Search This Blog

Monday 24 October 2022

PATASHIKA - 4

 

    Simulizi : Patashika

    Sehemu Ya Nne (4)







    “HELLEN, inawezekana akawa anaongea ukweli.”

    “Sijui Milka, lakini ungemwona wakati anaongea nami na Maganga tulipokuwa kwake, usingemtilia shaka. Anaoneka kujua habari zetu za utotoni vizuri sana. Sasa shida ni kuwa tutawezaje kuthibitisha akisemacho?”

    “Japokuwa amenilea na kunikuza sijawahi kumpenda Mzee Paul, kwangu hakuwa kama baba kwa kweli. Mtu katili sana. Hivyo nitafurahi sana kujua kuwa yeye siyo baba yangu mzazi. Siku hiyohiyo nitaachana na mambo ya utawa na nitakuwa huru. Halafu hii inamaanisha mimi na Maganga siyo ndugu, usikute hata mama zetu ni tofauti.”

    “Ha ha ha ha!, Milka bwana, usiniambie kuwa utafurahi kusikia Maganga si ndugu yako.”

    “Heeeh!, we Hellen, nikijua hilo mbona nguvu zote nitaelekeza kwa Maganga. Aisee! nampenda sana Maganga, na namjua vizuri sana, wala hatonisumbua kumpata yule. Sielewi kwa nini Vivian alikuwa anashindwa kumpata?”

    “Hii balaa! Ila kwa kweli Maganga hata mimi nilivyomuona siku ile nakutana nanyi pale Kijijini, alinivutia kwa kweli, ila nikahisi ni mtu na mpenzi wake kwa jinsi mlivyokuwa mmekumbatiana. Maganga kifaa kwa kweli, sema ndiyo hivyo mimi yule ni kaka yangu maana kwa namna zote ni ndugu yangu. Kwa maelezo yao wote wawili yanaonyesha kuwa Mzee Paul ni baba yangu. Ila kama ulivyosema, nimekutana na kuongea na baba yangu kwa siku moja tu katika maisha yangu ila katika siku hiyo moja tu baba yangu alikuwa tayari kuniua. Hii inaonyesha ni jinsi gani asivyonihitaji. Kiu ya heshima na ufahari wa kutaka aonekane mwema mbele ya kanisa na jamii ndiyo iliyomfanya awe tayari kuniua mimi. Kweli nikifikiria hilo suala linaniuma sana, kuwa kuna watu ambao huwatoa sadaka za kafara watu wengine ili mradi wao wapate kile wakitakacho. Milka, sijui kama nitamsamehe baba yangu Mzee Paul.”

    “Daaah!, Hellen, kweli hiyo habari imenisikitisha sana. Nikifikiria jinsi mtu niliyedhani kuwa ni baba yangu alivyompiga mama yangu na kupelekea kifo chake, halafu na hili unalonisimulia nashindwa kupata nafasi ya huyo Mzee moyoni mwangu. Hali hii yote tuliyomo ndani yake ni kwa sababu yake.”

    “Milka, hebu turudi kwenye hiki kisa tulichopo sasa. Hivi nini kilifanya hasa Mzee Paul na wale watu wengine wawili wawe radhi kuangamiza Kijiji kizima namna ile?”

    “Hellen, kwa kweli sijui hasa ni nini, ila nakumbuka nilimsikia Mzee Paul akimuuliza mtu mmoja kuwa anataka aonyeshwe Maganga alipo. Hivyo inawezekana mauaji na ukatili wote ule ilikuwa ni katika harakati za kumtafuta Maganga.”

    “Daaah!, na wale watu walikuwa ni nani, maana walivyokuwa wakifanya mambo yao ni kama nilikuwa naangalia sinema ya mapigano jinsi wale wababe wa kivita wafanyavyo! Halafu, Milka, hivi si unasema Mzee Paul alikuwa amevunjika mguu?”

    “Hilo hata mimi linanishangaza sana Hellen, maana siku kadhaa kabla ya tukio, Mzee Paul ndio alikuwa amerejea toka Hospitali ambako nilikuwa nimempeleke kwa ajili ya matibabu ya mguu. Alikuwa amevunjika mguu, hii ni kwa mujibu wa madaktari wa hospitali zote mbili, ile ya Katunguru misheni na ile ya Wilaya ya Sengerema. Sasa nashangaa jana yalipotokea yale alikuwa mzima haswa wala hakuwa na dalili yoyote ya kuonyesha kuwa alikuwa amevunjika mguu.”

    “Na wale watu na lile gari je, Milka?

    “Sijui, Hellen!”
    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Mhhh!, nahisi kuna kitu hapa Milka.”

    “Hata mimi nahisi Mzee Paul ni zaidi ya vile tulivyokuwa tunamfahamu. Japo alikuwa mtu wa Kanisa lakini matendo yake na misimamo yake mara zote haikuwa sawasawa. Halafu alikuwa akimchukulia na kumwongoza Maganga zaidi ya baba awezavyo kufanya kwa mtoto.”

    “Unamaanisha nini Milka?”

    “Mzee Paul ni mvivu sana wa kufanya kazi, lakini tofauti na wazee wengine pale Kijijini hatukuwa tunapungukiwa chakula wala sikuwahi kumsikia akilalamika juu ya upatikanaji wa mahitaji yetu yote ikiwemo karo za shule.

    Kwa vipindi tofauti nilikuwa najiuliza namna ambavyo alikuwa akipata pesa. Hakuwa na rafiki wa kusema huyu ndiye msiri wa baba. Sasa kuwaona wale watu pale Kijijini wakiwa wanachukua amri za kijeshi toka kwa Mzee Paul kunanifanya nifikirie mara mbilimbili. Hellen, unajua lile gari nililoliona limepaki pale nyumbani ni moja ya yale magari ya kifahari?”

    “Mmmmh! kwa kweli kilichonitoa Dar sasa nakiona. Ila unajua nini Milka?”

    “Mmh, niambie Hellen?”

    “Sijutii hata kidogo, nimetii kile ambacho marehemu mama yangu aliniomba nikifanye. Pia, nikifikiria sana, naona kuja kwangu ndiyo kumefanya haya yote yametokea…”

    “Kivipi Hellen kuja kwako unakuunganisha na haya yote? Maana kama ni Mzee Paul kumpiga mama lilikuwa limeshatokea sasa mbona unataka kujitwisha lawama mdogo wangu?!”

    “Hapana Milka, nimeshasema sijutii kwa lolote lililotokea, ila ninachosema ni kuwa kama nisingekuja Mzee Paul asingeenda kunining’iniza kwenye mti kule shambani. Mwasumbi asingeniona na kuja kuniokoa, na kisha utaona Mwasumbi alipata nafasi ya kuongea na mimi na Maganga kwa sababu ya lile tukio alilolifanya Mzee Paul...”

    “Hellen, kwa hiyo unaona sasa, ina maana aliyesababisha haya si wewe bali ni Mzee Paul na tamaa zake…”

    “No, Milka, Mzee Paul ana sehemu yake lakini nina sehemu yangu kubwa tu!”

