaya. Liligongwa na magari mengine yaliyokuwa kwenye kasi kubwa, yalilisomba na kuliburuza ubavu ubavu. Wakati watu bado wako kwenye taharuki kubwa, Jacob Matata aliokota vitu vyake alivyokuwa ameviagusha wakati wa purukushani halafu akafanikiwa alijipenyeza katikati ya watu, kabla haijawa shida kubwa.

————————————————————
RIWAYA HII SI YA KUKOSA KITABU CHAKE. KITABU KINATOKA WIKI IJAYO KWA WALIOWEKA ODA NA KULIPIA.
————————————————————

Poka Kingu alitabasamu, ‘ndio maana ushujaa mwingine miye huwa siupendi’, alijiwazia. ‘Kilichowafanya watake kumchukua mzima-mzima ni nini? Shenzi zao wamepata walichostahili’. Hata hivyo Poka Kingu hakufanikiwa kumwona Jacob Matata alivyotoweka. Poka alijilaumu kwa kukubali kuambukizwa uzembe na wale wazembe waliokuwa wakitaka kuonekana mashujaa mbele ya mtu anayewazidi uwezo. Alijitahidi kadiri alivyoweza lakini hakufanikiwa kumwona tena. Hii ilimaanisha apange mbinu mpya za kuweza kupata mwenendo wa Jacob Matata.

* * *

Njia za vichochoroni zilimfikisha vichochoro vya Buguruni. Safari yake iliishia kwenye moja ya nyumba ambayo ilionekana kuwa wenye nyumba walikuwa wamesafiri muda mrefu. Jacob Matata ndiye alikuwa mpangaji wa nyumba hii, hakuwa akiitumia, ila alikuwa mwaminifu kwa mwenye nyumba wake, ambaye alikuwa akimpa kodi nono. Alikuwa ameweka mtu ambaye alikuwa akimsafishia mara moja kwa mwezi na kisha humlipa kwa kazi hiyo tu.

Aliingia ndani na kuangalia vitu vyake harakaharaka. Kisha akachukua daftari lake na zile nakala za kitabu alizokuwa amefanya toka nyumba ya hazina. Hapo kazi ya kusoma ikaanza upya. Alikisoma kitabu Patashika kuona jinsi mwandishi Japhet Nyang'oro alivyokuwa ameelezea matukio kwa kina.
Baada ya kusoma kwa kina na kuunganisha matukio kadhaa, hatimaye aliafikiana na muhtasari aliokuwa ameuandika wakati akiwa safe house.

Sasa aliona lazima aanzie Upanga NHC nyumba namba 41A. Alihis kuwa Afande Mwenda Lucas, alikuwa amegundua kitu hadi akaitaja nyumba hiyo kwenye ripoti yake aliyokuwa anaikusanya. Baada ya hapo angemtafuta mtu anayeitwa Luteni Frank Misanya, maana huyu alikuwa kwenye ripoti na hata Nana mke wa Afande Lucas alisema kuwa mumewe alimtaja. Japo aliona ingekuwa rahisi kwake kuweza kufuatilia watu au mtu aliyeweka kinasa sauti kwa Nana lakini alijikumbusha kuwa uzoefu unamwambia kuwa ukiwa kwenye upelelezi mgumu kama huo si vema kufuata njia rahisi maana hakuna adui aliye fundi wa mambo angependa kuacha nyayo zake kirahisi kama si mtego. Hivyo aliamua kumwacha Nana na mazingira yake kama kiporo.

* * *

Saa tisa na robo alasiri, wakati Jacob Matata anakata shauri kuanzia Upanga NHC nyumba namba 41A, Poka Kingu na yeye alikuwa kwenye hesabu zake.
“Wapelelezi ni kama Inzi tu, wanapoona kinyesi hawaachi kuzungukia hapo. Nina hakika atarudi tena kwa Nana, hivyo watatu mtakwenda nyumbani kwa marehemu Lucas Mwenda kumngoja Jacob Matata. Nina hakika baada ya kuona kile kifaa tulichomwachia Nanalungu kwa vyovyote atataka kwenda ili asubiri yeyote atakeyekwenda akabiliane nae na kuweza kutufikia. Hakuna anayeweza kukabiliana na Jacob Matata hapa kati yenu, hivyo mtakachofanya mkimuona tu ni kumfuatilia kila anapokwenda na kunipa taarifa. Nataka kujua ameweka kambi wapi. Maana sasa anatafutwa sana na vyombo vya usalama hivyo najua kuna sehemu amejizika ili isijulikane alipo.” Poka Kingu alisema kwa vijana wake ambao alikuwa amewakusanya wamsaidie kufanya kazi ya kukusanya taarifa na kufuatilia watu huku yeye akiwa amejiwekea kazi ya kung’oa visiki.


