Search This Blog

Tuesday 20 December 2022

KWA AJILI YENU WANANGU, NITAMWAGA DAMU - 4

  




Simulizi: Kwa Ajili Yenu Wanangu, Nitamwaga Damu 

Sehemu Ya Nne (4)



"Kwa maelezo yake ni kwamba waliachana pale pale Restaurant mara baada ya umeme kukatwa."

Roberto aliendelea kutiririka kama vile yeye ndiye aliwatorosha maana maswali yalimwandama.


"Ingieni kwenye gari hatuna la kusubiri hapa."

Roberto aliona watakesha na maswali hivyo akaona waondoke mahali hapo.


"Kwa hiyo tunaelekea wapi?"

Jasmine aliuliza.


"Hapa lazima tufike mpaka Uwanja wa Ndege hapo tutajua uelekeo ni upi lakini lazima tufike pale."

Roberto alijibu na kuliondoa gari kwa kasi kama vile anataka kuingia kwenye mashindano ya magari.


"Lakini tunatakiwa tuwe tunaangalia makazi yaliyo porini tunaweza kuona chochote."

Jackline alitoa wazo ambalo Roberto alipingana nalo.


"Wamesema waliondokea pale uwanjani hivyo hakuna haja ya kuanza kuingia porini mwisho wa siku tutauliza mpaka nyani."


"Haya kaka tumekuelewa kanyaga mafuta basi mwendo gani huo?"

Jasmine alimkubalia lakini ajabu alitaka mwendo uongezwe kitu kilichomshangaza Roberto ambaye muda huo alikuwa anacheza na spidi zaidi ya tisini halafu barabara ni ya vumbi. Lakini mara Jessica alimpigia simu Jackline.


" Niambie mdogo wangu? "

Jackline alipokea.


"Nikiangalia hapa naona hamko mbali sana kati yenu na Mahmoud lakini hao wengine hawapatikani mpaka sasa."

Jessica alimpa majibu ya system yake inavyoonesha.


"Hatuko mbali?"

Jackline aliuliza huku akimpa ishara Roberto asimamishe gari.


"Ndiyo Jackline hapo mlipo uelekeo wa magharibi umbali wa kilometa sabini na nne."

Jessica alimuelekeza.


"Ooh my God' kwa hiyo tunatakiwa tuelekee huko? Sijui inakuwaje maana hata barabara hakuna."

Jackline aliongea akiwa kashusha kioo cha gari kuona kama anaweza kuona barabara ambayo wanaweza kuingia.


"Tafuteni lazima kuna sehemu mnaweza kuona kijinjia."


"Basi sawa mdogo wangu ngoja tuangalie uwezekano."

Jackline alikata simu na kuwaangalia wenzake waliokuwa wakimsubiri amalize kuongea na simu.


"Au turudi mpaka kwenye ule mgahawa kama tunaweza au kuulizia njia kwa wenyeji."

Roberto alishauri.


"Hebu tushukeni kwanza tuangalie eneo hili kama tunaweza kuona sehemu ya kupita hata kama hakuna barabara kikubwa tupate eneo wazi au lenye uwazi lisilo na miti."

Jasmine akaona waanze kwanza eneo hilo kutafuta sehemu ya kupita kabla ya kurudi mpaka kule mgahawani ambako walisimama kula.


JE NINI KITAENDELEA?




Jessica na Titiana walifika kwenye maziko ya Nesi wa St. Mathew Hospital aliyeuawa siku moja iliyopita na Titiana. Nesi huyu alizikwa kwenye eneo maalum ambalo lilitengwa na Hospitali hiyo kwa ajili ya wafanyakazi wake. Miongoni mwa waombolezaji waliohudhuria msiba huu walikuwa ni hawa mabinti wawili ambao wao kufika kwao hapo haikuwa kuhakikisha wanashuhudia anavyozikwa mhudumu huyu la hasha wao walikuwa na lengo jingine kabisa la kuangalia kama wanaowatafuta nao ni miongoni mwa waombolezaji katika msiba huo.


"Unajua nini Jessica?"

Titiana alianzisha mazungumzo huku macho yake yakiwa yanazunguka kila kona ya umati ule wa waombolezaji.


"Hapana sijui kuna nini?"

Jessica alimjibu kwa swali huku naye akiwa anafuatilia kila hatua kwenye tukio lile la kuuhifadhi mwili wa Nesi lakini kwa macho ya kuiba sana alikuwa akimkagua kila aliyekuwa mbele yake hivyo kama ungekuwa pembeni yao usingeweza kujua kama walikuwa pamoja kutokana na kuongea huku kila mmoja kaelekeza macho yake sehemu nyingine kabisa.


"Kwanza kwa mavazi yetu haya ni nani atatutilia mashaka? Si hivyo tu hakuna anayetufahamu hapa Australia labda Bi Elizabeth aamke huko aliko aje hapa ndiye atatutambua."

Titiana alijinasibu kwa mwenzake kutokana na mavazi yao ambayo hayakutofautiana na ya wengine. Lakini wakiwa wanapiga zogo lao mara macho ya Jessica yaliweza kumng'aza mrembo mmoja ambaye alikuwa nyuma ya watu waliokuwa mbele yao huku akiwa anazungusha macho huku na kule huku machoni akiwa katupia miwani ya jua. Kitendo cha mara kwa mara kutoka pale na kwenda pembeni kuongea na simu kilimpa hofu Jessica ambaye alianza kumfuatilia na kama haitoshi aliamua kuelekea upande ule ule aliokuwepo.


"Usiondoke hapa hakikisha yule mwenye miwani ya jua hakupotei machoni kwako."

Jessica alimnong'oneza Titiana na kuondoka kuelekea upande aliokuwa kasimama mrembo huyo. Alitembea kwa vituo kama vile alikuwa akitaka kusogea mbele ili aweze kuona kwa ukaribu kilichokuwa kikiendelea na mwishowe alifika eneo lile na kuanza kumuangalia aliposimama.


"Nyambafuuuu....... Ina maana kashapotea?"

Jessica aliishiwa pozi baada ya kuambulia sifuri.


"Lete habari?"

Jessica alimuuliza Titiana.


"Best nilikuwa nachati na Roberto nilipoinua macho nikaambulia chenga tu."

Majibu ya Titiana yalimkwaza sana Jessica akajikuta anamkatia simu na kuanza kumtafuta. Aliondoka pale na kuanza kumtafuta mtu huyo ambaye alishindwa kuelewa kaelekea wapi. Lakini wakati anajiuliza kaenda wapi mara aliweza kumuona pembeni kidogo na eneo lile akiwa na anaongea na simu. Hakutaka kupoteza muda aliamua kumfuata kwa kujificha ficha lakini alichelewa kwani mrembo yule aliingia kwenye gari na kuondoka na kumuacha Jessica akiwa kalitumbulia macho gari lile, hakutaka kukata tamaa akaifuata taxi iliyokuwa imesimama eneo la maegesho ya magari yaliyokuwa yamefika kwenye msiba.


"Titiana nimemuona kaondoka natakiwa kumfuatilia hivyo ungana nami naelekea kaskazini."

Jessica alimuelekeza Titiana huku akiingia kwenye Taxi na kukata simu.


"Kaka natakiwa kuelekea hii barabara ya kaskazini naishia wapi? Nitakuelekeza mbele ya safari."

Jessica alimjulisha dereva Taxi wakati akifunga mkanda. Na safari ikaanza kuelekea huko.


"Umeshaondoka tayari?"

Titiana alimuuliza Jessica kwa ujumbe mfupi.


"Ndiyo tunaondoka hivi sijui kama tutamkuta."

Jessica alimjibu Titiana.


"Poa na mimi niko nyuma yenu tunaweza kumpata."

Titiana naye alimwambia kuwa yuko nyuma yao kwa hiyo tayari magari mawili yalikuwa yakimfukuzia yule mwanadada.


"Tunaishia wapi dada yangu?"

Dereva wa ile taxi alimuuliza Jessica anakoelekea.


"Kuna gari limeondoka muda si mrefu tunatakiwa kulifukuzia."

Jessica alimjibu.


"Kuna usalama dada yangu?"

Yule dereva taxi alimuuliza tena Jessica.


"Ni wa kutosha kaka kuna mkoba wangu niliuacha mle sasa wakati nimejisahau na msiba nikaliona linaondoka hivyo sikuwa na chaguo zaidi ya kulifukuzia."

Jessica alimjibu.


"Usijali dada yangu lazima tutalikuta tu."

Dereva huyo alimpa moyo Jessica. Na wakati huo huo ujumbe uliingia kwenye simu ya Jessica.


"Bado tunaendelea kulitafuta eneo hilo waliopo wakina Mahmoud japo tumechoka sana kwani ni zaidi ya masaa mawili tunatembea kwa miguu msituni kutokana na kukosa barabara ya kupitishia gari."

Jessica aliusoma kisha akamjibu.


" Poleni sana, kwa hiyo gari mmelitelekeza wapi? "

Alimuuliza.


" Kuna shamba moja huko nyuma babu mmoja anaishi hapo tumemuomba tuliache baada ya kutuelekeza kuwa mbele hakupitiki kwa gari."

Roberto alimfafanulia.


" Komaeni kikubwa kama kuna matumaini."

Jessica aliongeza.


" Matumaini yapo Jessica tuna kilometa kama thelathini na sita kufika huko kulingana na system yangu."

Roberto alimjibu.

Dereva Taxi alimtoa kwenye kuchati Jessica baada ya kumtupia swali.


"Dada yangu naona kilometa zinasoma tu wala hatuoni dalili za hilo gari unaonaje tukiishia hapa?"

Aliulizwa.

Jessica alitulia kwa muda kutafakari jambo hilo kwani kijana huyo alikuwa sahihi kutokana na muda walioutumia huku giza nalo likiwa limeanza.


"Hebu ngoja kwanza."

Jessica alimwambia dereva huyo na kuinua simu ili ampigie Titiana kujua yuko wapi.


"Vipi mmefika wapi?"

Alimuuliza.


"Gari lenyewe lilikuwa kimeo tumesimama sehemu moja hivi ambayo siifahamu vizuri dereva anabadili tairi."

Titiana alimjibu.


"Basi vizuri sisi wenyewe tumeamua kugeuka tu kwani tunazidi kusonga mbele ambako hakuna matumaini ya kulipata gari hilo."

Jessica alimjibu.


"Kumbe mnaweza kutukuta hapa hapa mkiwahi."


"Hakuna tatizo wifi wa miye."

Jessica alimjibu na kukata simu.


****


Baridi la Makete liliwachanganya wakina Henry kiasi cha kuanza kulaani kwenda eneo hilo. Lakini pamoja na wao kulalamika juu ya baridi hilo waliwashangaa wenyeji wakiwa hawana Makoti wakikata mitaa.


" Hawa jamaa ngozi zao zikoje mbona hawana wasiwasi na hili baridi?"

Dereva Taxi alimuuliza mama mmoja ambaye aliwauzia Ulanzi.


"Ninyi ni wageni na sisi ni wazaliwa hivyo hii baridi kwetu haitusumbui."

Mama huyo alimjibu.


"Oya malizia kichupa chako si unakumbuka walisemaje madaktari kule Hospitali?"

Dereva yule alimuuliza.


"Aa..aa..chana na m....mi..mi kijana unanipangia la kuvaaanyaaa? Mimi ndiyo Henry au nik......."

Kabla hajaendelea mwenzake alimnyanyua na kutoka naye nje kwani alijua kuwa anaweza kuropoka siri zao.


"Unanishika hivyo mimi? Au umesahau kama mimi ni Bosi wenu? Nitawalaza njaa ohhhhooooo..."

Henry aliendelea kujigamba mbele yao huku akiongea kwa sauti ya kilevi.


"Tunajua kaka lakini hapa si mahala pake hebu tuondoke hapa."

Mwenzake alimjibu.


"Kumbe waoga eeee mngeendelea kuninyea ningewaonesha kazi. Watu wangu ila hii kitu ni nomaaa kidogo tu niko chapa chapa."

Henry aliukubali muziki wa Ulanzi wa Makete, alivyosimuliwa namna ilivyo yeye akaona asiandikie mate akataka kuonja ladha na kujikuta akiendelea kupakia moja baada ya nyingine.

Mara simu ya Henry iliita ikabidi mwenzake ndiye aichukue na kuipokea.


" Ndiyo Bosi nakusikia."

Kijana huyo alianza baada ya kuipokea.


"Vipi Hamza anaendeleaje? Na Henry yuko wapi?"

Mackdone alimuuliza juu ya Hamza na pia alitaka kujua Henry yuko wapi.


"Hamza bado ila kesho Oparesheni inaanza Bosi, kaka Henry katoka kidogo."

Alidanganya kijana huyo.


"Mwambie kuwa napenda mtu makini aache uzembe nahitaji taarifa kila wakati."

Mackdone kama alijua vile kuwa Henry hayuko sawa kwani si kawaida kwa Henry kuwa kimya kwa muda mrefu hivyo.


"Sawa Bosi nitamwambia akija."

Kijana huyo alimjibu lakini hakuwa na uhakika kama alisikiwa kutokana na Mackdone kumkatia simu.


"Jamani si mmemsikia Bosi anavyosema? Hebu tuwahi hospitali tukajue kinachoendelea huko."

Kijana huyo aliwaambia wenzake wakiwa wanaingia kwenye gari.


"Halafu Oscar nakuona namna unavyokipambania kiti changu, aliyekwambia uchukue simu yangu nani?"

Henry alimwambia Oscar mara baada ya kuinuka pale chini alipokuwa akitapika na kuingia kwenye gari.


"Kaka Henry ubaya wangu uko wapi? Hivi kwa hali hiyo ungeongea na Bosi kweli?"

Oscar alimuuliza.


"Unajidai kujali sana eee?"

Henry alimuuliza tena.


"Jamani hebu acheni malumbano kumbukeni mko ugenini huku mnatakiwa kushikamana."

Dereva Taxi aliwaambia baada ya kuona kama wanatofautiana hivi.


"Kelele wewe marehemu mtarajiwa unaongea nini subiri muda wako ufike tukuoneshe sisi ni wakina nani."

Kile ambacho Oscar hakutaka kuona kikitokea hatimaye kikatokea baada ya Henry kutoa siri.


" Unasemaje kaka? "

Dereva aliuliza baada ya kuisikia kauli ya Henry.


" Acha naye huyo kajilewea Ulanzi hajui akiongeacho."

Ilibidi Oscar aingilie kati mara baada ya Henry kuvujisha siri ambayo walitegemea kuitekeleza siku za mbele.


"Poa nimekuelewa Oscar."

Dereva huyo alimjibu Oscar lakini tayari kengele ya hatari iligonga kichwani na hivyo kuingia hofu. Aliendesha gari na kufika Hospitali huku kichwani akiendelea kuichekecha kauli ya Henry.


"Mlikuwa wapi ninyi tumewatafuta sana hapa mgonjwa wenu anahitaji damu ya kutosha kuelekea kwenye Oparesheni yake."

Daktari waliyekutana naye getini aliwauliza.


"Tunaomba utusamehe Daktari ugeni ni shida tulipotea na kujikuta tuingia sehemu moja wanaiita sijui Ipelele?"

Dereva Taxi yule alidanganya huku Henry akiwa hajitambui kwenye siti ya nyuma.


"Mliondokaje bila wenyeji? Huko Ipelele mbona mbali sana?"