    “Eeeeh!, bibie haya vyovyote vile, sasa tuko hapa. Hivi hapa ni wapi na watu hawa wana mpango gani na sisi?

    “Milka bwana, sasa unaniuliza mimi wakati wote tumejikuta hapa, ila ninachoweza kusema ni kuwa, Askofu Alphonso anahusika sana na sisi kuwa hapa, maana kabla fahamu hazijanipotea nilipokuwa kwenye ule moto ndani ya nyumba, nilimwona akitokea na kuja pale nilipokuwa. Nahisi kama niliongea maneno japo sikumbuki ni maneno gani. Inaonekana kama tuko sehemu ambayo kuna nyumba za kotazi, maana nikichungulia nje naona kama nyumba zote zinafanana. Halafu naona raia wengi hapa hasa wanaume wamevalia sare za jeshi.”

    “Daaah! ngoja tuone.” Kabla Milka hajamalizia ile kauli yake, mlango wa chumba walichokuwemo ulifunguliwa. Aliingia askari Jeshi mmoja wa kike akiwa amebeba mafurushi mawili. Hakuwasalimia, aliwarushia kila mmoja furushi moja la nguo. Kisha akawafanyia ishara wamfuate. Hakuna aliyebisha wala kuuliza, walikuwa wameshaona mengi na sasa walijikuta wako tayari kwa lolote, wakati huu hawakuwa na hakika nani alikuwa mwema au mbaya kwao. Yule askari alitembea kwa mwendo wa kiaskari japo usichana bado ulionekana dhahiri kwa jinsi nyonga zake zilivyokuwa zikinesa wakati akitembea.







    “Ingieni kwenye gari.” Alisema yule mwanajeshi wa kike. Kama mwanzo, hawakubisha waliingia. Wakati wameshaingia kwenye gari, gari lingine lililoonekana kuwa la jeshi lilifika eneo lile. Yule askari jeshi aliyekuwa kwenye gari walilopanda Hellen na Milka alipoliona lile gari lingine likiwasili, alishuka na kwenda lilipokuwa limeegeshwa. Baada ya kuongea na mtu aliyekuwa anaendesha lile gari lingine walionyesha kama kukubaliana kitu. Yule askari wa kike alienda upande wa nyuma wa gari akafungua mlango.

    “Toka nje!” Alisema. Mara akatokea binti aliyeoneka kuwa amechafuka sana. Alikuwa ni Vivian.

    “Nifuate!” Yule askari jeshi wa kike aliongea kama alivyokuwa ameongea na Hellen na Milka, hakuwa mtu wa maneno mengi. Alimwongoza Vivian hadi pale palipokuwa na gari alilokuwa amewaweka Milka na Hellen. Alimfungulia mlango, yeye aliwaona Milka na Hellen kabla wao hawajamwona, hivyo Milka na Hellen walipogeuka upande wa mlangoni walikutana na sura mbili, ya yule askari na ya Vivian. Milka alitaka kupiga kelele lakini alikutana na sura ya Vivian huku akiwa amefanya ile ishara ya kuweka kidole katikati ya mdomo kuashiria kuwa anyamaze. Hivyo Milka akaishia kufanya kama mtu aliyepotewa na kwikwi iliyokuwa imekuja kwa nguvu. Vivian akaingia ndani ya gari mlango wa nyuma wa gari aina ya Land Rover 110 ulifungwa. Dakika chache baadae gari lilitiwa moto. Zaidi ya ule mlango walioingilia, upande huo wa nyuma hakukuwa na mlango mwingine wala dirisha kwa hiyo hawakuweza kujua walikuwa wakielekea wapi. Gari hilo ambalo muungurumo wake ulionyesha kuwa lilikuwa likiendeshwa kwa fujo na kasi kubwa lilikwenda bila kusimama huku likionekana kupiga kona kadhaa. Kule nyuma walikokuwa abiria kulikuwa kimya kabisa, kwani Milka alipojaribu kuongea Vivian alimwashiria kuwa anyamaze.

    “Huyu ndiyo Hellen?” Vivian alimuuliza Milka kwa kunong’ona. Milka alitingisha kinywa kwa namna ya kukubali.

    “Ameshakusimulia walichoambiwa na Mwasumbi?” Vivian alinong’ona tena. Kama hapo awali, Milka alitingisha tena kichwa kuitikia.

    “Usimwambie mtu yeyote aliyokusimulia Mwasumbi, wakijua tu kuwa unajua wanakuua na utasababisha na Maganga auwawe.” Milka alinong’ona huku akionyesha msisitizo kwa macho, mdomo na mikono yake.

    “Maganga na Mwasumbi wako wapi?” Hatimaye Milka alihoji kwa kunong’ona.

    “Mwasumbi au Askofu Alphonso wa bandia nimemwacha yuko anapambana nao. Maganga sijui yuko wapi.” Vivian alisema huku akionyesha kuwa hakuwa na hamu ya kuongea tena.

    “Na…”

    “Shiiiiii!, tutaongea tukipata nafasi na tukiendelea kuwa hai.” Vivian alikatisha swali la Hellen. Vivian alijua kuwa walikuwa na mengi ya kuongea lakini haukuwa wakati muafaka kufanya hivyo. Hata hivyo maneno machache aliyoongea Vivian yaliwafanya Milka na Hellen waweze kuunganisha mambo machache juu ya mlolongo mrefu wa maswali waliyokuwa nayo. Kutokana na maelezo hayo mafupi ya Vivia, ikawa dhahiri vichwani mwa Hellen na Milka kuwa Mwasumbi ndiye aliyekuwa amewaokoa, kama Mwasumbi ndiye aliyejifanya kuwa Askofu Alphonso wa bandia. Na sasa imani yao kwa Mwasumbi ikaimarika zaidi na kuanza kutoa nafasi ya kuyaamini yote ambayo walipata kuyasikia toka kwa Mwasumbi.

    Ghafla walisikia gari likipiga honi na kisha baada ya dakika chache walisikia kitu kama lango kubwa likiburuzwa. Baada ya ukimya kidogo, gari liliingizwa na baadaye wakasikia lango likiburuzwa tena. Walisikia mlango wa upande wa dereva wa lile gari ukifunguliwa, kisha ukafungwa. Hapo zikasikika hatua za watu wakiwa wanatembea. Baadaye wakasikia kama mlio wa geti likiwa linafunguliwa. Hatimaye mlango wa gari walilokuwemo ulifunguliwa. Yule mwanajeshi wa kike pamoja na wanaume wengine wawili walikuwa wamesimama. Waliangaliana kwa muda na macho ya kina Vivian, Milka na Hellen.

    “Shukeni!” Alisema yule mwanajeshi wa kike. Hakuna aliyebisha, alianza Vivian, akafuatia Hellen kisha Milka.

    “Mfuateni huyo!” Alisema yule mwanajeshi wa kike huku akionyesha kwa mmoja wa wale wanaume. Wasichana wale watatu wakaingizwa ndani. Ilikuwa nyumba nzuri ya kisasa iliyokuwa na kila kitu ndani. Hawakuweza kuona upande wa nje maana sehemu waliyokuwa wameshukia ilikuwa kwa ndani, sehemu ya kuegeshea gari.