Saa tisa na robo alasiri, wakati Jacob Matata anakata shauri kuanzia Upanga NHC nyumba namba 41A, Poka Kingu na yeye alikuwa kwenye hesabu zake.
“Wapelelezi ni kama Inzi tu, wanapoona kinyesi hawaachi kuzungukia hapo. Nina hakika atarudi tena kwa Nana, hivyo watatu mtakwenda nyumbani kwa marehemu Lucas Mwenda kumngoja Jacob Matata. Nina hakika baada ya kuona kile kifaa tulichomwachia Nanalungu kwa vyovyote atataka kwenda ili asubiri yeyote atakeyekwenda akabiliane nae na kuweza kutufikia. Hakuna anayeweza kukabiliana na Jacob Matata hapa kati yenu, hivyo mtakachofanya mkimuona tu ni kumfuatilia kila anapokwenda na kunipa taarifa. Nataka kujua ameweka kambi wapi. Maana sasa anatafutwa sana na vyombo vya usalama hivyo najua kuna sehemu amejizika ili isijulikane alipo.” Poka Kingu alisema kwa vijana wake ambao alikuwa amewakusanya wamsaidie kufanya kazi ya kukusanya taarifa na kufuatilia watu huku yeye akiwa amejiwekea kazi ya kung’oa visiki.

Wakati Poka Kingu akiwa anatoa maelezo hayo, Luteni Frank Misanya na Nanalungu Bin Muhusin walikuwa wanaanza maongezi yao kwa njia ya simu.
“Naona mambo yanatunyookea!’’ Nana alisema.
“Haswa, wale vijana tuliokuwa nao siku ile tunamhoji Sabodo Sumari wote wameuawa leo!’’ Frank alisema.
“Oooh! maskini, wanaoneka walikuwa vijana wakakamvu sana. Imekuwaje, vifo vyao ni sehemu ya mkakati au janga limewafika?’’ Nana alihoji.
“Sehemu ya mkakati, Mzee aliwakabidhi kwa Jacob Matata, Jamaa kawaswaga wote!’’ Frank alisema kwa sauti baridi.
“Miye nilijua Jacob kawekewa watu makini baada ya kuwataarifu kufika pale msibani. Nilifanikiwa kumfanya ajue kuwa niko upande wake. Halafu niliona jinsi alivyonitamani. Jacob mgonjwa wa wanawake aisee, yaani katika mazingira kama yale ya msiba bado akawa ananimezea mate! Ila ni bonge la mkaka, bsi tu! Sasa mkakati hapo ni upi?’’ Nanalungu ambaye ni mke wa Inspekta Mwenda alisema.
“Ni sehemu ya kukulinda wewe Nana. Tungekosea Jacob angewahi kujua kuwa wewe ulitupa taarifa zake. Ila kwa hivi tulivyofanya Jacob Matata ataendelea kukuamini. Lakini nahisi kama Mzee hatuamini kuwa tunaweza kukabiliana na Jacob au kuna namna anataka asife sasa.” Frank Misanya alisema.
“Halafu nina ujumbe wako toka kwa mzee” Frank Misanya alisema
“Nini tena, niko msibani jamani au hamjui? Nana alisema kwa mshituko.
“Anasema umeshamaliza kazi ngumu, baada ya kuwaua Inspekta Menda na Sabodo unatakiwa upumzike. Hivyo kasema nenda kajichimbie kule Masaki kwenye nyumba uliyojengewa na Sabodo Sumari, hadi hapo utakapopewa maelekezo mengine.” Misanya aliongeza.