Poleni sana wakati mwingine msiondoke peke yenu. Kesho msiondoke mpaka tuwapime viwango vyenu vya damu pamoja na makundi yenu ya damu kama yanaendana na ya mgonjwa."

Daktari alikubaliana na uongo wa Dereva Taxi. Baada ya kuachana nao walicheka sana baada ya kufanikiwa kwa uongo wao huku Oscar akimpongeza dereva huyo kwa uongo alioutengeneza kwa muda mfupi.


JE NINI KITAENDELEA?





Jessica alirejea na kumpitia Titiana pale njiani ambapo gari lao lilikuwa limepata hitilafu hivyo alimkabidhi dereva wa ile taxi hela yake kisha yeye Titiana akaingia kwenye taxi ambayo aliikodi Jessica na kurejea mjini. Ilikuwa tayari ni usiku ambao haukuwa mzuri sana kwani kulikuwa na baridi kali lakini wakina Jessica hawakujali hilo baada ya kuachana na yule dereva Taxi hawakuona sababu ya kurejea hotelini hivyo wakaona washike njia kuelekea nyumbani kwa Daktari Yakoub.


"Najua muda huu lazima atakuwa msibani au Hospitali kama ni zamu yake sisi tuelekee nyumbani kwake tukimkuta asante tusipomkuta tutaingia ndani kwa namna yoyote ile na kumsubiri akifika tu amekwisha."

Titiana alimwambia Jessica juu ya safari yao ya kuelekea kwa Daktari Yakoub ambako yeye anapafahamu vizuri mno.


" Lakini muda huu ni mapema sana ujue na vipi kuhusu majirani au hana? "

Jessica alimuuliza.


" Njia tunayokwenda kuitumia hata hao majirani zake hawawezi kujua chochote wewe twende majibu utanipa."

Titiana alimuondoa hofu Jessica juu ya kushtukiwa na majirani zake Daktari Yakoub.

Hivyo waliingia kwenye mtaa ambao anaishi Daktari Yakoub kwa miguu hawakuona sababu ya kuchukua gari kuwafikisha hapo.


" Tunauleta mtikisiko mwingine eneo hili mara baada ya mtikisiko wa kwanza wa nesi ambaye tayari yuko zake huko ahera."

Titiana aliongea hayo huku akikagua kichupa chake kidogo ambacho sijui kilikuwa na nini ndani yake.


"Jessica tumeshafika nyumba yenyewe ni ile pale yenye gari."

Titiana alimjulisha mwenzake kuwa wamefika.


"Hee kwa hiyo nyumba yake haina hata fensi?"

Jessica alishangaa sana baada ya kuoneshwa nyumba hiyo ambayo haikuwa na fensi yoyote wala mlinzi na hii ilidhihirisha kuwa Daktari Yakoub alikuwa ni mtu wa kawaida tu hakuwa maarufu kwenye taaluma yake.


"Ndiyo maana nilikwambia hata hao majirani zake watapatwa na mshangao kuanzia kesho asubuhi."

Titiana aliongea huku akitoa simu yake ambayo aliitafuta namba ya Daktari Yakoub na kumpigia huku wakiwa mita kadhaa kutoka yalipo makazi ya Daktari huyo.


"Niambie Tiana."

Aliongea Daktari Yakoub mara baada ya kuipokea simu.


"Pole na mchoko wa pilika za hapa na pale za msiba wa mhudumu wenu."

Titiana alimjibu.


"Nashukuru Mungu tumemsindikiza salama kwenye makazi yake ya milele na hivi sasa namalizia shughuli moja hapa kazini kisha nitaelekea nyumbani maana siyo kwa mchoko huu."

Daktari Yakoub aliweza kumueleza Titiana ratiba yake ya muda huo bila kujua kama anayeongea naye yuko mazingira ya nyumbani kwake akimsubiri.


" Aisee pole sana mimi mwenyewe leo nimeona niingie mjini kujichanganya kidogo kwenye hizi night clubs si unajua tena ukiona kichwa hakiko sawa unakitafutia dawa."

Titiana alimdanganya Daktari Yakoub.


"Daa umenikumbusha mbali sana mambo yangu hayo."


"Wala usijali wakati mwingine tutakuwa pamoja kuburudika kwa leo pumzisha akili Daktari."

Titiana aliendelea kumliwaza Daktari Yakoub.


"Poa dada Tiana."

Daktari alimjibu Titiana ambaye alikata simu na kumpa ishara Jessica kumuonesha sehemu ambayo wanatakiwa kupitia. Waliizunguka nyumba ile mpaka nyuma ambako kuna mlango ambao hutumika kwa dharura na walipoufikia Titiana alichukua ufunguo wake wa bandia na kuuzamisha kwenye kitasa na kukitekenya hakikubisha sana kilijibu, wakaingia ndani na kuufunga kama ulivyokuwa na kuelekea mpaka sebuleni ambako waliweza mikoba yao kisha wakazama chumbani huko kilichofanyika ilikuwa ni kuchukua kichupa kile na kukifungua kisha Titiana alimwaga kidogo unga uliokuwa ndani yake juu ya bedcover' kisha akamgeukia Jessica na kutabasamu.


"Kazi kwisha turudi zetu sebuleni tumsubiri mgeni wetu arudi."

Titiana alimjulisha Jessica kuwa ni muda wa kumsubiri Daktari Yakoub ambaye hakuwa na habari kama nyumbani kwake kuna wageni wanamsubiri. Na kwa kuwa walikuwa kwenye mawindo hawakuwasha hata taa walitumia taa za kwenye simu na baada ya kurejea sebuleni walizizima na kusalia giza. Haikuchukua muda mrefu mara Daktari Yakoub aliwasili nyumbani kwake na kupaki gari lake kwenye maegesho yake kisha akaongoza mpaka kwenye mlango wa kuingilia ndani akaufungua na kuingia ndani kisha akawasha swichi ya sebuleni ambayo iliwasha taa zote za ile nyumba. Lakini hakuweza kubaini chochote mle ndani, aliifuata TV yake akaiwasha huku akivua koti lake na kuliweka kwenye sofa la pembeni yake.


"Tumechoka na taarifa hizo sasa."

Alijisemesha baada ya kuiona taarifa iliyokuwa ikimuelezea Nesi wao aliyeuawa na watu wasiojulikana huku mtangazaji akieleza kilichotokea na kwa kuwa hakua tayari kuiangalia taarifa hiyo aliinuka na kuingia chumbani kwake. Huko alijitupa mzima mzima na kujilaza chali huku macho yakiwa kwenye taa ambayo ilikuwa ikizungukwa na mdudu mithili ya mbu hivi.


"Yaani kuna wadudu wengine ni sugu sana pamoja na kupuliza dawa ile asubuhi lakini bado haka kapo kam......."

Alishindwa kuendelea kwani tayari macho yake yalikuwa mazito sana huku kichwa akianza kukiona kizito kupita kiasi na hapo hapo usingizi mzito ulimpitia na hakuweza kujua kilichoendelea muda huo.

Mlango ulifunguliwa na Titiana alichungulia kwanza ndani kisha akaingia.


"Daktari Yakoub unajidai jeuri kwangu mimi? Hapa ni maji marefu na leo ndiyo utanifahamu vizuri mwanaharamu wewe."

Titiana aliongea huku akimfunga kamba mwili mzima pale pale kitandani kisha kumalizia na kumfunga kitambaa kizito mdomoni.


"Kifuatacho?"

Jessica alimuuliza.


"Ni kuipekua nyumba yote kutafuta kinachotuhusu na kwa namna nyumba ilivyo sisi tukomae na simu zake pamoja na hiyo laptop yake tujue kuna nini muda huo tunamsubiri azinduke."

Titiana alimjibu Jessica ambaye alianza mara moja kuipekua laptop ambayo baada ya kuiwasha alikutana na hitajiko la password lakini kwa kuwa naye ni mtukutu kwenye vitu kama hivyo alichukua simu yake pamoja na 'usb wire' akauchomeka kwenye simu na kwenye laptop kisha akaiwasha app yake ya 'my key' na kuifungua ambayo haikuchukua muda password ilitoka hapo moja kwa moja aliingia kuangalia mafaili ya muhimu pamoja na documents zake za siri alizipitia moja baada ya nyingine.


"Kuna chochote ulichokibaini huko?"

Jessica alimuuliza Titiana ambaye naye alikuwa akigombana na simu ya Daktari Yakoub.


"Ngoja kwanza kuna vitu nimeviona hapa nitakujulisha vipi wewe?"

Na yeye alimuuliza.


"Kuna miamala nimeiona ilifanyika kutoka kwenye akaunti moja hapa naifuatilia na kuingia kwenye akaunti ya Daktari zaidi ya dola elfu saba mia sita ziliingizwa...."

Baada ya kuchunguza vizuri jina la mtumaji aliweza kuliona hakuwa mwingine zaidi ya Vivian.


" We Titiana aliyemtumia ni Vivian."

Jessica alimjulisha Titiana.


" Okey sawa majibu tumepata kumbe huyu ndiye aliyemtorosha Bi Elizabeth na kulipwa kiasi hicho cha fedha.


" Unajua nini hapa, kama alitoroshwa kutoka pale Hospitali halafu hakuna kilichofanyika maana yake hata mganga mkuu wa hii Hospitali anahusika pia."

Jessica alionesha wasiwasi wake juu ya sakata la kuondolewa kwa Bi Elizabeth.


"Na mimi huku nimepata jumbe ambazo zilitumwa na Vivian juu ya kila kitu kuhusu kutoroshwa kwa Bi Elizabeth na amba......"

Kabla Titiana hajamaliza kuongea mara Daktari Yakoub alipiga chafya na kuwafanya kusitisha kila kitu na kumfuata pale kitandani.


"Habari yako Daktari??"

Titiana alimsabahi huku akivua kofia yake kumfanya Daktari Yakoub aweze kumtambua vizuri.


"Haaa Titiana umeingiaje hapa?"

Daktari Yakoub alimuuliza.


"Kwani wewe unafikiri tumeingiaje? Bila shaka utakuwa na mabunio ya majibu ya kile tulichokifuata hapa kwako hivyo cha msingi anza kutupa majibu tu."

Jessica aliingilia kati na kumjibu Daktari Yakoub huku akimtoa kitambaa cha mdomoni huku bastola ikiwa kwenye paji la kichwa.


" Mbona sura zenu haziendani na yale mnakotaka kuyafanya? Au ninyi ndiyo mliomuua Nesi wetu? "

Daktari Yakoub aliwauliza lakini badala ya kujibiwa alioneshwa ishara ya kumtaka afunge domo lake kwani ataiaga dunia mapema akiwa bado anaipenda.


"Daktari Yakoub wewe ni mtu smart sana na mwenye malengo yako ya baadaye hivyo nitakushangaa kama utakuwa ni mhusika mkuu wa utoroshwaji wa mgonjwa aitwaye Bi Elizabeth kwa kitita cha njaa kilichokupa kiwewe...."

Kabla Jessica hajamaliza alikatishwa na Daktari Yakoub ambaye aliingilia kati maelezo yake.


" Dada mbona sielewi chochote juu ya kile unachokizungumza? "

Daktari Yakoub alimgomea.


" Ohhh kweli hujui chochote? "

Jessica alimuuliza tena swali huku Titiana akiwa katulia pembeni kama hajui chochote huku macho yake yakiwa kwenye simu kama vile alikuwa akichati na mtu.


" Kweli kabisa sifahamu chochote kwanini niwadanganye Titiana mwenyewe anajua kila kitu kunihusu mimi na ndiyo maana niliamua kumsaidia kwa kuanza kumpeleleza yule mwanadada aitwaye Vivian."

Yakoub alijitetea.


"Anasemaje huyo?"

Titiana kama vile alizinduka usingizini aliinuka pale alipokuwa kaketi na kumtwanga swali.


"Eti hajui chochote kile kwani hata wewe ni shahidi wake kutokana na kukusaidia kumpeleleza Vivian."

Jessica alimwelezea Titiana.


"Okay vizuri naomba ripoti ya huyo Vivian."


"Nitakwambia lakini kwanza nifungueni hizi kamba zinaniumiza."

Kauli ile ya Daktari Yakoub ilimfanya Jessica amsogelee na kumtandika risasi ya sikio kwa kutumia bastola yake yenye kiwambo cha sauti ambayo ililichana vipande vipande sikio.


"Bila shaka sasa tunaweza kuongea kwani maumivu yamekupungua au vipi Daktari Yakoub."

Jessica aliongea huku akiiangalia vizuri bastola yake wakati huo Daktari Yakoub alikuwa akiugulia maumivu huku Titiana akiwa keshamfunga solutepu kuzuia kelele ambazo alianza kuzitoa. Wakiwa wanaendelea kumpa suluba Daktari Yakoub mara simu ya Titiana iliita na kumfanya asogee karibu na dirisha ambako aliangaza kwanza nje kisha akaipokea.


"Jamani sweet u hali gani?"

Titiana alianza mara baada ya kuipokea simu ya Roberto.


"Niko poa kabisa kipenzi japo tumechoka sana kwa hii safari."

Roberto alimjibu.


"Enhh mmefanikiwa kufika eneo hilo mpenzi?"

Titiana alimuuliza tena.


"Yes hivi ndivyo tunaingia hapa kijijini ambapo signo imesimama na tunachokifanya hapa ni kuanza kuitafuta hiyo nyumba ambayo wapo."

Roberto alimwambia Titiana.


"Sasa kipenzi siungalie umbali kutoka hapo ulipo?"

Titiana alimpa wazo.


"Tunatamani kufanya hivyo lakini simu hazina chaji kabisa na hivi nimekupigia mara baada ya kuiwasha ikakubali lakini wote hapa simu zetu hazina kitu na muda wowote hatutapatikana kabisa kwani nikiangalia juu sioni hata waya wa umeme uliopita au kuingia kwenye hiki kijiji......"

Kama ambavyo alisema Roberto simu ilikata na Titiana alipojaribu kupiga haikupatikana tena hivyo akaamua kumpigia Jasmine ambaye na yeye hakupatikana wala Jackline, alishusha pumzi ndefu kiasi cha kumfanya Jessica kugeuka kumtazama.


JE NINI KINAKWENDA KUTOKEA?





Baada ya kuingia ndani ya kijiji hiki ambacho kilionekana kutokuwa na wakaaji wengi sana ikionesha kuwa kilikuwa ni cha wakulima kwa muonekano wake. Kilikuwa kimya sana muda huu ambao wakina Jackline waliingia huku baridi likipuliza kiasi cha kuwapa hofu wakina Jackline kulihimili kwa kuwa makoti yao mazito waliyaacha kwenye gari baada ya kugundua ni eneo lenye joto lakini baada ya kufika kijijini hapa mambo yamebadilika. Walifika kwenye kijumba kimoja ambacho kilionekana mhusika wake alikuwa hajalala japo ilikuwa ni usiku wa manane yapata saa tisa usiku hivyo waliamua kukisogelea kwani waliona moto kupitia kwenye nyufa za kuta.


"Mwenyewe hodi, hodi hodi mwenyewe."

Roberto alibisha hodi baada ya kuufikia mlango huku wakina Jackline wakiwa wamejibanza upenuni mwa kijumba hicho.


"Nani huyo?"

Sauti nzito ilijibu kutoka ndani.


"Samahani mwenyewe naomba kuonana na wewe tafadhali."

Roberto alimjibu huku akimchungulia kupitia vitundu vilivyokuwa kwenye mlango wa bati.