    “Haya ndiyo yatakuwa makao yenu ya muda wakati tukisubiri maelekezo mengine kuwahusu. Mtapata huduma zote muhimu, na mtapewa chakula kizuri, msisite kutoa mapendekezo ya chakula mkitakacho.” Alisema yule mwanajeshi wa kike. Huku akiwa amemkumbatia mmoja wa wale wanaume. Wasichana watatu hawakuwa na la kujibu. Yule mwanajeshi wa kike na yule mwanaume hawakuishia kukumbatiana tu wakaanza kunyonyana ndimi. Milka, Hellen na Vivian wakabaki wamesimama wanashangaa. Wawili hao hawakuishia hapo wakaanza kufanya ile michezo yao ya kimahaba yenye kutia ashki. Walipozidiwa wakavutana hadi chumba kingine huko miguno ya mahaba na makelele ya kudai na kuridhika vilisikika.



    ***********http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    Jenerali Mmbando au JM kama vijana wake wa jeshi walivyozoea kumwita alikuwa ofisini kwake asubuhi hii. Tofauti na siku nyingine, leo alikuwa amevaa kiraia jambo ambalo liliwafanya MPs wengi wabaki na maswali ya kujiuliza kuwa kulikoni, haikuwa kawaida yake kuonekana akiwa hajavaa sare za jeshi saa za kazi. Muda pekee ambao alionekana akiwa hajavaa sare za kazi ni kuanzia saa mbili na nusu usiku hadi saa nne na nusu, muda ambao huwa kwenye chumba maalum cha mazoezi ya mbinu za kulinda mwili na kushambulia kwa kutumia mwili. Muda huo alivalia mavazi yake maalum kwa ajili ya mchezo huo na hujihusisha kikamilifu katika kuwaongezea uzoefu askari maalum walioko kwenye kambi aliyokuwa akiishi. Akishatoka kwenye hayo mazoezi huvaa tena mavazi yake ya kijeshi na kuelekea ilipo maktaba na hujifukia huko kusoma vitabu na majarida mbalimbali. Tofauti na wakuu wengine wa kijeshi waliokuwa wamepewa nyumba za kifahari uraiani na kuishi maisha ya kifahari, Jenerali Mmbando hakutaka kuishi namna hiyo. Hakuwa na mke, hakuwa na mtoto, hakuwa akikaa na ndugu yeyote. Yeye mwenyewe ndiyo alikuwa kila kitu kwake. Mtu pekee ambaye waliwahi kuishi pamoja kwa muda mrefu alikuwa ni msichana wa kazi aliyekuwa akiitwa Sophia. Aliishi na msichana huyo kwa miaka tisa hadi pale siku moja alipotoweka na hakuwahi kuonekana tena. Kuondoka kwa Sophia maishani mwake kulimfanya asiwe na mpango wa kuishi na mtu yeyote. Mambo mawili ambayo kila alipokuwa akifikiria kuhusu Sophia yalimfanya asiwe na mpango wa kuishi na mtu yeyote. Moja ni vile alivyokuwa amemuamini Sophia na kumfanya kuwa mtu wake wa karibu sana. Hawakuwa wakiishi tena kama bosi na mfanyakazi wa ndani bali waliishia kuishi kama marafiki wakubwa, hivyo hakutegemea Sophia angeweza kuondoka kwa staili aliyoondoka. Katika muda wote alioishi na Sophia, Jenerali Mmbando alikuwa amemfundisha Sophia mambo ambayo yalimfanya kuwa mpiganaji wa kutisha. Alianza kwenda naye mazoezi, kisha wakawa marafiki katika mazoezi. Ile kasumba iliozoeleka miongoni mwa watu kuwa wasichana ni wepesi sana katika kujifunza ilithibitika kwa Jenerali Mmbando kwani kasi ya Sophia kuchukua mazoezi na kwenda mbele zaidi ilimshangaza sana.

    “Sikiliza Sophia, hivi vitu unajifunza ni kwa ajili ya kujilinda mwili wako pale inapolazimika. Kwa namna yoyote usitumie kuwatisha watu wala kuharibu amani ya sehemu yoyote.” Ilikuwa ni sehemu ya onyo ambalo Jenerali Mmbando alikuwa akimpa Sophia kila mara walipokuwa wakimaliza hatua fulani ya mafunzo na kuingia kwenye hatua nyingine. Onyo hilo lilimfanya msichana Sophia kuwa mpole zaidi, alikuwa na tabia ya upole, ila upole wake uliongezeka mara dufu kwa kadiri alivyokuwa akizama kwenye mazoezi na mafunzo aliyokuwa akipewa na Jenerali Mmbando.

    Jambo la pili lilomfanya jenerali Mmbando kujiapiza kutokuishi na mtu au kutoa mafunzo kwa raia ni tetesi ambazo alikuja kuzipata miaka michache baadaye kuhusu Sophia. Inasemekana wakuu wachache wa jeshi walikuwa wametengeneza timu fulani ya siri kwa ajili ya kutafuta taarifa za siri kwa manufaa yao binafsi. Hilo lilikuwa likijadiliwa ndani ya jeshi lakini kilichomshangaza ni kuwa mmoja kati wa watu wa juu katika kuendesha operesheni hiyo ya siri alikuwemo msichana Sophia.

    Hivyo asubuhi hii alikuwa katika nguo za kiraia, ndani ya ofisi yake. Hakuwa na faili lolote zaidi ya kompyuta laptop yake na CD kadhaaa. Aliiweka kompyuta hiyo juu ya meza kisha akaanza kuangalia kwa makini kilichokuwa kikitokea. Aliendelea kufanya hivyo kwa saa kadhaa huku kadri muda ulivyokuwa ukitoweka moshi wa Sigara uliendelea kukijaza chumba huku Sigara kadhaa zikiwa zimeshateketea.



    * * *



    Siku hii nyingine, Makamanda hawa walikuwa katika mkutano wa siri kwenye moja ya nyumba za siri za jeshi. Walikuwa watu watatu, wote wakiwa na vyeo vya juu sana katika jeshi. Katika kikao hicho, Jenerali Mmbando alitakiwa kutoa taarifa moja nyeti kwa Mkuu wa Majeshi ambaye alikuwa ameandamana na Mzee mmoja wa makamo. Kikao kilikuwa kimepamba moto.

    “Ukweli ni kuwa miaka zaidi ya ishirini iliyopita ilikuwa ya wasiwasi mkubwa na giza kwa upande wangu. Kama mnavyofahamu kuwa kazi ya kuandaa operesheni niliiweka chini ya KAPTEN, ambaye nilimwondoa kwenye shughuli zote za kawaida ili awe na nafasi nzuri ya kushughulikia hilo. Kutokana na sababu za kiufundi, baada ya tukio la kulipuliwa ile Wodi ya Wazazi ya Hospitali ya Bugando Mwanza, KAPTEN alipendekeza kuwachukua, Luteni Mwasumbi na Luteni Paul.