********

ILIPOFIKA saa kumi kasoro dakika kumi na tano alasiri wakati ambao msako dhidi yake ulikuwa umepamba moto, Jacob Matata aliingia mtaani nia yake sasa ikiwa ni kwenda Upanga NHC nyumba namba 41A. Hatimaye alifika Mzumbe University Cumpas ya Dar es salaam, akiwa katika mavazi yenye utata, ambayo si rahisi mtu kumtambua. Kwa vile alijua kuwa alikuwa anatafutwa, aliamua kubadili sana uvaaji na mwoneka wake. Kufanya isiwe rahisi kujulikana hadi atakapofikia hatma ya kisa hiki. Japo hakuwa na hakika ya kumaliza akiwa hai au la.
Alitembea taratibu, ungedhani anaelekea Regent. Lakini akaiacha hiyo barabara na kuchukua ile ya vumbi. Hapo alitembea taratiibu, hadi kwa mbali aliweza kuiona ile nyumba na 41A ya shirika la nyumba.

Alipapasa bastola yake kiunoni, huku akiendelea kutembea taratibu hadi alipokuwa amesimama kwenye mlango wa kuingilia ndani upande wa uani. Eneo la nje lilimwashiria wazi kuwa hakukuwa na mtu aliyekuwa akiishi eneo hilo. Hata hivyo sheria mojawapo ya upelelezi ni kutokuamua mambo kwa kudhani. Mara nyingi ukionacho ni tofauti na uhalisia wake, usione ukadhani.

Hivyo dakika chache baadae alikuwa ameshaingia ndani, alizunguka maeneo yote bila kuona dalili yoyote ya kuwa na mtu anaishi ndani. Alikagua sehemu ya chini kabla ya kupanda ngazi kwenda upande wa juu, maana nyumba hiyo ilikuwa na ghorofa moja. Alipanda kwa hadhari kubwa. Alifika kwenye kibaraza cha sehemu ya juu. Alianza kuangalia chumba kimoja baada ya kingine hadi alipofungua malango wa chumba cha tatu taratibu huku mapigo yake ya moyo yakienda kasi. Bastola ikiwa imara mkono wake wa kulia. Taratibu aliingia ndani. Chumba kilikuwa ukiwa huku kukiwa na mifupa ya mtu iliyokuwa imelala chini. Inaonyesha mtu huyo alikufa siku nyingi, akaoza na sasa mifupa ikawa pale chini kama mti. Jacob Matata alishangaa sana.
Kama mtu alikufa, akaoza, mwili ukaliwa na wadudu hadi sasa amebakia mifupa inamaana hakuna mpangaji mwingine kwenye ile nyumba kwa muda mrefu sana?
Ina maana hata majirani hawakutambua kuwa jirani yao alitoweka?
Ina maana majirani hao hawakusikia hata harufu ya ule mwili?
Kama hakuna mpangaji shirika limechukua hatua gani?
Kama kuna mpangaji, huyo mpangaji ni nani?

Maswali yote hayakuwa na majibu.

Tofauti na alivyopanga, saa kumi na robo jioni, Jacob Matata alikuwa amesimama nyuma ya mlango wa Afisa Mahusiano ya wateja wa Shirika la Nyumba Makao Makuu.

Alikaribishwa na mama mmoja wa makamo. Baada ya kujitambulisha mahojiano yalianza.
"Kama nilivyokutaarifu kwenye simu, kazi yangu imenifikisha nyumba namba 41A. Ningependa kujua nini unajua kuhusiana na nyumba hii hasa ukizingatia kuwa ni mali yenu. Nani mpangaji wake kwa sasa?’’ Jacob Alisema huku macho yake yakiwa katikati ya uso wa huyo mama. "

Asante, mara baada ya kunipigia nimeitisha faili linalohusiana na hiyo nyumba. Nyumba hiyo ina mpangaji wa muda mrefu sana." Aliongea yule mama huku akiwa anapekuapekua lile faili.
"Okay, je, ni nani huyo mpangaji wa muda mrefu?’’ Jacob Alihoji.
"Si utamaduni wetu kutaja majina ya wateja wetu kwa mamlaka zisizo rasmi......" Yule Afisa alisema na kukatishwa na Jacob.
"Kujua siri ndiyo kazi yangu, hivyo usijali hapa ndiyo nyumbani kwake na Mr. Siri." Jacob alisema.

“Hiyo haitowezekana kaka yangu.” Mama aliweka ngumu. “Sawa mama, nakutakia kazi njema.” Jacob Matata alisimama na kuondoka.



MWISHO WA SEASON 1 
ENDELEA KUFUATILIA SEASON 2

MWISHO





0 comments:

Post a Comment

Blog