"Nimekuuliza wewe ni nani sihitaji maelezo mengine hapa."

Sauti hiyo ilisimamia kwenye swali lake la kutaka kumfahamu aliyebisha hodi muda huo pale mlangoni.


"Mimi ni ndugu yako kaka kutoka mjini nimepatwa na tatizo nahitaji msaada wako."

Roberto alimjibu huku akiendelea kumfuatilia kupitia kwenye vitundu vile. Yule mtu alikuja na kufungua mlango lakini kwa tahadhari hakuchungulia nje alichokifanya alimruhusu mgongaji ambaye Roberto aingie,hivyo aliingia ndani.


" Naitwa mzee Minyetye ni mkazi na mganga wa tiba za asili hapa kijijini Chanze karibu kijana."

Mzee Minyetye alijitambulisha akiwa anaurudisha mlango baada ya Roberto kuingia ndani.


"Asante mzee wangu mimi na wenzangu wawili ambao bado wako nje wakisubiri ridhaa yako waweze kuingia ndani tumepotea njia baada ya gari letu kuishiwa mafuta na wakati tukitafuta makazi ya watu kwenye msitu huu uliokizunguka kijiji chenu tumejikuta tukipotea hivyo tukiwa tunazunguka kutafuta msaada zaidi ndiyo tukaona mwanga kutoka kwenye nyumba hii."

Roberto alijieleza kwa mwenyeji wake huyo mzee Minyetye.


" Unasema uko na wanzako wawili?"

Mzee Minyetye alimuuliza.


" Ndiyo wako hapo nje."

Roberto alimjibu.


" Si uwaambie nao waingie ndani watakauka kwa baridi hili."

Mzee Minyetye aliinuka na kuuendea mlango kuufungua ili kuwakaribisha walio nje.


"Mko wapi ninyi wageni ingieni ndani."

Akiwa anachungulia nje aliwakaribisha wakina Jasmine ambao walijitokeza.


"Tunashukuru mzee."

Jasmine alimjibu huku wakimfuata mwenyeji wao ndani.


"Karibuni, karibuni."

Aliwakaribisha ndani huku akitafuta vikalio alivyokuwa kaviweka kwenye kichumba ambacho aliingia na kijinga cha moto.

Baada ya kupata alirudi na kuwakabidhi wageni wake.


"Kwanza poleni sana kwa kupotea kwenye msitu wetu ambao wengi waliokuja huku asilimia kubwa walipotea na hii ni kutokana na aina ya miti na matunda yanayopatikana msituni humo."

Mzee Minyetye aliwapa pole wageni wake kwa kuwasimulia sifa ya msitu wao.


"Asante mzee wetu inakuwaje miti na matunda yahusike na upotevu wa watu?"

Jackline alimuuliza mzee Minyetye.


"Kweli ninyi ni watu wa mjini, huku kuna miti ambayo majani yake ukiyakanyaga tu lazima upoteze uelekeo pia kuna matunda ambayo nayo ukiyakanyaga tu lazima upotee na katika hilo ninaamini hata ninyi mlikanyaga kati ya hivyo."

Mzee Minyetye alifunguka.


"Mzee wangu waswahili wa huko uswahilini wanasema tembea uone na leo tumetembea na kuja kuyafahamu haya ambayo sikuwahi yajua hata siku moja."

Roberto aliongea huku akiusogelea moto vizuri.


"Vitu kama hivi vinafahamika na jamii iishiyo vijijini zaidi lakini kwa wale wa mjini hawayajui haya."

Mzee Minyetye alimjibu huku akigonga gonga makaa ya moto ambapo alikuwa ameweka kisufuria juu yake.


"Sijui tunaanzaje kumuuliza hapa?"

Jackline alimnong'oneza Jasmine sikioni.


"Wanangu kuna nini mbona mnaongea kwa sauti chini? Kama mna tatizo semeni muweze kusaidiwa."

Kumbe mzee Minyetye alikuwa kawasikia hivyo akawataka waseme kile walichonacho waweze kusaidiwa kama hawatojali katika hilo.


"Ni kweli mzee kama ambavyo umesema hapo mwanzo kuwa msitu wenu huu umepoteza wengi kutokana na hayo matunda na majani hivyo na sisi pia tuna mashaka hayo kwani kuna wapendwa wetu wamepotea na hatujui wako wapi mpa muda huu na ujio wetu huku ni kuwatafuta wao."

Roberto aliona aweke wazi sababu za wao kuwepo pale muda ule.


" Wamepotea lini na wako wangapi?"

Mzee Minyetye aliwauliza.


" Wako wanne, wakubwa wawili wa kiume na watoto wawili mapacha."

Jackline alirukia kujibu swali hilo akihisi Roberto anaweza kukosea kutoa majibu.


"Oooh vizuri hebu ngoja kwanza tuone."

Mzee Minyetye aliinuka na kuingia kwenye kichumba kile alichoingia mwanzo kuchukua viti kisha alirejea akiwa na vifaa fulani ambavyo viliwatisha kidogo wakina Jackline kwani hawakuwahi kuviona vilikuwa ni vibuyu vyenye shanga pamoja na mapembe ya wanyama yapatayo mawili huku vibuyu navyo vikiwa viwili na kichwani alikuwa kajifunga lemba la rangi nyekundu.


"Taja majina ya hao wapendwa wenu humo."

Mzee Minyetye alimwambia Roberto huku akimkabidhi kibuyu kimojawapo. Na kwa kuwa mhusika alikuwepo pale Roberto aliona ni vyema akimkabidhi kile kibuyu Jackline ambaye alikipokea na kisha kufanya kama ambavyo aliambiwa na mzee Minyetye na baada ya kumaliza alimrudishia mzee.


"Ng'ota vala, Ng'ota vala chele chichi bala kun'yaa weree shutyaa kadola... Ng'otaaaaaa beke byaaaatu."

Ni maneno ambayo wakina Jackline hawakuweza kujua maana yake ambayo yalizungumzwa na mzee Minyetye kwenye kile kibuyu ambacho alikipokea kutoka kwa Jackline.


" Anazungumza nini hapo mbona siokoti chochote? "

Jasmine aliongea chini chini huku akirudi nyuma kwa hofu kutokana na matendo ambayo alikuwa akiyafanya muda ule.


"Jasmine tulia basi tuweze kumsikilizia kwanza."

Roberto alimtuliza Jasmine ambaye alionesha hofu kwa yaliyokuwa yakiendelea mle ndani.


"Poleni kwanza kwa kilichowapata wanangu, hapa nikiangalia nawaona watoto wawili na mtu mzima mmoja wakiwa ndani ya ardhi yetu huku mtu mwingine aliyesalia akiwa kwenye hatari kubwa."

Mzee Minyetye alitoa maelezo hayo ambayo yaliwashtua sana wakina Jackline.


" Wako wapi sasa hao ndugu zetu? Na huyo mwingine amekutwa na nini? "

Roberto alimuuliza mzee Minyetye.


" Hawa watatu nawaona ndani ya ardhi yetu lakini huyu mwingine mwenye damu moja na hawa watoto kafungiwa kwenye jengo moja lililo ndani ya jiji la Gaborone."

Minyetye alitoa maelezo ambayo yaliwachanganya wakina Jasmine huku Jackline akionekana kuchanganyikiwa zaidi baada ya kupata taarifa zile.


" Binti jitulize kwanza tulifanyie kazi hili la watoto ambao usiku huu huu tunakwenda kuwachukua lakini huyo mwingine mlolongo ni mrefu japo nitawapa jina ya jengo hilo."

Mzee Minyetye aliongea hayo huku akiuendea mlango ambao aliufungua na kisha kuwataka wamfuate.


****


Titiana aliporudi pale kitandani alimtandika Daktari Yakoub ngumi nzito ya shavuni ambayo ilimfanya atoe ukelele japo alikuwa kafungwa ile solutepu mdomoni kitu kilichomfanya Jessica amuangalie Titiana.


"Kumetokea nini kwenye simu?"

Aliona amuulize kwani alihisi kuna jambo amekutana ambalo si kawaida na ndiyo maana kaja na mihasira yake.


"Hakuna kitu Jessica huyu mpuuzi anatuchukulia muda wetu kumbuka tunacheza na muda sisi."

Titiana aliongea huku akimtoa ile solutepu mdomoni Daktari Yakoub.


"Sasa unachotakiwa ni kunipa majibu ya maswali yafuatayo tofauti na hapo nitakuambia ni kwanini niko hapa."

Titiana alimwambia Daktari Yakoub.


"Maswali gani hayo dada Titiana?"

Daktari Yakoub aliuliza.


"Kwanza tambua kuwa mimi siyo dada yako hilo liweke akilini pili nataka kujua aliko Vivian pamoja na Bi Elizabeth pia tueleze hela ulizoingiziwa kwenye akaunti yako zilikuwa ni za nini?"

Titiana alimtupia maswali ambayo yalimfanya Daktari Yakoub kujivuta nyuma kidogo kwa hakuyategemea.


" Jibu haraka bwana unamtolea nani macho yako? "

Jessica alimshtua baada ya kuona kaduwaa asijue aanze na lipi.


" Naaam! Jamani mimi sifahamu walipo wakina Vivian na hizo fedha zijaziona hivyo sifahamu zimetoka wapi?"

Majibu ya Daktari Yakoub yaliwaudhi wakina Jessica kiasi cha kumfuata pale kitandani na kuanza kumpiga mingumi hovyo hovyo ilmradi tu kupunguza hasira.


" Kuna wewe jeuri eee? "

Jessica alimuuliza Daktari Yakoub akiwa anamkita kisu pajani.


" Dada yangu unaniumiza kwa kosa nisilolijua hakika."

Daktari aliongea akiwa kwenye maumivu makali ya kisu ambacho alichomwa na kikaachwa hapo hapo.


"Mpaka hapo nimebaini wewe ni miongoni mwa watu wa Mackdone ambao wamekula kiapo cha uaminifu kwake na ndiyo maana huwezi kueleza waliko wakina Bi Elizabeth kwani wewe ndiye uliyewatorosha usiku ule ukishirikiana na yule nesi ambaye alikuwa jeuri kama wewe halafu unasema hujui chochote siyo? "

Titiana alimsogelea na kumuwekea bastola mdomoni akiwa kapandwa na hasira kwani hata hayo maelezo hayakuwa yakisikika vizuri kwa hasira.


" Sasa niambie utaongea au hauko tayari kuongea chochote? "

Kabla hajajibu swali la mwanzo Titiana alimtupia swali jingine safari hii akiwa kaiandaa bastola yake huku Jessica akiwa anachungulia dirishani.


"Najua niongee nisiongee lazima mtaniua tu kuficha utambulisho wenu hivyo sioni sababu ya kuwaeleza waliko fanyeni mliloamua kulifanya kwangu."

Daktari Yakoub alimjibu Titiana.

Majibu yale yalimsogeza karibu Jessica ambaye alikuwa na kisu mkononi akamchania shati lake kisha alimkita kisu kifuani na kuanza kukizungusha kwa kukisukuma ndani na kukitoa nje.


" Mmechelewa sana muda wameshaondoka kurudi Afrika na amesha....ameshazi....zin..zinduka na tayari mtu wenu mm...mmoja yuko mik....miko......"

Hakumalizia kauli yake alipoteza uhai wake na kuwafanya wakina Titiana kutazamana kutokana na kile walichokisikia japo kwa hakumalizia.


" Kwa hiyo Vivian keshaondoka na Bi Elizabeth kurudi Afrika ya Kusini? Kwamba tayari keshapona? Na huyo wanayemshikilia ni nani au ndiyo Daktari Abbas?"

Titiana alijiuliza maswali ambayo wote wawili hawakuwa na majibu kwani walishindwa kujua wamuulize nani kwa sababu kati ya wakina Jackline hakuna ambaye yuko hewani kutokana na simu zao kutokuwa na chaji. Wakiwa pale ndani hawajui wafanye nini mara simu ya Daktari Yakoub iliita haraka sana Titiana aliichukua na kuangalia aliyepiga ni nani na ndipo alipobaini kuwa ni Vivian hivyo akaliandaa koo lake tayari kwa kuiiga sauti ya Daktari Yakoub kisha aliipokea.


"Daktari Yakoub tunakushukuru sana ushirikiano wako kuanzia mwanzo mpaka sasa tukiwa tunashuka uwanja wa ndege hapa Gaborone. Lakini jiandae kuna mtu wetu anaikaribia nyumba yako kukamilisha misheni yetu kama ujuavyo huwa hatuachi alama nyuma yetu tunashukuru waliomuua nesi waliturahisishia kazi hivyo nikutakie safari njema ya Ahera Daktari wangu ambaye nilikupenda sana."

Vivian aliongea mengi ambayo yalimfanya Titiana kusalia kimya akimsikiliza tu kwani alishindwa aongee nini wakati mpigaji hakutoa nafasi hiyo kwani baada ya kumaliza alikata simu. Titiana aliitupa kitandani ile simu na kukaa huku akijikuna kichwa.


" Ni nani na anasemaje?"

Jessica alimuuliza.


"Kuna mgeni anakuja hapa hivyo tunatakiwa kumshughulikia katumwa na wakina Mackdone kuja kumuua Daktari Yakoub huku Bi Elizabeth na Vivian wakiwa ndani ya jiji la Gaborone."

Jessica alimfuata Titiana akamvuta atoke pale kitandani kisha akamfunika vizuri Daktari Yakoub na akampa ishara ya kutaka wajifiche kumsubiri huyo aingie ndani. Lakini Titiana hakuona sababu ya kujificha badala yake akachukua laptop, simu na vifaa vingine muhimu vya Daktari Yakoub na kumtaka Jessica waondoke zao huyo mtu hana umuhimu kwao kwani waliyemtageti tayari yuko Afrika. Hivyo walitoka nje kupitia mlango waliotumia kuingia.


"Hebu subiri kwanza."

Jessica aliongea hivyo baada ya kubaini kuwa kuna gari limefika na kupaki mbele ya nyumba ya Daktari Yakoub hivyo hakuona sababu ya kuondoka alichokifanya ni kutembea kwa kuufuata ukuta mpaka kwenye kona ambapo alichungulia lilipo gari na alichokiona ni mtu mmoja ambaye alishuka na kuufungua mlango kama ni mwenyeji wa nyumba hiyo na alipohakikisha kuwa kaingia ndani alimpa ishara Titiana amfuate. Walilifikia lile gari Jessica aliingia chini ya uvungu huku Titiana akijificha kwenye maua bastola mkononi.

Kwa alichokutana nacho ndani alitoka nje haraka simu ikiwa sikioni huku akiangalia huku na kule kwa hofu.


"Bosi kuna watu wanaotufuatilia mbona Daktari Yakoub naye kauawa dakika sifuri zilizopita maana damu bado mbichi kabisa."

Kijana huyo aliongea hayo na mkubwa wake kumpa taarifa ya kile alichokutana nacho ndani lakini pamoja na kuangalia pande zote anaonekana hakuwa makini kwani akiwa bado anaongea na simu huku mkono mmoja ukiwa kwenye mlango wa gari akiingiza ufunguo ili aufungue.


"Usipate shida bado tupo hatujaondoka tulia hivyo hivyo usitingishike."

Sauti ya Titiana ilimshtua kijana huyo ambaye aliona ajaribu bahati yake ya kujiokoa lakini alichelewa kwani Jessica alishaibuka na kumkata mtama maridhawa uliompeleka chini na kuanguka kama furushi. Na kabla hajafanya chochote Jessica alishamkalia juu bastola ikiwa kwenye paji la uso la kijana huyo.