    Hasa kwa vile wao walkuwa wanahusika na wale watoto waliozaliwa, huku dalili za awali zikionyesha kuwa yule mtoto wa kiume angeweza kuwa amewekewa kitu na yule Daktari wa Kiyahudi. Uchunguzi wa awali ulionyesha kuwa chochote alichowekewa Maganga yule mtoto wa Paul ingechukua miaka zaidi ya ishirini na minane kuweza kuonekana na hakukuwa na namna nyingine ya kusoma alama hizo mwilini mwake. Kutokana na unyeti wa jambo hili na utaratibu wake kuwa mrefu sana sikutaka kuwa na mawasiliano ya karibu sana na KAPTEN, ili kutoamsha maswali vichwani mwa watu. Nasema imekuwa miaka migumu sana kwa sababu miaka saba baadaye nilipoteza mawasiliano na KAPTEN, si hilo tu, nilipoteza hata nyendo zake na mahali alipokuwa. Nadhani mnaelewa kuwa kupoteza nyendo na mawasiliano na KAPTEN ilimaanisha kupoteza mawasiliano na Paul na Mwasumbi ambao sasa ndiyo walikuwa kwenye uwanja wa matukio. Ni wazi kuwa KAPTEN atakuwa alipata watu au mtu ambao watakuwa wamemwahidi maslahi makubwa na hivyo kwa sasa anawafanyia kazi. Ili kuimarisha timu yake, ndipo KAPTEN akamchukua Sophia, nadhani mkuu unaelewa namaanisha nini, nikiongelea Sophia.

    Pamoja na jitihada zote za makusudi, lakini sikuwa nimefanikiwa kujua hawa watu wako wapi hadi wiki chache zilizopita nilipopata mawasiliano ya Luteni Mwasumbi. Mwasumbi alinieleza kuwa kwa miaka yote hiyo wamekuwa wakifuatilia kwa karibu sana maisha ya kijana Maganga. Mwasumbi aliniambia kuwa Maganga ana alama mwilini mwake ambayo alichorwa na yule Daktari wa Kiyahudi wakati wa kuzaliwa, alama hiyo inaonyesha mahali ambapo Myahudi huyo alikuwa ameficha karatasi zilizokuwa na kanuni ya kutengenezea silaha ya kudhibiti bomu la Atomic. Mwasumbi alinitaarifu kuwa ilikuwa imebaki wiki moja tu ambapo KAPTEN na kundi lake wangeenda kwenye Kijiji ambacho Paul alikuwa akimlea Maganga ili kumchukua na kufanya utaratibu wa kuzisoma hizo alama mwilini mwake kisha kuendesha operesheni ya kuzichukua karatasi hizo. Sikuwa na hiari, maana sikuwa na muda, ilibidi nimuamini Mwasumbi na kumwamuru kumtorosha Maganga kabla KAPTEN na kundi lake hawajafika Kijijini pale. Niliona heri nusu shari kuliko shari kamili, kama nisingekubaliana na Mwasumbi nisingekuwa na njia mbadala ya kuweza kumfikia huyo Maganga kwa muda nilikuwa nao mkononi. Mwasumbi alifanikiwa kumchukua Maganga siku moja kabla vijana wa KAPTEN na kumpeleka kwenye kituo chetu maalum cha uchunguzi. Kwa msaada mkubwa wa wataalamu wetu tuliweza kufanikiwa kujua eneo ambapo karatasi hizo zimehifadhiwa. Hivyo nikatuma timu ya wataalamu ili kwenda kuangalia uwezekano wa kuzichukua. Katika hilo kundi la wataalamu hakuna aliyekuwa anajua walikuwa wanakwenda kuchukua nini. Nasikitika kusema kati ya vijana ishirini waliokwenda, walirudi vijana watatu tu wakiwa hai. Wengine wote walifia eneo la tukio.” Jenerali Mmbando aliweka tuo na kuruhusu mate kupita kooni.

    “Ulituma watu wa namna gani?” Aliuliza yule Mzee aliyetambulishwa kama Mtaalamu wa Ufundi.

    “Nilichukua vijana sita kutoka AK218, wanne toka CA10 na waliobaki walikuwa Makomandoo toka mbegu maalumu.” Jenerali Mmbando alieleza.

    “Khaaaah!, haiwezekani. Watu uliowasema wana uwezo wa kupambana na jeshi kubwa sana sasa ilikuwaje wakabaki watatu tu?” Mkuu wa Majeshi aling’aka.

    “Labda kama walikuwa wanapambana na mizimu!” Aliongeza yule Mzee Mtaalamu wa Ufundi.

    “Myahudi huyo amezihifadhi hizo karatasi ndani ya pango lillilokaa kama shimo. Pango hilo liko kwenye pori moja, kwa mujibu wa video camera ambazo tulikuwa tumewafunga wale vijana walitumbukia pangoni mule, ni dhahiri kuwa Myahudi huyo ameamua kutumia kila alichonacho kuhakikisha karatasi hizo haziangukii katika mikono asiyoitaka. Video camera zinaonyesha kuwa ndani ya shimo hilo kuna joka kubwa sana, joka hilo ni mbegu ya kipekee sana, lina kasi na shabaha ya ajabu. Hivyo yeyote anayetaka kuzifikia hizo karatasi ni lazima kuliangamiza hilo joka. Mnaweza jiuliza na kushangaa kuwa inawezekanaje ikawa shida kuua nyoka mmoja. Hakika kuua lile joka si kazi ngumu ila kuna kitu cha ziada, kuta za pango hilo zimechomekwa mashine fulani kuzunguka shimo lote, mashine hizo hufyatua mishale kutokea pande zote na mishale hiyo husambaa kulenga pande zote za shimo. Inavyoonyesha ni kuwa chuma kinachotengeneza ncha ya mishale hiyo ina madini maalum ambayo husukumana na mfumo wa mwili wa yule nyoka na hivyo kila ile mishale inapokuwa inamkaribia yule nyoka hubadilisha mwelekeo. Mashine hizo, huamshwa na mtikisiko wa moyo wa binadamu. Hivyo kuna umbali fulani ambao mashine hizo mfumo wake huamshwa na mapigo ya moyo wa binadamu yaliyo jirani na hizo mashine. Moja ikishafyatua, na nyingine huendelea kufyatua michale hiyo midogo kama misumari ya inchi mbili. Wataalamu wanadai kuwa inawezekana mishale hiyo ikawa na sumu maana video zilionyesha kuwa, haimchukui mtu dakika nyingi kuendelea kuwa hai mara baada ya kuchomwa au hata kukwaruzwa na mishale hiyo. Kwa ilivyo sasa hakuna namna mtu anaweza kuingia akapona. Baada ya kugundua hilo tukafikiria kutumia mabomu, ili kuharibu hizo mashine na kuliua lile joka. Hapo tena tukakabiliana na kikwazo kingine. Kwa mujibu wa zile video camera walizokuwa wamevaa wale watu walioingia shimoni na baadae kuuawa ama na ile mishale au lile joka, inaonyesha kuwa hizo karatasi ziko kwenye boksi ambalo kuta zake zimetengenezwa kwa baruti maalum ambayo italipuka mara ipatapo moto au joto kali sana. Hivyo kupiga bomu kuna maanisha kuziteketeza zile karatasi.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Hivyo baada ya harakati hizo kwa wiki nzima iliyopita, tumeamua kuwa wapole na kwenda taratibu. Ni wazi kuwa Myahudi huyo kaamua kutumia ubunifu wa hali ya juu kuweza kufanya hivyo, haijulikani kama kafanya mwenyewe au kasaidiwa na Wayahudi wenzie, maana kinachotushangaza ni jinsi mtu ambaye ni Daktari kuweza kufanya ufundi wa namna ile. Kwa hali ya siasa ilivyo Duniani kwa sasa, hasa kwa upande wa mahusiano ya Israeli na nchi za Kiarabu iko wazi kuwa Wayahudi wanajua kuwa kuendelea kuishi kwao hapa duniani haitakiwi kuwa hiari bali lazima. Wamejivika umiliki wa siri muhimu na ujuzi ambao Dunia nzima inabidi iende nao kwa makini. Nadhani mnaelewa kuwa Marekani mara zote imekuwa upande wa Wayahudi kwa kila jambo, na siri ni moja tu kuwa katika zile silaha tatu ambazo Marekani inajivunia kuwa nazo zote zimebuniwa na Wayahudi, na inasemekana watu hao kwa kila silaha kali wanayobuni wanatengeneza na Silaha mbadala wa kuidhibiti. Kinachofanya Marekani na mataifa makubwa washindwe kuwatowesha hawa Wayahudi ni hii mbinu yao ya kuficha hizo silaha mbadala. Kanuni ya silaha mbadala hukabidhiwa kwa Myahudi asiyejulikana aliyeko sehemu isiyodhaniwa wala kufikiriwa Duniani. Kwa hivyo huwezi kujua nani salama na nani hatari. Mara nyingine binafsi simlaumu Nyerere kwa maamuzi aliyoyachukua, hawa watu ni hatari sana." Jenerali Mmbando alielezea kwa makini na utaratibu mkubwa.

    “Mmmmh!, hii kitu imekaa vibaya sana makamanda, kabla sijauliza maswali ya ufafanuzi hebu tuambie una mkakati gani kuhakikisha tunaweza kuzifikia hizo karatasi kabla ya KAPTEN na wowote walio nyuma yake, maana wasiwasi alionao Mkuu wa Nchi, ni kama zikiangukia mikononi mwa watu wasio salama, amani ya Dunia inaweza vurugika ndani ya miezi michache na kushuhudia mauaji ya kutisha. Lazima ieleweke kuwa kwa hali ilivyo duniani kwa sasa, ni vema kukawa na nchi zenye nguvu kuliko nchi nyingine. Hii inaweka usawa duniani, na nchi zenye nguvu ndizo ziwe na hasara kubwa pindi amani ya dunia ikipotea. Ikitokea kuwa uwezo wa kijeshi ukaangukia mikononi mwa nchi ambayo haina hasara kubwa kwa kupotea kwa amani duniani, au nchi ndogondogo tu isiyo na uongozi imara ikapata umiliki wa silaha hizi za kutisha lazima tujue kuwa dunia haitokalika tena. Sasa hebu tuambie unafanya nini ili kuhakikisha tunafanikiwa?”

    Mkuu wa majeshi aliuliza huku akimwangalia Jenerali Mmbando na yule Mzee Mtaalamu wa Ufundi aliyeonekana kuwa na umri mkubwa.

    “Kuna mambo matatu hapa; kwanza ni Mwasumbi, ninaamini bado anaweza kuwa na namna ya kunisaidia kufikia mwisho wa suala hili, pili Maganga wakati wanaendelea kumpa mafunzo ya kujihami na mbinu za mapigano, wataalamu waendelee kuuchunguza mwili wake kuona kama kuna lolote linalohusiana na namna ya kutuwezesha kuzichukua zile karatasi, tatu nataka kujua KAPTEN yuko katika hatua gani juu ya hili, maana kwa sasa nina kila sababu ya kumwita muasi, labda kama wewe mkuu una taarifa mbadala, maana wewe ndiye unajua karibu kila jambo ndani ya jeshi. Najua na yeye anazitafuta hizo karatasi, kwa hivyo nataka nijue ana taarifa gani, kwa vyovyote tutakuwa tumemvuruga sana kwa kitendo cha kumchukua Maganga. Nataka kujua kama tofauti na Maganga ana mtu yeyote ambaye huenda anaweza kuwa na alama nyingine mwilini kama alivyokuwa Maganga. Maana ikumbukwe kuwa wakati wa ule usiku ambao ile wodi ya kujifungulia inalipuliwa kulizaliwa watoto wengi, sasa inawezekana yule Myahudi aliamua kutawanya taarifa kwa watoto tofauti. Tatu, nataka kujua Paul yuko wapi na anajua nini kuhusu Maganga, maana yeye ndiye amekuwa kama mzazi wa Maganga kwa miaka yote hiyo, lakini lengo kuu ikiwa ni kusubiri wakati wa kuweza kuzipata taarifa toka mwilini mwa Maganga. Kama ujuavyo kuwa wataalamu wamebaini kuwa kabla ya wiki ile iliyokusudiwa isingewezekana kusizoma zile alama na herufi zilizokuwa mwilini mwa Maganga. Hivyo tulimchukua kwa wakati muafaka maana matumizi yake ndiyo yalikuwa yamewadia." Alisema Jenerali Mmbando taratibu na kwa uhakika. Mkuu wa Majeshi alimwangalia Jenerali Mmbando, kisha akamgeukia yule Mzee ambaye yeye alimtambulisha kama Mtaalamu wa Ufundi, alimwangalia kwa ule mtindo wa kama anamwuliza una lolote.

    “Asante kijana wangu!”

    “Kijana wako? Mkuu wa Majeshi unamwita kijana wako? Mbona siwaelewi?” Jenerali Mmbando alihamaki mara baada ya kumsikia yule Mzee, Mtaalamu wa Ufundi akimwita Mkuu wa Majeshi - kijana wangu.

    "Jenarali, achana na hilo, niachie mimi, haya tuendelee.” Mkuu wa Majeshi alimtuliza Mmbando, ambaye baada ya kuambiwa hivyo na mkuu wake akatulia na kushusha pumzi ndefu.

    “Kwa nini unahisi kuwa Mwasumbi anaweza kuwa na taarifa za ziada dhidi ya Maganga? Je, unahisi KAPTEN na Paul bado wako shirika? Unadhani nani anaweza kuwa nyuma ya KAPTEN, namaanisha nchi gani?” Aliuliza yule Mzee kwa sauti ya kutetemeka.





    “Siku ile wakati Paul akiliandaa kundi lake kwenda Kijijini kwa ajili ya kumchukua Maganga, nilimsihi sana Mwasumbi aondoke kwa sababu alikuwa ameshafanya alichotakiwa kufanya.” Mmbando alianza kujibu taratibu. Kisha akaendelea.