UNAFIKIRI NINI KINAKWENDA KUTOKEA?



Kijana huyu aliishiwa pozi mara baada ya kuwekwa mtu kati na mabinti ambao kwa haraka haraka ukiwaona huwezi kuamini kama wana vurugu kiasi hicho kutokana na sura zao za upole na huku ukimuangalia Jessica usoni ana sura ya tabasamu muda wote lakini linapokuja suala la kiutendaji anakuwa mtu mwingine kabisa.


"Sasa unaweza kuukwepa mdomo huu wa chuma kwa kutueleza ulikuwa unaongea na nani na kwanini umekuja hapa kwa Daktari Yakoub?"

Jessica alimuuliza maswali hayo huku akiwa anaisugua sugua bastola kwenye paji la uso la kijana huyo.


"Naombeni msinifanye chochote kibaya mimi siyo mtu mbaya bali nilikutana na dada mmoja ambaye alinipa kazi ya kuja kumuwekea sumu daktari Yakoub na hakutaka nihoji kwanini?"

Alitoa utetezi wake mbele ya warembo hao.


"Unasemaje?"

Jessica alimuuliza.


"Nilipewa hii kazi na dada mmoja hivi....." Kabla hajamaliza sentensi yake alikutana na kofi la usoni ambalo lilimfanya aone nyota nyota machoni.


"Usitufanye sisi watoto wadogo hapa kumbuka hatuna muda wa kupoteza hapa tueleze ukweli unasema dada mmoja kwamba humfahamu? Mtu asiyekufahamu angewezaje kukupa kazi hii ya hatari alijuaje kama unaiweza?"

Jessica alimtupia mengine ambayo yalimfanya kijana huyo kujiumauma kutoa jibu linaloeleweka.


" Alini....alini....unajua nini dada mimi naitwa Hens Tylenol ni mtoto wa mzee Tylenol ambaye ni mfanyabiashara maarufu wa maua hapa Australia hivyo mnaweza kusema chochote kile na baba yangu akatekeleza."

Kijana huyo aliyejitambulisha kwa jina la Hens alihamisha mada nyingine.


" Hatujakuuliza baba yako ni nani hapa mshenzi wewe? "

Titiana alikuja kwa nyuma na kumtandika risasi ya mguu. Kisha walimfunga kamba na kitambaa cha usoni kisha walimrushia kwenye gari lake na Titiana alichukua funguo mfukoni mwake na kuiwasha gari la Hens na kuondoka.


" Tunakwenda naye wapi huyu mpuuzi? "

Jessica alimuuliza.


"Simu yake ni msaada kwetu yeye si chochote hivyo popote ni makazi yake ya kudumu."

Titiana alimjibu.


Hivyo walipita barabara inayoingia kwenye viunga vya Hospitali ya St. Mathew na kisha gari lilishika njia kutoka maeneo hayo na kuelekea mjini. Wakiwa njiani kuna simu iliingia kwenye simu ya Jessica.


" Jessica ni mimi Roberto nimeazima simu hapa, Mahmoud na wakina Nathan tumewakuta wamehifadhiwa kwa kijumba cha bibi mmoja ambaye aliwapa hifadhi."

Roberto alimwambia Jessica kwa kutumia simu ya kuazima na kumueleza kile kilichotokea Gaborone.


"Oooh Yesu hakika wewe ni jibu la maswali yetu, vipi hawajapatwa na majeraha yeyote?"

Jessica alimuuliza mara baada ya kusikia wamepatikana.


"Si unaufahamu muziki wa Mahmoud wangeanzia wapi?"

Roberto alimjibu.


"Kwa hiyo mnaelekea wapi muda huu maana tumenasa taarifa za wakina Vivian pamoja na Bi Elizabeth kutua huko masaa kadhaa yaliyopita."

Jessica alimueleza kile wanachokijua juu ya Bi Elizabeth pamoja na Vivian.


"Kwamba Bi Elizabeth karejea huku na vipi kuhusu hali yake?"

Roberto alimuuliza.


"Kapona kiasi hivyo wamerejea mara baada ya kujua kuwa kundi letu liko nyuma yao."

Jessica alimjibu.


"Vizuri ngoja tutaongea baadaye kidogo simu yangu ikijaa."

Roberto alimaliza na kukata simu na kumfanya Jessica kumgeukia Titiana aliyekuwa nyuma ya usukani na kumuelekeza kuwa aliyepiga simu alikuwa ni Roberto na Titiana aliitikia kwa kichwa. Na walipowasili katikati ya msitu ambao Titiana huupenda sana waliacha barabara na kuingia ndani ya msitu huo na tayari ilikuwa ni saa kumi na mbili asubuhi japo kulikuwa na kigiza bado kilichokuwa kimeambatana na vimanyunyu vya mvua vilivyokuwa vikidondoka taratibu kwenye majani yaliyoupamba vilivyo msitu. Baada ya kusimama walimshusha Hens kwenye gari na kumtupa chini kulipokuwa kumelowana kwa maji maji ya mvua iliyokuwa ikiendelea kunyesha taratibu kama haitaki hivi.


"Hens bila shaka unaweza kusali sala zako za mwisho tuweze kuachana nawe."

Titiana alimwambia Hens huku akimtoa kile kitambaa cha usoni.


"Naombeni msiniue mdogo wenu bado mdogo sana na ni juzi juzi tu nimemvisha pete ya uchumba mpenzi wangu Gabriella, Naombeni sana msinifanye chochote."

Hens ilibidi aanze kujitetea mara baada ya kuona warembo waliokuwa mbele yake hawakuwa na mzaha hata kidogo juu yake.


"Nafasi yako ya kuendelea kuishi unayo lakini itakuwa iwapo tu utaongea ukweli juu ya unaowatumikia."

Jessica alimfuata pale chini na kumnong'oneza sikioni kisha akainuka na kurudi karibia na lilipokuwa gari.


"Sawa nitawaambia, mimi nilitafutwa na Daktari Yakoub na kuelezwa kuwa kuna mwadada aitwaye Vivian anatafuta mtu wa kufanya naye kazi kwa kipindi hiki ambacho atakuwa hapa Australia hivyo nikakubali kwani mishe nyingi sana nimefanya na Daktari Yakoub ambaye amehusika na uuzaji wa viungo vya binadamu aliokuwa akiwafanyia upasuaji."

Hens alianza kutiririka mbele ya wakina Jessica.


" Kwa hiyo wewe na Daktari Yakoub mmefanya kazi pamoja kwa muda mrefu siyo?"

Titiana alimuuliza.


" Nyingi sana na kubwa ikiwa ni ya madawa ya kulevya na tuna genge letu ambalo linatikisa hapa mjini na mshukukuru mlinishtukiza mnafikiri mngetoka salama?"

Hens aliona awaeleze kila kitu ambacho alikijua bila shaka ni kutokana na kumuona izrael akiivizia roho yake.


" Vivian yuko wapi? Na kwanini ulikuja kwa Daktari Yakoub? "

Titiana alimuuliza swali jingine.


" Kwa Daktari nilikuja kummaliza mara baada ya kushindwa kutunza siri ya kutoroshwa kwa Bi Elizabeth ambako aliwaeleza Bodi ya wakurugenzi ya Hospitali ya St. Mathew wakati wakimhoji sababu yeye ndiye alikuwa Daktari wa zamu siku ile na kuhusu Vivian tayari yuko Gaborone kumshughulikia mateka aliyetekwa majuma kadhaa uwanja wa ndege."

Hens alifunguka.


" Kivipi? Bi Elizabeth si bado mgonjwa? Na huyo mateka unalijua jina lake? "

Jessica alimuuliza huku Titiana akiitega simu yake vizuri kwa ajili ya kumrekodi.


" Ha ha ha ha ha kumbe ninyi ni wageni kwenye mchakato huu? Poleni sana dada zangu, naomba niwaambie kuwa Mackdone ni mtu hatari sana na siku zote huwa hafanyi kazi kwa hasara hata siku moja yeye hujenga urafiki na watu wake wa karibu kisha kuwatumia kwa maslahi yake binafsi. Bi Elizabeth ni kweli alikuwa mgonjwa wa koma mara baada ya kupata ajali ambayo aliitengeneza mwenyewe Mackdone na baada ya kukaribia kupata fahamu aliwaambia madaktari pale Afrika ya Kusini kumchoma shindano za dawa ambayo ingemlaza kitandani kwa muda wa mwezi mmoja kisha taratibu zikafanywa akaletwa huku ambako alifikishwa St. Mathew Hospital na kukutana na Daktari Yakoub ambaye alimuandaa na kisha kumshindilia madawa ya kulevya ambayo kayapeleka Gaborone Botswana."

Simulizi ya Hens iliwatoa macho wakina Jessica kwani ni kitu ambacho hawakukitarajia wao walijua kuna undugu baina ya Bi Elizabeth na Mackdone kumbe ni Utumwa usiokuwa na maana. Walipoisikia hadithi hiyo hawakutaka kupoteza muda eneo kwani kila kitu walikisikia kutoka kwa Hens hivyo Jessica alimfuata Hens pale chini na kumfyatulia risasi tatu za kichwani kisha waliondoka na kumuacha Hens hapo akiwa marehemu pamoja na gari lake.


"Tukitoka hapa nafikiri tukaungane na wenzetu kule Botswana kama ulivyosikia kuwa Daktari Abbas yuko mikononi mwa Mackdone."

Jessica alimwambia Titiana wakiwa njiani kutoka porini kuja barabarani.


"Ni kweli japo nina uhakika hawatamfanya chochote mpaka Bi Elizabeth apate ahueni kwa majeraha yake mara baada ya kutolewa madawa."

Titiana alikubaliana naye japo alijenga imani kwa kile alichokiamini.


"Hivi itakuwaje pindi atakapojua kuwa mtu anayemuamini alimtumia kwenye kusafirisha madawa ya kulevya? Kweli hii Dunia haijaishiwa vituko."

Jessica aliongea huku akiisimamisha Bajaj iliyokuwa ikija.


"Watajua wao wenyewe sisi tujitahidi jioni ya leo tuwe Uwanja wa Ndege ili ikiwezekana kesho tuwe Botswana."

Titiana alimjibu huku wakiingia kwenye Bajaj hiyo ambayo iliwapeleka mpaka hotelini ambako huko walikwenda kujiandaa kwa safari ikiwa ni pamoja na kukata tiketi mtandaoni.


NDANI YA GABORONE BOTSWANA


Ikiwa ni asubuhi ya saa tano wakina Jessica walikuwa wanatoka ndani ya jengo la uwanja wa ndege kwa kutumia moja ya taxi zinazofanya safari zake kutoka Uwanjani hapo na kuelekea maeneo mbalimbali ya mji wa Gaborone. Ilikuwa ni siku nzuri ambayo walikuwa wakiisubiri kwa hamu sana kuungana na wenzao hasa Titiana alikuwa na furaha isiyo na kifani kwani alijua kukanyaga ardhi ya nchi hiyo anakwenda kuungana na mpenzi wake Roberto ambaye wakina Jackline wanaamini kuwa bado wana mgogoro ambao wao waliumaliza muda mrefu.


"Dada zangu kituo wapi?"

Dereva Taxi huyo aliwauliza.


"Katutue kwenye Hoteli ya Sky."

Jessica alimjibu mara baada ya kugoogle Hoteli zote za mjini hapo na kuona huduma zinazopatikana kwenye Hotel hizo.

Baada ya kuwasili hotelini hapo walimlipa dereva haki yake kisha wakashusha mabegi yao na kuachana naye. Titiana alianza kuvuta begi kuingia ndani ya 'Sky Hotel' ndipo Jessica alipomshika mkono.


"Unakwenda wapi?"

Alimuuliza.


"Sky Hotel' si ndiyo hii hapa?"

Titiana alimjibu kwa swali.


"Niliamua kumzingua tu yule dereva Taxi si unajua tena ni miongoni mwa wachoma utambi wakubwa? Tageti yangu ilikuwa ni 'Meridian Vovo Hotel' ambayo haiko mbali kutoka hapa kwa namna nilivyoicheki mtandaoni."

Jessica alimjibu Titiana hivyo waligeuza na kuingia kwenye Bajaj ambayo iliwafikisha kwenye Hotel hiyo ya 'Meridian Vovo' wakampa nauli yake kisha wakaingia ndani mpaka mapokezi ambako baada ya kuandikisha walioneshwa vyumba vyao.


" Ndani ya Afrika tena? Kama utani vile."

Jessica aliongea huku akijitupa kitandani kwake huku Titiana yeye akiingia kuoga.


"Mimi kama ujuavyo furaha yangu iko wapi? Wacha nioge zangu kisha mengine yafuate."


Baada ya kuoga Titiana aliipiga namba ya Roberto kuona kama anapatikana kwani mpaka wanaingia Botswana hakuna Roberto wala Jackline wala Jasmine aliyejua ujio wao, walifanya safari kimya kimya.


JE NINI KINAKWENDA KUTOKEA NDANI YA GABORONE BOTSWANA?



Baada ya mapumziko walitoka kwa lengo la kwenda kutafuta baadhi ya mahitaji ambayo yatawasukuma kwa kipindi chote ambacho watakuwa ndani ya Gaborone hivyo walitoka ndani ya Meridian Vovo Hotel' na kutoka zao mpaka maeneo ya 'Mandela Plaza' ambapo hapo waliingia na kwenda moja kwa moja mpaka kwenye duka la mavazi. Hapo walinunua mavazi ambayo zaidi yalikuwa ni ya kiume.


"Mimi nadhani hizi suruali nne za jinsi mvuto zanitosha labda niongeze na makoti marefu kadhaa hivi maana nataka tukiingia kitaa iwachukue muda kutubaini."

Titiana alimwambia Jessica ambaye alikuwa bize na 'heads cover' ambazo zilimvutia kimuonekano.


"Fanya fasta mimi nakusubiri tu wewe hapa."

Jessica alimjibu Titiana.


"Niko kamili sasa tunaweza kuondoka."

Titiana aliongea akiwa anafanya malipo ya vitu alivyonunua yeye na vile vya Jessica na baada ya kukamilisha walitoka na kuelekea eneo moja ambalo huuza magari yaliyotumika linalofahamika kama 'Forks Motors' ambalo haliko mbali sana jengo la 'Mandela Plaza'.


"Kaka habari."

Jessica alimsalimu kijana waliyemkuta mapokezi.


"Salama dada zangu, karibuni."

Aliwakaribisha.


"Tunashukuru sana kaka, ni mitambo gani ya kijanja unayo hapa?"

Jessica alimuuliza yule kijana ambaye moja kwa moja aliwatolea kitabu chenye kila aina ya magari waliyonayo.


"Mnaweza kuangalia hapa yapo ya kila aina."

Aliwaambia huku akiwakabidhi kile kitabu.


"Pamoja na hiki lakini wewe tayari unajua ni mashine gani ndogo lakini ikiatamia barabara kila mmoja abakie macho kodo."

Titiana alijaribu kumfafanulia kijana huyo wa 'Forks Motors' ambaye aliupokea ushauri huo na kuwapeleka yaliko magari hayo.


"Mizigo yenyewe ni hii hapa na haya mnayoyaona hapo ndiyo yenye kasi sana na hupita popote pale kutokana na muundo wa hizo tairi."