    “Lakini alikataa kwa madai kuwa kuna mambo alitakiwa kuyaweka sawa. Tulivutana sana, maana sikutaka aonane na Paul au KAPTEN kwa ajili ya usalama wake na operesheni kwa ujumla, lakini hata hivyo alikataa akidai ni kwa faida ya nchi na damu yake pia. Nilipomtaka kufafanua hilo akaniambia, next time. Kwa hivyo ninahisi kuna la ziada. Ila hakuwa na muda wa kunieleza na alionekana kutokuwa mtu aliyetulia. Pia, labda niseme hili linaweza kuwa la muhimu, Maganga ni mtoto wa damu wa Mwasumbi.

    Kapteni na Mwasumbi bado wana mawasiliano, kwa mujibu wa Mwasumbi, mmoja kati ya vijana waliokuwa kwenye gari lililoenda kumchukua Maganga na Paul pale Kijijini lilikuwa la kijana wa KAPTEN, Mwasumbi aliweza kumtambua. Hivyo kwa vyovyote vile Paul yuko na KAPTEN. Paul ni mpiganaji mzuri sana ila hawezi kuwa na kundi la kuendesha operesheni, kwa vyovyote, KAPTEN alipewa tenda na akamshirikisha Paul na Sophia.

    Na kuhusu ni nani anaweza kuwa anahusika katika kuwatumia KAPTEN na kundi lake hapo naweza kuihusisha Japan. Utakumbuka ile miaka baada ya Nyerere kuwatimua Wayahudi kwa sababu za kisiasa. Lakini jeshini tunajua kuwa hii sababu ya kuwepo hizi karatasi hapa nchini ilikuwa sababu kuu, China, Japan na Urusi zilijisogeza karibu sana na Nyerere. Usiku ule kabla ile wodi haijalipuliwa na yule Daktari wa Kiyahudi kuuawa kama walivyodai japo sasa tunajua kuwa yupo hai, balozi wa Japan alikuwa ameomba kwenda kutembelea Hospitali ya Bugando. Balozi huyo aliweka wazi kuwa yeye na timu yake walikuwa wamepanga kwenda kwenye wodi ya watoto. Mnakumbuka jinsi ile ndege ya kutisha ya Japani ilivyokuwa imekuja na watu wa kazi, ni wazi kuwa walikuwa wanalenga kwenda kumchukua yule Daktari wa Kiyahudi. Nadhani kwa namna moja ama nyingine taarifa za kijasusi zilitembea haraka zaidi na hivyo Daktari yule akachukuliwa na kusingiziwa kufa. Hivyo tangu hapo Japan imekuwa mstari wa mbele kuhusu suala hili na nadhani kuanzia hapo walianza upelelezi wao kwa kasi zaidi.

    Itakumbukwa kuwa hadi sasa, Japan ndiyo nchi pekee ambayo imewahi kupigwa kwa bomu la Atomic, wanajua machungu na madhara ya bomu hilo kuliko nchi yoyote. Na itakuwa shangwe kwa nchi yao kusikia kuwa nchi yao ina silaha ya kuweza kuwakinga na bomu la Atomic." Jenerali Mmbando alisema huku akionyesha kuwa amechoka kutoa maelezo.

    “Sikiliza Jenerali, hili suala ni nyeti mno kuweza kuchukuliwa kwa mzaha, maana madhara yake yanaweza kusababisha dunia nzima kutoweka, sasa ninachotaka kusema ni kuwa, fanya mambo yako ukijua kuwa huna nafasi ya kufanya mzaha hata kidogo. Pia, ukae ukijua, mimi na Mkuu wa Nchi, tunalifuatilia suala hili kwa makini sana. Tunajua kuwa majasusi wa Nchi za Magharibi wako hapa nao wanahitaji sana hizo karatasi, tena wao wanazihitaji kwa udi na uvumba. Hivyo uyafanyayo yafanye kwa kasi na usahihi mkubwa. Ukihitaji msaada wowote usisite kutuambia. Ila nina ushauri kwako, fikiria kumwangamiza Mwasumbi, kama kweli Maganga ni mwanae na kuna mambo anayahusisha na damu yake, basi huyo mtu si salama kabisa katika hii operesheni. Damu nzito kuliko maji, heri nusu shari kuliko shari kamili. Mmalize Mwasumbi. Labda la mwisho ambalo ningependa ufafanuzi kidogo na kutaka kujua kwa vipi unamhusisha Sophia na KAPTEN?” Mkuu wa Majeshi alimalizia maelezo yake kwa swali.

    “Kuna siku KAPTEN alikwenda Hospitali ya Bugando kuchunguza mambo fulani ayajuayo yeye, mkanda wa camera wa siku hiyo unamwonyesha akiwa na Sophia. Si hiyo tu, kuna wakati mwingine yeye na vijana wake walivamia nyumba moja iliyokuwa ikikaliwa na Majasusi wa Kihindi, camera ya ulinzi pia, inamwonyesha Sophia na KAPTEN wakiwauwa majasusi hao huku wote wawili wakiwa wamevalia Sare za Jeshi. Na kila Sophia alipotaka kuua alimrushia mtu ua jekundu. Mara kadhaa KAPTEN alisikika akimwita Sophia kwa jina la UA JEKUNDU." Jenerali Mmbando alieleza huku akikabidhi faili la maelezo yake mkononi kwa Mkuu wa Majeshi, ambaye alilikabidhi kwa yule Mzee, Mtaalamu wa Ufundi.

    “Kwa zaidi ya miaka 40, huyu ndiye amekuwa mtunza siri mkuu wa jeshi letu, siri ambazo hazitakiwi kujulikana na wakuu wengine ndani ya jeshi, huhifadhiwa na huyu Mzee. Hajulikani sana na watu lakini kila Mkuu wa Jeshi, mpya anapokuja lazima Rais amtambulishe kwa huyu mtu na kila Rais mpya akija lazima Mkuu wa Majeshi amtambulishe kwa huyu Mzee. Hivyo jisikie salama kabisa hili faili kuwa mikononi mwake. Na baada ya hiki kikao huwezi kumwona tena labda kama nitamhitaji.” Mkuu wa Majeshi alisema. Baada ya hapo yalifuata mazungumzo ya kawaida na vicheko vya hapa na pale.