Aliwasimulia kijana huyo ambaye alikuwa akiwazungusha kutoka gari moja mpaka jingine. Lakini macho ya Jessica yalitua kwenye gari moja dogo lenye rangi nyekundu.


" Wee kaka lile gari pale lina sifa gani? "

Jessica alimuuliza kijana huyo huku akilisogelea lile gari.


"Hii ni aina mpya kabisa ya gari kutoka nchini Tanzania ikiwa imetengenezwa na Karakana ya Jeshi la nchi hiyo na kuyaita Nyumbu. Na kama mlionavyo hili ni Nyumbu C8 gari la kisasa kabisa ambalo kwa sasa linafanya vizuri sokoni."

Kijana huyo alilielezea gari hilo.


" Sasa kaka yangu umetoa maelezo marefu sana lakini kwa mujibu wa bango lenu ni kwamba mnajishughulisha na magari yaliyotumika tu iweje na haya mapya muwe nayo? "

Jessica alimuuliza.


" Ni kweli kabisa usemacho dada yangu sisi huuza magari yaliyotumika lakini Umaarufu wa kampuni yetu ulitufanya kuingia mkataba wa kibiashara na serikali ya nchi hiyo kwa ajili ya haya magari ya Nyumbu."


"Okay sawa bwana ndiyo inakwenda kwa bei gani? Maana macho yetu yamenata kwenye hili ili na sisi tuandike historia ya kuwa watu wa mwanzo kuendesha magari kutoka kwa Mwalimu Nyerere."

Titiana alimtaka awatajie bei ya hilo gari.


"Kwa sasa nchi hiyo iko chini ya kiongozi mwingine anayefahamika kama John Pombe Magufuli 'Hapa kazi Tu' na inasemekana huyu Rais kaiweka nchi hiyo kwenye mstari hatari."

Kijana huyo ambaye alionekana kupendezwa na mfumo wa Uongozi wa Rais wa Tanzania alijisahau mpaka ambacho alichoulizwa.


" Kaka samahani wenzako tuna haraka tunataka kujua gharama ya hili gari bwana."

Jessica aliona amkatishe.


" Samahani, hilo linauzwa dola elfu kumi na mbili lakini naweza kuwafanyia dola elfu kumi na moja keshi."

Baada ya kutajiwa kiasi hicho cha fedha Jessica alitoa kadi yake na kufanya malipo na baada ya kukamilika waliingia kwenye hilo gari na kuondoka sehemu hiyo na kurejea hotelini kwao.


" Nyumbu C8 ni mashine aise yaani unagusa tu dude hilooo hatari sana na kwa namna lilivyo litatufaa sana kwenye kazi yetu."

Titiana aliweza kulisifia gari hilo wakati huo wakipaki kwenye maegesho ya magari pale Hotelini.


"Wajipange safari hii tumekuja kivingine si wale wa miaka kadhaa nyuma."

Jessica alimjibu huku akishusha mizigo yao kwenye gari lao. Lakini wakiwa wanamaliza kutoa mizigo yao mara kuna kijana alitoka ndani ya hoteli hiyo akiongea na simu na kuongoza upande ule wa maegesho.


"Bi Elizabeth bado hajazinduka na Daktari wake anasema mpaka kesho kutwa atakuwa sawa na kuhusu yule mateka ni pasua kichwa Bosi yaani pamoja na mateso tunayoendelea kumpatia lakini hajaongea lolote kuhusu waliko watoto wake pamoja mke wake...."

Maongezi hayo yalivuta usikivu wa masikio ya Jessica ambaye alimpa ishara Titiana ya kusubiri kwanza ili aendelee kumsikiliza kijana huyo.


" Tunachosubiri ni amri yako Bosi hata ukisema leo sisi ni utekelezaji tu na si kingine."

Jessica alijifanya kusikiliza simu yake kama kuna maelekezo alikuwa anapata huku akisogea upande ule aliko yule kijana bila shaka alitaka kujua zaidi kijana huyo alikuwa anaongea na nani.


" Nashukuru Bosi ngoja niwahi najua Vivian na Nawane watakuwa na hofu nami kwani nimechukua muda mrefu toka tulipoachana."

Baada ya kuongea hivyo alikata simu na kuangalia huku na kule kisha aliingia kwenye gari lakini kabla hajafanya chochote Jessica alikuwa mlangoni akigonga kioo cha mbele.


" Nikusaidie nini mrembo? "

Kijana huyo alimuuliza mara baada ya kushusha kioo na kumchungulia.


"Samahani kaka unafanya biashara ya Taxi?"

Jessica alimuuliza huku simu ikiwa bado sikioni kama kuna mtu anawasiliana.


"Samahani dada kuna mtu naongea naye mara moja nitakupigia baada ya dakika kadhaa."

Alitoa simu sikioni kisha akawa kama vile anakata simu na akaiweka kwenye mkoba wake na kisha kuinamia pale kwenye kioo.


"Ndiyo kaka."

Alikuwa tayari kumsikiliza kijana huyo ambaye alikuwa katulia akimsubiri amalizane na simu.


"Samahani mrembo mimi sifanyi biashara ya Taxi ila kama hutojali naweza kukupa lifti."

Kijana huyo alimjibu huku akimfungulia mlango aweze kuingia.


"Aisee asante sana kwa msaada wako kaka yangu."

Jessica alimshukuru huku akiuweka mkoba wake sawa mapajani.


"Wala usijali mrembo si unajua tena kwa mrembo kama wewe ni kidume gani anaweza kukataa?"

Kijana huyo alimjibu huku akiwa kaliachia tabasamu lake na macho yake yakiwa kwa Jessica akiamini kaokota dodo kwenye shamba la miwa.


"Hamna bwana nina urembo gani mimi hapa mwili umekaukiana kiasi hiki?"

Jessica alimjibu kijana huyo ambaye alikuwa kaelekeza macho yake kwenye kioo cha juu akilirudisha gari nyuma.


"Siku zote warembo ndivyo mlivyo huwa hampendi kusifiwa hata kidogo."

Kijana huyo aliendelea kumganda Jessica na muda huu walikuwa wakiiacha hoteli hiyo.


"NIKO NYUMA YENU TARATIBU SIMU USIITELEKEZE."

Ulikuwa ni ujumbe kutoka kwa Titiana aliyekuwa nyuma akiwafuatilia.


***


Baada ya kuondoka kule kijijini ambako waliwaacha watoto Natalie na Nathan chini ya mzee Minyetye ambaye aliwaahidi kuwalinda kwa kipindi chote ambacho watakuwa mjini na aliwashauri wafanye hivyo kwa usalama wa watoto kutokana na maadui wanaowawinda waliwasili mjini na kuanza kulitafuta jengo hilo ambalo walielekezwa na mzee Minyetye ambako inasadikika kuwa ndiko alikohifadhiwa Daktari Abbas.


"Hii kali ndugu zanguni humu wote ni wageni wa jiji sasa hilo jengo tutalifikiaje sijui?"

Jackline aliwaambia wenzake muda huo alikuwa akilisogelea jengo moja ambalo lilionekana ni kuukuu hivi na kisha kusimama mbele kidogo kama mita hamsini kutoka lilipo geti la jengo hilo. Na walipokuwa wakishuka garini kuna gari lilikuja na kusimama getini kisha walishuka watu wawili mwanaume na mwanamke lakini kilichowashangaza ni mwanaume yule alionekana kama vile kudhibitiwa na yule mwanamke.


"Wenzangu mnaelewa kinachoonekana mbele yetu? Maana mimi naona kama filamu hivi."

Aliongea Mahmoud ambaye alikuwa katoa macho yake kufuatilia kile walichokuwa wanakiona nyuma yao. Lakini ghafla hali ya hewa ilichafuka mara baada ya walinzi wa jengo lile ambao walitokea juu ya fensi ile na kuanza kufanya mashambulizi kuwaelekea watu wale.


"Oooh kumechafuka tuondokeni harakaaaa..."

Jackline aliongea akiingia garini na wenzake kufuata kisha kuondoka kasi kwa kuhofia kushambuliwa kwani hawakuwafahamu wale watu walikuwa wakina nani. Walitimua vumbi kama vile wako kwenye mashindano ya magari.


"Hivi jamani yule mwanamke alikuwa ni nani? Na kwanini alimshikilia yule kijana?"

Roberto aliwauliza wakina Jackline.


"Mimi ndiyo nimechanganyikiwa kabisa kwa nililoliona pale mpaka nina wasiwasi kama yule mwanamke ambaye sijui kama ni askari iwapo ni mzima au kapoteza maisha maana si kwa zile risasi."

Jasmine aliongea hayo huku akifungua kopo la maji ili aweze kunywa.


"Au yule mzee Minyetye alitaka kutukamatisha kwa Mackdone?"

Jackline alionesha hofu juu ya mzee Minyetye aliyekuwa kawapa maelekezo ya eneo hilo. Na muda huo walikuwa tayari maeneo ya katikati ya mji na kusimamisha gari lao mbele ya Restaurant moja inayofahamika kama Olympics kwa ajili ya kupata chochote kwani muda huo tayari ilikuwa ni magharibi jua likiwa linazama taratibu kabisa.

Waliingia wakachukua nafasi na kuagiza chakula kutoka kwa wahudumu wa humo Restaurant. Lakini wakiwa wanaendelea kutoa maelekezo kwa mhudumu huyo mara zoezi lilisimama ghafla huku macho yao yalihamia kwenye televisheni kubwa iliyokuwa mle ndani ambayo iliwashtua kidogo kwa mlio na maandishi yaliyojitokeza.


"BREAKING NEWS........"


NI BREAKING NEWS YA NINI?




"Katika mtaa mmoja unaofahamika kama 'Blackhawks' kumetokea majibizano ya risasi baina ya makundi mawili ambayo mpaka sasa haijafahamika sababu kutokana na wapiganaji kutokomea mtaani mara baada ya askari wa doria kutokea. Mtu mmoja mwenye jinsi ya kiume amekutwa eneo hilo akiwa kafariki, habari kamili endelea kufuatilia vipindi vyetu vinavyofuata... "

Taarifa ile iliwashangaza kidogo wakina Jackline.


" Inawezekana walikuwa wamedhulumiana hela?"

Roberto aliongea akichota chakula.


" Hapana mwenzenu bado nina mashaka na jengo lile kwanini tukio litokee sehemu ambayo tulikuwa tumeelekezwa?"

Jackline alionesha hofu juu ya mtaa ule.


"Sasa kama aliyekufa ni mwanaume vipi yule mwanamke? Amepona kweli?"

Jasmine aliuliza juu ya kile ambacho walikishuhudia eneo lile. Hakika walikosa majibu ya maswali yao kwani hakukuwa na mtu wa kuwapa majibu hayo hivyo waliamua kula haraka haraka kisha kurudi tena mtaa ule kujaribu kuona kama wanaweza kufanya chochote ndani ya jengo lile.


"Lakini tunatakiwa tupite barabara tuliyotokea kwa usalama wetu."

Jasmine alitoa ushauri kwa wenzake hivyo kila mmoja alikubaliana na wazo lake, baada ya kumaliza kupata chakula walitoka na kuingia kwenye gari lao na safari ya kurudi mtaa ule wa 'Blackhawks'. Wakiwa barabara wanachana mbuga mara walimuona kando ya barabara akiwa anajivuta kwa tumbo huku mkono mmoja akiwa kauelekeza juu.


"Jackline hebu simamisha gari."

Jasmine aliongea aliongea mara baada ya kumuona mtu huyo upande wake akijivuta kutoka mtaroni na kuomba msaada. Baada ya gari kusimama walishuka kumfuata mtu huyo aliyekuwa akihitaji msaada.


"Whaaaat ! Siamini macho yangu hata kidogo au naota jamani."

Jasmine aliongea kwa mshangao baada ya kumkuta mtu huyo na kumtambua kuwa ni mdogo wake Jessica akiwa katapakaa damu mwili mzima.


"Haw....hawani...weziiiii waleee....." Alishindwa kuendelea akakata kauli na kuwafanya wakina Jackline kutazamana.


"Jessica kaja lini huku? Na anafanya kazi na nani? Kwa hiyo katugeuka?"

Roberto alijiuliza swali huku akiwa anabonyeza simu yake.


"Titiana uliachana lini na Jessica?"

Roberto alimuandikia meseji mpenzi wake kumuuliza ni lini waliachana huko Australia.


"Mmemuona popote?"

Badala ya kujibu yeye aliuliza swali jingine.


"Tumemuona? Kivipi?"

Roberto aliuliza tena.


"Aliniacha hotelini na kuingia kwenye gari moja la kijana fulani ambaye alimshakia sijui waliongea nini nikamuona akipanda hilo gari hivyo na mimi nikaanza kuwafukuzia lakini tulipofika eneo moja hivi ambalo lilikuwa na msongamano wa magari tulipoteana."

Titiana alimuelekeza Roberto.


" Ina maana mko hapa hapa Gaborone? "

Roberto aliendelea kumtupia maswali Titiana ambaye hakumjibu tena swali hilo na badala yake alimzimia simu kabisa.


" Kuna nini Roberto mbona kama vile kuna? Maana umesimama hapo muda mrefu tunakupigia honi ndiyo kwanza huna habari."

Jackline alimuuliza baada ya kumfuata pale mbele ya gari.


"Bado nawaza huyu Jessica imekuwaje tumemkuta hapa na anahusika vipi na wale watu?"

Roberto aliamua kudanganya.


"Hebu tumuwahishe kwanza Hospitali hayo mengine ni baada ya kuzinduka."

Jackline alimjibu Roberto na kumshika mkono kuelekea kwenye gari ambako walipanda na kuondoka huku Jasmine akiwa amekaukiwa kwa kilio.


"Tunampeleka Hospitali gani?"

Jackline aliuliza huku Mahmoud yeye muda wote alikuwa kimya akimuangalia tu Jessica bila shaka alikuwa akimuuliza maswali ya kimoyomoyo kwani kitendo cha kumuokota eneo lile na kabla walishuhudia tukio maeneo yale kila mmoja alikuwa na maswali yake juu ya Jessica kwani wao walijua yuko zake Brazil huku Roberto yeye alijua alikuwa Australia.


"Kwa usalama mimi nafikiri tumpeleke kijijini kwa mzee Minyetye akamshughulikie kiasili maana hatujui maadui zake ni wakina nani?"

Roberto alitoa pendekezo ambalo kila mmoja alikubaliana na wakati huo Jackline alisimamisha gari na kushuka kisha akamtaka Mahmoud aje kuendesha ili yeye arudi nyuma kumtuliza Jasmine ambaye alikuwa akiendelea kulia tu na hakuwa tayari kutulizwa na mtu pamoja na jitihada zote za Roberto.

Mahmoud baada ya kuingia kwenye usukani aliondoa gari kasi kuelekea kijijini kumuwahisha Jessica kwenye matibabu.


"Roberto unaonaje kama ukimtafuta Titiana maana naingiwa na hofu mwenzenu."

Jackline alimwambia Roberto hayo huku naye machozi yakimtoka, hivyo Roberto alimtumia ujumbe Titiana kuwa ampigie simu Jackline na kumtaka amueleze kila kitu juu yake na Jessica kuwa ndani ya Gaborone. Dakika sifuri kabla Roberto hajapiga simu mara simu ya Jackline iliita na kumfanya Roberto kutabasamu kiaina.


"Haloo naongea na nani mwenzangu?"

Jackline aliuliza baada ya kupokea simu kwani ni namba mpya iliyompigia.


"Naitwa Titiana, kwema wifi?"

Titiana alijitambulisha.


"Titiana? Mbona code ni ya Botswana?"

Alimuuliza baada ya kuangalia na kuiona namba kiunganishi ni ya nchi waliyopo.


"Yes my wifi ni mimi na niko hapa hapa Botswana."

Titiana aliamua kueleza ukweli kama alivyoelezwa na Roberto afanye.


"Makubwa!!! Kwa hiyo ulikuwa na Jessica?"

Jackline alimuuliza.


"Ndiyo ila tumepoteana kama masaa mawili yaliyopita."

Titiana aliendelea kumsimulia.


"Uko wapi maana nina maswali mengi ya kukuuliza?"

Jackline alimuuliza.


"Niambie ulipo nitakuja ila mimi muda huu napatikana 'Meridian Vovo Hotel' ndipo tulipofikia sisi."

Hakuwa na la kuongeza mara baada ya kujua sehemu anayopatikana alikata simu na kuiweka mfukoni huku akimuangalia Roberto.


***


"Imekuwaje huko?"

Mackdone alimuuliza Henry.


"Kila kitu kimekwenda vizuri na Hamza ameshajitambua japo anaongea mambo yasiyoeleweka bila shaka ni kutokana na Oparesheni aliyofanyiwa."

Henry alimjibu Mackdone.


"Kazi ambayo niliwapa mmeitekeleza?"

Mackdone alimuuliza swali jingine ambalo hakulitegemea hata kidogo.


"Bosi kifupi yule mtu alitutoroka siku mbili zilizopita na hatujui kaelekea wapi kama ujuavyo huku sisi ni wageni."

Henry alimjibu Bosi wake Mackdone ambaye kwa sasa alikuwa kajichimbia nje ya mji wa Pretoria nchini Afrika ya Kusini.


"Nimebaini ninyi hamko makini na kazi ninazowapatia hivyo basi ponapona yenu ni kuhakikisha huyo mtu anapatikana na mkimkosa tu jibu mnalo."

Baada ya kumwambia hivyo Henry alimkatia simu na kuipokea simu ya Nawane ambayo ilikuwa ikiingia.


"Enhh umesema nini kimetokea huko?"

Mackdone alimuuliza Nawane.


"Bosi mtu wako ambaye ulituongezea sifuri kabisa kwani alitekwa na msichana ambaye hatujamtambua katokea wapi."

Nawane alimwambia bosi wake kilichotokea.


"Katekwa?"

Alimuuliza tena.


"Si kwamba alitekwa tu bali kauawa wakati wa mashambulizi baina yetu na msichana huyo ambaye alitukimbia baada ya askari kutokea na kwa namna alivyokuwa akikwepa risasi anaonekana kabisa si wa kawaida japo tulimuotea kadhaa hivi."

Nawane alimjibu.


"Unaongea nini mshenzi, mnafanyaje mambo kijinga hivyo sasa angalia askari wameshalijua hilo eneo letu hujui ni hatari? Na huyo mwanamke mkamuachia aondoke hamjui lazima atapeleka taarifa kwa waliomtuma?"

Mackdone alichanganywa na taarifa za Nawane juu ya kilichowapata.


" Hapana bosi tumechukua tahadhari haraka kwa kumuondoa Daktari Abbas pale na pia vijana wetu wako mtaani kumsaka msichana huyo mpaka apatikane."

Nawane alishajua nini kitafuata kwa taarifa mbovu kama hizo hivyo ilibidi amtulize kwa majibu yake.


"Okay hakikisheni kila kitu kinakuwa sawa, tumeelewana?"

Mackdone alimtahadharisha Nawane na kukata simu.


"Ole wao waniletee ujinga hapa nitawakoboa wabichi wabichi mpaka wakome."

Mackdone alijisemesha mwenyewe huku akitoa sigara na kuiwasha. Kisha akasimama na kuelekea dirishani na kuanza kuivuta huku akitazama uzuri wa jiji la Pretoria mida hiyo ya usiku. Lakini ghafla simu yake iliingia ujumbe mfupi ambao aliufungua na kuusoma.


"KWA CHOCHOTE AMBACHO UNAKIFANYA JUA KIKO WAZI HIVYO HUNA UJANJA. NA KWA TAARIFA YAKO TUMEBAINI YOTE ULIYOMFANYIA BI ELIZABETH HUKU UKIJIDAI KUMSAIDIA JIANDAE MACKDONE."


Ujumbe ule ulimchanganya sana na kumfanya aamue kuipiga ile namba ambayo ilituma ujumbe.


" Shiiiit..... "

Mackdone alichukia mara baada ya kutoipata hewani ile namba. Alirudia tena na tena lakini hali ilikuwa ni ile ile kitu ambacho kilimfanya ampigie Vivian.


"Naam Mkuu."

Vivian aliitika mara baada ya kupokea simu.


"Ni hivi Vivian kuna mtu anatufuatilia na kwa namna inavyoonekana anafahamu kila kitu kumhusu Bi Elizabeth na kile tulichomfanyia hivyo kuweni makini zaidi na ikiwezekana imarisheni ulinzi kwenye hilo jengo na hakikisheni hao vifaranga wa huyo Daktari wanapatikana wakiwa hai ili kabla ya kifo chao ni lazima warudishe faida kwa kutubebea madawa kuyapeleka Mexico."

Mackdone alimweleza Vivian na kisha kukata simu na kuitupa kitini na kisha aliifuata pakiti ya sigara na kuichomoa nyingine na kuiweka mdomoni.


JE NINI KITAENDELEA?




Walifika kijijini na haraka wakamshusha Jessica ambaye muda huyo alikuwa hajitambui hata kidogo na hakujua yuko wapi na kwa upande mwingine wakina Jackline walikuwa wakijiuliza juu ya lile tukio lililotokea kwani walilishuhudia kwa macho yao japo hawakujua ni nani aliyekuwa akipambana na kundi lile.


"Abee shemeji..."

Jackline aliitika baada ya kuipokea simu ya Daktari Hans.


"Mmefikia wapi shemeji? Kapatikana rafiki yangu?"

Daktari Hans aliuliza.


"Shemeji mpaka sasa hakuna chochote tulichoambulia japo tulikuwa tunalikaribia eneo alilohifadhiwa."

Jackline alimjibu Daktari Hans.


"Ni nini kiliwazuia msimfikie?"

Daktari Hans aliendelea kumtupia maswali Jackline ambaye alishindwa kuyahimili.


"Shemeji samahani kuna jambo tunalifanya hapa nitakueleza baadaye kidogo."

Jackline alimjibu na kisha alikata simu na kurudi pale chini ya mti alipokuwa kalala Jasmine baada ya kulia kwa muda mrefu alipitiwa na usingizi.


"Hivi mama ni nani anayefanya haya?"

Nathan alimuuliza mama yake baada ya kukaa chini.


"Mwanangu haya mambo ni makubwa sana mtayajua tu pindi mkiwa wakubwa, sawa Mwanangu?"

Jackline alimjibu mtoto wake huku akimpigapiga mgongoni na machozi yakiendelea kumtoka na macho yake yakiwa kwa Natalie aliyekuwa akipiga maembe.


"Mzee Minyetye niambie tafadhali anaendeleaje kuna uwezekano wa kupona?"

Jackline alimuuliza mzee Minyetye alipotoka nje akiwa na kibakuli chenye maji ya rangi ambayo bila shaka ilikuwa ni dawa.


"Naomba mnipe muda wa kutosha niifanye kazi yangu kwa umakini mkubwa."

Mzee Minyetye alimjibu Jackline huku akiingia kijumba alichokuwa Jessica. Jackline aliona isiwe shida aliinuka pale alipokuwa na watoto wake na kuwafuata wakina Roberto waliokuwa ndani ya gari.


" Vipi kuna matumaini yoyote? "

Roberto alimuuliza Jackline.


"Mmh naona tuendelee kumuombea kwa Mungu maana namuuliza mganga ananijibu kuwa tumpe muda wa kutosha hivyo naona tutoke kidogo tukaonane na Titiana atueleze ilikuwaje."

Jackline alimjibu Roberto huku akipanda ndani ya gari huku watoto wake wakilia pale chini.


" Mama unatuacha tena? "

Natalie alimuuliza swali ambalo lilimfanya Jackline ashuke kwenye gari na kuwafuata pale chini kisha akawakumbatia.


" Sikilizeni wanangu wapendwa siyo kwamba nawaacha, nawaachaje peke yenu kwenye mazingira kama haya? Lakini inabidi nifanye hivyo kama mnavyojua baba yenu bado hajapatikana hivyo tunaendelea kumtafuta tupate kujua yuko wapi lakini pia nimeshaongea na mama yenu mdogo Shamimu aje awafuate mkaishi kule aliko mpaka amani irejee."

Jackline aliwaelezea kwa kirefu watoto wake juu ya kinachowafanya kutengana nao mara kwa mara.


" Hivi mtampata baba yetu akiwa hai kweli mama? "

Natalie aliuliza kwa sauti ya upole huku akimuegea mama yake begani.


" Mimi nina uhakika baba yetu atapatikana tu, ila mimi siwezi kuondoka mpaka baba yangu apatikane."

Nathan aliongea kitu ambacho kilichomfanya mama yake amvute karibu yake.


" Msijali wanangu baba yenu tutampata tu ninachowaomba msimsumbue tena babu kama mlivyofanya mwanzo na hata hivyo kwa sasa mtabakia na mama yenu mdogo, sawa? "

Jackline aliwapa maelezo ambayo kidogo yaliwatuliza.


"Sawa mama tumeelewa, byeeeee...."

Waliondoka huku Natalie akimuaga na kumpungia mkono wa kwaheri. Hivyo wao walipanda kwenye gari na kuondoka. Wakiwa njiani Jackline alimtumia ujumbe mfupi Jasmine.


"Jasmine usiondoke tunarudi muda si mrefu kuna vitu tunavifuatilia mjini."

Na baada ya kuutuma ujumbe huo aliiweka simu yake mfukoni.


"Hivi jamani ninyi muonavyo Jessica anaonesha dalili ya kupona kweli?"

Mahmoud aliwauliza wenzake akiwa nyuma ya usukani.


"Tuko tayari kwa lolote wapendwa kwani haya yamekuwa ndiyo maisha yetu toka tumejitambua hapa chini ya jua. Tumepoteza wapendwa wetu wangapi jamani kikubwa ni kumuombea tu Mungu aweze kumponya Jessica apone na kuungana nasi kwa mara nyingine."

Roberto alitoa jibu ambalo kila aligeuka kumtazama maana lilikuwa la kijasiri sana.


" Ni kweli lakini tuwe na matumaini naye kuwa muda wowote atapona tu hizo hofu mlizonazo zishindwe na ni roho za Kishetani mnatakiwa mzikemee zitoke."


Jackline aliwajibu baada ya kuona wenzake wana wasiwasi na hali ya Jessica.


"Sawa dada Jackline lakini hofu ni lazima kumbuka na sisi ni binadamu hofu ni muhimu."

Roberto alimjibu.


Baada ya safari ya muda mrefu kidogo waliwasili mjini na kuelekea moja kwa moja mpaka Hotel ya 'Meridian Vovo' na kuingia ndani kisha kulipaki gari na kutafuta sehemu tulivu wakaketi kisha Jackline akamtafuta Titiana kwenye simu huku Roberto akiwa katulia tuli kama vile hajui kinachoendelea.


"Tumefika hapa 'Meridian Vovo' uko wapi?"

Jackline alimwambia Titiana mara baada ya kupokea simu.


"Okey nakuja niwakute nilikuwa nimetoka mara moja maana mpaka sasa Jessica hajarudi hivyo sijui kilichomkuta."

Titiana alimjibu.


"Basi usichelewe sana tuweze kulijadili hilo kwa pamoja."

Jackline alimtaka awahi kurudi kutoka huko aliko.


"Bila shaka wifi yangu mwenyewe."

Titiana alimjibu na kisha akakata simu. Wakati anaiweka simu mfukoni mara macho yake yakagonnga kwa msichana mmoja aliyepita na kuingia ndani ya hoteli hiyo na hivyo Jackline akampa ishara Roberto amfuatilie msichana huyo. Roberto aliinuka na kumfuata nyuma msichana huyo ambaye Jackline alimfananisha.


"Umemfahamu huyo msichana?"

Jackline alimuuliza Mahmoud aliyekuwa akicheza na simu yake.


"Yupi huyo?"

Mahmoud aliuliza swali kama vile hakujua kilichoendelea mpaka Roberto anaondoka.


"Uko wapi wewe?"

Jackline alimuuliza kwa ghadhabu kidogo.


"Kuna vitu navifuatilia kutoka kwenye lile jengo ambalo Jessica alifanyiwa ule unyama."

Mahmoud alimjibu huku akiwa bado anacheza na simu.


"Okay lakini hiyo kazi hebu achana nayo kwanza kuna kanyama kameingia humo ndani na Roberto kaingia kukawinda hivyo kaa mkao wa kula."

Jackline alimwambia Mahmoud huku akiinua simu yake kuongea na Titiana ambaye alimpigia.


"Niambie Titiana?"

Jackline alimuuliza.


"Nimeshafika uko wapi?"

Titiana alimjulisha kuwa kafika.


"Njoo huu upande ambao kuna miavuli."

Jackline alimuelekeza Titiana.


"Okay nimekuona."

Titiana alimjibu na kukata simu.

Na baada ya dakika kadhaa Titiana aliwasili pale alipokaa Jackline.


"Hey my sister-in law' waooooo.."

Titiana alimrukia Jackline baada ya kumfikia.


"Jamani wifi wa mieee ndiyo nini sasa kwa mlichotufanyia?"

Jackline hakutaka kupoteza muda alimtupia swali.


"Ni stori ndefu kidogo wifi hebu twende ndani ili nikabadili na hizi nguo maana zimechafuka mpaka basi."

Titiana alimjibu Jackline na hivyo walielekea ndani ambako kuna chumba chao. Lakini walipokuwa kwenye ngazi kuelekea ghorofani kwa chini waliweza kumuona Roberto na Mahmoud wakiwa kwenye moja ya mlango wametulia kwa nje huku masikio yao yakiwa yametegeshwa.


"Wanafanya nini pale wakina Robbie?"

Titiana alimuuliza Jackline baada ya kuwaona wakina Roberto wakiwa kwenye moja ya milango ya hoteli hiyo.


"Wewe twende zetu watatupa taarifa baada ya kuikamilisha kazi yao."

Jackline hakuwa tayari kumueleza hivyo alimtaka wawasubiri wenyewe watatoa majibu hivyo waliachana nao na kuendelea kupanda ngazi. Walifika na kuingia kwenye chumba cha wakina Titiana.


"Wee Titiana hebu niambie ilikuwaje mpaka leo hii mko hapa maana kwa namna hiki chumba kilivyo inaonesha ni namna gani mlijiandaa, hee na hizi si ni nguo za Jessica? Kwa hiyo ni kweli mlikuwa pamoja?"

Jackline alishangazwa na kile alichokutana nacho mle chumbani kwani wakina Jessica walikuwa na mabegi ya nguo ya kutosha kuashiria kuwa hawakuwa watu wa kuondoka karibuni.


" Ukionacho ni sahihi kabisa wifi yangu kama ambavyo nilikwambia kuwa nitakueleza kila kitu tukiingia ndani na hiki ndicho nilimaanisha."

Titiana alianza.