    *************

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    MAGANGA ALIJIANGALIA TENA, hakuamini kuwa ule ulikuwa ni mwili wake kwa jinsi ulivyokuwa umeharibika kwa mikwaruzo na usugu uliokuwa umetokea mara. Alijiangalia mikono yake, ilikuwa kama ya wale waponda kokoto aliyekuwa kwenye kazi hiyo kwa miaka mingi, aliangalia vidole vyake, akaviinua, akavichezesha, vikatoa mlio kama wa mti uliovunjwa, vilikuwa vimekakamaa sana. Alipojiangalia miguuni hakutaka kukubali kuwa ni yeye, alipoangalia nyayo za miguu yake akasahau kuwa alikuwa yeye lakini alipojiangalia kwenye kioo kilichokuwa mle bafuni alikutana na sura yake ambayo ilimthibitishia alikuwa bado ni Maganga, Maganga Paul au Maganga Mwasumbi, hakuwa na hakika ni jina gani la pili ajipe. Hakuwa na namna ya kuthibitisha, ila jambo moja alikuwa na hakika nalo, yeye alikuwa Maganga. Alifungulia maji ya bomba na kuyaruhusu yapite mwilini kwake, aliyaacha kwa muda huku akiwa anapumua taratibu akisikiliza jinsi yale maji yalivyokuwa yakitonesha majeraha yaliyotokana na kuchubuliwa na miti na mawe wakati akiwa kwenye kile kilichoitwa ‘Mafunzo.’

    Mafunzo, kama wenyewe walivyoyaita na alivyoambiwa na Askofu Alphonso kwa njia ya ujumbe uliokuwa kwenye ile karatasi siku ya kwanza alipoingia humo ndani yalikuwa yamemfanya awe mtu tofauti kabisa. Zilikuwa zimepita siku nyingi tangu aingie kwenye hiyo himaya, kwa akili yake alikadiria kuwa zingekuwa zimeshapita siku zaidi ya arobaini. Kutoka na mambo yalikuwa yakifanyika hapo, Maganga alikuwa ameshajikinai, hakuwa anajali tena kuhusu maisha yake wala kesho, hakuwa na haja yoyote ya kujua majibu ya maswali mengi aliyokuwa nayo kichwani wiki ya kwanza aliyokuwa ndani ya hiyo himaya.

    Hakuwa anajua chochote katika eneo hilo zaidi ya hicho chumba alichokuwemo na kuwa usiku wote ulitumika kwa ajili ya mazoezi ambayo aliyafanya gizani na watu asiowajua, wasio na huruma wala utu. Watu waliokuwa wakifanya vitendo zaidi kuliko kuongea. Watu waliojua kutoa amri na kusimamia utekelezaji wake.

    Mchana kuna watu walikuwa wakija kuufanyia uchunguzi mwili wake, Maganga hakujua walikuwa wakitafuta nini mwilini mwake, lakini ilikuwa wazi kuwa kile walichokuwa wakikitafuta kilikuwa na umuhimu mzito sana, maana aliwaona jinsi walivyokuwa wakitumia vifaa vya kisasa na walionekana kuwa walikuwa watu wenye ujuzi mkubwa katika walichokuwa wakikifanya. Walitumia saa nyingi katika kuupekua mwili wake, mwili ambao usiku ulikuwa ukichubuliwa kwa maumivu ya mazoezi na mazingira ya mazoezi hayo, mchana ulikuwa ukitomaswa tomaswa na kuminywa minywa na watu wengine walioonekana kutafuta kitu toka mwilini mwake. Wakati mwingine walichukua damu yake na kuifanyia uchunguzi mkubwa. Waliulizana wakajibizana, wakakubaliana, wakabishana, wakakataliana ili mradi tu ulikuwa uchunguzi ambao ulileta kero kubwa kwa Maganga ambaye alikuwa akihitaji kupumzika kwa ajili ya mikiki mikiki ya usiku.

    Kitu kimoja tu ambacho alishindwa kuamua kama achukie au kukifurahia ni uwezo wake wa kufanya mambo fulani fulani ulikuwa umeshabadilika kwa kiasi kikubwa. Alikuwa na uwezo wa kukimbia kwa namna ya ajabu sana, alikuwa na uwezo wa kupigana kwa namna ambayo yeye mwenyewe hakuelewa ni ipi maana haya kuwa mafunzo rasmi ila alijikuta akilazimika kuyajua kutokana na mazingira yenyewe ya mafunzo na waalimu walivyokuwa. Hakuelewa kama ndiyo kuchanganyikiwa au la, alijikuta ana uwezo wa kuhisi kwa kiwango cha juu sana. Kwa vile mafunzo yake kwa sehemu kubwa yalifanyika gizani, ilibidi ajifunze kutegemea hisia zake badala ya macho kumwezesha kuona. Hivyo akiwa gizani hisia zake zilikuwa na uwezo wa kuona sawa na anavyotumia macho akiwa nuruni. Hofu kwake ilikuwa msamiati, ila kilichochukua nafasi badala ya hofu ni kutotaka kukosea maagizo, hakuwa anaogopa ila badala yake hakuwa anataka kukosea maana kukosea kulimsababisha apate kipigo kikali kwa mwalimu yeyote aliyekuwa anamfundisha siku hiyo.





    Wakati wanaingia kwenye nyumba, Vivian, Hellen na Milka walikuwa wamechoka sana, hakuna kitu walikuwa wakikihitaji zaidi ya kupumzika. Ndiyo maana miili yao haikuhisi chochote walipoona na kusikia makelele ya yule askari wa kike alivyokuwa akifanya mapenzi na yule mwanamume waliyemkuta kwenye hiyo nyumba. Wangehisi vipi wakati miili yao na akili vilikuwa taabani kwa uchovu. Vivian mara ya mwisho kulala usingizi wa maana ilikuwa ni wakati anamuuguza mama yake Maganga Hospitali ya Sengerema.

    Lakini tangu mwanamke yule alipofariki, mambo mengi yalitokea na tangu hapo hakuwa amepata nafasi ya kupumzika. Hivyo mwili wake na akili yake vilikuwa vimechoka sana. Milka ni kama ilivyokuwa kwa Vivian na Hellen. Walikuwa na hamu ya kusimuliana yaliyowakuta na kujua kwa nini walikuwa mahali pale lakini uchovu wa akili na mwili havikuwaruhusu kufanya hivyo.

    Baada ya kila mtu kuwa amekabidhiwa kitanda chake, waliletewa chakula kizuri sana, wakala. Kilichofuata kikawa ni kukalala usingizi. Walilala hadi wakachoka. Alikuwa ni Milka aliyefanya jaribio la kutoka chumbani kwake, baada ya kuwa ameoga na kubadilisha nguo alizokuwa amevaa. Lile furushi walilokuwa wamepewa kila mmoja yeye na Hellen lilikuwa na nguo, hivyo alichagua moja iliyomuenea vemaa akavaa. Baadaye ndipo akajaribu kitasa cha mlango, ulikuwa wazi. Kwanza alianza kutembea kwa wasiwasi, lakini alipogundua kuwa ilionekana hakukuwa na mtu alitembea kwa kawaida. Hakujua alikuwa akienda wapi maana nyumba hiyo ilikuwa na vibaraza vingi na vyumba vingi. Hakuwa na jingine zaidi ya kutaka kuonana na Vivian na Hellen, alijua wazi kuwa wangekuwa kwenye moja ya vyumba vilivyokuwa kwenye hiyo nyumba. Hivyo taratibu akaanza kujaribu kitasa cha kila mlango, ni katika kufanya hivyo mlango mmoja ulifunguka. Akachungulia ndani, macho yake yalikutana na yule mwanajeshi wa kike na jamaa yake wakiwa fofofo huku wakiwa kama walivyozaliwa. Aliurudishia ule mlango. Akaendelea na ziara yake hadi alipofikia chumba kingine kilichofunguka, alichungulia, humo alipokelewa na macho ya Hellen na Vivian, Hellen ndiyo alikuwa anavaa.