"Kipi hicho mbona unaniweka roho juu juu kiasi hicho?"

Jackline aliuliza.


"Ni hivi wifi yangu baada ya kumaliza kozi yangu na kumaliza utata wetu kati yangu na Roberto nilipanga kuelekea Australia kwa mapumziko lakini kabla ya kuondoka nilimshirikisha mpenzi wangu kwa namna nimjuavyo Roberto nilijua angenizuia lakini cha aja.."

Kabla hajamaliza simu ya Jackline iliita hivyo aliona aipokee tu na hivyo kumfanya Titiana atulie kwanza.


" Ndiyo Roberto, lete habari !! "

Jackline alipokea.


" Huyu mtu bado yuko ndani lakini kuna simu aliyokuwa akiongea nayo imetupa mwanga mzuri."

Roberto alimsimulia Jackline.


" Mwanga kivipi Roberto? "

Jackline alisimama mle chumbani na kumuuliza Roberto huku akilifuata dirisha.


" Ni mtu wa Mackdone huyu msichana na walichokifanya baada ya kutokea lile tukio la jana ni kwamba wamemhamisha Daktari Abbas na kumpeleka kwenye jengo liitwalo 'Dighton Sunset' ila sijui linapatikana wapi?"

Roberto alimfafanulia Jackline.


"Msiondoke hapo huyo si ndiyo yule fundi feki aliyejiita Dorice? Lazima kupitia yeye tutalifikia hilo jengo hivyo kuweni makini."

Jackline aliona amdokeze Roberto kumhusu Nawane.


"Okay ndiyooo mimi nilishindwa kumtambua kutokana na mtindo wake wa nywele, kumbe wacha sisi tuweke doria hapa."

Roberto alimjibu.


"Vizuri na sisi tuko huku juu kwenye chumba cha wakina Titiana kuna vitu tunafanya hivyo tujuzeni kila kinachotokea hapo."

Lakini wakati Roberto amejisahau na simu na kule Mahmoud ameelekeza macho yake kwenye mlango wa chumba cha Nawane mara alikuja mtu kwa nyuma na kumkaba Roberto shingoni.


" Tulia hivyo hivyo mpekuzi wa vitu vya watu wewe ukienda kinyume nami nitakufungulia dunia mpya, sawa?"

Roberto aliishiwa pozi hakuwa na jeuri tena na ukizingatia pale alipokuwa ilikuwa mbali kidogo na alipokuwa Mahmoud lakini Jackline aliweza kuyasikia maneno yale kutokana na Roberto kutoizima simu.


" Ongoza mwenyewe mpaka kwenye chumba mlichokuwa mnakivizia haraka na mikono yako iwe juu."

Mtu huyo alimuamrisha Roberto ambaye hakuwa na jinsi yoyote zaidi ya kuongoza alikokuwa Mahmoud.

Kabla hawajavuta hata hatua kumi alitokea Jackline na Titiana na kumvamia yule mtu.


" Aaaaahhhhh.......... "

Ulikuwa ni ukelele ambao aliutoa mtu huyo mara baada ya kutandikwa teke la tumboni na Roberto hii ilikuwa ni baada ya mtu huyo kujisahau na kugeuka kupambana na wakina Jackline na kumsahau Roberto.


"Sasa unaweza kutueleza wewe ni nani? Na ni nani aliyekutuma hapa na pia tueleze aliye kwenye kile chumba ukoje naye?"

Roberto akiwa kamuelekezea bastola alimuuliza maswali mfululizo.


"Unafikiri naweza kuufanya upuuzi kama huo? Brother umechelewa katika hilo."

Baada ya kuongea hayo walishangaa mtu huyo akianza kutoa damu mdomoni na puani.


"Wewe umefanya nini? Hebu jibu maswali yetu."

Roberto aliendelea kumtupia maswali.

Lakini haikuchukua muda mtu yule alipoteza maisha na hivyo kuwafanya kumkagua mwilini mwake.


"Daaa hili kundi ni hatari aisee hebu cheki hapa."

Titiana aliongea hayo mara baada ya kukiona kitu kidogo muundo wa golori mfano wa kiulezi kikiwa mdomoni.


"Ni nini hicho?"

Roberto aliuliza.


"Hii ni sumu ambayo ukiiweka tu mdomoni ndani ya dakika mbili lazima uwe mfu."

Titiana alimjibu mpenzi wake.


"Aliwezaje kuimeza wakati nimemtaiti hapa."

Roberto aliuliza tena.


"Honey ulimtaiti ndiyo lakini kumbuka ulimfunga mikono?"

Swali hilo lilimfanya Roberto kutulia kimya huku Jackline akiwa tayari kambananisha mhudumu wa Hotel ile ambaye muda wote alikuwa akipiga simu ambayo Jackline alihisi anawataarifu Polisi.


JE NINI KITAENDELEA?




"Unampigia nani simu wewe kinyago?"

Jackline alimuuliza huku kamuelekezea bastola mhudumu huyo.


"Ni..nili...nilikuwa namp...nampigia mp....mpenzi wangu tu haki ya Mungu."

Mhudumu huyo kwa hofu alimjibu huku akipiga alama ya kidole shingoni kuashiria alichokisema ni kweli tupu. Lakini Jackline alimuangalia machoni kwa muda kisha alimsogelea na kumpiga ngumi nzito ya kichwa ambayo ilimpeleka chini yule mhudumu na kisha Jackline alirudi na kuwapa ishara ya kuelekea kwenye chumba alichokuwa kaingia yule msichana ambaye ni Nawane.


"Vipi hajaonesha pua yake?"

Jackline alimuuliza Mahmoud ambaye muda wote alikuwa pale mlangoni.


"Hajafanya hivyo."

Mahmoud alimjibu Jackline na kuusogelea mlango ili achungulie kupitia tundu la kitasa.


"Haina haja kaka Mahmoud."

Roberto alimwambia Mahmoud kabla hajafanya vile na kumsukuma pembeni kisha aliupiga teke mlango na ukakubali na wote wakaingia ndani.


"Mwanaharamu huyu !!!"

Titiana aliongea baada ya kukutana na chumba kikiwaangalia tu kikiwa tupu hakina mtu.


"Kapitia hapa Kimburu huyu."

Jackline aliwaambia wenzake mara baada ya kufunua pazia la dirishani na kuiona kamba iliyosalia ikining'inia.


"Tuondokeni hakuna la kusubiri hapa."

Roberto aliwaambia huku naye akipita dirishani kupitia kamba ile ile na wakina Jackline wao wakipita mlangoni. Walipofika nje waliyafuata magari yao na safari hii waliungana na lile gari la Titiana ambalo walilinunua na Jessica liitwalo NYUMBU lakini kabla ya kuondoka walishauriana kidogo na kisha Mahmoud akatoka ndani ya ile Hotel kwa mguu na wakina Jackline waliondoka na kwenda kusimama mbele kidogo. Huku nyuma Mahmoud aliifuata Bajaj moja ambayo ilikuwa imesimama ng'ambo ya hiyo Hotel na kuingia ndani yake huku dereva wa hiyo Bajaj akiwa anarekebisha taa.


"Suka eee achana na hiyo kazi kwanza njoo huku."

Mahmoud alimwita dereva Bajaj huyo.


"Naam brother."

Dereva Bajaj huyo alikuja na kuitika.


"Unaweza kunipeleka Dighton Sunset?"

Mahmoud alimuuliza.


"Mmmhh kaka ni mbali huko lakini."

Dereva huyo alimjibu huku akiwasha Bajaj.


"Na ndiyo maana nikaingia humu najua hilo wewe si unafanya biashara?"

Mahmoud alimuuliza.


"Ndiyo nafanya lakini pia eneo hili si salama pia kwani lilikuwa makazi ya watu weupe na baada ya kuondoka yaliachwa tupu na hivyo wanyang'anyi na makundi ya Kimafia kujitwalia eneo hilo lenye majengo mengi."

Stori ya dereva Bajaj ilimvutia sana Mahmoud ambaye naye alisogea kiti cha mbele ili aweze kumsikia vizuri dereva huyo.


" Kwani wewe unalijua vipi eneo hilo?"

Dereva Bajaj huyo alimuuliza Mahmoud.


" Mmh hapana mimi nimeitwa na rafiki yangu ambaye aliniambia nije mjini na kumfuata huko ambako anajishughulisha na kilimo."

Mahmoud alimjibu.


"Okay watakuwa ni wale ambao hulima mpunga na mbogamboga karibu na majengo hayo lakini pia kuna tetesi kuwa ni miongoni mwa wafanya matukio ya kijambazi na hicho kilimo ni changa la macho kwetu wapita njia."

Mahmoud aliifurahia safari hiyo kwani alipata habari ambayo alikuwa akiitafuta.


" Kwa hiyo kutoka hapa mpaka huko kuna umbali gani? "

Mahmoud alimuuliza.


" Kwa sasa tumebakiza kama kilometa ishirini hivi kufika, unafikiri ni kwa kupotea? Hapana kwani hii barabara imepita katikati ya majengo hayo."

Wakati dereva Bajaj huyo akiwa kajisahau na maelezo yao macho ya Mahmoud yalikuwa kwenye site mirror za Bajaj hiyo akilifuatilia gari ambalo aliliona likiwa linawafuata kitu kilichomshangaza ni kuliona gari hilo badala ya yale ya wakina Jackline.


" Hili gari vipi tena mbona wakina Jackline siwaoni kuna nini?"

Mahmoud alijiuliza swali hilo kimoyomoyo.


"Kaka mbona umeduwaa au stori yangu imekutia hofu tayari?"

Dereva Bajaj huyo alimuuliza baada ya kuona mteja wake kaduwaa kimya huku akiwa mbali kimawazo.


"Hapana lakini kama binadamu mwingine hofu lazima na ninachokihofia hapa ni juu ya rafiki yangu huyo anaweza kuniingiza kwenye shughuli zake za siri, hebu simamisha Bajaj kwanza nipunguze petroli."

Maelezo ya Mahmoud yalimfanya dereva Bajaj kuanza kucheka huku akiipaki pembeni Bajaj.


" Ha ha ha ha ha kweli brother wewe ni muoga sana simulizi fupi tu mpaka mkojo? "

Wakiwa wanashuka mara lile gari liliwapita kasi na macho ya Mahmoud yalichungulia mle ndani ya lile gari kisha akaendelea kumwaga petroli yake na mara magari ya wakina Jackline yalitokea na kuwapita lakini yalisimana mbele yao.


" Kumekucha kaka nilikwambia lakini kuwa huku si kuzuri hata kidogo sasa wamekuja wenye eneo kama hatujaolewa bila kupenda hapa..."

Dereva Bajaj huyo aliongea huku akiwa anaingia ndani ya Bajaj kutaka kutoroka.


"Usifanye hivyo ungana nami tuweze kupambana nao."

Mahmoud alimuomba kwa kejeli.


"Weeeee niache niokoe roho yangu mimi, chakufanya nipe changu niondoke Mungu wangu watu wenyewe ndiyo hao wanakuja."

Lakini akiwa anataka kuigeuza Bajaj yake huku akimtaka Mahmoud ampe ujira wake.


"Hebu shuka kwenye Bajaj tuongee kidogo."

Mahmoud alimwambia huku bastola ikiwa mkononi imemuelekea kijana huyo.


"Mungu wangu kumbe na wewe ni miongoni mwao?"

Dereva Bajaj huyo aliongea akishuka mikono ikiwa juu.


"Si mbaya kihivyo ila ukitaka niuoneshe ubaya wangu naweza pia."

Mahmoud alimwambia dereva Bajaj.


"Kwa hiyo unataka nifanye nini?"

Dereva alimuuliza Mahmoud.


"Nina uhitaji msaada wako kwenye hili."

Mahmoud alimjibu huku wakina Jackline nao wakiwasogelea pale walipokuwa.


"Sikiliza mimi na hao unaowaona hapa ni wahanga, kuna kundi limemteka mtu wetu na kumhifadhi ndani ya majengo hayo ya Dighton Sunset na kwa namna ulivyolielezea eneo hilo utakuwa msaada kwetu."

Mahmoud alimfafanulia dereva Bajaj huyo.


"Kumbe ni hivyo kaka? Wala msihofu nitawasaidia katika hilo kikubwa ni kuhakikisha nakuwa salama."

Alimjibu Mahmoud.


"Kuhusu hilo tuachie sisi kwani hii ni timu kubwa na tuko vizuri kwenye kila idara na iwapo tutawatia adabu watu hao utapata mtaji wa Bajaj nyingine zaidi ya tano."

Jackline alimhakikishia dereva Bajaj huyo ambaye muda huo alianza kushusha pumzi baada ya kupata uhakika kuwa siyo watu wabaya kwake. Baada ya kukubaliana waliianza safari tena huku Jackline akiwa na Mahmoud kwenye Bajaj pamoja na dereva Bajaj huyo huku Titiana na Roberto wao wakiingia kwenye magari na safari ikaanza kuelekea Dighton Sunset. Na kwa kuwa kijana wa Bajaj eneo lile analifahamu vizuri aliwaongoza wakina Titiana.


"Waambieni wa nyuma yetu wafiche magari kwenye kimsitu hicho huku tunakwenda kwa miguu."

Dereva Bajaj alimwambia Mahmoud aliyekuwa naye mbele huku yeye akiiingiza Bajaj kwenye chaka lililo karibu na kijito kinachotiririsha maji kuelekea kwenye majengo hayo.


" Ingizeni magari kwenye kipori kinachoonekana hapo mbele yenu kisha tufuateni huku mbele."

Jackline alimwambia Roberto naye akamjulisha Titiana.

Walipofanikiwa kuyaficha walitembea kwa miguu mpaka walipo wakina Jackline na kupanga mkakati wa namna ya kuingia kwenye yale majengo.


" Naombeni mnisikilize ndugu zangu tutaingia ndani kwa kutumia hiki kijito ambacho kinapita katikati ya majengo yale mnayoyaona, japokuwa kimepita katikati lakini wao wanatumia majengo ya mbele yale kule yanayotazama barabarani hivyo haitakuwa rahisi kwa wao kuhisi chochote juu yetu kikubwa ni ninyi kuweka kichefuchefu pembeni maana kuna harufu mbaya sana."

Dereva Bajaj aliwapa maelezo ambayo yaliwashangaza wakina Jackline yaani kama vile anafanyia pale kambini.


" Umelijuaje hili eneo na siri zake zote hizo au uliwahi kuwa kibaraka wao? "

Jackline alimuuliza kijana huyo.


" Kwanza jina langu naitwa Ryan niliwahi fanya kazi hapa kipindi hicho wanalima mpunga kwa wingi na hata Bajaj yangu ni zao huku nilikuwa natumia kijito hiki kuiba magunia kwa sasa inatosha tunaweza kuondoka."

Ryan alimaliza kujitambulisha.


"Kumbe!!! Wewe ni kiboko aisee."

Titiana alimvulia kofia Ryan wakati huo wakiianza safari kuingia kwenye maji.


"Huuu huuuu maji haya ni ya baridi aise tutafika salama kweli?"

Titiana alilalamika akiwa ndani ya maji ambayo yalikuwa ya baridi sana.


"Punguzeni kelele tumeingia kwenye Himaya nyingine tusijeotewa na maadui wetu."

Ryan aliwaambia wenzake huku yeye akiwa mbele kama vile eneo analopita lina maji ya moto na kuwafanya wote kupita anamopita yeye.


sultanuwezo.com:

Walitembea mpaka eneo ambalo lilikuwa na kinjia kinachopita kwenye matete na kutokea kwenye kijumba ambacho hutumika kuchujia maji yanayotumika kwa matumizi mengine kama vile kunywa na matumizi mengine. Waliingia kwe kijumba hicho na kutua vibegi vyao na kila mmoja kuanza kuandaa mashine yake.


"Hizo tumieni wenyewe mimi naomba kisu kimoja tu."

Ryan alimwambia Roberto ambaye alitaka kumkabidhi bastola. Baada ya kila mmoja kushika kifaa chake walitoka na kutawanyika makundi mawili ambapo moja liliongozwa na Jackline pamoja Titiana huku Mahmoud akiwa na Roberto pamoja na Ryan.


" Tutakutana kwenye jengo lile pale ambalo ni ghala la mazao na ninaamini humo ndimo anaweza kuwa kahifadhiwa nina uhakika kwani wengi wamefanyiwa umafia humo."

Ryan aliwapa maelekezo wakina Jackline kisha walitawanyika kwa kupita kwenye viuchochoro kwa tahadhari.


TIMU NDIYO HIYO IMEINGIA DIGHTON SUNSET JE, ITAFANIKIWA CHINI YA DEREVA BAJAJ RYAN?




Ndani ya chumba alicholazwa Hamza katika Hospitali ya St. Consolata kulikuwa na furaha ya ajabu kwa wakina Henry pamoja na Hamza mwenyewe. Hakuna siku ambayo ilikuwa ni ya kipekee katika hospitali hii kama ilivyokuwa leo na hii ni mara baada ya Hamza kuzinduka.


"Mkuu Madaktari wa Hospitali hii ya Makete ni balaa maana kwa namna alivyokuwa Hamza niliamini kuwa umetuleta huku kutalii tu kwa upande wa Hamza nilijua anasubiri muda wake wa kuelekea ahera lakini ndiyo tena wamempigania mpaka amepona."

Henry alimsimulia Mackdone kile kilichotokea kwa Hamza lakini tofauti na matarajio yake Mackdone alimuuliza swali fupi tu na kumkatia simu na wala hakuwa na sababu ya kusubiri majibu.


" Umemaliza au bado."

Mackdone alimuuliza Henry.


" Mmh mbona hivi tena?"

Henry alijiuliza swali hili akiiangalia simu yake kuhakikisha kile kilichopelekea mawasiliano na Mackdone yakatike akidhani labda ni mtandao lakini mtandao ulikuwa vizuri hivyo kwa shingo upande aliiweka simu mfukoni na kurejea ndani.


" Kasemaje Bosi? "

Rafiki yake Henry alimuuliza swali.


"Si unamjua Bosi wako kwake kila kitu hukichukulia poa, kasema hakuna shida tujiandae kwa safari ya kurejea nyumbani."

Henry alimjibu.


"Afanye hivyo maana hili baridi la huku limenishinda kabisa."


"Limekushibda wewe lakini kwa upande wangu aaa burudani kabisa kwanza ukichanganya na hiki kinywaji cha asili cha Ulanzi we mama wacha kazi ya ulimi kulamba lipsi tu, watu wa huku wanafaidi sana aisee na kwa utamu huu hata nikiondoka lazima nitarudi Makete hii kwanza ukiangalia jiografia yake utafikiri tuko Ujerumani? Kweli Tanzania imebarikiwa bwana."

Henry aliisifia Makete na kuahidi kuwa atarejea tena.


" Unaongea nini wewee? "

Jamaa yake alimfokea baada ya kuona Henry kajisahau.


" Bwana mdogo achana na mimi halafu kumbuka ni mkubwa wako siyo unanikamatakamata tu nitakuharibia."

Henry alimfokea rafiki yake na kisha kumsukuma kitu kilichopelekea aanguke chini.


" Nashukuru Bosi kwa ulilonifanyia hapa lakini kumbuka kuwa mambo yako ya kijinga ndiyo yaliyopelekea tukampoteza yule dereva Taxi na kwa hili nakuahidi tukifika tu nyumbani nitamjulisha Mackdone siwezi kuadhibiwa kwa ujinga wako halafu unanisukuma?"

Maneno ya rafiki yake yalimfanya amuangalie kwa hasira.


" Unasemaje wewe? "

Henry alimuuliza.


" Acheni hizo ninyi kwanini mnataka kupigana? Henry njoo hapa."

Hamza aliwazuia baada ya kuona wanataka kushikana mashati.


" Naam kaka.. "

Henry alimjibu Hamza.


"Nahitaji uji mzito nasikia njaa."

Hamza alimwambia Henry.


"Ngoja nikakununulie kaka narudi sasa hivi."

Henry alimjibu na kutoka mle chumbani.


"Na wewe hapo hebu njoo hapa."

Hamza alimwita huyu kijana mwingine.


"Naam."

Aliitika.


"Hivi hapa tuko wapi?"

Hamza alimuuliza na bila shaka hii ni kutokana na kuwa sawa kiakili.


"Huku kaka ni Tanzania na hapa ni Hospitali ya St. Consolata iliyoko Makete ya Njombe."

Kijana huyo alimjibu.


"Makete Tanzania? Kwamba hospitali yetu ilishindwa kunitibu?"

Hamza aliendelea kudadisi.


"Hapana lengo la kuletwa huku ilikuwa ni kwa ajili ya usalama tu."

Kijana huyo alimjibu.


"Okay vizuri una simu hapo nimpigie mke wangu kumjulisha naendeleaje si mlimwambia kuwa niko Tanzania?"

Swali la Hamza lilimchanganya kijana wa watu ambaye hakujua amjibu nini kwani alijua nini kitatokea iwapo atamueleza ukweli kuwa mke wake ni marehemu.


***


Walisonga mbele kulifikia jengo hilo ambalo waliambiwa na Ryan kuwa ndilo limekuwa likitumika mara nyingi kuhifadhia mateka. Wakiwa wananyata kusogea kwenye jengo hilo mara Jackline alihisi harufu ya manukato kutoka kwenye kiunga cha maua na hivyo aliamua kurudi nyuma kidogo na kuchungulia.


"Kuna nini?"

Titiana alimuuliza Jackline huku na yeye akirudi nyuma na kufanya kama alivyofanya Jackline. Lakini Jackline hakumjibu kitu zaidi ya kutumbua macho mara baada ya kuwaona watu wawili wakiwa wameketi kwenye viunga vya maua wakiwa wamejiachia wakinywa na kuvuta sigara.


"Nafasi hii ya leo siwezi kuipoteza hata kidogo mshenzi wewe."

Jackline aliongea huku akiichomoa bastola yake na kuikagua kama iko tayari kwa shambulizi.


"Mmhh haitakuwa hatari kwetu na kwa wenzetu? Kumbuka tumekubaliana tunaingia wapi."

Titiana alimtahadharisha Jackline.


"Ni kweli kabisa Titiana lakini kwa hili wacha iwe tu."

Jackline alimjibu huku akiiweka bastola sawa na Titiana akaona isiwe shida naye akaitoa yake na kuielekeza kule kule huku akisubiri amri kutoka kwa Jackline.


"Kaa sawa nikihesabu mpaka tatu tunafyatua wewe kwa yule mwenye kofia na mimi nakomaa na huyo mwingine."

Jackline alimpa maelekezo Titiana.


"Sawa sawa."

Titiana alimjibu huku akimuweka kwenye tageti huyo aliyeelekezwa.


"Moja... Mbili...... Taaaaaaatu...."

Jackline alihesabu na kisha wakazifyatua risasi ambazo zilikwenda moja kwa moja kwa wale wasichana waliokuwa pale wakila bata bush lao kama vile hakuna kufa.


"Mamaaaaaa......"

Ulisikika ukelele huo kutoka kwa mmoja wa wale wasichana na kuwafanya wakina Jackline kugonga mikono kama ishara ya ushindi kwao.


"Mbona unanizuia tena wacha niwamalize kabisa."

Titiana alikasirika baada ya kuona Jackline anamzuia asiwafyatulie risasi nyingine za kuwateketeza kabisa.


"Mpaka sasa hawajajua risasi zimetokea wapi na hivyo hata hao wasaidizi wao watashindwa kujua ni nani aliyewafanyia hivyo, ukiwafyatulia nyingine watabaini tulipo hivyo hapa tujifiche kwanza kuusoma mchezo kule najua wakina Roberto wataumaliza mchezo."

Jackline alimjibu Titiana.


" Poa nimekupata."

Titiana alimjibu akiitoa kwenye tageti bastola yake.


" Angalia kule mbele kinachoendelea."

Jackline alimwambia Titiana.


" Haa yule si Vivian? "

Titiana alimuuliza Jackline baada ya kumuona mtu ambaye alimkimbia Australia akiwa kafika kutoa msaada kwa majeruhi wao.


"Tumevamiwa tayari ninyi hapa haraka sana sambaeni kila uchochoro wa kambi hii kuwatafuta wale wote waliofanya tukio hili na kuwaleta wakiwa hai na ninyi wengine kaongezeni ulinzi kwenye jengo la mateka."

Vivian alitoa maelekezo kwa vijana huku yeye na wenzake wawili wakiwachukua majeruhi na kuanza kuwakokota mpaka kwenye chumba ambacho kiko mita chache kutoka kwenye lile ghala.


" Si unaona wanamowaingiza? Wakitoka tu sisi tunabadili najua ambaye ataingia mle atakuwa ni tabibu tu."

Jackline alimwambia Titiana wakati huo wakiwa bado wanaendelea kufuatilia kinachoendelea mbele ya macho yao. Wakiwa wamejituliza pale kwenye maua yaliyo karibu na kijito mara kuna mmoja wa walinzi alipita karibu na pale walipojificha akiwa hana hili wala lile alijikuta akibanwa mdomo kwa nguvu kutoka nyuma yake.


"Mhhhhhhhhhhhh...."

Aliishia kutoa mlio ambao haukufika kokote kutokana na namna ambavyo alibanwa na Jackline.


"Umewahi kuziona hizi sura?"

Titiana alimuuliza mlinzi huyo ambaye alitikisa kichwa kuashiria hawajui.

Pasipo kupoteza muda wowote Titiana alielekeza bastola kwenye sikio la kulia na kumfyatulia risasi ambayo ilimpeleka chini na hivyo kutoa nafasi kwa wakina Jackline kumvutia kichakani ambako huko walimvua zile sare na kisha Titiana akavalia.


"Naonekanaje hapa?"

Titiana alimuuliza Jackline mara baada ya kutupia zile sare za yule mlinzi.


"Acha maswali tuondoke hapa tuelekee kwenye lile jengo walimoingizwa watu wetu lazima tukawafungie kazi."

Jackline alimwambia Titiana na kisha wakaondoka.


"Tumechungulia kwenye hili jengo hakuna mtu yeyote ndani yake ila kuna chumba pembeni yake ndiyo tunaangalia namna ya kukichunguza nacho."

Ujumbe uliingia kwenye simu ya Jackline ambaye baada ya kuusoma alimpa ishara ya wao kusonga mbele.


"Lile ghala halina mtu hivyo tunatakiwa tuingie mle ndani kabla ya Daktari kufika."

Jackline alimwambia Titiana wakati huo wakiwa hatua chache kukifikia kile chumba. Na walipoufikia mlango ule hawakuwa na la kusubiri kwa kutumia bastola zao zenye viwambo vya sauti walikisambaratisha kitasa na kuingia ndani ambamo waliwakuta wale wasichana waliowafyatulia risasi.


"Umefuata nini humu ndani?"

Nawane aliuliza baada ya kuiona sura ya Jackline ambayo si ngeni machoni pake.


"Nimeifuata roho yako ambayo ilinikimbia awamu ya kwanza, unafikiri na leo itanikimbia?"

Jackline alimjibu na kumuuliza.


"Unafikiri mtafanikiwa katika hili? Hakuna aliyewahi kutoka salama ndani ya hili jengo."

Nawane japo alikuwa akitiririkwa damu nyingi lakini hakujali aliendelea kuonesha jeuri mbele ya wakina Jackline kitendo hicho kilimuudhi Titiana ambaye alimtandika risasi ya kichwa yule msichana mwingine ambaye alikuwa akikoroma tu huku damu zikiendelea kumbubujika.


"Umefanya nini sasa?"

Nawane aliuliza baada ya kumshuhudia mwenzake akienda chini.


"Hizo ni salamu tu Nawane aka Dorice."

Titiana alimjibu huku akiihamishia bastola upande wake Nawane.


"Yaani ninyi labda mfanikiwe kutumaliza kabla wenzetu hawajafika lakini iwapo nitapona mtanit......"

Kabla Nawane hajamaliza kuongea mara mlango ulifunguliwa na kuingia mwanaume aliyedhaniwa kuwa ni Daktari.


"Kuna nini tena?"

Daktari huyo aliuliza mara baada ya kumuona mlinzi akiwa kamuelekezea bastola Nawane wakati huo Jackline alishajificha nyuma ya mlango.


"Karibu Daktari fuata kilichokuleta maswali mengine hayakuhusu."

Jackline alimwambia akitokea nyuma ya Daktari.


"Unasemaje wewe?"

Daktari aliuliza huku akiingiza mkono mfukoni kwa lengo la kutoa bastola yake ambayo haikufanya kazi kwani alijikuta akienda chini baada ya kukutana na risasi ya kichwa.


"Nawane hizi bado ni salamu tu kwako, nikuhakikishie kuwa kupitia chumba hiki tuwapuliza mmoja baada ya mwingine usalama wako ni kutuonesha chumba mlichowahifadhi watu wetu."

Jackline alimuuliza huku akiwa kamkanyaga tumboni.


"Kwa hilo mnafikiri mtafanikiwa na kwa taarifa yenu kuna wengine wanaingia hapa muda si mrefu ambao hamtaamini macho yenu na bila shaka hapo ndiyo mtaamini kuwa sisi ni profeshino zaidi yenu."

Nawane alimjibu Jackline.


"Wengine? Wakina nani hao?"

Jackline alimuuliza swali Nawane ambaye alianza kulegea.


"Una...unataka kuwa.....kuwaj.....hata mimi sifah......"

Kabla hajamalizia kauli yake alikata moto na kuwashangaza wakina Jackline kwa mara nyingine.


"Hapana huyo hajafa atakuwa kazimia tu lete maji yale pale tumzibue."

Jackline hakutaka kuamini kama Nawane kafa kienyeji kiasi hicho. Titiana alileta maji na kumwagia lakini hakuweza kuzinduka na hapo ndipo walipoamini.


"Mshenzi huyu anakufaje kijinga hivyo?"

Titiana aliuliza kwa ghadhabu akiupiga ngumi ukuta.


"Simu ya mzee Minyetye haipatikani sijui kapatwa na nini?"

Jackline alimwambia Titiana baada ya kumkosa hewani mzee wao anayemshughulikia Jessica.


"Mbona hata Jasmine naye hapatikani hewani kuna nini huko kijijini?"

Titiana naye alishangaa baada ya kumkosa Jasmine hewani na hivyo kumpigia simu Roberto.


"Mko salama ninyi huko?"

Titiana aliwauliza.


"Mmekwama wapi ninyi sisi tuko nje ngome walipita njia yetu kama vile waliambiwa tuko upande ule tulijibana kwa muda lakini walizidi kuongezeka kuimarisha ulinzi tukaona turudi nyuma kwanza."

Roberto alimfafanulia Titiana.


0 comments:

Post a Comment

Blog