    "Hamjambo warembo?” Milka alisabahi baada ya kuwa ameingia ndani.

    "Hatujambo hofu kwako." Vivian alijibu.

    "Mimi nimeota ndoto mbayambaya tu." Hellen alisema huku akiwa anajaribu nguo ya ndani kati ya zile zilizokuwa kwenye furushi alilokuwa amepewa na yule mwanajeshi wa kike.

    "Utaachaje kuota baada ya haya yote yaliyotokea?!” Milka alisema huku macho yake yakikagua mwili wa Hellen.

    "Khaa!, mnaniangalia hadi naona aibu, acheni hizo.” Hellen alisema baada ya kuona Milka na Vivian walivyokuwa wakimwangalia kama wanaomkagua.

    "Eeeeh!, bibie nina kaka mimi, unajuaje labda kanipa kazi ya kumtafutia." Milka alisema

    "Mmmmh! Padri yule hayawezi haya." Hellen alijibu.

    "Hata angekuwa anayaweza, yule ni kaka yako." Vivian alidakia. "Aaaaah!, hakuna ajuaye kwa sasa maana mchanganyiko huu wa habari naweza jikuta nafaa tu kula na Padri." Hellen alisema huku akiwa ameshamaliza kuvaa.

    "Hebu tuacheni ujinga hapa, nadhani inatakiwa tuulizane na tujuzane nini kinaendelea na nanmna ya kujinasua hapa. Na kwa jinsi mambo yalivyo kwanza nataka tufahamiane maana nimekuja kugundua inawezekana hata hatujuani hapa!” Milka aliwagutua wenzie.

    "Shiiiiiii!” Vivian alisema. "Hadi tutakapoona kuna usiri na usalama wa kuongea." Neno hilo alilisema kwa kunong'ona katika Lugha ya kisukuma. Milka alielewa lakini Hellen hakuelewa.

    "Sijaelewa…!” Hellen alisema. Harakaharaka kwa vile alikuwa jirani naye, Vivian alimvuta Hellen na kumnong'oneza kile alichokuwa amesema. Wote watatu wakatazamana, wakanyamaza. Baadae wakaendelea na maongezi ya kawaida ya wasichana wakutanapo lakini kwa makubaliano kuwa wasiongelee kabisa mambo yaliyotokea Kijijini Katunguru. Onyo alilokuwa amepewa na Mwasumbi bado lilikuwa kichwani mwa Vivian hivyo hakutaka kuongelea lolote pasipo kujua nani mwingine angekuwa anasikiliza.

    Waliongea wakachoka, walienda sebuleni wakaweka mikanda ya video, wakaangalia wakachoka. Jambo moja lililowashangaza ni kuwa hawakumwona tena yule mwanajeshi wa kike aliyewaleta wala wale wanaume wawili waliowakuta, mtu pekee aliyekuwa akiwahudumia alikuwa Bibi mmoja, ambaye mwanzoni walijitahidi sana kumwongelesha na kumuuliza maswali kadhaa lakini hakuonekana kuwajali kabisa. Mwishoni walikuja kugundua kuwa Bibi yule alikuwa bubu na kiziwi. Bibi huyo alikuwa akipika chakula na kufanya usafi wa aina zote kwenye hiyo nyumba. Walipojaribu kutoka nje waligundua kuwa nyumba ilikuwa imefungwa na hakuna ambaye angeweza kutoka nje.

    Hawakuwa na mawasiliano ya aina yoyote na ulimwengu wa nje. Walipohakikisha kuwa hakukuwa na mtu yeyote ndani ya nyumba hiyo ndipo walipoamua kuongelea mkasa uliokuwa umewapa.

    Alianza Milka, alisimulia yote yaliyokuwa yametoke siku ile walipokuwa Kijijini Katunguru ambapo walishuhudia Paul na wanaume wengine wawili wakiteketeza eneo zima kwa sababu tu ya kumtafuta Maganga. Kisha wakaelezea jinsi kwa namna ya kimiujiza walivyoweza kuokolewa na Askofu Alphonso.

    "Sitaongea mengi sana, ila kuna mambo ambayo najua mkiyajua yanaweza kuwasaidia. Askofu Alphonso mnayemsema, hakuwa Askofu Alphonso yule wa siku zote, bali yule alikuwa ni Mzee Mwasumbi aliyekuwa amevaa sura ya bandia iliyokuwa inafanana na sura ya Askofu Alphonso...." Vivian alisema lakini kauli yake ilikatwa na Hellen.

    “Eheee!, umesema Mwasumbi umenikumbusha...” Hapo Hellen akasimulia wakati yeye na Maganga walipokuwa kwa Mwasumbi na yote waliyokuwa wameyasikia. Milka na Vivian wakabaki vinywa wazi. Lakini Vivian akawa na picha kubwa zaidi kichwani mwake. Alikuwa na maswali kadhaa aliyokuwa akijiuliza, kama Milka na Maganga ni watoto wa Mwasumbi, ina maana hao watatu ni watoto wa mtu mmoja - Mwasumbi. Sasa ilikuwaje akaishia kwenye mikono ya wazazi anaoishi nao sasa.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Kwa kweli sielewi kwa nini hawa watu wametufungia hapa?” Hellen alisema.

    “Kwa vyovyote ilivyo, watu hawa watakuwa wanajuana na Mwasumbi, maana hadi sasa mkombozi wetu sote hapa ni mmoja na nadhani mnajua ni kwa nini ametuokoa, sababu iko wazi nayo ni kuwa Mwasumbi anajua sisi ni watoto wake. Na kwa mujibu wa maelezo ya Hellen inaonyesha japo anajua kuwa Hellen si mwanae ila anamjua vizuri sana, mama yake Hellen..." Milka alieleza. Wote wakatingisha vichwa kukubaliana naye.

    “Kama Mwasumbi na Paul walikuwa marafiki, mnataka kuniambia kuwa watu hawa urafiki wao ulivunjwa na wanawake tu au kuna kitu kingine nyuma ya hayo? Na kwa nini Mwasumbi aliendelea kufuatilia maisha ya Paul kwa siri? Msiniambie kuwa ni kwa sababu tu alijua kuwa Paul alikuwa anaishi na wanawe. Maana jinsi Mwasumbi alivyotuokoa inaonyesha wazi kana kwamba alikuwa anajua nini kingetokea na alikuwa amejiandaa siku nyingi kutuokoa. Vyovyote ilivyo nahisi kuna haja ya kuwa na mazungumzo na Mwasumbi, inaonekana ana mengi anayojua kutuhusu, hasa asili yetu na kwa nini tuko kwenye hali hii...” Milka alisema huku akiwaangalia wenzie kwa zamu. Wote walikuwa wakiongea kwa sauti za kunong'ona.







    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog